Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 8/15 kur. 9-10
  • Ni Nani Peke Yake Aliye Mshikamanifu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Nani Peke Yake Aliye Mshikamanifu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ushikamanifu kwa Kitu Gani?
  • “Wewe Peke Yako Ni Mwaminifu-Mshikamanifu”
    Mkaribie Yehova
  • Watazame Wale Waaminifu-Washikamanifu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Kukabili Mtihani wa Uaminifu-Mshikamanifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Ushikamanifu Kwa “Ufalme wa Bwana Wetu na wa Kristo Wake”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 8/15 kur. 9-10

Ni Nani Peke Yake Aliye Mshikamanifu?

Habari zilizo katika makala hii na katika makala mbili zinazofuata za mafunzo zilitolewa siku ya kwanza ya “Ushikamanifu kwa Ufalme” Kusanyiko la Wilaya la Mashahidi wa Yehova. Makusanyiko hayo ya Kikristo, yaliyofanywa sehemu zote za kaskazini na kusini ya ikweta muda wa miezi kadha iliyopita, yamehudhuriwa na watu zaidi ya 3,028,796, na 33,627 walibatizwa. Huu ni wakati unaofaa kurudia kujikumbusha chakula hiki kizuri cha kiroho, kwa maana matayarisho yanaendelea kufanywa ili kuwe na “karamu” nyingine nono kwenye “Kwali ya Ufalme” Makusanyiko ya Wilaya yanayokuja.

MTU aliye wa kutokeza zaidi katika ulimwengu mkubwa wote, wa juu na chini, mwenye sifa ya ushikamanifu, ndiye Muumba mwenyewe! Viumbe vyake vyote vyenye akili vimeipata sifa hiyo kwake. Watu wanaouthamini sana ushikamanifu wanaweza kumwomba Yeye awaonyeshe ushikamanifu nyakati za shida. Ndiyo sababu mtumishi wa Abrahamu, mzee wa ukoo na babu ya wafalme, alimwomba sana Yehova Mungu aliyekuwa bwana wake amwonyeshe upendo wake mshikamanifu, bila ya mtumishi huyo kufanya kimbelembele. (Mwanzo 24:14) Alipokuwa bado akingoja kuwa mfalme juu ya Israeli, Daudi mzao wa Abrahamu, alimwambia Yehova maneno yanayofuata katika zaburi moja, kulingana na mambo aliyojionea mwenyewe: “Kwa mtu mshikamanifu wewe utatenda kwa ushikamanifu.” (2 Samweli 22:26, NW; Zaburi 18:25, NW) Vilevile, nabii Musa, aliyekuwa wakili wa Mfalme wa kimbingu, Yehova, katika taifa la Israeli, alimtukuza Yehova Mungu kuwa mwenye sifa ya ushikamanifu, wakati alipokuwa akilibariki taifa la kikuhani la Lawi na kusema:

“Thumimu yako na Urimu yako vina [mshikamanifu] wako [Lawi], uliyemjaribu huko Masa; ukateta naye kwenye maji ya Meriba. Aliyemtaja baba yake na mama yake, mimi sikumwona; wala nduguze hakuwakubali; wala hakuwajua watoto wake mwenyewe; maana [Walawi] wameliangalia neno lako, wamelishika agano lako.”​—Kumbukumbu la Torati 33:4, 5, 8, 9.

Kama Musa angalikuwako, bila shaka nabii huyo angaliweza kujiunga na wenye kuimba wimbo uliotungwa miaka zaidi ya 1,600 baadaye, unaoitwa “ule wimbo wa Musa aliye mtumwa wa Mungu na ule wimbo wa Mwana-kondoo [Yesu Kristo],” ambao una maneno haya: “Kazi zako ni za haki na za kweli, Mfalme wa umilele. Ni nani ambaye kweli hatakuogopa wewe, Yehova, na kutukuza jina lako, kwa sababu wewe peke yako u mshikamanifu? Kwa maana mataifa yote watakuja na kuabudu mbele zako, kwa sababu amri zako zimeonyeshwa wazi.”​—Ufunuo 15:1-4, NW.

Daudi mtunga zaburi alisema ivyo hivyo juu ya ubora wa sifa hizo za kimungu, kwa maana yeye aliandika hivi: “Yehova ni mwenye haki katika njia zake zote na ni mshikamanifu katika kazi zake zote.” (Zaburi 145:17, NW) Kwa kuwa Yehova ndiye Mwamuzi Mkubwa Zaidi, yeye ataishughulikia kesi ya wale wanaomwabudu na kumtumikia, sawa na vile malaika alivyomwambia: “Wewe, Uliyeko sasa na uliyekuwako zamani, Wewe uliye mshikamanifu, kwa sababu umeyafanya maamuzi haya.”​—Ufunuo 16:4, 5, NW.

Katika lugha ya nabii Musa na Daudi mtunga zaburi, neno la Kiebrania la ushikamanifu tunalolizungumza lina wazo la fadhili, la kuwa mwenye fadhili kwa upendo. Watafsiri wengine wa Biblia wanapendelea zaidi kulitafsiri neno hilo la Kiebrania (hhesʹed) kuwa “fadhili za upendo.” Tunakuwa na maoni yenye fadhili tunapouona ushikamanifu kuwa fadhili, kuwa jambo la kukumbuka mambo fulani yasiyopasa kusahauliwa hata kidogo, hivi kwamba ushikamanifu unakuwa si jambo lenye ubaridi, jambo linalotegemea kufuata sheria tu au kutumia haki ya hukumu tu. Hiyo ni sifa inayokuwa ndani ya mtu binafsi, nayo inaonyeshwa kwa sababu ya kuchochewa na upendo na kuthamini.

Tunakumbuka jinsi mtawala fulani katika nchi ya Kanaani alivyoona kwamba Mungu wa kweli alikuwa pamoja na Abrahamu alipokuwa mgeni wa muda huko, basi akamjia Abrahamu akamwambia: “Basi sasa uniapie kwa Mungu, ya kuwa hutanitenda hila, wala mwanangu, wala mjukuu wangu, lakini kwa kadiri ya fadhili [ya ushikamanifu] niliyokutendea utanitendea mimi, na nchi hii ambayo umetembea ndani yake [ukiwa mgeni].” (Mwanzo 21:22, 23) Tunakumbuka pia jinsi Eliezeri alivyomtolea sala Yehova Mungu wakati Abrahamu alipomtuma baadaye huyo mtumishi wake akamtafutie mke Isaka mwanawe mpendwa, akisema: “Basi huyu [msichana niliyesimulia sifa zake] na awe ndiye uliyemchagulia mtumishi wako Isaka; na kwa hayo nitajua ya kuwa umemfadhili [kwa ushikamanifu] bwana wangu.”​—Mwanzo 24:14.

Ushikamanifu kwa Kitu Gani?

Abrahamu mzee wa ukoo alitimiza ahadi aliyomwapia mtawala yule katika nchi ya Kanaani, naye Yehova Mungu akafanya alivyoombwa na Eliezeri, mtumishi wa Abrahamu, katika sala, akampa Isaka mke aliyemfaa. Walakini, juu ya mambo mengine yote, Mungu Mwenye Nguvu Zote, Yehova, ni mshikamanifu kwa kitu gani? Ni kwa ufalme wake, uufalme wake mwenyewe, kwa maana kwa kustahili yeye ndiye Mwenye Enzi Kuu aliye juu ya ulimwengu mkubwa aliouumba, wa juu na chini. Yeye hawezi kujikana awe mwingine. Alipata kuwa Mfalme juu ya ukoo mashuhuri wa wazao wa Abrahamu, lile taifa la Israeli, hasa wakati alipowakomboa utumwani katika nchi ya Misri akawaingiza katika Nchi ya Ahadi mwaka wa 1467 K.W.K. akilitimiza agano lisilofutika alilolifanya pamoja na Abrahamu. Halafu Yehova aliwapa mawakili wake wenye kuonekana kwa miaka 350, nao wakawa waamuzi mpaka siku za Mwamuzi Samweli. Wakati Hana, mama ya Samweli, alipomtoa afanye utumishi mtakatifu wa Mungu kwenye hema yake takatifu huko Shilo, mama huyo alitamka unabii wenye kuonyesha kungekuwa baadaye na mfalme aonekanaye wa kulitawala taifa la Israeli akisema: “[Yehova] ataihukumu miisho ya dunia; naye atampa mfalme wake nguvu, na kuitukuza pembe ya [mtiwa mafuta] wake.”​—1 Samweli 2:10.

Siku hizo za Mwamuzi Samweli Waisraeli waliomba wabadilishiwe serikali yenye kuwatawala. Walimdai Mwamuzi Samweli wakisema: “Tufanyie mfalme atuamue.” Jambo hilo halikumchukiza Samweli tu, bali na Yehova Mungu. Yeye alimwambia Samweli hivi: “Hawakukukataa wewe [usiwe mwamuzi], bali wamenikataa mimi, ili nisiwe mfalme juu yao,” (1 Samweli 8:1-7) Mungu aliwaruhusu wawe na mfalme wa kibinadamu mwenye kuonekana, Sauli mwana wa Kishi. Hata hivyo, Mungu hakukataa kuendelea kuwa na enzi kuu juu yao. Kulingana na kusudi la agano lake, Mungu alikuwa mshikamanifu kwa uufalme wake usioonekana wa kimbingu, juu ya watu wake aliowachagua. Mfalme wao wa pili wa kibinadamu akawa Daudi, aliyekuwa hapo kwanza mchungaji, mwana wa Yese wa Bethlehemu, mji wa Yudea.

Ushikamanifu ulionekana wazi kwa njia gani wakati wa uufalme wa Daudi? Jambo hilo lilikuwa mfano wa kitu gani? Nalo ulizo la ushikamanifu linatuhusu sisi leo kwa njia gani? Makala inayofuata itajibu maulizo hayo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki