Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 12/1 kur. 8-13
  • “Utimizeni Wokovu Wenu Wenyewe”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Utimizeni Wokovu Wenu Wenyewe”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Dhabihu za Sifa Zinazokubalika
  • Pamba Kufundisha Kwako na Kazi Njema
  • Kazi ya Kuburudisha Kuelekea Wokovu
  • Mwenye Shughuli Katika Kazi Zisizo Hai au Katika Utumishi wa Yehova?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • ‘Kufanya Kazi Kwa Bidii na Kujikaza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Ni Lazima Tufanye Nini Tuokolewe?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Kufanya Kazi Pamoja na Yehova kwa Uaminifu-Mshikamanifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 12/1 kur. 8-13

“Utimizeni Wokovu Wenu Wenyewe”

“Utimizeni wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.”​—Wafilipi 2:12.

1. (a) Ni nani au nini kinachosifu Yehova bila kusema maneno, na jambo hilo linawezekanaje? (b) Ni akina nani wengine wanaokaribishwa kufanya hivyo?

KAZI za Yehova zinamsifu. “Msifuni, jua na mwezi; msifuni, nyota zote zenye mwanga.” Ingawa vitu hivyo havina uwezo wa kusema, vinataja sifa zake. Ndivyo na milima na vilima, mimea na wanyama, ndege na vitambaavyo. (Zaburi 148:3, 9, 10; 19:1-4) Vinawezaje kutoa sifa hizo bila kusema? Inawezekana kuwa hivyo kwa sababu kazi huonyesha namna mwenye kuifanya alivyo. Jambo hilo limetajwa waziwazi kuhusu kazi za Yehova: “Mambo yake yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake.” (Warumi 1:20) Ikiwa inapasa viumbe visivyo na usemi vimpe sifa, si zaidi sana wale walio na uwezo wa kusema! Kwa hiyo inafaa kwamba Zaburi 146 mpaka 150 zinaanza na kumalizika kwa kutokeza mwito wa jumla, “Haleluya”! (“Sifuni Yah, enyi watu!”, NW)

2. Ni kazi gani zinazopasa kuletea Ukristo wetu sifa?

2 Sawa na vile kazi za Yehova zinavyomwonyesha alivyo, ndivyo kazi zetu zinavyotuonyesha tulivyo. Je! zinatufunua sisi kuwa watafutaji wa utajiri au wasifaji wa Yehova? Kazi ya kwanza kabisa ambayo ni lazima Wakristo waifanye sasa ni kutimiza maneno haya ya Yesu: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” Yeye alisema yafuatayo akiwaaga wanafunzi wake: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 24:14; 28:19, 20, NW) Tunapotoa ‘ushuhuda barabara kutoka nyumba kwa nyumba,’ kazi yetu ya kuhubiri inapasa kuwa na kiwango bora. Hivyo tunaweza kuwa na msimamo mzuri mbele za Wafalme Yehova na Kristo Yesu. “Je! wamwona mtu mwenye bidii katika kazi zake? Huyo atasimama mbele ya wafalme.”​—Matendo 20:20, 21; Mithali 22:29.

3. Tunazoezwaje kwa ajili ya kazi hii, na kwa sababu gani ni lazima tuwe wastadi wa kuifanya?

3 Biblia imetolewa ili tupate maagizo na mazoezi tunayohitaji kabisa, ili “mutu wa Mungu awe mukamilifu, ametengenezwa kabisa kwa kila tendo jema.” Kwa hiyo kwa funzo la faragha na la kikundi, kwa kuhudhuria mikutano ya kundi kwa ukawaida na kwa kushiriki katika programu zenye mazoezi “jitahidi [kabisa kabisa, NW] kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli.” (2 Timotheo 3:17, ZSB; 2:15) Shetani, mungu wa mfumo wa ulimwengu mwovu wa sasa, amefumanisha mawongo mengi sana ya kidini na kuyatandaza kama kitambaa juu ya mataifa mpaka wasioamini wanapofushika wasizione habari njema za ufalme wa Kristo zinazotolea watu nuru. Lakini Neno la Yehova ni kama upanga wenye makali mawili na Mashahidi wa Yehova lazima watumie ustadi katika kuupunga-punga upanga huo wakichane-chane kitambaa hicho chenye kupofusha watu na kuacha nuru ing’ae ndani ya akili na mioyo ya wanaume, wanawake na watoto wanyofu wenye mfano wa kondoo.​—2 Wakorintho 4:3, 4.

Dhabihu za Sifa Zinazokubalika

4. Sifa tunayotoa inafananishwa na nini, na ni ukosefu gani unaoonyeshwa kwenye Malaki 1:6-8?

4 Maneno yetu ya kumsifu Yehova yanafananishwa na dhabihu ambazo watu walitakwa watoe na sheria ya Musa: “Na tumpe Mungu dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake.” Maneno pia yanafananishwa na “ng’ombe dume wachanga wa midomo yetu.” (Waebrania 13:15; Hosea 14:2, NW) Dhabihu zilizotolewa chini ya Torati zilipasa kuwa bila waa, na makuhani waliolipuza takwa hilo walikemewa na Yehova, kama inavyosimuliwa kwenye Malaki 1:6-8:

“Mwana humheshimu baba yake, na mtumishi humcha bwana wake; basi, kama mimi ni baba yenu, heshima yangu iko wapi? na kama mimi ni bwana wenu, kicho changu ki wapi? [Yehova] wa majeshi awauliza ninyi, enyi makuhani, mnaolidharau jina langu. Nanyi mwasema, Tumelidharau jina lako kwa jinsi gani? Mnatoa chakula kilichotiwa unajisi juu ya madhabahu yangu. Nanyi mwasema, Sisi tumekutia unajisi kwa jinsi gani? Kwa sababu mwasema, Meza ya [Yehova] ni kitu cha kudharauliwa. Tena mtoapo sadaka aliye kipofu, si vibaya! na mtoapo sadaka walio vilema na wagonjwa, si vibaya! Haya! mtolee liwali wako; je! atakuwa radhi nawe? au atakukubali nafsi yako?”

5. Tunaweza kuepukaje kutoa dhabihu za sifa zenye mawaa?

5 Je! dhabihu tunazotoa leo, “ng’ombe dume wachanga wa midomo yetu” na “tunda la midomo” yetu, zinakuwa bila waa kwa kadiri tulivyo na uwezo wa kuzitoa bila waa? Je, kwa funzo na mazoezi na matumizi ya uwezo wa akili zetu tumezifanya dhabihu zetu za sifa ziwe nzuri kwa kadiri tuwezavyo kuzifanya? Je! tunafanya uchunguzi na kufikiria sana maneno ya kweli, tuyaseme kwenye nyumba za watu ipendezavyo? “Kwa sababu huyo Mhubiri alikuwa na hekima, aliendelea kuwafundisha watu maarifa; naam, akatafakari, akatafuta-tafuta, akatunga mithali nyingi. Huyo Mhubiri akatafuta-tafuta ili apate kuona maneno yapendezayo, na yale yaliyoandikwa kwa unyofu, yaani, maneno ya kweli.”​—Mhubiri 12:9, 10.

6. Ni kwa njia gani tunaweza kufanya iwe rahisi zaidi watu kuukubali ujumbe wa Ufalme?

6 Ni vigumu watu kukubali kwamba wamekosea na wanahitaji kubadili njia yao ya kuwaza, hasa kuhusu jambo lenye kukasirisha watu upesi kama vile maoni yao ya kidini. Je! sisi tunajaribu kuwarahisishia mambo? Je! tunajiweka katika hali yao, kama mtume Paulo? Yeye alisema: “Nalikuwa kama Myahudi kwa Wayahudi, ili niwapate Wayahudi; kwa wale walio chini ya sheria, nalikuwa kama chini ya sheria, (ingawa mimi mwenyewe si chini ya sheria,) ili niwapate walio chini ya sheria. Kwa wale wasio na sheria nalikuwa kama sina sheria, (si kwamba sina sheria mbele za Mungu, bali mwenye sheria mbele za Kristo), ili niwapate hao wasio na sheria. Kwa wanyonge nalikuwa mnyonge, ili niwapate wanyonge. Nimekuwa hali zote kwa watu wote, ili kwa njia zote nipate kuwaokoa watu. Nami nafanya mambo yote kwa ajili ya Injili ili kuishiriki pamoja na wengine.”​—1 Wakorintho 9:20-23.

7. Ni kwa njia gani tunaweza kufanya mahubiri yetu yapate uwezo mwingi zaidi wa kuvuta watu?

7 Je! sisi ni wenye ufahamu wa huruma na fadhili, na je! maneno yetu yana maponyo? “Yule ambaye ni mwenye hekima katika moyo ataitwa ufahamu, na yeye aliye mtamu katika midomo yake huongeza uwezo wa kuvuta watu kwa maneno. Semi za kupendeza ni sega la asali, tamu kwa nafsi na maponyo kwa mifupa.” Je! sisi tunajifunza ili tuonyeshe ufahamu wenye busara tunapotolea wengine ushuhuda kuhusu ufalme wa Mungu, kwa njia hiyo tukiongeza uwezo wa kuvuta watu katika usemi wetu? “Moyo wa yule mwenye hekima hufanya kinywa chake kionyeshe ufahamu wenye busara, na kwenye midomo yake unaongeza uwezo wa kuvuta watu.” (Mithali 16:21, 24, 23, NW) Chumvi (munyu) inaongeza ladha kwenye chakula ambacho kingalikuwa si kitamu, naye Paulo anatumia uhakika huo kuonyesha kwamba chakula cha kiroho tunachotolea wengine kinapasa kiwe cha kupendeza ili wakile: “Maneno yenu yawe na neema sikuzote, yakikolea munyu, mpate kujua jinsi iwapasavyo kumjibu kila mtu.”​—Wakolosai 4:6.

Pamba Kufundisha Kwako na Kazi Njema

8. Ni jambo gani linalohitajiwa kabisa ndipo tuweze kuepuka kulaumiwa kuwa wanafiki?

8 Zaidi ya kazi za kuzihubiri habari njema, kazi za kufuata yale tunayoyahubiri zinahitajiwa kabisa tusije tukalaumiwa kuwa wanafiki. Mtume Paulo alilijua sana jambo hilo. Aliwanenea waalimu fulani wa Kiyahudi wa siku zake kwamba walikuwa na hatia ya unafiki: “Wewe umfundishaye mwingine, je! hujifundishi mwenyewe? Wewe usemaye kwamba mtu asizini, wazini mwenyewe? Wewe uchukiaye sanamu, wateka mahekalu? Wewe ujisifuye katika torati, wamvunjia Mungu heshima kwa kuiasi torati?” (Warumi 2:21-23) Paulo aliijua waziwazi hatari ambayo ingeweza kumwelekea yeye katika jambo hilo, akasema: “Nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa [kwa njia fulani].”​—1 Wakorintho 9:27.

9. Ni hoja (sababu) gani zinazoonyesha ule usemi wa kidini wa kwamba ‘ukiisha kuokoka, umeokoka daima’ si wa kweli?

9 Hiyo inaonyesha kwamba Paulo hakukubaliana na maoni yanayoshikiliwa na wanadini wengi wa siku hizi, yaani, ‘Ukiisha kuokoka, umeokoka daima.’ Tukiisha kumkubali Yesu kuwa mwokozi na mkombozi wetu, na kuweka maisha zetu wakf kwa Yehova Mungu, huo ndio mwanzo tu wa kutembea katika njia inayoelekea kwenye wokovu, wala huo sio mwisho. Kwa hiyo Paulo anatushauri tuendelee ‘kutimia zwokovu wetu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.’ (Wafilipi 2:12) Kwa sababu gani tuendelee ‘kutimiza’ na kwa sababu gani tufanye hivyo “kwa kuogopa na kutetemeka,” ikiwa kweli ‘ukiisha kuokoka, umeokoka daima’? Inawezekana kuanguka na kuiacha njia, na haiwezekani kwa wengine wanaoanguka kurudia toba tena, “kwa sababu wanamtundika Mwana wa Mungu upya.” Na Yesu mwenyewe alisema kwamba inawezekana mtu mwingine “akaitwaa taji yako.” Alisema hivi pia katika maneno yake juu ya “umalizio wa mfumo wa mambo”: “Yeye ambaye amevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Waebrania 6:4-6, NW; Ufunuo 3:11; Mathayo 24:3, 13, NW) Msimamo tulio nao sasa mbele za Mungu ndio unaoangaliwa, si ule tuliokuwa nao zamani, uwe ulikuwa mwema au mbaya. (Ezekieli 33:12-16) Hiyo ndiyo sababu ni lazima tuendelee kujitahidia mahubiri ya ufalme, tuendelee kuzoea mwenendo unaofaa, kisha tufanye mambo hayo yote mawili tukiwa na woga unaofaa wa kuangalia tusije tukapungukiwa.

10. Ni mapambo gani yanayopasa kuambatana na mafundisho yetu, na matokeo yatakuwa nini?

10 Wakristo wanaonywa kwa upole ‘wawe wenye kiasi, timamu katika akili, wastahivu katika tabia, si wachongezi wala wenye kunywa kwa wingi sana, wenye upendo katika mahusiano ya kijamaa, safi katika mwenendo, safi katika usemi na wafanya kazi wazuri.’ Nayo sababu ni nini kwa hayo yote? “Ili neno la Mungu lisitukanwe.” Pia, ili kwa mwenendo wa namna hiyo “wayapambe mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote.” Kwa kuongeza mapambo hayo ya mwenendo mwema kwenye mahubiri yao, Mashahidi wa Yehova wanakuwa “kielelezo cha matendo mema.” (Tito 2:1-10) “Walio matajiri wa ulimwengu wa sasa uwaagize,” mtume Paulo akaamuru, “wasijivune, wala wasiutumainie utajiri usio yakini, bali wamtumaini Mungu atupaye vitu vyote kwa wingi ili tuvitumie kwa furaha. Watende mema, wawe matajiri kwa kutenda mema, wawe tayari kutoa mali zao, washirikiane na wengine kwa moyo; huku wakijiwekea akiba iwe msingi mzuri kwa wakati ujao, ili wapate uzima ulio kweli kweli.”​—1 Timotheo 6:17-19.

11. Ni uhitaji gani wa lazima unaotimizwa na maisha haya ya sasa, yajapokuwa yana siku chache zenye kujawa na taabu?

11 Maisha ya sasa yanayofuatwa na ulimwengu si maisha ya kweli kweli. “Yeye asiyejizuia nafsi yake [katika kutosheleza uchu wake] amekufa ingawa yu hai.” (1 Timotheo 5:6) Walakini, maisha haya yanatimiza uhitaji huu mkuu, yaani, ‘kuwa matajiri kwa kutenda mema,’ ‘kujiwekea akiba iwe msingi mzuri kwa wakati ujao,’ ‘kushika kwa imara uzima ulio kweli kweli’ katika milki ya ufalme wa Yehova utakaosimamiwa na Kristo. Tungeweza kuwa na vitu vyote vinavyoweza kupatikana katika maisha ya sasa, lakini maisha hayo yakiwa matupu bila kazi njema yangekuwa yamepotezwa bure na hayangefaa kitu. Siku za maisha ya sasa ni chache tena zimejawa na taabu na maumivu, huzuni na mateso, kihoro na mambo yenye kukatisha tumaini, uovu na kifo. Siku ni chache, lakini tunazo za kutosha tuweze kuwa matajiri katika kazi njema kama hatutakawia. Kufanya kazi hizo kunatuletea furaha na uradhi, amani na kutosheka, kujisikia kwamba maisha yana maana na kusudi, kupata afya ya kiroho na uzima wa milele.

Kazi ya Kuburudisha Kuelekea Wokovu

12. Ni jambo gani linalokuwa la kuwamaliza nguvu Mashahidi wa Yehova waaminifu, lakini ni nini kinachowapa burudisho?

12 Ingawa huenda likaonekana kuwa jambo la ajabu, kuacha kuutangaza ufalme wa Yehova nyakati hizi zenye ubaridi na upinzani mwingi kunaweza kuwamaliza nguvu Mashahidi wa Yehova wenye uaminifu wa kazi. Wanaposema wanapata kitulizo na burudiko. Wakati Yeremia alipoamua kutokuhubiri, ujumbe wenyewe ulikuwa kama moto ndani ya mifupa yake, na mwishowe alipaza sauti akisema: “Nimekwisha, nikawa hoi kwa kuufungia ndani—siwezi kuvumilia hivyo.” (Yeremia 20:9, An American Translation) Elihu alikihitaji kitulizo cha kunena kweli ambazo alikuwa amezifungia ndani yake kwa muda mrefu: “Mimi nimejaa mambo ya kusema, na akili yangu yanihimiza mimi niseme. Akili yangu ni kama divai iliyofungiwa ndani ya chupa, iliyo tayari kujitupa nje kwa nguvu, kama chupa mpya-mpya. Lazima nijiondolee mkazo huo kwa kunena.” (Ayubu 32:18-20, Moffatt) Baada ya kufanya kazi hiyo Elihu aliburudika. Mungu aliburudika alipomaliza kazi yake ya uumbaji. Kwa Yesu, kufanya kazi ya Yehova kulikuwa kama chakula chenye kuburudisha. Na kutimiza kazi ya kuhubiri sasa kunaburudisha Mashahidi wa Yehova. ‘Wanapanda juu kwa mbawa kama tai.’​—Isaya 40:31.

13. Huu ndio wakati wetu kufanya nini, na kufanya hivyo kunasaidia nani na kwa njia gani?

13 Huu ndio wakati wa kujifunza Neno la Mungu Biblia, kuacha kulingana na mtindo wa huu mfumo mwovu wa zamani, wakati wa kugeuzwa kwa kubadili nia yako. “Msiwe mkipenda wala ulimwengu wala vitu vilivyomo katika ulimwengu.” “Ulimwengu unapita na ndivyo na tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:15, 17, NW; Warumi 12:2, NW) Jipatie utayari wa kufariji waombolezao kwa habari njema za ufalme wa Mungu. Pamba mafundisho yako kwa kuzaa matunda ya kiroho katika maisha yako ya kibinafsi​—“upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza.” (Wagalatia 5:22, 23, NW) Saidia wapole wabadili nia zao, wawe matajiri katika kazi njema, kisha wabaki milele katika dunia ya paradiso. (Zaburi 37:11, 29) Wasaidie watimize wokovu wao huku wewe ukiendelea kujitimizia wako mwenyewe.

14. (a) Ni onyo gani la upole linaloonyesha namna ya kupata wokovu linalotolewa, na kwa sababu gani linafaa sana sasa? (b) Tukitumia onyo hilo lituhusu sisi binafsi, tunaweza kuwa nini na kufanya nini?

14 Hizi ni siku za hatari na wakati umepunguzwa, kwa hiyo Mungu anaonya hivi kwa upole: “Lihubiri neno, uwe ukifanya hivyo kwa haraka katika majira yenye kufaa, katika majira yenye matata.” “Mwe imara, bila kuondoleka, sikuzote mwe na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, mkijua kwamba kazi yenu yenye bidii si ya bure kuhusiana na Bwana.” “Msitange-tange katika kazi yenu. Mpashwe moto kwa roho. Mtumikieni Yehova.” (2 Timotheo 4:2; 1 Wakorintho 15:58; Warumi 12:11, NW) Kwa njia zote hizo “utimizeni wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka . . . mpate kuwa wana wa Mungu wasio na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka; ambao kati ya hao mnaonekana kuwa kama mianga katika ulimwengu, mkishika [sana] neno la uzima.”​—Wafilipi 2:12, 15, 16.

—Kutoka The Watchtower, August 1,1982.

◻ Kazi za Yehova zinamsifu namna gani?

◻ Ni dhabihu za namna gani zinazokubalika kwa Mungu leo?

◻ Tunaweza kufanyaje iwe rahisi kwa wengine kuukubali ujumbe wa Ufalme?

◻ Ni kwa kazi njema gani tunahitaji kupamba kufundisha kwetu?

◻ Ni utendaji gani unaoburudisha watumishi wa Mungu?

◻ Huu ndio wakati wa kuwa tukifanya nini?

[Blabu katika ukurasa wa 10]

Je! tunafanya uchunguzi na kufikiria sana maneno ya kweli, tuyaseme kwenye nyumba za watu ipendezavyo?

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Kazi za kufuata yale tunayoyahubiri zinahitajiwa kabisa tusije tukalaumiwa kuwa wanafiki

[Picha katika ukurasa wa 9]

Kazi za Yehova zinazostaajabisha zinaonyesha yeye ni Mungu wa namna gani. Kazi zetu zinaonyesha sisi ni watu wa namna gani

[Picha katika ukurasa wa 11]

Kueleza wengine kweli za Biblia ni kazi yenye kuburudisha

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki