Shule ya Gileadi—Ina Umri wa Miaka 50 na Yaendelea Kufanikiwa
“PANA mahali pengi ambapo ushahidi kuhusu Ufalme haujatolewa kwa kadiri kubwa,” ndivyo alivyosema N. H. Knorr kwa darasa la kwanza la Gileadi katika Februari 1, 1943, siku ambayo shule hiyo ilifunguliwa. Aliongeza hivi: “Lazima iwe kuna mamia na maelfu ya watu ambao wangeweza kufikiwa kama kungekuwa wafanyakazi zaidi shambani. Kwa neema ya Bwana, watakuwako wengi zaidi.”
Na wamekuwako wafanyakazi wengi zaidi—mamilioni zaidi! Idadi ya wahubiri wa Ufalme imeongezeka kutoka 129,070 katika mabara 54 katika 1943 hadi 4,472,787 katika mabara 229 katika 1992! Shule ya Gileadi imechangia sana ushahidi ambao umetokeza ongezeko hilo. Baada ya miaka 50 inaendelea kutimiza fungu muhimu katika kuwazoeza wafanyakazi wamishonari kutumikia kokote wanakohitajiwa katika shamba la ulimwengu.
Katika Machi 7, 1993, kulikuwa wageni walioalikwa pamoja na washiriki wa familia ya Betheli ya U.S. 4,798 waliokusanyika kwenye Jumba la Kusanyiko la Jersey City, katika New Jersey, kwa ajili ya uhitimu wa darasa la 94. Pindi hiyo ya pekee kwelikweli iliandaa pia fursa ya kukumbuka ile miaka 50 ya Shule ya Gileadi. Je! ungependa kujua kidogo juu ya programu hiyo?
Baada ya wimbo wa kufungua, George D. Gangas wa Baraza Linaloongoza alitoa sala yenye bidii. Kisha, baada ya maelezo ya utangulizi ya mwenyekiti, Carey W. Barber, wahitimu—na wote waliohudhuria—walisikiliza kwa uangalifu mfululizo wa hotuba fupi.
Robert W. Wallen alitoa hotuba ya kwanza, juu ya kichwa “Wewe Huko Peke Yako Kamwe.” Kwa sauti changamfu, alisema hivi: ‘Katika siku za usoni, pindi zitatokea maishani mwako ambapo utahisi upweke sana, ukiwa mbali sana na familia na rafiki.’ Basi, inaweza kusemwaje kwamba, “Wewe huko peke yako kamwe?” Alieleza hivi: ‘Kwa sababu nyinyi nyote mna uwezo wa kuwasiliana na Yehova Mungu mara hiyo.’ Aliwahimiza wahitimu wathamini sana lile pendeleo la sala na walitumie kila siku. Kisha, kama vile Yesu, wataweza kusema, “Mimi si peke yangu.” (Yohana 16:32) Maneno hayo yalikuwa yenye kitia-moyo kama nini kwa wahitimu!
Akikuza kile kichwa “Shika Sana Tumaini Lako” (kilichotegemea andiko la siku, Machi 7), Lyman A. Swingle wa Baraza Linaloongoza alisema baada ya hapo juu ya uhitaji wa kuwa na sifa mbili—uvumilivu na tumaini. ‘Shutumu, uadui, chuki, kufungwa gerezani, hata kifo, ni sababu kwa nini uvumilivu unahitajiwa kwa upande wa Wakristo,’ akasema. ‘Nguvu zipitazo zile za kawaida ambazo Mashahidi wa Yehova wanaweza kutwaa katika nyakati za uhitaji hazina mwisho. Bila shaka hilo latumainisha, hasa kwa nyinyi wahitimu.’ Namna gani tumaini? ‘Tumaini ni la lazima,’ akaeleza. ‘Kama vile chapeo hulinda kichwa cha mwenye kuivaa, ndivyo tumaini la wokovu linavyolinda na kuhami nguvu za akili za Mkristo, likimwezesha adumishe uaminifu-maadili.’—1 Wathesalonike 5:8.
Msemaji aliyefuata, Ralph E. Walls, alichagua kichwa chenye kusisimua, “Tunaweza Kuponyokaje Hadi Kwenye Usalama wa ‘Panapo Nafasi’?” Mahali hapo “panapo nafasi” ni wapi? (Zaburi 18:19) “Hali ya kukombolewa inayoleta amani ya akili na usalama wa moyo,” msemaji akaeleza. Tunahitaji kukombolewa kutoka katika nini? ‘Kutoka katika wewe mwenyewe—kasoro zako mwenyewe.’ Aliongeza hivi: ‘Tunahitaji pia kukombolewa, kutoka katika hali za nje zinazochochewa na Shetani.’ (Zaburi 118:5) Tunaweza kuponyokaje hadi kwenye usalama wa panapo nafasi? ‘Kwa kujitahidi kupata amri za Yehova katika yote tunayofanya na kwa kumsihi Yehova kwa imani kwa ajili ya mahangaiko yetu yote.’
“Ni Nini Kilichoko Mbele?” ndicho kilichokuwa kichwa kilichochaguliwa na Don A. Adams. Na ni nini kwa kweli kilichokuwa mbele kwa ajili ya wamishonari hao wapya? Kipindi cha marekebisho, akaeleza. “Pia kuna baraka nyingi mbele yako.” Kikiwa kielelezo, aliwaambia juu ya wamishonari wawili ambao baada ya kuzoea mgawo wao waliandika hivi: “Fikiria ile siku bora zaidi ambayo umepata kuwa nayo katika utumishi, na ndivyo ilivyo kila siku. Tunahitaji fasihi zaidi sikuzote, na watu hutuomba mafunzo daima.” Msemaji alielekeza maelezo mengine kwa familia na marafiki wa wahitimu: ‘Hakuna uhitaji wa kuwahangaikia wahitimu hawa. Mwaweza kuwasaidia kwa kuwaandikia maneno yenye kitia-moyo.’—Mithali 25:25.
Wafunzi wa shule walitoa hotuba zilizofuata. Jack D. Redford alichagua kichwa “Usitumaini Chochote Kutoka kwa Yeyote.” Ugumu mmoja ambao wahitimu watakabili ni kupatana na watu, akaeleza. Ni nini kiwezacho kusaidia? “Puuza kasoro zao. Usitazamie mengi mno kutoka kwa watu wengine. Usitazamie sikuzote kupata kiasi kamili cha kile unachoona kuwa ni haki yako. Kumbuka kwamba watu wengine si wakamilifu, na fadhili hiyo itakuwezesha upatane nao. Uwezo wako wa kupatana na watu wengine utaonyesha kadiri ya ukomavu wako.” (Mithali 17:9) Kwa hakika, kutumia shauri hilo lenye hekima kutawasaidia wahitimu kufanya marekebisho yenye mafanikio ya kuwa wamishonari katika bara la kigeni!
“Tuna hazina hii katika vyombo vya udongo,” lasema 2 Wakorintho 4:7. Ulysses V. Glass, msajili wa Shule ya Gileadi, alieleza juu ya andiko hilo alipokuwa akikuza kile kichwa “Watumaini Ndugu Zako Waaminifu, Waliojaribiwa.” “Vyombo vya udongo” ni nini? “Ni lazima iwe vinarejezea sisi tukiwa wanadamu wasio wakamilifu,” akasema. “Hazina” ni nini? “Ni huduma yetu ya Kikristo,” yeye akaeleza. (2 Wakorintho 4:1) Tunapaswa kufanya nini na hazina hiyo? “Hazina ambayo Yehova ametukabidhi haipaswi kufichwa mahali fulani. Kwa hiyo, nyinyi wapendwa mtakaokuwa wamishonari, gawanyeni hazina hiyo kokote mwendako, na kufundisha wengine wengi jinsi ya kuigawanya.”
Ulikuwa wakati wa kukumbuka ya zamani kwa furaha wakati Albert D. Schroeder alipoanza kusema, kwani alikuwa ndiye msajili wa Shule ya Gileadi ilipoanza. “Nusu Karne ya Mazoezi ya Kitheokrasi” ndicho kilichokuwa kichwa chake. “Yehova ajua namna ya kutoa mazoezi yenye matokeo, na ndivyo ambavyo amefanya,” akasema. Namna gani? Ndugu Schroeder alirejezea yale mazoezi yaliyopokewa kupitia shule mbili zilizoanzishwa miaka 50 iliyopita—Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Shule ya Gileadi. Alionyesha kwamba New World Translation kimekuwa chombo chenye thamani katika kuandaa ujuzi sahihi. Aliwahakikishia wahitimu hivi: “Mwaweza kwenda kwenye migawo yenu ya kigeni mikiwa na uhakika kabisa kwamba Sosaiti itawapa ugavi wa kutosha wa ujuzi sahihi wa makusudi ya Yehova.”
Milton G. Henschel, msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, alisema juu ya kichwa “Zaidi ya Kuwa Washindi.” Ndugu Henschel alitwaa kichwa chake kutoka katika andiko-mwaka la 1943: “Zaidi ya kuwa washindi kupitia yeye aliyetupenda.” (Warumi 8:37, King James Version) Hilo lilikuwa andiko-mwaka lililofaa, akaeleza, kwa sababu katikati ya Vita ya Ulimwengu 2, ndugu zetu katika nchi nyingi walikuwa wakipatwa na mnyanyaso mwingi. Ndugu Henschel alisoma sehemu-sehemu kutoka katika toleo la Mnara wa Mlinzi lililozungumzia andiko-mwaka hilo na kisha akaeleza hivi: “Makala hii ya Mnara wa Mlinzi [Januari 15, 1943, Kiingereza] ilisomwa katika mwezi wa Februari na darasa la kwanza la Gileadi, na iliwatayarisha kwa ajili ya yale yaliyokuwa mbele.” Wengi wa wahitimu wa ile miaka 50 ambayo imepita tayari wamejithibitisha kuwa washindi, akaeleza. Namna gani darasa la 94? “Kaeni karibu na Yehova, kaeni karibu na upendo wake, kisha ushindi wenu utahakikishwa.”
Baada ya hotuba za asubuhi, mwenyekiti alishiriki salamu fulani zilizopokewa kutoka mabara mbalimbali. Halafu wakati ukafika uliokuwa ukitazamiwa sana na wale wenzi wa ndoa 24—ugawanyaji wa diploma. Kwani, wanafunzi wa Gileadi walikuwa sasa wahitumu wa Gileadi kirasmi! Walikuwa wametoka nchi 5, lakini migawo yao ilikuwa ikiwapeleka hadi mabara 17, kutia ndani Hong Kong, Taiwan, Msumbiji, na sehemu za Ulaya Mashariki.
Baada ya pumziko, programu ya alasiri ilianza kwa Funzo la Mnara wa Mlinzi lililofupishwa, lililoongozwa na Robert L. Butler. Kisha wahitimu wakaigiza baadhi ya maono yenye kutokeza waliyokuwa wamefurahia walipokuwa wakitoa ushahidi karibu na Wallkill, New York. Programu hiyo ilionyesha mojawapo mambo ambayo bila shaka yaliwaleta Gileadi—upendo wao wenye kina kirefu kwa ajili ya huduma ya shambani.
Baada ya programu ya wanafunzi, wasikilizaji wengi walijiuliza kama programu ingeonyesha jambo la pekee ili kuadhimisha miaka 50 ya Shule ya Gileadi. Hawakukatishwa tamaa!—Ona sanduku linaloandamana, “Kupitia Miaka 50 ya Shule ya Gileadi.”
Miaka 50 iliyopita, Ndugu Knorr alionyesha kwamba yeye alikuwa mtu mwenye imani na mwono-mbele. Usadikisho wake kwamba Shule ya Gileadi ingefanikiwa ulionyeshwa katika hotuba yake ya kufungua kwa darasa la kwanza, aliposema hivi: “Tunaamini kwamba, kulingana na jina layo, ‘rundo la ushahidi’ litatoka hapa na kwenda hadi sehemu zote za ulimwengu na kwamba ushahidi huo utasimama kama nguzo isiyoweza kuharibiwa kamwe kwa utukufu wa Mungu. Nyinyi mkiwa wahudumu waliotawazwa rasmi mtamtumainia kikamili yule Aliye Juu Zaidi, mkijua ya kwamba yeye atawaongoza na kuwaelekeza katika kila wakati wenye uhitaji, na mtajua pia kwamba yeye ni Mungu wa baraka pia.”a
Miaka 50 baadaye, Shule ya Gileadi yaendelea kufanikiwa! Wahitimu wa darasa la 94 sasa wana pendeleo la kuwafuata wale wahitimu zaidi ya 6,500 ambao wamewatangulia. Na wamtumainie kikamili yule Aliye Juu Zaidi wafanyapo sehemu yao katika kurundika lile “rundo la ushahidi” litakalosimama likiwa nguzo kwa utukufu wa Yehova Mungu.
[Maelezo ya Chini]
a Katika Kiebrania neno “Gileadi” lamaanisha “Rundo la Ushahidi.”—Mwanzo 31:47, 48, NW.
[Sanduku katika ukurasa wa 25]
Takwimu za Darasa
Jumla ya wanafunzi: 48
Hesabu ya nchi zilizowakilishwa: 5
Hesabu ya nchi walikogawiwa kwenda: 17
Umri wa wastani: 32
Miaka ya wastani katika kweli: 15.3
Miaka ya wastani katika huduma ya wakati wote: 9.6
[Sanduku katika ukurasa wa 26, 27]
KUPITIA MIAKA 50 YA SHULE YA GILEADI
Ni njia gani iliyo bora zaidi ya kuikumbuka historia ya Gileadi kuliko kupitia maono ya wale walioishi wakati huo—wahitimu wa mapema, wafunzi, na wengine waliosaidia kuipanga? Wasikilizaji walifurahi waliposikiliza ile sehemu “Kupitia Miaka 50 ya Shule ya Gileadi,” iliyoongozwa na Theodore Jaracz.
Ni hali zipi zilizoongoza kwenye kuanzishwa kwa shule hiyo? Ndugu Schroeder alieleza kwamba yeye pamoja na wafunzi wengine wawili walipewa miezi minne tu ya kuipanga shule hiyo. “Lakini kufikia Jumatatu, Februari 1, 1943, tulikuwa tayari kwa ajili ya kuwekwa wakfu.”
Ilikuwaje kwa wale wamishonari wa kwanza waliotumwa nje? Ndugu Henschel alikumbuka hivi: “Tulipanga kwamba idara ya usafirishaji ya Sosaiti ifunge katika masanduku makubwa ya mbao mali zote ambazo [wamishonari] walitaka kuchukua. Masanduku hayo yalipowasili, waliyafungua kwa uangalifu, wakaziondoa mali zao. Lakini waliyatumia masanduku hayo kutengeneza fanicha.” Hatimaye, akasema, Sosaiti ikapanga kuwe na makao ya mishonari yenye vifaa vya kiasi.
Baada ya hapo kwenye programu, baadhi ya wahitimu wa madarasa ya mapema ya Gileadi ambao sasa walikuwa washiriki wa familia ya Betheli ya U.S. walishiriki kumbukumbu zao, hisia zao, na maono yao. Maelezo yao kwa kweil yaligusa mioyo ya wote waliohudhuria.
“Baada ya mimi kupokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la kwanza la Gileadi, nilipata kujua kwamba mama yangu alikuwa na kansa. Lakini kwa kuwa alikuwa amefanya upainia tangu umri wa miaka 16 na kuendelea, alinishauri kwa nguvu niukubali mwaliko huo. Kwa hiyo nikiwa na hisia-moyo zilizochanganyika na nikimtumaini Yehova, nilisafiri hadi South Lansing. Nilifurahia sana na kuthamini sana mazoezi ya Gileadi. Mama yangu alimaliza mwendo wake wa kidunia muda fulani baada ya uhitimu wangu.”—Charlotte Schroeder, alitumikia katika Meksiko na El Salvado.
“Kwa kuwa Yehova alikuwa tayari amenitunza katika sehemu ya ulimwengu nilimokuwa, niliona kwamba kokote nilikokwenda kungekuwa bado dunia yake, naye angenitunza. Kwa hiyo nilifurahi sana kukubali mwaliko wa kwenda kwenye darasa la kwanza.”—Julia Wildman, alitumikia katika Meksiko na El Salvado.
“[Kazi ya umishonari] ilikuwa nzuri ajabu! Tungeweza kuongea penye kila mlango. Katika mwezi wa kwanza, niliangusha vitabu 107 na kuongoza mafunzo ya Biblia 19. Mwezi wa pili nilikuwa na mafunzo ya Biblia 28. Bila shaka, kulikuwa mambo fulani ambayo tulihitaji kuyazoea—joto, jasho, wadudu. Lakini lilikuwa pendeleo zuri ajabu kuwa huko. Ni jambo ambalo nitathamini sana sikuzote.”—Mary Adams, darasa la pili, kuhusu mgawo wake katika Kuba.
“Halihewa ilikuwa kimojawapo vizuizi vikubwa ambavyo tulihitaji kuvumilia katika Alaska. Katika sehemu ya kaskazini ilikuwa baridi mno, halijoto zikishuka hadi digrii 50 chini ya Sentigredi sufuri na baridi hata zaidi. Vijiji vya Wahindi na mahali-mahali padogo palipotengwa katika kusini-mashariki mwa Alaska palifikiwa ama kwa mashua ama kwa ndege.”—John Errichetti, darasa la tatu.
“Kwangu mimi Gileadi ilikuwa mwaliko kutoka kwa Yehova kupitia tengenezo lake la kidunia ili kutuimarisha kiroho na kutuonyesha njia nzuri ajabu ya maisha.”—Mildred Barr, darasa la 11, alitumikia katika Ailandi.
Mahojiano mengine yenye kufurahisha yalifuata—Lucille Henschel (darasa la 14, alitumikia katika Venezuela), Margareta Klein (darasa la 20, alitumikia katika Bolivia), Lucille Coultrup (darasa la 24, alitumikia katika Peru), Lorraine Wallen (darasa la 27, alitumikia katika Brazili), William and Sandra Malenfant (darasa la 34, walitumikia katika Moroko), Gerrit Lösch (darasa la 41, alitumikia katika Austria), na David Splane (darasa la 42, alitumikia katika Senegal).
Namna gani wale ndugu waliotumikia wakiwa wafunzi? Baadhi yao walihojiwa pia—Russell Kurzen, Karl Adams, Harold Jackson, Fred Rusk, Harry Peloyan, Jack Redford, na Ulysses Glass. Walifikiria pendeleo lao, wakionyesha jinsi ambavyo limewaathiri hadi leo hii.
Ushuhuda wenye kusisimua juu ya matokeo mazuri ya wamishonari waliozoezwa Gileadi ulitolewa na Lloyd Barry, aliyetumikia katika Japan. Katika 1949, wakati wamishonari 15 walipotumwa huko, kulikuwa wahubiri waliopungua 10 katika Japan nzima. Lakini miaka 44 baadaye, kuna wapiga mbiu ya Ufalme zaidi ya 175,000 katika bara hilo! Ndipo Robert Wallen aliposimulia juu ya mafanikio yenye kutokeza ambayo baadhi ya wamishonari wamekuwa nayo katika kuwasaidia watu waingie katika kweli, kutia ndani dada mmoja mishonari ambaye amekuwa katika Panama kwa miaka zaidi ya 45 na ambaye amewasaidia watu 125 kufikia hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa.
Upeo wa programu yote ulifikiwa wakati wote waliohudhuria na ambao walikuwa wahitimu wa Gileadi walipoalikwa waende jukwaani. Huo ulikuwa wakati wenye kugusa moyo kwelikweli. Miminiko wenye kuendelea wa akina ndugu na dada—89 katika familia ya Betheli kutia ndani wahitimu waliokuwa wametembelea—walitembea kupitia mstari katikati ya safu za viti na kupanda ngazi hadi jukwaani. Wale ndugu ambao wametumikia wakiwa wafunzi katika miaka iliyopita walijiunga nao, na kisha darasa la 94 likajiunga nao—wote wakiwa karibu 160!
“Je! kazi ya Shule ya Gileadi katika kuwazoeza wamishonari kwa ajili ya mabara ya kigeni imefanikiwa?” akauliza Ndugu Jaracz. “Uthibitisho wa miaka 50 ambayo imepita unajibu ndiyo kwa kishindo!”
[Picha katika ukurasa wa 25]
94th Graduating Class of the Watchtower Bible School of Gilead
In the list below, rows are numbered from front to back, and names are listed from left to right in each row.
(1) De La Garza, C.; Borg, E.; Arriaga, E.; Chooh, E.; Purves, D.; Fosberry, A.; Delgado, A.; Drescher, L. (2) Scott, V.; Fridlund, L.; Kettula, S.; Copeland, D.; Arriaga, J.; Thidé, J.; Olsson, E.; Widegren, S. (3) Delgado, F.; Keegan, S.; Leinonen, A.; Finnigan, E.; Fosberry, F.; Halbrook, J.; Berglund, A.; Jones, P. (4) Watson, B.; Frias, C.; Chooh, B.; Halbrook, J.; Purves, J.; Finnigan, S.; Jones, A.; Cuccia, M. (5) Scott, G.; Copeland, D.; Drescher, B.; De La Garza, R.; Leinonen, I.; Keegan, D.; Watson, T.; Kettula, M. (6) Widegren, J.; Borg, S.; Cuccia, L.; Berglund, A.; Olsson, B.; Frias, J.; Fridlund, T.; Thidé, P.