Wakf na Mfano Wake
1. Ishara ya kitambulisho cha mtu inawezaje kuwa jambo zuri, kama ilivyokuwa kwa habari ya Wayahudi wanyofu kabla ya uharibifu wa Yerusalemu mwaka 607 K.W.K.?
ISHARA au mfano wa kitambulisho cha mtu au cheo chake rasmi chaweza kuwa jambo zuri, ndiyo, jambo la lazima. Kwa mfano, Yerusalemu ulipokuwa karibu kuharibiwa mwaka 607 K.W.K., “mtu” wa mfano alitumwa aende akatie alama vipaji vya nyuso vya Waisraeli wenye mioyo minyofu ili awalinde wasiuawe. Ni wale wachache tu ambao walikasirishwa sana na ‘mambo ya kuchukiza yaliyokuwa yakifanywa’ katikati ya kile ambacho kilipaswa kuwa mji mtakatifu wa Mungu ndio waliotiwa alama ya kupata wokovu.—Eze. 9:1-7
2. Ni mambo gani yenye kutambulisha yanayozungumzwa katika Ufunuo sura ya 7, na hayo yanahusianaje na wokovu?
2 Leo “dhiki ile iliyo kuu” inakaribia kuufyatukia ulimwengu huu wote. Kwa hiyo Ufunuo 7:1-8 unatuambia kwamba wale “malaika wanne” walioko kwenye pembe nne za dunia wameagizwa wazishikilie zile pepo nne zisivume na kutokeza tufani yenye kuleta uharibifu mkubwa sana au “dhiki” mpaka hesabu iliyowekwa ya waliochaguliwa wa Mungu ikamilike kutiwa muhuri katika vipaji vya nyuso zao. Vilevile, hiyo inatoa wakati wa “mkutano mkubwa” ujisafishe “katika damu ya Mwana-Kondoo” ili watambuliwe kuwa wanastahili kuiokoka “dhiki ile iliyo kuu.”—Ufu. 7:9-14; Mt. 24:21, 22.
3, 4. Kwa habari ya kuhani mkuu Myahudi, ‘ishara ya wakf’ juu ya kilemba chake ilikuwa ukumbusho wa nini?
3 Katika Israeli wa kale ukuhani uliwekwa. Musa alikuwa ametekeleza maagizo kamili yaliyotoka kwa Yehova ya kutengeneza mavazi ya kumtambulisha kuhani mkuu. Kuhusu kilemba imeandikwa hivi: “Nao wakafanya hilo bamba la hiyo taji takatifu la dhahabu safi, na kuandika juu yake andiko, mfano wa [ishara] wa kuchorwa kwa muhuri, mtakatifu kwa Bwana [‘Aliyetakaswa kwa Yahweh,’ The Jerusalem Bible]. Nao wakatia ukanda wa rangi ya samawi ili kulifunga katika hicho kilemba upande wa juu.”a—Kut. 39:30, 31; 29:6; Law. 8:9.
4 Huo ‘mfano wa wakf’ (NW) ungekuwa ukumbusho kwa kuhani mkuu na kwa watazamaji wote kwamba alikuwa ‘ametakaswa’ au amewekwa wakf na Mungu kwa ajili ya utumishi mtakatifu kwa niaba ya kikundi cha watu waliowekwa wakf. Yeye pamoja na makuhani wenzake wangeongoza katika kufundisha watu na kutoa dhabihu zenye kukubalika za ondoleo la dhambi, ambazo zingewasaidia kuishi kulingana na wakf wao kwa Mungu. Hizo zingeendeleza msimamo mtakatifu uliowekwa wakf wa taifa hilo, kwa maana walionywa kwamba kama wangemwacha Yehova yeye naye, angewaacha na kuwatupilia mbali kwa maadui wao.—Kum. 28:15, 25, 63.
5. Ingawa leo hakuna Myahudi mwenye jina Cohen ni nani anayeweza kujitambulisha mwenyewe kuwa kuhani mkuu wa jamaa ya Haruni, na kwa sababu gani hali yetu ina tumaini?
5 Historia ya huzuni ya Waisraeli imejawa na misiba waliyoipata kama matokeo ya kuacha amri za Mungu na utumishi wao uliowekwa wakf kwake. Baada ya uharibifu wa pili wa Yerusalemu na hekalu lake mwaka 70 W.K., kuhani mkuu pamoja na mfano wa wakf juu ya kilemba chake ulikoma. Leo hakuna Myahudi mwenye jina la jamaa Cohen (maana yake “Kuhani”) anayeweza kujithibitisha kuwa kuhani mkuu wa Israeli. Basi, hali yetu ni ile isiyo na tumaini? Hapana! kwa maana kuhusu Mwana wa Mungu aliyetukuzwa, tunasoma hivi: “Kuhani mkuu kama huyo alitufaa sisi, mshikamanifu, mnyofu, asiye na unajisi, aliyetengwa na wenye dhambi, na kuwa juu zaidi ya mbingu, . . . alijitoa mwenyewe.”—Ebr. 7:26, 27, NW.
6, 7. Je! Yesu alizaliwa katika kabila la kikuhani la Israeli, na angewezaje kuwa kuhani mkuu?
6 Kwa kuwa Yesu alikuwa Mwana wa Mungu, hakuhitaji kuwa mshiriki wa kabila la Lawi au wa jamaa ya kikuhani ya Haruni ili awe kuhani wa Mungu. Hiyo ingewezekana kulingana na mpango mzuri sana wa Yehova Mungu. Mfalme Daudi aliongozwa na roho ya Mungu atabiri juu ya mzao huyo mwenye kutokeza sana ambaye angekuwa juu zaidi ya mababu zake wa kifalme: “Usemi wa Yehova kwa Bwana wangu ni: ‘Keti kwenye mkono wangu wa kiume mpaka mimi niweke adui zako kama kiti cha miguu yako.’ Fimbo ya nguvu zako Yehova ataituma toka Sayuni akisema hivi: ‘Nenda uwe ukishinda katikati ya adui zako.’ Watu wako watajitoa wenyewe kwa moyo wa kupenda siku ya jeshi lako la vita. Katika fahari za utakatifu [kwa mapambo matakatifu], kutoka tumbo la uzazi la mapambazuko unalo shirika la wanaume vijana kama matone ya umande. Yehova ameapa (na yeye hataghairi): ‘Wewe ni kuhani mpaka wakati usiojulikana kulingana na namna ya Melkizedeki!’”—Zab. 110:1-4, New World Translation; An American Translation.
7 Kwa hiyo, mpaka siku hizi zetu, Yesu Kristo aliyetukuzwa anaendelea kuwa Kuhani Mkuu wa kifalme, aliye juu zaidi ya makuhani wakuu wa Israeli ya kale pamoja na mfano wa wakf wao unaoonekana. Yeye ana cheo si kwa sababu ya kuwa kuhani wa Kilawi bali kwa sababu ya ahadi nzito iliyoapwa ya Yehova Mungu.
MFANO KWA WALE ‘WANAOJITOA WENYEWE KWA MOYO WA KUPENDA’
8. Kwa sababu gani hii ndiyo siku ya ‘jeshi la vita’ la Kristo, na wale wanaojitoa wenyewe kwa moyo wa kupenda sasa wanaendeleaje katika jambo hilo?
8 Wanafunzi wa huyo Kuhani Mkuu wa kifalme, Kristo Yesu, sasa ‘wanajitoa wenyewe kwa moyo wa kupenda’ katika siku ya ‘jeshi lake la vita.’ Wao wanajiweka wakf kwa Yehova Mungu katika jina la huyu Kuhani Mkuu wa kifalme, na kubatizwa katika maji uwe mfano wa wakf wa huo. Hawa ndio ambao hesabu yao kamili lazima mwishowe itiwe muhuri kabla ya kufyatuka kwa “dhiki ile iliyo kuu.” Wao, pamoja na wenzi wao wa ule “mkutano mkubwa” ‘wanajitoa wenyewe kwa moyo wa kupenda’ kama vile matone ya umande katika kuwaletea watu ujumbe wa wokovu wa Mungu wenye kuburudisha.—Ufu. 7:2-4, 9, 10, 14.
9. Katika Warumi 12:1, 2, Paulo anawapa Wakristo waliotiwa mafuta shauri gani?
9 Akiwaandikia wanafunzi wa miaka 1,900 iliyopita, mtume Paulo alisema hivi: “Nawasihi kwa huruma za Mungu, mtoe miili yenu dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu yenu ya akili. Na mwache kufanyizwa kulingana na mtindo wa taratibu hii ya mambo, bali mgeuzwe kwa kubadili akili zenu ili mpate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.”—Rum. 12:1, 2, NW.
10, 11. (a) Kwa hiyo Paulo anawasihi Wakristo wa mataifa katika Rumi ikiwa ni kufuatia mazungumzo gani? (b) Mpango huo ulikuwa wonyesho wa huruma nyingl sana kwa upande wa Mungu katika njia gani?
10 Ombi hilo lililotangulia linafuata tu baada ya mazungumzo ya Paulo juu ya mzeituni wa mfano. Taifa lililowekwa wakf la Israeli lilikuwa uzao wa asili wa “rafiki” ya Mungu, Ibrahimu, kama matawi katika mzeituni wa shamba. Kwa hiyo wao ndio waliokuwa wa kwanza kuwa “uzao wa Ibrahimu” kulingana na ahadi aliyopewa. (Mwa. 12:3; 22:17, 18; Gal. 3:16, 29; Yak. 2:23) Walakini ni mabaki tu ya Wayahudi wa asili waliomkubali Yesu kuwa Masihi na wakahamishwa kutoka kuwa uzao wa asili wa Ibrahimu wa kidunia na kuwa uzao wa kiroho wa Ibrahimu Mkuu Zaidi, Yehova (Rum. 11:5, 7) Wale waliosalia waling’o,lewa wasiwe “matawi.” Ili kuweka wengine mahali pao, Mungu aliwageukia watu wasiokuwa Wayahudi, au, ule mzeituni-mwitu wa mfano, ili atoe “matawi” ya kutosha ayapandikize kwenye mzeituni wa shamba wa kiroho ambao washiriki wake wangekuwa matawi 144,000 yenye kumwegemea Ibrahimu Mkuu Zaidi, Yehova Mungu, Chanzo cha baraka zote.—Rum. 11:13-33; Ufu. 14:1.
11 Kwa hiyo ulikuwa wonyesho wa huruma nyingi sana kwa upande wa Mungu kwa Warumi wale na watu wengine wote wasiokuwa Wayahudi waliotahiriwa kufanywa wawe sehemu ya uzao wa kiroho wa Ibrahimu kwa ajili ya baraka ya jamaa za dunia kupitia ufalme wa Mungu. (Efe. 2:12; Gal. 3:26-29) Jambo hilo liliweka mbele yao mwendo wa kujinyima. Walakini hilo ndilo lililokuwa pendeleo pekee ambalo wakati huo Mungu alikuwa akiwapa viumbe wanadamu, na lilikuwa pendeleo la pekee kama nini! Bila kupita mipaka inayofaa, mtume Paulo aliandika na kuwaambia hivi: “Jitoeni wenyewe kwa Mungu kama walio hai baada ya kufa, na viungo vyenu kwa Mungu kuwa silaha za haki. Kwa maana dhambi [haipasi kuwatawala] ninyi, kwa sababu hamwi chini ya sheria [sheria ya Musa], bali chini ya neema.”—Rum. 6:13, 14.
12. Ni mambo gani yangetiwa ndani kwa wanafunzi Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho wanapoambiwa, ‘jitoeni wenyewe kwa Mungu kama walio hai baada ya kufa’?
12 Ingawa hapa Paulo anawaandikia wale ambao tayari walikuwa Wakristo waliojiweka wakf, “watakatifu,” yeye hapuzi yale ambayo walikuwa wameyafanya hapo kwanza ndipo wakaweka wakf maisha zao, aliposema hivi: “Jitoeni wenyewe kwa Mungu kama walio hai baada ya kufa.” Lakini wanapaswa kuishi kulingana na wakf huo katika mwendo huo wa kujitoa dhabihu. Kama wasingefanya mambo hayo, basi wao, wakiwa ni matawi yaliyochukua mahali pa mengine, wangeng’olewa, vilevile.” (Rum. 1:7; 11:21, 22) Zaidi ya hayo, maneno hayo yaliyoandikwa chini ya uongozi wa Mungu yangesomwa na wanafunzi wa Kristo Yesu wakati ujao nayo yangewapa kitia-moyo chenye nguvu cha kuchukua hatua zote za lazima ili waingie katika huo uhusiano pamoja na Mungu wa kujiweka wakf na kubatizwa, na kuuendeleza. Ili wauhifadhi uhusiano wao pamoja na Mungu uliowekwa wakf, wakiisha kuufanya, wangekuwa katika vita yenye kuendelea ya kuvifanya viungo vya mwili wao viwe silaha za haki mahali pa kuvitiisha kwenye utawala wa dhambi. Hiyo ingekuwa ni kutii maneno ya Yesu: “Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike [mti wake wa mateso], anifuate.”—Mt. 16:24.
“MKUTANO MKUBWA” WA WATU WENYE KUTOA MFANO
13. Je! inafaa kwa wale wenye tumaini la kidunia kujiweka wakf kwa Mungu na kuonyesha jambo hilo kwa ubatizo wa maji?
13 Duniani pote leo watu zaidi ya 2,300,000 wanajiunga katika kutangaza habari njema za Ufalme, na wengi wa hawa wamejitoa wenyewe kwa ubatizo katika maji kuwa mfano wa wakf wao. Kwenye sherehe ya kila mwaka ya Chakula cha jioni cha Bwana, wanaopungua 10,000 kati ya hawa wanakula mkate wa mfano na divai ya mfano ili kukiri kwamba wao ni wanafunzi wa Kristo wenye tumaini la kimbinguni. Walakini je! wale wengine wote kwa kufaa wanajiweka wakf na kuonyesha hilo kwa ubatizo wa maji? Hakika kabisa wanafanya hivyo, kwa maana wao, vilevile, lazime waingie katika uhusiano unaofaa pamoja na Mungu kupitia Mchungaji Mwema, Kristo Yesu, ili waiokoke “dhiki ile iliyo kuu” ambayo iko mbele karibu na kupata urithi kwa kuwa sehemu ya “dunia mpya” ya Mungu.—2 Pet. 3:13, NW; Ufu. 21:1-4.
14. Ni uhusiano gani mwema ambao kwa kufaa umo ndani ya lile “kundi moja” la yule Mchungaji Mwema, Kristo Yesu?
14 Kwa hiyo walio wengi kabisa wa mashahidi waliojiweka wakf kwa Yehova hawana tumaini lo lote la kimbinguni la kuwa warithi washirika pamoja na Yesu Kristo katika Ufalme ulio juu. Wao hawadai kuwa ni Waisraeli wa kiroho waliozaliwa na roho ya Yehova. Hata hivyo bila kutengeka wanashirikiana na mabaki ya Waisraeli wa kiroho wakiwa washiriki wa kundi moja chini ya uongozi wa “Mchungaji mmoja,” Yesu Kristo. (Yohana 10:16) Hilo ni jambo lenye kufaa sana upande wao na kulingana na Maandiko linafaa.
15. (a) Ni nani, zaidi ya Wayahudi wa asili, waliotoka Misri na mwishowe wakaingia katika Nchi ya Ahadi, na huko walikuwa kama nani? (b) Wao wanafananisha nani leo?
15 Ebu hapa na tufanye kama ambavyo andiko katika 1 Wakorintho 10:18, NW linavyotuambia tufanye, “kiangalieni kile ambacho ni Israeli kwa njia ya mwili.” Wakati wa kutoka Misri chini ya uongozi wa Musa si wote walioondoka ambao walikuwa Waisraeli wa asili waliotahiriwa. “Na kundi kubwa la watu waliochangamana nao wakakwea pamoja nao; na kondoo na ng’ombe, wanyama wengi sana.” (Kut. 12:38) Waisraeli walipoingia Nchi ya Ahadi, watu hao walikuwa “mgeni aliye ndani ya malango yako.” (Kut. 20:10; Hes. 35:15; Law. 19:9, 10) Hilo kundi kubwa la watu waliochangamana wa kale lilifananisha “mkutano mkubwa” wa wale “kondoo wengine” wa Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, wa leo.—Yohana 10:14, 16; Ufu. 7: 9-17.
16, 17. (a) Ni katika njia gani lile “kundi kubwa la watu waliochangamana” lilibatizwa pamoja na Waisraeli kwa kusema kwa njia ya mfano? (b) Ni nani ambao wametoroka Misri ya mfano ya kisasa, na ni nani watakaopatwa na uharibifu chini ya hali kama zile zile katika Bahari Nyekundu?
16 Katika siku za Musa “kundi kubwa la watu waliochangamana” lilishiriki mambo kama hayo pamoja na Waisraeli waliotahiriwa, kutia ubatizo ulio bora. Kuhusu ubatizo huo, mtume Paulo aliandika, katika 1 Wakorintho 10:1-4: “Baba zetu walikuwa wote chini ya wingu; wote wakapita kati ya bahari; wote wakabatizwa [katika] Musa katika wingu na katika bahari; wote wakala chakula kile kile cha roho; wote wakanywa kinywaji kile kile cha roho; kwa maana waliunywea mwamba wa roho uliowafuata na mwamba ule ulikuwa ni Kristo.” Kwa hiyo, katika njia ya mfano, Waisraeli na “kundi kubwa la watu waliochangamana” walibatizwa ingawa hawakulowa maji kwa njia halisi.
17 Ubatizo huo wa kimwujiza uliofanywa na Yehova Mungu uliwaweka kwa Musa awe kiongozi wao aliyetolewa na Mungu, kama kwamba tu walikuwa wamebatizwa katika yeye kwa njia halisi. Walakini huo haukuwa ubatizo katika kifo, kama ilivyokuwa kwa Wamisri waliokuwa wakiwafuata. (Kut. 14:1-15: 21) Leo tunakaribia hali kama iyo hiyo. Mabaki waaminifu wa Waisraeli wa kiroho na wenzi wao ule “mkutano mkubwa” wameondoka katika Misri ya mfano. (Ufu. 11:7, 8) Wanapiga hatua kwenda kwenye Taratibu Mpya ya mambo chini ya ufalme wa mileani wa Kristo. Musa Mkuu Zaidi, Bwana Yesu Kristo aliyetukuzwa anawaongoza. Ulimwengu wenye uadui unawafuata, ukiwa umeazimia kwamba hawatakwenda mahali pa usalama. Wamisri wa mfano wanaelekea uwanja wa vita wa Mungu, Har-Magedoni ambapo watabatizwa kwa moto, uharibifu. Hakuna ye yote wao atakayeachwa akiwa hai asimulie hadithi hiyo yenye kuogopesha sana. (Ufu. 16:14-16; Mt. 3:11, 12) Kama ilivyokuwa katika matukio ya Bahari Nyekundu, mauaji katika Har-Magedoni hayatatia ye yote wa Israeli wa kiroho au ule “mkutano mkubwa” wa wale “kondoo wengine” wa Musa Mkuu Zaidi.
18. Wale wa “mkutano mkubwa” watakuwaje kami “kundi kubwa la watu waliochangamana” baada ya kuondoka Misri chini ya uongozi wa Musa?
18 Wale waaminifu wa ule “mkutano mkubwa” hawabaki-baki nyuma kwa moyo nusu wakitaka kurudi kwenye Misri ya mfano iliyopigwa kwa mapigo chini ya uongozi wa Farao wayo, Shetani Ibilisi. Kwa nyuso zenye kutazama mbele wanaendelea kushirikiana na mabaki ya Waisraeli wa kiroho, kama kundi moja. (Yohana 10:16) Kama vile kundi kubwa la watu waliochangamana lilivyookoka likaipita Bahari Nyekundu, ndivyo wale wa ule “mkutano mkubwa” wa kisasa wakavyojikuta kwenye fuo za wokovu baada ya “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.”
19. Sana-sana ni tangu wakati gani wale ambao ni washiriki wa ule “mkutano mkubwa” wa kisasa wamekuwa wakijitoa wabatizwe katika maji, nao wamesafishaje kitambulisho chao cha kutoa ibada safi kwa Mungu?
19 Sana-sana tangu mwaka 1935 wale ambao sasa ni washiriki wa ule “mkutano mkubwa” wamekuwa wakijitoa wabatizwe katika maji kuwa mfano wa wakf wao usiowekewa masharti kwa Mungu kupitia Musa Mkuu Zaidi. Wamesafisha mavazi yao ya kuwatambulisha na kuyafanya kuwa “meupe katika damu ya Mwana-Kondoo,” Musa Mkuu Zaidi. (Ufu. 7:9-14 Wanamtolea Mungu ibada safi.
20. Wale wa “mkutano mkubwa” wanamwabudu Yehova wapi, na hilo lilitabiriwaje katika Zekaria 8:20-23?
20 Huu “mkutano mkubwa” wa waabudu safi umo katika hekalu la kiroho la Yehova Mungu mchana na usiku. (Ufu. 7:15-17 Wao walifananishwa na wale ambao nabii Zekaria alitangulia kuwaona wakiabudu kwenye hekalu la Yehova baada ya kurudishwa katika Yerusalemu kufuatia kufunguliwa kwa Waisraeli kutoka Babeli katika mwaka 537 K.W.K. Kuhusu hilo, twasoma hivi katika Zekaria.— 8:20-23:
“[Yehova] wa majeshi asema hivi, Itatokea halafu ya kwamba watakuja mataifa na wenyeji wa miji mingi; wenyeji wa mji huu watauendea mji huu, wakisema, Haya! twendeni zetu kwa haraka tuombe fadhili za [Yehova], na kumtafuta [Yehova] wa majeshi; Mimi nami nitakwenda. Naam, watu wa kabila nyingi na mataifa hodari watakuja Yerusalemu kumtafuta [Yehova] wa majeshi, na kuomba fadhili za [Yehova].
“[Yehova] wa majeshi asema hivi, Siku hizo watu kumi, watu wa lugha zote za mataifa, wataushika upindo wa nguo yake yeye aliye Myahudi; naam, wataushika wakisema, Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.”
21. Ni katlka njia gani ule “mkutano mkubwa” ‘unashika upindo wa nguo ya mtu aliye Myahudi,’ na ni kwa sababu gani wana tumaini la kuokoka “dhiki ile iliyo kuu”?
21 Nia ya hao “watu kumi, watu wa lugha zote za mataifa” inaonyesha kujitoa kwa Mungu wa kweli wa pekee anayeishi, Yehova Mungu! Leo kujitoa huko kunakubalika Kwake kupitia “Myahudi” mkuu zaidi aliyepata kuwa duniani “Mwana-kondoo” ambaye wakati mmoja alitolewa dhabihu, yaani, Yesu Kristo. Kwa uaminifu wanamwiga Yesu kwa kubatizwa ndani ya maji kwa mfano wa kujitoa wenyewe na pia, kwa habari yao, ni mfano wa kujiweka wakf kwa moyo wote kwa Mungu uyo huyo. Kwa ‘kuushika upindo wa nguo’ ya mabaki ya Wayahudi wa kiroho 144,000, wanakusanyika na “watu” kwenye Yerusalemu wa juu, Yerusalemu wa kimbinguni. Katika hekalu lake la kiroho linalowakilishwa na mabaki ambao wangali duniani, wao wanatoa “utumishi mtakatifu” kwa Mungu Aliye Juu Zaidi, Yehova, mchana na usiku. Tumaini lao ni kuiokoka “dhiki ile iliyo kuu,” ili waendeleze utumishi wao uliowekwa wakf kwa Mungu milele duniani. Kutambulishwa kwao kunakofaa kuwa wao wamejiweka wakf bila kuweka masharti yo yote na kubatizwa kuwa watumishi wa Mungu kunawaweka katika njia ya kupata utimizo wa jambo hilo, na kuhakikishiwa kwamba “Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu . . . katika roho na kweli.”—Yohana 4:23, 24.
Footnotes]
a Usemi “ishara ya wakf” ni tafsiri ya neno la Kiebrania nezer, ambalo kitabu Exhaustive Concordance of the Bible cha Strong kinaeleza hivi: ‘[kwa] kufaa kitu kilichotengwa, yaani wakf (wa kujitenga wa kuhani au Mnaziri); kwa hiyo (kwa halisi) vifundo vya nywele ambavyo havijanyolewa; pia (kwa njia ya mfano) taji (hasa ya kifalme):—kutakaswa, taji, nywele, kutengwa.
Je! kwa kurudia wewe unaweza kujibu maulizo haya?
□ Ni kwa njia gani fikira zilielekezwa kwenye ukuhani mkuu uliowekwa wakf na Yehova kwa ajili ya utumishi mtakatifu wake?
□ Yesu aliwezaje kuwa kuhani mkuu?
□ Kulingana na Warumi 12:1, 2, NW, wale wanaokuwa wanafunzi Wakristo wanapaswa kufanya nini?
□ Kuhusu ubatizo, ule “mkutano mkubwa” unalinganaje na “kundi kubwa la watu waliochangamana” ambao waliambatana (walifuatana) na Waisraeli kutoka Misri?
□ Kwa habari ya ubatizo, wale “watu kumi, watu wa lugha zote za mataifa” wanamwigaje Yesu?