Wahitimu Wa Gileadi Waingia Njia ya Maisha Yenye Kuthawabisha
HUU ni wakati wenye furaha kama nini, uhitimu wa darasa la 90 la Gileadi!” Kwa maneno hayo, mwenyekiti, Karl F. Klein wa Baraza Linaloongoza, alitanguliza programu ya uhitimu. Akikumbuka wakati Watchtower Bible School of Gilead ilipoanza, aliongeza: “Nani angewaza, huko nyuma katika 1943, wakati darasa la kwanza la Gileadi lilipohitimu, kwamba miaka 48 baadaye tungekuwa bado tukikusanyika pamoja kwa uhitimu wa darasa lingine bado—la 90?”
Hata hivyo, siku ya Machi 3, 1991, siku yenye ujoto usio wa wakati wayo katika New Jersey, wageni waalikwa na washirika wa familia ya Betheli zaidi ya 4,000 walikusanyika kwenye Jumba la Kusanyiko la Jiji la Jersey, ng’ambo ile nyingine tu ya mto kutoka Jiji la New York, kwa ajili ya uhitimu wa wamisionari wapya hawa. Kabla ya kuingia maisha ya umisionari, wahitimu hao wangepokea shauri la kabla ya kuondoka siku hiyo ya uhitimu wao.
Programu ilifunguliwa kwa wimbo. Baada ya hapo, wote waliohudhuria waliguswa moyo kwa kina kirefu wakati Frederick W. Franz, msimamizi wa Watchtower Bible School of Gilead, mwenye miaka 97 alipotoa sala ya kufungua. Halafu, baada ya maelezo ya kutanguliza ya mwenyekiti, wahitimu—na wote waliohudhuria—walisikiliza kwa upendezi mfululizo wa hotuba fupi, zenye kutumika.
Max H. Larson wa Halmashauri ya Kiwanda alisema kwanza, juu ya kichwa “Wafanya Kazi Wenzi Pamoja na Yehova.” Baada ya kuelekeza fikira kwenye safina ya kuhifadhi ambayo Noa na familia yake walijenga, alisema hivi: “Leo Yehova anakusanya familia ya ulimwenguni pote ya mamilioni, naye akusudia kuchukua familia hiyo kubwa kupitia dhiki kubwa.’ Kwa jinsi gani? Kupitia safina ya ki-siku-hizi—paradiso ya kiroho! ‘Nyinyi,’ akakumbusha wahitimu, ‘mtakwenda sehemu tofauti-tofauti za dunia, ambapo mtakuwa wafanya kazi wenzi pamoja na Yehova katika kujenga safina ya ki-siku-hizi.’ Akiwatayarisha kwa yale yaliyokuwa mbele yao, alisema hivi: “Itahitaji kazi kwa upande wenu. Itahitaji subira. Mtakabili vizuizi. Hapo ndipo mtakapohitaji ustadi ambao kuzoezwa kwenu kumewapa.”
Daniel Sydlik, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alikuwa amezuru wamisionari wa muda mrefu katika Japan na Costa Rica. Akikuza kichwa “Njia Yenu ya Maisha Ni Yenye Kuthawabisha,” alishiriki baadhi ya madokezo yenye kusaidia ambayo alikuwa amepata kutoka kwa wamisionari hao waliofaulu. Yeye alieleza kwamba, dada mmoja alienenda kwa kufuata mashauri ambayo mama yake alikuwa amempa: ‘Penda utumishi wa shambani. Fanya urafiki na watu. Shiriki maisha yako na wengine, nayo itamaanisha furaha kwako.’ Dada mwingine alisema hivi: “Miaka ilipopita, tumekuja kuthamini kwamba ikiwa hatutazamii mengi sana kutoka kwa wengine, hatutatamauka rahisi. Tendo lolote la fadhili na kufikiria wengine linalofanywa kwa ajili yetu huwa na umaana wa zaidi kwetu.’ Kutumia shauri lenye kutumika kama hilo bila shaka kutasaidia wahitimu hao wawe wamisionari wenye kufaulu pia.
“Mwe wastahimilivu kuelekea wote,” lasema 1 Wathesalonike 5:14, NW. Leon Weaver wa Halmashauri ya Idara ya Utumishi alieleza juu ya andiko hilo alipokuwa akisema juu ya kichwa “Uwe Mwenye Subira Katika Utendaji Wako Wote.” Ni nani waliohusika katika “wote” ambao tunapaswa kuzoea subira kuelekea wao? Msemaji alijibu: ‘Wale ambao utakutana nao katika utumishi wa shambani. Akina dada na akina ndugu katika kundi lenu jipya. Wamisionari wenzenu. Wale katika tawi. Mwenzi wako wa ndoa. Wewe mwenyewe.’ Kwa nini uwe mwenye subira katika utendaji wako wote? ‘Akina dada na akina ndugu,’ msemaji akaeleza, ‘subira hupunguza mkazo na wasiwasi. Subira hutokeza amani. Subira huendeleza tumaini likiwa hai. Subira hutusaidia kudumisha shangwe yetu katika kutumikia.’
Albert D. Schroeder, mshiriki wa Baraza Linaloongoza na mwandishi-tarihi wa kwanza wa shule ya Gileadi, alisema halafu. Akisema juu ya kichwa “Endeleeni Kufuata Mfano Wenu—Yesu Kristo,” alitegemeza maelezo yake juu ya Wafilipi sura ya 2. “Acheni akili hii [“Hii iwe kufikiri kwenu,” kielezi-chini] iwe ndani ya ninyi, ambayo ilikuwa pia katika Kristo Yesu,” wasema mstari wa 5, NW. ‘Hilo laonyesha,’ msemaji akaeleza, ‘kwamba tunahitaji kuwa na kufikiri kulikosawazika, hata kama Yesu mwenyewe alivyokuwa na kufikiri kulikosawazika.’ Akianza na mstari wa 6, NW, halafu akafanya mchanganuo wenye kupendeza, akionyesha kwamba Paulo kwanza hutoa uthibitisho mbalimbali kwamba Yesu alikuwa na kufikiri kulikosawazika (mistari 6-8) halafu aorodhesha njia ambazo katika hizo Yehova alimthawabisha Yesu kwa mwendo wake wa utiifu (mistari 9-11). ‘Hiyo ni sehemu ya pendeleo lako,’ akamalizia, ‘kuwa ukihubiri juu ya Bwana Yesu Kristo, ukisaidia wengine kuwa na akili ile ile aliyokuwa nayo.’
Ni maneno gani ya kuaga ambayo wafunzi wa shule wangekuwa nayo kwa wanafunzi wao? Jack D. Redford alisema juu ya kichwa “Uwezo wa Kufikiri Utakulinda.” (Mithali 2:10, 11) ‘Mwendapo nje sasa,’ alieleza, ‘furaha yenu haitategemea juu ya wewe ni nani au juu ya ni nini ulicho nacho au hata juu ya uhakika wa kwamba wewe ni mhitimu wa Gileadi. Furaha yenu itategemea juu ya jinsi mnavyofikiri. Mkizoeza uwezo wenu wa kufikiri na kutumia maarifa yenu, mtakuwa na furaha.’ Akionyesha umaana wa uwezo wa kufikiri, alieleza hivi: “Tofauti kati ya tendo lililo haki na tendo lisilo haki ni fikira. Jambo unalofikiri linaamua kile unachofanya.’ J. D. Redford alimalizia kwa maneno haya ya kitia moyo kwa wanafunzi: ‘Kuna watu wengi sana wenye uelewevu mwingi ulimwenguni walio hafifu katika kufikiri, na kuna watu wengi wa akili ya kiasi ambao wamekuwa wenye ustadi katika kufikiri. Kwa hiyo pateni ustadi huo. Pigeni moyo konde kutumia akili zenu. Tumieni maarifa yenu. Wezaneni na matatizo. Pataneni na watu. Kubalini mamlaka. Mwe wenye matokeo katika kazi yenu. Vumilieni katika migawo yenu.’
Ulysses V. Glass, mwandishi-tarihi wa shule, alichagua kichwa “Yehova Anategemeza Mkono Wetu,” chenye msingi wa Zaburi 37:23, 24. ‘Ni lazima nisifu darasa hili,’ alionelea, ‘juu ya kupendezwa kwao katika kujifunza.’ Aliwakumbusha juu ya misaada mingineyo ambayo Yehova aliandaa katika kuwategemeza—Neno la Mungu, mtumwa mwaminifu mwenye akili chini ya uongozi wa Yesu kutolea Maandiko maana na ufahamu, vichapo mbalimbali, mikutano, na mikusanyiko. ‘Misaada ambayo mmetumia katika masomo yenu,’ aliendelea, ‘ni kama gongo na fimbo. Tunaihitaji kwa ajili ya tegemeo letu la kiroho, nayo inatuwezesha pia kusema na mamlaka katika kuwasilisha Neno la Mungu kwa wengine.’ Kwa kumalizia alikuwa na maneno haya ya kushauri wanafunzi: ‘Moyo wenu ukijawa na upendo kwa watu, mioyo yenye kufuatia haki itaitikia. Mtafaulu katika huduma yenu, nanyi mtajua kwamba Yehova anategemeza mkono wenu.’
Msemaji wa mwisho katika programu ya asubuhi alikuwa Carey W. Barber wa Baraza Linaloongoza, aliyechagua kichwa “Ingieni kwa Kupitia Mlango Ulio Mwembamba.” Akieleza juu ya Luka 13:23, 24, alionyesha kwamba: ‘Wengi hutaka mibaraka ya uhai, lakini ni wachache wanaotaka kujitahidi kwa nguvu ya kutosha ili kuipata.’ Vipi juu yetu? ‘Ni vizuri sisi tujiulize, “Mfano huu wa mlango mwembamba unamaanisha nini kwangu kibinafsi?”’ Wale wanaoshindwa kuingia kupitia mlango ulio mwembamba hushindwa, si kwa sababu haiwezekani, bali kwa sababu hawataki kujitahidi wenyewe. ‘Yehova haombi mambo mengi mno kwetu,’ msemaji alieleza. ‘Kwa msaada wa Yehova,’ akamalizia, ‘sisi sote na tujitahidi kwa nguvu ambayo yatosha ili kujipenyeza kupitia mlango mwembamba kuingia ulimwengu mpya wa uhai wa milele, amani, shangwe, na furaha, kwa utukufu wa milele wa Yehova!’
Baada ya maelezo hayo, mwenyekiti aliwasilisha salamu zilizopokewa kutoka sehemu mbalimbali za dunia. Sasa wakati ulikuwa umefika wahitimu wapokee diploma zao. Wanafunzi walikuwa wametoka nchi sita—Kanada, Finland, Ujerumani, Uingereza, Uswisi, na United States. Ingawaje, migawo yao itawapeleka kwa mabara kama Argentina, Benin, Bolivia, Jamhuri ya Dominica, Papua New Guinea, Peru, St. Lucia, na Taiwan. Na wahitimu walionaje siku hiyo ya uhitimu wao? Katika barua yenye kugusa moyo iliyoelekezwa kwa Baraza Linaloongoza na familia ya Betheli, kwa sehemu walisema hivi: “Tuna uhakika wa kupata tegemezo la Baraza Lina-loongoza, familia ya Betheli, na tengenezo zima la Yehova. Tunapokabili majaribu yaliyo mbele yetu, tegemezo hilo ni jambo ambalo tutathamini. Tunashukuru kweli kweli kwa jambo hilo.”
Baada ya kituo, programu ya alasiri ilianza na Funzo la Mnara wa Mlinzi lililofupishwa, lililoongozwa na Karl. A. Adams. Baada ya hilo, wanafunzi waliigiza maono ya kihalisi ya kupiga shabaha moyoni katika kufundisha Neno la Mungu. Hatimaye, wote waliohudhuria, kutia na wahitimu wa darasa la 90, walionea shangwe drama ya wakati unaofaa yenye kichwa Epuka Wasiwasi wa Maisha, iliyotolewa na wahubiri wa mahali hapo.
Mwenyekiti, Karl Klein, alisema kwa niaba ya wote aliposema katika maelezo yake ya kumalizia: “Kwa kweli imekuwa vyema kwetu kuwapo hapa siku hii ya tatu ya Machi 1991!” Ndipo programu hiyo yenye kupendeza ikaisha kwa wimbo wa kufunga, ukifuatwa na sala ya Harold J. Dies.
[Sanduku katika ukurasa wa 27]
Takwimu za Darasa
Hesabu ya nchi zenye kuwakilishwa: 6
Hesabu ya nchi walikogawiwa: 10
Jumla ya hesabu ya wanafunzi: 24
Umri wa wastani: 31.2
Miaka ya wastani katika kweli: 15
Miaka ya wastani katika huduma ya wakati wote: 11
[Picha katika ukurasa wa 26]
Darasa la 90 la Kuhitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Mnara wa Mlinzi
Katika orodha iliyopo chini, mistari imepewa namba kuanzia mbele mpaka nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto mpaka kulia katika kila mstari.
(1) Miller, M.; Helenius, S.; Marsh, L.; Kleeman, A.; Loosli, Y.; Nizan, H. (2) Skogen, R.; Nutter, D.; Noack, E.; Diehl, L.; Hair, J. (3) Marsh, C.; Helenius, H.; Loosli, M.; Danio, A.; Danio, A.; Nizan, D. (4) Miller, L.; Noack, J.; Hair, L.; Kleeman, W.; Skogen, D.; Diehl, S.; Nutter, W.