Kutii Kwa Ushikamanifu Utaratibu wa Kitheokrasi
“Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, Ndugu wakae pamoja, kwa umoja. Kama umande wa Hermoni ushukao milimani pa Sayuni.”—Zaburi 133:1, 3.
1. Neno la Yehova linaelezaje jamaa yake ya kidunia ya watumishi waliojiweka wakf?
MANENO hayo yanaeleza vizuri sana jamaa ya wale ambao wamejiweka wakf kwa Mzazi wao mmoja, Yehova Mungu! Na yeye kwa hakika anaisimamia hii jamaa yake ya duniani pote katika njia nzuri sana. Kwa upendo yeye anawapa mahitaji yao yote.—Zaburi 145:16.
2. Kutii utaratibu wa kitheokrasi kunamaanisha nini?
2 Lakini, Yehova anatumia imara kusisitiza kwamba watoto wake wote wenye kujitoa wawe na amani na umoja. (1 Wakorintho 1:10) Na matokeo hayo mazuri yanakuja kwa sababu ya watumishi wa Mungu kutii kwa ushikamanifu utaratibu wa kitheokrasi. Maana yake hiyo nini? Kwa kuwa utawala wa Mungu unaitwa theokrasi (utawala wa Mungu), kutii utaratibu wa kitheokrasi kunamaanisha kutii sheria, amri na kanuni zinazotoka kwa Mungu.—Isaya 33:22.
3. Yesu alielezaje maoni yake juu ya kutii utawala wa Mungu?
3 Mfano bora zaidi wa kutii kwa ushikamanifu utaratibu wa kitheokrasi ni ule wa Yesu Kristo. Huko mbinguni yeye alikuwa “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.” (Wakolosai 1:15) “Yehova mwenyewe alinitokeza mimi niwe mwanzo wa njia yake, wa mapema zaidi kati ya matendo yake ya kale. Tangu wakati usiojulikana niliwekwa, tangu mwanzo tangu nyakati za mapema zaidi ya dunia. . . . Nikawa kando ya [Mungu] nikiwa mfanyi kazi stadi, nami nikawa aliyependwa kipekee naye siku baada ya siku, nikiwa nafurahi mbele yake wakati wote.” (Mithali 8:22, 23, 30, NW) Furaha yake katika kutii utawala wa Mungu ilionekana wazi alipokuwa duniani, kwa maana Yesu alieleza hivi: “Mimi sikushuka kutoka mbinguni ili niyafanye mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenipeleka.” (Yohana 6:38) Ikiwa sehemu ya kufanya mapenzi ya Mungu, yeye alikuwa mwangalifu sana afundishe mawazo ya Mungu, wala si yake mwenyewe. “Mafunzo yangu si yangu mimi, ila ni yake yeye aliyenipeleka,” Yesu alisema. (Yohana 7:16) Hiyo ilikuwa nia nzuri kama nini ya kuigwa na watumishi wote wa Mungu!
4. Eleza namna ulivyo mpango wa kitheokrasi wakati wetu?
4 Kwa sababu ya kutii kwa ushikamanifu utawala wa kitheokrasi, hata kufikia kifo, Yesu alithawabishwa kwa kupewa uzima usio na mwisho wa kimbingu. Pamoja na hayo, yeye alipewa “mamlaka yote mbinguni na duniani.” (Mathayo 28:18) Naye, alikabidhi Wakristo watiwa mafuta waaminifu “vitu vyake vyote” duniani. Hawa Yesu aliwaita “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mathayo 24:45-47) Thawabu yao ni kushiriki siku moja katika utawala wa kimbingu pamoja na Kristo wakiwa “makuhani” na “wafalme” katika ufalme wake. (Ufunuo 14:1, 4; 20:6) Leo, mabaki ya huyu “mtumwa mwaminifu” yangali hai duniani. Kazi zao ni kutia kupokea na kupokeza watumishi wote wa Yehova wa kidunia chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. Cheo chao ni sawa na kile cha Paulo na wafanyi kazi wenzake wakati mtume huyo aliposema juu ya kweli nzuri sana anazowapa Mungu watu wake. “Mungu ametufunulia sisi kwa [roho].” (1 Wakorintho 2:9,10) Vilevile wao wanaongoza katika utumishi wa kuuhubiri Ufalme ambao lazima utimizwe “katika dunia yote inayokaliwa na watu” kabla ya mwisho wa huu mfumo wa mambo uliohukumiwa maangamizi.—Mathayo 24:14, NW.
Matokeo ya Mwenendo Mbaya
5, 6. (a) Ni matokeo gani yaliyompata Hawa na Adamu kwa ajili ya kutaka kujitegemea pasipo Yehova? (b) Yehova anashughulikaje na ‘mbwa-mwitu waliovaa mavazi ya kondoo’?
5 Basi inahitajiwa sana kila mmoja aliye katika jamaa ya Mungu awe ni mmoja wa mabaki waliotiwa mafuta au mmoja wa “mkutano mkubwa,” aitii kwa ushikamanifu mipango hii ya yule Theokrati Mkuu na Mwanaye-Mfalme, Kristo Yesu, kama anavyopokezwa “mtumwa mwaminifu” duniani! Kwa kuwa utaratibu wa kitheokrasi unaanzia kwa Yehova mwenyewe na kurudi chini, hatungependa kamwe kumwiga Shetani Ibilisi kwa kutaka kujitegemea bila utawala wa kitheokrasi. Kumbuka matokeo yenye kusikitisha yaliyompata Hawa aliposikiliza kusihi kwa udanganyifu kwa Shetani kwamba asitii utaratibu wa kitheokrasi. Kwa maneno mengine, Shetani alimwambia hivi: ‘Jitegemee pasipo Mungu. Fikiri yako mwenyewe. Jiamulie mwenyewe yaliyo mema na yaliyo mabaya. Kisha utakuwa kama Mungu. Hakika wewe hutakufa.’ (Mwanzo 3:1-5) Huenda maneno hayo yakawa yalisikika kuwa yenye kuvutia, lakini ulikuwa ni uongo. (Yohana 8:44) Mume wake alipojiunga naye katika kuacha kutii utaratibu wa kitheokrasi, walifukuzwa kutoka bustani ya Edeni na kutoka jamaa ya Mungu ya washikamanifu. Muda si muda, kama Yehova alivyokuwa ameonya, hukumu ya kifo ilitekelezwa juu ya wote wawili.—Mwanzo 2:17.
6 Vivyo hivyo leo, wo wote kati ya watu wa Yehova wanaojiingiza katika mafundisho ya kujitegemea na yaliyo tofauti, wanamwiga si Mungu, bali Shetani Ibilisi. Hata hivyo, Yehova huona yanayotokea kati ya jamaa yake na anatoza hesabu. (Mithali 15:3) Yeye hatawaendekeza watu wenye mfano wa mbwa-mwitu ambao wangependa kuwanyafua (kuwameza) watu wake wenye mfano wa kondoo, bali yeye kwa wakati unaofaa huchukua hatua ya waziwazi. (Mathayo 7:15-23) Kama vile baba mwenye upendo, yeye hulinda hali njema ya kiroho ya jamaa yake.—Ezekieli 34:11-16.
7. (a) Haruni na Miriamu walikosa kuthamini jambo gani? (b) Matokeo yakawa nini?
7 Mifano mingine ya Biblia vilevile inakazia hatari ya kutokutii kwa ushikamanifu utaratibu wa kitheokrasi. Kwa mfano, Miriamu na Haruni walimchukua Musa vivi hivi tu kwa sababu ya uhusiano wao naye wa kijamaa hata wakafikia hatua ya kukipinga cheo chake katika kundi la kale la Mungu la Israeli. (Hesabu 12:1, 2) Walishindwa kuuthamini uhakika wa kwamba Yehova Mungu mwenyewe ndiye aliyekuwa amemgawia Musa mamlaka ya pekee, jambo hilo likiwa limethibitishwa kwa miujiza mingi. Yehova aliwakumbusha hivi: “Mtumishi wangu, Musa . . . [amekabidhiwa] nyumba yangu yote; kwake [nimenena] mdomo kwa mdomo. . . . Basi mbona ninyi hamkuogopa kumnenea mtumishi wangu, huyu Musa?” Kisha, “hasira za [Yehova] zikawaka juu yao.” Haruni alikemewa vikali sana, naye Miriamu akapigwa kwa ukoma na kufukuzwa nje ya kambi ya Israeli kwa siku saba.—Hesabu 12:7-15.
8. Kisa cha Mfalme Sauli kinaonyesha nini?
8 Halafu kuna Mfalme Sauli wa Israeli ya kale aliyekataa kumngojea Yehova. Badala yake, akatoa dhabihu kwa kimbele-mbele hata ingawa yeye hakuwa kuhani. Kisababu chake kisichofaa kilikuwa kusema kwamba alikuwa katika hatari ya kupoteza jeshi lake lote kwa kuachwa bila msaada. Hata hivyo, hilo lilikuwa jeshi la nani? La Sauli au la Yehova? Nabii Samweli alimwambia hivi: “Umefanya upumbavu; hukuishika amri ya [Yehova], Mungu wako . . . Lakini sasa ufalme wako hautadumu.” (1 Samweli 13:13,14) Uufalme ulitwaliwa kutoka kwa Sauli na kupewa ‘mtu mwenye kuupendeza moyo wa Yehova.’ Kwa hiyo, kwa sababu ya kukosa kutii Sauli alipata hasara kubwa na kwa sababu pia ya kukosa toba ya kweli alipojulishwa jambo hilo. Jambo hilo linaonyesha kwamba Yehova huona utendaji wa kimbelembele, wa kujitegemea, usio wa kitheokrasi kati ya watu wake.—Mithali 11:2.
9. Kwa sababu gani Mfalme Uzia aliondoshwa mbali na watu?
9 Kisa cha Mfalme Uzia wa Yuda kinafanana na hicho. Ingawa yeye alikuwa ndiye mfalme aliyetiwa mafuta atawale watu wa Yehova, hakuwa na ruhusa ya kutumika katika cheo cho chote cha kikuhani. Lakini alijikaza afanye kazi ya makuhani. Makuhani walipinga kwa nguvu na kusema hivi: “Si haki yako, Uzia kumfukizia [Yehova] uvumba, ila ni haki ya makuhani wana wa Haruni, waliofanywa wakfu, ili wafukize uvumba; toka katika patakatifu; kwa kuwa umekosa.” Kisha, akionyesha kukosa kwake kutubu, Uzia aliwaghadhibikia makuhani, akaongezea dhambi yake ya kimbelembele. “Alipowaghadhibikia makuhani, ukamtokea ukoma katika paji la uso wake . . . kwa sababu [Yehova alikuwa] amempiga.” Akaendelea kuwa mkoma mpaka siku yake ya kufa, aliondoshwa mbali na watu, “alitengwa na nyumba ya [Yehova].”—2 Mambo ya Nyakati 26:16-21.
10. Paulo alielezaje juu ya wale waliopinga kuwekwa kwake na Yesu?
10 Mtume Paulo alizungumza juu ya watu fulani waliopinga kuwekwa kwake kwa pekee na Kichwa cha kundi la Kikristo, Yesu Kristo. (2 Wakorintho 11:12) Lakini Paulo alisema kwamba watu hao walikuwa “mitume wa uongo, watendao kazi kwa hila, wanaojigeuza wawe mfano wa mitume wa Kristo. Wala si ajabu. Maana Shetani mwenyewe hujigeuza awe mfano wa malaika wa nuru.” (2 Wakorintho 11:13, 14, NW) Watu hao walikuwa na makusudi yao wenyewe ya kichoyo ya kuendesha. Paulo alikuwa ameonya juu ya mtu wa namna hiyo akisema hivi: “Katika ninyi wenyewe watainuka watu, wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao. Kwa hiyo kesheni.” (Matendo 20:30, 31) Paulo aliwasihi sana kina ndugu, kutia hao wenye kujifanya kuwa mitume, wasiruhusu ugomvi na mashindano yaharibu umoja na hali ya kuzaa ya kundi la Kikristo. Ikiwa wo wote walikosa kutii shauri hilo lenye kuongozwa kwa roho, basi walikuwa wakisonga kwenye msiba kwa hakika.—Wagalatia 1:7-9.
11. Yehova analindaje upatano wa jamaa yake ya kidunia?
11 Mwandikaji wa Biblia mwenye kuongozwa na Mungu, Yohana, alisema hivi: “Kila apitaye cheo, wala asidumu katika mafundisho ya Kristo, yeye hana Mungu. . . . Mtu akija kwenu, naye haleti mafundisho hayo, msimkaribishe nyumbani mwenu, wala msimpe salamu. Maana yeye ampaye salamu azishiriki kazi zake mbovu.” (2 Yohana 9-11) Ndiyo, Yehova atalinda roho njema na upatano wa jamaa yake.
Kujihadhari Leo
12. Yehova anawakusanya wale wote wanaompenda kwenye nini?
12 Katika hizi “siku za mwisho” Yehova anawakusanya wale wanaompenda na kuwaingiza katika tengenezo moja lenye umoja na upatano. Watu wa mataifa yote wanatii mwito huu, “Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova], nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.” (Isaya 2:2, 3) Angalia kwamba Yehova anawafundisha watu katika njia zake ili watembee katika mapito yake, wala si katika njia zao wenyewe wala mapito yao wenyewe.—Yeremia 10:23, 24.
13. (a) Kwa sababu gani tunapaswa hasa kujihadhari sasa? (b) Tunahitaji nini ili kushinda makusudi ya Shetani?
13 Hata hivyo, sasa Shetani ni “mwenye ghadhabu nyingi.” Yeye anajua kwamba ana “wakati mchache tu” kabla hajaondoshwa. Kwa hiyo “kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze.” (Ufunuo 12:12; 1 Petro 5:8) Kwa hiyo, tunahitaji kujihadhari na jitihada zo zote za mungu wa ulimwengu huu, Shetani Ibilisi, za kutokeza mashindano na mgawanyiko kati ya washiriki wa jamaa ya Yehova. “Basi angalieni sana jinsi mnavyoenenda; si kama watu wasio na hekima, bali kama watu wenye hekima, mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu. Kwa sababu hiyo msiwe wajinga, bali mfahamu ni nini yaliyo mapenzi ya [Yehova].” (Waefeso 5:15-17) Kwa kutumia kwa faida mipango ya Yehova kwa ajili ya hali nzuri yetu ya kiroho, tutajengwa, tusafishwe, tuwe na silaha za kutosha. Kwa njia hiyo tutaweza kujikinga na mipango miovu ya hila ya Shetani na kulishinda kusudi lake.—Waefeso 6:10-13.
14. Kwa sababu gani kuna hatari kubwa ya kujifikiria sana sisi wenyewe zaidi ya tunavyopaswa?
14 Nia ya akilini ambayo lazima tuwe macho kujilinda nayo, ni ile ya kujifikiria sisi ni bora sana kuliko itupasavyo kufikiri. (Warumi 12:3) Nia hiyo inaweza kumfanya Mkristo afikiri kwamba amepewa na Mungu agizo la pekee bila agizo hilo kuipitia ile njia ambayo Yehova huitumia kutolea jamaa yake kweli na uongozi. Kwa sababu hiyo, kufanya hivyo kungekuwa ni kujitenga au kujiweka katika uhusiano wa pekee pamoja na Yehova ambao ndugu au dada wale wengine katika jamaa hiyo hawana. Lakini kujitenga kwa namna hiyo kunaweza kuongoza kwenye msiba tu: “Ajitengaye na wengine hutafuta matakwa yake mwenyewe; hushindana na kila shauri jema.”—Mithali 18:1.
Kumngojea Yehova
15. (a) Je! ni jambo linalofaa kutolea mawaidha jamii ya “mtumwa” ya Yehova? (b) Eleza jinsi utii wa kitheokrasi ulivyoonyeshwa katika karne ya kwanza.
15 Nyakati nyingine, watu fulani wanajisikia wakiwa na wajibu wa kuionyesha jamii ya “mtumwa” mafundisho fulani ya kitengenezo ambayo wao wanaona yanapasa kurekebishwa upya. Bila shaka, mawaidha ya kutaka maendeleo yafanywe yanafaa, sawa na maulizo ya kutaka maelezo zaidi. Mfano wa hilo ni wakati Paulo, Barnaba na wengine walipopelekwa “Yerusalemu kwa mitume na wazee” kuhusu tohara. Wakati wazee hao katika Yerusalemu walipoamua jambo hilo, chini ya uongozi wa roho takatifu, ndipo walipowapeleka kina ndugu katika miji mbalimbali ili kuwapa “zile amri zilizoamriwa na mitume na wazee walioko Yerusalemu, ili wazishike.” Kutii kwa ushikamanifu amri hizo kulileta baraka ya Yehova. Kwa hiyo, “[makundi] yakatiwa nguvu katika ile Imani, hesabu yao ikaongezeka kila siku.”—Matendo 15:1-16:5.
16. (a) Ni roho gani inayofaa kuonyeshwa baada ya kutoa mawaidha? (b) Paulo anashaurije juu ya kushughulika na wale wanaoonyesha roho isiyofaa?
16 Baada ya kutoa mawaidha roho inayofaa ni kuridhika kuacha jambo hilo lifikiriwe kwa njia ya sala na ndugu waliokomaa wanaoongoza kazi katika tengenezo la Yehova. Lakini ikiwa wale wanaotoa mawaidha hayo hawatosheki na wanaendelea kubishania jambo hilo katika makundi wakiwa na kusudi la kuungwa mkono na wengine, basi iweje? Jambo hilo lingetokeza migawanyiko, lingeweza kuikengeusha imani ya wengine. Kwa hiyo Paulo anashauri hivi: “Waangalieni wale wafanyao fitina [wanaotokeza migawanyiko] na mambo ya kukwaza kinyume cha mafundisho mliyojifunza; mkajiepushe nao.” Vilevile Paulo alimshauri Tito ‘kuwakaripia wale wanaopinga,’ na kuongeza hivi: “Ni lazima kufumba vinywa vya hawa, kwa kuwa watu hawa hawa wanaendelea kukengeusha jamaa nzima kwa kufundisha mambo wasiyopaswa . . . Kwa sababu iyo hiyo uwe ukiwakaripia kwa ukali.”—Warumi 16:17, 18; Tito 1:9-13, NW.
17. Sisi leo tunawezaje kuiga nia njema ya Daudi?
17 Neno la Mungu linasema hivi: “Ujuzi [maarifa] huleta majivuno, bali upendo hujenga.” (1 Wakorintho 8:1) Kwa hiyo, ni vema kama nini kuendelea kuwa wenye shughuli katika kazi kuu ya kutangaza ufalme mzuri ajabu wa Mungu, kusema mambo yenye kujenga, kutia nguvu imani ya wengine na yetu, huku tukingojea kwa subira Yehova atimize mapenzi yake kupitia njia yake aliyoiweka’ (Warumi 14:19; Wafilipi 4:8, 9) Mwigeni Daudi aliposema hivi: “Kwa maana nilikungojea wewe, Ee Yehova; nawe ukanijibu, Ee Yehova Mungu wangu.” (Zaburi 38:15, NW) Sikuzote kumbuka jambo la maana la kufikiria kama alivyosema Paulo, yaani, “kwamba nyote mnene mamoja; wala pasiwe kwenu faraka, bali mhitimu katika nia moja na shauri moja.” (1 Wakorintho 1:10) Kwa sababu kanuni hiyo inatumiwa katika jamaa ya Yehova ulimwenguni pote tunaona matokeo mazuri ajabu. Hakika, “jinsi ilivyo vema, na kupendeza, ndugu wakae pamoja, kwa umoja”!—Zaburi 133:1.
Je! Unaweza Kujibu Maulizo Haya:
◻ Yesu aliwekaje mfano bora wa kutii utaratibu wa kitheokrasi?
◻ Matokeo ya kukosa kutii utaratibu wa kitheokrasi yanaweza kuwa nini?
◻ Kwa sababu gani tunapaswa kujihadhari hasa na Shetani leo?
◻ Tunapotoa mawaidha, tunapaswa kuwa na nia gani?
[Picha katika ukurasa wa 14]
Kwa sababu ya kutokutii utaratibu wa kitheokrasi, Mfalme Uzia alipigwa kwa ukoma