Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 1/1 kur. 4-6
  • ‘Wale Tisa Wako Wapi?’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Wale Tisa Wako Wapi?’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuwaonyesha Kuthamini Washiriki wa Jamaa
  • Nje ya Jamaa
  • Kwa Nini Uonyeshe Shukrani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Kwa Nini Uonyeshe Uthamini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
  • Kumwonyesha Mungu Kuthamini Kwetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Kuthamini Kumeenda Wapi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 1/1 kur. 4-6

‘Wale Tisa Wako Wapi?’

TOFAUTI kati ya watu wanaoonyesha kuthamini na wale wanaopuza kufanya hivyo ilionyeshwa vizuri katika masimulizi ya Biblia ya wakoma kumi walioponywa na Yesu Kristo. Wakoma hao, waliokatazwa na Torati kumkaribia ye yote, walimfikia Yesu alipokuwa akiingia katika kijiji fulani. Walisihi awarehemu. Yesu aliona kwamba walikuwa wakoma akawaambia: “Enendeni, mkajionyeshe kwa makuhani.” Halafu jambo gani likatokea? Maandishi yaliyoongozwa kwa roho yanaongeza hivi:

“Ikawa walipokuwa wakienda walitakasika. Na mmoja wao alipoona kwamba amepona, alirudi, huku akimtukuza Mungu kwa sauti kuu; akaanguka kifudifudi miguuni pake, akamshukuru; naye alikuwa Msamaria. Yesu akajibu, akanena, Hawakutakaswa wote kumi? Wale kenda wa wapi? Je! hawakuonekana waliorudi kumpa Mungu utukufu ila mgeni huyu [wa taifa jingine, NW]?”​—Luka 17:11-19.

‘Inasikitisha sana!’ huenda ukatamka. ‘Wote kumi waliponywa bali ni mmoja tu aliyeonyesha kuthamini kwake.’ Hakika, sote twapaswa kuweka moyoni somo lililotolewa na maelezo na ulizo la Yesu. ‘Wale tisa wako wapi?’ Ndiyo, na kisa hicho chapasa kutuchochea tuonyeshe kuthamini.

Kuwaonyesha Kuthamini Washiriki wa Jamaa

Kuna nafasi nyingi za kuwaonyesha wengine kuthamini, kutia rafiki na washiriki wa jamaa. Iko hivyo hata katika mambo madogo-madogo: kwa ajili ya zawadi ambayo haikutazamiwa, kwa kutembelewa na rafiki, kwa ajili ya chakula kitamu, au kwa ajili ya nguo zetu kuoshwa na kupigwa pasi.

Watoto mnaweza kuwaonyesha wazazi wenu kuthamini. Namna gani? Kwa kufanya kazi za nyumbani mara moja bila kunung’unika, kwa kuweka chumba chenu safi na nguo zenu nadhifu. Mnaweza kuonyesha kuthamini kwa ajili ya elimu mnayopewa kwa kujitahidi sana darasani na wakati wa kufanya masomo ya kufanyiwa nyumbani. Katika nchi moja inakadiriwa kwamba inagharimu kufikia dola 54,000 (za Marekani) kumlea mtoto afikie miaka kumi na minane (18). Ni lini mara ya mwisho ulipowashukuru wazazi wako kwa ajili ya yote ambayo wamekufanyia?

Wazazi, je, mnaonyesha kuthamini kwa ajili ya mambo yanayofanywa na watoto wenu? Ni kweli huenda wasifanye jambo vizuri kama unavyoweza kulifanya. Walakini neno la kuthamini kwa ajili ya jitihada yao litawafurahisha. Na litawatia moyo watoto wako wafanye vizuri hata zaidi wakati ujao.

Waume, je, mnakumbuka usemi ‘kazi ya mwanamke haimaliziki kamwe’? Basi, je, mnawasifu wake zenu ili kazi yao isiwe ya kuchosha? Biblia inasema hivi juu ya “mke mwema”: “Wanawe huondoka na kumwita heri; mumewe naye humsifu, na kusema, Binti za watu wengi wamefanya mema, lakini wewe umewapita wote.” (Mithali 31:10, 28, 29) Mume anaweza kumwonyesha mke wake kuthamini katika njia nyingi, kama kwa kwenda nje jioni pamoja au kwa wonyesho wa upendo.

Wake vilevile wana nafasi nyingi za kuonyesha kuthamini. Ili atoe vitu vya lazima maishani, wakati mwingi mume lazima afanye kazi pamoja na watu wenye hali mbalimbali za hasira na tabia, na jambo hilo laweza kuwa lenye kushusha moyo sana. Kwa hiyo, anaporudi nyumbani, ni jambo la kumchangamsha moyo kama nini kukaribishwa kwa upendo au kuambiwa na mke maneno machache ya kuthamini kwa ajili ya yale anayofanyia jamaa! Ndiyo, na mwanamume anaweza kuwa mwenye shukrani kama nini kwa ajili ya kuwa na mke mwema​—na mke mwenye kuthamini! Biblia inasema hivi: “Kima chake chapita kima cha marijani. Moyo wa mumewe humwamini, wala hatakosa kupata mapato. Humtenda mema sikuzote wala si mabaya, siku zote za maisha yake.”​—Mithali 31:10-12.

Wazazi wanaozeeka vilevile wanahusika. Wametufanyia mengi wakati wa miaka mingi iliyokwisha. Watoto ni “urithi wa [Yehova],” walakini kuwalea ni daraka kubwa. (Zaburi 127:3) Kwa kweli, kufanya hivyo kwaweza kuitwa shughuli ya kuzoeza ya miaka ishirini (20). Hata hivyo wengi hawawaonyeshi wazazi wao shukrani kwa ajili ya miaka yote hiyo ya utumishi na kujinyima. Mara nyingi sana, wazazi wazee-wazee wanasukumizwa kwenye makao ya wazee. Bila shaka, katika visa vingine huenda uangalizi wa ustadi katika mahali huko ukawa lazima. Lakini hata wageni wawe wamezoezwa vizuri namna gani, uangalizi wao peke yake kwa walio wazee-wazee haulingani kamwe na wakati wanapokuwa na jamaa zao wenyewe. Kwa hiyo, inapokuwa lazima na inapowezekana, ni njia bora kama nini kuwaonyesha wazazi wetu wanaozeeka kuthamini na kuwakaribisha waishi pamoja nasi! Mtume Paulo alilisema jambo hilo hivi: “Kumbuka ikiwa mjane ana watoto au wajukuu kwanza ni daraka lao kuonyesha ukweli wa dini yao katika nyumba zao wenyewe kwa kuwalipa wazazi wao kwa ajili ya yale ambayo wamefanyiwa, na Mungu anaukubali utumishi huo mara moja.” (1 Timotheo 5:3, 4, Phillips) Kama ilivyo, wazazi wanaozeeka na babu na nyanya wanapaswa kushirikiana na kuonyesha kuthamini yale wanayofanyiwa.

Nje ya Jamaa

Washiriki wa jamaa wanapotuonyesha kuthamini jambo tulilosema au tulilofanya, jambo hilo linachangamsha moyo wetu kama nini! Vivyo hivyo, inachangamsha mioyo ya wale walio nje ya jamaa yetu tunapoonyesha kuthamini na kwa ajili ya yale wanayofanya au kusema. Pindi za kufanya hivyo ni nyingi sana hata kwamba hatuwezi kutaja zote.

Pengine umeanza karibuni kuongeza ufahamu wako wa Biblia kupitia funzo la kibinafsi na ushirika wa Mashahidi wa Yehova. Je! si inathawabisha kiroho kupata maarifa ya Neno la Mungu? Hakika unathamini hilo. Na namna gani washirika Wakristo ulio nao sasa? Maandiko yanasema kwamba Yehova ‘angetikisa mataifa yote’ na kwamba “vitu vinavyotamaniwa” vya mataifa yote vingekuja kwenye nyumba ya ibada yake. Kwa wazi hivyo “vitu vinavyotamaniwa” ni watu wanaoumiminikia “mlima wa nyumba ya [Yehova],” na sasa wanamwabudu “katika roho na kweli.” (Isaya 2:2-4; Hagai 2:7; Yohana 4:23, 24) Ni wenye upendo, wanyofu, wenye adili na waliojitoa kwa Mungu na kanuni zake za uadilifu. Na ebu wazia tu! Katika ulimwengu wenye kujawa na tabia kama ukosefu wa upendo, ukosefu wa unyofu na kutokushukuru, wewe umependelewa kuwa na washirika wazuri wenye sifa ya kimungu. (2 Timotheo 3:1-5) Je! hatupaswi kuthamini sana kwa ajili ya ushirika wao? Hakika, ndiyo.

Kwa upande mwingine, pengine tumekuwa tukifuata njia ya maisha ya Kikristo kwa miaka mingi. Ikiwa ndivyo, fikiria juu ya wale ambao wamekuwa Wakristo waaminifu wenzetu kwa muda fulani. Hakika ingefaa kuwathamini kwa ajili ya fadhili zao nyingi kwa neno na kwa tendo. Je! tumekwisha kuwa wageni katika nyumba yao? Au, je, tumefurahia chakula pamoja nao? Basi, licha ya kuthamini kwa maneno, je, haingefaa kuandika barua fupi au kutuma kadi ya kuthamini?

Bila shaka, kila mmoja wetu anaweza kuona njia nyingi za kupata furaha kubwa zaidi yeye mwenyewe na wengine pia kwa kuonyesha kuthamini kwetu kwa moyo mweupe. Basi na tuwe kama yule mkoma mmoja aliyeponywa ambaye alikuwa mwenye roho ya kuthamini kweli kweli. Na tusiwe wasio na shukrani, kama wale wakoma wengine walioponywa ambao juu yao Yesu aliuliza hivi: ‘Wale tisa wako wapi?’

Ni wazi twapaswa kuwaonyesha wanadamu wenzetu kuthamini. Lakini namna gani juu ya Yule aliyefanya vitu vyote? (Ufunuo 4:11) Baadhi ya sababu tunazopaswa kumthamini ni sababu gani? Na twawezaje kuonyesha shukrani zetu kwa Yehova Mungu?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki