Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 6/1 kur. 21-23
  • Wahitimu wa Gileadi Wakubali Zawadi ya Utumishi wa Umishonari

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wahitimu wa Gileadi Wakubali Zawadi ya Utumishi wa Umishonari
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Habari Zinazolingana
  • Wahitimu Wa Gileadi Waingia Njia ya Maisha Yenye Kuthawabisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Shule ya Gileadi—Ina Umri wa Miaka 50 na Yaendelea Kufanikiwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Wamisionari Wapya Wanajitahidi Kufanikiwa Kweli Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Mfurahieni Yehova na Kushangilia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 6/1 kur. 21-23

Wahitimu wa Gileadi Wakubali Zawadi ya Utumishi wa Umishonari

KATIKA Machi 1, 1992, wale washiriki 22 wa darasa la kuhitimu la 92 la Watchtower Bible School of Gilead walikubali zawadi—zawadi ya utumishi wa Umishonari. Alipokuwa akihutubia darasa hilo, Lloyd Barry wa Baraza Linaloongoza alitaarifu hivi: “Na ipokeeni zawadi hiyo zuri ajabu kwa shangwe nyingi, na itumieni ili kuwaletea wengine shangwe.”

Wageni waliokaribishwa na washiriki wa familia ya Betheli wapatao 4,662 walikusanyika kwenye Jumba la Kusanyiko la Jersey City, katika New Jersey, kwa ajili ya programu ya kuhitimu. Wengine wapatao 970 kwenye vifaa vilivyoko New York vya Watchtower Society katika Brooklyn, Wallkill, na Patterson waliunganishwa kwa nyuzi za simu. Wote walisikiliza kwa makini wakati wahitimu walipokuwa wakipewa mawaidha ya kuwaaga ambayo yangewasaidia kuthamini sana ile zawadi ya utumishi wa umishonari na kuitumia kwa hekima.

Programu ilifunguliwa kwa uimbaji mchangamfu wa wimbo nambari 155, “‘Mkaribishane’!” Baadaye, wote waliguswa moyo wakati Frederick W. Franz, msimamizi wa Shule ya Gileadi mwenye umri wa miaka 98, alipotoa sala yenye kuhisiwa moyoni. Halafu, mwenyekiti, Carey Barber wa Baraza Linaloongoza, alikaribisha wote kwenye programu ya kuhitimu akasema: “Hakujapata kuwa uhitaji mkubwa zaidi wa wamishonari wa Gileadi kuliko leo.” Baada ya maelezo yake, alikaribisha mfululizo wa hotuba fupi zenye kusaidia.

Curtis Johnson wa Halmashauri ya Kao la Betheli alikuwa wa kwanza kusema, akikuza kichwa “Tunza Vema Bustani Yako.” Ndugu Johnson alionyesha kwamba wamishonari hao wapya wapatapo migawo yao, kila mmoja wao atakuwa na bustani ya kiroho ya kulima. (1 Wakorintho 3:9) Watu wa Yehova ulimwenguni pote ni bustani ya kiroho inayomea uadilifu na sifa mbele ya mataifa yote. (Isaya 61:11) ‘Jinsi utunzavyo bustani yako ya kiroho wakati ujao,’ msemaji akakazia, ‘itaathiri sana mafanikio yako katika mgawo wako wa umishonari.’ Ni nini kitakachowasaidia watunze vema bustani yao ya kiroho? ‘Yehova aweza kuwa ukuta wa ulinzi unaozingira bustani yako ya kiroho. Ukiazimia kukuza vitendo vinavyofaa, kudumisha ukaribu naye kwa sala, na kisha kutenda kulingana na sala zako.’

Halafu, Lloyd Barry alisema juu ya kichwa “Furahini Katika Bwana Sikuzote.” (Wafilipi 4:4) Akiwa na ujuzi wa umishonari wa miaka zaidi ya 25 katika Japani ambao angeweza kutumia, alikuwa na madokezo yenye kutumika ya kuwasaidia wahitimu hao waonee shangwe zawadi ya utumishi wa umishonari. Alionelea hivi: ‘Mtapata kwamba shangwe mliyo nayo katika utumishi wa Mungu itawasaidia mshinde mikazo ya mawazo na labda baadhi ya matatizo ya kimwili ambayo yatawapata.’ (Mithali 17:22) Aliwakumbusha wahitimu kwamba huenda wakakabili hali na mambo ambayo ni tofauti sana na yale ambayo wamezoelea. Huenda ikawa lazima wajifunze lugha mpya. ‘Mtahitaji kujitahidi kujifunza lugha hiyo. Lakini mwezapo kuwasiliana kwa uhuru na watu katika lugha yao wenyewe, hilo pia litaongezea shangwe yenu.’

Akikuza kichwa “Kazia Zawadi Macho Yako,” Eldor Timm wa Halmashauri ya Kiwanda alifuata. Zawadi hiyo ni nini? Uhai wa milele! Ili kuipata ni lazima tukazie zawadi hiyo macho yetu. Msemaji huyo alizungumzia baadhi ya mambo yenye kufanana na yaliyo tofauti kati ya Wakristo walio katika shindano la mbio la kupata uhai na wapiga mbio katika mashindano ya riadha ya karne ya kwanza. Sawa na wapiga mbio hao, ni lazima Wakristo wajizoeze kwa bidii, wafuate sheria, na wajiondolee mizigo yenye kuwalemeza. Lakini tofauti na wapiga mbio halisi, Wakristo wamo katika shindano la mbio lenye urefu wa maisha yao nao wanajitahidi kupata zawadi ya milele. Badala ya kuwa na mshindi mmoja, wote wanaopiga mbio hadi mwisho katika shindano la kupata uhai wataipokea zawadi. Ndugu Timm alimalizia hivi: ‘Ili tupate zawadi ya uhai, ni lazima tuwe na amani pamoja na Yehova, Mpaji zawadi. Na ili tuwe na amani pamoja na Yehova, ni lazima tuwe na amani pamoja na ndugu zetu.’

Milton Henschel wa Baraza Linaloongoza alifuata akisema juu ya kichwa “Kwa Faraja ya Maandiko, Tuna Tumaini.” (Warumi 15:4) ‘Kwa miezi mitano iliyopita,’ akaanza msemaji, ‘mmekuwa na shughuli nyingi mkitumia Biblia. Kuikaribia sana kumetukia. Mna tumaini lenye nguvu. Mwendapo kwenye migawo yenu, tafadhali mkumbuke ni kwa nini tumaini lenu ni lenye nguvu. Ni kwa sababu mmekaa karibu na Maandiko.’ Ili kuonyesha mfano wa usimulizi wa Biblia unaochochea tumaini, msemaji alirejezea Waamuzi sura 6 hadi 8, zinazosimulia jinsi Gideoni alivyopewa utume wa kukomboa Israeli kutoka katika uonevu wa Midiani. Baada ya kuzungumzia usimulizi huo na umaana wao kwa siku yetu, alisema hivi: ‘Mpatapo nafasi ya kuwa karibu na Maandiko na kufikiria mambo hayo, itawaburudisha. Mtapata moyo mkuu.’

Wote walikuwa na hamu ya kusikia ni mawaidha gani ya kuaga ambayo wale wafunzi wakuu wawili wa shule wangewatolea wanafunzi. Jack Redford alikuwa wa kwanza kusema juu ya kichwa “Fanya Jambo Lifaalo.” Aliwakumbusha wahitimu: ‘Kwenye Gileadi mlizoezwa kikamili juu ya lile lifaalo kulingana na Maandiko. Sasa mwaenda kwenye migawo ya umishonari yenye ugumu. Na twajua kwamba labda mtapata matatizo magumu njiani. Yajapokuwa hayo, na zijapokuwa hisia zenu wenyewe, twajua kwamba mwaweza kufanya jambo lifaalo.’ Ni nini kitakachosaidia? Kwanza, kuwa na maoni yafaayo juu ya wengine. Msemaji alisema hivi: ‘Msitazamie ukamilifu kutoka kwa kutokamilika.’ Kuwa na maoni yafaayo juu ya hali zenye kujaribu kwaweza kusaidia pia. ‘Sisi sote tunapatwa na hali tofauti maishani,’ yeye akasema. ‘Mtu yeyote aweza kushughulika na hali nzuri. Ni jinsi ushughulikavyo na hali mbaya itakayoamua kama utavumilia katika utumishi wa umishonari.’—Yakobo 1:2-4.

Msajili wa shule, Ulysses Glass, alichagua kichwa “Kuna Tumaini Gani kwa Wakati Ujao?” Kwa sauti ya kibaba, aliwatia moyo wahitimu wadumishe tumaini lao likiwa linawaka kwa uangavu. (Mithali 13:12) ‘Tumaini lianzapo kupotea huenda hilo lisionekane wazi,’ akaeleza. ‘Hali huenda zikatufanya tujishughulikie wenyewe badala ya uhusiano wetu na Mungu. Huenda tukawa wagonjwa au kuhisi tunatendewa vibaya na wengine. Wengine huenda wakawa na vitu vingi vya kimwili kuliko sisi au huenda wakawa na matokeo bora zaidi katika huduma, na huenda tukawa wenye wivu kidogo. Tukiruhusu mambo hayo yatunase polepole, upesi uhalisi wa tumaini la Ufalme utafifia moyoni na akilini mwetu, na huenda hata tukaacha kuvumilia katika shindano la mbio la kupata uhai.’ Ni nini kiwezacho kufanywa? ‘Ni lazima hatua chanya ichukuliwe ili tuweze kuhuisha tena tumaini letu. Ni lazima tujaze akili na mioyo yetu ahadi za Mungu za hakika na kuelekeza fikira zetu kamili kwenye uhalisi wa Ufalme wa Mungu. Na ni lazima tuanzishe tena uwasiliano wetu pamoja na Mungu, kwani hilo kwa kweli litaongoza kwenye shangwe.’

Karl Klein wa Baraza Linaloongoza ndiye alitoa hotuba ya kuhitimu. Kichwa chake kilikuwa “Kwa Nini Tuwe Wanyenyekevu?” Na jibu la swali hilo ni nini? ‘Kwa sababu hilo ndilo jambo lifaalo na la haki kufanya, na jambo la hekima na la upendo kufanya,’ akaeleza katika maneno yake ya kufungua. Wasikilizaji walivutiwa alipozungumzia mifano minne ya unyenyekevu ambayo twafanya vema kuiga: (1) Yehova Mungu, ambaye kwa hakika alikuwa mnyenyekevu aliposhughulika na Abrahamu na Musa (Mwanzo 18:22-33; Hesabu 14:11-21; Waefeso 5:1); (2) Yesu Kristo, ‘aliyejinyenyekeza akawa mtiifu mpaka kifo juu ya mti wa mateso’ (Wafilipi 2:5-8, NW; 1 Petro 2:21); (3) Mtume Paulo ‘aliyemtumikia Bwana kwa unyenyekevu wote’ (Matendo 20:18, 19; 1 Wakorintho 11:1); na (4) ‘wale wanaotuongoza,’ kama vile msimamizi wa kwanza wa Sosaiti, Ndugu Russell, aliyeandika hivi wakati mmoja: “Kazi ambayo katika hiyo Bwana amependezwa kutumia stadi zetu zenye unyenyekevu imekuwa zaidi kazi ya kujenga upya, kurekebisha, kupatanisha kuliko kuwa kazi ya kuanzilisha.” (Waebrania 13:7) Ndugu Klein aliorodhesha sababu nyingine zenye nguvu za kuwa wanyenyekevu. Kwa hakika, kutii lile shauri kuwa wanyenyekevu kutasaidia wahitimu watumie kwa hekima zawadi ya utumishi wa umishonari!

Baada ya maelezo hayo, mwenyekiti alishiriki salamu zilizopokewa kutoka sehemu mbalimbali za dunia. Wakati ulikuwa umefika wa wahitimu kupokea diploma zao. Walikuwa wametoka nchi saba—Kanada, Finland, Ufaransa, Maurishiasi, Uholanzi, Uswede, na United States. Lakini migawo yao ya umishonari inawapeleka kwenye nchi 11—Bolivia, Estonia, Grenada, Guatemala, Hondurasi, Hangari, Maurishiasi, Peru, Togo, Uturuki, na Venezuela.

Baada ya pindi fupi ya pumziko, programu ya alasiri ilianza kwa Funzo la Mnara wa Mlinzi lililofupishwa lililoongozwa na Joel Adams wa Halmashauri ya Idara ya Utumishi. Baada ya hapo, wahitimu waliigiza baadhi ya maono ya utumishi wa shambani waliyokuwa wamefurahia wakati wa muhula wa shule. Mwishowe, drama Kwa Nini Tutii Utaratibu wa Kitheokrasi? ilitolewa ili kuwanufaisha wasikilizaje wote, kutia na wahitimu.

Kwa kweli, wahitimu hao waliondoka kwenda kwenye migawo yao ya kigeni wakiwa na mawaidha na kitia-moyo kitakachowasaidia waitumie zawadi ya utumishi wa umishonari ili kuletea shangwe si wao wenyewe bali na wengine pia.

[Chati katika ukurasa wa 22]

Takwimu za Darasa

Hesabu za nchi zenye kuwakilishwa: 7

Hesabu za nchi walikogawiwa: 11

Hesabu ya wanafunzi: 22

Umri wa wastani: 33:4

Wastani wa miaka katika kweli: 16.7

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 11.8

[Picha katika ukurasa wa 23]

Darasa la 92 la Kuhitimu la Watchtower Bible School of Gilead

Katika orodha iliyopo chini, mistari imepewa namba kuanzia mbele mpaka nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto mpaka kulia katika kila mstari.

(1) Chan Chin Wah, M.; Bouancheaux, N.; Chapman, B.; Östberg, A.; Cole, L.; Jackson, K.; Meerwijk, A. (2) Smith, J.; Wollin, K.; Chapman, R.; Gabour, N.; Chan Chin Wah, J.; Smith, C.; Edvik, L. (3) Bouancheaux, E.; Östberg, S.; Cole, K.; Jackson, R.; Gabour, S.; Edvik, V.; Meerwijk, R.; Wollin, G.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki