Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 12/1 kur. 21-25
  • Shangwe Ambayo Kumtumikia Yehova Kumeniletea

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Shangwe Ambayo Kumtumikia Yehova Kumeniletea
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kukua Katika United States
  • Kutoka Kazi ya Redio Hadi Gerezani
  • Huduma ya Wakati Wote
  • Uzazi na Kuhubiri Chini ya Marufuku
  • Kuwalea Watoto Wetu Katika United States
  • Kutumika Katika Peru
  • Ekwedori Inaita
  • Maisha ya Kutajirisha, Yenye Kuthawabisha
  • Wamishonari Wasukuma Mpanuko wa Ulimwenguni Pote
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kutafuta Ufalme Kwanza Huridhisha na Huleta Furaha Maishani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Sehemu ya 4—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kukaza Macho na Moyo Kwenye Tuzo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 12/1 kur. 21-25

Shangwe Ambayo Kumtumikia Yehova Kumeniletea

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA GEORGE BRUMLEY

Nilikuwa nimemaliza tu kufundisha darasa la redio kwa wanafunzi polisi wachanga wa Maliki Haile Selassie wakati mmoja wao aliponiambia kifaragha kwamba alijua ya kwamba nilikuwa mishonari wa Mashahidi wa Yehova. “Je! waweza kujifunza Biblia na mimi?” akauliza kwa hamu.

KWA kuwa kazi yetu ilikuwa imepigwa marufuku katika Ethiopia, ningaliondoshwa nchini, kama vile Mashahidi wengine walikuwa wameondoshwa, ikiwa wenye mamlaka wangepata kujua juu yangu. Nilitaka kujua ikiwa mwanafunzi huyo alikuwa mwenye moyo mweupe au ikiwa alikuwa mpelelezi wa serikali aliyetumwa kuninasa. Nikiwa kichwa cha familia mwenye watoto wadogo watatu wa kulea, wazo la kupoteza kazi yangu na kulazimishwa kuacha nchi hiyo na marafiki niliopata kuwapenda lilinihofisha.

‘Lakini’ huenda ukauliza, ‘Mwamerika mwenye familia ya kutegemeza alikujaje kupendelea kuishi katika kaskazini mwa Afrika, mbali na nyumbani na watu wa ukoo?’ Niruhusu nieleze.

Kukua Katika United States

Katika miaka ya 1920, nilipokuwa ningali katika shule ya msingi, baba yangu aliandikisha gazeti Mnara wa Mlinzi na akapokea seti ya vitabu Studies in the Scriptures. Baba alifurahia kusoma na akavisoma vitabu hivyo kwa hamu sana. Alikuwa mtu mwenye kuchekesha-chekesha na kutania-tania, kama inavyoonyeshwa na njia ambayo angefanya vitimbi na wageni ambao angealika siku za Jumapili. Alikuwa na kitabu kizuri cha majalada ya ngozi chenye maneno “Biblia Takatifu” katika herufi za dhahabu kwenye upande wa mbele na mgongoni. Alikuwa akianza mazungumzo kwa kusema, “Naam, ni Jumapili. Je! waweza kutusomea mistari michache?”

Mgeni alikubali sikuzote, lakini alipofungua kitabu hicho, hakuna hata ukurasa mmoja uliokuwa na maandishi! Bila shaka, mtu huyo angeshangaa. Halafu baba alikuwa akisema kwamba ‘wahubiri hawajui lolote juu ya Biblia,’ kisha alikuwa akichukua nakala ya Biblia na kusoma Mwanzo 2:7. Hapo, ikieleza juu ya uumbaji wa mwanadamu wa kwanza, Biblia husema hivi: “Mtu akawa nafsi hai.”—Mwanzo 2:7.

Baba alikuwa akifafanua kwamba mtu hana nafsi bali ni nafsi, kwamba mshahara wa dhambi ni kifo, na kwamba mtu anapokufa, amekufa kwa kweli, bila ufahamu wa lolote. (Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4; Warumi 6:23) Hata kabla sijajua kusoma vema, nilikuwa nimeshika maneno ya Mwanzo 2:7. Hizo ndizo kumbukumbu za kwanza nilizo nazo za jinsi ilivyo shangwe kwa kweli kujua kweli za Biblia na kuzishiriki pamoja na wengine.

Kwa kuwa wakati huo tulikuwa tukipokea Mnara wa Mlinzi nyumbani kwetu, familia nzima ilianza kufurahia chakula hicho cha kiroho. Nyanya yangu kutoka upande wa mama yangu alikuwa akiishi nasi, naye alikuwa mhubiri wa kwanza wa habari njema katika familia yetu. Hakukuwa kundi katika Carbondale, Illinois, tulikoishi, lakini mikutano isiyo rasmi ilifanywa. Mama alikuwa akitupeleka sisi watoto watano hadi ng’ambo ile nyingine ya mji ambako wanawake wazee-wazee walikuwa wakiongoza funzo la Mnara wa Mlinzi. Sisi pia tukaanza kushiriki katika huduma ya shambani.

Kutoka Kazi ya Redio Hadi Gerezani

Nilifunga ndoa katika 1937 nilipokuwa mwenye miaka 17 tu. Nilijaribu kupata riziki kwa kutengeneza redio na pia kufundisha ustadi huo. Baada ya kuzaliwa kwa watoto wawili, Pegi na Hank, ndoa yangu ilivunjika. Talaka hiyo ilikuwa kosa langu; sikuwa ninaishi maisha ya Kikristo. Jambo la kwamba sikupata kuwalea watoto wangu wawili wenye umri mkubwa zaidi limeniumiza moyo katika maisha yangu yote.

Vita ya Ulimwengu 2 ilianza na ikanifanya nifikirie juu ya mambo mengi. Vikundi vya kijeshi vilinitolea nafasi ya kuwa luteni na kufundisha redio kwa wanajeshi wapya, lakini kufikiria kwangu juu ya maoni ya Yehova juu ya vita kulinichochea nianze kusali kila siku. Andikisho langu la Mnara wa Mlinzi lilikuwa limeisha, na Lucille Haworth alipokea taarifa ya kumalizika kwalo akanitembelea. Perry Haworth, aliyekuwa baba ya Lucille, na wengi wa familia yake kubwa walikuwa wamekuwa Mashahidi tangu miaka ya 1930. Tukapendana na Lucille na kufunga ndoa katika Desemba 1943.

Katika 1944, nilibatizwa na kujiunga na mke wangu katika huduma ya wakati wote nikiwa painia. Upesi niliitwa kujiunga na jeshi lakini nikakataa kujiandikisha. Kwa sababu hiyo, nilipokea hukumu ya miaka mitatu katika gereza la serikali katika El Reno, Oklahoma. Ilikuwa shangwe kuteseka kwa ajili ya Yehova. Kila asubuhi nilipoamka na kutambua nilikokuwa na sababu ya kuwa huko, nilihisi uradhi mwingi na nikamshukuru Yehova. Baada ya vita sisi tuliokuwa wenye miaka zaidi ya 25 tulianza kufunguliwa kwa masharti. Niliachiliwa katika Februari 1946.

Huduma ya Wakati Wote

Nilipoungana tena na Lucille, alikuwa akipainia katika ule mji mdogo wa Wagoner, Oklahoma. Hatukuwa na gari, kwa hiyo tulitembea kila mahali, tukieneza mji mzima. Baadaye tulihamia Wewoka, Oklahoma. Upesi nilipata kazi kwenye stesheni ya redio nikaanza kazi ya kusambaza habari. Kufanya kazi muda wa saa sita kila siku na kutimiza saa za painia hakukuwa rahisi, lakini tulishangilia kwa ajili ya lile pendeleo tulilokuwa nalo katika kumtumikia Yehova. Tuliweza kununua gari kwa wakati uliofana na mkusanyiko katika Los Angeles katika 1947. Huko tukaanza kufikiria juu ya kupeleka maombi ya Watchtower Bible School of Gilead kwa ajili ya mazoezi ya umishonari.

Tulitambua ya kwamba hiyo ingekuwa hatua kubwa, na hatukutaka kuwa wepesi sana wa kufanya uamuzi wa kuondoka United States. Nilikuwa bado nimehuzunika sana kwa habari ya kupoteza watoto wangu, kwa hiyo nilijaribu tena kuwapata chini ya utunzaji wangu. Kwa sababu ya mtindo-maisha wangu wa zamani na kwa kuwa nilikuwa nimekwisha fungwa gerezani, hilo halikufaulu. Kwa hiyo tuliamua kujaribu kuwa wamishonari. Tulialikwa kwenye darasa la 12 la Gileadi.

Tulihitimu shule katika 1949, lakini mwanzoni tulipewa mgawo wa kutembelea makundi katika Tennesse. Baada ya miaka mitatu ya kazi ya kusafiri katika United States, tulipokea barua kutoka ofisi ya msimamizi wa Watch Tower Society ikituuliza kama tungekuwa na nia ya kufundisha shule katika Ethiopia kuongezea kufanya kazi ya kuhubiri. Takwa moja la serikali hiyo lilikuwa kwamba wamishonari wafundishe. Tulikubali, na katika kiangazi cha 1952, tuliondoka kwende Ethiopia.

Tulipofika Ethiopia, tulifundisha madarasa ya shule ya msingi asubuhi na kuongoza madarasa ya Biblia bila malipo alasiri. Upesi wengi sana walianza kuja kwenye mafunzo ya Biblia hivi kwamba mara nyingi tulikuwa tukifundisha Biblia muda wa saa tatu au nne kila siku. Baadhi ya wanafunzi hao walikuwa polisi; wengine walikuwa walimu au mashemasi katika shule za mishonari na shule za Dini ya Orthodoksi ya Kiethiopia. Nyakati nyingine kulikuwako 20 au zaidi katika kila darasa la funzo la Biblia! Wanafunzi wengi waliacha dini bandia na kuanza kumtumikia Yehova. Tulisisimuka sana. Tena, nilipoamka kila asubuhi, nilimshukuru Yehova.

Uzazi na Kuhubiri Chini ya Marufuku

Katika 1954 tulipata kujua kwamba tungekuwa wazazi, kwa hiyo tulihitaji kuamua ama kurudi United States ama kubaki Ethiopia. Bila shaka, kubaki kungetegemea kupata kwangu kazi ya kimwili. Nilipata kazi nikiwa mha-ndisi wa kusambaza habari, nikimwendeshea Maliki Haile Selassie stesheni ya redio. Kwa hiyo tulibaki.

September 8, 1954, binti yetu Judith alizaliwa. Nilifikiri kwamba nilikuwa na usalama wa kazi kwa sababu ya kumfanyia kazi maliki, lakini baada ya miaka miwili nilipoteza kazi yangu. Hata hivyo, katika muda unaopungua mwezi mmoja, niliajiriwa kazi na Idara ya Polisi—na kwa mshahara wa juu zaidi—kufundisha darasa la vijana kutengeneza redio za kupokea na kutoa habari. Katika miaka mitatu iliyofuata, wana wetu Philip na Leslie walizaliwa.

Wakati uleule uhuru wetu wa kushiriki katika kazi ya kuhubiri ilikuwa ikibadilika. Kanisa la Orthodoksi la Ethiopia lilikuwa limeishawishi serikali iondoshe wamishonari wote wa Mashahidi wa Yehova. Kwa kushauriwa na Sosaiti, nilibadili visa yangu kutoka kazi ya mishonari hadi kazi ya kimwili. Kazi yetu ya mishonari ilipigwa marufuku, tukalazimika kuwa wenye hadhari na busara. Mikutano yote ya kundi iliendelea, lakini tulikutana katika vikundi vidogo vya funzo.

Polisi walipekua-pekua nyumba za watu waliodhaniwa kuwa Mashahidi. Hata hivyo, bila wao kujua, luteni wa polisi mmoja aliyekuwa mwabudu wa Yehova alitutahadharisha sikuzote wakati upekuzi huo ungefanywa. Likiwa tokeo, hakuna fasihi zozote zilizochukuliwa miaka hiyo. Tulifanya Mafunzo ya Mnara wa Mlinzi yetu Jumapili kwa kwenda kwenye mikahawa ukingoni mwa mji ambako meza za mandari zilipatikana ili kuweza kula nje.

Ni wakati huo, nilipokuwa nikifundisha redio kwa wanafunzi polisi, kwamba mwanafunzi yule niliyekuwa nimemtaja mwanzoni aliniomba funzo la Biblia. Nilidhani kwamba alikuwa mwenye moyo mweupe, kwa hiyo tulianza. Baada ya mafunzo mawili tu, mwanafunzi wa pili alikuja pamoja naye, kisha wa tatu. Niliwatahadharisha wasimwambie kamwe mtu yeyote kwamba walikuwa wakijifunza na mimi, na hawakufanya hivyo kamwe.

Katika 1958 Kusanyiko la Kimataifa la Mapenzi ya Kimungu lilifanywa katika Stediamu ya Yankee ya New York na Polo Grounds. Wakati huohuo Pegi na Hank, pamoja na washiriki wengine wengi wa familia yangu kubwa, walikuwa wamekuwa Mashahidi wenye bidii. Nilifurahia kama nini kuweza kuhudhuria! Sikufurahia tu muungano pamoja na watoto wangu wawili wenye umri mkubwa zaidi na washiriki wengine wa familia bali pia nilisisimuka kuona umati huo mkubwa mno wa watu zaidi ya robo ya milioni wakiwa wamekusanyika kwenye siku ya mwisho ya mkusanyiko huo!

Mwaka uliofuata msimamizi wa Sosaiti, Nathan H. Knorr, alikuja kututembelea katika Ethiopia. Alikuwa na madokezo mazuri juu ya kuendeleza kazi chini ya marufuku na alipendezwa pia na familia yetu na jinsi tulivyokuwa tukifanya kiroho. Nilieleza kwamba tulikuwa tukiwafundisha watoto kusali. Nilimwuliza kama angependa kumsikiliza Judith akisali. Alisema ndiyo, na baadaye akamwambia: “Hiyo ilikuwa nzuri sana, Judith.” Halafu wakati wa mlo nilimwomba Ndugu Knorr kama angetutolea sala, na alipomaliza, Judith akasema: “Hiyo ilikuwa nzuri sana, Ndugu Knorr!”

Kuwalea Watoto Wetu Katika United States

Kandarasi (mkataba) yangu na Idara ya Polisi ilimalizika katika 1959. Tulitaka kubaki, lakini serikali ilikataa kukubali kandarasi zangu mpya. Kwa hiyo tungeweza kwenda wapi? Nilijaribu kuingia nchi nyinginezo kulimokuwa na uhitaji mkubwa wa ndugu lakini sikuweza kufanya hivyo. Tukiwa tumehuzunika kwa kadiri fulani, tulirudi United States. Tulipowasili, tulikuwa na muungano wa familia wenye shangwe. Watoto wangu wote watano walipata kufahamiana wakapendana mara tu ya kukutana. Wamekuwa karibu tangu wakati huo.

Tulikaa katika Wichita, Kansas, ambako nilipata kazi nikiwa mhandisi wa redio na mtangaza muziki wa redio. Lucille alianza kuzoea kufanya kazi za nyumbani, na watoto walihudhuria shule karibu na nyumbani. Niliongoza funzo la Mnara wa Mlinzi la familia kila Jumatatu usiku, nikijaribu sikuzote kulifanya liwe lenye shauku na lenye kupendeza. Tulichunguza kila siku kuona kama kulikuwako matatizo yoyote shuleni.

Watoto mmoja mmoja walipojiunga katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, mazoezi hayo yaliwasaidia na elimu yao. Tuliwazoeza kutoka utoto katika utumishi wa shambani. Walijifunza kutoa fasihi za Biblia kwenye milango, na walienda nasi kwenye mafunzo ya Biblia nyumbani.

Tulijaribu pia kuwafundisha watoto mambo ya msingi juu ya maisha, tukieleza kwamba kila mmoja wao asingeweza sikuzote kuwa na kile ambacho mmoja wa wale wengine alikuwa nacho. Kwa mfano, zawadi ileile haingeweza kupatikana kwa wote. “Iwapo ndugu au dada yako apokea kitu cha kuchezea,” tulikuwa tukisababu nao, “na wewe haupati kimoja, je, inafaa ulalamike?” Bila shaka, nyakati nyingine watoto wale wengine walipokea kitu fulani, kwa hiyo hakuna aliyepuuzwa. Tuliwapenda wote sikuzote, kutokumpendelea kamwe mmoja zaidi ya wale wengine wawili.

Nyakati nyingine watoto wengine waliruhusiwa wafanye mambo ambayo watoto wetu hawakuruhusiwa kufanya. Mara nyingi nilisikia, “Fulani anaweza kufanya hivyo, kwa nini sisi hatuwezi?” Nilijaribu kueleza, lakini nyakati nyingine jibu lililazimika kuwa tu, “Wewe si wa familia hiyo; wewe ni mmoja wa akina Brumley. Sisi tuna kanuni tofauti.”

Kutumika Katika Peru

Tangu kurudi kutoka Ethiopia, Lucille na mimi tulikuwa tumetamani kushiriki katika kazi ya mishonari tena. Mwishowe, katika 1972, nafasi ikaja kwenda Peru, Amerika Kusini. Peru ikawa mahali bora zaidi pa kuwalea watoto wetu katika miaka yao ya utineja. Ushirika waliofurahia pamoja na wamishonari, mapainia wa pekee, na wengine waliokuwa wamekuja kutumika uliwasaidia wajionee wenyewe jinsi walivyo na shangwe wale ambao kwa kweli hutafuta masilahi ya Ufalme kwanza. Philip aliuita ushirika wake mbano wa marika unaofaa.

Baada ya muda fulani marafiki wa zamani kutoka Kansas walipata habari juu ya kadiri ya mafanikio tuliyokuwa nayo katika huduma ya Ufalme, wakajiunga nasi katika Peru. Nilipanga nyumba yetu kama makao ya mishonari. Kila mmoja aligawiwa wajibu mbalimbali ili sisi sote tuwe na wakati wa kufurahia huduma ya shambani. Tulikuwa na mazungumzo ya andiko la Biblia mezani kila asubuhi. Huo ulikuwa wakati wenye furaha sana kwetu sote. Tena, nilipoamka kila asubuhi na kutambua nilikokuwa na sababu ya kuwa huko, nilimshukuru sana Yehova kimoyo-moyo.

Hatimaye Judith aliolewa akarudi States, ambako aliendelea katika huduma ya wakati wote. Baada ya miaka mitatu ya utumishi wa painia wa pekee, Philip alipeleka ombi akakubaliwa kwa utumishi wa Betheli katika Brooklyn, New York. Mwishowe, Leslie pia alirudi United States. Waliondoka wakiwa na hisia zilizochanganyika, na mara nyingi wametuambia kwamba kuwapeleka Peru kulikuwa jambo bora zaidi tulilopata kuwafanyia.

Uchumi wa Peru ulipozidi kuwa mbaya, tulitambua kwamba sisi pia tungalipaswa kuondoka. Tuliporudi Wichita katika 1978, tulipata kikundi cha Mashahidi wenye kusema Kihispania. Walituomba tubaki ili tuwasaidie, tukakubali kwa furaha. Kundi lilifanyizwa, na upesi tukalipenda kama yale tuliyokuwa tumetumikia nyuma.

Ekwedori Inaita

Ujapokuwa ugonjwa wa ghafula ulioniacha nikiwa nimepooza kwa sehemu, nilitamani sana kwamba Lucille na mimi tungeweza kutumikia tena katika nchi nyingine. Katika 1984 mwangalizi asafiriye alituambia juu ya ukuzi katika Ekwedori na uhitaji wa huko wa wazee Wakristo. Nilieleza kwamba ningeweza kufanya kidogo katika huduma ya shambani kwa sababu ya kulemaa kwangu, lakini alinihakikishia kwamba hata mzee mwenye miaka 65 aliyepooza kwa sehemu angeweza kusaidia.

Baada ya yeye kuondoka hatukuweza kulala usingizi usiku kucha, tukiongea juu ya uwezekano wa kwenda Ekwedori. Lucille alikuwa na tamaa iyo hiyo ichomayo ya kwenda niliyokuwa nayo. Kwa hiyo tulitangaza juu ya biashara yetu ndogo ya kudhibiti visumbuaji na tukaiuza katika majuma mawili. Tuliuza nyumba yetu katika siku kumi tu. Hivyo, katika miaka yetu ya umri mkubwa zaidi, tulirudi tena kwenye shangwe yetu kubwa zaidi, ile ya utumishi wa mishonari ugenini.

Tulikaa katika Kuito, na utumishi wa shambani ulikuwa wenye kufurahisha, kila siku ikileta ono au tukio jipya lenye kusisimua. Lakini, katika 1987 nilichunguzwa na kupatikana kuwa na kansa ya utumbompana; nilihitaji upasuaji wa mara hiyo. Tulirudi Wichita kwa ajili ya upasuaji huo, uliofanikiwa. Tulikuwa tumerudi Kuito kwa miaka miwili tu wakati kansa ilipopatikana tena, na tukahitaji kurudi United States kabisa. Tulikaa katika Karolina Kaskazini, tunakoishi kwa sasa.

Maisha ya Kutajirisha, Yenye Kuthawabisha

Wakati ujao wangu wa kimwili hauna uhakika. Nililazimika kupata kolostomi (mpasuo tumboni wa kutolea kinyesi) katika 1989. Hata hivyo, ningali naweza kutumikia nikiwa mzee na kuongoza mafunzo ya Biblia pamoja na wale wanaokuja nyumbani kwangu. Muda wote wa miaka iliyopita, tumesaidia mamia kihalisi kwa kupanda, kutia maji, au kumea mbegu ya kweli. Hiyo ni shangwe ambayo haififii kamwe, haidhuru ni mara ngapi inaporudiwa.

Kwa kuongezea, nimekuwa na shangwe kubwa ya kuona watoto wangu wote wakimtumikia Yehova. Pegi ameandamana kwa miaka 30 na mume wake, Paul Moske, katika kazi ya kusafiri katika United States. Philip na mke wake, Elizabeth, pamoja na Judith, wanaendelea katika utumishi wa pekee wa wakati wote katika Betheli ya Brooklyn, New York. Hank na Leslie na wenzi wao ni Mashahidi wenye bidii, na ndugu na dada zangu wanne pamoja na familia zao kutia na watu wa ukoo zaidi ya 80, wote wanamtumikia Yehova. Na Lucille amekuwa mke Mkristo mwenye mfano mzuri kwa miaka yetu ya ndoa karibu 50. Katika miaka ya karibuni amefanya kazi nyingi zisizopendeza bila kulalamika katika kunisaidia kutunza mwili wangu wenye kudhoofika.

Kwa kweli, maisha yangu yamekuwa yenye shangwe. Yamekuwa yenye furaha zaidi ya vile maneno yawezavyo kusimulia. Kumtumikia Yehova ni shangwe kubwa sana hivi kwamba ni tamaa yangu ya kuhisiwa moyoni kumwabudu milele kwenye dunia hii. Sikuzote mimi hukumbuka Zaburi 59:16, inayosema: “Nitaziimba nguvu zako asubuhi, nitaziimba fadhili zako kwa furaha. Kwa kuwa ndiwe uliyekuwa ngome yangu, na makimbilio siku ya shida yangu.”

[Picha katika ukurasa wa 23]

George Brumley pamoja na maliki Mwethiopia Haile Selassie

[Picha katika ukurasa wa 25]

George Brumley na mke wake, Lucille

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki