Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 4/15 kur. 18-22
  • Tabibu Luka Afanya Kazi Iliyo Bora Zaidi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tabibu Luka Afanya Kazi Iliyo Bora Zaidi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mtu Mwenyewe Mwenye Kukiandika Kitabu
  • Inakupasa Utazamie Nini?
  • Kueleza Mambo kwa Njia ya Kidaktari
  • Alipenda Kutaja Habari za Wanawake na Sala
  • “Habari Njema” kwa Watu Wote
  • Luka—Mfanyakazi Mwenzi Mpendwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Kitabu Cha Biblia 42—Luka
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Johari Kutokana na Gospeli ya Luka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Luka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 4/15 kur. 18-22

Tabibu Luka Afanya Kazi Iliyo Bora Zaidi

WEWE una maoni gani juu ya madaktari? Muda wote wa historia watu wameheshimu matabibu. Watu wasiokuwa na ustaarabu walikuwa wakiheshimu sana waganga wao wa kienyeji kama vile watu wa kisasa wanavyoheshimu wanadamu wao. Kwa sababu gani?

Ingawa nguvu za miili yetu za kujiponya zinashinda karibu theluthi tatu za magonjwa yetu bila usaidizi wa dawa, madaktari wenye kudhamiria mambo wanasaidia mara nyingi kumfanya mgonjwa aamini na kutumaini kwamba atapata nafuu. Pia, matabibu wameweza kutusaidia kwa maarifa yao ya dawa zenye matokeo mazuri na ustadi wao wa kuponya. Kwa hiyo, watu wengi wanavutwa na matabibu kwa kuwachukua hao kuwa watu wanaotimiza kazi nzuri ajabu.

Hata hivyo Biblia inaeleza habari tabibu aliyebadili kazi yake aweze kusaidia watu kwa njia kubwa zaidi. Yeye ni mfano mwema kwetu juu ya namna tunavyoweza kutumia maisha zetu kwa njia yenye faida.

Mtu huyo, Luka, aliishi katika karne ya kwanza WK. Paulo, yule mtume Mkristo, alimwita Luka “yule tabibu mpendwa,” na kama tutakavyoona, maandishi ya alikuwa daktari. (Wakolosai 4:14) Walakini, inastahili kuangaliwa kwamba sifa ya Luka haikutokana na kutibu wagonjwa au waliojeruhiwa. Bali, alisifika kwa sababu ya mambo aliyofanya baada ya kuwa Mkristo.

Ingawa Luka angaliweza kukaa katika mji mmoja na kujichumia pesa nyingi aishi kwa starehe, yeye alichagua kupatwa na magumu kwa kuambatana na Paulo katika safari za umisionari. Na baadaye Luka alitia bidii kuchunguza mambo na kuandika masimulizi ya Injili maana yake ni “habari njema.” Kwa jitihada zake za kueneza habari njema za Kikristo, kutia na uandikaji wa Injili yake na Matendo ya Mitume, Luka alionyesha kwamba mema ambayo mtu anaweza kutimiza katika kazi za Kikristo yanayapita hata yale yanayoweza kufanywa na tabibu mwenye ujuzi mwingi katika kutibu ugonjwa au kupunguza maumivu kwa muda. Tunaweza kuithamini zaidi kazi nzuri ya Luka kwa kuangalia baadhi ya mambo yanayohusu mtu huyo na masimulizi yake ya Injili.

Mtu Mwenyewe Mwenye Kukiandika Kitabu

Wengine wamedai kwamba Luka alikuwa Mtaifa kwa sababu ya jina lake la Kigiriki, kwa sababu ya namna ya kuandika kwake na uhakika wa kwamba katika Wakolosai 4:10-14 Paulo anataja “watu wa tohara” kisha baadaye anamtaja Luka. Walakini, hiyo ni njia ya fasiri ya watu tu nayo haipatani na vile Warumi 3:1, 2 inavyoonyesha. Hapo tunaambiwa kwamba Mungu aliwakabidhi ‘Wayahudi’ matamko matakatifu yake. Kwa hiyo huenda ikawa Luka alikuwa Myahudi mwenye kusema Kigiriki akiwa na jina la Kigiriki.

Maandishi ya Luka yanathibitisha kwamba alikuwa mtu mwenye elimu nyingi. Aliandika kwa namna safi ya Kigiriki chenye kutiririka vizuri. Mitungo ya mistari ya maneno yake ni migumu kuliko ile iliyo katika Injili zile nyingine, naye anatumia upana mkubwa wa maneno mapya yasiyo ya usemi ule wa kikawaida.

Utangulizi wa Injili yenyewe unaonyesha pia kwamba Luka alikuwa mtu mwenye elimu nyingi. Unaanza kwa kusema: “Ijapokuwa wengi wamejitwalia kazi ya kukusanya taarifa ya mambo ya uhakika ambayo yanaaminiwa kiukamili miongoni mwetu, sawa na wale ambao tangu mwanzo walikuwa mashahidi wenye kujionea kwa macho . . . , mimi niliazimu pia, kwa sababu nimefuatia mambo yote tangu mwanzo kwa usahihi, kuyaandika kwa utaratibu wenye kufuatana vizuri . . . ili wewe upate kujua kiukamili ule uhakika wa mambo ambayo umefundishwa kwa mdomo.” (Luka 1:1-4, NW) Uandikaji huo unafanana na matangulizi yaliyoandikwa kwa ustadi katika vitabu vya mambo ya Kigiriki.

Hapa Luka anahakikishia wasomaji wake kwamba yeye haandiki mambo aliyosikia tu wala haandiki mapokeo yaliyosemwa kwa mdomo tu. Kwa sababu gani? Kwa sababu ni wazi Luka hakuwa mwanafunzi Yesu alipokuwa duniani. Luka alifanya uchunguzi wa uangalifu kati ya “mashahidi wenye kujionea kwa macho” wakati alipokuwa akitayarisha Injili yake. Pia, alichunguza maandishi mengine yenye kulingana na habari za nyakati hizo, ‘akafuatia mambo yote tangu mwanzo kwa usahihi.’ Jambo hilo linapasa kutuongezea hali ya kuyaamini maandishi ya Luka.

Lakini Luka alizipataje habari ndefu hizo alizoandika? Kinapofikia mahali fulani katika masimulizi ya safari za Paulo, kitabu cha Matendo kinaacha kutumia namna ya umoja au wingi wa mtu wa tatu (“yeye,” “aka-,” “wao,” “waka-”) na kuanza kutumia namna ya wingi wa mtu wa kwanza (“sisi,” “tuka-,” “-etu”). Inaeleweka kutokana na jambo hilo kwamba Luka alianza kusafiri pamoja na Paulo wakati wa safari yake ya pili ya umisionari. (Matendo 16:10) Ni wazi kwamba kwa kuambatana na Paulo Yerusalemu kwenye mwisho wa safari ya tatu, Luka angeweza kuhojia huko wanaume na wanawake waliokuwa mashahidi wa kujionea kwa macho yao wenyewe huduma ya Yesu. (Matendo 21:1, 7, 15-18) Pia huenda ikawa kwamba Luka alichunguzia hati za maandishi huko, kama zile zilizotumiwa kutayarisha maandishi ya ukoo wa vizazi kwenye Luka 3:23-38.

Mtume Paulo alifungwa gerezani huko Kaisaria kuanzia karibu na mwaka 56 mpaka wa 58 WK. Kwa kuwa Luka aliandika Injili yake kabla ya kitabu cha Matendo (kilichomalizwa karibu na mwaka wa 61 WK), inaelekea kwamba Luka alitumia wakati wake vizuri akaandika Injili yake Paulo alipokuwa amefungwa gerezani.

Inakupasa Utazamie Nini?

Utapata faida nyingi sana kwa kusoma kitabu cha Luka kilichoandikwa kwa uangalifu, kitabu chenye uchangamshi habari nyingi za kufundisha mtu. Kwa kufanya hivyo, unaweza kutazamia njia yenye faida hali fulani fulani za kupendeza au mambo yaliyoelezwa kwa njia ya kutokeza. Tunaweza kutaja manne namna hiyo.

Jambo la kwanza ni matumizi ya Luka ya maneno na maelezo ya kidaktari. Wanawake na sala pia ni mambo yaliyotajwa kwa njia ya pekee katika Injili ya Luka, kwa hiyo fungua macho uone mambo mawili hayo. Jambo la nne ni kwamba Luka aliandika kwa ajili ya watu wote. Ili uwe na hamu ya kukisoma kitabu hicho, acha tuone baadhi ya mifano yenye kuonyesha mambo manne hayo.

Kueleza Mambo kwa Njia ya Kidaktari

Injili zote zinaripoti miujiza ya Yesu, lakini unaposoma Luka angalia ni mara nyingi namna gani anasimulia maponyo ya Yesu. Kisha angalia namna ya usemi unaotumiwa au maelezo yenye kufunua kirefu hata mambo madogo-madogo.

Kwa mfano, mara nyingi Luka anaeleza mambo ya kitiba ambayo Mathayo na Marko wanayaacha. Ingawa hao wawili wanatuambia Petro alikata sikio la Malko, Luka anataja wazi kwamba lilikuwa sikio la kuume na kwamba Yesu alikirudisha kiungo hicho cha mwili kilichokatwa. Je! maelezo hayo si ya mtu aliye daktari? (Mathayo 26:51; Marko 14:47; Luka 22:50, 51) Vivyo hivyo, Luka anaripoti kwa usahihi kwamba mama-mkwe wa Petro “alikuwa ameshikwa na homa kali, kwamba Yesu aliponya mtu ‘mwenye kujaa ukoma’ na mwingine ambaye “mkono wake wa kuume umepooza.”​—Luka 4:38, 39; 5:12-14; 6:6-10.

Kuna ushuhuda mwingine mwingi wa kuonyesha Luka alikuwa daktari. Alipokuwa akiripoti kwamba Yesu “aliwaponya wengi magonjwa yao, na misiba, na pepo wabaya,” Luka alitofautisha maponyo yaliyokuwa ya namna ya kimwili tu na yale yaliyohusiana na mashetani. (Luka 7:21) Luka peke yake ndiye anayetueleza kwamba wakati Yesu alipokuwa akisali muda mfupi tu kabla hajakamatwa, ‘alikuwa katika dhiki’ na kwamba “hari yake ikawa kama matone ya damu yakidondoka.” (Luka 22:44) Kupendezwa kwa tabibu huyo na hali ya kueleza mambo kulihusika hata katika ripoti aliyotoa juu ya mifano ya Yesu. Luka peke yake ndiye anayetueleza mfano wa yule ‘Msamaria mwema.’ Je! wewe unakumbuka namna Msamaria huyo alivyotibu majeraha ya mtu aliyepatikana kando ya njia? Maelezo ya Luka yanalingana na namna watu walivyokuwa wakitibiwa siku hizo. Na je! Unakumbuka namna Luka alivyoeleza waziwazi kabisa hali ya afya mbaya ya Lazaro? Angalia maelezo hayo katika Luka 16:20. Kabla ya kufunga ukurasa huo, angalia katika mstari wa 24 namna tajiri anavyolia, “ninateswa.” Luka alitumia neno la Kigiriki kwa maumivu au kihoro (huzuni) lisilotumiwa na mwandikaji mwingine wa Biblia, lakini ambalo lilitumiwa mara nyingi na matabibu Wagiriki kama Hippokrato, Aretaeo na Galeni.

Alipenda Kutaja Habari za Wanawake na Sala

Unaposoma kitabu cha Luka tafuta ushuhuda wa kuonyesha alikuwa na huruma ya kupendezwa na habari za wanawake, na labda hiyo inaonyesha hali ya huruma iliyomvuta atake kuwa mwana-dawa. Kwa mfano, sura ya kwanza inaeleza habari zinazotajwa na Injili hiyo tu kuhusu Elisabeti, mama yake Yohana Mbatizaji, na hata zinataja mama huyo alijisikia kitoto kikiruka katika tumbo lake la uzazi. Sura iyo hiyo inaeleza habari za uchangamshi juu ya vile Mariamu alivyojisikia kuhusu wazo la kuwa mama ya Masihi.

Baadaye katika Injili ya Luka utajifunza juu ya: Ana nabii-mke; mjane wa Naini; mwanamke aliyekuwa amekuwa mtenda dhambi lakini akaosha miguu ya Yesu kwa machozi yake; wanawake waliohudumia Kristo kutokana na mali zao; kuponya kwa Yesu mwanamke aliyekuwa amekuwa akitokwa na damu muda mrefu; maoni ya kinyumbani yenye kutofautiana kati ya Martha na Mariamu; “mwanamke, aliye wa uzao wa Ibrahimu” aliyekuwa amelemaa muda wa miaka 18 kisha ile mifano ya mwanamke aliyepoteza sarafu na mjane na hakimu.​—Luka 2:36-38; 7:11-15, 36-50; 8:1-3, 43-48; 10:38-41; 13:11-16; 15:8-10; 18:2-8.

Je! wewe unafikiri orodha hiyo inataja habari zote za wanawake katika kitabu cha Luka? Kama wewe ni mwanamke, una pendezwa na wanawake au ungependa kuona namna tabibu Luka alivyopendezwa sana kwa huruma kuandika habari za wanawake, soma masimulizi yake yote uone habari nyingi zaidi za namna hiyo. Unapofanya hivyo, angalia namna Luka anavyotaja sala mara nyingi.

Utakuta kwamba ni Luka peke yake anayetaja sala kadha za Yesu. Kwa mfano Luka peke yake ndiye anayetuambia kwamba Yesu alikuwa akisali wakati mbingu zilipofunguka kisha roho takatifu ikamiminwa juu yake na kwamba baadaye Kristo alisali usiku kucha. (Luka 3:21; 6:12) Ikiwa ungependa kuona mifano mingine, fungua Luka 5:16; 9:18, 28; 11:1; 23:46. Pia, Luka anatueleza mifano kadha ya Yesu juu ya sala, kama ile inayohusu yule rafiki wa usiku wa manane, hakimu dhalimu na Farisayo na mkusanya-kodi.​—Luka 11:5-13; 18:1-8, 10-14.

“Habari Njema” kwa Watu Wote

Inaelekea kuwa Mathayo aliandika Injili yake kwa Wayahudi hasa, na Marko akaandika yake kwa Warumi, lakini Luka aliandika “habari njema” kwa watu wote. Kionyesho kimoja cha jambo hilo ni kwamba Luka anafuatisha ukoo wa Yesu wa vizazi mpaka huko nyuma kwa Adamu, baba wa kwanza wa wanadamu wote. (Luka 3:23, 38; linganisha Mathayo 1:1, 16.) Katika Injili yake yenye kuvuta watu wa ulimwengu mzima, Luka anatusaidia tuone kwamba ujumbe wa Kristo na kazi alizotenda ungeweza kuletea mtu faida hata kama yeye ana hali gani​—Msamaria mwenye ukoma, mkusanya-kodi aliyekuwa tajiri na hata mwizi aliyelaaniwa mwenye kufa juu ya mti. (Luka 17:11-19; 19:2-10; 23:39-43) Utahisi pia Luka akivuta mioyo ya wote waliokuwa ‘wamepotea,’ katika uhakika wa kwamba anaandika mifano ya Yesu juu ya kondoo yule aliyepotea sarafu iliyopotea, mwana mpotevu na Farisayo na mkusanya-kodi. (Luka 15:4-32 18:9-14) Unaposoma Injili ya Luka, fungua macho uone mifano mingine ya vile Luka anavyotolea watu wote tumaini.

Bila shaka, kuna mambo mengine mengi ya kutokeza unayoweza kuona katika Injili ya Luka. Lakini kwa ujumla kitabu hicho kinapasa kuonwa kuwa kimeandikwa na mtu mwenye elimu na uangalifu, lakini kina masimulizi yenye uchangamshi na yenye kuvutia juu ya maisha ya Yesu. Ni masimulizi ya Injili yanayoonyesha wazi kwamba sasa “habari njema” zinaweza kupatwa na watu wote.

Hasa katika kipindi chetu “habari njema” hizo zinathaminiwa. Tabibu Luka ndiye mwandikaji wa pekee wa Injili aliyeandika unabii wa Yesu wa kwamba wakati ungekuja ambao, kwa sababu ya taabu kubwa duniani mwishoni mwa mfumo wa mambo, ‘watu wangevunjika mioyo kwa kuogopa na kutazamia.’ Lo, Luka pia alifurahi kama nini kuyaandika maneno ya Yesu ya faraja kwenye Luka 21:25-28!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki