Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 12/1 kur. 21-23
  • Wamisionari Zaidi kwa Ajili ya Mavuno ya Duniani Pote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wamisionari Zaidi kwa Ajili ya Mavuno ya Duniani Pote
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Habari Zinazolingana
  • Makao Mapya kwa Ajili ya Shule ya Umisionari ya Gileadi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Baraka za Elimu ya Gileadi Zaenea Ulimwenguni Pote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Mazoezi ya Gileadi Katika Imani Iliyo Takatifu Sana
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Shule ya Gileadi—Ina Umri wa Miaka 50 na Yaendelea Kufanikiwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 12/1 kur. 21-23

Wamisionari Zaidi kwa Ajili ya Mavuno ya Duniani Pote

SEPTEMBA ni mwezi wa mavuno kwa wakulima, lakini mavuno yenye maana zaidi yalivuta umati mkubwa kwenye Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova la Jersey City, ng’ambo ile nyingine tu ya Mto Hudson kutoka Jiji la New York, mnamo Septemba 8, 1991. Darasa la 91 la Watchtower Bible School of Gilead lilikuwa likihitimu. Washirika 4,263 hivi wa familia ya Betheli na wageni walioalikwa walikuwako, kukiwa na wengine 1,151 waliounganishwa kwa nyuzi za simu hadi makao makuu ya Brooklyn na mashamba ya Wallkill na Patterson.

Msimamizi wa shule ya Gileadi, Frederick W. Franz, anayekaribia umri wa miaka 98, alifungua programu kwa sala yenye kugusa moyo na yenye kicho kingi chenye staha. Albert D. Schroeder, mshirika wa Baraza Linaloongoza na msajili na mfunzi wa zamani wa shule hiyo, alitumikia akiwa mwenyekiti wa programu ya kuhitimu. Aliwakumbusha wahudhuriaji juu ya Zaburi 2:1, 2 na unabii mwingine mbalimbali uliotabiri kuhusu wakati huu wenye msukosuko na ghasia miongoni mwa mataifa. Hali hiyo ya mchafuko imemaanisha kufunguliwa kwa mashamba mengi mapya kwa ajili ya mavuno.

Hotuba ya kwanza ya siku hiyo ilitolewa na George M. Couch, mshirika wa Halmashauri ya Betheli. Kichwa chake kilikuwa “Hesabu Mibaraka Yako.” Aliwakumbusha wanafunzi wa Gileadi kwamba haiwi kamwe mapema mno kuanza zoea hilo. Alisema kwamba wanafunzi wenyewe walibarikiwa kwa hakika lakini kwamba mibaraka hiyo ilikuwa imekuja baada tu ya jitihadi nyingi. Vivyo hivyo, Yakobo mwenye umri wa miaka 97 alipigana mweleka na malaika usiku kucha—kwa ajili tu ya kupokea baraka moja. (Mwanzo 32:24-32) Ndugu Couch aliwasihi wanafunzi wasikaze fikira kwenye mawazo yasiyofaa bali wapate kuwa baraka kwa wengine kwa kusitawisha amani ya akili kupitia sala na kupiga moyo konde.

John E. Barr wa Baraza Linaloongoza alisema baadaye juu ya kichwa “Mpendane Nyinyi kwa Nyinyi.” Wafuasi wa Yesu walikuwa na nia ya kufa kwa ajili ya mmoja na mwenzake. “Je! mnahisi upendo wa aina hiyo ukibubujika mioyoni mwenu?” akauliza wanafunzi. ‘Bila upendo huo, akasema, sisi si kitu. Hivyo ndivyo ilivyo.’ (1 Wakorintho 13:3) Ndugu Barr alionyesha njia fulani zenye kutumika za kuonyesha upendo. Aliwatia moyo wanafunzi wawatendee wamisionari wenzao kwa staha, wakitafuta sikuzote njia yenye busara ya kusema mambo. ‘Sahauni matatizo madogo madogo,’ akawashauri, akitaja 1 Petro 4:8. Alionyesha kwamba hata siku za wamisionari za kupika zilikuwa pindi ambapo wangeweza kuonyesha upendo kwa kuona kazi hiyo kuwa zaidi ya wajibu tu usiopendeza. Aliwakumbusha wanafunzi hivi: “Hatuachi kamwe kuwiwa na ndugu na dada zetu upendo.”—Warumi 13:8.

“Una Uhakika Jinsi Gani?” ndicho kichwa chenye kupendeza kilichokuzwa na David A. Olson wa Halmashauri ya Idara ya Utumishi. Alikazia maeneo mawili ya uhakika: katika Yehova na tengenezo lake, tukiwa na sababu nyingi sana za kufanya hivyo (Mithali 14:6; Yeremia 17:8); na katika sisi wenyewe. Wamisionari wana sababu ya kuwa na kadiri fulani ya uhakika katika wao wenyewe, kama vile mandhari-nyuma yao ya kuwa wahudumu na amana ambayo Yehova na tengenezo lake limewakabidhi. Mtume Paulo alionyesha uhakika wa jinsi hiyo kwa sababu kama hizo. (1 Wakorintho 16:13; Wafilipi 4:13) Lakini, Ndugu Olson alionya dhidi ya kuwa na uhakika wa kupita kiasi unaoenezwa na ulimwengu, kama unavyotolewa mfano mzuri na mwandishi mashuhuri ambaye yaripotiwa alisema hivi: “Mara nyingi mimi hujinukuu. Hilo huongeza ladha kwa mazungumzo yangu.” Hata hivyo, uhakika unaposawazishwa na unyenyekevu waweza kuchochea uhakika katika wengine. Hilo kwa hakika lilikuwa kweli kwa habari ya Paulo.—Wafilipi 1:12-14.

Kisha Lyman A. Swingle wa Baraza Linaloongoza akawahimiza wanafunzi hivi: “Enendeni Mashambani Ili Kuvunwa, Enyi Wahitimu wa Gileadi!” Alisema kwamba hiyo ilikuwa siku ya mavuno kwa Shule ya Gileadi na kwa udugu wa ulimwenguni pote, wakati wahitimu wangeenda mbele na kuungana na maelfu wa wahitimu waliowatangulia ambao bado walikuwa katika kazi ya umisionari—wengine kutoka madarasa ya kwanza, ya pili, na ya tatu ya miaka ya 1940! Ndugu Swingle alisema kwamba wakati huo wa nyuma hakuna yeyote aliyejua kwamba kazi ya umisionari ingeendelea kwa miaka mingine 50, au kwamba Unazi, Ufashisti, na vizuizi vingine vya kiserikali kwa kazi ya kuhubiri vingeporomoka. “Ikiwa tunatiwa hofu na yale ambayo Yehova amefanya katika wakati uliopita,” akauliza, “vipi wakati ujao?” Alimaliza kwa mwito wenye kuchochea kwa wanafunzi: “Enendeni mashambani!”

Baada ya hapo Wafunzi wakuu wawili wa Shule ya Gileadi walihutubia darasa la 91 kwa mara ya mwisho. Jack D. Redford aliongea juu ya kichwa “Twaeni Hekima.” Shule ya Gileadi, akawaambia wanafunzi, hufundisha maarifa na uelewevu, lakini ni lazima wajitwalie hekima, uwezo wa kutumia maarifa yao kwa njia inayofaa. Aliwasihi wanafunzi wakatae ile hekaya kwamba wamejifunza yote kutoka Gileadi. “Ni yale unayojifunza baada ya shule ndiyo yaliyo na maana zaidi.” Miongoni mwa mambo ambayo ni lazima wajifunze bado ni: kushughulika na wengine kwa amani, kuweza kusema “Pole” kwa mwenzi, kwa wamisionari wenzao, na kwa ndugu na dada wa mahali pale; wawe na hadhari kutoamini maoni ya kwanza yenye kuvutia na kung’amua kwamba kila tatizo linahusisha mambo mengi, likihitaji uelewevu mwingi wa hali kabla ya kutoa shauri lenye hekima; na kustahi ndugu wa mahali fulani kwa uwezo wao wa kukabiliana na hali zilizo ngumu.—Mithali 15:28; 16:23; Yakobo 1:19.

Ulysses V. Glass, msajili wa Shule ya Gileadi, alifanya Wafilipi 3:16 kuwa kichwa cha hotuba yake. Aliwasifu darasa hilo kwa maendeleo waliyofanya na kuwahimiza waendelee kulingana na andiko hilo. Ingawa wanafunzi wapaswa waendelee kutwaa maarifa sahihi, alionyesha kwamba, hawangepata kamwe kujua kila kitu. Alitoa kielezi cha jambo hilo kwa kutumia saa yenye kuhesabu dakika kwa tarakimu badala ya mikono. Mwenye saa hiyo huenda akajua jinsi ya kuifanyiza kazi bila kujua jinsi hasa inavyofanya kazi. Vivyo hivyo, wamisionari hawapaswi kuwadharau wale ambao, ingawa hawana maarifa yenye kina kama wao, hujua jambo lililo la maana—jinsi ya kumhofu Yehova. (Mithali 1:7) Alikumbusha darasa umaana wa kudumisha ‘jicho sahili.’ (Mathayo 6:22, NW) Jicho la kiroho laweza kutatanishwa vile jicho la kimwili liwezavyo. Wengine, kwa mfano, hawana mwono wa kutazama mambo kwa maoni mapana—wakikazia fikira kwenye mambo machache sana hivi kwamba hawaoni picha nzima—hali wengine, tofauti na hao, huona mambo yasiyo na maana sana na hukengeushwa fikira kila mara kutoka kwa mambo yenye maana ambayo huhitaji kushughulikiwa nao.

Hotuba ya mwisho ya asubuhi hiyo ilikuwa na kichwa “Kutambulisha na Kufanya Kazi Pamoja na Tengenezo la Yehova,” iliyotolewa na Theodore Jaracz wa Baraza Linaloongoza. Ndugu Jaracz alisema kwamba ingawa kuna maelfu ya matengenezo na mashirika ulimwenguni, ni moja tu kati ya hayo yote ambalo halitokani na ulimwengu. Ni jinsi gani ya kutambua lile linalomwakilisha Yehova? Neno la Mungu linaandaa alama za kutambulisha. Biblia inaonyesha kwamba uumbaji wake wa kimbingu umepangwa kitengenezo kwa hali ya juu sana. (Zaburi 103:20, 21; Isaya 40:26) Tengenezo la Yehova la kidunia laweza pia kutambulishwa kwa utaratibu walo na pia kwa kutengwa kwalo na ulimwengu, kwa ushikamano walo na kanuni za Biblia, kwa kiwango chalo cha juu sana cha usafi wa kiadili, na kwa upendo ulio miongoni mwa washirika walo. Ndugu Jaracz alisihi wanafunzi wa Gileadi wasaidie wengi wawezavyo katika migawo yao watambulishe tengenezo la Yehova Kimaandiko. Kufuatana na hilo, alitoa tangazo lenye kusisimua: Shule ya Gileadi karibuni itaongezeka ukubwa mara mbili, kuwa na wanafunzi 50 hivi katika darasa la 93! Pia, madarasa ya Shule ya Upanuzi ya Gileadi katika Ujerumani yataanza katika wakati karibu na huo. Makofi yalipigwa kwa muda mrefu na kwa kishindo kikubwa sana!

Ukiwa upeo wa asubuhi hiyo, wanafunzi wote 24 wa Gileadi walipokea diploma zao. Karibuni wangekuwa njiani kuelekea nchi 12 tofauti-tofauti kuzunguka ulimwengu. Darasa hilo lilitoa azimio lenye kuhisiwa moyoni, wakishukuru Baraza Linaloongoza na familia ya Betheli. Baada ya chakula cha mchana, Ndugu Charles J. Rice wa Halmashauri ya Watchtower Farms aliongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi lililofupishwa. Kisha wahitimu wakatokeza programu changamfu, wakiigiza maono fulani waliyokuwa nayo katika utumishi wa shambani katika muda wa mtaala wao wa miezi mitano huko Wallkill, New York. Baada ya hapo, wahubiri waliowakilisha makundi kadhaa ya mahali hapo walifanya drama yenye kichwa Vijana Wanaomkumbuka Muumba Wao Sasa.

Kufunga programu, Ndugu George Gangas, mshirika wa Baraza Linaloongoza aliye na umri wa miaka 95, alimtolea Yehova sala yenye uhai kama kawaida yake. Wahudhuriaji waliondoka wakiwa na furaha, kila mmoja wao bila shaka akiwa amesukumwa kuwa na ushiriki mkubwa zaidi katika kazi ya mavuno ya duniani pote.

[Picha katika ukurasa wa 22]

Takwimu za Darasa

Hesabu za nchi zenye kuwakilishwa: 6

Hesabu za nchi walikogawiwa: 12

Hesabu ya wanafunzi: 24

Hesabu ya wenzi wa ndoa: 12

Umri wa wastani: 33.4

Wastani wa miaka katika kweli: 16.13

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 11.3

[Picha katika ukurasa wa 23]

Darasa la 91 la Kuhitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Mnara wa Mlinzi

Katika orodha iliyopo chini, mistari imepewa namba kuanzia mbele mpaka nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto mpaka kulia katika kila mstari

(1) McDowell, A.; Youngquist, L.; Skokan, B.; Wargnier, N.; Miller, Y.; Muñoz, M. (2) Bales, M.; Perez, D.; Attick, E.; Vainikainen, A.; Mostberg, K. (3) DePriest, D.; DePriest, T.; Perez, R.; Wargnier, J; Muñoz, J.; Miller, J. (4) McDowell, S.; Bales, D.; Skokan, M.; Attick, C.; Youngquist, W.; Vainikainen, J.; Mostberg, S.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki