Kukubali kwa Shangwe Mwelekezo wa Yehova
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ULYSSES V. GLASS
Lilikuwa tukio lisilo la kawaida. Kulikuwa na wanafunzi 127 tu katika darasa lenye kuhitimu. Lakini kulikuwa na wahudhuriaji 126,387 wenye shauku, waliokuja kutoka mataifa mbalimbali. Tukio hilo lilikuwa kuhitimu kwa darasa la 21 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower, kulikofanywa Julai 19, 1953 katika Stediamu ya Yankee ya New York City. Kwa nini tukio hilo likawa muhimu sana maishani mwangu? Acheni niwaeleze kwa ufupi vile hali zilivyokuwa.
NILIZALIWA Februari 17, 1912 jijini Vincennes, Indiana, Marekani, miaka miwili hivi kabla ya Ufalme wa Kimesiya kuanza kutawala, kama inavyofafanuliwa kwenye Ufunuo 12:1-5. Mwaka uliotangulia, wazazi wangu walikuwa wameanza kujifunza Biblia kwa kutumia mabuku Studies in the Scriptures. Kila Jumapili asubuhi, Baba angeisomea familia habari kutoka kwa kimojawapo cha vitabu hivyo, kisha tungeizungumzia.
Mama alitumia mambo aliyokuwa akijifunza ili kuelekeza kufikiri kwa watoto wake. Alikuwa mtu mzuri sana—mwenye fadhili na tayari sana kusaidia. Tulikuwa watoto wanne, lakini Mama aliwapenda hata watoto wa majirani. Alitumia wakati pamoja nasi. Alifurahia kutusimulia hadithi za Biblia na kuimba pamoja nasi.
Pia alialika nyumbani kwetu watu mbalimbali waliokuwa wahudumu wa wakati wote. Walikaa kwa siku moja au mbili tu, mara nyingi wakifanya mikutano na kutoa hotuba nyumbani kwetu. Tuliwapenda hasa wale waliotoa vielezi na kutusimulia hadithi. Wakati mmoja mwaka wa 1919, yapata mwaka mmoja baada ya vita ya ulimwengu ya kwanza kwisha, ndugu aliyezuru alitoa maelezo ambayo hasa yalitulenga sisi watoto. Alizungumzia kujitakasa—ambako sasa tunakuita kwa usahihi zaidi kujiweka wakfu—naye akatusaidia tujue jinsi jambo hilo lilivyoathiri maisha yetu. Baadaye nilipoenda kulala jioni hiyo, nilisali kwa Baba yangu wa kimbingu, nikamwambia kwamba nilitaka kumtumikia daima.
Hata hivyo, baada ya mwaka wa 1922 mahangaiko mengine ya maisha yalielekea kufanya nitangulize mambo mengine. Tulihama-hama, tukawa hatushirikiani na kutaniko la watu wa Yehova. Baba alikaa mbali kwa sababu ya kazi yake ya reli. Funzo letu la Biblia halikuwa la kawaida. Nilihudhuria mitaala ya shule nikitumainia kuwa msanii wa matangazo ya biashara nami nilikuwa nikipanga kwenda chuo kikuu maarufu.
Kurekebisha Mambo Niliyokazia Fikira Maishani
Katikati ya miaka ya 1930, ulimwengu ulianza kujitayarisha tena kwa ajili ya vita ya ulimwengu. Tulikuwa tukiishi Cleveland, Ohio, wakati mmoja wa Mashahidi wa Yehova alipotutembelea. Tulianza kufikiria kwa uzito yale tuliyojifunza tukiwa watoto. Kaka yangu, Russell, alichukua mambo kwa uzito, naye ndiye aliyebatizwa kwanza. Mimi sikuchukua mambo kwa uzito, lakini Februari 3, 1936, mimi pia nikabatizwa. Uthamini wangu wa kile ambacho kujiweka wakfu kwa Yehova huhusisha ulikuwa ukikua, nami nilikuwa nikijifunza kukubali mwelekezo wa Yehova. Mwaka huohuo, dada zangu wawili, Kathryn na Gertrude, wakabatizwa pia. Sote tukaanza utumishi wa wakati wote tukiwa mapainia.
Hata hivyo, hilo halikumaanisha kwamba hatukufikiria mambo mengine. Nilisikiliza kwa makini wakati shemeji yangu aliponiambia juu ya msichana mmoja mrembo sana aitwaye Ann, aliyekuwa amesisimuka sana aliposikia juu ya kweli naye alikuwa aje kwenye mikutano nyumbani kwetu. Wakati huo Ann alikuwa akifanya kazi ya ukarani katika ofisi ya kisheria, naye akabatizwa katika kipindi cha mwaka mmoja. Sikuwa nimepanga kuoa, lakini ilikuwa dhahiri kwamba Ann alipenda kweli kabisa. Alitaka kujihusisha kabisa na utumishi wa Yehova. Yeye hakuwa kamwe mtu wa kusema, “Naweza kufanya jambo hili?” Badala yake, angeuliza, “Ni njia gani bora zaidi ya kufanya jambo hili?” Naye aliazimia kutekeleza jambo hilo. Nilivutiwa na mtazamo huo wenye kufaa. Mbali na hayo, yeye alikuwa mrembo sana, naye bado ni mrembo. Alipata kuwa mke wangu, na muda si muda, akawa mwenzi wangu katika utumishi wa painia.
Mazoezi Yenye Thamani Tukiwa Mapainia
Tukiwa mapainia tulijifunza jinsi ya kuridhika tukiwa na chakula kingi na tukiwa na kidogo pia. (Wafilipi 4:11-13) Jioni ilikuwa ikikaribia siku moja, nasi hatukuwa na chakula chochote. Tulikuwa na senti tano tu za Marekani. Tuliingia katika duka la nyama, nami nikauliza, “Je, unaweza kutuuzia soseji ya senti tano?” Mwenye duka alitutazama, kisha akakata vipande vinne. Nina hakika soseji hiyo ilikuwa ya thamani kubwa kuliko senti tano, nayo ikawa kwetu chakula chenye lishe.
Lilikuwa jambo la kawaida kukabili upinzani mkali tukiwa katika utumishi. Katika mji mmoja karibu na Syracuse, New York, tulikuwa barabarani tukigawanya vikaratasi vya kukaribisha watu huku tukibeba mabango ya kuvuta fikira kwenye mkutano wa pekee wa watu wote. Watu wawili wa miraba minne wakanishika na kunisukuma-sukuma. Mmoja wao alikuwa ofisa wa polisi, lakini hakuwa amevaa yunifomu, naye akakataa ombi langu la kutaka nione beji yake. Ndipo Grant Suiter kutoka Betheli ya Brooklyn akaja wakati huohuo, akasema tungeenda kwenye kituo cha polisi ili kutatua jambo hilo. Ndipo akaipigia simu ofisi ya Sosaiti ya Brooklyn, na ili kuandaa kesi ya kuweka mwongozo, sisi wawili tukaagizwa tutoke tena siku hiyohiyo tukiwa na mabango na vikaratasi vya kukaribisha watu. Kama ilivyotarajiwa, tukakamatwa. Hata hivyo, tulipowaambia polisi hao kwamba wangeshtakiwa kwa kutukamata isivyo halali, wakatuachilia.
Siku iliyofuata matineja kadhaa wenye fujo wakavamia mahali tulipofanyia kusanyiko letu kwa kuchochewa na kasisi fulani, nao polisi hawakuonekana popote. Wahuni hao walipiga sakafu ya mbao kwa magongo ya besiboli, wakavurumisha chini baadhi ya wasikilizaji kutoka kwenye mabenchi, na kupanda kwenye jukwaa ambapo waliinua bendera ya Marekani na kusema kwa sauti kubwa, “Isalimuni! Isalimuni!” Kisha wakaanza kuimba wimbo mmoja maarufu wa Marekani. Walivunja mkutano huo kabisa. Tulikuwa tukipatwa moja kwa moja na yale Yesu aliyomaanisha aliposema: “Kwa sababu nyinyi si sehemu ya ulimwengu, bali nimewachagua nyinyi kutoka ulimwenguni, kwa ajili ya hili ulimwengu huwachukia.”—Yohana 15:19.
Hotuba hiyo ya watu wote ilikuwa hasa nakala ya hotuba iliyotolewa na J. F. Rutherford, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society wakati huo. Mimi na Ann tulikaa katika mji huo kwa siku kadhaa na kutembelea watu ili kuwatolea fursa ya kusikiliza hotuba hiyo nyumbani kwao. Baadhi yao walikubali toleo hilo.
Kujitolea Kutumikia Katika Nchi za Kigeni
Baada ya muda, njia mpya za utumishi zikatokea. Kaka yangu Russell na mke wake Dorothy, walialikwa kuhudhuria pamoja darasa la kwanza la Shule ya Gileadi, mwaka wa 1943, kisha wakatumwa Kuba wakiwa mishonari. Dada yangu Kathryn alikuwa katika darasa la nne. Yeye pia alipewa mgawo wa kwenda Kuba. Baadaye alipewa tena mgawo wa kwenda Jamhuri ya Dominika kisha Puerto Riko. Namna gani mimi na Ann?
Tuliposikia juu ya Shule ya Gileadi na uhakika wa kwamba Sosaiti ilitaka kutuma mishonari katika nchi nyingine, tuliona kwamba tungependa kujitoa kutumikia katika nchi za kigeni. Kwanza, tulifikiria kwenda bila kupewa mgawo, labda tuende Mexico. Lakini tukaamua kuwa ingekuwa vema zaidi kungoja na kuacha Sosaiti itupe mgawo baada ya kuhudhuria Shule ya Gileadi. Tuling’amua kwamba huo ulikuwa mpango ambao Yehova alikuwa akiutumia.
Tulialikwa kuhudhuria darasa la nne la Shule ya Gileadi. Lakini muda mfupi kabla ya darasa hilo kuanza, N. H. Knorr, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society wakati huo, akafahamu vema zaidi udhaifu mbalimbali wa Ann uliotokana na kuugua ugonjwa wa kupooza akiwa mtoto. Alizungumza nami kuhusu udhaifu huo na kuamua kwamba halingekuwa jambo la hekima kututuma kwenda kutumikia katika nchi nyingine.
Miaka miwili hivi baadaye, nilipokuwa nikifanya kazi ya kabla ya mkusanyiko, Ndugu Knorr akaniona tena, akaniuliza kama tulikuwa bado tunapendezwa na kuhudhuria Shule ya Gileadi. Aliniambia kwamba hatungepewa mgawo wa kwenda nchi za kigeni; alikuwa akifikiria jambo jingine. Kwa hiyo, darasa la tisa liliposajiliwa Februari 26, 1947, sisi tukawa miongoni mwa wanafunzi walioandikishwa.
Hatungeweza kusahau kamwe siku hizo tulizokuwa Gileadi. Mitaala ilikuwa na mambo mengi sana ya kiroho. Tulifanya urafiki wa maisha. Lakini kuhusika kwangu na shule hiyo kulitia ndani mambo mengi zaidi.
Katikati ya Washington na Gileadi
Shule ya Gileadi ilikuwa bado mpya kwa kadiri. Serikali ya Marekani haikuwa imefahamu vya kutosha malengo ya shule hiyo, hivyo maswali mengi yalikuwa yakiulizwa. Sosaiti ilitaka kuwa na mwakilishi huko Washington, D.C. Huko ndiko tulikotumwa miezi kadhaa baada ya kuhitimu kutoka Gileadi. Nilipaswa kuwasaidia wale walioalikwa kuja Gileadi kutoka nchi nyingine wapate viza na pia kuwasaidia wenye kuhitimu wapate hati za kisheria ili waweze kutumwa nchi za kigeni kwa kazi ya umishonari. Maofisa fulani walikuwa na maoni mazuri na wenye kusaidia. Wengine walichukia Mashahidi sana. Baadhi yao, waliokuwa na maoni ya kisiasa yenye nguvu, walisisitiza kwamba tulikuwa na uhusiano na watu waliowaona kuwa hawafai.
Mwanamume mmoja ambaye nilienda ofisini mwake alituchambua vikali kwa kuwa hatusalimu bendera au kwenda vitani. Baada ya yeye kupiga kelele kwa muda kuhusu hayo, hatimaye nilisema hivi: “Nataka ujue, nawe wajua, ya kuwa Mashahidi wa Yehova hawapigani vita na yeyote ulimwenguni. Sisi hatujiingizi katika shughuli za ulimwengu. Sisi hatupigani katika vita vyao wala hatushiriki katika siasa zao. Sisi ni wasiokuwamo kabisa. Tayari tumeshinda kabisa matatizo mnayokabili; sisi tuna umoja katika tengenezo letu. . . . Sasa, unataka tufanye nini? Je, unataka turudie njia yenu ya kufanya mambo na kuacha ile yetu?” Hakusema lolote baada ya hayo.
Tulitenga siku mbili kamili kila juma ili kushughulika na maofisa wa serikali. Mbali na hayo, tulikuwa tukitumikia tukiwa mapainia wa pekee. Wakati huo, hilo lilihusisha kutumia muda wa saa 175 katika huduma kila mwezi (baadaye muda huo ulibadilishwa ukawa saa 140), hivyo, mara nyingi tuliendelea na utumishi hadi usiku. Tulifurahia utumishi. Tuliongoza mafunzo mengi mazuri ya familia nzima-nzima, nazo zikafanya maendeleo mazuri. Mimi na Ann tuliamua tusipate watoto, lakini kwa njia ya kiroho, tumepata si watoto tu bali pia wajukuu na vitukuu. Wanatufurahisha kama nini!
Mwishoni mwa mwaka wa 1948, nilipata mgawo mwingine. Ndugu Knorr alinieleza kuwa Ndugu Schroeder, msajili na mmoja wa wafunzi wa Shule ya Gileadi, angeshughulika na kazi nyingine muhimu, hivyo nikaombwa niwe nikifundisha madarasa ya Gileadi ikihitajika. Huku nikiwa mwenye wasiwasi mwingi, nilirudi Gileadi, huko South Lansing, New York, tarehe 18 Desemba, nikiwa na Ann. Mwanzoni, tungekaa Gileadi kwa majuma kadhaa tu kila pindi, kisha tungerudi Washington. Hata hivyo, hatimaye ikatokea kwamba nilikaa zaidi Gileadi kuliko Washington.
Wakati huu, kama vile nilivyotaja awali, ndipo darasa la 21 la Gileadi lilipohitimu kwenye Stediamu ya Yankee jijini New York. Hivyo, nikiwa mmoja wa wafunzi, nilipata pendeleo la kushiriki katika programu hiyo ya kuhitimu.
Utumishi Kwenye Makao Makuu ya Ulimwengu
Katika Februari 12, 1955, tulianza mgawo mwingine wa utumishi. Tukawa washiriki wa familia ya Betheli kwenye makao makuu ya ulimwengu ya tengenezo la Yehova lenye kuonekana. Lakini hilo lingehusisha nini? Kimsingi, kuwa tayari kufanya kazi yoyote tuliyogawiwa na kushiriki katika kazi zilizohitaji mtu ashirikiane na wengine. Bila shaka, tulikuwa tumefanya hivyo hapo awali, lakini sasa tungeshirikiana na kikundi kikubwa zaidi—familia ya Betheli kwenye makao makuu. Tulikubali kwa furaha mgawo huu mpya kuwa uthibitisho wa mwelekezo wa Yehova.
Sehemu kubwa ya kazi yangu ilihusisha mambo yaliyohusiana na vyombo vya habari. Kwa sababu ya kutamani habari zenye kusisimua na kwa sababu ya kupata habari kutokana na vyanzo vyenye kutuchukia, waandishi wa habari walikuwa wameandika mambo mabaya kuhusu Mashahidi wa Yehova. Tulijitahidi sana kuboresha hali hiyo.
Ndugu Knorr alitaka kuwa na uhakika kwamba sisi sote tulikuwa na mengi ya kufanya, hivyo kulikuwa na migawo mingine pia. Baadhi ya migawo hiyo ilihitaji nitumie ustadi niliopata nikiwa msanii wa matangazo ya biashara. Mingine ilihusisha kituo cha redio cha Sosaiti, WBBR. Kulikuwa na kazi ya kufanya kuhusiana na sinema zilizofanyizwa na Sosaiti. Bila shaka, historia ya kitheokrasi ilifundishwa kwenye mtaala wa Gileadi, lakini sasa miradi mbalimbali ilianzishwa ili watu zaidi wa Yehova wafahamishwe kinaganaga historia hiyo ya tengenezo la kisasa la kitheokrasi, na kuufahamisha umma pia. Mazoezi ya Gileadi pia yalitia ndani kusema mbele ya watu, na kazi ilihitajika kufanywa ili mambo ya msingi ya kuzungumza mbele ya watu yaweze kupatikana kwa akina ndugu makutanikoni. Hivyo, kulikuwa na mengi ya kufanya.
Kuwa Gileadi kwa Ukawaida
Katika 1961, mazoezi ya waangalizi wasafirio na wafanyakazi wa ofisi za tawi yakiwa yanakaribia, Shule ya Gileadi ilihamishiwa Brooklyn, ambapo Watch Tower Society ina ofisi zake kuu. Nikarudi tena darasani—wakati huu nikiwa sifunzi tu badala ya wafunzi wengine, bali nikiwa mshiriki wa kawaida wa kitivo hicho. Ni pendeleo lililoje! Nina uhakika kabisa kwamba Shule ya Gileadi ni zawadi kutoka kwa Yehova, zawadi ambayo imenufaisha tengenezo lake lote lenye kuonekana.
Huko Brooklyn madarasa ya Gileadi yalikuwa na fursa ambazo wanafunzi wa madarasa yaliyotangulia hawakupata. Kulikuwa na wahadhiri wengi zaidi wenye kuzuru na ushirika wa karibu pamoja na Baraza Linaloongoza, na pia ushirika mkubwa pamoja na familia ya Betheli kwenye makao makuu. Pia iliwezekana kwa wanafunzi kupata mazoezi katika taratibu za ofisi, shughuli za makao ya Betheli, na katika kazi mbalimbali za kiwandani.
Kadiri miaka ilivyopita, idadi ya wanafunzi ilibadilika na idadi ya wafunzi vilevile. Mahali pa kufanyia shule hiyo pia palibadilishwa mara kadhaa. Sasa shule hiyo inafanyiwa katika mazingira yenye kupendeza ya Patterson, New York.
Kufanya Kazi Pamoja na Wanafunzi
Imekuwa furaha iliyoje kufundisha madarasa hayo! Hapa pana vijana ambao hawapendezwi na kufanya mambo katika mfumo wa zamani. Wao huacha nyuma familia zao, rafiki zao, makao yao na watu wenye kuzungumza lugha yao. Tabia ya nchi, chakula—kila kitu kitakuwa tofauti. Hata hawajui wataenda nchi gani, lakini mradi wao ni kuwa mishonari. Si lazima uwachochee watu wa aina hiyo.
Nilipoingia darasani, sikuzote nilikuwa na lengo la kufanya wanafunzi wastarehe. Hakuna mtu ajifunzaye vizuri ikiwa hajastarehe na ni mwenye wasiwasi. Ni kweli, nilikuwa mfunzi, lakini nilijua vile kuwa mwanafunzi kunavyomaanisha. Niliketi kwenye viti hivyo wakati mmoja. Bila shaka, walijifunza kwa bidii na kujua mengi huko Gileadi, lakini nilitaka pia wafurahie kuwa huko.
Nilijua kwamba walipoenda kwenye migawo yao, kungekuwa na mambo ambayo wangehitaji ili kufanikiwa. Walihitaji imani yenye nguvu. Walihitaji unyenyekevu—unyenyekevu mwingi sana. Walihitaji kujifunza kupatana na watu wengine, kukubali hali mbalimbali na kusamehe kwa hiari. Walihitaji kuendelea kusitawisha matunda ya roho. Walihitaji pia kupenda watu na kupenda kazi waliyotumwa kufanya. Hayo ndiyo mambo niliyojaribu kuwakazia wanafunzi daima walipokuwa Gileadi.
Kwa kweli sijui nimefunza wanafunzi wangapi. Lakini najua jinsi nihisivyo kuwahusu. Baada ya kukaa nao darasani kwa miezi mitano, niliwapenda sana. Kisha nilipowatazama wakipanda jukwaani kupokea diploma zao siku ya kuhitimu, nilijua kwamba walikuwa wamekamilisha mtaala huo kwa mafanikio na karibuni wangeondoka. Ilikuwa kana kwamba sehemu ya familia yangu ilikuwa ikiondoka. Ungewezaje kuepuka kuwapenda watu ambao walikuwa tayari kujitoa na kufanya kazi ambayo hawa vijana watakuwa wakifanya?
Miaka kadhaa baadaye, wanaporudi kutembea, mimi huwasikia wakisimulia furaha yao katika utumishi, nami hujua kwamba wangali katika migawo yao, wakifanya kile walichozoezwa kufanya. Hili hunifanya nihisije? Nakwambia, ninahisi vizuri sana.
Kuutazamia kwa Hamu Wakati Ujao
Macho yangu hayaoni vizuri sasa, nami hupatwa na vivunja moyo ambavyo huletwa na hali hiyo. Siwezi tena kufundisha katika darasa la Gileadi. Mwanzoni, ilikuwa vigumu kufanya rekebisho hilo, lakini maishani mwangu mwote nimejifunza kukubali hali na kuzivumilia. Mara nyingi mimi humfikiria mtume Paulo na “mwiba [wake] katika mwili.” Paulo alisali mara tatu kupata kitulizo kutokana na hali hiyo yenye kusumbua, lakini Bwana akamwambia: “Fadhili yangu isiyostahiliwa yakutosha wewe; kwa maana nguvu yangu inafanywa kamilifu katika udhaifu.” (2 Wakorintho 12:7-10) Paulo aliendelea kuvumilia hali hiyo. Ikiwa angeweza kufanya hivyo, mimi napaswa kujitahidi. Ingawa sifunzi tena darasani, ninashukuru kwamba ningali naweza kuwaona wanafunzi wakiingia na kuondoka kila siku. Wakati mwingine naweza kuzungumza nao, nami hufurahi kufikiria mtazamo mzuri wauonyeshao.
Yale yatakayotokea wakati ujao ni mazuri ajabu kuyafikiria. Msingi unawekwa sasa. Gileadi imetimiza fungu kubwa katika kuweka msingi huo. Baada ya dhiki kubwa, wakati hatikunjo zinazotajwa kwenye Ufunuo 20:12 zitakapofunguliwa, elimu zaidi yenye kina kuhusu njia za Yehova itatolewa kwa muda wa miaka elfu moja. (Isaya 11:9) Lakini mambo bado. Huo hasa ni mwanzo tu. Kwa umilele wote, kutakuwa na mengi zaidi ya kujifunza kumhusu Yehova na mengi zaidi ya kufanya huku tuonapo makusudi yake yakitimizwa. Nina uhakika kabisa kwamba Yehova atatimiza ahadi zake zote tukufu, nami nataka kuwapo kushiriki kukubali mielekezo ambayo Yehova atatutolea wakati huo.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Kuhitimu kwa wanafunzi wa Gileadi katika Stediamu ya Yankee ya New York mwaka wa 1953
[Picha katika ukurasa wa 26]
Gertrude, mimi, Kathryn, na Russell
[Picha katika ukurasa wa 26]
Nikifanya kazi ya kupanga mkusanyiko nikiwa pamoja na N. H. Knorr (mbali kushoto) na M. G. Henschel
[Picha katika ukurasa wa 26]
Nikiwa katika studio ya kutangazia habari ya WBBR
[Picha katika ukurasa wa 29]
Nikiwa katika darasa la Gileadi
[Picha katika ukurasa wa 31]
Nikiwa na Ann, hivi karibuni