Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w04 4/1 kur. 24-28
  • Tumebarikiwa Sana kwa Kujidhabihu Katika Mambo Madogo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tumebarikiwa Sana kwa Kujidhabihu Katika Mambo Madogo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Familia Yetu Yaungana Katika Ibada ya Kweli
  • Magumu Yaliyohitaji Tujidhabihu
  • Mapendeleo Baada ya Ubatizo Yafanya Tujidhabihu Zaidi
  • Twaanza Utumishi wa Upainia wa Pekee
  • Twapata Eneo Jipya
  • Twapata Baraka kwa Kujidhabihu Maishani
  • Nimebarikiwa Sana kwa Kudumisha Roho ya Umishonari
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Mungu Aikuza Katika Alaska
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Kukubali kwa Shangwe Mwelekezo wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Wakati Ujao kwa Vijana wa Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
w04 4/1 kur. 24-28

Simulizi la Maisha

Tumebarikiwa Sana kwa Kujidhabihu Katika Mambo Madogo

LIMESIMULIWA NA GEORGE NA ANN ALJIAN

Mimi na mke wangu hatukufikiri kamwe kwamba siku moja tungetatanishwa na maneno “mwalimu” na “panya.” Wala hatukufikiri kamwe kwamba tukiwa na umri wa miaka 60 na kitu tungekuwa tukifikiria herufi zisizo za kawaida katika jitihada ya kuwasiliana na watu kutoka Mashariki ya Mbali. Hata hivyo, hivyo ndivyo mimi na Ann tulivyofanya mwishoni mwa miaka ya 1980. Acheni tuwaambie jinsi tulivyobarikiwa sana kwa kujidhabihu kwa miaka mingi iliyopita.

NILITOKANA na ukoo wa familia ya Waarmenia na nilikuwa mshiriki wa Kanisa la Armenia. Ann alikuwa Mkatoliki. Sote wawili tuliachilia mbali baadhi ya mambo tuliyoamini baada ya kuoana mwaka wa 1950. Nilikuwa na umri wa miaka 27 naye Ann 24. Tuliamua kuishi katika chumba cha orofa kilichokuwa juu ya duka nilipofanyia biashara ya kufua nguo huko Jersey City, New Jersey, Marekani. Kufikia wakati huo nilikuwa nimeendesha biashara hiyo kwa miaka minne hivi.

Tulinunua nyumba nzuri yenye vyumba vitatu huko Middletown, New Jersey, mwaka wa 1955. Nyumba hiyo ilikuwa umbali wa kilometa 60 kutoka mahali nilipofanyia biashara yangu siku sita kwa juma. Kila siku nilirudi nyumbani jioni nikiwa nimechelewa. Nilionana na Mashahidi wa Yehova tu walipokuja mara kwa mara mahali pangu pa kazi na kuniachia vichapo vya Biblia. Nilifurahia sana kusoma vichapo hivyo. Ingawa nilitumia wakati wangu mwingi na pia kujishughulisha sana na biashara hiyo, nilianza kuiheshimu sana Biblia.

Muda si muda nilitambua kwamba kituo cha redio cha Watchtower cha WBBR, kilikuwa kikitangaza hotuba za Biblia wakati nilipokuwa nikiendesha gari kwenda na kutoka kazini. Nilisikiliza kwa makini hotuba hizo, na nilizidi kupendezwa nazo sana hivi kwamba niliwaomba Mashahidi waje kunitembelea. Mnamo Novemba 1957, George Blanton alinitembelea nyumbani kwangu na kuanza funzo la Biblia pamoja nami.

Familia Yetu Yaungana Katika Ibada ya Kweli

Ann alihisije kuhusu mambo hayo yote? Acheni awaeleze.

“Kwanza kabisa, nilipinga vikali. Nilisumbua sana wakati George alipokuwa anajifunza Biblia hivi kwamba aliamua kujifunzia mahali pengine, naye alifanya hivyo kwa miezi minane. Wakati huo, George alianza kuhudhuria mikutano Jumapili kwenye Jumba la Ufalme. Ndipo nikajua kwamba alichukua kwa uzito funzo lake la Biblia kwa kuwa Jumapili ndiyo tu iliyokuwa siku yake ya kupumzika. Hata hivyo, aliendelea kuwa mume na baba mzuri, na mtazamo wangu ukaanza kubadilika. Hata nyakati nyingine nilipokuwa nikipangusa vumbi kwenye meza ndogo, wakati hakuna mtu aliyekuwa akinitazama, nilikuwa nikichukua gazeti la Amkeni!, ambalo mara nyingi George aliacha juu ya meza hiyo, na kulisoma. Nyakati nyingine, George alinisomea makala za Amkeni! ambazo hazikuzungumzia mafundisho ya kidini moja kwa moja, na ambazo sikuzote zilikazia Muumba.

“Jioni moja, George alipokuwa ameenda kujifunza Biblia pamoja na Ndugu Blanton, nilichukua kichapo fulani ambacho mwana wetu, George, mwenye umri wa miaka miwili alikuwa amekiweka juu ya meza, kando ya kitanda changu. Kichapo hicho kilizungumzia tumaini la wafu. Ingawa nilikuwa nimechoka nilianza kukisoma kwa kuwa nyanya yangu alikuwa tu amekufa, na nilikuwa nimeshuka moyo sana. Nilielewa mara moja kweli ya Biblia kwamba wafu hawateseki mahali fulani na kwamba watafufuliwa wakati ujao. Muda si muda, niliketi wima kitandani, nikisoma kwa hamu na kupiga mistari mambo ambayo nilitaka kumwonyesha George aliporudi nyumbani baada ya funzo lake la Biblia.

“Mume wangu hakuamini kwamba nilikuwa mtu yuleyule. Alipoondoka nyumbani, nilikuwa nikimpinga, na sasa nilikuwa nimesisimuliwa na kweli nzuri za Biblia nilizojifunza! Tulikaa macho hadi usiku wa manane tukizungumza kuhusu Biblia. George alieleza kusudi la Mungu kuelekea dunia. Nilimwuliza usiku huohuo kama angeweza kujifunzia nyumbani ili niweze kushiriki funzo hilo.

“Ndugu Blanton alipendekeza kwamba wana wetu wawili washirikishwe katika funzo letu. Tulifikiri kwamba walikuwa wachanga sana, kwa kuwa mmoja alikuwa na umri wa miaka miwili tu na yule mwingine miaka minne. Hata hivyo, Ndugu Blanton alituonyesha andiko la Kumbukumbu la Torati 31:12, linalosema: ‘Wakutanishe watu, wanaume na wanawake na watoto wadogo . . . , ili wasikilize na ili wajifunze.’ Tulithamini mwelekezo huo na hata tukapanga watoto wawe wakitoa maelezo wakati wa funzo hilo la Biblia. Tulikuwa tukitayarisha maelezo yetu pamoja, lakini hatukuwaambia kamwe kile watakachosema. Tunahisi kwamba jambo hilo lilisaidia kuwaelekeza watoto wetu kuifanya kweli iwe mali yao. Tutathamini sikuzote mwongozo ambao Ndugu Blanton alitutolea ili kuisaidia familia yetu ikue kiroho.”

Magumu Yaliyohitaji Tujidhabihu

Kwa kuwa sasa tulijifunza Biblia pamoja, tulikabili matatizo mapya. Na kwa kuwa duka langu lilikuwa mbali sana na nyumbani, kwa kawaida nilifika nyumbani saa 3:00 usiku. Kwa sababu hiyo, sikuweza kuhudhuria mikutano siku nyingine za juma isipokuwa Jumapili tu. Wakati huo, Ann alikuwa akihudhuria mikutano yote na alikuwa akifanya maendeleo haraka. Mimi pia nilitaka kuhudhuria mikutano yote na pia kuongoza funzo la familia lenye matokeo. Nilijua kwamba nilipaswa kufanya mabadiliko fulani. Hivyo, nikaamua kutumia muda mfupi zaidi kazini, hata kama hiyo ingemaanisha kupoteza baadhi ya wateja wangu.

Mpango huo ulikuwa mzuri sana. Tuliliona funzo la familia kuwa lenye uzito sawa na mikutano mingine mitano ya juma kwenye Jumba la Ufalme. Tuliita funzo hilo mkutano wetu wa sita. Hivyo tukapanga siku na saa hususa za kufanya funzo hilo—Jumatano kila juma saa 2:00 usiku. Nyakati nyingine baada ya chakula cha jioni, tulipomaliza kuosha vyombo, mmoja wetu angesema, “Wakati wa ‘mkutano’ umekaribia!” Ann angeanzisha funzo hilo kama ningechelewa, nami ningeliendeleza mara tu nilipofika.

Jambo lingine lililotuimarisha na kutuunganisha tukiwa familia ni kusoma pamoja andiko la kila siku asubuhi. Lakini tukawa na tatizo katika kupanga jambo hilo. Kila mtu aliamka saa tofauti. Tulizungumzia jambo hilo na tukaamua sote tuwe tukiamka wakati mmoja, kula kiamsha-kinywa saa 12:30 asubuhi, na kuchunguza andiko la kila siku pamoja. Mpango huo ulitufaa sana. Wana wetu walipokuwa watu wazima, waliamua kwenda kutumika Betheli. Tulihisi kwamba kuzungumzia andiko la kila siku kuliwasaidia kiroho.

Mapendeleo Baada ya Ubatizo Yafanya Tujidhabihu Zaidi

Nilibatizwa mwaka wa 1962, na baada ya kuendesha biashara yangu kwa miaka 21, niliiuza na kuajiriwa kazi karibu na nyumbani ili niwe karibu zaidi na familia yangu kusudi tuweze kumtumikia Yehova pamoja. Kwa kufanya hivyo, tulipata baraka nyingi. Sote tuliweka mradi wa kuwa watumishi wa wakati wote. Tulianza kutimiza mradi huo mapema miaka ya 1970 wakati Edward, mwana wetu mkubwa, alipoanza huduma ya wakati wote, au upainia wa kawaida, mara tu baada ya kumaliza shule ya sekondari. Muda mfupi baadaye, mwana wetu George alianza upainia, na muda si muda Ann naye akaanza. Wote watatu walinitia moyo sana kwa kunisimulia mambo waliyoona katika mahubiri. Tukiwa familia tulizungumzia jinsi tunavyoweza kurahisisha maisha yetu ili sote tuweze kuwa watumishi wa wakati wote. Tuliamua kuuza nyumba yetu. Tulikuwa tumeishi katika nyumba hiyo kwa miaka 18 na tulilelea watoto wetu humo. Tuliipenda sana nyumba yetu, lakini Yehova akabariki uamuzi wetu wa kuiuza.

Edward alialikwa Betheli mwaka wa 1972, naye George mwaka wa 1974. Ingawa mimi na Ann tuliwakosa, hatukufikiria sana kwamba ingekuwa vizuri waishi karibu nasi, waoe, na kupata watoto. Badala yake tulifurahi kwamba wana wetu walikuwa wakimtumikia Yehova huko Betheli.a Tulikubaliana na andiko la Methali 23:15, linalosema: “Mwanangu, ikiwa moyo wako umekuwa na hekima, moyo wangu utashangilia, naam, moyo wangu.”

Twaanza Utumishi wa Upainia wa Pekee

Wana wetu walipokuwa wakitumika Betheli, sisi tuliendelea kufanya upainia. Ndipo siku moja mwaka wa 1975, tukapokea barua iliyotualika kuanza upainia wa pekee katika eneo lisilogawiwa mtu huko Clinton County, Illinois. Tulishangaa wee! Hiyo ilimaanisha kwamba tungehama New Jersey, ambako tulikuwa karibu na wana wetu walioishi huko New York, na ambako tulikuwa na marafiki na watu wa ukoo. Hata hivyo, tuliona mgawo huo kuwa unatoka kwa Yehova, nasi tulipata baraka zaidi kwa kujidhabihu kuufanya.

Baada ya kuhubiri eneo hilo kwa miezi kadhaa, tulianza kufanya mikutano katika ukumbi wa jamii huko Carlyle, Illinois. Lakini tulitaka kuwa na mahali pa kudumu pa kukutania. Ndugu mmoja mwenyeji na mke wake walipata uwanja wenye nyumba ndogo ambayo tulikodisha. Tuliisafisha pamoja na choo chake kilichokuwa nje, na kuigeuza kuwa mahali padogo pa kufanyia mikutano. Tunamkumbuka kwa upendo farasi mmoja aliyevutiwa nasi. Mara nyingi aliingiza kichwa chake dirishani ili kuona kilichokuwa kikiendelea kwenye mikutano!

Baada ya muda mfupi, Kutaniko la Carlyle lilianzishwa, na tulifurahi kwamba tulisaidia katika kuanzishwa kwa kutaniko hilo. Tulisaidiwa na wenzi wa ndoa wachanga, Steve na Karil Thompson, mapainia waliokuwa pia wamekuja kuhubiri katika eneo hilo lisilogawiwa mtu. Ndugu na dada Thompson walikaa huko kwa miaka kadhaa na baadaye wakahudhuria Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower na kwenda katika mgawo wa mishonari Afrika Mashariki, ambako wanatumikia katika kazi ya kusafiri.

Muda si muda, mahali petu padogo pa kufanyia mikutano palianza kujaa sana, hivyo tukahitaji jumba kubwa zaidi. Ndugu yuleyule mwenyeji na mke wake walitusaidia tena kwa kununua uwanja ambao ulifaa zaidi kwa ajili ya Jumba la Ufalme. Miaka michache baadaye, tulifurahi kama nini tulipoalikwa wakati wa kuwekwa wakfu kwa Jumba jipya la Ufalme lililojengwa huko Carlyle! Nilipata pendeleo la kutoa hotuba ya wakfu. Tulifurahia mgawo wetu huko nasi tuliuona kuwa baraka kutoka kwa Yehova.

Twapata Eneo Jipya

Katika mwaka wa 1979 tulipata mgawo mpya wa kwenda Harrison, New Jersey. Tulitumikia huko kwa muda wa miaka 12 hivi. Wakati huo tulianzisha funzo la Biblia na mwanamke mmoja Mchina, na hilo lilifanya tupate mafunzo mengine mengi ya Wachina. Wakati huohuo, tulipata habari kwamba kulikuwa na maelfu ya wanafunzi na familia za Wachina walioishi katika eneo letu. Kwa sababu hiyo, tulitiwa moyo tujifunze Kichina. Ingawa hiyo ilimaanisha kutumia wakati kila siku kujifunza lugha hiyo, tulianzisha mafunzo mengi ya Biblia yenye kufurahisha pamoja na Wachina wanaoishi katika eneo letu.

Katika miaka hiyo, tulijikuta katika hali zenye kuchekesha, hasa tulipojaribu kuzungumza Kichina. Siku moja, Ann alijijulisha kwa mwenye nyumba kuwa “panya” wa Biblia badala ya “mwalimu” wa Biblia. Maneno hayo yanafanana sana. Mwenye nyumba alitabasamu na kusema: “Tafadhali ingia ndani. Sijawahi kamwe kuzungumza na panya wa Biblia.” Bado tunapambana na lugha hiyo.

Halafu tukapewa mgawo wa kwenda katika eneo lingine la New Jersey, ambako tuliweza kuendelea kuhubiri katika eneo wanakoishi Wachina. Baadaye, tuliombwa kuhamia Boston, Massachusetts, ambako kikundi cha Wachina kilikuwa kimeanzishwa miaka mitatu hivi iliyopita. Tumekuwa na pendeleo la kukisaidia kikundi hicho kwa miaka saba iliyopita na tumefurahi kuona kikundi hicho kikiwa kutaniko mnamo Januari 1, 2003.

Twapata Baraka kwa Kujidhabihu Maishani

Katika andiko la Malaki 3:10, tunasoma mwaliko wa Yehova kwa watu wake walete matoleo na dhabihu ili awamwagie baraka zake hata kusiwe na uhitaji tena. Tuliuza biashara niliyoipenda sana na pia nyumba yetu tuliyoipenda sana. Tulidhabihu vitu vingine pia. Hata hivyo, tulipata baraka nyingi ikilinganishwa na mambo madogo tuliyodhabihu.

Yehova ametubariki kwelikweli! Tumeridhika kuona watoto wetu wakiikubali kweli, nasi tumepata shangwe inayotokana na huduma ya wakati wote yenye kuokoa uhai, na tumeona kwamba Yehova ametutimizia mahitaji yetu. Kwa kweli, tumebarikiwa sana kwa kujidhabihu katika mambo madogo!

[Maelezo ya Chini]

a Bado wanatumikia kwa uaminifu huko Betheli. Edward na mke wake Connie, wako Patterson, naye George na mke wake Grace, wako Brooklyn.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Louise na George Blanton pamoja na Ann, mwaka wa 1991

[Picha katika ukurasa wa 26]

Jumba la Ufalme la Carlyle, lililowekwa wakfu Juni 4, 1983

[Picha katika ukurasa wa 27]

Tukiwa na Kutaniko la Kichina lililoanzishwa hivi karibuni la Boston

[Picha katika ukurasa wa 28]

Tukiwa na Edward, Connie, George, na Grace

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki