Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 8/1 kur. 12-16
  • Jeshi Hodari la Yehova la Wapiganaji wa Wakati Wote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jeshi Hodari la Yehova la Wapiganaji wa Wakati Wote
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • WAPIGANAJI-MAPAINIA KATIKA JESHI LA KIROHO
  • KUHESABU GHARAMA
  • KUFANYA ZAIDI—KAMA WALIVYOFANYA WANAZIRI
  • ‘JE! MIMI NINAWEZA KUPAINIA?’
  • Baraka za Huduma ya Painia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Yehova Ategemeza Jeshi Lake la Watumishi wa Wakati Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Mapainia Hutoa na Kupokea Baraka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Mambo Tunayoweza Kujifunza Kutoka kwa Wanadhiri
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 8/1 kur. 12-16

Jeshi Hodari la Yehova la Wapiganaji wa Wakati Wote

“[Uwe] askari mwema wa Kristo Yesu. Katika jeshi, hakuna askari anayejiingiza katika maisha ya kiraia, kwa sababu lazima awe katika utumishi wa mtu aliyemwandikisha.”​—2 Timotheo 2:3, 4, The Jerusalem Bible.

1, 2. Ni mwito gani wa kutaka wahubiri ulitolewa miaka 100 iliyopita, na matokeo yalikuwa nini?

“WAHUBIRI 1,000 WATAKIWA” Kichwa hicho cha habari kilitokea katika kichapo kimoja miaka 100 hivi iliyopita, walakini tangazo hilo lisilo la kawaida halikuwa tangazo la kibiashara katika gazeti lo lote lile. Pamoja na hayo, itikio lilikuwa kubwa zaidi ya wachapaji walivyotazamia. Ni nani waliotoa mwito huo, na ni nani waliouitikia? Vilevile, leo wewe unahusikaje?

2 Ilikuwa wakati wa mwaka wa pili wa kuchapwa kwalo, kwamba gazeti linalojulikana sasa ulimwenguni pote kuwa Mnara wa Mlinzi likawa na mwito huo wenye kuchochea wa kutaka wahubiri. Walakini utafutaji huo haukuwa wa kutaka viongozi wa kidini wajaze mimbari (jukwaa) za kanisa. Biblia haiwatolei cheo kama hicho wale wanaotumikia wakiwa wahubiri wa ujumbe wa Mungu. Mahali pake, katika mwaka 1881 wachapaji wa Mnara wa Mlinzi walikuwa wakitafuta watu wenye nia ya “kwenda kwenye miji mikubwa au midogo, kulingana na uwezo wao, wakiwa Makolpota au Waeneza Injili.” Mwito huo ulitolewa kwa wale wenye nia na wanaoweza kutumia wakati wote wao wakihubiri kweli ya Biblia. Wale walioitikia walianza wakiwa kama mtiririko mdogo, wachache hapa na wachache hapa, mwishowe wakafikia 300 mwaka 1885. Hata hivyo, sasa wamefurika wakawa maelfu, makumi ya maelfu, kufikia wastani ya 151,180 wakati wa mwaka 1981.

3. Jina la wahubiri hao limebadilikaje?

3 Mashahidi wa Yehova hawawaiti tena wahubiri hao wa wakati wote “makolpota,” ambao ni usemi wa Kifaransa uliokazia sehemu moja tu ya kazi yao, kueneza Biblia na vitabu vinavyohusiana nayo. Hiyo ni sehemu ndogo ya utendaji wao mkubwa. Neno jingine linatoa maana kamili kwa kazi ya jeshi hilo la kiroho la waeneza injili, wanaopeleka “habari njema.” (2 Timotheo 2:3, 4; Luka 8:1; 10:1) Neno hilo ni “painia.”

WAPIGANAJI-MAPAINIA KATIKA JESHI LA KIROHO

4. Msingi na maana ya neno “painia” ni nini?

4 Kwa sababu gani jina “painia” linawafaa Mashahidi wa Yehova ambao wanaweza kuwa wahubiri wa wakati wote? Hapo kwanza neno hilo lilikuwa na maana ya kijeshi, inayohusu askari, ingawa si askari wa kawaida anayekwenda kwa miguu. Lilikuwa na maana ya mhandisi (fundi) wa kijeshi, ambaye alitangulia jeshi lote na kujenga madaraja, barabara na mahandaki. Kwa hiyo, “kupainia” kukaja kuwa na maana ya kufungua njia, na “painia” alikuwa mtu aliyeongoza, aliyejisogeza mbele ujapokuwako upinzani, kama vile masetla wa kwanza wa Magharibi ya Amerika ya Kaskazini walivyofanya. Neno hilo linatumiwa kwa mtu asiyetishika, mtu anayejisukuma mbele mpaka mradi wake unapotimizwa. Hayo ni masimulizi yanayojaa kama nini kwa wale ambao wakati Wote ni “askari” wa Kristo Yesu wanaojinyima!a

5. Kwa sababu gani Wakristo wanaweza kuitwa “askari”? (Filemoni 2; Wafilipi 2:25)

5 Wakristo wote wa kweli wanaweza kufananishwa na askari wanaopiga vita ya Kiroho. (1 Timotheo 6:12; 2 Timotheo 4:7; Yuda 3) Tuna adui mmoja ambaye ameazimia kutuharibu—Shetani. Yeye amepanga kwa utaratibu jeshi lake la mashetani wasioonekana, pamoja na taratibu mbovu yake ya mambo, likawa jeshi hatari la kuwapinga wanafunzi wa kweli wa Kristo. Hata hivyo, duniani pote, Wakristo 2,300,000 hivi wanaitikia amri hii iliyoongozwa kwa roho: “Chukueni hatua ya kumpinga [Ibilisi] mkithibitika katika imani.” (1 Petro 5:9) Wao ni Mashahidi wa Yehova ambao, ingawa wao wenyewe ni dhaifu na hoi, wanafaulu katika vita hiyo ya kiroho ya kupigana na adui huyo hatari.​—Yakobo 4:7, 8, 10.

6. Ni kwa njia gani nyingine neno “askari” linawafaa Wakristo?

6 Askari aliye vitani anaweka jambo moja tu akilini, pigano lililo karibu. Yeye hawezi kuvutwa fikira na mambo yasiyo ya maana sana. Mtume Paulo alimwambia hivi mshiriki kijana Mkristo, Timotheo: “Chukuliana na fungu lako la matatizo, kama askari mwema wa Kristo Yesu. Katika jeshi, hakuna askari anayejiingiza katika maisha ya kiraia, kwa sababu lazima awe katika utumishi wa mtu aliyemwandikisha.” (2 Timotheo 2:3, 4, JB) Bila shaka, Paulo na Timotheo hawakuwa wanajeshi wa taifa fulani au wa mamlaka fulani ya kilimwengu. Kitabu An Expository Dictionary of New Testament Words cha W. E. Vine kinasema kwamba “askari” maana yake “kwa njia ya mfano ni mtu anayevumilia magumu kwa sababu ya Kristo.”

7. Mapainia wametimiza sehemu gani katika jeshi la Kikristo la wapiganaji wa kiroho?

7 Kati ya mamilioni hayo ya wapiganaji Wakristo wenye kufanikiwa, kuna jeshi la watangulizi, wahudumu wa wakati wote. Wengi wao “wamepainia” kweli kweli katika maana ya kwamba wamesonga mbele ya jeshi lote, na kufungua njia. Mara nyingi mapainia wamekwenda kwenye maeneo ambayo habari njema za ufalme wa Mungu uliosimamishwa hazijapata kuhubiriwa. Misionari wengine wenye kupainia wamekwenda nchi za ugenini ambako walipaswa kujifunza mila ngeni na lugha ngumu-ngumu, wakakabili magumu, maradhi na dini za kishetani. Wamejenga madaraja ya kupita vizuizi vyote hivyo, wakashambulia kwa silaha za kiroho na kusimamisha “sehemu za ulinzi kando ya madaraja” ambazo zimesitawi zikawa makundi yenye nguvu. Wamefungua njia ya kwenda kwenye maeneo ambayo miaka michache baadaye jeshi zima la wapiganaji-Wakristo limehubiri ujumbe wa Kristo wa ukombozi wa kiroho.​—Isaya 60:22.

8. Faida ya kuwa na wenye kujitolea katika jeshi hilo la kiroho ni nini? (Waamuzi 7:3)

8 Mwaka uliopita, kwa wastani kulikuwako 151,180 ya wapiganaji hao wa wakati wote katika shamba la ulimwenguni pote kila mwezi. Wote wamejitolea na hakuna askari wa kulipwa. (Zaburi 110:3) Hiyo inafaa, kwa sababu askari wanaoingizwa katika jeshi lo lote kwa kulazimishwa, au ambao wanatumikia ili wapate faida, mara nyingi wanakuwa wenye nia mbili vita inapokuwa yenye kivumbi. Wanakosa ujasiri na wanajitoa kwa masharti fulani au wanatoroka. Lakini ni kwa sababu gani, ikiwa mapainia wamejitoa, bila zawadi za kimwili, wanatoa wakati wao wote na hali kuna mamilioni mengine ya Wakristo waliojitoa wasiofanya hivyo? Je! hiyo inamaanisha kwamba wanapainia kwa sababu katika wakati ujao wanatazamia kupata zawadi kubwa zaidi ya wale ambao hali zao zinawaruhusu watumie saa 10, 20, 30 au hivyo kila mwezi katika huduma? Hapana, mapainia wanyofu wanajikaza katika njia hiyo ikiwa ni wonyesho wa kujitoa kwao kwa nafsi yote kwa Yehova Mungu. Kama ilivyo kwa kila Mkristo aliyejiweka wakf kweli kweli, wanataka kufanya yote wanayoweza katika kumtumikia Mungu wetu mwenye upendo. Basi ni nani wanaoweza na wanaopaswa kupainia? Tafadhali tafakari juu ya hali na maoni yako mwenyewe.

KUHESABU GHARAMA

9. Kwa sababu gani huenda Wakristo wengine wasiweze kupainia?

9 Mtu anapochanganua kama yeye anaweza au anapaswa kuwa mhudumu painia, mambo kadha yanapasa kuchunguzwa. Hali zake za kibinafsi maishani zinaamua kwa kadiri fulani. Kuna madaraka yanayopasa kuchukua mahali pa kwanza kabla ya kuhubiri kwa wakati wote. (Kumbukumbu la Torati 24:5) Mtume Paulo aliandika kwamba Mkristo ambaye hangetoa mambo ya lazima ya maishani ya kimwili kwa watu wa nyumba yake “ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.” (1 Timotheo 5:8) Kwa hiyo, kwa wengine, madaraka ya jamaa yanaweza kufanya upainia usiwezekane kwa wakati huu. Hali za namna tofauti zinahusu afya na umri. Hayo ni mambo ya kuchunguzwa ingawa kuna wengi wenye afya mbaya au walio wazee-wazee, wanaotumikia wakiwa mapainia.

10. Imani inahusikaje katika kupainia?

10 Vilevile, lazima askari huyo painia, awe na imani thabiti, kwa maana kutumikia katika cheo hicho si rahisi. Paulo anahusianisha moja kwa moja imani na utangazaji wa Mkristo wa ile kweli mbele ya watu wengi, kwa kuandika hivi: “Piga vita vile vizuri vya imani; shika uzima ule wa milele ulioitiwa, ukaungama maungamo mazuri mbele ya mashahidi wengi.” (1 Timotheo 6:12) Ingawa imani inatakiwa kwa wote waliomo ndani ya jeshi la Mungu, kuna tofauti kati ya kuonyesha imani katika kazi ya kuhubiri pindi kwa pindi na kufanya hivyo saa nyingi kila siku. Hata hivyo, twaweza kusema kwamba kuzungumza mara nyingi ile kweli na wengine kunaweza kuongeza imani ya mtu.​—2 Wathesalonike 1:3.

11. (a) Wakristo wote wanatoa dhabihu ya namna gani? (b) Huenda dhabihu gani nyingine ya ziada ikahitajiwa katika kupainia?

11 Vilevile, kuna jambo lile linalohusu kutoa dhabihu. Katika maana moja utumishi wote unaotolewa kwa Mungu kwa usafi na unyofu unaweza kuonwa kuwa ni kumtolea yeye dhabihu. (Waebrania 13:15, NW) Kwa hiyo, kupainia kwa kusudi linalofaa—kumsifu Mungu na kuwasaidia watu wengine watoke katika utumwa wa taratibu ya Shetani—kwa hakika hiyo ni dhabihu bora. Hata hivyo kupainia kunataka dhabihu ya namna nyingine. Wakati ambao Mkristo alikuwa akiutumia kufuatia mno mambo ya kibinafsi lazima uelekezwe kwenye kuhubiri na kufundisha anapokuwa akipainia. Wakati uliokuwa ukitumiwa kujipatia na kulipia vitu vya kimwili huenda sasa ukapunguzwa. Ndiyo, kujinyima kunatakiwa katika kupainia. Maelfu ya mapainia wameridhika na kupunguza hali yao ya kiuchumi na ya kuwa na mali—kwa kufanya kazi ya kimwili siku moja, mbili au pengine tatu katika juma ili wajiruzuku na bado wawe na wakati wa kutosha kwa ajili ya huduma yao.​—2 Timotheo 2:4.

KUFANYA ZAIDI—KAMA WALIVYOFANYA WANAZIRI

12. Kwa sababu gani wengine wanapainia, na Waisraeli fulani wa kale waliwezaje kufanya zaidi katika ibada yao?

12 Wengi ambao wamechukua utumishi wa painia wamesukumwa na tamaa ya kutaka kufanya zaidi. Hiyo si tamaa ya kutaka kushindana wala yenye kiburi ya kutaka kufanya zaidi ya ndugu na dada zao Wakristo, bali ni tamaa ya kutaka kufanya zaidi katika kuonyesha upendo kwa Yehova na jirani zao. (Mathayo 22:37-39) Wanaziri ni mfano wenye kuvutia katika Biblia. Wanaume na wanawake Waisraeli wa kale wangeweza kujitolea wawe Wanaziri, jina ambalo linatokana na neno la Kiebrania na·zirʹ, ambalo maana yake ni aliye wakf, aliyetengwa, aliyetofautishwa. Ili kuwa Mnaziri mtu alitakiwa atoe ahadi nzito, walakini hatupaswi kulinganisha jambo hilo na uamuzi wa Mkristo wa kutaka kupainia, kwa maana kufanya hivyo hakutii kutoa ahadi nzito inayoambatana na madaraka ya utawa. Hata hivyo, tunaweza kufikiria mifanano fulani yenye masomo mazuri kwetu kati ya Wanaziri na mapainia.

13, 14. (a) Eleza kizuizi kimoja walichokuwa nacho Wanaziri. (b) Kuna ufanani gani na mapainia?

13 Mwisraeli ambaye alijitolea kutumikia akiwa Mnaziri alikubali vizuizi fulani vilivyosaidia kukazia mgawo wake wa ‘kutengwa’ au wa ‘kutofautishwa’ katika kumwabudu Yehova. Kizuizi kimoja kilihusu chakula na vinywaji, kama inavyosimuliwa katika Hesabu 6:3, 4 (NW). Mnaziri hangeweza kunywa vinywaji vyenye kulevya au mazao ya mzabibu. (Zaburi 104:15) Ingawa kulikuwako kadiri fulani ya kujinyima, hakuna chakula kinachohitajiwa sana na mwili alichokatazwa. Kwa hiyo kizuizi hicho hakikuleta taabu.

14 Mapainia wanaofanikiwa hawawekei maisha yao mkazo juu ya mambo ya kimwili kama chakula au vitu vya anasa, bali mkazo unakuwa juu ya utumishi wao unaomletea Mungu sifa. Hilo ni jambo la lazima ili kupata furaha yenye kutia mizizi sana na yenye kudumu, furaha ambayo inatafutwa sana bila kupatikana na watu wengi ambao kwa maoni ya kimwili huenda wakaonekana kuwa wenye maisha “bora.” (Linganisha Luka 12:16-21.) Kwa kuishi maisha yasiyo na mambo mengi au yenye mambo mepesi ya kimwili huenda vilevile kukaleta faida ambazo mara nyingi zinapuzwa kwa urahisi. Wataalamu wa afya wanaripoti juu ya hatari nyingi za kula na kunywa vitu vinavyomnenefya sana mtu. Walakini painia ambaye kwa kawaida anakula chakula kisicho na vitu vingi vya kunenefya, ingawa kimesawazika na ni chenye kulisha mwili, na anayeunganisha jambo hilo pamoja na kutembea kwingi katika kuhubiri kwake kwa kwenda nyumba kwa nyumba, yaelekea atakuwa na afya bora. Watu wenye nyumba kubwa, vifaa vya karibuni sana, na mali nyingine nyingi, wanajua kwamba vitu hivyo vinaleta “maumivu ya kichwa” yenye kurudi-rudi, au matatizo. Mifanano kati ya Hesabu 6:3, 4 na upainia yastahili kufikiriwa nasi.

15. Kizuizi kinachohusu nywele za Wanaziri kinatoa kielelezo gani?

15 Kizuizi cha pili cha Wanaziri kilikuwa kwamba hawangeweza kukata nywele za vichwa vyao. (Hesabu 6:5) Nywele zao ndefu zingewezesha wengine wawatambue. Baadaye Paulo alieleza kwamba nywele ndefu za mwanamke Mkristo ni kumbukumbu la hali yake ya kuwa mtiifu. (1 Wakorintho 11:3-15) Kwa kukumbuka nywele ndefu za Mnaziri, je! hatuwezi kukubali kwamba ndugu au dada Mkristo anayejitolea apainie anaonyesha, kwa kadiri kubwa, kujitiisha kwake kwa Yehova Mungu? Mapendezi mengi ya kibinafsi yanawekwa kando au kuchukua mahali pa pili ili huduma hiyo iangaliwe kwanza. Painia anajifunza kumtegemea Mungu, na kujitiisha chini ya Mungu.

16. Tunaweza kuthamini nini kutokana na hali ya Wanaziri kuhusiana na maiti?

16 Takwa la mwisho kwa Wanaziri lilikuwa kwamba hawakupaswa kugusa mwili wo wote uliokufa, hata kama mtu wa ukoo wa karibu kama mzazi angekufa. (Hesabu 6:6, 7) Kwa njia hiyo Mnaziri angeendelea kuwa mtakatifu na safi, asiyechafuliwa. (Linganisha takwa kwa kuhani mkuu katika Mambo ya Walawi 21:10, 11.) Leo hakuna Mkristo ye yote, kutia painia ye yote, anayekatazwa kufanya mipango ya maziko au kuhudhuria maziko ya mtu wa ukoo wa karibu. Walakini, kama ilivyokuwa kwa Wanaziri, mapainia wanataka kuepuka zoea lo lote au mwendo usiofaa unaoweza kuwafanya wasistahili. Wanataka kuwa mfano mwema. Na ikiwa painia, anayeipenda jamaa yake, yu katika mgawo wa mbali na kwa hiyo hawezi kuwatembelea kama ambavyo ingaliwezekana kama angalikuwa karibu anapata uradhi kwa kujua kwamba Yehova anatambua kujinyima kwake kwa njia hiyo.

17. Kwa sababu gani kuwa Mnaziri hakukuwa sherehe fulani tu? Namna gani kupainia?

17 Biblia inaonyesha kwamba Mwisraeli aliyekuwa Mnaziri hakuwa akifanya tu sherehe fulani ya kidini. Mahali pake, yeye alikuwa akichukua njia ya maisha ya maana, yenye kuridhisha, kwa maana Mungu alisema mtu wa namna hiyo ‘aliishi kama Mnaziri kwa Yehova.’ (Hesabu 6:2, NW) Vivyo hivyo, utumishi wa painia leo ni njia ya maisha na ni yenye kufurahisha!

‘JE! MIMI NINAWEZA KUPAINIA?’

18. Sote tunapaswa kuuliza ulizo gani? Kwa sababu gani?

18 Wakristo wote wameungana katika kumwabudu Mungu. Sisi ni jeshi moja la wapiganaji kwa ajili ya ile kweli. Inapasa iwe tamaa yetu kufanya yote tuwezayo katika vita hiyo. Ni tamaa yetu kufanya yote tuwezayo. Kwa hiyo, kila mmoja wetu anaweza kujiuliza ulizo hili la wakati unaofaa: ‘Je! mimi ninaweza kutumikia nikiwa painia?’ Katika kufikiria hilo, makala inayofuata itakusaidia uone namna Yehova anavyoweza kukutegemeza ikiwa unaweza kushiriki katika huduma ya painia.

[Maelezo ya Chini]

a Kitabu Webster’s Third New International Dictionary chini ya “painia,” kinasema hivi juu ya ufafanuzi mmoja: “mfanyi kazi wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova.”

JE! UMEKAZA AKILINI  . . .

◻ Kwa sababu gani wahudumu wa wakati wote kwa kufaa wanaitwa mapainia?

◻ Kwa sababu gani Biblia inawafananisha Wakristo na askari?

◻ Mambo unayopaswa kufikiria ili uwe painia?

◻ Jinsi Wanaziri wanavyotoa mfano mwema kuhusu mapainia?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Ni kwa sababu gani kwa kufaa Wakristo wanafananishwa na askari hodari?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kutumikia kama painia kunawezaje kuleta furaha na afya?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki