Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 8/1 kur. 21-25
  • Kukaza Macho na Moyo Kwenye Tuzo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kukaza Macho na Moyo Kwenye Tuzo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Huduma ya Wakati Wote
  • Kwenda Kwenye Mgawo Wetu
  • Migawo Mipya
  • Kurudi Marekani
  • Kwenda Shule ya Gileadi Tena
  • Twapewa Mgawo Kwenda Argentina
  • Kurudi Marekani Tena
  • Kutafuta Ufalme Kwanza Huridhisha na Huleta Furaha Maishani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Kuufuatia Mradi Uliowekwa Tangu Umri wa Miaka Sita
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Nimeazimia Kuendelea Kumtumikia Muumba Wangu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Tulipewa Mradi Maishani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 8/1 kur. 21-25

Kukaza Macho na Moyo Kwenye Tuzo

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA EDITH MICHAEL

Katika miaka ya mapema ya 1930, tulikuwa tukiishi karibu na St. Louis, Missouri, Marekani, wakati mmoja wa Mashahidi wa Yehova alipotembelea. Ndipo tu kamba ya nguo ikakatika, ikiangusha matopeni nguo nyeupe zenye kutakata za mama. Yeye alikubali vitabu vilivyotolewa, ili huyo mwanamke aondoke tu, kisha akaviweka juu ya rafu, akivisahau.

HIYO ilikuwa miaka ya mshuko wa kiuchumi, na baba aliachishwa kazi. Siku moja aliuliza ikiwa kulikuwa na chochote cha kusoma nyumbani. Mama akamwambia juu ya vile vitabu. Alianza kuvisoma, na punde si punde akasema kwa mshangao hivi: “Mama, hii ndiyo kweli!”

“Ah, ni dini inayotaka fedha tu sawa na zile nyinginezo zote,” mama akajibu. Hata hivyo, baba alimsihi sana mama aketi na kuyasoma maandiko pamoja naye. Mama alipofanya hivyo, yeye akasadikishwa pia. Baadaye wakaanza kuwatafuta Mashahidi wakagundua kwamba walikutana katika jumba lililokodishwa, karibu na katikati ya St. Louis, jumba lililotumiwa pia kwa ajili ya dansi na matukio mengine.

Baba na mama walienda nami—nilikuwa na miaka ipatayo mitatu—tukalipata jumba hilo, lakini dansi ilikuwa ikiendelea. Baba alipata kujua wakati mikutano inapofanywa, nasi tukarudi baadaye. Tulianza pia kuhudhuria funzo la Biblia la kila juma karibu na mahali tulipoishi. Lilifanywa nyumbani mwa yule mwanamke aliyekuwa ametutembelea kwa mara ya kwanza. “Mbona hamji na wana wenu pia?” yeye akauliza. Mama aliona aibu kusema kwamba hawakuwa na viatu. Alipoeleza hivyo hatimaye, viatu viliandaliwa, na ndugu zangu wakaanza kuhudhuria mikutano pamoja nasi.

Mama alipewa eneo la kuhubiri karibu na nyumbani kwetu, naye akaanza huduma ya nyumba hadi nyumba. Nilienda pamoja naye, nikijificha nyuma yake. Kabla ya yeye kujifunza kuendesha gari, tulikuwa tukitembea zaidi ya kilometa moja ili kupata basi lililotupeleka mikutanoni katika St. Louis. Hata kulipokuwa na barafu na theluji, hatukukosa mikutano kamwe.

Katika 1934, mama na baba walibatizwa. Nilitaka kubatizwa pia, nami nikaendelea kusisitiza mpaka mama akamwomba Shahidi mwenye umri mkubwa zaidi aongee nami juu ya jambo hilo. Yeye aliniuliza maswali mengi kwa njia ambayo ningeweza kuelewa. Kisha akawaambia wazazi wangu kwamba sipaswi kuzuiwa nisibatizwe; huenda kukadhuru ukuzi wangu wa kiroho. Kwa hiyo nilibatizwa kiangazi kilichofuata, nilipokuwa ningali na umri wa miaka sita.

Nilipenda kile kijitabu Home and Happiness, nilichokuwa nacho nyakati zote, hata nikikiweka chini ya mto wangu nilipokuwa nikilala. Nilimwomba mama anisomee kitabu hicho mara kwa mara, mpaka nilipokijua kwa moyo. Jalada lacho lilikuwa na picha ya msichana mdogo akiwa katika Paradiso pamoja na simba. Nilisema kwamba nilikuwa huyo msichana mdogo. Picha hiyo imenisaidia kukaza macho yangu kwenye tuzo la uhai katika ulimwengu mpya wa Mungu.

Nilikuwa mwenye haya sana, lakini ingawa huenda nikawa ninatetemeka, sikuzote nilijibu maswali kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi la kutaniko.

Kwa kusikitisha, baba alihofu kwamba angeipoteza kazi yake, kwa hiyo aliacha kushirikiana na Mashahidi. Ndugu zangu pia waliacha.

Huduma ya Wakati Wote

Mama aliwaruhusu mapainia fulani, au wahudumu wa wakati wote, waegeshe gari lao liburutalo nyumba, katika uwanja wetu wa nyuma, na baada ya shule nilijiunga nao katika huduma. Upesi nikataka kupainia, lakini baba alipinga hilo, akiamini kwamba nilipaswa kupata elimu zaidi ya kimwili. Hatimaye mama akamsadikisha baba aniruhusu kupainia. Kwa hiyo katika Juni 1943, nilipokuwa na miaka 14, nilianza huduma ya wakati wote. Ili kuchangia gharama za nyumbani, nilifanya kazi ya kimwili isiyo ya wakati wote, na nyakati nyingine nilifanya kazi ya wakati wote. Hata hivyo nilifikia mradi wangu wa kila mwezi wa saa 150 katika kazi ya kuhubiri.

Baada ya muda fulani nilipata mshiriki wa kupainia naye, Dorothy Craden, aliyekuwa ameanza kupainia Januari 1943, alipokuwa na miaka 17. Alikuwa amekuwa Mkatoliki mchaji, lakini akabatizwa baada ya kujifunza Biblia kwa miezi sita. Kwa miaka mingi alikuwa chanzo cha kitia-moyo na nguvu kwangu, nami nikawa hivyo kwake. Tukawa wenye ukaribu zaidi kuliko dada wa kimwili.

Kuanzia 1945, tulipainia pamoja katika miji midogo katika Missouri ambako hakukuwa na makutaniko. Katika Bowling Green tulinadhifisha jumba fulani la kukutania; mama alikuja akatusaidia. Kisha tukatembelea nyumba zote mjini kila juma na kuwaalika watu kwenye hotuba ya watu wote ambayo tulikuwa tumepangia ndugu kutoka St. Louis waje kutoa. Tulikuwa na hudhurio la kila juma la watu kati ya 40 na 50. Baadaye tukafanya vivyo hivyo katika Louisiana, tulikokodi hekalu la dini ya Freemason. Ili kulipia gharama ya kukodi hayo majumba, tuliweka masanduku ya mchango, na kila juma gharama zote zililipwa.

Halafu tukaenda Mexico, Missouri, tulikokodi jengo lenye duka. Tulilitengeneza ili litumiwe na kutaniko dogo huko. Hilo jengo lilikuwa na vyumba vyenye kupakana nalo tulimoishi. Tulisaidia pia kupangia hotuba za watu wote katika Mexico. Kisha tukaenda jiji kuu la jimbo, Jefferson City, ambako kila asubuhi ya siku za juma, tuliwasiliana na maofisa wa umma ofisini mwao. Tuliishi katika chumba kimoja juu ya Jumba la Ufalme pamoja na Stella Willie, aliyekuwa kama mama kwetu.

Kutoka huko sisi watatu tukaenda miji ya Festus na Crystal City, iliyokuwa karibu-karibu. Tuliishi katika nyumba ya kuku iliyokuwa imegeuzwa kuwa makao, nyuma ya nyumba ya familia yenye kupendezwa. Kwa kuwa hakukuwa na wanaume waliobatizwa, tuliongoza mikutano yote. Kazi yetu isiyo ya wakati wote ilikuwa kuuza virembeshi. Hatukuwa na vitu vingi vya kimwili. Kwa kweli, hatukuwa na fedha za kutosha za kutengenezea viatu vyetu vyenye mashimo, kwa hiyo kila asubuhi tulitia karatasi ngumu mpya ndani yavyo, na usiku kila mmoja wetu alifua nguo yake pekee.

Mapema katika 1948, nilipokuwa na umri wa miaka 19, Dorothy nami tulipokea mialiko ya kwenda kwenye darasa la 12 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower kwa wamishonari. Baada ya mtaala huo wa miezi mitano, wale wanafunzi mia moja walihitimu katika Februari 6, 1949. Huo ulikuwa wakati wenye furaha sana. Wazazi wangu walikuwa wamehamia California, na mama akaja mwendo huo wote kutoka huko ili awepo.

Kwenda Kwenye Mgawo Wetu

Wahitimu 28 walipewa mgawo kwenda Italia—sita, kutia ndani Dorothy na mimi, tulienda jiji la Milan. Machi 4, 1949, tuliondoka New York katika meli ya Kiitalia Vulcania. Safari ilichukua muda wa siku 11, na bahari iliyochafuka ilifanya wengi wetu tupatwe na ugonjwa wa bahari. Ndugu Benanti alikuja kwenye bandari ya Genoa ili kutulaki na kutupeleka Milan kwa gari-moshi.

Tulipowasili kwenye makao ya mishonari katika Milan, tulipata maua ambayo msichana mchanga Mwitalia alikuwa ameweka katika chumba cha kila mmoja wetu. Miaka kadhaa baadaye, msichana huyo, Maria Merafina, alienda Gileadi, akarudi Italia, na yeye nami tukatumikia pamoja katika makao ya mishonari!

Ile asubuhi baada ya sisi kuwasili Milan, tuliangalia nje kupitia dirisha la bafu. Barabarani nyuma ya nyumba yetu kulikuwa na jengo kubwa lililokuwa limetupiwa bomu. Ndege fulani ya Marekani ya kuangushia mabomu ilikuwa imeangusha bomu kwa aksidenti iliyoua familia zote 80 zilizokuwa zikiishi humo. Wakati mwingine, mabomu yaliyolengwa kwenye kiwanda fulani yalikosa shabaha yakaangukia shule na kuua watoto 500. Kwa hiyo watu hawakuwapenda Wamarekani.

Watu walikuwa wamechoka na vita. Wengi walisema kwamba ikiwa vita nyingine ingeanza, wao wasingeenda mahali pa kujikinga na mabomu bali wangebaki nyumbani na kufungua gesi na kufa humo. Tuliwahakikishia kwamba hatukuwa huko ili kuwakilisha Marekani wala serikali nyingine yoyote yenye kufanyizwa na wanadamu, bali tulikuwa huko ili kuwakilisha Ufalme wa Mungu, ambao utakomesha vita vyote na kule kuteseka kunakoletwa navyo.

Katika lile jiji kubwa la Milan, lile kutaniko pekee la watu wapatao 20 lilikutana katika makao ya mishonari. Maeneo ya kuhubiri hayakuwa yamefanyizwa bado, kwa hiyo tulianza kutoa ushahidi katika jengo kubwa lenye makao kadhaa. Kwenye mlango wa kwanza, tulikutana na Bw. Giandinotti, aliyetaka mkewe aache kanisa, kwa hiyo alikubali kimojapo vichapo vyetu. Bi. Giandinotti alikuwa mwanamke mwenye moyo mweupe, aliyekuwa na maswali mengi. “Nitafurahi mjuapo Kiitalia,” yeye akasema, “ili mweze kunifundisha Biblia.”

Dari katika nyumba yao zilikuwa juu na taa haikutoa mwangaza mwingi, kwa hiyo usiku alikuwa akiweka kiti chake juu ya meza awe karibu zaidi na taa ili kusoma Biblia. “Nikijifunza Biblia pamoja nanyi,” yeye akauliza, “je, ningali naweza kwenda kanisani?” Tulimwambia kwamba huo ulikuwa uamuzi wake. Alienda kanisani kila Jumapili asubuhi, na kuja kwenye mikutano yetu alasiri. Kisha siku moja akasema, “Siendi kanisani tena.”

“Kwa nini?” tukauliza.

“Kwa sababu wao hawafundishi Biblia, nami nimeipata kweli kwa kujifunza Biblia pamoja nanyi.” Alibatizwa, akajifunza na wanawake wengi walioenda kanisani kila siku. Baadaye alituambia kwamba ikiwa tungalimwambia asiende kanisani, yeye angaliacha kujifunza na labda asingalijifunza kweli kamwe.

Migawo Mipya

Hatimaye Dorothy na mimi, pamoja na wamishonari wengine wanne, tulipewa mgawo wa kwenda jiji la Italia la Trieste, lililokuwa likikaliwa na vikosi vya Waingereza na Wamarekani. Kulikuwa na Mashahidi wapatao kumi tu, lakini idadi hiyo iliongezeka. Tulihubiri katika Trieste kwa miaka mitatu, na tulipoondoka, kulikuwa na watangazaji 40 wa Ufalme, 10 kati yao wakiwa mapainia.

Mgawo wetu uliofuata ulikuwa jiji la Verona, ambako hakukuwa na kutaniko. Lakini kanisa lilipowasonga wenye mamlaka za kilimwengu, tulilazimika kuondoka. Dorothy na mimi tulipewa mgawo wa kwenda Roma. Tukiwa huko tulikodi chumba chenye fanicha, na tulihubiri eneo lililokuwa karibu na Vatikani. Tulipokuwa huko ndipo Dorothy alipoenda Lebanoni ili kuolewa na John Chimiklis. Tulikuwa tumekuwa pamoja karibu miaka 12, nami nilimkosa kwelikweli.

Katika 1955 makao mapya ya mishonari yalifunguliwa katika sehemu nyingine ya Roma kwenye barabara iitwayo New Appian Way. Mmoja wa wale watu wanne katika makao hayo alikuwa Maria Merafina, yule msichana aliyekuwa ameweka maua katika vyumba vyetu ule usiku tulipowasili Milan. Kutaniko jipya lilifanyizwa katika eneo hili la jiji. Baada ya mkusanyiko wa kimataifa katika Roma kiangazi hicho, nilipendelewa kuhudhuria mkusanyiko katika Nuremberg, Ujerumani. Ilisisimua kama nini kukutana na wale waliokuwa wamevumilia minyanyaso mingi sana chini ya utawala wa Hitler!

Kurudi Marekani

Katika 1956, kwa sababu ya matatizo ya afya, nilirudi Marekani kwa likizo la ugonjwa. Lakini sikuacha kamwe kukaza macho yangu kwenye tuzo ya kumtumikia Yehova sasa na milele katika ulimwengu wake mpya. Nilipanga kurudi Italia. Hata hivyo, nilikutana na Orville Michael, aliyetumikia kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York. Tulioana baada ya ule mkusanyiko wa kimataifa wa 1958 katika New York City.

Muda mfupi baadaye tulihamia Front Royal, Virginia, tulikofurahia kutumikia pamoja na kutaniko dogo. Tuliishi katika nyumba ndogo nyuma ya Jumba la Ufalme. Hatimaye, katika Machi 1960 ikawa lazima turudi Brooklyn kutafuta kazi ya kimwili ili kulipia gharama zetu. Usiku tulifanya kazi ya kusafisha benki tofautitofauti ili tuweze kuendelea kuwa katika utumishi wa wakati wote.

Tulipokuwa Brooklyn, baba yangu akafa, na mama ya mume wangu akapatwa na mshutuko mdogo wa akili. Kwa hiyo tukaamua kuhamia Oregon ili kuwa karibu na mama zetu. Sote wawili tulipata kazi za kimwili zisizo za wakati wote, tukaendelea na huduma ya upainia tukiwa huko. Katika vuli ya 1964, sisi na mama zetu tulisafiri kwa gari ng’ambo ya Marekani ili kuhudhuria mkutano wa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society katika Pittsburgh, Pennsylvania.

Wakati wa ziara yetu huko Rhode Island, tulitiwa moyo na mwangalizi wa mzunguko, Arlen Meier, na mke wake tuhamie jiji kuu la jimbo, Providence, ambako uhitaji wa watangazaji wa Ufalme ulikuwa mkubwa zaidi. Mama zetu walituhimiza tukubali mgawo huo mpya, kwa hiyo tuliporudi Oregon, tuliuza vingi vya vitu vyetu vya nyumbani, tukahama.

Kwenda Shule ya Gileadi Tena

Katika kiangazi cha 1965, tulihudhuria mkusanyiko katika Yankee Stadium. Tukiwa huko tulijaza ombi la Shule ya Gileadi tukiwa mume na mke. Yapata mwezi mmoja baadaye, tulishangaa kupokea fomu za maombi za shule hiyo, zilizopasa kurudishwa katika siku 30. Nilikuwa na wasiwasi kwenda nchi ya mbali kwa kuwa mama hakuwa na afya nzuri. Lakini alinitia moyo hivi: “Zijazeni fomu hizo za maombi. Wajua sikuzote wapaswa kukubali pendeleo lolote la utumishi ambalo Yehova hutoa!”

Hilo liliamua mambo. Tulizijaza fomu hizo za maombi, tukazituma. Ulikuwa mshangao ulioje kupokea mialiko ya kwenda kwenye darasa la 42, lililoanza Aprili 25, 1966! Wakati huo Shule ya Gileadi ilikuwa Brooklyn, New York. Muda usiozidi miezi mitano baadaye, sisi 106 tulihitimu katika Septemba 11, 1966.

Twapewa Mgawo Kwenda Argentina

Siku mbili baada ya kuhitimu, tulikuwa njiani kwenda Argentina katika ndege ya Peruvian Airlines. Tulipowasili Buenos Aires, mwangalizi wa tawi, Charles Eisenhower, alitulaki kwenye uwanja wa ndege. Alitusaidia kupitia idara ya forodha kisha akatupeleka kwenye tawi. Tulikuwa na siku moja ya kuifungua mizigo yetu na kustarehe; kisha masomo yetu ya Kihispania yakaanza. Tulijifunza Kihispania muda wa saa 11 kwa siku katika mwezi wa kwanza. Katika mwezi wa pili, tulijifunza hiyo lugha kwa muda wa saa nne kwa siku na tukaanza kushiriki katika huduma ya shambani.

Tulikuwa Buenos Aires kwa miezi mitano kisha tukapewa mgawo kwenda Rosario, lililo jiji kubwa kuelekea kaskazini, mwendo wa muda wa saa nne kwa gari-moshi. Baada ya kutumikia huko kwa miezi 15, tulitumwa kuelekea kaskazini zaidi kwenda Santiago del Estero, jiji lililomo katika mkoa wa jangwa lenye joto. Tulipokuwa huko, katika Januari 1973, mama yangu akafa. Sikuwa nimemwona kwa miaka minne. Jambo lililosaidia kunitegemeza katika huzuni yangu lilikuwa lile tumaini hakika la ufufuo pamoja na kujua kwamba nilikuwa nikitumikia mahali ambapo mama alitaka nitumikie.—Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15.

Watu katika Santiago del Estero walikuwa wenye urafiki, na ilikuwa rahisi kuanzisha mafunzo ya Biblia. Tulipowasili katika 1968, kulikuwa na watu wapatao 20 au 30 waliohudhuria mikutano, lakini miaka minane baadaye kulikuwa na watu zaidi ya mia moja katika kutaniko letu. Kwa kuongezea, kulikuwa na makutaniko mapya mawili yenye watangazaji kati ya 25 na 50 katika miji ya karibu.

Kurudi Marekani Tena

Kwa sababu ya matatizo ya afya, katika 1976 tulipewa mgawo wa kurudi Marekani tukiwa mapainia wa pekee—katika Fayetteville, North Carolina. Huko kulikuwa na watu wengi wenye kusema Kihispania waliotoka Amerika ya Kati na ya Kusini, Jamhuri ya Dominika, Puerto Riko, na hata Hispania. Tulikuwa na mafunzo mengi ya Biblia, na hatimaye kutaniko la Kihispania likaanzishwa. Tulikuwa katika mgawo huo kwa miaka ipatayo minane.

Hata hivyo, tulihitaji kuwa karibu zaidi na mama-mkwe wangu, aliyekuwa mzee-mzee na asiyejiweza. Yeye aliishi Portland, Oregon, kwa hiyo tulipokea mgawo mpya wa kwenda kwenye kutaniko la Kihispania katika Vancouver, Washington, ambako si mbali na Portland. Kutaniko lilikuwa dogo tulipowasili katika Desemba 1983, lakini tunaona wapya wengi.

Katika Juni 1996, nilikamilisha miaka 53 ya utumishi wa wakati wote, na mume wangu alikamilisha miaka 55 katika Januari 1, 1996. Katika miaka hii mingi, nimekuwa na pendeleo la kusaidia mamia ya watu yapate ujuzi wa kweli ya Neno la Mungu na kuweka wakfu maisha zao kwa Yehova. Wengi kati yao sasa hutumikia wakiwa wazee na wahudumu wa wakati wote.

Nyakati nyingine mimi huulizwa ikiwa ninakosa jambo lolote kwa sababu ya kutokuwa na watoto. Jambo la hakika ni kwamba, Yehova amenibariki kwa kunipa watoto na wajukuu wengi wa kiroho. Ndiyo, maisha yangu yamekuwa yenye maana na ya kuthawabisha katika utumishi wa Yehova. Naweza kujilinganisha na binti Yeftha, aliyetumia maisha yake katika utumishi wa hekalu naye hakupata watoto kamwe kwa sababu ya pendeleo lake kubwa la utumishi.—Waamuzi 11:38-40.

Ningali nakumbuka nikijiweka wakfu kwa Yehova nilipokuwa msichana mdogo tu. Ile picha ya Paradiso ingali dhahiri akilini mwangu sasa kama ilivyokuwa wakati huo. Macho yangu na moyo wangu ungali umekazwa juu ya tuzo la uhai wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu. Ndiyo, tamaa yangu ni kumtumikia Yehova, si kwa miaka ipatayo 50 tu, bali milele—chini ya utawala wa Ufalme wake.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Dorothy Craden, mikono yake ikiwa kwenye mabega yangu, na mapainia wenzetu katika 1943

[Picha katika ukurasa wa 23]

Katika Roma, Italia, pamoja na wamishonari wenzangu katika 1953

[Picha katika ukurasa wa 25]

Pamoja na mume wangu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki