Wapiga-mbiu wa Ufalme Waripoti
Mungu Aikuza Katika Alaska
IKIWA imefunikwa chini ya theluji na barafu, mbegu ndogo yasubiri fursa ya kusitawi hadi kukomaa. Katika ile miezi mitatu mifupi ifanyizayo kiangazi cha Alaska, mbegu ya kabeji iliyo na kipenyo cha milimeta tatu yaweza kukua kufikia kilogramu 40! Ndiyo, nchi hiyo ambayo wakati mmoja ilidhaniwa na wengi kuwa ardhi kame, iliyoharibiwa na theluji yaweza kutokeza mazao mengi.
Hilo ni kweli hasa kuhusu shamba la kiroho katika Alaska. Huko, katika nchi ya majira marefu ya baridi kali, Mashahidi wa Yehova waendelea kupanda mbegu ya Ufalme. Kama vile katika sehemu nyingine za dunia, Mungu huikuza mbegu katika mioyo yenye rutuba.—1 Wakorintho 3:6, 7.
● Akiwa ndani ya basi la shule, Shahidi mchanga aitwaye Vanessa alimchunguza kwa makini mwanafunzi mwenzake, Ann, ambaye aliketi peke yake sikuzote. Ann alionekana kuwa mwenye huzuni, kwa hiyo Vanessa akamwalika Ann aketi kando yake. Si ajabu Ann alikuwa na huzuni! Mama yake alikuwa amekufa kutokana na mshiko wa moyo, na muda mfupi baadaye, baba yake akafa kutokana na kansa. Hiyo ndiyo sababu Ann alikuwa akiishi na jamaa zake huko Alaska.
Vanessa alipitia nyumbani kwa mfahamiwa wake mpya alipokuwa katika utumishi wa shambani Jumamosi moja na kumwachia broshua Je! Kweli Mungu Anatujali? Jumatatu iliyofuata, Ann alimtafuta shuleni huyo Shahidi mchanga. Ann alikuwa na maswali mengi ya Biblia, ambayo Vanessa aliweza kuyajibu. “Mnaabudia wapi?” akauliza. Jioni hiyo Ann akahudhuria mkutano wake wa kwanza kwenye Jumba la Ufalme.
Haikuchukua muda mrefu kabla yatima huyo mwenye umri wa miaka 17 hajapata ‘baba’ na ‘mama’ wengi, kama vile alivyoahidi Yesu. (Mathayo 19:29) Nayo ilikuwa pindi yenye shangwe kama nini kumwona Ann mwenye furaha na tabasamu akionyesha wakfu wake kwa Yehova kwa kubatizwa katika maji kwenye “Wajumbe wa Amani ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya!
● Katika maeneo ya mbali ya eneo kubwa la Aktiki ya Alaska—ambapo vijiji vimetenganishwa kwa mamia ya kilometa za nyika—ndege yenye mitambo miwili ya Watch Tower Society imetumiwa kupanda mbegu ya Ufalme katika jumuiya zaidi ya 150. Lakini ukuzi wa kiroho kupitia funzo la kawaida la Biblia hutegemea kuandikiana barua. Kwa kuwa kuandika barua ni jambo gumu kwa watu wengi, mwalimu wa Biblia ahitaji kuwa mbunifu ili adumishe upendezi wa mwanafunzi. Hilo laweza kutimizwaje?
Kathy aliongoza funzo la Biblia lenye kuendelea na Edna, ingawa waliishi sehemu zilizotenganishwa kwa umbali wa kilometa 600! Badala ya kunakili tu maswali yaliyo katika msaada wa kujifunzia, Kathy alitayarisha karatasi nyingine yenye maswali, akaandaa nafasi ya kuandika majibu. Baada ya Edna kujaza majibu, Kathy alimjibu na kutia ndani maelezo ihitajiwavyo ili kuweka wazi hoja fulani. Kathy ataarifu hivi: “Mimi nilitenga Jumatano jioni kwa ajili ya ‘funzo’ letu, nami nilijaribu kushikamana nalo kama vile ningefanya na miadi mingine ya funzo la Biblia. Pia nilimpelekea Edna bahasha yenye anwani yangu, na stampu. Kwa kuwa ilichukua majuma mawili kupeleka barua, kwa njia fulani funzo la kuandikiana barua lilionekana kuwa la polepole.”
Wazia msisimko uliotokea wakati ambapo Kathy na Edna walikutana uso kwa uso kwenye mkusanyiko wa wilaya katika Anchorage baada ya miezi kumi ya kujifunza kupitia barua! Hao Mashahidi waliterema kwamba katika wahudhuriaji mlikuwemo wanafunzi wa Biblia na wengine wenye kupendezwa kutoka katika vijiji kadhaa vilivyo peke yake katika Alaska.
Ingawa huenda nyakati nyingine ukuzi ukaonekana kuwa wa polepole, “miche” fulani yaweza kuota haraka ipatapo nuru ya kweli. Kwa wastani, wasifaji wa Yehova zaidi ya mia moja hubatizwa katika Alaska kila mwaka! Twasema, “Asante, Yehova,” kwa kuikuza!