Kuzaliwa kwa Taifa la Kifalme katika Nchi Iliyozaliwa Upya
“Je! nchi yaweza kuzaliwa siku moja? Taifa laweza kuzaliwa mara? Maana Sayuni, mara alipoona utungu, alizaa watoto wake.”—Isaya 66:8.
1. Katika Julai 26, 1931, ni tendo gani lililochukullwa na Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote kwenye kusanyiko lao katika Columbus, Ohio, na ni tendo gani kama hilo lililochukuliwa baadaye ulimwenguni pote?
ZAIDI ya nusu karne iliyopita—tukitaja tarehe yenyewe ni siku ya Jumapili alasiri, Julai 26, 1931—kikundi fulani cha watu kilitokea katika tamasha ya ulimwengu, kikitetea jina fulani. Katika siku hiyo isiyosahaulika maelfu mengi ya Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote, waliokusanyika pamoja katika kusanyiko kuu la Columbus, Ohio, Marekani, kwa umoja walipitisha azimio ambalo kupitia hilo walichagua kuitwa kuanza wakati huo kuendelea kwa jina lenye msingi wa Biblia “mashahidi wa Yehova.” (Isaya 43:10-12, NW) Baada ya muda mfupi makundi yote ya Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote katika dunia nzima walipitisha azimio hilo na kulichukua jina hilo la pekee. Jina hilo jipya limeendelea kuwapo!
2. (a) Wachukuaji wa jina hilo lenye msingi wa Biblia wamevumilia nini tangu wakati huo? (b) Wanapata maneno gani ya kuwapa uhakikisho katika Isaya 66:5?
2 Kwa sababu ya jina hilo la heshima mashahidi hao wa Mungu Aliye Juu Zaidi wamepatwa na chuki ya ulimwengu, hata ile ya Jumuiya ya Wakristo, ambayo washiriki wayo wanadai kuwa ni ndugu za kidini wa wale wote wanaodai kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo. Chuki hiyo imejitokeza sana na kujionyesha kwa namna ya mateso ya jeuri, na kifo kikawapata wengi. Ili kutia moyo wale wanaolichukua jina hilo ambao wanaishi kulingana na heshima ya jina hilo, yaliwajia maneno haya yenye kutoa uhakika ya muda wa miaka 2,500 iliyopita yaliyohifadhiwa kwa ajili yetu na mmoja wa manabii wenye kutokeza sana wa Biblia: “Sikieni neno la Yehova, enyi watu mnaotetemeshwa na neno lake: “Ndugu zenu wanaowachukia ninyi, wanaowazuia msiingie kwa sababu ya jina langu, walisema, ‘Yehova na atukuzwe!’ Lazima yeye pia atokee kwa shangwe kwa upande wenu, na wao ndio watakaoaibishwa.’”—Isaya 66:5, NW.
3. Mashahidi wa Yehova wanaonyeshaje kwamba wanatetemeshwa na Neno lake, na, licha ya kulisikia, wanafanya nini?
3 Mashahidi wa Yehova wa leo ndio ‘watetemeshwao na neno lake.’ Wao wanaogopa kutenda kinyume cha Neno lake lililoandikwa. Hiyo ndiyo sababu wakati wote wanajifunza Maandiko yaliyoongozwa kwa roho. Wanatambua Mbuni wa Biblia kuwa Mungu na Baba ya Bwana wao na Mwokozi Yesu Kristo. Wanavikubali vitabu vyote 39 vya Maandiko ya Kiebrania na vitabu vyote 27 vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kuwa neno la Yehova, ambalo wanapaswa kulisikia na kutenda kulingana nalo pia.
4. (a) Ni nini sababu ya msingi ya Jumuiya ya Wakristo kuwachukia ndugu zao na kuwazuia wasiingie? (b) Walisema kusudi lao la kufanya hivyo ni nini?
4 Hasa ni kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wanachukiwa na Jumuiya ya Wakristo, na watu wanaodai kuwa katika udugu wa Yesu Kristo? Kwa sababu gani Jumuiya ya Wakristo inawazuia wasiingie katika vyeo vya wale wanaotambuliwa kuwa Wakristo, na haitaki kuwa na uhusiano nao kwa sababu haina jambo linalofanana na wao? Yehova mwenyewe anatoa sababu ya hilo, kwa kusema: “Kwa sababu ya jina langu.” Na bado wale wanaowachukia na kuwazuia wasiingie wanatoa sababu ya juu zaidi ya kufanya hivyo kwa kutamka hivi: “Yehova na atukuzwe!” Au, kwa kutumia tafsiri za Biblia zinazoepuka kulitumia jina hilo la kimungu, wanatangaza hivi: “Bwana na atukuzwe.” Hata hivyo, Bwana Mungu haoni kuchukia kwao na kujitenga kwao na ushirika wa mashahidi wake kuwa jambo la kumtukuza.
5. (a) Yehova anapojitokeza kwa kujionyesha, ni nani wanaofurahishwa? (b) Kwa wengine kuaibishwa kunamaanisha nini kwao?
5 Atakapojitokeza kwa kujionyesha ili awape wengine kibali yake na kuwakataa wengine, ni nani wanaofanywa wafurahi wakati huo wa kujitokeza? Ni nani wanaofanywa waaibike? Kwa wale wanaochukiwa na kuwazuiwa wasiingie kwa sababu ya jina lake, Yehova anasema hivi: “Lazima yeye pia atokee kwa shangwe kwa upande wenu, na wao ndio watakaoaibishwa.” Hiyo ilimaanisha taabu kubwa sana kwa wale wenye kujiingiza katika kuwachukia na kuwazuia wasiingie. Taabu hiyo ya kale yenye kuwapata ilitangulia kufananisha taabu kubwa zaidi ya zote ambayo karibuni itakuja juu ya wachukiaji na wenye kuzuia Mashahidi wa Yehova wasiingie katika huu “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Katika maneno yanayofuata nabii Isaya anaendelea kutaja hilo, akisema hivi: “[Kuna] sauti ya fujo itokayo mjini! Sauti itokayo hekaluni! Sauti ya [Yehova] awalipaye adui zake adhabu!”—Isaya 66:6.
6. Ni mji gani ambao kutoka humo “sauti ya fujo” ilisikika, na sababu ya sauti hiyo ilikuwa nini?
6 Mji huo usiotajwa kwa jina ambao juu yake ingekuja “sauti ya fujo” bila shaka ni Yerusalemu, kwa maana huko ndiko lilikokuwa hekalu la ibada ya Yehova. Wazo linalotolewa hapo ni kwamba Yehova anakuja kwenye hekalu lake afanye ukaguzi, naye hapendezwi na jinsi anavyokuta ibada yake ikiendeshwa. Ibada hiyo ni ya tu, desturi, ya kinafiki. Jambo hilo lilililetea jina lake takatifu suto. Jambo ambalo lingeonyesha kukataa kwa Yehova hilo lingekuwa ni “fujo” yenye kutokezwa na shambulio la Wababiloni wenye kuushinda ulimwengu wote, ambao Yehova angetumia wawe vyombo vyake katika ‘kulipa adui zake adhabu,’ wazoefu wa ibada ya kinafiki ambao walishushia heshima hekalu lake. Hao walikuwa maadui wa Yehova kwa sababu walikuwa wachukiaji wenye uadui juu ya wale ‘waliotetemeshwa sana na neno lake’ na kama alivyosema kuwa waliwazuia wasiingie “kwa sababu ya jina langu.”—Isaya 66:2, 5, NW.
7. Unabii wa Isaya ulitimizwa wakati gani, Yeremia alipatwa na nini, na ni nani alihakikisha neno la Yehova linatimia?
7 Kwa hiyo, katika karne iliyofuata, wakati wa siku za manabii Yeremia, Ezekieli na Danieli, Yehova aliyatumia majeshi ya Babiloni kama mawakili wake ili ‘kuwalipa adhabu’ Waisraeli wenye kuvunja agano. Jambo hilo lilitokeza “fujo” kama nini katika Yerusalemu mwaka 607 KWK wakati mji wote ulipoharibiwa, wala hata hekalu lenye kuvutia sana lililojengwa na Mfalme Sulemani halikuhifadhiwa! Wayahudi waliookoka walihamishwa mpaka Babiloni. Wayahudi wachache walioachwa katika nchi hiyo mwishowe walitorokea Misri, na kumburuta nabii Yeremia pamoja nao. Kwa njia hiyo utabiri wake ulitimizwa wakati wa uharibifu kamili wa nchi hiyo. Hivyo, pia, eneo ambalo wakati mmoja lilikaliwa na taifa likaacha kuwa nchi ya taifa lililokuwa hai likiwa na Yehova Mungu kama Mfalme walo wa kimbingu. Wayahudi waaminifu ‘waliotetemeshwa na neno la Mungu’ wakaona kwamba neno lake ni kweli.
8, 9. (a) Yerusalemu wa mfano wa kisasa ni nini? (b) Kulingana na unabii wa Yesu, itapatwa na nini, na kwa sababu gani?
8 Matukio yenye kushtua sana kupita yale ya mwaka 607 KWK yanawangojea wachukiaji na wanaowaepuka Mashahidi wa Yehova, ambao leo ndio wanaotetemeshwa na Neno la Yehova. Mambo hayo yote yenye msiba yaliyotokea huko-o-o nyuma katika siku za Yeremia, Ezekieli na Danieli “yaliwapata wao kwa jinsi ya mifano, yakaandikwa ili kutuonya sisi, tuliofikiliwa na miisho ya zamani.” (1 Wakorintho 10:11) Halafu kwa hakika itasikika “sauti ya fujo itokayo mjini,” Yerusalemu wa mfano chini ya laana ya kimungu, yaani, Jumuiya ya Wakristo. Kama Israeli wa kale, Jumuiya ya Wakristo, pia, inadai kuwa imo katika agano pamoja na Mungu, katika “agano jipya” pamoja na Yesu Kristo akiwa Mpatanishi walo. (Waebrania 8:7-9) Lakini haijaishi kupatana na uhusiano wa agano inaodai kuwa nao pamoja na Mungu. Kwa hiyo “dhiki kubwa,” iliyofananishwa na ile iliyokuwa juu ya Yerusalemu ya kale, inaingojea Jumuiya ya Wakristo, kulingana na utabiri wa Yesu mwenyewe:
9 “Maana wakati huo kutakuwa na dhiki kubwa, ambayo haijapata kuwako tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka leo, wala haitapata kutokea tena. Kama siku hizo hazingalipunguzwa, hakuna binadamu ye yote ambaye angeokoka; lakini siku hizo zitapunguzwa kwa ajili ya wale walioteuliwa.”—Matayo 24:21, 22, HNWW; Marko 13:19, 20.
10. Ni nini kingine, licha ya Jumuiya ya Wakristo, kitakachopatwa na dhiki hiyo, na ni nani watakaokuwa “wanadamu” watakaookoka?
10 Hiyo dhiki kubwa isiyo na kifani inakaribia sana. Itatoka mkononi mwa Mungu yule wa “walioteuliwa,” Yehova. Itaikumba, si Jumuiya ya Wakristo peke yake, mfano wa kisasa wa Yerusalemu, bali pia ile ambayo Jumuiya ya Wakristo imekuwa na urafiki mkubwa nayo, taratibu yote ya mambo ya ulimwengu. (Yakobo 4:4) Wakristo walio wakf na kubatizwa wa leo wanaotetemeshwa na Neno la Yehova ndio watakuwa “binadamu” watakaookolewa.
Uzazi Usiozuilika, Ulioharakishwa
11. (a) Kuzaliwa kwa mwanadamu kunatanguliwa na kipindi gani, lakini je, jambo kama hilo lingetokea katika kisa cha Yerusalemu wenye kujengwa upya? (b) Yerusalemu mwingine ungejengwa hapo kwa agizo la nani? (c) Je! Isaya alitabiri ni kwa muda gani mahali ulipokuwa Yerusalemu wa kale pangeendelea kuwa ukiwa mahame?
11 Sasa, turudi kwenye unabii unaosisimua wa Isaya! Ikiwa ni faraja baada ya taraja lenye huzuni alilotoka tu kueleza chini ya uongozi wa Mungu, sasa anatabiri juu ya tukio lenye kufurahisha. Kuzaliwa kwa watoto halali ni jambo ambalo wazazi wa waliooana kwa wakati unaofaa wanangojea kwa shauku nyingi na kwa matumaini makubwa sana. Kwa viumbe wa kibinadamu, lazima kuzaa kutanguliwe na wakati uliowekwa na Mungu wa ukuzi kamili wa mtoto anayetakwa. Lakini kwa habari hii Mbuni Mkuu wa tendo la kuzaa alitabiri jambo lisilo la kawaida kulingana na mpango wake mwenyewe. Nabii wake Isaya alikuwa ametabiri juu ya uharibifu wa mji uliochafuliwa wa Yerusalemu, na hivyo mji wa kwanza uliojengwa juu ya Mlima Sayuni ungekoma. Lakini mji mwingine ungetokea juu ya Mlima Sayuni uo huo kwa agizo la mshindi Mwajemi, Koreshi Mkuu, mtumishi wa Yehova ambaye angeipindua Milki ya Babiloni. (Isaya 44:28; 45:1) Lakini Isaya hakutabiri ni kwa muda gani Yerusalemu wa kale haungekuwapo na hivyo uwe bila “watoto,” au raia. Wala Isaya hakutabiri ni kwa muda gani Mlima Sayuni na nchi yote yenye kuhusiana nao ingekuwa ukiwa mahame, wenye kuepukwa na watu.
12. Nchi mpya ingetokeaje katika ulimwengu wa kale, nayo ingekuwa nchi ya nani?
12 Hata hivyo, katika siku za Koreshi Mkuu, Yerusalemu mwingine ungetokea na kuwa mama ya “watoto” wengi, yaani, raia na wakaaji wengi, wenye kuishi katika milki uliogawiwa. Je! hiyo ilimaanisha kwamba “nchi” fulani ingetokea katika ulimwengu wa kale, nchi ambayo ingekuwa ya watu ambao wakati mmoja hawakuwa “taifa”? Jibu la kiunabii la Yehova Mungu kwa ulizo hilo lilikuwa Ndiyo!
13, 14. (a) Wakati mwaka wa Yubile ya kawaida yenye kufuata ungefika baada ya kuhamishwa kwao, je, Wayahudi waliotekwa nyara wangerudishwa kwenye nchi yao? (b) Je! kwa mara nyingine Yerusalemu ungekuwa mama ya “watoto” kupitia jitihada zisizokuwa za kawaida kwa upande wa watekwa nyara Wayahudi, na Isaya 66:7, 8 ilitabiri nini juu ya jambo hilo?
13 Kwa hiyo ulizo lilikuwa, Wakati gani na jinsi gani? Kupitia nabii wake Yeremia, Yehova alitabiri kwamba nchi ya lililokuwa wakati mmoja “taifa” ingekaa ukiwa kwa miaka 70, mpaka upite wakati wenye urefu wa miaka 20 zaidi ya kile kipindi cha Yubile cha miaka 50. Kwa hiyo, mwaka wa Yubile ya kawaida ulipofika 573 KWK, hakungekuwa na sherehe ya Yubile katika hiyo iliyokuwa nchi ya kwao hapo kwanza, na hakungekuwako Yerusalemu, wala Sayuni, ikitokea ili izae jamii ya raia wawe “wana,” au “watoto” wake. Kwanza ni katika mwaka 537 KWK ndipo Wayahudi wo wote wahamishwa waliookoka wangerudi katika nchi iliyokuwa ya kwao hapo kwanza. Jambo hilo lingetokea bila watekwa nyara hao Wayahudi wa Babiloni kujika-a-a-za sana isivyo kawaida. Lingekuwa tendo la Mungu, kwa kupatana na ahadi yake ya kiunabii. Kama ilivyoonekana haielekei kuwa hata kidogo, “taifa” ambalo hapo kwanza lilikuwa limehamishwa lingetokea katika nchi iliyohifadhiwa na Yehova Mungu kwa ajili yalo. Akitazama baada ya msiba wa taifa lote wa mwaka 607 KWK, Yehova alidokeza kutokea kwa jambo hilo, alipomchochea Isaya aseme hivi baada ya hayo:
14 “Kabla hajaona [yaani, Yerusalemu mwingine] utungu alizaa; kabla maumivu yake hayajampata, alizaa mtoto mwanamume. Ni nani aliyesikia neno kama hili? Ni nani aliyeona mambo kama haya? Je! nchi yaweza kuzaliwa siku moja? Taifa laweza kuzaliwa mara? Maana Sayuni, mara alipoona utungu, alizaa watoto wake.”—Isaya 66:7, 8.
15. Kisa hicho cha wakati wa kuzaa kinafanana na kile kinachoelezwa katika Ufunuo 12:1-17?
15 Uzazi huo usio wa kawaida ni kinyume kabisa cha masimulizi ya uzazi wa mtoto mwanamume yanayosimuliwa katika kitabu cha mwisho cha Biblia Takatifu. Humo, katika Ufunuo, 12:1-17, twasoma: “Na ishara kuu ilionekana mbinguni; mwanamke aliyevikwa jua, na mwezi ulikuwa chini ya miguu yake, na juu ya kichwa chake taji ya nyota kumi na mbili. Naye alikuwa ana mimba, akilia, hali ana utungu na kuumwa katika kuzaa. Ikaonekana ishara nyingine mbinguni; na tazama, joka kubwa jekundu, alikuwa na vichwa saba na pembe kumi, na juu ya vichwa vyake vilemba saba. Na mkia wake wakokota theluthi ya nyota za mbinguni, na kuziangusha katika nchi. Na yule joka akasimama mbele ya yule mwanamke aliye tayari kuzaa, ili azaapo, amle mtoto wake. Naye akazaa mtoto mwanamume, yeye atakayewachunga mataifa yote kwa fimbo ya chuma. Na mtoto wake akanyakuliwa hata kwa Mungu, na kwa kiti chake cha enzi. . . . Joka akamkasirikia yule mwanamke, akaenda zake afanye vita juu ya wazao wake waliosalia, wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu.”
16. Lazima tutambue mwanamke huyo wa “ishara” na “mtoto mwanamume” wake kuwa nini au nani?
16 Kwa kuwa hakuna mwanamke ye yote duniani mwenye mwezi chini ya miguu yake na duara la nyota kumi na mbili (12) penye kichwa chake kama taji, mwanamke wa “ishara” aliyetangulia kusimuliwa lazima awe wa mfano. Kwa kuwa mtoto wa mwanamke huyo alikubaliwa na kutambuliwa na Mungu, lazima Yeye awe ndiye aliyemtia mimba. Kwa hiyo, ni kama kwamba mwanamke huyo ameolewa na Mungu. Tukiisha kuchunguza mambo hayo, mwanamke huyo wa “ishara” katika mbingu lazima awe anafananisha tengenezo la Mungu lililo kama mke la viumbe wa kiroho wa kimbingu, ambao kati yao Mwanaye mzaliwa pekee, Yesu Kristo, ndiye mkuu. Vivyo hivyo, mtoto wa mwanamke huyo, “mwanamume,” ni wa mfano, na anafananisha ufalme wa Mungu kwa sababu mtoto huyo mwanamume alinyakuliwa mpaka kwenye kiti cha enzi cha Mungu. Ili kufanya ufalme huo usiwe jambo la kuwazia tu, lazima awepo mtu atumike kama mtawala wa kifalme. Mtu huyo halisi ndiye ambaye Yehova Mungu alifanya naye agano kwa ajili ya ufalme.
17. Kwa hiyo ni jinsi gani Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu akawa mwenye haki ya kukalia kiti cha enzi kando ya Babaye?
17 Ndiyo, huyo alikuwa Mwana wake mzaliwa pekee, Yesu Kristo, ambaye, kwa sababu ya kuzaliwa kwake kwa kibinadamu kwa mwujiza katika Bethlehemu na katika nasaba ya jamaa ya Mfalme Daudi wa Israeli, alikuwa mrithi wa asili wa ufalme huo. (Isaya 9:6, 7; Luka 22:29, 30; Mathayo 1:17-25) Basi, kwa kufaa, kuhusiana na huyo “mwanamke” wa kimbingu ilikaziwa kwamba mtoto wake alikuwa “mwanamume,” kwa kuwa cheo cha kifalme kilihifadhiwa kwa ajili ya mtoto mwanamume katika nasaba ya kifalme ya Daudi.
18. Kwa hiyo hali zinazohusu kuzaliwa kwa yule mtoto mwanamume zinatofautianaje na zile zinazoelezwa katika Isaya 66:7, 8, kama inavyoonyeshwa na American Standard Version?
18 Hali zote hizo zinazohusu kuzaliwa kwa “mtoto mwanamume,” wa “mwanamke” wa kimbingu zinatofautiana na zile ambazo zimeandikwa katika unabii wa Isaya, sana sana kuhusiana na habari ya kuwa na mimba na utungu wa kuzaa. Kwa hiyo kuna sababu za maana kukata maneno kwamba yule “mtoto mwanamume” wa Isaya 66:7 anahusu hali tofauti ya kiunabii na ile ya yule “mtoto mwanamume,” katika Ufunuo 12:5. Kwa wazi huyo “mtoto mwanamume” anafananisha “taifa” lililozaliwa katika “nchi” ile katika unabii wa Isaya. Zaidi ya hayo, kwa habari ya Waisraeli waliorudishwa, uufalme, au utawala, halikuwa ndilo jambo kuu katika kusimamishwa kwao tena katika Yerusalemu mwaka 537 KWK. Mfalme katika nasaba ya Daudi hakuwekwa tena juu ya kiti cha enzi. Kwa kuwa Yudea ilikuwa jimbo la Uajemi, wao walikuwa chini ya utawala wa Mfalme Koreshi aliyekuwa ametoa amri ya kujenga upya hekalu na kurudisha ibada ya kweli katika Yerusalemu. Hata hivyo, kurudishwa huko kulitokea ghafula, bila kutazamiwa. Kulingana na American Standard Version, Isaya 66:7, 8 inasema: “Kabla hajapata utungu wa kuzaa, alizaa; kabla hajapatwa na uchungu, alizalishwa mtoto mwanamume. Ni nani amepata kusikia jambo kama hilo? ni nani amepata kuona mambo kama hayo? Je! nchi itazaliwa katika siku moja? je, taifa litazaliwa mara moja? kwa maana mara tu Sayuni alipopatwa na utungu wa kuzaa, alizaa watoto wake.”
19. (a) Ni nani walioona kama kwamba kuzaliwa kwa taifa la Israeli baada ya uhamisho kulikuwa kumeharakishwa, na kwa sababu gani? (b) Kizazi kilichoanza kukaa katika nchi ya babu zao kilikuwaje kizazi kipya kabisa, na hiyo ilikuwa nchi iliyozaliwa upya kwa maana gani?
19 Kulingana na unabii huo, kuzaliwa kwa taifa la Israeli baada ya uhamisho, ni kama kwamba kuliharakishwa. Kulitokea kwa ghafula yenye kushangaza kwa ulimwengu huo wa kale, katika mwaka 537 KWK. Ulimwengu huo wa kipagani haukutazamia kamwe taifa la Israeli lililokuwa limekufa kwa muda mrefu liwe hai tena, katika nchi yalo lenyewe liliyopewa na Mungu. Hakika ilikuwa Sayuni mpya iliyoanzishwa, na kuzaa taifa jipya. Tunakumbuka kwamba Waisraeli walihamishwa mpaka Babiloni katika nyakati mbalimbali, maandishi ya Biblia yanaonyesha kwamba 10,000 walihamishwa wakati wa utumwa wa kwanza katika mwaka 617 KWK. Baadaye mamia mengi walihamishwa. (2 Wafalme 24:14; Yeremia 52:28-30) Hata hivyo, kati ya wale walioachwa huru kutoka nchi hiyo ya kipagani katika mwaka 537 KWK na walioanza kukaa juu ya nchi hiyo ya babu zao walikuwamo wanaume 42,360, zaidi ya watumwa wengi na wenye kazi ya kuimba. Waisraeli hao walikuwa ni kutia na hesabu fulani ya wanaume wazee ambao walikuwa wameona hekalu ambalo Mfalme Sulemani alijenga katika Yerusalemu. (Ezra 2:64, 65; 3:12) Kwa hiyo, kwa sehemu kubwa kilikuwa ni kizazi kipya kabisa kilichoanza kukaa katika nchi hiyo kikiwa na kusudi la kujenga hekalu jipya. Sayuni mpya ilitokea juu ya nchi iliyozaliwa upya. Ikawa mama ya taifa jipya lililotoka uhamishoni. Makao yalo yalikuwa katika jimbo jipya la Waajemi la Yudea.
20. Mfano wa kisasa wa hayo ulitokeaje katika kisa cha Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote katika mwaka wa kwanza baada ya vita wa 1919?
20 Je! kuna mfano wa kisasa wa ‘kuzaliwa’ kwa Waisraeli waliorudishwa kama “taifa” katika mwaka 537 KWK? Ndiyo, kwa maana katika mwaka uliofuata vita ya ulimwengu ya 1914-1918 “taifa” la kiroho lilizaliwa, chini ya usimamizi wa Koreshi Mkuu Zaidi, Mfalme Yesu Kristo aliyetawazwa! Namna gani hivyo? Wakati wa vita hiyo makao makuu ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, Biblia na Trakti, shirika la uchapishaji la Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote, lilikuwa limehamishwa kutoka Brooklyn, New York, na kuhamishiwa tena kwenye makao madogo zaidi katika Pittsburgh, Pennsylvania. Vitabu vyayo vya karibuni zaidi vilikuwa vimepigwa marufuku katika Kanada na Marekani, na msimamizi wa Sosaiti, katibu-mweka hazina wayo, na washiriki wengine sita wa wafanyi kazi wa makao makuu walikuwa wamehukumiwa vifungo virefu katika mwaka 1918. Kusudi la maadui waliotokeza hayo yote lilikuwa kama lile linaloelezwa katika Zaburi 83:4: “Njoni, tuwakatilie mbali wasiwe taifa; na jina la Israeli halitakumbukwa tena.” Lakini katika masika ya 1919, waliachiliwa, jambo hilo likashangaza sana Jumuiya ya Wakristo! Mwaka uo huo Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote wenye kuteswa walifanya kusanyiko lao la kwanza baada ya vita katika Cedar Point, Ohio. Wahudhuriaji wa kusanyiko hilo walitangaziwa uchapishaji wa gazeti jipya, kuongezea gazeti la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), yaani, The Golden Age (sasa linaitwa Amkeni!).
21. Kwa hiyo, miaka mitano baada ya mwisho wa Nyakati za Mataifa, nini kilichozaliwa, kitumike katika cheo gani, na jinsi gani hivyo katika “nchi” iliyozaliwa upya?
21 Kwa hiyo, miaka mitano baada ya mwisho wa “nyakati za Mataifa” katika mwaka 1914, na kusimamishwa kwa ufalme wa Mungu mikononi mwa Koreshi Mkuu Zaidi, Yesu Kristo, “taifa” jipya lilianzishwa, “taifa” la kiroho. Washiriki wa “taifa” hili jipya wangetumika wakiwa mabalozi wa ufalme wa Mungu uliotoka kuzaliwa karibuni katika mbingu na wakiwa mashahidi wenye kulichukua jina lake. Yeye ameliweka “taifa” hilo katika “nchi” iliyo haki yalo, makao yalo ya utendaji ya kidunia, “nchi” yalo ya mfano, wakati huu ambao Nyakati za Mataifa za kukanyaga-kanyaga tengenezo lake lionekanalo chini ya miguu zimekwisha.—Luka 21:24, AV.
22. Yehova alitokeza maulizo gani juu ya uweza wake wa kuwa Baba ya “taifa” hilo, na, katika kujibu, yeye alitendaje kwa mfano ule wa kale na katika mfano wa kisasa?
22 Yehova Mungu Mweza Yote ndiye aliyekuwa mwenye daraka la kuzaliwa huko kwenye kutokeza, naye alikuwa ameazimia kwamba hakuna cho chote kingekuzuia. Katika Isaya 66:9 yeye alikuwa amesema hivi: “Je! mimi nilete wana karibu na kuzaliwa [kwa kuvunja mfuko wa maji ya mimba], nisizalishe? asema [Yehova]; mimi nizalishaye, je! nilifunge tumbo [la uzazi]? asema Mungu wako.” Jibu lake la kwanza kwa maulizo hayo yenye kutatiza lilikuwa kuwafungua watu wake kutoka Babiloni katika mwaka 537 KWK kisha kuufanya Yerusalemu ujengwe na ujawe na wakaaji Wayahudi wakiwa watoto wa Yerusalemu. Jibu la Mungu la kisasa la mfano, la maulizo yake mwenyewe lilikuwa ni kufanya Yerusalemu wa mfano, tengenezo lake la kimbingu, liwe na mimba hata likazaa “taifa” la kiroho duniani. Jambo hilo lilikuwa chini ya uongozi wa Koreshi Mkuu Zaidi, Mfalme aliyetoka kutawazwa mbinguni. Kuzaliwa huko kulikotokea katika mwaka uliofuata vita wa 1919, kukatokeza kikundi cha watu, “wana” wa Sayuni, ambao walikuwa wamejitoa kabisa kwa ajili ya faida za ufalme wa Mungu uliosimamishwa na ambao waliendeleza kutokuwamo kwao kabisa kuelekea serikali za kisiasa za ulimwengu huu. Mungu Mweza Yote hakuruhusu cho chote kizuie kutimizwa kabisa kwa kusudi lake tangu mwaka 1914 na kuendelea mpaka sasa hivi!
Baada ya funzo hili la Isaya 66:5-8, je, wewe unaweza kujibu maulizo yafuatayo:
Mstari 5: “Ndugu” wanachukiaje na kuzuia waabudu wa kweli wasiingie? “Ndugu” hao wanaaibishwaje?
Mstari 6: Ni katika njia gani kulikuwa “sauti ya fujo itokayo mjini” katika nyakati za kale? Katika siku za kisasa?
Mstari 7: Ni nani huyo “mtoto mwanamume” anayezaliwa na “mwanamke” bila ‘utungu wa kuzaa’? Je! huyo ni sawa na “mtoto mwanamume” katika Ufunuo 12:5?
Mstari 8: Ni katika njia gani “taifa” na “nchi” zilizaliwa ghafula na bila kutazamiwa katika mwaka 537 KWK?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Ufalme, ukiwa kama mtoto aliyetoka kuzaliwa, ulizaliwa na “mwanamke” wa Mungu katika mwaka 1914
Katika mwaka 1919, Israeli ya kiroho ‘ilizaliwa‘ ghafula katika “nchi” yayo