Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 3/1 kur. 26-29
  • Watu ‘Wenye Hisia Kama Zetu’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Watu ‘Wenye Hisia Kama Zetu’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Musa Alitoka Kwenye Uhakika wa Kupita Kiasi Hadi Usikivu
  • Eliya Alikuwa na Hisia Kama Zetu Wakati wa Kutoa Nidhamu
  • Yeremia Alionyesha Moyo Mkuu Kijapokuwa Kivunjamoyo
  • Yesu Alikuwa na Hisia Kama Zetu
  • Uhakika wa Yehova
  • Eliya “Akaomba kwa Bidii Mvua Isinye”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Je, Utakuwa Mwaminifu Kama Eliya?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Alifarijiwa na Mungu Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Alikaa Macho, na Alingoja
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 3/1 kur. 26-29

Watu ‘Wenye Hisia Kama Zetu’

ALIKUWA mfalme na nabii lakini pia baba mwenye upendo. Mmoja wa wana wake alikua akawa mtu asiyefaa kitu na mwenye kiburi. Katika jaribio lenye kuazimia la kunyakua kiti cha ufalme, mwana huyo alianzisha vita ya wenyewe kwa wenyewe, iliyokusudiwa kumwua baba yake. Lakini katika pigano lililofuata, huyo mwana ndiye aliyeuawa. Baba alipopata kujua juu ya kifo cha mwana wake, alienda peke yake kwenye paa na kutoa machozi: “Mwanangu Absalomu! Ee mwanangu! mwanangu Absalomu! laiti ningalikufa badala yako, Absalomu, mwanangu, mwanangu!” (2 Samweli 18:33) Huyo baba alikuwa Mfalme Daudi. Sawa na manabii wengine wa Yehova, alikuwa “mtu mwenye hisia kama zetu.”—Yakobo 5:17.

Katika nyakati za Biblia wanaume na wanawake waliosema kwa niaba ya Yehova walitoka katika matabaka yote ya maisha nao walikuwa watu wa kawaida. Sawa nasi, walikuwa na matatizo na waliteseka kutokana na kutokamilika. Baadhi ya manabii hao walikuwa nani, na hisia zao zilikuwaje kama zetu?

Musa Alitoka Kwenye Uhakika wa Kupita Kiasi Hadi Usikivu

Musa alikuwa nabii mashuhuri wa kabla ya nyakati za Ukristo. Hata hivyo, hata alipokuwa na umri wa miaka 40, hakuwa tayari kutumikia akiwa msemaji wa Yehova. Kwa nini? Ingawa ndugu zake walikuwa wakionewa na Farao wa Misri, Musa alilelewa katika nyumba ya Farao naye alikuwa “mwenye nguvu katika maneno na vitendo.” Rekodi yaendelea kutuambia hivi: “Alikuwa akidhani ndugu zake wangefahamu ya kwamba Mungu alikuwa akiwapa wao wokovu kwa mkono wake.” Akiwa na uhakika kupita kiasi, alitenda kwa kutumia nguvu akimtetea mtumwa Mwebrania, akamwua Mmisri.—Matendo 7:22-25; Kutoka 2:11-14.

Sasa Musa alilazimika kukimbia, naye aliishi miongo minne iliyofuata akiwa mchungaji katika Midiani iliyokuwa mbali. (Kutoka 2:15) Mwishoni mwa wakati huo, Musa, sasa akiwa na umri wa miaka 80, alipewa utume na Yehova wa kuwa nabii. Lakini Musa hakuwa na uhakika kupita kiasi tena. Alihisi kuwa hastahili hata kidogo hivi kwamba alitilia mashaka kupewa utume kwake na Yehova awe nabii, akitumia semi kama, “Mimi ni nani, hata niende kwa Farao?” na, “Niwaambie nini?” (Kutoka 3:11, 13) Kwa uhakikishio na msaada wenye upendo wa Yehova, Musa alisonga mbele katika kutimiza mgawo wake kwa mafanikio makubwa.

Je, wewe umeruhusu kuwa na uhakika kupita kiasi kukuongoze kufanya au kusema mambo yaliyothibitika kuwa yasiyo ya hekima, kama alivyofanya Musa? Ikiwa ndivyo, kubali mazoezi zaidi kwa unyenyekevu. Au je, umepata kuhisi kuwa huna sifa za kustahili kutimiza madaraka fulani ya Kikristo? Badala ya kuyakataa, kubali msaada utolewao na Yehova na tengenezo lake. Yule aliyemsaidia Musa aweza kukusaidia wewe pia.

Eliya Alikuwa na Hisia Kama Zetu Wakati wa Kutoa Nidhamu

“Eliya alikuwa mtu mwenye hisia kama zetu, na bado katika sala alisali mvua isinye; na mvua haikunya juu ya nchi kwa miaka mitatu na miezi sita.” (Yakobo 5:17) Sala ya Eliya ilipatana na mapenzi ya Yehova ya kulitia nidhamu taifa lililokuwa limegeukia mbali kutoka Kwake. Hata hivyo, Eliya alijua kwamba ukavu aliokuwa akiombea ungesababisha kuteseka kwa binadamu. Sehemu kubwa ya Israeli ilikuwa ya ukulima; umande na mvua vilikuwa uhai wa watu. Ukavu wa kuendelea ungeleta taabu ya kupita kiasi. Mimea ingenyauka; mazao yangekosa kufaulu. Wanyama wa nyumbani waliotumiwa kwa ajili ya kazi na chakula wangekufa, na familia kadhaa zingeelekea kufa njaa. Ni nani ambaye angeteseka zaidi? Watu wa kawaida. Mjane alimwambia Eliya baadaye kwamba alikuwa na konzi la unga na mafuta kidogo tu yaliyosalia. Alitarajia kabisa-kabisa kwamba yeye na mwana wake wangekufa njaa karibuni. (1 Wafalme 17:12) Ili Eliya asali alivyosali, lazima awe alikuwa na imani imara ya kwamba Yehova angewatunza watumishi Wake—matajiri au maskini—ambao hawakuwa wameacha ibada ya kweli. Kama vile rekodi ionyeshavyo, Eliya hakutamaushwa.—1 Wafalme 17:13-16; 18:3-5.

Miaka mitatu baadaye, wakati ambapo Yehova alionyesha kwamba upesi angeleta mvua, tamaa ya kutoka moyoni ya Eliya ya kuona ukavu ukiisha ilionekana katika sala zake za kurudia-rudia, zenye juhudi nyingi alipokuwa ‘akisujudu kifudifudi, akiinama uso mpaka magotini.’ (1 Wafalme 18:42) Alimhimiza mhudumu wake kwa kurudia-rudia: “Kwea sasa, utazame upande wa bahari” chochote cha kuonyesha kwamba Yehova amesikia sala yake. (1 Wafalme 18:43) Lazima awe alihisi shangwe iliyoje wakati ambapo mwishowe, kwa kujibu sala yake, “mbingu i[li]toa mvua na nchi ikazaa matunda yayo”!—Yakobo 5:18.

Ikiwa wewe ni mzazi au mzee katika kutaniko la Kikristo, huenda ukalazimika kumenyana na hisia nyingi utoapo rekebisho. Hata hivyo, hisia hizo za kibinadamu zapasa kusawazishwa na usadikisho wa kwamba nidhamu hiyo ni ya lazima nyakati nyingine na kwamba itolewapo kwa upendo, hiyo “hutoa tunda lenye kufanya amani, yaani, uadilifu.” (Waebrania 12:11) Matokeo ya kutii sheria za Yehova sikuzote huwa yenye kutamanika. Sawa na Eliya, twasali kutoka moyoni kwamba zitekelezwe.

Yeremia Alionyesha Moyo Mkuu Kijapokuwa Kivunjamoyo

Kati ya waandikaji wote wa Biblia, huenda Yeremia ndiye aliyeandika mengi zaidi juu ya hisia zake mwenyewe. Akiwa kijana, alisitasita kukubali utume wake. (Yeremia 1:6) Hata hivyo alianza kutangaza neno la Mungu akiwa na moyo mkuu sana, akakabili upinzani mkali kutoka kwa Waisraeli wenzake—kuanzia kwa mfalme hadi kwa mtu wa kawaida. Nyakati nyingine upinzani huo ulimletea hasira na machozi. (Yeremia 9:3; 18:20-23; 20:7-18) Kwenye pindi tofauti alishambuliwa na kikundi cha wafanya-ghasia, akapigwa, akatiwa mkatale, akatiwa gerezani, akatishwa kuuawa, na kuachwa afe katika matope chini ndani ya tangimaji tupu. Nyakati nyingine hata ujumbe wa Yehova uliumiza, kama vile itolewavyo kielezi na maneno yake: “Mtima wangu, mtima wangu! naumwa katika moyo wangu wa ndani.”—Yeremia 4:19.

Hata hivyo, alipenda neno la Yehova, akisema: “Maneno yako yalikuwa ni furaha kwangu, na shangwe ya moyo wangu.” (Yeremia 15:16) Wakati huohuo, mtamauko ulimwongoza kumlilia Yehova hivi: “Yamkini wewe utakuwa kwangu kama kijito kidanganyacho, na kama maji yasiyodumu,” kama yale ya kijito kidogo kikaukacho kwa urahisi. (Yeremia 15:18) Hata hivyo, Yehova alielewa hisia zake zenye kuhitilafiana, akaendelea kumtegemeza hivi kwamba angeweza kutimiza utume wake.—Yeremia 15:20; ona pia 20:7-9.

Je, wewe hukabili mtamauko au upinzani katika kutimiza huduma yako, kama alivyofanya Yeremia? Mtegemee Yehova. Endelea kufuata mwelekezo wake, na Yehova atathawabisha jitihada zako pia.

Yesu Alikuwa na Hisia Kama Zetu

Nabii mkubwa zaidi wa wakati wote alikuwa Mwana wa Mungu mwenyewe, Yesu Kristo. Ingawa alikuwa mwanadamu mkamilifu, hakukandamiza hisia zake. Sisi husoma mara nyingi juu ya hisia zake za ndani, ambazo lazima ziwe zilionekana katika uso wake na katika kuitikia kwake wengine. Mara nyingi Yesu “a[li]sukumwa na sikitiko,” naye alitumia usemi huohuo kufafanua watu katika vielezi vyake.—Marko 1:41; 6:34; Luka 10:33.

Lazima awe alipaaza sauti yake alipowaondolea mbali wauzaji na wanyama kutoka katika hekalu kwa maneno haya: “Ondoleeni mbali vitu hivi kutoka hapa!” (Yohana 2:14-16) Dokezo la Petro, “Uwe mwenye fadhili kwako mwenyewe, Bwana,” lilitokeza jibu lenye nguvu, “Nenda nyuma yangu, Shetani!”—Mathayo 16:22, 23.

Yesu alikuwa na shauku ya kipekee kuelekea watu fulani waliokuwa karibu naye hasa. Mtume Yohana alifafanuliwa kuwa “mwanafunzi ambaye Yesu alikuwa na kawaida ya kumpenda.” (Yohana 21:7, 20) Nasi twasoma hivi: “Basi Yesu alimpenda Martha na dada yake na Lazaro.”—Yohana 11:5.

Yesu angeweza kuwa na hisia zenye kuumizwa. Akihisi jambo la huzuni kubwa juu ya kifo cha Lazaro, “Yesu akatokwa na machozi.” (Yohana 11:32-36) Akifunua maumivu ya moyo yaliyosababishwa na kusalitiwa kwake na Yudasi Iskariote, Yesu alinukuu usemi wenye kuchoma sana kutoka katika Zaburi: “Yeye aliyekuwa na kawaida ya kujilisha mkate wangu ameinua kisigino chake dhidi yangu.”—Yohana 13:18; Zaburi 41:9.

Hata alipokuwa akipata maumivu makali kwenye mti, Yesu alionyesha kina cha hisia yake. Alimkabidhi kwa wororo mama yake kwa “mwanafunzi ambaye yeye alimpenda.” (Yohana 19:26, 27) Alipoona uthibitisho wa toba katika mmojawapo wa watenda-maovu aliyetundikwa kando yake, Yesu alisema hivi kwa huruma: “Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” (Luka 23:43) Twaweza kuhisi kutokea kwa ghafula kwa hisia katika kilio chake: “Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniachilia mbali?” (Mathayo 27:46) Na maneno yake ya kufa yafunua upendo na kutumaini kwake kutoka moyoni: “Baba, ndani ya mikono yako naikabidhi roho yangu.”—Luka 23:46.

Hilo hutupa sisi sote uhakikishio kama nini! “Kwa maana tuna kuhani wa cheo cha juu, si mmoja asiyeweza kushiriki hisia za udhaifu wetu mbalimbali, bali mmoja [Yesu] ambaye amejaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini asiye na dhambi.”—Waebrania 4:15.

Uhakika wa Yehova

Yehova hakughairi kamwe chaguo lake la wasemaji. Alijua uaminifu-mshikamanifu wao kwake, naye aliachilia kwa huruma udhaifu mbalimbali wa wale ambao hawakuwa wakamilifu. Hata hivyo alitarajia wote watimize utume wao. Kwa msaada wake waliweza kufanya hivyo.

Acheni tuonyeshe kwa subira uhakika katika ndugu na dada zetu waaminifu-washikamanifu. Watakuwa wasio wakamilifu sikuzote katika mfumo huu wa mambo, kama vile sisi tutakavyoendelea kuwa. Hata hivyo, hatupaswi kuwahukumu kamwe ndugu zetu kuwa hawastahili upendo na uangalifu. Paulo aliandika hivi: “Ingawa hivyo, sisi tulio na nguvu twapaswa kuchukua udhaifu wa wale wasio na nguvu, na si kuwa tukijipendeza wenyewe.”—Waroma 15:1; Wakolosai 3:13, 14.

Manabii wa Yehova walipatwa na hisia-moyo zote ambazo sisi hupata. Hata hivyo, walimtumaini Yehova, na Yehova aliwategemeza. Zaidi ya hilo, Yehova aliwapa sababu za shangwe—dhamiri njema, kung’amua kibali chake, waandamani waaminifu-washikamanifu waliowategemeza, na uhakikishio wa wakati ujao wenye furaha. (Waebrania 12:1-3) Acheni tushikamane na Yehova pia tukiwa na uhakika kamili huku tukiiga imani ya manabii wa zamani, watu ‘wenye hisia kama zetu.’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki