Wakati Ujao kwa Vijana wa Leo
BAADA ya George kufanya kazi kwenye kampuni ya bima alilazimika kuiacha kwa sababu za kibinafsi. Wakati huo umri wake ulikuwa miaka 20. Ndiyo kusema umri wake ulikuwa ni kama unalingana na wa kile kilichoitwa “kizazi kilichopotea.” Lakini baada ya yeye kuondoka, mwanamke mwenye umri wa miaka 40 aliyekuwa amefanya kazi pamoja naye alimwandikia barua inayofuata:
“Mimi ningependa kutumia nafasi hii nikutakie bahati nzuri, afya nzuri, furaha na mafanikio wakati ujao. Limekuwa jambo la kufurahisha kukujua wewe na kufanya kazi pamoja nawe. Wewe ni kijana mzuri, kijana mwenye kuletea jamaa yao sifa. Katika hizi siku na kizazi hiki chenye kuendesha mambo shaghala-baghala, wakati ambao vijana wa leo wanaonekana ni kama hawajui la kufanya, mtu anakuwa ni kama amefika mahali penye hewa safi anapokuta kijana mwungwana na mwenye kuheshimu watu kama wewe. Mungu na akubariki daima.”
Ni wazi kwamba George yuko tofauti na vijana wengi wa leo. Yeye ‘haonekani ni kama hajui la kufanya.’ Kwa sababu gani? Katika barua moja, yeye alieleza sababu: “Kwa kusaidiwa na Biblia, wazazi wangu wameniongoza katika maisha mpaka nikafikia hali yangu ya sasa.”
Ndiyo, wazazi wa George waliona uhitaji wa kumwongoza katika ile mitego iliyokabili kijana mwenye kuendelea kukua. Lakini kwa sababu gani wao walipata matokeo mazuri na hali wazazi wengine wengi wameshindwa? Kama George alivyosema, sababu ni kwamba wao walitegemea ‘msaada wa Biblia.’ Ni kweli kwamba leo mtu anaonekana kuwa wa kizamani akiitegemea Biblia impe uongozi. Lakini hapo tumeona kisa ambapo kutumia mashauri ya Biblia kulisaidia sana.
Ikiwa wewe ni mzazi, je! ungependa kujua mengine ya mambo ambayo wazazi wa George walimfunza alipokuwa akiendelea kukua, mambo ambayo yalimkuza vizuri sana alipokuwa kijana? Au, ikiwa wewe ni tineja, ingefaa wewe mwenyewe uyafikirie mengine ya mambo hayo. Yalimsaidia George akaepuka hali ya kukaa bila lengo lo lote na ya kukosa kutosheka ambayo ina watu wengi leo ulimwenguni. Yanaweza kukusaidia wewe ivyo hivyo.
Mwanzo Ulio Bora Zaidi
Kwanza, ni wazi kwamba wazazi wa George walitambua lilikuwa daraka lao kumlea yeye, wala si la mtu mwingine.Walijua kwamba maneno yanayofuata yaliyo katika Biblia hayaelekezwi kwa mtu mwingineyo ila ni kwa wazazi: “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” (Mithali 22:6) Na bila shaka, George alikuwa na nia ya kukubali malezi ambayo wazazi wake walijitahidi kumpa.
Biblia inafananisha watoto wadogo na “mishale mkononi mwa shujaa.” (Zaburi 127:4) Ili mshale uweze kuwa wenye mafaa na mafanikio katika wakati wa uhitaji, ni lazima mshale huo utayarishwe kwa ustadi. Ili mshale uipate shabaha, manyoya yanawekwa upande ule mwingine ulio tofauti na ncha yake. Yanawekwa pia kwa kupindika kidogo ili mshale huo uzunguke vuruvuru kidogo unapokuwa hewani. Usipozunguka namna hiyo utapotoka ulikose lengo lake.
Vivyo hivyo, vijana wasipopewa mwelekezo imara, watapotoka kwa wepesi wauache mwendo unaofaa. Jambo hilo linaonekana katika uchunguzi uliofanywa kati ya vijana wapatao 5,000 wa baina ya umri wa miaka 10 na 18 katika shule 160 za nchi yote ya Uingereza. Kati ya wale wa miaka 10, asilimia 70 kati yao waliwaza kwamba kila mtu anapaswa kupelekea Mungu sala, lakini kati ya wale wa miaka 18 ni asilimia 34 tu waliowaza hivyo.
Kwa sababu gani pana tofauti kati ya watoto wa umri mdogo na wale wa umri mkubwa zaidi? Ni wazi kwamba hao matineja walikuwa wameharibiwa wakati wa ukuzi wao na maoni ya kudharau maendeleo na kupuza mambo ya kimungu ya ulimwengu wenye kuwazunguka. Au labda walikuwa wameuliza maulizo kisha kukawa hakuna mtu wa kuweza kuyajibu.
Kitu cha Kuishilia
Kwa sababu gani George hakuwa ameharibiwa na maoni hayo ya kudharau mambo ya kimungu? Yeye anasema kwamba alifunzwa na wazazi wake “njia nzuri ajabu na sifa zenye upendo” za Yehova Mungu. Kwa hiyo, yeye alijisikia akiwa na uhusiano pamoja na Mungu. Akajihisi anamjua Mungu na kwamba hata yeye anajulikana na Mungu. Jambo hilo lilimpa George mwelekezo, mradi katika maisha. Tena lilimsaidia aendelee kufuata viwango bora vya kitabia.
Lakini kuna faida gani ya kuwa na viwango bora na miradi ya kitabia na huku wakati ujao unaonekana kuwa wenye mashaka mengi, tena huu mfumo mzima wa mambo unaonekana ni kama unabomoka-bomoka?
Kuzidi kuharibika kwa huu mfumo wa mambo hakushangazi wanafunzi wenye kuichunguza Biblia bila mchezo. Wao wanajua kwamba Biblia inaonya kuwa katika siku zetu watu wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao . . . ,” na kadhalika. Na, bila shaka, mambo haya haya ndiyo yameufanya ulimwengu ukose uthabiti.—2 Timotheo 3:1-5.
Walakini, Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu ameona kwamba mwanadamu anafuata mwenendo mbaya naye hatauacha uendelee kuwa hivyo mpaka milele. Bali, yeye ‘atawaharibu hao waiharibuo nchi.’ (Ufunuo 11:18) Lakini mambo hayataishia hapo. Biblia inaahidi pia “mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13, NW.
Wenye kusimamia mambo katika huo mfumo mpya hawatakuwa ni wanasiasa wadanganyifu wala wanaviwanda wasio na huruma. Bali, tunaahidiwa hivi: Watenda mabaya wataharibiwa, bali “Wamngojao [Yehova] ndio watakaoirithi nchi. . . . Wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:9, 11.
Labda baada ya kusoma maneno haya, wengine watasema hivi: ‘Wapi! Haiwekani!’ Lakini yule kijana George anaamini inawezekana. Na ndivyo maelfu ya watu wengine walio kama yeye. Wao hawafanyi kukuru-kakara ya kuamini mambo bila kuthibitishiwa. Wala hawadanganyiki kwa wepesi tu. Bali, wao walitaka uthibitisho sawa na vijana wa kisasa kila mahali, kabla hawajaamini mambo. Na wakati walipoufikiria uthibitisho wa kwamba ahadi hizo ni za kutegemeka, walitosheka.
Sisi tunapendekeza usizikatae ahadi hizi bila kujichunguzia mwenyewe kwamba Ingawaje, kuna tumaini gani jinginelo kwa wakati ujao?
Maisha Yenye Mafanikio Sasa
Labda wewe unaweza kuelewa sababu inayofanya vijana kama George wawe tofauti sana na vijana wengi wa leo. Wao ni vijana wa hali za kikawaida, katika maana ya kwamba wanalazimika kukabili mikazo na magumu yale yale ambayo vijana wengine wote wanalazimika kuyakabili wanapoendelea kukua. Lakini wao wamejiwekea mbele yao wakati ujao mzuri. Wanajisikia wakiwa na mwelekezo, kwa hiyo wao hawako katika hali ‘ya kutokujua la kufanya.’ Tena, kwa sababu wanaiamini Biblia wanajitia katika hali ya kuweza kutegemea chanzo bora kabisa cha uongozi ambacho kinawasaidia waepuke mitego na kufanikisha maisha zao sasa.
Kwa mfano, mara nyingi vijana wanajaribu kuwa tofauti na watu wale wengine baada ya kuchukizwa na ulimwengu huu. Lakini, wanapofanya hivyo, je! Wanajipatia kitu cho chote chenye mafaa bora kuliko ya watu hao wengine? Je! Si kweli kwamba waasi wengi walio vijana na washerati zaidi. Wenye kukosa zaidi usawaziko, wenye jeuri zaidi au wachoyo zaidi ya mfumo huu wanaoulaumu?
Ni kweli kwamba Biblia inatutia moyo tuwe tofauti. Inasema: “Mwache kufanyanyizwa kulingana na mtindo wa huu mfumo wa mambo.” Lakini zaidi ya hilo, inaonyesha namna tunavyoweza kuwa tofauti kwa njia yenye mafanikio. “Mgeuzwe yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Warumi 12:2, NW) Kwa hiyo, Mkristo halisi anakuwa tofauti kwa kuendelea kufuata viwango bora zaidi ya vile vinavyofuatwa katika ulimwengu. Anajaribu kuishi maisha yake kama Mungu anavyosema, na kwa njia hiyo yeye hachafuliwi na ulimwengu.
Tena, Yesu alisema: “Kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35, NW) Watu wengi hawana nia hiyo. Leo watu wana maoni ya kwamba inawapasa ‘wajitafutie nafasi ya kwanza’ kwa kuwapita wenzao. Lakini je! Nia hiyo imeleta furaha? Ni wazi haikuleta. Kwa hiyo Mkristo anayefuata mashauri ya Biblia na kutenda kwa njia isiyo ya kichoyo anatenda ipasavyo. Je! Wewe hujaona namna ‘ukarimu unavyozaa ukarimu’? Mtu mkarimu anafanya mazingira yake yapendeze katika hali ya maisha. Yeye pia anakuwa mwenye furaha kwa sababu anasitawisha sifa ambazo Mungu ndiye aliziweka hapo mwanzoni ndani ya mwanadamu.—Luka 6:38,NW.
Biblia inashauri pia tufanye kazi kwa bidii, tusiwe wavivu wala tusitegemee wengine watulishe. (Waefeso 4:28; 2 Wathesalonike 3:12) Shauri hilo linatufaidi. Tuliumbwa katika hali ya kufanya kazi, naye mtu anatosheka na kufurahi sana kwa kutimiza mambo. (Mhubiri 2:24) Wale wanaoepuka kazi wanaharibika kitabia na kimwili.
Vivyo hivyo, tunaonywa tusifanye pesa ziwe mungu wetu. Ni lazima tujitafutie riziki, lakini kufanya upataji wa pesa uwe ndio mradi wetu wa kwanza maishani kunaweza kutokeza mambo ya kuhuzunisha. Biblia inasema: “Hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha.” (1 Timotheo 6:9, 10) Labda wewe umesoma habari za watu waliotia bidii nyingi sana ili wawe matajiri wakubwa. Je! walipata furaha kwa kufanya hivyo? Mara nyingi, kilichoharibika ni afya yao, furaha yao, jamaa na rafiki zao walipokuwa wakifuatia mradi huo.
Hapana, Mungu anatupa sisi mambo yenye thamani zaidi tunayopaswa kujitahidia. Watu wenye hekima wanalifuata shauri hili: “Watende mema, wawe matajiri kwa kutenda mema, wawe tayari kutoa mali zao, washirikiane na wengine kwa moyo; huku wakijiwekea akiba iwe msingi mzuri kwa wakati ujao, ili wapate uzima ulio kweli kweli.”—1 Timotheo 6:18, 19.
Je! maneno hayo yanasikika kuwa yenye ubora kwako? Bila shaka, kisicho na ubora ni njia isiyo na kanuni ambayo inatumiwa kufanya mambo katika ulimwengu huu. Lakini mamilioni ya watu leo wanakuta kwamba njia ya maisha yanayotegemea kumtumikia Mungu na wanadamu wenzetu, na pia inayotegemea tazamio la uhakika la kufurahia wakati ujao mzuri ambao Mungu ameweka mbele yetu, ina mafanikio na ni ya kiasi pia. Inafaidi.
Kufikia hapo, ikiwa wewe ni mzazi, huenda ukawa unajisikia hivi: ‘Mimi sina uwezo wa kuwapa watoto wangu tumaini hakika hivyo katika wakati ujao, wala sina uwezo wa kuwapa kanuni hizo ngumu za kuishilia. Mimi sina maarifa ya kutosha.’ Au huenda matineja wakawa wakishangaa na kujiuliza hivi: ‘Ningeweza kupata wapi habari za namna hiyo?’ Kusema kweli, habari zile za msingi zimo katika Biblia. Lakini wazazi wa George walisaidiwa na Mashahidi wa Yehova kuzipata habari hizo. Hao wanafunzi wenye kuichunguza Biblia wana moyo wa kutaka kusaidia watu wote—vijana kwa wazee—wapate maarifa yale yale waliyo nayo hao wenyewe na kuwasaidia wajionee mafaa ya maarifa hayo.
Kwa sababu gani usikubali wakusaidie? Si lazima maisha yako yakuvuruge moyo na kuwa bila kusudi. Ikiwa wewe ni kijana—na hata kama wewe si kijana sana—kwa sababu gani usiufuate mfano wa maelfu ambao, kama George, wamejipatia mwelekezo katika maisha zao. Furahia maisha yenye kutosheleza sasa, kisha uwe na tumaini hakika la kwamba mambo yatakuwa na mafanikio katika wakati ujao.
[Blabu katika ukurasa wa 23]
Usizikatae ahadi hizi bila kuzichunguza kwanza. Ingawaje, kuna tumaini gani jinginelo kwa wakati ujao?
[Picha katika ukurasa wa 20]
Vijana wasipokuwa na mwelekezo imara, watapotoka
[Picha katika ukurasa wa 21]
Jambo la kusikitisha ni kwamba waasi wengi walio vijana leo ni wenye jeuri zaidi au ni wachoyo zaidi ya mfumo wa mambo wanaoulaumu?
[Picha katika ukurasa wa 21]
Wakati walipoufikiria uthibitisho wa kwamba ahadi hizo ni za kutegemeka, walitosheka