Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 8/15 kur. 11-16
  • Ushikamanifu Kwa “Ufalme wa Bwana Wetu na wa Kristo Wake”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ushikamanifu Kwa “Ufalme wa Bwana Wetu na wa Kristo Wake”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mfalme “Ambaye ni Haki Yake”
  • Wakati wa Hukumu kwa Washikamanifu
  • “Kondoo Wengine” Washikamanifu
  • Je! Wewe ni Mshikamanifu kwa Mfalme Mpya wa Dunia?
    Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
  • “Wewe Peke Yako Ni Mwaminifu-Mshikamanifu”
    Mkaribie Yehova
  • Watazame Wale Waaminifu-Washikamanifu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Mchezo wa Kuigiza wa Kusanyiko
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 8/15 kur. 11-16

Ushikamanifu Kwa “Ufalme wa Bwana Wetu na wa Kristo Wake”

“Mimi nitakuwa na shauku yenye upendo kwa wewe, O Yehova nguvu yangu. Kwa mtu mshikamanifu wewe utatenda kwa ushikamanifu.”​—Zaburi 18:1, 25, NW.

1. (a) Daudi aliuitikia ushikamanifu wa Yehova kwa njia gani? (b) Daudi alikubali jambo gani hata alipokuwa mzee?

KWA USHIKAMANIFU Yehova Ndiye aliyemwinua Daudi akalie kiti cha kifalme ili kutawala Israeli wote. Jambo hilo lilitukia mwaka wa 1070 K.W.K. Daudi aliyetawazwa alizithamini hizo fadhili za upendo, akamtambua Mungu daima kuwa Mfalme wake, na hivyo akamtambua kuwa ndiye Mfalme Mkubwa Zaidi juu ya Israeli. Akimtaja Masihi hasa, mzao wa mbali wa Daudi, Mungu alisema hivi: “Nami nimemweka mfalme wangu juu ya Sayuni, mlima wangu mtakatifu.” (Zaburi 2:6) Akimtambua (akimkubali) Mtawala halisi wa kimbingu, Daudi alisema: “Uisikie sauti ya kilio changu, Ee Mfalme wangu na Mungu wangu, kwa maana Wewe ndiwe nikuombaye. [Yehova], asubuhi utaisikia sauti yangu.” (Zaburi 5:1-3) Wakati Daudi alipompokeza kiti cha kifalme Sulemani mwanawe katika siku za uzee wake, Daudi alimtolea Mungu sala mbele ya kusanyiko lote la Israeli akasema: “Ufalme ni wako, Ee [ Yehova ], nawe umetukuzwa, u mkuu juu ya vitu vyote. Utajiri na heshima hutoka kwako wewe, nawe watawala juu ya vyote.”​—1 Mambo ya Nyakati 29:11, 12.

2. (a) Ni ulizo gani la vizazi vingi ambalo tunapaswa tulikubali leo? (b) Ni ulizo gani la maana sana ambalo lazima kila mmoja wetu ajibu mwenyewe sasa?

2 Uhakika huo wa maana sana uliokubaliwa na Mfalme Daudi mbele ya watu wengi zamani za kale ndio hata sisi viumbe vya kibinadamu, tusio wafalme, tunapaswa kuukubali bila kuona aibu. Biblia Takatifu imefundisha tangu kale lile ulizo la kwamba Yehova Mungu ndiye mwenye utawala au enzi kuu juu ya ulimwengu mkubwa wa juu na chini. Hiyo ndiyo kesi ya kisheria, ya kimungu, iliyo mbele ya makundi yote ya watu na mataifa yote ili ikatwe kwa mara ya mwisho kabisa. Katika hizi siku za mwisho ndipo ulizo hili litapasa kuamuliwa kabisa mbele ya zote mbingu na dunia. Atakayeshinda na kuondolewa lawama ni Yehova, athibitishe kabisa ana enzi kuu na uufalme. Ulizo la maana lililo mbele yetu ili liamuliwe ni hili, Ni nani sasa atakayedumisha ushikamanifu kwa ufalme wa Yehova? Msimamo wetu wa sasa kuhusu jambo hilo ndio utakaoamua kama tutapata uzima wa milele au tutapatwa na uharibifu wa milele!

3. Ni msiba gani mkubwa uliotukia mwaka wa 607 K.W.K., lakini kwa sababu gani haukuonyesha kwamba Yehova si mshikamanifu?

3 Walakini, je! Yehova Mungu aliukana ufalme wake huko nyuma mwaka 607 K.W.K.? Mbona tuulize ulizo hilo? Kwa sababu mwaka huo aliiruhusu Milki ya Kibabeli ikiongozwa na Nebukadreza iliharibu jiji la Yerusalemu na hekalu lake pia, kisha ikaupindua ufalme wa Wayahudi mpaka leo hii. Ni kweli kwamba ndivyo ilivyotukia, lakini Mungu hakuukana uufalme wake au utawala wake kwa kuliruhusu jambo hilo litukie. Kusema kweli Yeye ndiye aliyeamuru kwamba Yerusalemu, jiji la kifalme, liharibiwe. Ingawa hivyo, hilo halikuwa tendo la kukosa ushikamanifu kwa ufalme wake msaidizi uliokuwa mfano wa ufalme mwingine kwa kutawala watu wake aliowachagua. Yeye alitenda tu kulingana na masharti yaliyokuwa yamewekwa katika agano alilolifanya pamoja na Israeli, ambalo liliongezwa kwenye agano la kale lililofanywa pamoja na Abrahamu. Kufikia mwaka huo wenye msiba wa 607 K.W.K., Yuda na mabaki ya Israeli walikuwa wamekuwa wavunjaji wabaya sana wa agano. Basi Mungu aliwachukulia hatua kulingana na masharti yaliyokuwa katika agano lake la Torati lililopatanishwa na Musa kwenye Mlima Sinai.

Mfalme “Ambaye ni Haki Yake”

4. Maneno ya Ezekieli 21:25-27 yaliyoongozwa na Mungu yanaonyeshaje kwamba Yehova ni mshikamanifu?

4 Kwa habari ya mfalme wa mwisho wa Yudea mwenye kukaa Yerusalemu, Mungu alimwongoza Ezekieli nabii wake (aliyekuwa amekwisha kuhamishiwa Babeli) aseme hivi: “Na wewe, Ewe mtu mwovu, uliyetiwa jeraha kiasi cha kukuua, mkuu wa Israeli, ambaye siku yako imekuja, katika wakati wa uovu wa mwisho; Bwana [Yehova] asema hivi; Kiondoe kilemba, ivue taji; haya hayatakuwa tena kama yalivyo; kikweze kilicho chini, kakishushe kilichoinuka. Nitakipindua, nitakipindua, nitakipindua; hiki nacho hakitakuwa tena, hata atakapokuja yeye ambaye ni haki’ yake [ya kisheria, NW]; nami nitampa.”​—Ezekieli 21:25-27.

5. (a) Kwa sababu gani kuharibiwa kwa ufalme kungekuwa kwa muda tu? (b) Jambo hilo lilithibitishwa namna gani miaka zaidi ya 600 baadaye?

5 Kulingana na maneno hayo Bwana Mungu Yehova bado alishikilia kwa imara mambo ya Ufalme. Kuharibiwa kwa ufalme wake msaidizi duniani kungekuwa kwa muda tu. Katika wakati wake unaofaa mtu fulani angekuja akiwa na haki ya kisheria ya kuuchukua uufalme wa Kimasihi, naye Bwana Mungu Yehova angempa huyo uufalme huo. Kabla wakati huo haujafika ilimpasa huyo angoje asiitumie haki ya kisheria ya kuwa mfalme. Kwa kuwa haki ya agano ilikuwa imekaa katika jamaa ya kifalme ya Daudi, ilikuwa lazima yule ambaye alipaswa kuja na ambaye angepewa uufalme awe ni mzao wa Mfalme Daudi mwaminifu. Agano hilo lilifanywa pamoja na Daudi ili kuwe na ufalme wa milele katika ukoo wa jamaa yake kwa sababu ya ushikamanifu wake kwa UufaIme wa milele wa Yehova. (2 Samweli 7:8-16) Zaidi ya karne sita baadaye, au katika mwaka wa 2 K.W.K., malaika aliyetumwa na Mungu alimtokea mzao wa kike wa Mfalme Daudi, akamwambia kwamba angekuwa ndiye mama ya mrithi wa Daudi ambaye aliahidiwa. Malaika aliendelea kusema: “[Yehova] Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake. Ataimiliki nyumba ya Yakobo hata milele, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho.” Jina lake alipaswa aitwe Yesu.​—Luka 1:32, 33; Mathayo 1:18-23.

6. (a) Yesu alikuwaje mrithi mwenye haki ya kuupata ufalme wa Daudi? (b) Kwa sababu gani huo ufalme uliongezeka ukaacha kuwa ufalme wa kidunia tu?

6 Alipozaliwa katika jiji alimozaliwa Daudi, yaani, Bethlehemu, Yesu Mwana wa Mungu aliyetoka mbinguni alikuwa mrithi wa kiasili wa ahadi ya agano la Ufalme ambayo Mungu alikuwa amemwahidi Daudi babu yake. Haki ya kuupata Ufalme ikawa yake kulingana na sheria na kulingana na asili ya kuzaliwa. Lakini wakati Yesu alipobatizwa na kutiwa mafuta kwa roho takatifu ya Mungu Baba yake wa kimbinguni, ufalme huo uliongezeka ukaacha kuwa serikali ya kidunia tu yenye kuitawala nyumba ya Yakobo au Israeli. Wakati huo yeye alizaliwa kwa roho ya Baba yake wa juu angani na hivyo akawa Mwana wa Mungu wa kiroho, mwenye kuwekewa uzima wa kimbingu. Basi alitiwa mafuta kwa roho ya Mungu na hivyo akawa ndiye Masihi, jina hilo la cheo likimaanisha Aliyetiwa Mafuta.​—Matendo 4:27; 10:38; Isaya 61:1-3.

7. (a) Kwa sababu gani Yesu hakuupokea ufalme wa Kimasihi moja kwa moja? (b) Kwa wakati huo, ni uufalme gani ambao wafuasi wake waliotiwa mafuta wangeukubali?

7 Kwa kuwa sasa ufalme ulikuwa wa kimbingu, Mungu hakumpa yeye ufalme huo alipokuwa hapa duniani, wala hakumpa mara tu alipokwisha kupaa na kurudi mbinguni. Ingawa alitambuliwa kuwa Mfalme juu ya kundi lake la kiroho la wanafunzi watiwa-mafuta waliopo duniani, alipaswa angojee mwisho wa yale ambayo Yesu mwenyewe aliyaita “majira ya Mataifa,” au, “nyakati zilizowekwa za mataifa” ndipo apewe ufalme huo wa Kimasihi.​—Wakolosai 1:13; Luka 21:24.

8. (a) “Nyakati zilizowekwa za mataifa” ni kipindi cha urefu gani, na ni matukio gani yenye maana kubwa yaliyoonekana kuonyesha kwamba nyakati hizo zilikuwa zimekwisha? (b) Ile “ishara” imekuwaje jambo la kuvuta macho, na ni sehemu gani ya ishara hiyo imekuwa yenye kuonekana wazi sana?

8 Hizo “nyakati zilizowekwa” zilikuwa zimekwisha kuanza mwaka 607 K.W.K. wakati jiji la Yerusalemu lilipoharibiwa mara ya kwanza na Wababeli na baadaye nchi ya Yudea ikaachwa utupu kabisa. Kulingana na kitabu cha unabii wa Danieli, sura ya 4, “nyakati” hizo zilipasa kuwa saba, zikiwa na jumla ya miaka 2,520. Kwa hiyo, kwa kuwa nyakati hizo zilianza wakati jiji la Yerusalemu lilipoachwa utupu kabisa pamoja na nchi ya Yuda na Benyamini mapema katika vuli ya mwaka 607 K.W.K., zingemalizika katika vuli ya mwaka 1914 W.K. Basi Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilitokea katika nusu ya mwisho ya mwaka 1914 kukiwa na kusudi fulani. Kwa njia hiyo unabii ule alioutoa Yesu juu ya “ishara” yenye kuonyesha “umalizio wa taratibu ya mambo” ulianza kutimizwa. (Mathayo sura 24, 25, NW; Marko sura ya 13; Luka sura ya 21) Tangu wakati huo “ishara” iliyotabiriwa imezidi kuwa wazi na yenye kuvuta sana akili nyakati zote. Alipokuwa akionyesha jambo ambalo lingeonekana wazi sana la “ishara” hiyo, Yesu alisema hivi: “Na habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”​—Mathayo 24:14, NW.

9, 10. (a) Kwa habari ya ulizo la ushikamanifu, sasa ulikuwa umefika wakati gani (b) Wakati huo watu wa kimbingu wasio washikamanifu walitupwa nje kwa njia gani, kisha kukawa na matokeo gani kwenye dunia yetu?

9 Ah, ndiyo, sasa ulifika wakati uliongojwa sana wa kumpa Mwana wa Mungu aliyetukuzwa mbinguni ufalme wa Daudi, kwa sababu yeye peke yake ndiye aliyekuwa na ‘haki ya kisheria’ ya kuupata kulingana na sheria ya Mungu iliyo bora kupita zote. Basi ilikuwa lazima vita itokee mbinguni. Kwa sababu gani?

10 Kwa sababu wakati huo yule Mfalme wa Kimasihi alianza kutawala, wakati wake ukawa umefika wa kuwaondosha mbinguni wapinzani wote wa ile serikali mpya, yaani, Shetani Ibilisi na malejioni (majeshi) yake ya mashetani. Hao walivurumishwa chini duniani, ambako taratibu ya mambo yenye kuongozwa na mashetani ilikuwa ingali imesimama. Majeshi maovu hayo ya kimalaika yamezuiwa milele yasizikanyage mbingu za Mungu wanakokaa malaika wake washikamanifu. Malaika hao waasi-walaaniwa wataendelea kuzuiwa hivyo kwenye ujirani wa dunia mpaka watakapofungwa katika shimo kubwa sana la kuzuiwa kabisa kabisa kwa muda wa miaka elfu moja. Hiyo “vita mbinguni” na matokeo yake imesimuliwa kiunabii katika sura ya 12 ya Ufunuo. Walipokwisha kuondoshwa mbinguni, ulitokea mshindo wa wimbo wa ushindi wa kimalaika: “Sasa kumekuwa wokovu, na nguvu, na ufalme wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo [Masihi] wake; kwa maana ametupwa chini mshitaki wa ndugu zetu, yeye awashitakiye mbele za Mungu wetu, mchana na usiku”! (Ufunuo 12:10) Tukio hilo lilikuwa na maana gani kwa wakaaji wa hii sayari ya kidunia? Kulitokea ole mwingi sana kwa wanadamu wote duniani!

Wakati wa Hukumu kwa Washikamanifu

11, 12. (a) Ni jaribu gani la ushikamanifu ambalo sasa linatukia? (b) Mahubiri ya ule Ufalme yanahusika namna gani? (c) Ni kwa njia gani huu ni wakati wa mavuno, na inaelekea kuwa malaika wanatumiwa kwa njia gani?

11 Wakati huu wa “ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu,” umekuwa kipindi cha kujaribu ushikamanifu wa watu—kuona kama wanaonyesha ushikamanifu kwa taratibu ya mambo ya Ibilisi iliyohukumiwa maangamizi au wanauonyesha ushikamanifu ufalme wa Mungu ambao sasa umekwisha kusimamishwa katika mbingu ukiwa mikononi mwa Yesu Kristo. (Ufunuo 12:12) Huu ni wakati ambao lazima wote wenye kujiita wanafunzi wa Kristo wahukumiwe ionekane ni kwa kadiri gani wanavyouonyesha ushikamanifu ufalme huo uliosimamishwa. Je! watakuwa wahubiri wenye joto wa hizo habari njema za ufalme “katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote”? Kipindi hiki cha katikati kinafananishwa pia na wakati wa mavuno wa kutenganisha Wakristo wa kweli na wale wa uongo. Ni sawa tu na Yesu alivyotabiri katika mfano wake wa ngano na magugu (au kwekwe): “Mavuno ni mwisho wa taratibu ya mambo, nao wavunaji ni malaika.” (Mathayo 13:39, NW) Inaelekea kuwa, malaika hao ndio wanaotumiwa na Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu kuitimiza amri yake iliyoonyeshwa katika Zaburi 50:5, NW: “Nikusanyie washikamanifu wangu uwalete nilipo, wale wanaokata kauli ya agano langu kuhusu dhabihu [Kiebrania: wale wanaokata agano langu].”

12 Mungu anawaambia hivi watu wajiitao Wakristo wanaoshindwa kulipita lile jaribu la kuonyesha ushikamanifu kwa ule Ufalme: “Una haki gani wewe kutaja-taja sheria zangu za uongozi, hata uweze kuchukua agano langu katika kinywa chako?”​—Zaburi 50:16, NW.

13, 14. (a) Eleza ni “agano” gani linalotajwa na Zaburi 50:5, 16? (b) Lazima Wakristo waliotiwa mafuta wawe “washikamanifu” kwa maagano gani mawili?

13 “Agano” linalotajwa katika mistari iliyotangulia (5, 16) si agano la kibinafsi liliofanywa na washikamanifu kuhusu dhabihu ya kibinafsi yenye kutolewa na mtu binafsi. Bali, ni agano la taifa zima. Agano la Torati ya Musa lililofanywa pamoja na taifa la Israeli kwenye Mlima Sinai katika Uarabu lilitumiwa kwa unabii kulifananisha agano jipya lililofanywa pamoja na “taifa takatifu” la Israeli wa kiroho kupitia yule Musa Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo, akiwa ndiye mpatanishi (Yeremia 31:31-34) Katika usiku wa Siku ya Kupitwa ya mwaka 33 W.K. Yesu alikianzisha Kijio cha Bwana, au Chakula cha Jioni, kisha akasema: “Kikombe hiki kinamaanisha lile agano jipya kwa uwezo wa damu yangu, ambayo itamwagwa chini kwa ajili yenu.” (Luka 22:20, NW) Kwa hiyo agano jipya lilifanywa liwe halali (lifae) na damu ya dhabihu iliyomwagika wakati wa kufa kwa Yesu Kristo. Wale washikamanifu” ambao Yesu anawaingiza katika agano jipya wanaingizwa katika “agano . .. kwa ajili ya ufalme.” (Luka 22:28-30, NW; Mathayo 26:29; Marko 14:25; Zaburi 116:15) Halafu?

14 Ni lazima Wakristo ambao wameingizwa katika lile agano jipya, ambalo ni “agano . . . kuhusu dhabihu,” wawe washikamanifu kwalo, kisha wawe pia washikamanifu kwa lile “agano . . . kwa ajili ya ufalme.” Hao ni Waisraeli wa kiroho Israeli wa Mungu.”​—Wagalatia 6:16.

15. Ni kwa njia gani mbalimbali lazima Waisraeli wa kiroho wajithibitishe kuwa “washikamanifu”?

15 Wakati wa huu “mwisho wa taratibu ya mambo ‘ mabaki ya hao Waisraeli wa kiroho wangali duniani. Hasa wao ndio wenye wajibu wa kutenda kupatana na unabii huu wa Yesu: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14, NW) Wao hawawezi kuuepuka wajibu huo, ikiwa wanataka kuwa washikamanifu kwa “ufalame wa Bwana wetu [Yehova] na wa Kristo wake.” (Ufunuo 11:15) Hawawezi kuwa sehemu ya hii taratibu ya mambo iliyohukumiwa maangamizi pamoja na siasa zayo, ubiashara wayo wa kichoyo na dini yayo ya uongo. Wakristo waliotiwa mafuta wanaisali kwa shauku yenye bidii ile sala ambayo Bwana wao aliwafundisha: Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, Ufalme wako uje, Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Badala ya kuzishiriki siasa za hii taratibu ya mambo iliyogawanyika-gawanyika, lazima wao walitende bila kuyumba-yumba lile alilolisema Bwana wao, yule “Mfalme wa wafalme na Bwana wa Mabwana,” yaani: “Basi endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na haki yake, na mambo yote haya mengine mtaongezewa.” (Ufunuo 19:16; Mathayo 6:33, NW) Kwa njia hiyo tu ndivyo wanavyoweza kujithibitisha kwamba wao ndio “washikamanifu” wa Israeli wa kiroho ambaye ‘amefanya agano pamoja na Yehova Mungu kuhusu dhabihu,’ dhabihu ya Yesu, aliyelipatanisha agano jipya.

“Kondoo Wengine” Washikamanifu

16. Vifungu vya Maandiko vilivyotajwa hapa vinaonyeshaje kwamba kuna jamii nyingine ya watu wengi walio washikamanifu?

16 Ile jamii ya watu waliojiweka wakf na kubatizwa, iliyotangulia kufananishwa na lile “kundi kubwa la watu waliochangamana” na Waisraeli wakati wa kutoka Misri na wakati agano la Torati lilipokuwa likifanywa kwenye Mlima Sinai, lazima ithibitishe leo kwamba ina ushikamanifu wa kiasi icho hicho. (Kutoka 12:38; Hesabu 11:4) Jamii hiyo ni sawa na “mkutano mkubwa” anaousimulia mtume Yohana katika Ufunuo 7:9-17. Katika mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi wao wanaonyeshwa pia kuwa “kondoo” wanaowatendea mema ndugu za kiroho za Mfalme Yesu Kristo, tangu alipoanza kutawala mwaka wa 1914.​—Mathayo 24:3; 25:31-46.

17. (a) Huu “mkutano mkubwa” ni sehemu ya nini, nao unakuwa “kundi moja” pamoja na nani? (b) Ni kwa njia gani wanaweza ‘kujibariki wenyewe pasipo shaka’? (Mwanzo 22:15-18, NW)

17 Washikamanifu hao ni wa wale “kondoo wengine” ambao Yesu alisema hawakuwa wa “zizi hili [la Kiabrahamu],” zizi ambamo “kundi dogo” la watu 144,000 limo. Hata hivyo huu “mkutano mkubwa” wa washikamanifu unakuwa “kundi moja” pamoja na wale walio katika “zizi” hilo kwa kushirikishwa karibu-karibu na warithi hao wa ufalme wa Baba yao wa kimbingu. (Yohana 10:16; Luka 12:32) Ili wao waweze kubaki katika hilo “kundi moja” na wale “washikamanifu” walio katika lile agano jipya pamoja na Yehova Mungu kuhusu dhabihu ya Kristo, lazima wao pia waonyeshe wana ushikamanifu kwa ufalme wa Bwana Mungu wetu Yehova na wa Kristo wake.

18. (a) Thawabu wanayopewa sasa wale wanaojithibitisha kuwa washikamanifu ni nini? (b) Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunauthamini ushikamanifu wa Yehova kwetu sisi?

18 Thawabu wanayoipata kwa sasa wale wanaojithibitisha kuwa washikamanifu ni kubwa. Kwa sababu Mfalme Daudi wa kale alimthamini Yehova Mungu aliye Mfalme wa kimbingu, yeye alimwambia hivi: “Kwa mtu mshikamanifu wewe utatenda kwa ushikamanifu.” (Zaburi 18:25, NW; 2 Samweli 22:26, NW) Tena Daudi alisema: “Yehova ni mpenda haki ya hukumu, naye hatawaacha washikamanifu wake.” (Zaburi 37:28, NW) Mithali 2:8 inatuhakikishia hivi, katika tafsiri ya New World: “Yeye atailinda njia yenyewe ya washikamanifu wake.” Aha, kumbe, Yehova ndiye mwenye ushikamanifu ulio mkamilifu, naye Kristo wake anamwiga kwa ukamilifu katika kuwa na sifa hiyo. Tunapouthamini ushikamanifu ambao Mungu ametuonyesha kupitia Kristo, acheni sisi tuthibitishe katika hii siku ya hukumu kwamba tuna ushikamanifu kwa Yehova na kwa ufalme wake uliosimamishwa ukiwa mikononi mwa Yesu Kristo ambaye ndiye Mwana wake aliye mshikamanifu zaidi!

KWA KURUDIA, USHIKAMANIFU UNAONYESHWAJE KATIKA—

◻ Tendo la Daudi la kumkubali Yehova kuwa Mfalme?

◻ Kufikiliza hukumu kwa Yehova juu ya jiji la Yerusalemu lisilo na imani?

◻ Upaji wa Mungu wa ufalme wa Daudi kwa Mwanawe mwaka wa 1914?

◻ Tendo la Mfalme wa Kimasihi la kufanya vita mbinguni?

◻ Utendaji wa leo wa mabaki watiwa-mafuta?

◻ Uungaji-mkono ambao “mkutano mkubwa”unawatolea mabaki?

[Picha katika ukurasa wa 14]

Majeshi yote ya kimalaika yasiyokuwa na ushikamanifu kwa Mungu yaliondoshwa mbinguni na kutupwa nje wakati Mwana mshikamanifu wa Mungu alipoanza kutawala

[Picha katika ukurasa wa 15]

Ushikamanifu kwa Ufalme unamtaka mtu awe mhubiri mwenye bidii nyingi kwa kueleza wengine habari za Ufalme huo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki