Baraka za Elimu ya Gileadi Zaenea Ulimwenguni Pote
ELIMU katika ulimwengu huu wa kale una thamani ndogo tu. Kwa kuwa inategemea hasa mawazo ya kibinadamu badala ya kweli ya Mungu, haiwezi kutoa kusudi la kweli maishani. Lakini Shule ya Gileadi ni tofauti. Katika maneno yake ya utangulizi kwenye uhitimu wa darasa la 93 la Gileadi, Theodore Jaracz wa Baraza Linaloongoza alieleza kwamba shule hiyo huandaa elimu yenye maana ya kweli. Kama vile Zaburi 119:160 husema, “Jumla ya neno [la Mungu] ni kweli.” Kwa hiyo wasikilizaji karibu 6,000 walisikiliza wakiwa na msisimuko mwingi programu hiyo ya uhitimu katika Septemba 13, 1992.
Hotuba ya kwanza ya asubuhi, iliyotolewa na Lon Schilling (Shiling) wa Halmashauri ya Watchtower Farms ilikuwa na kichwa “Endeleeni Kuushinda Ulimwengu na Mtawala Wao.” Ndugu Schilling alikazia Ufunuo 12:11 na kuonyesha kwamba mstari huo huonyesha njia tatu za kushinda: (1) kupitia damu ya Mwana-Kondoo, (2) kupitia kutoa ushahidi, na (3) kwa kuwa na roho ya kujidhabihu. Aliwakumbusha wanafunzi kwamba watumishi wa Yehova wengi wameonyesha roho hiyo na hata wamekabili kifo kwa nia ili kuhifadhi uaminifu-mshikamanifu na uaminifu-maadili wao.
“Lindeni Amana Yenu Nzuri” ndicho kichwa kilichokuzwa na John E. Barr wa Baraza Linaloongoza. Kwa sauti yenye uchangamfu iliyo kawaida yake, alilinganisha ile amana ya mmoja kwa mwenzake iliyo kati ya Yehova na watumishi wake na amana inayositawishwa katika ndoa nzuri. Akitumia habari kutoka 2 Timotheo 1:12, 13, aliwahimiza wanafunzi walinde amana yao kwa kushikilia kwa kuthamini sana “kielelezo cha maneno yenye uzima” katika Biblia. Alikazia kufanya funzo la kibinafsi liwe sehemu ya muhimu ya ratiba ya kila siku na akahimiza wanafunzi kwa fadhili wasiache kamwe maelezo yao mikutanoni yawe ya kidesturi tu lakini kuyafanya yawe yenye maana sikuzote.
William Van De Wall wa Halmashauri ya Idara ya Utumishi alitoa hotuba iliyofuata, “Onyesheni Hangaikio Lenye Upendo Kwa Watu Wenye Mfano wa Kondoo.” Aliwauliza wanafunzi sifa ambazo wangetaka daktari wa familia yao awe nazo akawahimiza wasitawishe hisia-mwenzi, huruma, na rehema hiyohiyo ambayo wangethamini.
Daniel Sydlik (Sidlik) wa Baraza Linaloongoza alisema kwa njia yenye kuchochea juu ya kichwa “Mambo Yote Yanawezekana kwa Mungu.” Aliwakumbusha wanafunzi kwamba Abrahamu na Sara walichekelea lile taraja lililoonekana kutowezekana la kuwa na mwana katika umri wao wa uzee. Ahadi nyingi za Mungu zinaonekana kutowezekana kwa maoni ya kibinadamu; lakini kama vile malaika alivyomwuliza Abrahamu, “kuna neno gani lililo gumu la kumshinda BWANA [Yehova, NW]?” (Mwanzo 18:14) Ndugu Sydlik aliwahimiza wanafunzi waonyeshe imani katika uwezo wa Mungu wa kufanya yasiyowezekana, wasiache kamwe imani hiyo ififie au iyumbeyumbe, haidhuru ni majaribu gani huenda wakakabili.
Wafunzi Watoa Shauri
Wafunzi wawili wa Gileadi walisema baada ya hapo. Kwanza, Jack D. Redford alikuza kichwa “Kufanya Jina Zuri na Mungu.” Kile kifanyacho jina kuwa baya au zuri, akasababu, ni mtu mwenye jina hilo. Alitofautisha majina kama vile Adamu, Nimrodi, Yezebeli, Sauli, na Yuda na majina kama vile Noa, Abrahamu, Ruthu, Paulo, na Timotheo. Kila jina lina mawazo na hisia nyingi zinazolihusu kwa sababu ya mwendo wa maisha wa mwenye jina hilo. Aliwauliza wanafunzi ni aina gani ya jina ambalo wangekuwa nayo miaka 10, 100, au hata 1,000 baadaye—jina la mtu mwenye kuacha kazi bila kutimiza au mlalamikaji au lile la mishonari mwaminifu? Kazia fikira masuluhisho na makusudio kuliko matatizo, akawashauri.
“Unalinda Imani Yako Vema Kadiri Gani?” ndicho kichwa chenye kuchochea fikira kilichokuzwa na Ulysses V. Glass. Alifananisha imani imara na dira nzuri inayoelekeza kwenye njia ifaayo sikuzote. Dira katika gari yaweza kuathiriwa na ugasumaku nyinginezo zaidi ya zile za dunia, uga hizo zahitaji kukatishwa. Vilevile, ulimwengu huu wa zamani hutokeza uvutano mwingi uwezao kukengeusha au kudhoofisha imani yetu tukiuruhusu. Alipoonya darasa dhidi ya uvutano huo, Ndugu Glass aliwapongeza pia kwa kufahamu kwao sana mitazamo na hisia za wengine.
Hotuba ya mwisho ya asubuhi hiyo ilitolewa na Albert D. Schroeder (Shroda), mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Aliwatia moyo wanafunzi “Dumisheni Roho ya Umishonari,” akiwapongeza kwa kuonyesha roho ileile ya umishonari kama vile darasa la kwanza lilivyoonyesha katika 1943, alipokuwa akitumikia akiwa msajili wa shule. Alisema kwamba walikuwa wenye kupendezwa na watu, wahubiri kiasili, wanaopenda kuongozwa na roho ya Mungu. Endeleeni kukuza roho hiyo, mkitumia New World Translation kikamili katika funzo la kibinafsi, akahimiza. Alimalizia na mazungumzo ya mstari kwa mstari ya Zaburi 24 ikiwa kielelezo.
Halafu, wanafunzi wa Gileadi wakawa wahitimu wa Gileadi! Walipewa diploma zao wakati migawo yao ya mishonari ilipokuwa ikisomwa kwa sauti kubwa, ikiambatana na makofi mengi kutoka kwa wasikilizaji.
Katika alasiri, Calvin Chyke (Chaiki) wa Halmashauri ya Kiwanda aliongoza funzo la Mnara wa Mlinzi. Programu ya wanafunzi yenye kupendeza ikafuata, iliyohusu maono ya wanafunzi shambani wakati wa muda wa mtaala huo wa miezi mitano na ilionyesha pia slaidi za baadhi ya nchi walikogawiwa. Kwa kuongezea, wenzi wa ndoa wenye umri mkubwa zaidi walihojiwa, na wakashiriki baadhi ya hekima na ujuzi ambao wamepata kutoka kwa miaka mingi wakiwa wamishonari. Alasiri ilimalizia kwa drama ya wakati unaofaa ikiwa na kichwa Msidanganyike au Kumdhihaki Mungu.
Wasikilizaji waliondoka wakiwa wamechangamshwa, wakisisimuka kuona kile ambacho elimu katika kweli ya Mungu iwezacho kufanya na wakifurahi kujua kwamba manufaa za elimu hiyo zitaendelea kuhisiwa ulimwenguni pote. Wamishonari hao 48 wanapoondoka kwenda kwenye migawo yao, sala nyingi zinawafuata, zikionyesha tumaini na uhakika wenye kuhisiwa moyoni kwamba hao waaminifu watakuwa baraka kwa watu wa Mungu kokote wanakoenda.
[Sanduku katika ukurasa wa 19]
Takwimu za Darasa
Hesabu ya nchi zenye kuwakilishwa: 7
Hesabu ya nchi walikogawiwa: 18
Hesabu ya wanafunzi: 48
Hesabu ya wenzi wa ndoa: 24
Wastani wa umri: 32.8
Wastani wa miaka katika kweli: 15.3
Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 10.4
[Sanduku katika ukurasa wa 20]
DARASA-NYONGEZA LA GILEADI LAHITIMU
Katika Juni 21, 1992, kikundi cha wamishonari 24 walihitimu kutoka darasa la nne la Shule-Nyongeza ya Gileadi katika Selters/Taunus, Ujerumani. Darasa hilo, lenye waliooana 11 na dada waseja 2 waliotoka nchi saba, walikuwa na wastani wa umri wa miaka 32, miaka 14 tangu ubatizo, na miaka 8.5 ya utumishi katika kazi ya kueneza evanjeli wakati wote. Zaidi ya 2,000 walihudhuria uhitimu huo.
Ndugu Jaracz alifungua programu hiyo kwa mazungumzo juu ya Mithali 11:24, linalosema hivi: “Kuna atawanyaye, lakini huongezewa zaidi.” Alisema kwamba wanafunzi walikuwa karibu kutawanywa na kwa hakika wangeendeleza ongezeko.
Hotuba zenye kutia moyo zilitolewa na Richard Kelsey, mratibu wa Halmashauri ya Tawi ya Ujerumani; Wolfgang Gruppe wa Idara ya Utumishi; Werner Rudtke na Edmund Anstadt, ambao pia ni washiriki wa Halmashauri ya Tawi; na wafunzi wawili, Dietrich Förster na Lothar Kaemmer. Albert Schroeder wa Baraza Linaloongoza alitoa ile hotuba kuu yenye kupendeza iliyokuwa na kichwa “Endeleeni Kuwa Watafutaji-tafutaji Vito vya Kiroho.” Upeo wa programu ulikuwa utoaji wa migawo kwenye nchi 11 katika Afrika, Amerika ya Kati, Ulaya ya Mashariki, na baada ya hayo mhitimu mmoja alisoma barua kutoka kwa darasa kupelekwa kwa Baraza Linaloongoza yenye kuonyesha uthamini wenye kuhisiwa moyoni.
[Picha katika ukurasa wa 18]
Darasa la 93 la kuhitimu la Watchtower Bible School of Gilead
Katika orodha iliyopo chini, mistari imepewa nambari kuanzia mbele kurudi nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila mstari.
(1) Hitesman, C.; West, P.; Evans, D.; Hipps, M.; Simonelli, N.; Wood, S.; Corkle, M.; Flores, C.; Thomas, J. (2) Jones, M.; Nissinen, J.; Sponenberg, M.; Zachary, K.; Ravn, G.; Backman, M.; Wettergren, A.; Evans, D.; Flores, R.; Caporale, G. (3) Simonelli, N.; Rechsteiner, M.; Rechsteiner, M.; Ruiz-Esparza, L.; Gerbig, B.; Simpson, C.; Zanewich, C.; Zachary, B.; Ricketts, L.; (4) Simpson, J.; Backman, J.; Corkle, G.; Gerbig, M.; Ricketts, B.; Bagger-Hansen, L.; Jones, A.; Zanewich, K.; Ravn, J.; Hipps, C. (5) Sponenberg, S.; Hitesman, A.; Caporale, L.; Ruiz-Esparza, S.; Thomas, R.; Bagger-Hansen, B.; Wood, M.; West, M.; Wettergren, C.; Nissinen, E.