Sura 21
Kupokea kwa Uchangamshi Wale Wanaorudi
1. Ni watu wa namna gani wanaozungumzwa katika sura hii?
KUNA watu wengi ambao wakati fulani wamekutana vya kutosha na ukweli wa Biblia. Wamejua kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli na kufahamu habari fulani juu ya makusudi yake. Wasijapokuwa Mashahidi wa Yehova, huenda wamejifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Au labda wazazi wao walikuwa Mashahidi. Wengi wa hao wamehudhuria mikutano michache kwenye Jumba la Ufalme. Huenda hata wameshiriki kidogo kuwapa wengine ujumbe wa Ufalme. Lakini hawakutoa maisha zao wafanye mapenzi ya Mungu. Kwa nini?
2. (a) Kwa nini walitangatanga kutoka kwenye tengenezo la Yehova? (b) Kwa nini wanaanza kuwaza kwamba afadhali wangerudi?
2 Ulimwengu unatoa vitu vyenye kuvutia wanavyofikiri wanavitaka, vitu wanavyodhani vitawaongezea furaha ya maisha, kisha wanatangatanga kutoka kwenye tengenezo la Yehova wakivitafuta-tafuta vitu hivyo. Ingawa hivyo, baadaye baadhi yao wanafahamu kwamba hawakupata aina ya maisha waliyotazamia kupata. Wanakuja kupata fahamu za kuona uhakika wa kwamba wakiendelea kama walivyo, watakuja kuangamizwa pamoja na ulimwengu. Hawajasahau usalama na wingi wa chakula cha kiroho kilicho katika “nyumba” ya Yehova, na sasa wanataka wawe humo tena. Lakini Yehova atawakubali?
MWANA MPOTEVU ARUDI
3. (a) Katika mfano wa mwana mpotevu, ni simulio gani ambalo Yesu alitoa la hali iliyo kama hiyo? (b) Yule baba anafananisha nani?
3 Jibu limeonyeshwa katika mfano wa Yesu unaojulikana sana wa mwana mpotevu. Ukiwa mfano, Yesu alisimulia juu ya mwanamume aliyekuwa na wana wawili. Yule mwana mdogo akamwomba babaye ampe sehemu yake ya mali. Alipopata sehemu hiyo, akasafiri kwenye nchi ya mbali, ambako aliponda ovyo kila kitu katika maisha ya upotovu. Ndivyo alivyoponda mali yote. Njaa kuu ilipoipata nchi hiyo, kijana huyo, kwa sababu ya kupata taabu sana, akalazimika kuchunga nguruwe, lakini hakuruhusiwa hata kula chakula cha nguruwe. Akitikiswa na matatizo yaliyomkaba, akarudiwa na fahamu zake. Akakumbuka jinsi watu walioajiriwa katika nyumba ya babaye walivyokuwa na maisha mazuri, kisha akakaza nia arudi. Arudipo angeukiri mwendo wake wenye dhambi na kuomba apokewe tena, si kama mwana, bali kama mtumishi aliyeajiriwa. (Luka 15:11-19) Lakini, kwa sababu ya mambo yote aliyokuwa amefanya, je! baba yake angemruhusu arudi? Yehova, aliyefananishwa na baba huyo katika mfano huo, angeonaje kurudi kwa mtu huyo?
4. Baba alimpokeaje mwanaye aliporudi?
4 Akisimulia kwa njia ya wazi sana hisia za Yehova katika shauri hilo, Yesu aliendelea kusema: “[Mwana mdogo] alipokuwa angali mbali, baba yake alimwona, akamwonea huruma, akaenda mbio akamwangukia shingoni, akambusu sana. Yule mwana akamwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; sistahili kuitwa mwana wako tena. Lakini baba aliwaambia watumwa wake, Lileteni upesi vazi lililo bora, mkamvike; mtieni na pete kidoleni, na viatu miguuni; mleteni ndama yule aliyenona mkamchinje; nasi tule na kufurahi; kwa kuwa huyu mwanangu alikuwa amekufa, naye amefufuka; alikuwa amepotea, naye ameonekana. Wakaanza kushangilia.”—Luka 15:20-24.
MFANO HUU UNAHUSUJE WAKATI WA LEO?
5. (a) Ni nani aliyefananishwa na mwana mkubwa katika mfano wa Yesu? (b) Ni nani, basi, aliyefananishwa na mwana mdogo, yule mpotevu?
5 Katika mfano huu yule mwana mkubwa, mzaliwa wa kwanza, analingana kwa kufaa na “kundi la wazaliwa wa kwanza ambao wameandikishwa majina yao katika mbingu.” (Waebrania 12:23, New World Translation) Vipi yule mwana mdogo? Bila shaka anafananisha kikundi kingine kuliko “kundi dogo” la walio na tumaini la kimbingu. Si wote walio wa “kondoo wengine” wa Bwana wanafaa kusimuliwa kuwa ndio yule mwana mdogo, lakini baadhi yao wanafaa. Hata kabla kukusanywa kwa “kondoo wengine” hakujatokeza sana, kuanzia mwaka wa 1935, walikuwako watu waliojua kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli. Walijua habari ya tumaini la maisha ya kidunia chini ya Ufalme wake, lakini hawakuwa na wazo lo lote la kuwa watu wa “kundi la wazaliwa wa kwanza” walio na matumaini ya kimbingu. Lakini badala ya kujitoa wenyewe kwa utumishi wa Yehova, wakazama katika shughuli za kilimwengu. Walivichukua “vitu” ambavyo Mungu aliwajalia, wakati na uhai aliowaruhusu wawe nao, wakatumia vitu hivyo kwa raha ya kibinafsi yenye choyo. Lakini mwaka wa 1935 wakati watumishi wa Yehova walipofahamu waziwazi mara ya kwanza utambulishi wa “mkutano mkubwa,” wengi waliolingana na mwana mdogo walijitoa wenyewe kwa moyo wote ili wafanye utumishi katika nyumba ya Baba. Ulikuwa wakati wa kushangilia kama ule aliosimulia Yesu katika mfano wake.
6. Katika utimizo, watu fulani walionyeshaje mwelekeo wa yule mwana mkubwa, lakini mabaki wote walikuwa hivyo?
6 Ni kweli kwamba, wakati huo, si kila mtu alishiriki kushangilia kufika huko kwa jamii iliyofananishwa na mwana mdogo. Katika mfano wake Yesu alionyesha kwamba ingekuwa hivyo. Lakini si wote wa mabaki ya “kundi dogo” walioonyesha roho hiyo, na katika mfano wake Yesu aliacha njia wazi hata kwa ajili ya wale ambao hapo kwanza hawakupendezwa, washiriki furaha aliyo nayo Yehova mwenyewe wakati watenda dhambi hao wanapotubu kweli kweli.—Luka 15:7, 10, 25-32.
7, 8. (a) Miaka ya majuzi, ni nini kimefanya wengine wawe mbali na nyumba ya Yehova? (b) Ni katika njia zipi baadhi yao walihisi kama mwana mpotevu? (c) Kwa nini warudi?
7 Ingawa hivyo, tangu matukio hayo ya miaka ya kuanzia mwaka wa 1935, wengine wamefahamu kwamba wao, pia, wako kama mwana mpotevu huyo kwa mambo fulani. Wanaijua sana nyumba ya kiroho ya Yehova, tengenezo lake linaloonekana, lakini namna ya maisha yao imewatoa ikawapeleka mbali nalo, kana kwamba kwenye “nchi ya mbali.” Hawakupinga watumishi wa Yehova, lakini namna yao ya kuishi haikupatana na viwango vya Neno la Mungu. Labda wamejenga maisha yao yote juu ya kazi yao ya kimwili na wao wenyewe wakakosa kuona uzito wa madaraka yao mbele za Mungu na hatari ya nyakati tunamoishi. Baadhi yao waliudhika kwa sababu ya makosa ya wengine ambao wakati huo walikuwa wakishirikiana na kundi na hawakumngojea kwa saburi Yehova asahihishe makosa. Lakini wote hao walipojitenga na nyumba ya imani, walikuja kuingia katika hali zipi?
8 Baadaye, baadhi yao wamefahamu kwamba wamekuwa maskini kiroho. Wanaona kwamba vipindi vyo vyote vifupi vya raha walivyo navyo haviwaletei furaha yenye kuendelea. Huenda wakaona pia kwamba namna yao ya kuishi inawaharibu kimwili, kimoyo na kiroho. Ndani yao wanajiona utupu, kama wanavyojiona wale wote wasio na Mungu na wasio na tumaini. (Waefeso 2:12) Wanafahamu kwamba wakati walipokuwa wenye furaha kweli kweli ni wakati ule tu walipokuwa katika “nyumba” ya Yehova. Wanataka kurudi. Warudi? Kuendelea katika hali yao ya umaskini kunaweza kuwaletea faida gani? Kukawia kungeweza kuleta msiba. Wakiendelea kuung’ang’ania ulimwengu, watapoteza uhai wao wakati utakapoharibiwa.
9. (a) Kwa nini Yehova anataka watu kama hao warudi? (Ezekieli 18:23) (b) Linalotakwa upande wao ni nini?
9 Lakini watu kama hao wanaweza kurudi? Yehova anawakaribisha kwa uchangamshi warudi, na tengenezo lake lionekanalo linawatolea msaada wa upendo wale wanaofanya hivyo. (Zekaria 1:3, 4) Ni jambo gani linalotakwa? Kama inavyoonyeshwa katika mfano wa Yesu, ni lazima warudiwe na fahamu zao, wachukue hatua ya kwanza ya kurudi na kukiri kwamba wamemtenda Mungu dhambi. Ikiwa walishiriki mwenendo ulio mbaya sana na usio wa Kikristo, ni lazima wawape wazee ushahidi wenye kusadikisha kwamba sasa wameacha kabisa namna hiyo ya kuishi na sasa wametubu kweli kweli. Sasa tamaa yao ya moyo ni lazima iwe kumtumikia Yehova wakiwa sehemu ya tengenezo lake linaloonekana. (Luka 15:18-21; Mithali 28:13) Ikiwa jambo hilo ndilo lililo katika moyo wao kweli kweli, wanaweza kuwa na hakika kwamba kuacha kwao njia na mawazo yao mabaya na kumrudia Yehova kutaleta furaha nyingi. (Isaya 55:7) Ingawa hivyo, ili furaha yao wenyewe isiwe ni raha tu ya kupokewa tena kwa uchangamshi kwenye Jumba la Ufalme, kujengwa upya kiroho ambako ni timamu kunahitajiwa.
KUJENGA JUU YA MSINGI ULIO TIMAMU
10. (a) Ni mwelekeo gani juu ya matakwa ya Yehova ambao wenye kutubu wanahitaji kusitawisha? (b) Wanaweza kusitawishaje uhusiano wa kibinafsi na ulio wa karibu sana pamoja na Yehova?
10 Ni jambo la maana hasa kwamba wo wote wanaorudi kwenye nyumba ya Yehova wazijue sana sehemu mbalimbali za utu wa Yehova na kusitawisha uhusiano wa kibinafsi ulio karibu sana na yeye. Wanahitaji kufahamu kwamba yote ambayo Yehova anataka kwetu ni kwa faida yetu wenyewe kweli kweli. Amri zake haziondoi furaha ya maisha bali, badala yake, zinatulinda ili tusifanye mambo ambayo huenda yakaleta msisimuko wa muda na kumbe yanaongoza kwenye mavuno machungu. (Isaya 48:17; Wagalatia 6:7, 8) Anapotutia nidhamu, ni kwa sababu anatupenda. (Mithali 3:11, 12) Funzo la kibinafsi likifuatwa na kutafakari mambo tunayojifunza, sala ya bidii na hudhurio la kawaida la mikutano yatatusaidia tujifunze kuweka tumaini letu kamili katika Yehova, kumtegemea atuelekeze katika kila tunalofanya.—Mithali 3:5, 6.
11. Wale waliokuwa wamepotea watasaidiwaje kwa (a) kusitawisha uchukivu wa ubaya? (b) kutafuta ufahamu? (c) kutogeuka-geuka katika kufuata viwango vya kimungu? (d) kujifunza kufikiria matokeo ya lo lote wanalopanga kufanya? (e) kuwaonyesha wengine hangaikio la upendo
11 Huenda wale waliopotea walikuwa wamejua lililokuwa jema na lililokuwa baya. Lakini sasa ni lazima wasitawishe pia uchukivu wa ubaya na ni lazima waendelee kufanya hivyo muda wote wanapozungukwa na ubaya huo. (Zaburi 97:10) Watasaidiwa kufanya hivyo ikiwa si maarifa tu wanayotafuta bali pia ufahamu. Kwanza, hiyo inahusu kuona mambo kuhusiana na Mungu. Twahitaji tutambue njia mbalimbali anazotumia kutuagiza na jinsi kuitikia kwetu shauri lake kunavyogeuza uhusiano wetu pamoja naye. (Mithali 4:7; 9:10) Ni lazima tuthamini umaana wa kutogeukageuka, kufuata viwango vya Yehova wakati wote, katika kila tunalofanya. (Tito 2:11, 12; 1 Wathesalonike 4:7) Uangalifu pia umepaswa utumiwe ili tusifikirie raha ya muda tu bali yale ambayo huenda yakawa ndiyo matokeo ya maamuzi yetu. (Linganisha Mithali 20:21; 23:17, 18; Waebrania 11:24-26.) Pia imetupasa tuhangaikie kwa upendo namna mambo tunayosema na kufanya yanavyoweza kuwa na matokeo kwa wengine.—Warumi 15:1, 2.
12. (a) Ni kujua nini juu ya Shetani na mbinu anazotumia kutasaidia kutulinde sisi? (b) Ni nini kinachohitajiwa ili tushinde vita hii?
12 Sisi tukiwa Wakristo tutatiwa nguvu sana kwa kufahamu kwamba tuko katikati ya vita vya kiroho. Mpinzani wetu mkuu ni Shetani Ibilisi, pamoja na mashetani wake. Yeye anatumia kila njia inayowezekana ili atuondoe kwenye kazi ya maana ya Ufalme ambayo Yehova ametupa tuifanye. Lengo lake ni kutushawishi ili tuweke kando viwango vya Yehova, tuwe sehemu ya ulimwengu ambao yeye ni mtawala. Mara nyingi mitego yake inaelekeza kwenye tamaa za kawaida (za kuwa na furaha, raha ya mwili, upendo na shauku), lakini yeye anatuchochea tuzipe tamaa hizo cheo kikubwa kinachopotoa kusudi lazo au tuzitosheleze kwa njia zisizofaa. Tunaweza kushinda vita hiyo ya kupigania maisha zetu za kiroho kwa kutumia tu kwa ukamili silaha zote ambazo Mungu anatoa.—Waefeso 6:11-18.
13. (a) Tunaweza kupataje burudisho la nafsi zetu? (b) Kwa nini kumtumikia Yehova kwa kufuata mfano wa Yesu kunatuletea furaha kweli kweli?
13 Yesu alisema kwamba ikiwa tungemwendea tukabebe “nira” yake, tungepata burudisho la nafsi yetu. (Mathayo 11:29, 30) Kubeba “nira” maana yake ni kutumikia. Lakini kumtumikia Yehova kwa kufuata mfano wa Mwanaye kunaleta burudisho la kweli. Namna gani? Kwa sababu kunaleta uhuru wa kweli. Sisi si watumwa wa dhambi tena, hatumo katika utumwa wayo. Tusifanye mambo tunayojua haitupasi kufanya na labda tunayoona afadhali tusingekuwa tukiyafanya. (Yohana 8:32, 34-36) Ikiwa utu wetu wa Kikristo umejengwa juu ya Yesu Kristo kuwa msingi, tutalithamini daraka lake katika kusudi la Yehova, tutamsikiliza na kujifunza kwake. Yeye alifurahia kufanya mapenzi ya Babake. Tutajifunza kufanya hayo pia. (Yohana 4:34; Zaburi 40:8) Kwa sababu ya kufuata sana viwango vya adili vya Mungu tutaweza kufurahia dhamiri safi. Badala ya kuishi tu kwa ajili yetu wenyewe, tutaona furaha inayotokana na kutoa. (Matendo 20:35) Maisha yatakuwa na kusudi la kweli kwetu. Zaidi ya yote, tutakuwa na furaha ya kujua kwamba sisi tuna kibali ya Yehova mwenyewe, Baba ya wote wanaokuwa wanaye.—Mithali 10:22.