Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 10/15 kur. 11-15
  • Saa ya Hatari Inakaribia!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Saa ya Hatari Inakaribia!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Je! Utalisikiliza Onyo?
  • Mwito wa Haraka Unaotolewa kwa Wanyenyekevu
  • Mahali pa Kutafuta Msaada
  • Ile Gharika—Onyo Kutokana na Wakati Uliopita
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Huu Ndio Wakati Tunaopaswa Kuwa Wenye Kulinda Zaidi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Je! Wewe Walaani Vikali Ulimwengu Kupitia Imani Yako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Tutatembea Katika Jina la Yehova Mungu Wetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 10/15 kur. 11-15

Saa ya Hatari Inakaribia!

INGAWA wameonywa sana, na serikali za kibinadamu zikashindwa mno kutimiza mambo yafaayo kwa muda wa karne nyingi, wanadamu hoi wasio wakamilifu, wanajipeleka mbele kwa kiburi wasonge na mipango yao. Lakini wao hawatafanya hivyo kwa muda mrefu sana. Tusitie shaka kamwe kwamba Mungu aliye Baba ya Bwana yetu Yesu Kristo anaweza kulitimiza kusudi lake alilolitangaza kupitia nabii wake: “Na katika siku za wafalme hao [wenye kutawala ‘wakati wa mwisho’] Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”​—Danieli 2:44; 12:9.

2. (a) Yesu aliifananishaje hali inayowaelekea wanadamu sasa? (b) Ni onyo gani lililotolewa, na matokeo yakawa nini?

2 Kikiwa ni kionyesho kingine cha kukaribia kwa saa hiyo ya hatari, Yesu alitushauri tutazame tuone kitu kingine. Alizitaja hali zilizokuwapo duniani siku za Nuhu na kuwakumbusha wafuasi wake kwamba watu wa siku hizo walijishughulisha kabisa na tumipango twao tudogo-tudogo na kuishi kikawaida tu kulingana na maoni yao. Yesu alisema: “Kwa maana kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu. Kwa kuwa kama vile siku zile zilizokuwa kabla ya Gharika watu walivyokuwa wakila, na kunywa, wakioa na kuolewa, hata siku ile aliyoingia Nuhu katika safina, wasitambue, hata Gharika ikaja, ikawachukua wote, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu.” (Mathayo 24:37-39) Watu hao walionywa na ujumbe ambao Nuhu alizidi kuutangaza kumi la miaka baada ya kumi jingine la miaka. (2 Petro 2:5) Lakini onyo hilo lilikuwa na matokeo gani juu ya wengi wa watu hao? Yesu alisema, ‘Hawakutambua.’ Hawakupendezwa na Nuhu wala ujumbe wake. Basi ndivyo ikawa kwamba “Noa tu akabaki, nao walio pamoja naye ndani ya safina,” nafsi nane tu.​—Mwanzo 7:23, ZSB.

Je! Utalisikiliza Onyo?

3. Watu wanaliitikiaje onyo wakati huu?

3 Je! tutasema kweli kwamba hatujapewa onyo? Sisi tunayaona kwa macho yetu mambo yale yale yaliyokuwa yakitendeka siku za kizazi cha Nuhu. Ebu ona jinsi watu wengi wanavyopuza ujumbe unaotangazwa na Mashahidi wa Yehova leo, wakiutupia maneno ya dharau au kuudhihaki. Wengi wamejiingiza sana katika mipango yao ya kila siku na mipango ya miaka mingi itakayokuja. Akili zao hata haziwi na nafasi ya kufikiria Mungu wala makusudi aliyo nayo kuhusiana na wanadamu na dunia hii. Wengi wa watu hao wanajisema kuwa ni Wakristo, nao ni wa madhehebu fulani-fulani za kidini, lakini wamefuata madhehebu hizo kwa kusudi tu la ‘kuheshimiwa’ na jamii ya kisasa ya watu inayoheshimu mtu kama ana dini fulani. Wao ‘hawalitambui’ lile onyo hata kidogo na kwa hiyo watakiona cha mtema kuni. Lakini namna gani wewe? Je! wewe utatumia hekima uzitii ishara za nyakati?

4. Paulo na Petro waliitabirije hali iliyopo?

4 Wewe umeona, sivyo?, jinsi milki na falme zinavyogawanyika-gawanyika visehemu-visehemu, jinsi mashirika ya kidini na ya kisiasa yanavyogawanyikana, mengine yakijitenga upande huu, mengine hapa na mengine hapa, na umeona jinsi watu wengi sana wanavyotaka kujiongoza wenyewe, njia yao iwe ya haki au isiwe. Je! mambo hayo hayauonyeshi ule unabii uliotabiriwa na mtume Paulo akisema: “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.” (2 Timotheo 3:1-4) Kwa uhakika tuuongezapo utimizo wa unabii huo kwenye mambo yale mengine yote aliyotabiri Yesu Kristo, tunaziona ishara za nyakati zikiwa na maana nyingi sana. Sisi tumo katika hizo “siku za mwisho,” nao ukosefu wa adabu unaweza kuonekana pande zote, katika shule, katika biashara, katika afisi za kazi, katika jamii ya watu kwa ujumla.​—Linganisha 2 Petro 3:3-7.

5. (a) Ni maulizo gani tunayopaswa kuchunguza sana? (b) Tazamio letu linatofautianaje na lile la walimwengu?

5 Siku hizi, wakati ambapo watu wenye kujitakia makuu na viongozi wa mataifa pia wanapoonyesha si wenye kujadilika na wanashindwa kuleta upatano wa madai yao yote yenye kupingana na kwa ugumu wa moyo kusonga mbele na mipango yao ya kufanya ulimwengu uwe afadhali, wewe utafanya nini? Ishara za nyakati zinakuonyesha ni mwendo gani salama upaswao kuufuata? Je! wewe utakuwa mwenye hekima na kiasi kuliko wale watu mashuhuri? Wao hawakioni kifo cha Kristo Yesu kilichokuwa dhabihu kuwa jambo la maana sana. Wanakataa kukubali kwamba alikufa, si ili sisi sote tuweze kuishi tu, bali pia awezeshe kuwe na Ufalme wake mtukufu atakaoutumia kuuharibu uwezo wa mungu wa ulimwengu huu, Shetani Ibilisi! (Waebrania 2:14) Lakini wewe unaweza kuonyesha unaziamini ahadi hakika za Muumba. Unaweza kutumaini matokeo mazuri sana ambayo Yehova anamhakikishia kila mtu anayemtumaini yeye.​—Zaburi 37:3, 4, 28, 29, 39, 40.

Mwito wa Haraka Unaotolewa kwa Wanyenyekevu

6. Ni mwito gani unaosikizishwa wenye kutaka tendo la haraka, na kwa sababu gani?

6 Kwako wewe na kwa wote wanaozisoma kwa usahihi ishara zote za nyakati, mwito huu wa haraka unatolewa kwa sauti kubwa na nabii wa Yehova Mungu: “Kabla haijawajilia hasira kali ya [Yehova], kabla haijawajilia siku ya hasira ya [Yehova]. Mtafuteni [Yehova], enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya [Yehova].” (Sefania 2:2, 3) Ni wazi kwamba Yehova angetokeza nafasi ya kuwaokoa wale wapendao amani na haki kutokana na taratibu ya mambo iliyohukumiwa maangamizi.

7. Tunaweza kujifaidi wenyewe kwa kujibu maulizo gani Ndiyo?

7 Badala ya kuwa na kiburi moyoni na kushikilia maoni yetu wakati huu zinapoendelea kuonekana ishara hizo (kama walivyo viongozi wengi wa ulimwengu wa kisiasa na kidini), je, wewe ni mnyenyekevu au mwenye kufundishika, mwenye utayari wa kuusikiliza kwa hamu nyingi mpango ule ambao Mungu ameufanya upate kuokoka? Je! umejaribu kuishi kulingana na kanuni za Biblia za haki, yaani, “hukumu” ya Yehova? Je! wewe unajisikia vibaya sana moyoni kwa sababu ya mambo unayoona au unayosikia yakiendelea kutendeka duniani, naam, hata katika ujirani wako mwenyewe? Wewe ukiwa tofauti na watu wenye kutosheka na hali zao za kibinafsi bila kujali ni mambo gani yanayowapata wengine maadamu wao wanapata kile wakitakacho maishani, je, huguswi sana moyoni na magumu, maonezi, hali zitakazoleta njaa kubwa karibuni ambazo mamilioni ya wanadamu wenzako walio hai watalazimika kuishi chini yazo? Ikiwa unajibu Ndiyo maulizo haya, basi labda wewe ni mmoja wa wale wanaoahidiwa na Yehova kufichwa katika siku ya ghadhabu yake.​—Isaya 26:20, 21; Ezekieli 9:4-7.

8. Tunawezaje ‘kutafuta unyenyekevu na haki’?

8 Ikiwa wewe ni mnyenyekevu, mwenye utayari wa kusikiliza mafundisho ya kimungu, ‘utautafutaje unyenyekevu na haki’? Huenda tayari ukawa ukijiuliza ulizo hilo akilini. Yesu, Yeye aliye mpole na mnyenyekevu, anakukaribisha uwe mwanafunzi wake kweli kweli. Ili uwe mwanafunzi ungetakwa uuchunguze mfano aliouweka, kazi aliyofanya maishani mwake alipokuwa duniani, kisha ujitahidi kufanya kama alivyofanya. Kumbuka kwamba yeye alifanya mema huku na huku, asiwatende kamwe uovu hata wapinzani wake. (Matendo 10:38) Mara nyingi kichwa cha mafundisho yake kilikuwa ufalme wa Mungu, na ndicho kilichokuwa kichwa cha mifano na sala zake. (Mathayo 4:17; Luka 8:1) Yeye hakufanana hata kidogo na falme za kisiasa za ulimwengu huu. (Yohana 18:36) Yeye alionyesha aliamini bila kutikisika kwamba Mungu ana uwezo wa kuwatimizia watumishi wake duniani ahadi Zake zote. Yesu alikataa kuwakubali wale wanaojisema wanamtumikia Mungu na kumbe upande mwingine wanafundisha mafundisho yasiyoungwa mkono na Neno la Mungu lililoandikwa. (Marko 7:5-8) Je! wewe uko tayari kumwiga katika mambo yote haya?

9. Yesu alituwekea mfano gani mzuri?

9 Kwa vyo vyote Yesu hakutenda bila kumtegemea Baba yake wa kimbingu. Kwa kweli, yeye alisema hivi: “Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda; kwa maana yote ayatendayo yeye, ndiyo ayatendayo Mwana vile vile.” (Yohana 5:19; 7:16-18) Tena alisema: “Naye aliyenipeleka yu pamoja nami; hakuniacha peke yangu; kwa sababu nafanya sikuzote yale yampendezayo.” (Yohana 8:29) Yeye hakuonyesha maelekeo yo yote ya kutumia uhai wake katika njia yake mwenyewe ili atosheleze tamaa na matakwa ya kibinafsi. Yeye alikataa kabisa utawala wa ulimwengu na umaarufu (umashuhuri) aliopewa na Shetani Ibilisi. (Luka 4:5-8) Je! wewe utakubali na kufuata mfano wa Yesu ili upate kibali na baraka ya Yehova Mungu?

Mahali pa Kutafuta Msaada

10. (a) Mungu ametoa kifaa gani chenye kutokeza sana, na tunawezaje kujifaidi nacho? (b) Maneno ya Yohana 17:3 yana maana gani kwetu sisi?

10 Hutaweza kuufuata mwendo huo kwa nguvu zako mwenyewe, maana njia atumiazo yule mdanganyaji namba moja ni za werevu na za hila sana! Utahitaji usaidizi wote ambao Mungu ameutoa kukuwezesha ufaulu. Msaada mkubwa sana ambao ametoa ni Biblia Takatifu. (2 Timotheo 3:16, 17) Kama wewe ujuavyo, mtu hawezi kujifunza yaliyomo katika Biblia kwa kuhudhuria tu hotuba fupi kila juma wala kwa kujitia katika desturi na sheria mbalimbali za ibada zinazofanywa kwa sababu hiyo ndiyo kawaida tu. Unahitaji masomo ya kujifunza Biblia, yako mwenyewe na pia ya jamaa yako. Kumbuka kwamba hiki ndicho Kitabu cha pekee kiwezacho kuthibitisha kwamba kiliandikwa na Muumba wa mbingu na dunia. Hakuna kitabu kinginecho cha mafunzo kinachoweza kuwapa wanafunzi wenye kumcha Mungu kitu kile kilichotajwa na Yesu, yaani: “Uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” (Yohana 17:3) Wako wanaume na wanawake wenye maarifa mengi ya Biblia walio tayari kukusaidia bila malipo wala masharti. Jambo la pekee linalokupasa kufanya ni kuwaomba Mashahidi wa Yehova wakusaidie, nawe utaupata msaada unaohitaji ili kuanza mafunzo yako.

11, 12. (a) Yehova amewawekea wale wanaojifunza Neno lake kwa unyenyekevu ahadi gani? (b) Majina yetu yanawezaje kuandikwa katika “kitabu cha ukumbusho” cha Mungu?

11 Mungu amewawekea ahadi nzuri kama nini wale ambao wanafikiri na kuzungumza kati yao juu ya faida zinazopatikana maishani kwa kujifunza yale ambayo Mungu na Kristo wamefunua juu yao wenyewe! Angalia jinsi jambo hilo linavyosemwa na mmoja wa manabii wa kale wa Yehova: “Ndipo [Yehova atakapotoza hesabu adui zake wenye kujitanguliza ambao walidhani wangeweza kutenda uovu milele bila kuadhibiwa] wale waliomcha [Yehova] waliposemezana wao kwa wao. Naye [Yehova] akasikiliza, akasikia; na kitabu cha ukumbusho kikaandikwa mbele zake, kwa ajili ya hao waliomcha [Yehova], na kulitafakari jina lake.”​—Malaki 3:16.

12 Hiyo inamaanisha mengi zaidi ya kuishi vizuri kwa heshima kwa kulingana na kanuni za ulimwengu. Inamaanisha kutwaa maarifa sahihi ya makusudi ya Mungu kwa wanadamu, na kujifunza yale anayotazamia kutoka kwetu, halafu kutumia maisha yetu tukimtumikia na kufanya mapenzi yake katika kila sehemu ya maisha. Ama sivyo, ni kwa njia gani nyingine tungetazamia Yehova ayaandike majina yetu katika “kitabu cha ukumbusho” chake? Angewezaje kutukumbuka kwa njia yenye kuleta wema ikiwa tunashindwa kuonyesha woga wa uchaji wa Neno na jina lake, na kukosa kuzungumza hayo pamoja na wanadamu wenzetu katika kila nafasi inayowezekana?​—Warumi 10:10.

13. (a) Tunaweza kufuata shauri gani la Yesu na la Paulo maishani mwetu? (b) Tunawezaje kujionyesha sisi kuwa watu “wenye hekima”?

13 Huenda mtu mwenye kufanya kazi, au mwanafunzi shuleni, au mke mwenye kazi nyingi za nyumbani akakata neno kwa kusema ana shughuli nyingi mno asiweze kuwa na wakati wa funzo la namna hiyo. Lakini ni vizuri kuyakumbuka maneno ya Yesu yenye fadhili yanayotuonya yakisema mipango ya mtu, tamaa zake kubwa za kupata kitu fulani, hata uzima wake wenyewe haujulikani utakuwaje: “Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi [au, uhai] yake?” (Mathayo 16:26) Halafu pia yako maneno yale ya mtume Paulo yanayoonyesha uharaka wa nyakati hizi ambapo tumezungukwa na ishara iliyo mbovu: “Basi angalieni sana jinsi mnavyoenenda; si kama watu wasio na hekima, bali kama watu wenye hekima; mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu. Kwa sababu hiyo . . . mfahamu ni nini yaliyo mapenzi ya [Yehova].” (Waefeso 5:15-17) Kwa sababu ya msiba ambao Yehova anakaribia kuuleta juu ya ulimwengu wote huu mbovu, ni vizuri kulitii shauri lake lililotolewa kupitia manabii wake: “Mtafuteni [Yehova] maadamu anapatikana.” “Yehova amesema hivi . . . , ‘Nitafuteni, mwendelee kuishi.’”​—Isaya 55:6; Amosi 5:4, NW.

14. (a) Wengi wanafanya kosa gani wakati huu, na kwa sababu gani?(b) Kwa habari hiyo, ni shauri gani zuri linalopatikana katika Yakobo 4:13-16?

14 Kuna wale wenye afya nzuri na nishati (nguvu) tele, ya akili na mwili, na kwa sababu hiyo huenda wasione sana wanahitaji kumtegemea Muumba. Kwa hiyo maelekeo ni kujifanyia mipango mikubwa ya wakati ujao na kupuza sehemu anayotimiza Mungu katika maisha zao. Wanaweka macho yao kwenye utajiri au heshima kati ya watu au maisha ya uzeeni ya starehe na uzembe. Mungu hayuko katika mafikira na mipango yao yote. Kwa hekima mwandikaji wa Biblia aliyeongozwa na Mungu anaonya hivi: “Basi, sasa sikilizeni ninyi mnaosema: ‘Leo au kesho tutakwenda katika mji fulani na kukaa huko mwaka mzima tukifanya biashara na kupata faida.’ Ninyi hamjui hata maisha yenu yatakavyokuwa kesho! Ninyi ni kama ukungu unaotokea kwa muda mfupi tu na kutoweka tena [maisha yenu ni mafupi hivyo.] Mngalipaswa kusema: ‘Mungu akitujalia tutaishi na tutafanya hiki au kile.’ Lakini sasa mwajivuna na kujigamba; majivuno ya namna hiyo ni mabaya.”​—Yakobo 4:13-16, HNWW.

15. Kwa sababu ya ishara za nyakati, twapaswa kutambua uhitaji gani wenye kutaka tendo la haraka wakati huu?

15 Kwa hiyo, hata cheo chako wakati huu maishani kiwe nini, kuna sababu yenye kutaka hatua ya haraka ushirikiane na wale watu zaidi ya milioni mbili duniani pote, ambao wanajulikana sana kuwa wanafunzi wa Biblia na watangazaji wa ujumbe wayo, na wanaotambulishwa hasa kwa utoaji wao wa ushuhuda kwa jina na ufalme wa Yehova.​—Isaya 43:10,12, NW; Mathayo 24:14.

Kila moja la maandiko yafuatayo linatupa shauri gani la maana sana katika wakati huu?

◻ Mathayo 24:37-39

◻ 2 Timotheo 3:1-4

◻ Sefania 2:2, 3

◻ Waefeso 5:15-17

◻ Yakobo 4:13-16

1. (a) Kwa sababu gani mipango ya wanadamu hoi haina budi kushindwa? (b) Ni kusudi gani la Mungu litakalotimizwa karibuni?

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Kama Yesu, lazima tuonyeshe imani isiyotikisika katika uwezo wa Mungu wa kutimiza ahadi zake zote

[Picha katika ukurasa wa 14]

siku ya Yehova ya kuondoa lawama inapokaribia, je, jina lako limeandikwa katika kitabu chake cha ukumbusho?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki