Wamisionari Wapya Wanajitahidi Kufanikiwa Kweli Kweli
JUMAPILI, Septemba 8, 1985, ilikuwa siku itakayokumbukwa sana na wale 4,351 waliosongamana ndani ya Jumba la Makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova lililojengwa vizuri sana Mjini Jersey. Walikuja kushuhudia kuhitimu kwa darasa la 79 la Shule ya Gileadi ya Sosaiti yetu.
Siku hiyo ilikuwa ya kukumbukwa sana kwa sababu hayo ndiyo yaliyokuwa matumizi ya kwanza ya hilo Jumba la Makusanyiko tangu liwekwe wakfu rasmi. Halafu, pia tangu mwaka 1970 hiyo ndiyo mara ya kwanza washiriki karibu wote wa jamaa ya Betheli ya United States kuwa pamoja ndani ya jengo moja. Jamaa hiyo, kutia na wafanya kazi wa Brooklyn na wa mashamba ya Sosaiti, imeongezeka ikawa zaidi ya 3,500. Kwa sababu Jumba la Makusanyiko Mjini Jersey limemalizwa, hatimaye kumepatikana jengo linaloweza kuwatoshea wote.
Siku hiyo ilikuwa ya kukumbukwa sana hasa kwa watumishi vijana 24 wa Yehova waliotoka katika nchi kumi mbalimbali wakajumlika kuwa darasa la 79. Walikuwa wametumia miezi mitano iliyotangulia wakiwa katika taaluma ya funzo la Biblia na matayarisho ya umisionari. Sasa, kulingana na maneno ya Albert Schroeder, aliyekuwa mwenyekiti siku hiyo, wao walikoma kuwa wanafunzi wa Gileadi wakawa wahitimu wa Gileadi.
Wakiwa katika starehe ya Jumba la Makusanyiko lenye vifaa vya kupepea hewa ndani, wamisionari hao 24 waliagwa kwa njia watakayoikumbuka muda mrefu. Mwenyekiti aliwakumbusha kwamba wakiwa Gileadi walijifunza mambo mengi. Lakini Gileadi ilikuwa imekazia jambo fulani la maana zaidi: hali ya kiroho. Ndipo mwenyekiti alipokaribisha wasemaji kadha wawaambie wenye kuhitimu maneno fulani ya mwisho.
Carey Barber, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alihutubu juu ya utafutaji wa furaha. Aliwakumbusha wenye kuhitimu kwamba Sulemani aliona kuwa anasa za ulimwengu huu hazileti furaha. (Mhubiri 2:1-11, 17) Kwa hiyo Yesu alikazia uhitaji wa mambo ya kiroho katika utafutaji wa furaha. (Mathayo 5:3) Basi, wenye kuhitimu wanapaswa kufuata shauri la Yesu. Halafu, hata umisionari wao ukitia ndani kuacha starehe fulani za kimwili, bado wanaweza kufanikiwa.
Msemaji aliyefuata, John Booth, pia wa Baraza Linaloongoza, aliwakumbusha wasikilizaji kwamba Paulo mmisionari mwenye umri mkubwa alimtia moyo Timotheo mmisionari mwenye umri mdogo azidi kufanya maendeleo katika mwenendo wa Kikristo, funzo la kibinafsi, na sala. (1 Timotheo 2:1, 8; 4:12-16) Wamisionari wapya hao wangehitaji kufanya maendeleo ya namna iyo hiyo ikiwa wanataka kufanikiwa. Halafu, mwandishi-mweka-hazina wa Sosaiti, Lyman Swingle, akataja kwamba hivi majuzi aliuliza wamisionari katika Brazili ni shauri gani wangependa kuwapa wamisionari wapya ili kuwasaidia wafanikiwe. Walimpa himizo la kwamba, “Kawaambie watakapofika kwenye migawo yao inawapasa waendelee kuisoma Biblia na kufanya uchunguzi wa Kibiblia.”
David Olson, wa Halmashauri ya Idara ya Utumishi, alieleza jambo lililoonwa kuhusu mwanamume mmoja aliyesimamia sehemu fulani ya ile shughuli iliyowezesha mwanadamu afike mwezini. Baadaye, mwanamume uyo huyo alijipatia riziki kwa kuwa mfagiaji wa maeneo ya kuwekea magari. Alijisikia akipata mafanikio zaidi katika hiyo kazi yake ya pili. Kwa sababu gani? Kwa sababu kazi yake mpya ilimruhusu awe na wakati wa kumtumikia Yehova na kutunza jamaa yake. Kwa kweli, wale wanaofurahia Yehova, sheria yake, na utumishi wake wanapata mafanikio ya kweli kweli.—Zaburi 1:1-3.
Ulysses Glass, mwandikishaji wa Gileadi, aliwapa heko wenye kuhitimu hao kwa sababu walichukua mambo kwa uzito na kuonyesha heshima. Alisema walipendezwa na mafunzo yao na wakataka sana wapate ufahamu kamili wa mambo. Akasema mambo hayo yangewasaidia katika migawo yao. Jack Redford mwalimu wa Gileadi akaongezea kwamba mwaka wa kwanza wa kuwa katika migawo yao ungekuwa mgumu. Hata hivyo, ili wafanikiwe inawapasa kufanya kazi kwa ukaribu pamoja na wamisionari wale wengine, wawe na subira, na kusitawisha furaha ya kiroho.—Mhubiri 7:8, 9.
Msemaji wa mwisho, Msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi Frederick Franz alifungua hotuba yake kwa maneno haya: “Lilikuwa jambo lenye faida niishi miaka 92 ili niwepo katika pindi ya namna hii!” Ndipo alipowaeleza wenye kuhitimu historia ya jinsi Gileadi ilivyoanzishwa na kuwahimiza wabaki wakiwa waaminifu katika migawo yao.
Baada ya hotuba zilizotolewa, wanafunzi walipokea diploma zao, kisha kukawa na mapumziko ya kujipatia viburudisho. Halafu wakatoa maelezo juu ya funzo la gazeti lililo la karibuni zaidi la Mnara wa Mlinzi likisimamiwa na Dean Songer wa Halmashauri ya Kiwanda. Kisha wakamfurahisha kila mtu kwa mambo yaliyoonwa, muziki, na mawonyesho ya jinsi walivyofurahia kuwa Gileadi na kuazimia wayatafute “mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:10) Mwishowe, wenye kuhitimu waliuonyesha kwa wakati wake huu mchezo wa kuigiza: Tafuta Uadilifu wa Mungu Ukaokolewe.
Basi siku hiyo ya kukumbukwa sana ikafikia mwisho. Ilikuwa siku ambayo itabaki katika fikira za wanafunzi hao kwa muda mrefu wanapofuata mashauri waliyosikia kisha wajitahidi kufanikiwa kweli kweli katika migawo yao ya umisionari.