Maswali kutoka kwa Wasomaji
◼ Yesu alikuwa na maana gani aliposema: “Taa ya mwili ni jicho; basi jicho lako likiwa safi, mwili wako wote utakuwa na nuru”?
Wengine wameshikilia maoni ya kwamba maneno hayo yaliyo kwenye Mathayo 6:22 yana maana inayohusiana na afya au tiba, kama kwamba kutazama jicho hasa ndiyo njia ya kujua kama mwili una magonjwa au udhaifu mbalimbali wa kimwili. Walakini, maoni hayo hayalingani na habari zinazouzunguka mstari huo. Hapo Yesu alikuwa ndiyo kwanza amalize kutoa onyo juu ya ‘kuweka hazina duniani.’ Halafu baada ya kusema maneno hayo yanayohusu “jicho,” akahimiza watu watumikie Mungu badala ya mali.—Mathayo 6:19-24.
Ni wazi kwamba Yesu alimaanisha kwamba wanafunzi wake waendelee kuwa na jicho “safi,” yaani, linaloelekezwa kwa unyofu wa moyo juu ya jambo moja badala ya kuvutwa litazame kando na mambo kama utajiri. Mkristo anayekaza fikira juu ya kufanya mapenzi ya Mungu ‘ni mwenye nuru,’ kwa maana anaangazia wengine nuru yake, na kufanya hivyo kunaletea Mungu utukufu.