Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 1/15 kur. 3-7
  • ‘Mrudieni Mchungaji wa Nafsi Zenu’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Mrudieni Mchungaji wa Nafsi Zenu’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mfano wa Mwana Mpotevu
  • Peke Yao Katika Nchi ya Mbali
  • “Alirudiwa na Fahamu Zake”
  • Je! Mimi Nimepita Kiasi Nisiweze Kurudi?
  • ‘Usiogope. Naam, Nitakusaidia’
  • “Yehova, Mungu Mwenye Rehema na Neema”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Wasaidieni Warudi Haraka!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Kupokea kwa Uchangamshi Wale Wanaorudi
    Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
  • “Nirudieni”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 1/15 kur. 3-7

‘Mrudieni Mchungaji wa Nafsi Zenu’

MIFANO miwili ya Yesu inayochangamsha moyo inaeleza vile Mungu anavyoonyesha hangaiko jingi kwa wale ambao wangali ni watu wake lakini wameiacha njia. Ebu wazia huzuni yenye kumsumbua sana mchungaji anayeacha kundi la kondoo 99 na kutafuta jangwani kondoo aliyepotea “hata amwone.” Au fikiria bidii ya mwanamke anayepoteza sarafu ya drakma, labda ikiwa sehemu ya fungu la sarafu nyingi za bei kubwa sana. Yeye anajitahidi vyo vyote awezavyo aipate​—anawasha taa na kufagia nyumba yake yote “hata aione.” Halafu kunakuwa na nderemo kama nini akiisha kuipata!—Luka 15:4-10.

Bila shaka unajua kwamba Yesu alikuwa akisema habari ya watu walio na uhusiano wa kujiweka wakf kwa Mungu, lakini kwa sababu mbalimbali wakapeperuka au ‘wakapotea.’ Labda wewe ni mmoja wao. Ile jitihada kubwa inayoonyeshwa katika mifano hiyo ya kutafuta kitu kinachothaminiwa sana huenda ikawa inakugusa moyo. Mifano hiyo inaonyesha namna Mungu, Mwanaye, malaika watakatifu na ndugu na dada zako wa kiroho wanavyopendezwa nawe. Mfano unaofuata hiyo miwili unatoa maelezo zaidi juu ya mwendo unaofuatwa na ‘aliyepotea.’

Mfano wa Mwana Mpotevu

Yesu anatumia uwazi wenye kukata moyo katika maelezo ya mfano wa mwana mpotevu, na anaonyesha (1) kwa sababu gani mtu angepeperuka, (2) jambo linaloweza kutukia wakati mtu ameenda zake, (3) jitihada inayohitaji kufanywa ili kurudi, na (4) nia ya Mungu ya ukaribishaji. Wale wana wawili wanaotajwa katika mfano wanaweza kulinganishwa na watu ambao wamepata kumjua Baba kama wewe, wakafurahia ‘chakula cha kusaza cha kiroho’ katika jamaa ya imani na kuweka wakf maisha yao kwa Yehova.​—Luka 15:11-32.

Kuna sababu mbalimbali zinazofanya wengine waondoke kwenye “nyumba” ya Baba yetu wa kimbingu, kama yule mwana mdogo. Mara nyingi sababu inakuwa ni kuongezeka tu kwa “masumbufu ya maisha” yenye kulemea mtu. (Luka 21:34) Pindi kwa pindi mavutano ya washirika wabaya yamezuia wengine wasiendelee ‘kuitii kweli.’ (Wagalatia 5:7, 8, 10, 12) Kuchukizwa na jambo fulani linalohusu mafundisho huenda likawa limefanya hesabu kadha ya watu “wakarejea nyuma” kwenye mambo ya zamani. (Yohana 6:60-66) Kama ilivyo, wakiwa wanafahamu waziwazi au wakiwa hawafahamu waziwazi, wengine wamekuwa na maoni ya kwamba mazingira yaliyo katika jamaa ya kiroho ya Yehova yanawekea watu vizuizi vya kupita kiasi. Watu hao wamekuwa kama yule mwana mpotevu, wasitake tena kuwa chini ya uangalizi wa Baba yao. Wanatafuta raha ya kutembea-tembea katika “nchi ya mbali.”

Peke Yao Katika Nchi ya Mbali

Baada ya yule mwana mpotevu kumaliza pesa zake zote hakupata hata kidonge kidogo cha uhuru na raha ila taabu tu. Aliharibu sana mwenendo wake mpaka akaishi “maisha ya uasherati.” Taabu zilipomkaza, shida yake ilimfanya ‘ajishikamanishe’ na mmoja wa raia za kule alikokuwa, kisha mtu huyo ‘akampeleka’ kuchunga nguruwe, hiyo ikiwa ndiyo kazi ya hali ya chini kabisa ambayo Myahudi angeweza kufanya. Hata njaa yake ilimfanya akitamani chakula cha nguruwe!—Luka 15:13-16.

John alikuwa amekuwa mzee wa kundi kabla hajafunga safari kwenda “nchi ya mbali” kwa njia ya kiroho. “Hakika kuifuata kweli ni ulinzi, lakini wakati mtu anapokuwa si mtendaji, anaacha kujikinga na mambo,” anaeleza John. “Hata kama hatafanya ubaya mkubwa sana, anaanza kufikiri si vibaya sana hata akiachilia mambo madogo-madogo. Anajiambia, ‘Ah, mimi sihudhurii mikutano yo yote ya kundi, kwa hiyo kuna ubaya gani katika jambo ninalofanya?’ “Shahidi mwingine ambaye alikuwa si mtendaji kwa miaka kadha alikubali wazi hivi: “Kweli mimi niliingia katika mwenendo mbaya. Nikajua upesi sana kwamba mtu akishirikiana na watu wa ulimwengu atazidi tu kuwa na tabia mbaya zisizo na kikomo. Njia ya pekee ya kufurahia ushirika wao ni kunyamaza usiwatajie Yehova. Unaponyamaza hivyo, umejianzia matata mengi.”

Hata hivyo wengi wanaokuwa wasiotenda hawapeperuki na kuingilia “maisha ya uasherati” kama yule mwana mpotevu wa mfano wa Yesu. Ingawa hivyo, wote wanapata kuufahamu mtengano unaokuja wasiwe na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Watu wawili waliooana ambao walipata kuwa wasiotenda “hawakuishika Biblia muda wa miaka 15,” na bado waliendelea kuwa safi katika tabia zao. Mke anaeleza hivi: “Tukitaja upande wa kimwili, mambo yalituendea vizuri kabisa miaka hiyo. Mtu akiwa katika hali hiyo anaweza kuongozwa aamini hakuna uhitaji wa kumrudia Yehova. Sisi tulijenga maisha yetu yote yategemee kazi zetu na yatutegemee sisi binafsi. Tukajaribu kujizuia tusikumbuke hata jambo moja linalohusiana na ile kweli, tukafikia kiasi cha kuhamia eneo jingine ambako hatukujulikana na mtu ye yote. Lakini hiyo ilikuwa furaha ya juu-juu tu. Kwa ndani tuliumia kweli kweli. Mume wangu akashuka moyo sana muda wa miaka mingi. Tukaacha kusali, hata kabla ya kula vyakula. Nilikosa usingizi siku nyingi nikiwa na wasiwasi kuhusiana na ile kweli na kujisikia mwenye hatia.” Mume wake aliongezea hivi: “Tulijisikia kama watu waliopangwa katika mstari wa kwenda kuuawa.”

Kuwa mbali na Yehova, kujisikia mpweke kabisa kiroho, ni hali yenye kuleta maumivu. Mwanamke mmoja Mkristo, aliyekuwa si mtendaji wakati mmoja, alisema hivi: “Hakuna kitu kizuri kama kuwa na upendeleo wa Yehova. Unapojisikia vibaya usiweze kumpelekea Yehova sala, au kuwa na mashaka kwamba yeye hatasikiliza sala zako, unakuwa katika hali ya kusikitisha sana.”

“Alirudiwa na Fahamu Zake”

Yule mwana mpotevu aliitambua hali ya maoni yake ya ndani ya kiroho kisha akayaitikia. Yesu alisema: “Alirudiwa na fahamu zake” (‘akazingatia moyoni mwake,’ UV). Maneno ya kwanza ya Kigiriki yaliyotumiwa hapo yana maana inayofuata yanapotajwa kwa njia halisi, “Yeye akajiingia mwenyewe.” Alikuwa amekuwa “kando yake mwenyewe,” katika ulimwengu usio halisi. Lakini sasa akaijua hali yake mwenyewe ya kweli, ya kiroho. Alifikiria amani na utele aliokuwa amefurahia katika nyumba ya baba yake.​—Luka 15:17, NW.

Ingawa mwana mpotevu ndiye aliyejichukulia mwenyewe hatua ya kutambua hivyo, mara nyingi ufahamu wa namna hiyo hupatikana na watu baada ya mazungumzo kadha ya kiroho kufanywa pamoja nao ili kuamsha mawazo yao ya ndani yaliyolala. Kwa mfano, wakati Diane alipokuwa si mtendaji alifunua mambo yake ya moyoni kwa Shahidi aliyekuwa amefahamiana naye, akasema: “Mimi siwezi kumrudia Yehova. Mimi simpendi, nami najua kwamba ili nirudi ni lazima niwe nampenda.” Shahidi huyo akamwuliza: “Wewe ulimpenda mume wako wakati alipoanza kukuchumbia?” “Hapana. Ningewezaje? Wakati huo sikumjua yeye,” akajibu Diane. “Hapo ndipo nikatambua,” Diane akakiri, “kwamba ningeweza kumpenda Yehova baada ya kupata kumjua tena. Baada ya hapo nikawasiliana na kundi nikaomba msaada. Mume mmoja na mke wake wakaelekezwa na wazee wakajifunza na mume wangu nami kwa zaidi ya mwaka mmoja, nasi tukawa watendaji tena.”

Lakini, kimoja cha vipingamizi vikubwa zaidi vya kurudi ni kuwa na maoni mazito sana ya hatia.

Je! Mimi Nimepita Kiasi Nisiweze Kurudi?

“Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; sistahili kuitwa mwana wako tena.” Hivyo ndivyo yule mwana mpotevu alivyojisikia baada ya ‘kurudiwa na fahamu zake.’ Wengine wamejisikia ivyo hivyo​—kuwa hawastahili kuitwa mmoja wa jamaa ya Mungu.​—Luka 15:17-19.

“Unatambua kwamba umempa Yehova kisogo kwa kujua. Kujisikia nikiwa na hatia hiyo kulinifanya nione vibaya sana,” akakiri Virginia. “Nilipoanza tena kuwa mtendaji, nilitatizika sana kuanza kusali tena. Nikaendelea kufikiri hivi, ‘Yehova ananiona kuwa nafaa nini, kwa kuwa nilimpa kisogo.’ “Wengine wamejisikia kwamba walitenda ile “dhambi isiyosameheka.”

Je! yule baba, aliyejua dhambi za mwanaye zilikuwa kubwa, aliziona kuwa zisizosameheka? Je! alikuwa baridi-baridi asitake kumkaribisha mvulana wake alipotokea tena? Hata kidogo! Yeye alikuwa amekuwa akitafuta mwanaye. Kulingana na maneno ya Yesu, “alipokuwa angali mbali, baba yake alimwona.” (Luka 15:20) Huenda ikawa majirani waliweza kuyaona matambara aliyovaa tu, ule uchafu tu, ile miguu isiyo na viatu tu, lakini kile ambacho baba aliona ni ‘mwanaye.’ Yeye alijua mwanaye alikuwa ametoka mbali sana. Ilikuwa wazi kwamba alikuwa ameyaacha “maisha ya uasherati” na akatubu kweli kweli.​—Mithali 28:13.

Baba alipiga mbio akakumbatie mwanaye. Jambo kubwa zaidi ambalo mwana alitumainia kutendewa ni kuwa ‘mtumishi wa kuajiriwa,’ mtu asiye mshiriki wa jamaa hiyo na hata katika mambo fulani awe chini zaidi ya mtumwa. Yeye hakuwaza kwamba babaye angeweza kuchukua hatua ya kusema: “Lileteni upesi vazi lililo bora, mkamvike; mtieni na pete kidoleni, na viatu miguuni; mleteni ndama yule aliyenona mkamchinje; nasi tule na kufurahi.” Yesu aliuonyesha vizuri ajabu mfano wa namna baba huyo alivyochukua hatua ya moyo wote!—Luka 15:22, 23.

Baba alijua kwamba yule mwana mpotevu alikuwa amekwisha kupata hasara kubwa​—yale maumivu yenye kudumu moyoni ya kuishi “maisha ya uasherati” na kuishiwa na pesa zake zote, ule uchungu mwingi sana wa kukosa marafiki na chakula na makao wakati wa njaa kubwa, aibu ya kula pamoja na nguruwe, na mwishowe, ile safari ndefu ya kurudi nyumbani. Vivyo hivyo, Yehova anajua kwamba mtu anapokuwa “amepotea” anataabika kweli kweli na haliwi jambo jepesi kwake kurudi. Hata hivyo Baba yetu wa kimbingu mwenye huruma, aliye ‘mwingi wa fadhili za upendo,’ ‘hatateta sikuzote wala kutulipa tunayostahili kwa kadiri ya maovu yetu’ ikiwa tutatubu kikweli na ‘kusemezana’ naye kunyosha mambo. Wengine ambao wametenda hata dhambi zilizo nzito walipokuwa wamekaa mbali na kundi la Kikristo, lakini wanaorudi wakiwa na toba ya kweli, kisha wanaungama dhambi zao mbele ya wazee, wanaweza kutazamia kutendewa kwa upendo na huruma hata wapone kabisa.​—Zaburi 103:8-10; 130:3; Isaya 1:18, 19.

Ni kweli kwamba Biblia inataja Wakristo fulani wasio waaminifu ambao dhambi zao hazisamehewi. Lakini, Paulo anaonyesha kwamba watu hao ni wale “waipingao” ile Kweli na kuikanyaga-kanyaga kwa madharau dhabihu ya ukombozi kwa kuikadiria kuwa yenye thamani ya kikawaida tu. (Waebrania 10:26-31) Lakini je! wewe umechukua hatua hiyo ya kupita kiasi? Jambo la kwamba wewe unazifikiria habari hizi zilizoandikwa hapa ukiwa na moyo mweupe, badala ya kuzidharau, linaonyesha ungali una upendo fulani kwa mambo ya kiroho. ‘Uhakika wa kwamba unajisikia ukiwa na hatia na kuhangaika moyoni unaonyesha kwamba wewe hujapita kiasi usiweze kurudi. Uwe na uhakikisho wa kwamba Yehova atajibu ombi lako unalolitoa kwa sala, sawa na vile alivyolijibu la Daudi, aliyemsihi sana hivi: “Unisamehe uovu wangu, maana ni mwingi.”​—Zaburi 25:11.

‘Usiogope. Naam, Nitakusaidia’

Wazee wawili walitembelea mume na mkeye waliokuwa si watendaji, lakini huko nyuma walikuwa wamekuwa ni mashahidi wenye juhudi ya ajabu. Mara tu mazungumzo yalipoanza, yule mume asiye mtendaji akajitetea moja kwa moja akisema alijua kwamba alilotakwa afanye ni kuwa katika utumishi wa shambani akifundisha wengine. “Sidhani unapaswa kufanya hivyo kwa sasa,” Russell, mmoja wa wazee hao, akatoa jibu hilo la kushangaza. “Kama wewe ungekuwa na mshiriki fulani wa jamaa yako aliye mgonjwa, ungemwambia aende nje akafyeke nyasi? Wala sisi hatutakuambia ‘ukafyeke nyasi.’ Sisi tunataka upone. Tunaweza kukusaidiaje?” Usaidizi wenye upendo, kutia ndani ukaribishaji wenye uchangamfu wa wazee hao, ulisaidia mume huyo na mkeye wapone kiroho, na hata sasa mume huyo anatumikia tena akiwa mzee.​—Linganisha Yakobo 5:14, 15.

Watu fulani wenye kutubu wanasita-sita kuja tena kwenye ushirika kwa sababu wanajisikia hawawezi kuchukua madaraka kamili yampasayo Shahidi, yote kwa safari moja. Lakini, Yehova ni mwenye kiasi. Kwa kawaida kupata nafuu ya hatua kwa hatua ndiko kunakofaa zaidi. Paulo alisema kwamba wengine ambao katika siku zake walikuwa “wavivu” kiroho walihitaji mtu wa kuwafundisha tena mambo ya msingi ya ile Kweli. (Waebrania 5:11, 12) Chakula hicho cha kiroho kinakuza nguvu na kufanya mtu aweze kuchukua hatua zile nyingine. Katika mahoji kadha yaliyofanywa pamoja na Mashahidi ambao wakati fulani walikuja kuwa wasiotenda lakini baadaye wakapona, wengi wao walisema kwamba walikuwa wamehitaji kupewa usaidizi kwa ukawaida. Hata hivyo wale walio katika kundi wana moyo wa kupenda sana kutoa usaidizi huo. Wanajisikia kama Yehova, aliyewaambia hivi watu wake wachaguliwa: “Usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia.”​—Isaya 41:10.

Ndiyo, Mungu anasema: “Nitakusaidia.” Huenda ikawa lazima uvunje ushirika wako na washirika wabaya. Huenda ikawa lazima uvumilie upinzani wa watu wa ukoo wako wasiokubali uhudhurie mikutano ya Kikristo. Huenda kukawa na mambo fulani utakayolazimika kuungama mbele ya wazee. (Zaburi 32:3-5) Lakini usisahau kamwe kwamba Yehova yupo ili akusaidie. Shahidi mmoja aliyepona alisema: “Yehova alinionyesha hatua moja moja tu, naye akanisaidia sana.” Mwingine aliongezea hivi: “Nilipokanyaga tu Jumba la Ufalme rafiki zangu wote wa zamani walinikumbatia-kumbatia na kunipiga mabusu mengi. Niliterema kwa vile walivyonionyesha furaha nyingi. Nikajiuliza, ‘Nilikuwa nikiogopa nini?’ “Ingawa huenda wengine wakawa na nia inayofanana na yule ndugu mkubwa wa mwana mpotevu walio wengi watafurahi sana kukuona ukirudi.​—Luka 15:25-32.

Sababu gani usijionjee mwenyewe? Mwanamke mmoja Mkristo aliyepona baada ya kukaa mbali na ushirika kwa muda fulani alitangaza hivi: “Hakuna mahali penginepo pa kupata amani ya ndani. Mambo yale mengine yote yaliniendea vizuri kabisa nilipokwisha kuwa mtendaji tena. Ulimwengu huu hauna kitu chenye thamani cha kumpa mtu. Unapojua kwamba unampendeza Yehova na kuwa na ulinzi wake unajisikia.vizuri sana. Unaweza kulala usiku. Sasa maisha yako yanakuwa yenye kuridhisha na unaweza kusitawisha tumaini halisi la kupata uzima katika Taratibu Mpya.”

Ikiwa wewe ni kondoo aliyepotea njia, unaombwa ukaribishe Shahidi aliyekuletea gazeti hili akusaidie kupashana habari na wazee wa kundi la mahali unapoishi. Jipatie furaha na uradhi unaotokana na kuufuata mwendo ulioelezwa na Petro: “Kwa maana mlikuwa kama kondoo, mkipotea; lakini sasa ninyi mmerudia mchungaji na mwangalizi wa nafsi zenu.”​—1 Petro 2:25, NW.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki