Wahitimu wa Gileadi Wahimizwa Wasitawishe Stadi Nzuri za Mawasiliano
SIKU ya Jumapili, Machi 4, 1990, watu zaidi ya 4,100 walijaza Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova la Jiji la Jersey kwa ajili ya sherehe ya kuhitimu ya darasa la 88 la Watchtower Bible School of Gilead. Wale wahitimu 24 walikuwa wametoka nchi 6 na sasa walikuwa wakitumwa kwenye jumla ya nchi 13.
Programu ilianza saa 4:00 asubuhi. Baada ya wimbo, George Gangas, ambaye sasa ana umri wa zaidi ya miaka 90 na ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alifungua kwa sala yenye hisia nyingi kwa Yehova. Kufuata hilo, mwenyekiti, C. W. Barber, pia mshiriki wa Baraza Linaloongoza na yeye mwenyewe akiwa ni mhitimu wa darasa la 26 la Gileadi, alizungumza juu ya mabadiliko ya haraka sana yanayotukia ulimwenguni. Alimalizia kwa kusema hivi: “Hakujapata kamwe kuwa na fursa nzuri zaidi kama iliyopo sasa ya kuwa washuhudiaji wa kwamba Yehova ni mkuu kupita wote na ni mwadilifu.” Halafu akasonga mbele na kujulisha wasemaji mbalimbali katika programu ya asubuhi.
Vernon Wisegarver, mshiriki wa Halmashauri ya Kiwanda katika Brooklyn, akacha-gua kichwa “Uwe Stadi Katika Kazi Yako.” Akivuta uangalifu kwenye kielezi cha mfua-vyuma wa kijijini aliyefua mnyororo imara, ulioshikizwa imara kwenye nanga, akaokoa uhai wa wote waliokuwa katika meli wakati wa dhoruba, alifananisha wahitimu wa Gileadi na mfua-vyuma. Kwa kufundisha watu juu ya Biblia, watawasaidia waunde mnyororo wenye kuokoa uhai wa sifa za kimungu, wakitumia stadi walizositawisha katika mazoezi yao ya Gileadi. Aliwatia moyo wahitimu hao waendelee kunoa stadi zao za kufundisha na kusimama mbele za aliye mkubwa zaidi wa Wafalme wote wakiwa “wafanya kazi wastadi.”
Halafu, John Barr, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, akaongea juu ya habari “Onja Uone Kwamba Yehova Ni Mwema.” Matamko yake yalitegemea msingi wa Zaburi 34:8, NW, ambayo husema: “Onjeni mwone kwamba Yehova ni mwema, Enyi watu; mwenye furaha ni yule mwanamume kakawana ambaye hufanya kimbilio katika yeye.” Aliwaonya hivi: “Onjeni kila kitu katika mgawo wenu wa kimisionari. Kijaribuni. Msikiogope. Ndipo mtaweza kujionea wema wa Yehova kwa njia msiyopata kuona. Msiwe wachagua vitu. Msiseme kamwe, ‘Sipendi hiki.’ Kionjeni.”
Charles Woody, mshiriki wa Halmashauri ya Idara ya Utumishi Brooklyn, alihutubu juu ya habari yake iliyochaguliwa, “Kuendeleza Maoni Yenye Usawaziko Juu Yetu Wenyewe.” Alisema hivi: “Sisi huona shangwe kuwa pamoja na wale walio na maoni yenye usawaziko juu yao wenyewe, ambao hawalazimishi mambo yafanywe sikuzote kama vile wao watakavyo, wenye haraka ya kupongeza na kujenga wengine, na ambao, ingawa wana maarifa, hawawafanyi wengine wahisi kwamba hawanayo.” Zaidi ya hilo alitaarifu hivi: “Nyinyi wamisionari mtataka kuvuta watu kwenye ukweli, si kufanya waondoe fikira zao kwenye huo. Tabia yenu ya unyenyekevu itakuwa yenye thamani sana katika kusaidia kutimiza jambo hilo.”
Lyman Swingle, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, ndipo akahutubu juu ya kichwa “Sura Zinazokuja, Zitatuambia Nini?” Alianza kwa kusema hivi: “Leo nyinyi mwaanza sura mpya katika maisha yenu. Mtaandika nini katika sura hizi sasa na kuendelea mpaka wakati ujao?” Aliwakumbusha hivi: “Kila jambo mfanyalo lapasa kumletea Yehova heshima na utukufu,” na akongezea hivi: “Hakikisheni kwamba maamuzi yenu yategemea msingi wa Neno la Mungu. Kumbuka Mithali 3:7, ambalo husema: ‘Usiwe mwenye hekima machoni pako.’ Mpatikane mkiwa waaminifu katika kutekeleza mgawo wenu.” Alimalizia kwa kusema hivi: “Sisi twatumaini kwamba hamtamaliza kamwe kuandika wasifu wenu, kwamba mtaishi milele.”
Halafu, Jack Redford, mmoja wa wafunzi wa shule, akawapa wahitimu waadhi huu: “Iweni Dhabihu Zilizo Hai.” Alianza kwa kusema hivi: “Utumishi wa kimisionari ni maisha ya kujidhabihu. . . . Sisi twawapenda nyinyi kwa roho yenu ya kujidhabihu.” Akinukuu kutokana na Wafilipi 2:17, NW, ambapo mtume Paulo alisema kwamba alikuwa amemwagwa kama toleo la kinywaji, ikimaanisha kwamba alikuwa na nia ya kujitumikisha sana akiwa dhabihu iliyo hai, akauliza hivi: “Lakini mara nyingi wamisionari huwa kama matoleo ya kinywaji kwa njia gani?” Halafu akasimulia maono mawili kuhusu wamisionari ambao hujitumikisha zaidi ya kiasi kinachotakwa. Mmoja alifanya matufali 16,000 kwa mikono yake mwenyewe akajenga Jumba la Ufalme la kwanza katika nchi aliyogawiwa. Ono lile jingine lilihusu dada aliyeandamana na mume wake kwenda huko nje porini, ambako hali za maisha zilikuwa za kishamba sana. Dada wa huko walimthamini sana dada huyo kwa sababu walitambua kwamba alikuwa akijimimina akiwa ‘dhabihu iliyo hai.’ Lakini ndipo mhutubu alipowakumbusha wanafunzi kwamba dhabihu haina thamani yoyote ikiwa haiambatani na utii. Akitumia usimulizi wa Mfalme Sauli na Waamaleki, alitoa waadhi huu: “Sikuzote kumbukeni kwamba utii ni bora kuliko dhabihu. Msijaribu kamwe kubishana na Yehova juu ya thamani ya mambo. Sikuzote fanyeni yale awaambiayo kufanya.”
Ndipo mwenyekiti akajulisha kwa mfunzi yule mwingine katika shule, Ulysses Glass. Ndugu Glass alianza kwa kusema: “Darasa la 88 lilikuwa na lingali darasa lenye furaha. Madarasa mengine pia yalikuwa yenye furaha. Basi, kwa nini furaha yenu yatokeza?” Alionyesha kwamba furaha “si mradi bali ni tokeo la kazi zifaazo. Zile hatua-hatua zinazofuatwa katika kufikia mradi ndizo huleta thawabu.” Alimnukuu mtungaji mmoja ambaye maisha yake yalibadilika kwa kuona hiki kifungu cha maneno: “Mafanikio ni safari, wala si mahali pale paendwapo.” Mtungaji alinadhiri kwamba angeacha kukadiri thamani ya furaha kwa msingi wa kufaulu kuwasili mahali pale aendapo badala ya kuyaona maisha yote yote kuwa safari yenye kuendelea. “Hakuna njia ya kwenda kwenye furaha,” yeye akasema. “Furaha ndiyo njia yenyewe.” Ndipo Ndugu Glass akaeleza kwamba darasa hili lilikuwa limeishika maana kuu ya maneno hayo. Alimalizia kwa maneno kutoka Zaburi ya 84 na akasema: “Endeleeni kutembea katika mahali penye maji maridhawa. Hata kama mtakabili matatizo gani, endeleeni kuwa na furaha iliyo ya wale wampendao na kumhofu Yehova.”
Ndipo ikaja hotuba kuu ya asubuhi hiyo, iliyotolewa na mshiriki mwingine wa Baraza Linaloongoza, Karl Klein, aliyechagua kichwa “Kusitawisha Mawasiliano ya Kikristo.” Alianza kwa kuwakumbusha wote kwamba Yehova ndiye mwasiliani mkubwa kupita wote. Mwana wake mzaliwa pekee, yule Logosi, alitumiwa kama Msemaji Mkuu wa Yehova, na akawasilisha mapenzi na maagizo ya Mungu kwa uumbaji wa kidunia. Yesu alipokuwa duniani, umati wa watu ulistaajabia njia yake ya kufundisha. Walikuwa hawajapata kamwe kusikia mtu akisema kama yeye. Kwenye Mathayo 28:19, 20, Yesu aliwatia moyo wanafunzi wake wawe wawasiliani wazuri kwa kwenda nje ulimwenguni, wakifundisha wengine amri zake na kuwafanya wao pia wawe wanafunzi.
Ndipo, akiwahutubia moja kwa moja wamisionari hao wa wakati ujao, Ndugu Klein akasema kwamba kuna njia nne za wamisionari kuhangaikia kusitawisha stadi nzuri za mawasiliano: kati ya mume na mke, pamoja na wengine katika makao ya kimisionari, pamoja na wale walio katika ofisi ya tawi ambako wamegawiwa, na pamoja na wale wanaokuta katika utumishi wa shambani. “Unaanza kuwasiliana kabla hujafungua kinywa chako,” Ndugu Klein akasema. “Hali ya kujichukua kwako na kujipamba huwasilisha maoni kwa mwenye nyumba.” Halafu akatoa vielezi kadhaa kuthibitisha wazo lake na akamalizia kwa mauidha haya: “Iweni wadhalili [wanyenyekevu] katika akili. Wekeni njia za mawasiliano zikiwa wazi. Jitahidini kuwa wawasiliani bora zaidi.”
Baada ya salamu kusomwa, kila mmoja wa wahitimu alipewa na mwenyekiti diploma za ustahili. Ndipo darasa hilo likatoa azimio lenye kuelekezwa kwa Baraza Linaloongoza na familia ya Betheli, likisomwa na Paul Angerville of Guadeloupe.
Kipindi cha alasiri kilianza na Funzo la Mnara wa Mlinzi. Baada ya hapo, wanafunzi walitoa programu iliyowapa wasikilizaji fursa ya kuona hali yao ya darasani, kuona vikutano vya starehe walivyokuwa navyo katika vyumba vyao, na kusikia mengi ya maono yao ya utumishi wa shambani tangu waje Gileadi miezi mitano iliyotangulia. Hatimaye, kulikuwa na drama nzuri yenye kichwa Kufanya Yafaayo Machoni pa Yehova. Drama hiyo iliigizwa na wahubiri kutoka Kundi la Lyndhurst, New Jersey. Siku ikamalizika kwa wimbo wa kumalizia, ikifuatwa na sala ya Fred Franz, msimamizi wa Sosaiti mwenye umri wa miaka 96.
[Sanduku katika ukurasa wa 27]
TAKWIMU ZA DARASA
Hesabu ya nchi zenye kuwakilishwa: 6
Hesabu ya nchi walikogawiwa: 13
Hesabu ya ndugu waseja: 2
Hesabu ya wenzi waliofunga ndoa: 11
Hesabu ya wanafunzi: 24
Umri wa wastani: 32.7
Miaka ya wastani katika ukweli: 14
Miaka ya wastani katika huduma ya wakati wote: 9
[Picha katika ukurasa wa 26]
Darasa Lenye Kuhitimu la 88 la Watchtower Bible School of Gilead
Katika orodha iliyo chini, safu zimepewa namba kutoka mbele kwenda nyuma na majina yameorodheshwa kutoka kushoto kwenda kulia katika kila mstari. (1) Magney, D.; Rogers, L.; Foster, S.; Foley, R.; Untch, L; Jonasson, G. (2) Buri, H.; Buri, B.; Krammer, M,; Hudson, D.; Underkoffler, J. (3) Angerville, P.; Olsson, M.; Jones, A.; Untch, R.; Krammer, A,; Hudson, C. (4) Foley, L.; Magney, J.; Jones, A.; Jonasson, H.; Foster, M.; Rogers, M,; Underkofller, R.