Ambayo Kuzaliwa kwa Taifa hilo Kumemaanisha kwa Wanadamu
1, 2. (a) Je! Yehova anayajibu maulizo yake mwenyewe katika Isaya 66:9? (b) Kulingana na Isaya 66:10-14, yeye anatoa mwito gani?
BADALA ya kujibu maulizo yake mwenyewe yaliyoandikwa katika Isaya 66:9 kwa kujibu waziwazi Hapana! Mungu alimchochea Isaya atoe mwito huu wa ushindi:
2 “Furahini pamoja na Yerusalemu, shangilieni kwa ajili yake, ninyi nyote mmpendao; furahini pamoja naye kuwa furaha, ninyi nyote mliao kwa ajili yake; mpate kunyonya, na kushibishwa kwa maziwa ya faraja zake, mpate kukama, na kufurahiwa kwa wingi wa utukufu wake. Maana [Yehova] asema hivi, Tazama, nitamwelekezea amani kama mto, na utukufu wa mataifa kama kijito kifurikacho, nanyi mtapata kunyonya; mtabebwa; na juu ya magoti mtabembelezwa. Mfano wa mtu ambaye mama yake amfariji, ndivyo nitakavyowafariji ninyi; nanyi mtafarijiwa katika Yerusalemu. Nanyi mtaona, na mioyo yenu itafurahi, na mifupa yenu itasitawi kama majani mabichi; na mkono wa [Yehova] utajulikana, uwaelekeao watumishi wake, naye atawaonea adui zake ghadhabu.”—Isaya 66:10-14.
3. Kwa njia hiyo wahamishwa Wayahudi waliorudishwa walifananishwa na nini, wakiwa na furaha gani, nao wangeona mkono wa nani katika jambo hilo?
3 Kwa njia hiyo wale waliorudishwa kutoka uhamisho walifananishwa na watoto waliozaliwa karibuni wenye kupewa kilishaji. Kwa wahamishwa Wayahudi kando ya mito ya Babiloni mitajo ya kunyonya matiti na kunywa maziwa ya matiti ilionyesha kwamba kungekuwako Yerusalemu mwingine ambao ungejengwa mahali ulipokuwa mji mkuu ulioharibiwa; vilevile kwamba angezaa idadi ya raia wengi au wakaaji na raia wengine wengi wa milki yake. (Linganisha Luka 13:34.) Kama akina mama wakati huo katika Mashariki ya Kati, Yerusalemu uliojengwa upya ungekuwa na watoto wake wakisimama juu ya goti lake la kushoto au la kulia, ili wabebwe; na, wakiisha kuketi, angewabembeleza kwa upendo juu ya paja lake. Wayahudi wale waliolipenda tengenezo la Yehova lionekanalo nyuma huko katika karne ya sita KWK wangefurahishwa na hilo, na wangeacha kuombolezea uhakika wa kwamba kwa miaka sabini ya uhamisho wao katika nchi ya kipagani hakukuwako Yerusalemu ulio mji mkuu wa watu waliochaguliwa wa Yehova. Furaha yao ilikuwa kama ile inayoelezwa katika Zaburi 126, tofauti na huzuni inayoelezwa katika Zaburi 137. Watumishi wa Yehova waliuona mkono wake ukiwaokoa.
4, 5. (a) Mabaki walitendaje “mkono” wa Mungu ulipojionyesha kwa ajili yao, na ni jambo gani walilothamini zaidi ya wakati mwingine wote? (b) Sasa ni wakati wa tendo gani jingine uliokuwa umefika? (c) Isaya anaelezaje jambo hilo?
4 Ndivyo ilivyokuwa kwa washiriki wa lile “taifa” la kiroho, ‘lililozaliwa’ katika mwaka 1919 WK. Baada ya kufunguliwa huru kwao kwenye kustaajabisha kutoka vizuizi vilivyowekwa wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na tisho la kufutiliwa mbali, walifurahi weee! Kuomboleza kwao kulikwisha. Walianza kuthamini sana kupita wakati mwingine wo wote kwamba Yehova ndiye Mungu wao na kwamba yeye ana tengenezo lionekanalo, sawa na alivyo na tengenezo lisiloonekana katika mbingu ambalo ni kama mke kwake. Tengenezo hilo lisiloonekana, ni “mama,” “Yerusalemu wa juu,” kwa mabaki. (Isaya 54:1-6; Wagalatia 4:26) Kwa hiyo, walipokusanywa pamoja tena kutoka hali yao ya mvurugo wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, walifurahia kupewa uangalizi wa upole, wakabebwa na kubembelezwa na “mama” huyo wa kiroho, “mke” wa Mungu aliye Baba yao. Wakiwa “watumishi” walio wakf kwake kupitia Ndugu yao mkubwa, Yesu Kristo, walifarijiwa kujua kwamba “mkono” wa Yehova ulikuwa ukitenda kwa kuwapendelea. Kinyume cha hayo, wakati wake wa ‘kuwaonea adui zake adhabu’ ulikuwa umefika. Hiyo ni kutia na wale wenye uadui kwa watangazaji wa ufalme wake uliozaliwa karibuni, kwa maana wale ambao ni adui wa watu wake walio wakf ni adui zake wa kibinafsi pia. Akieleza namna atakavyotekeleza adhabu yake, Yehova anaendelea kusema hivi:
5 “Maana [Yehova] atakuja na moto, na magari yake ya vita kama upepo wa kisulisuli; ili atoe malipo ya ghadhabu yake kwa moto uwakao, na maonyo yake kwa miali ya moto. Kwa maana [Yehova] atateta na wote wenye mwili, kwa moto na kwa upanga wake; nao watakaouawa na [Yehova] watakuwa wengi. Watu wale wajitakasao, na kujisafisha katika bustani, nyuma yake aliye katikati; wakila nyama ya nguruwe, na machukizo, na panya; watakoma pamoja, asema [Yehova]. Nami nayajua matendo yao na mawazo yao; wakati unakuja nitakapokusanya mataifa yote na lugha zote; nao watakuja, nao watauona utukufu wangu.”—Isaya 66:15-18.
6. Kwa hiyo Waisraeli wa siku za Isaya walikuwa wakivunjaje agano lao na kujichafua?
6 Katika siku ambazo Isaya aliandika maneno hayo, zaidi ya karne moja kabla ya uharibifu wa Yerusalemu katika mwaka 607 KWK, Waisraeli walikuwa wakivunja vibaya sana agano lao la taifa zima pamoja na Yehova, agano la torati (sheria) ambalo nabii Musa alikuwa mpatanishi walo. Walikuwa wakijitakasa wenyewe na kujisafisha wenyewe kwa ajili ya ibada ya sanamu katika bustani za pekee na walikuwa wakivunja sheria za Mungu zenye kuwakataza kula vitu fulani. Walijichafua wenyewe na kujitia unajisi wenyewe mbele za Mungu wa agano lao na hawakufanya lo lote kwa ajili ya utukufu wake.
7. (a) Yehova alitendaje kwa kupatana na mapatano ya agano lake ili amalize ugomvi huo? (b) Mungu ana ugomvi kama huo na nani leo?
7 Kwa hiyo yeye alileta juu ya wavunjaji hao wa agano hukumu zake moto-moto, kwa kupatana kabisa na mapatano yake ya agano. Aliutwaa “upanga” wa kufisha ili kumaliza ugomvi aliokuwa nao pamoja na wanadamu wote Wayahudi. Haishangazi kwamba maelfu machache tu waliokoka uharibifu usio na huruma ulioupata Yerusalemu, kisha wakaburutwa mpaka kwenye uhamisho mrefu katika Babiloni yenye kuabudu sanamu. Mataifa yote yenye kuwazunguka na vikundi-vikundi vya lugha walikuwa na lazima ya kushuhudia wonyesho huo wa utukufu wa Yehova akiwa Mungu mwenye kuweka agano, asiyesema uongo. Hayo yote yanatukumbusha kwa uzito kwamba Mungu uyo huyo ana ugomvi wa kadiri kubwa zaidi na Jumuiya ya Wakristo ya kisasa, ambayo inadai ilichukua mahali pa Israeli ya kale pa kuwa watu wa Yehova Mungu. Atautumia “upanga” wake wa kisasi kuichinja kabisa, kwa njia hiyo ajiletee utukufu.
“Ishara” Iliyowekwa Katikati ya Mataifa
8, 9. (a) Kwa kujiletea utukufu Yehova ametimiza kusudi lake baada ya kutokeza vitu gani na baada ya kisa gani cha watu wake? (b) Alilielezaje kusudi lake katika Isaya 66:19, 20?
8 Mungu Mweza Yote amepata utukufu kwa mataifa yote kwa kutimiza kusudi lake lisilobadilika kwa habari ya yale ambayo yangetokea baada ya kufanya “nchi” fulani ‘izaliwe siku moja’ na baada ya yeye kufanya “taifa” fulani ‘lizaliwe mara.’ Tunaposoma maneno yake yaliyoandikwa katika Isaya 66:19, 20, twaweza kukumbuka yale ambayo amefanya kwa utukufu tangu kuzaliwa kwa “taifa” lenye kufanyizwa na mabaki ya Waisraeli wa kiroho katika mwaka 1919 baada ya kuacha kuwa watu walio tengenezo wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, na wakawa na tumaini dogo sana au tazamio la kuokoka pigano hilo la ulimwengu. Yeye alisema hivi:
9 “Nami nitaweka ishara [oth, Kiebrania; signum, Vulgate ya Kilatini] yao, nami nitawatuma hao waliookoka kwa mataifa, Tarshishi, na Puli, na Ludi, wavutao upinde, kwa Tubali na Yavani, visiwa vilivyo mbali; watu wasioisikia habari yangu, wala kuuona utukufu wangu; nao watahubiri utukufu wangu katika mataifa. Nao watawaleta ndugu zenu wote kutoka mataifa yote, kuwa sadaka kwa [ Yehova], juu ya farasi, na katika magari, na katika machela, na juu ya nyumbu, na juu ya wanyama wepesi, mpaka mlima wangu mtakatifu Yerusalemu, asema [Yehova]; kama vile wana wa Israeli waletavyo sadaka yao nyumbani kwa [Yehova] katika chombo safi.”
10. Ishara” ambayo Mungu ‘aliiweka’ kati ya mataifa imekuwa ni nini?
10 Ni nini imekuwa “ishara” ambayo Yehova ‘ameweka’ kati ya mataifa tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza? Ni “ishara” iliyo hai. Mapema, katika unabii wa Isaya, mnenaji huyo wa Yehova alisema: “Angalieni, mimi na watoto hawa niliopewa na [Yehova] tu ishara na ajabu katika Israeli, zitokazo kwa [Yehova] wa majeshi, yeye akaaye katika mlima Sayuni.” (Isaya 8:18) Katika Waebrania 2:11-13 mtume Mkristo Paulo anayataja maneno hayo ya kiunabii na kuyatumia kuhusu Yesu Kristo na wanafunzi wake waliozaliwa kwa roho, akisema hivi: “Maana yeye atakasaye na hao wanaotakaswa wote pia watoka kwa mmoja. Kwa ajili hii haoni haya kuwaita ndugu zake; akisema, . . . Tazama, mimi nipo hapa na watoto niliopewa na [Yehova].”
11. Wale wanaofanyizwa kuwa “ishara” hiyo wamehubiri nini ulimwenguni pote tangu mwaka 1914, na kwa sababu gani walihitaji kukusanywa?
11 Kwa kupatana na hilo, “ishara” ambayo Yehova aliweka katikati ya mataifa ya dunia, ambayo “nyakati za Mataifa” zayo zilikwisha mwaka 1914, ni “taifa” la kiroho, ambalo washiriki walo wamehubiri ulimwenguni pote ufalme wa Mungu uliozaliwa katika mbingu mwishoni mwa “nyakati za mataifa zilizowekwa” katika mwaka 1914. (Luka 21:24, Authorized Version; New World Translation of the Holy Scriptures; Mathayo 24:14) Kwa sababu hiyo Yehova aliwakusanya pamoja mabaki ya Waisraeli wa kiroho waliokuwa wametawanywa na mateso makali wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza.
12. (a) Ni nani ambao wangeongezwa kwa mabaki waliookoka Vita ya Ulimwengu ya Kwanza? (b) Sana sana ni tangu wakati gani kutumwa kwa “waliookoka” kulipoanza kutokea?
12 Vilevile, kungali kulikuwa wengine ambao wangeletwa na kuongezwa kwa Waisraeli wale wa kiroho waliookoka Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, ili kufanyiza hesabu kamili ya mabaki ya “ndugu” za kiroho wa Kristo wakati huu. (Mathayo 25:40) Kwa kutokeza tangu kusanyiko kuu la kwanza lilipofanywa la Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote katika Cedar Point, Ohio, Marekani, katika kiangazi cha mwaka 1919, Yehova alianza kutuma baadhi ya wale “waliookoka” wa mabaki wa awali (kwanza) “kwa mataifa.” Alifanya hivyo kwa kutokeza sana kwenye kusanyiko la 1922 la IBSA kwenye mahali papo hapo kando ya ufuo wa Sandusky, Ohio, wakati msimamizi wa Sosaiti alipomalizia hotuba yake moto-moto yenye kuchochea wakusanyikaji kwa maneno haya: “Mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.” Baada ya hapo makundi ya mabaki ya Waisraeli wa kiroho walijitayarisha kutangaza ufalme wa Mungu uliosimamishwa, “kwa ushuhuda kwa mataifa yote,” kwa kuwapeleka washiriki wote shambani, “nyumba kwa nyumba” na waziwazi. Wote walikuwa mabalozi wa ufalme huo!—Matendo 20:20, NW.
13. Kwa utimizo wa unabii wa Isaya, ni nani wanaokusanywa kutoka kwa mataifa yote, na ni kama kwamba ni kwa njia gani ya haraka zaidi ya kutembea kwa miguu?
13 Katika kutimiza unabii wa Isaya, yote hayo yalitokeza ukusanyaji wa mabaki ya udugu wa kiroho, kwa njia zote za kusafirisha za haraka zaidi ya kutembea kwa miguu. Yehova alikuwa amesema kwamba angewapeleka “hao waliookoka” mpaka kwenye nchi za mbali-i, na alifanya hivyo kwa kuwapeleka “waliookoka” wakiwa hai katika vita ya ulimwengu na njaa kubwa, maradhi ya kuambukia na matetemeko ya ardhi yaliyotokea katika kipindi chenye kutokeza kifo cha 1914-1918 WK, na sana sana mateso yenye kuwaka sana juu ya wanafunzi wa Biblia waliokuwa wakishirikiana kwa juhudi na Sosaiti ulimwenguni pote. Sana sana mateso hayo yalitokeza kifo cha kiroho kwa wengine, hata wakakosa kujiunga katika kukusanya tena mabaki waliookoka baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, hasa mwito wa tendo la umoja ulipoanza kutolewa kupitia vichapo vilivyochapwa vya Sosaiti na kupitia wawakilishi wayo wenye kusafiri ambao waliyatembelea makundi.
14. “Waliookoka” ambao walikuwa wametumwa walisema juu ya nini, na hata walitumwa kwenye sehemu zisizo na maarifa gani?
14 Hata hivyo, wale waaminifu walifanya kama Yehova alivyokuwa ametabiri, ‘semeni juu ya utukufu wangu kati ya mataifa.’ (Isaya 66:19, NW) Wale watiifu “waliookoka” walienda katika nchi na “mataifa” yote yenye kufikilika, hata kwenye “visiwa vilivyo mbali,” wakisema juu ya utukufu wa ufalme wa Yehova ambao sasa ulikuwa umesimamishwa mbinguni katika mikono ya Mfalme wake, mwenye kutawala, Yesu Kristo. Wengi katika mataifa na visiwa hivyo vya mbali walikuwa hata hawajasikia ripoti juu ya Mungu wa kweli, Yehova, na walikuwa hawajapata kamwe kufahamu kwamba, kulingana na ishara za nyakati zilizotabiriwa, ufalme wake wenye utukufu ulikuwa umezaliwa mbinguni.—Ufunuo 12:1-5, 10.
15. Hao “ndugu” wa kiroho wanaoletwa kuwa ‘sadaka kwa Yehova’ lazima waendelee kujiweka katika hali gani ya kiroho, na kwa sababu gani?
15 Wale wote “waliookoka” waliwaleta wakiwa “ndugu” zao za kiroho waliwaleta “kuwa sadaka kwa [Yehova],” si kwa kiongozi fulani wa kibinadamu wa madhehebu ya kidini au kwa mamlaka fulani ya ulimwengu ya kisiasa ya duniani iliyokuwa ikishindania kuungwa mkono na watu walio wengi. Ili “sadaka” hiyo ikubalike kwa Yehova, ilipasa kuwa safi. Ni kwa sababu hiyo unabii huo unaeleza juu ya kuletwa kwa “sadaka” iliyo hai ikiwa “kama vile wana wa Israeli waletavyo sadaka yao nyumbani kwa [Yehova] katika chombo safi.” (Isaya 66:20) Ni kwa sababu hiyo wale “ndugu” za kiroho ambao wanafanyiza “sadaka” hiyo lazima wasiwe sehemu ya ulimwengu huu, ndiyo, lazima wajiweke wenyewe “pasipo mawaa” ya ulimwengu. (Yakobo 1:27) Lazima wajiweke wenyewe katika hali ya kutokuwamo kuelekea siasa zenye kuchafua za hii taratibu chafu ya mambo. Ni kwa sababu hiyo Yehova alisema wangeletwa “mpaka mlima wangu mtakatifu Yerusalemu.” Hiyo haifananishi Yerusalemu wa kisasa, mji mkuu wa Taifa la Israeli la kisiasa. Huo ni mji mkuu wa taifa ambalo asilimia 85 ni Wayahudi nalo ni mshirika wa tengenezo la Umoja wa Mataifa la kudumisha amani na usalama wa ulimwengu.
16. Kwa sababu gani Yehova hana cho chote katika Mashariki ya Kati kinachoweza kuitwa “mlima mtakatifu” wake?
16 Yerusalemu wa kisasa katika Mashariki ya Kati hauna “mlima mtakatifu” wo wote ambao Yehova angeuita ni mlima wake kwa maana ya kidini. Kwa sababu gani hivyo? Kwa sababu uliokuwa “mlima mtakatifu” wake hapo kwanza katika sehemu hiyo sasa juu yake kuna jengo takatifu la Waislamu, Kuba la Mwamba. Nalo ni la waabudu, si wa Yehova, bali wa Allah, mungu asiye na jina la kibinafsi.
17. Kwa hiyo ule “mlima mtakatifu Yerusalemu” ni nini, ambao kwao wale “ndugu” za kiroho wanaletwa tangu kuzaliwa kwa taifa hilo katika mwaka 1919?
17 Mambo yote yanayofaa yakichunguzwa kwa unyofu, jambo fulani la hakika linakuwa wazi: Katika utimizo wa kisasa wa Isaya 66:20 “mlima wangu mtakatifu” unahusu tengenezo lililo kama mama kwa Waisraeli wa kiroho, yaani, “Yerusalemu wa juu,” unaozungumzwa katika Wagalatia 4:26. Huo ndio Sayuni ‘uliozaa watoto wake,’ kulingana na Isaya 66:8. “Wana” hao wanafanyiza “taifa” ambalo ‘lilizaliwa mara,’ katika mwaka uliofuata vita kuu wa 1919. Kwa sababu hiyo, “ndugu” hao wa kiroho walioletwa na wale “waliookoka” tangu kuzaliwa huko kwa “taifa” waliletwa “kuwa sadaka kwa [Yehova]” na waliletwa kwenye uhusiano na tengenezo lake la kifalme, “Yerusalemu wa juu,” jambo hilo likiwa linafananishwa na Yerusalemu wa kidunia uliojengwa upya wa kale. Kwa wao kuletwa wawe “watoto” wake, waliletwa kwenye sehemu ionekanayo ya kidunia ya tengenezo la ulimwengu mzima la Yehova, wawe Wana-yerusalemu wa kiroho.
Kurudishwa kwa Ibada Safi ya Yehova
18. Kwa kuwa Yehova aliahidi kuchukua baadhi ya “taifa” lililozaliwa pia “kuwa makuhani na Walawi,” ni jambo gani la kufaa sana lililolipasa “taifa” hilo kufanya katika makao yalo ya utendaji?
18 Je! “taifa” hilo lililozaliwa karibuni liliitwaa ibada kamili ya Mungu mmoja aliye hai na wa kweli, Yehova, katika makao yao ya utendaji wa kiroho baada ya vita ile kuu? Ingefaa sana kufanya hivyo, kwa kuwa sasa walikuwa wamewekwa huru kutokana na upigaji wa ubwana wa Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Na ndivyo walivyofanya, kwa kupatana na tendo ambalo Yehova aliahidi angechukua kuhusiana na “taifa” hilo lililozaliwa karibuni, katika Isaya 66:21: “Na baadhi ya hao nitawatwaa kuwa makuhani na Walawi, asema [Yehova].” Lazima tukumbuke kwamba, katika kisa cha Waisraeli wakati wa ile miaka sabini (70) ya uhamisho wao katika Babiloni ya kale, kuanza mwaka 607 mpaka 537, hawakuwa na utendaji wa utumishi wa kuhani mkuu wa nasaba ya Haruni na makuhani wadogo na wa watumishi wao, Walawi, kwa kuwa hekalu ambamo walitumikia liliharibiwa. Kwa usahihi Yehova alikuwa ametabiri hilo, katika Hosea 3:4, 5, kwa kusema:
19. Yehova alikuwa ametabirije kurudishwa kwa ibada yake katika Hosea 3:4, 5?
19 “Kwa maana wana wa Israeli watakaa siku nyingi bila . . . sadaka, wala nguzo, wala naivera, wala kinyago; baada ya hayo wana wa Israeli watarejea, na kumtafuta [Yehova], Mungu wao, na Daudi, mfalme [Masihi] wao; nao watamwendea [Yehova] na wema wake kwa kicho siku za mwisho.”
20. Tendo hilo la Yehova lingetaka nini kitengenezwe, na wapi, na kijengwe kwa ajili ya mahitaji gani ya lazima?
20 Kwa njia hiyo, licha ya kutenda kama Mkombozi wao kutoka Babiloni, Yehova angeyatimiza mahitaji yao ya lazima sana, mahitaji yao ya kiroho. Yeye angemrudisha kuhani mkuu halali pamoja na makuhani wadogo wake, na wao wangesaidiwa na baraza ya Walawi. Jambo hilo lingetaka hekalu katika Yerusalemu lijengwe upya, ambamo wao wangetoa utumishi wao mbalimbali wa maana sana kwa “taifa” hilo ambalo lingezaliwa “mara.” Hilo lingetokea katika “nchi” ambayo ‘ingezaliwa siku moja,’ nchi ya kwao waliyoipenda. Ndiyo, hata ingawa jambo hilo lingeelekea kutotokea.—Isaya 66:8.
21. Ni jambo gani kama hilo lililotokea katika maana ya kiroho katika kisa cha “taifa” lililozaliwa upya tangu mwaka 1919 kuendelea?
21 Katika maana ya kiroho, jambo kama hilo limetokea kwa mabaki ya Israeli wa kiroho tangu Yehova Mungu alipowakomboa kutoka Babeli Mkuu (milki ya ulimwengu ya dini ya uongo) katika mwaka wa 1919 WK uliofuata ile vita kuu. Yeye alifunua wazi ufahamu wao wa cheo cha Mfalme wa Kimasihi, Yesu Kristo, kuwa ni Kuhani Mkuu wa Mungu. Yeye aliwasafisha kutokana na uchafu wo wote wa kidini ambao ulikuwa ungali umeshikamana nao kwa sababu ya kushirikiana na Babeli Mkuu na kuwa katika utumwa wake. Wakiwa washiriki wa “taifa lililochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu walio mali ya pekee” kuhusiana na Mungu Aliye Juu Zaidi, wakaja kuthamini vizuri zaidi kupita wakati mwingine wote uliotangulia namna na kwa sababu gani walipaswa kutokuwamo kabisa kuhusiana na mambo ya kisiasa ya ulimwengu huu wa kisasa. Waliona kwamba wakati ulikuwa umefika kwa Mungu mmoja aliye hai na wa kweli ‘kujifanyia jina.’ Na waliliona daraka lao la kushangilia jina la kibinafsi la Mungu, Yehova, juu ya majina mengine yote. Walilifahamu daraka lao la kuwa mashahidi kwa Mungu huyu ambaye jina lake lilikuwa limefichwa kwa karne nyingi, na kwa kufaa wakatwaa jina “mashahidi wa Yehova” katika mwaka wenye kukumbukwa wa 1931.—1 Petro 2:9, NW; Isaya 43:12, NW; 63:12.
22. Ingawa wokovu wa viumbe unahusika, ulizo la maana zaidi ni nini, fundisho ambalo ni la maana zaidi la Biblia, na kwa sababu gani?
22 Ingawa unazungumzwa kwa kufaa katika Biblia iliyoongozwa kwa roho, wokovu wa jamii ya kibinadamu kutokana na dhambi na mauti na utumwa wa Shetani Ibilisi na tengenezo lake silo jambo la maana zaidi, fundisho la maana zaidi la Biblia Takatifu. Kama ilivyosema makala ya kwanza, yenye kichwa “ukamilifu,” iliyotokea katika toleo la Agosti 15, 1941, la gazeti Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), ilisema hivi: “Kwa kurudia-rudia kusudi la Yehova la kufanya ulimwengu utawalwe na Serikali yake yenye haki linakaziwa katika Maandiko. Serikali yake ni Theokrasi ambayo juu yayo amemweka Kristo Yesu kuwa Mfalme. . . . Ulizo kuu lililotokezwa na utatizi wa ukaidi wa Shetani lilikuwa na lingali ni UTAWALA WA ULIMWENGU MZIMA.” (Mafungu 1, 19) Kwa hiyo, kusudi kuu la Mungu Aliye Juu Zaidi ni kuitetea enzi yake kuu ya ulimwengu mzima, ambaye ndiye peke yake aliye nayo. Jambo hilo atalifanya kwa utukufu hivi karibuni katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye uwanja wa pigano wa Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14-16) Ni wajibu, pendeleo, heshima ya hilo “taifa takatifu” la Israeli wa kiroho kuendeleza ukamilifu walo kuelekea utawala au enzi ya Yehova ya ulimwengu wote wa juu na chini, na kwa njia hiyo kuthibitisha Ibilisi kuwa mwongo.
23. Ni kushindwa kwa jitihada gani za mataifa adui kunakotimiza maneno ya Yehova katika Isaya 66:22?
23 Mpaka wakati huu uliosonga sana jitihada zote kwa upande wa mataifa ya kilimwengu ya tengenezo la Shetani lionekanalo za kufutilia mbali “taifa” la Yehova ‘lililozaliwa’ katika mwaka 1919 katika “nchi” yalo iliyozaliwa karibuni zimeshindwa. Jambo hilo limetimiza kwa uaminifu uhakikisho uliotolewa na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Mzima kwa maneno haya katika Isaya 66:22: “Kama vile mbingu mpya na nchi mpya, nitakazofanya, zitakavyokaa mbele zangu, asema [Yehova], ndivyo uzao wenu na jina lenu litakavyokaa.”
24. (a) Hali ya kudumu ya mbingu mpya na nchi mpya ya Mungu inatoa uhakikisho gani kwa mabaki ya Israeli wa kiroho? (b) Katika wakati ujao ulio karibu mabaki watafanywa kuwa sehemu ya nini?
24 He, hapana! Yajapokuwa yote ambayo Shetani Ibilisi na mashetani wake wasioonekana na tengenezo lake la kidunia linaloonekana huenda wakajaribu kuwafanya katika wakati ujao ulio karibu, mabaki ya Israeli wa kiroho na jina lao hawatafutwa. Uzao uonekanao wa kidunia wa tengenezo la Shetani na majina yao hayataendelea kuwapo kwa muda mrefu zaidi. Lakini, tofauti kubwa sana na hilo, uzao wa tengenezo la Yehova la ulimwengu mzima, mabaki ya Israeli wa kiroho, litaendelea kuwapo; wala jina lalo halitafutiliwa mbali na maadui walo na kusahauliwa. Kama vile ilivyo hakika mbingu mpya na nchi mpya ambazo Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Mzima Yehova anatengeneza zitaendelea kuwapo daima, ndivyo itakavyokuwa kwa kisa cha mabaki ya Israeli wa kiroho na majina yao yanayostahili. Hiyo maana yake si kwamba mabaki ya Israeli wa kiroho watakaa duniani milele. Hapana, lakini kwa wakati ujao ulio karibu watachukuliwa na kuunganishwa na Kuhani Mkuu wao, Yesu Kristo, katika “mbingu mpya” na watatumika kama makuhani wadogo kwenye hilo hekalu la kiroho.
25. (a) Yehova alianza ‘kufanya’ hizo ““mbingu mpya” wakati gani? (b) Sana sana ni tangu wakati gani wametokea wanaotarajia kuwa washiriki wa “nchi mpya”?
25 Yehova Mungu alianza kuzifanya hizo “mbingu mpya” mwishoni mwa “nyakati za mataifa zilizowekwa” katika mwaka 1914 WK, alipomkalisha Mwanaye aliyetukuzwa Yesu Kristo juu ya kiti cha enzi cha kimbingu, ili atawale akiwa Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana. Huyo ndiye “Mwana wa Daudi,” na, alipokuwa mwanadamu mkamilifu duniani, Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Mzima Yehova alifanya agano pamoja naye la ufalme wa milele. (Mathayo 21:15) Kutoka kwa kiti cha enzi chake cha kimbingu Mfalme Yesu Kristo anatawala juu ya dunia yetu. Kufanywa kwa “nchi mpya” (dunia mpya) hakumaanishi wala hakutaki dunia yetu halisi iharibiwe. Hapana, kwa maana sayari-Dunia “hudumu daima.” (Mhubiri 1:4) Ufalme wa Mungu kupitia Kristo utaibadili iwe Paradiso ya milele. Kwa kupatana na uhakika huo mzuri ajabu, kufanyizwa kwa “nchi mpya” kwamaanisha Yehova afanye jamii mpya ya kibinadamu yenye kupatana kikamilifu naye na “mbingu mpya” zake zenye haki. (2 Petro 3:13) Tayari ana mamilioni duniani wanaotarajia kuwa washiriki wa hiyo jamii ya “nchi mpya.” Hao wameonekana hasa tangu mwaka 1935 WK.
26. (a) Kuja kwa huo “mkutano mkubwa” katika ushirika na mabaki ya Waisraeli wa kiroho kulikuwa kumesemwaje katika Isaya 66:12? (b) Sasa “mkutano” huo unamtumikia Yehova wapi?
26 Wao wametoka katika mataifa yote, rangi, watu na lugha na wamejiweka wakf kwa Yehova Mungu kupitia Kristo aliye Kuhani Mkuu na wameonyesha wakf wao kwa kubatizwa katika maji kwa kumwiga Mchungaji Mwema wao, Yesu Kristo. (Yohana 10:14, 16) Mapema zaidi, katika Isaya 66:12, Yehova alikuwa amesema kwamba angewaelekezea mabaki ya Israeli wa kiroho, wanaofananishwa na “Yerusalemu wa juu,” kile anachokiita “utukufu wa mataifa,” nao ungekuwa “kama kijito kifurikacho.” Tangu mwaka 1935 kuelekezwa huko kwa “utukufu wa mataifa” kwa mabaki ya kiroho kumekuwa kukiendelea hatua kwa hatua kukiwa kwa namna ya “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wa Mchungaji Mwema, Mfalme Yesu Kristo anayetawala. (Ufunuo 7:9-17) Kwa sababu ya ushikamanifu wao kwa Serikali ya Kitheokrasi ya Yehova kupitia Kristo, Mchungaji Mwema amewafanya wakawa “kundi moja” pamoja na mabaki ya Waisraeli wa kiroho. Wanaletwa kwenye hekalu la kiroho la Yehova, inayoitwa “nyumba ya sala kwa mataifa yote.” (Isaya 56:7; Marko 11:17) Kwenye hekalu la kiroho la Mungu la sala ya mataifa yote “mkutano mkubwa” wenye utukufu ‘unamtolea utumishi mtakatifu mchana na usiku.’—Ufunuo 7:15, NW.
27, 28. Ni mara nyingi kadiri gani “mkutano mkubwa” kutoka kwa “wanadamu wote unakutana na mabaki na kujiunga kwao katika kazi ya kutoa ushuhuda kunatokeza nini?
27 Tukio hilo zuri sana la kisasa linalingana na yale ambayo Yehova anaendelea kusema, katika Isaya 66:23: “Na itakuwa, mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato, wanadamu wote watakuja kuabudu mbele zangu, asema [Yehova].”—Hagai 2:7-9.
28 Kulingana na ripoti, “mkutano mkubwa” kutoka kwa “wanadamu wote” wanafanya mikutano pamoja na mabaki ya Israeli wa kiroho kwa ukawaida, “mwezi mpya hata mwezi mpya [kila mwezi], na sabato hata sabato [kila juma].” Kwa ushikamanifu wanajiunga na mabaki waliotiwa mafuta katika kutoa ushuhuda wa waziwazi na kutoa ushuhuda nyumba kwa nyumba ili utabiri wa Yesu wa “umalizio wa taratibu ya mambo” utimizwe: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:3, 14, NW) Watu hao wanaotoka kwa “wanadamu wote” ambao wanakubali kuhubiri huko ‘wanakuja kuabudu’ mbele za Mwenye Enzi Kuu Yehova.
29, 30. (a) Isaya 66:24 inaonyeshaje kwamba waabudu hao kutoka kwa “wanadamu wote” wataiokoka ile “dhiki kubwa” ambayo itakomesha hii taratibu ya mambo? (b) Watakuwa msingi wa nini, na baadaye, wataongoza nani katika ibada ya Mfanya vitu vya kimbingu na vya kidunia?
29 Wakiwa waokokaji wa “dhiki kubwa” ambayo iko mbele kidogo tu ya ulimwengu, watashuhudia namna Yehova atakavyotetea enzi yake kuu ya ulimwengu wote wa juu na chini kwa kuwaharibu maadui wake mwenyewe na maadui wao katika “dhiki” hiyo ya ulimwenguni pote. Kuhusu hilo Isaya anamalizia unabii wake kwa maneno haya: “Nao [waokokaji wa hiyo dhiki] watatoka nje na kuitazama mizoga ya watu walioniasi; maana funza wao hatakufa, wala moto wao hautazimika;nao watakuwa chukizo machoni pa wote wenye mwili.”—Isaya 66:24.
30 Kama wale “mbuzi” waliolaaniwa wa mfano wa Yesu unaotimizwa wakati wa huu “umalizio wa taratibu ya mambo,” wale wanaomkosea Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova “watakwenda zao kuingia katika adhabu ya milele,” uharibifu wa milele. (Mathayo 24:3, NW; 25:31-46) Halafu, wakiwa msingi wa “nchi mpya,” wale warithi wa dunia wenye mfano wa kondoo watawakaribisha kati yao wale wanaofufuliwa kutoka kwa wafu wakiwa na mwili duniani. Watawaongoza hao waliofufuliwa wenye mwili wamwabudu kwa umoja Mfanyizaji aliyetetewa wa “mbingu mpya” na “nchi mpya.”—Isaya 65:17; 2 Petro 3:13.—Kutoka The Watchtower, July 1, 1982.
Wewe ungejibuje maulizo yafuatayo ambayo msingi wayo ni Isaya 66:8-20?
Mstari 8: “Taifa” la kiroho la Yehova lilipataje ‘kuzaliwa’ katika “nchi” yalo ya kiroho katika mwaka 1919?
Mstari 9-14: Yerusalemu uliwapaje “watoto” wayo kilishaji na utunzaji wa upendo? Jambo hilo linahusuje watoto wa kiroho katika nyakati za kisasa?
Mstari 15-18: Ni mazoea gani yaliyoletea Yerusalemu uharibifu katika mwaka 607 KWK, na kufananisha jambo gani la leo?
Mstari 19, 20: Yehova ameweka “ishara” gani “katika mataifa”? Kwa kusudi gani?
Wewe ungejibuje maulizo yafuatayo ambayo msingi wayo ni Isaya 66:19-24
Mstari 19: Baadhi ya “waliookoka” wamepelekwaje kwa “mataifa”? Na matokeo yakawa nini?
Mstari 20: Ni kwa njia gani “wana wa Israeli” wameleta “sadaka” kwa nyumba ya Yehova?
Mstari 21: Ni kwa njia gani wengine walitwaliwa watumike wakiwa “makuhani”?
Mstari 22: Akitaja juu ya uhakika wa “mbingu mpya na nchi mpya,” Yehova anatoa uhakikisho gani juu ya watu wake waliorudishwa?
Mstari 23: Ni kwa njia gani tunaona “wanadamu wote” wakisujudu mbele za Yehova “mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato”?
Mstari 24: Waokokaji wa “dhiki kubwa” watashuhudia nini ambayo yatawapata wanaomkosea Yehova?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Kama mama, Yerusalemu uliwatunza “watoto” wake kwa upendo
[Picha katika ukurasa wa 21]
Wakiwa wamekwisha ‘kuokoka’ kutoka “Babeli Mkuu,” Mashahidi wa Yehova wanakwenda wakiwa na ujumbe wa Ufalme