‘Kufanya Kazi Kwa Bidii na Kujikaza
“Tunafanya kazi kwa bidii na kujikaza, kwa sababu tumeweka tumaini letu katika Mungu aliye hai, ambaye ni Mwokozi wa watu wa namna zote, hasa wa waaminifu.”—1 Tim. 4:10, NW.
1-3. Sababu gani inafaa kwa Wakristo leo kukaza fikira juu ya maoni yao kuelekea kazi?
JE! UNAFURAHIA kufanya kazi kwa bidii? Je! unathamini jitihada na matendo yanayostahilisha? Iwapo ndivyo, unatofautiana sana na wengi leo.
2 Pengine umekwisha kuona kwamba, ingawa sikuzote kumekuwako watu wavivu, inaelekea kutopenda kazi kunaongezeka. (Mit. 20:4; 19:24; 2 The. 3:11) Twaona jambo hilo katika mashauri kama vile, ‘Usijisumbue. Usijitaabishe.’ Jambo ambalo linaanza kama kutopenda kazi yenye kuchosha linaweza kwa urahisi kuwa kuchukia kazi yo yote.
3 Tukiwa Wakristo, bila shaka twaona kwamba hatuna roho hiyo. Hata hivyo, ungekuwa upumbavu kuwa na maoni kwamba jambo hilo haliwezi kutupata wakati ulimwengu wote una maoni hayo yenye nguvu, tena yenye kuenea pote. Kwa kuchunguza maoni yetu juu ya kazi pindi kwa pindi tunaweza kufaidika, maana tuliyo nayo yaweza kuwa na matokeo juu ya sehemu yetu katika utendaji wa Kikristo ulio wa maana kwa Mungu.
WAFANYA KAZI WA KUIGWA
4. Kazi ni ya maana kadiri gani?
4 Watu wengi ambao wamechunguza maisha na ubora wayo wametoa maelezo juu ya maana ya kazi. Mkuu wa kiserikali Mjeremani Karl W. von Humboldt alisema hivi: “Kazi ni ya lazima kwa mwanadamu kama vile kula na kulala,” Kweli hiyo peke yake inawapa watu wengi sababu ya kufanya kazi na kufanya mambo. Hata hivyo, Wakristo wana sababu nyingine ya kusitawisha kuthamini kazi ya bidii: Katika jambo hilo, Yehova na Yesu Kristo wametuwekea mfano tunaopaswa kufuata.—Efe. 5:1; 1 Kor. 11:1.
5, 6. Kwa habari ya kazi Yehova na Yesu wanaweka mfano gani?
5 Ulimwengu wote mkubwa mno—tangu jua lenye kutoa joto jingi la nuklea mpaka kipepeo dhaifu—unashuhudia kwamba Mungu ni mfanya kazi. Viumbe vyake vyote vinavyoonekana ni “kazi” zake. Vilevile, kulinda na kuongoza watumishi wake wakati wote ni “kazi” tunazopaswa kuthamini. (Zab. 145:4-6, 10, NW; 8:4-9) Mwanawe, vilevile, ni mfanya kazi mwenye bidii. Baada ya kuacha useremala katika mji mmoja wa Galilaya, Yesu alisafiri mamia ya maili katika pande za mashambani zenye joto na vumbi ili asaidia watu—aponye, ahubiri, afundishe. (Mt. 4:17, 23-25; Luka 8:1; 9:57, 58) Ingawa alikuwa mkamilifu, Kristo alichoka na kuona njaa kwa kufanya kazi kwa muda mrefu hata usiku.—Mt. 21:18; Marko 1:32, 35; 6:32-34; Yohana 4:3-6, 34.
6 Basi tunaweza kuwa na hakika kwamba wala Mungu wala Yesu hawana maoni ya ‘usijisumbue.’ Kristo alisema hivi: “Baba yangu anatenda kazi hata sasa, nami ninatenda kazi.” (Yohana 5:17) Kwa kweli, alieleza kwamba “kazi” zake—alizofanya kwa kutegemezwa na Mungu alizofanya kwa kutegemezwa na Mungu—zilitoa ushuhuda kwamba alikuwa na kibali ya Mungu. (Yohana 10:25, 38) Nalo jambo hilo linahusika maishani mwetu. Kutimizwa kwa matumaini yetu yote yenye msingi wa Biblia kunategemea yote aliyofanya Yesu akiwa mwabudu wa Mungu mwenye kufanya kazi kwa bidii.
7. Twapaswa kuchunguzaje maoni yetu juu ya kazi?
7 Kila mmoja wetu anaweza, na anapaswa, kufikiria maoni na kiolezo chake kuhusiana na kazi. Katika jambo hilo hatupaswi kujilaumu vikali au kutaka mengi mno kutoka kwetu. Sisi sote tuna vizuizi vya kimwili pamoja na hali zenye kuzuia. Vilevile, mwendo wa Yesu unaonyesha kwamba kwa kufaa tunaweza kufurahia kupumzika, kustarehe, ushirika mzuri na raha fulani. (Marko 6:31; Luka 5:29; 7:34; Yohana 2:2-10; 12:2, 3) Walakini kutokamilika kunakokazia uhitaji wetu wa kupumzika kunaweza kutusukuma tufanye kupumzika kupite kiasi, kama inavyokaziwa na maonyo ya Biblia juu ya uvivu. Ukweli ni kwamba, kama vile kuwa na njaa kunavyofanya chakula kiwe kitamu zaidi, ndivyo kazi ya bidii inavyofanya kupumzika na kustarehe kufurahishe zaidi.—Mhu. 2:24; 5:12, 18.
8, 9. Wakristo wanapaswa kuwa wafanya kazi wa bidii wakati gani?
8 Neno “kazi” laweza kutukumbusha hasa kazi ya kimwili ambayo wengi wetu tunafanya ili tupate vitu vya lazima maishani. Shauri la Biblia laonyesha kwamba twapaswa kuwa waaminifu, wenye kujitahidi katika hilo. (Mit. 10:4; 22:29) Vilevile, hiyo yapaswa kuwa hivyo katika kazi zetu za nyumbani au hata katika masomo yetu ya shuleni, maana sehemu zote za maisha yetu zaweza kuonyesha maendeleo tuliyofanya kwa kutumia kanuni za Kikristo. Mtume Paulo aliandika hivi: “Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa [Yehova], wala si kwa wanadamu, mkijua ya kuwa mtapokea kwa [Yehova] ujira wa urithi.”—Kol. 3:23, 24.
9 Walakini, tuelekeze fikira sasa juu ya sehemu moja ya maisha ya Mkristo—kumsifu Mungu kwa kuhubiri na kufundisha. Kazi hiyo ni ya maana, kwa kuwa kupitia kwayo ‘tunaweza kujiokoa na wale wanaotusikia.’—1 Tim. 4:16.
10, 11. Tuna sababu gani za pekee za kufanya kazi kwa bidii katika kueneza imani ya Kikristo?
10 Angalia kwamba Paulo hakusema kwamba Mkristo apendezwe na wokovu wake tu. Anapaswa kuhangaikia kusaidia wengine wakubali Yesu kuwa Kristo na kuzoea utawa ambao “unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.” (1 Tim. 4:8) Baada ya kutaja taraja hilo, Paulo aliandika hivi:
“Kwa kuwa kwa kusudi hilo tunafanya kazi kwa bidii na kujikaza, kwa sababu tumeweka tumaini letu katika Mungu aliye hai, ambaye ni Mwokozi wa watu wa namna zote, hasa wa waaminifu.”—1 Tim. 4:10, NW.
11 Wazia hilo. Wokovu kutoka kwa Mungu—uzima wa milele katika furaha—unaweza kupatikana na “watu wa namna zote.” Walakini mwishowe ni nani watakaookolewa? Ni wale “waaminifu” peke yao, wale wanaositawisha na kuonyesha imani. Akithamini jambo hilo, mtume huyo hangeweza kuchukua mambo vivi hivi, akiishi maisha ya kawaida na nyakati nyingine, ikifaa, kuzungumza na wengine juu ya wokovu huo unaoweza kupatikana. Hasha! taraja la kuwa wengine wangeweza kujifunza ujumbe huo wa Kikristo na kuingia katika njia ya wokovu lilimvutia Paulo sana, la maana sana sana, hata akawa ‘anafanya kazi kwa bidii na kujikaza.’ Ndivyo unavyoona jambo hilo? Wewe binafsi fikiria mwendo wako wa utendaji katika mwezi uliopita au miezi sita iliyopita. Je! ni wazi kabisa kwako—na kwa wengine, hata na Mungu—kwamba unafanya kazi kwa bidii, ukijikaza?
KUFANYA KAZI KWA BIDII ILI KUENEZA UJUMBE WA UFALME
12. Kazi zinahusianaje na wokovu?
12 Wakristo wanajua kwamba hawawezi kuokolewa kwa kufanya kazi fulani tu, kana kwamba kufanya hivyo kunawastahilisha haki na wokovu. (Rum. 3:28) Hata hivyo ni kweli kwamba tukiwa na imani ya kweli, tutazaa kazi zinazotokezwa na imani hiyo. (Yak. 2:18-26) Basi inafaa kufikiria imani yetu na kazi zetu kwa njia ya sala.
13. Kulingana na Yesu, wanafunzi wake wangefanyaje baada ya kufa kwake?
13 Kwa ‘kufanya kazi kwa bidii na kujikaza,’ kama Paulo, twaweza kushiriki kutimiza ukweli wa kiunabii uliosemwa na Yesu. Alisema nini? Alisema akijibu ombi la Filipo, “Utuonyeshe Baba.” (Yohana 14:8) Yesu alisema hivi:
“Aliyeniona mimi amemwona Baba; . . . Hayo maneno niwaambiayo mimi siyasemi kwa shauri langu; lakini Baba akaaye ndani yangu huzifanya kazi zake. Amin, amin, nawaambieni, Yeye aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba.—Yohana 14:9, 10, 12.
14, 15. Katika Yohana 14:12, je! Yesu, alimaanisha kwamba wafuasi wake wangefanya miujiza mikubwa zaidi? Sababu gani?
14 Wanafunzi wa Yesu wangewezaje kufanya kazi kubwa kuliko alizofanya? Je! wewe unaweza kushiriki katika kufanya kazi kubwa kuliko hizo? Biblia inafunua kwamba Mungu aliwezesha Wakristo fulani wafanye miujiza, kama vile kufukuza pepo, kuponya wagonjwa na, katika visa vichache, kufufua wafu. Mambo hayo yalikuwa ya kuonyesha kwamba sasa alikuwa anashughulika na kubariki kundi Kikristo. (Matendo 3:2-8; 5:12-16; 9:36-40; 16:16-18) Walakini je! kazi hizo zilikuwa kubwa kuliko hizo alizofanya Yesu? Yeye aliponya wote waliokuja kwake na hata wengine wakiwa mbali, akalisha maelfu kwa mwujiza, akafufua wafu na kuamuru bahari na upepo. (Mt. 8:5-16, 23-27; 14:14-33; Yohana 11:39-44) Na zaidi, karama za kimwujiza za roho ambazo Wakristo wengine walionyesha zingekwisha au zingepita. (1 Kor. 13:8-10) Kwa hiyo ni kwa njia gani Wakristo wangefanya kazi kubwa kuliko za Yesu?
15 Yesu alikuwa amesema yale ambayo Baba yake alitaka aseme. Alifanya wema mkuu zaidi, wenye kudumu, si kwa miujiza yake, bali kwa mafundisho yake bora juu ya Ufalme.a (Luka 4:32, 43) Baada ya kufufuliwa Yesu aliwapa wafuasi wake mgawo wa kumwiga, ‘wafanye watu wa mataifa yote kuwa wanafunzi, kuwafundisha. (Mt. 28:19, 20, NW) Ndiyo, Wakristo wangefanya kazi kubwa ya kutoa ushuhuda. Ingekuwa yenye kadiri kubwa kuliko kuhubiri kwa Yesu, kwa wakati mrefu zaidi na kufikia watu wengi zaidi. Kwa njia hiyo wangefanya kazi kubwa kuliko hizo alizofanya.
16. Je! kazi ya Yesu ingekomeshwa na kufa na kupaa kwake kwenda mbinguni?
16 Kazi ya kuhubiri na kufundisha juu ya Ufalme ambayo Yesu alifanya haingekoma wakati wa kufa na kupaa kwake mbinguni. Akiwa huko angeendelea kuongoza kazi ya maana ya kutoa elimu, walakini akifanya hivyo kupitia kwa wafuasi wake. Luka anaendelea kusema kwamba kabla Yesu hajapaa mbinguni aliwaambia wanafunzi wake mengi zaidi ‘kuhusu ufalme wa Mungu.’ (Matendo 1:3) Mwishowe, aliwaambia hivi: “Mtakuwa mashahidi wangu mimi katika Yerusalemu na katika Yudea yote na katika Samaria na kwenye sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”—Matendo 1:8, NW.
17, 18. Katika siku ya Pentekoste 33 W.K., wafuasi ya Yesu walianzaje kutimiza maneno yake yaliyohusu kazi kubwa zaidi?
17 Baada ya muda mfupi wakaanza kufanya kazi kubwa kuliko za Yesu. Katika siku ya Pentekoste 33 W.K. Yesu alimwaga roho takatifu juu ya wanafunzi 120 waliokuwa wanangojea katika Yerusalemu. Kisha wakafanya nini? Kuzidisha chakula? Kufunza watu juu ya ukulima? Hata kuponya watu wagonjwa? Hapana, walianza kunena, kutangaza “matendo makuu ya Mungu.” (Matendo 2:1-11) Kisha mtume Petro akatoa ushuhuda wenye kusadikisha sana hata kwamba maelfu ya wasikilizaji wake wakamkubali Kristo.
18 Lazima iwe ilikuwa kazi kweli kweli kubatiza waamini wapya wengi siku hiyo. Inawezekana, walitawanyika kwenye vidimbwi katika mji wote. Kwa wazi mwishoni mwa siku wanafunzi hao waliripoti juu ya waliyokuwa wamefanya, maana masimulizi yanasema kwamba ‘waliolipokea neno lake wakabatizwa; siku ile wapata watu elfu tatu.’ Toka watu 120 mpaka zaidi ya 3,000 (ongezeko la asilimia zaidi ya 2,500) kwa siku moja. (Matendo 1:15; 2:41) Kweli kweli walikuwa wameanza kufanya kazi kubwa kuliko hizo alizofanya Yesu.
19. Je! hiyo ni kazi ambayo ingefanywa na mitume au wazee tu katika makundi?
19 Lakini huenda Wakristo wengine leo wakaona hivi, ‘Mimi si Petro wala Paulo. Wao ndio wangeweza kufanya kazi kubwa zaidi ya Yesu, sivyo? ’ Hilo ni ulizo linalofaa. Kitabu cha Matendo kinaonyesha kwamba mitume, waenezaji wa Injili wa pekee na wazee wa kiroho katika makundi kwa hakika walishiriki katika kuuhubiri Ufalme. Walakini angalia jambo hili la kweli linalosimuliwa na mwanafunzi Luka: “Siku hiyo [kundi] la Yerusalemu lilianza kuteswa vibaya. Waamini wote, isipokuwa tu wale mitume walilazimika kuwanyika katika sehemu za mashambani za Yudea na Samaria.” (Matendo 8:1, HNWW) Nao Wakristo hao waliotawanywa, vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake, walifanya nini? “Wale waliotawanyika wakaenda huko na huko wakilihubiri neno.” (Matendo 8:4) Ndiyo, wote walihubiri.
20. Sababu gani sasa ni jambo la maana sana sana tufikirie kushiriki katika kutimiza Yohana 14:12?
20 Leo Wakristo wa kweli wanaendeleza kuhubiri na kufundisha ambako Yesu alianzisha na ambako ndugu na dada zao wa karne ya kwanza waliendeleza. Walakini matukio ya kisasa yanayotimiza unabii wa Biblia yanatuonyesha kwamba karibuni Mungu atakomesha taratibu mbovu ya mambo iliyopo, hivyo amalize kuhubiri kwa kisasa kwa “habari njema hizi za ufalme.” (Mt. 24:14, NW) Kwa hiyo, kila mmoja wetu anaweza kuuliza hivi, ‘Je! mimi kwa sasa ninashiriki kabisa katika kazi hii ya maana ambayo Yesu alisema juu yake katika Yohana 14:12? Je! ninafanya kazi kwa bidii na kujikaza? Kazi hiyo itakapomalizwa, je! nitatosheka kwamba nilishiriki kikamilifu?’
MUNGU ANATAZAMIA MENGI KADIRI GANI?
21-23. Twaweza kufanya uchanganuzi gani kwa habari ya hali zetu?
21 Ili kushiriki katika njia yenye kutosheleza katika kazi ya Kikristo ya kuhubiri, hatupaswi kupuza matakwa ya lazima ya Kimaandiko kuhusiana na jamaa yetu, watu wa ukoo, kazi au shule. (1 Tim. 5:8) Naye Mungu asingetaka tujione kuwa na hatia katika kutimiza matakwa hayo; twapaswa kufanya hivyo kwa furaha. Lakini nyakati nyingine sisi tunaweza kufikiria kwa uzito wakati na utendaji wetu.
22 Wengi wetu tunaweza kufaidika kutokana na kujichunguza na kujiadibisha kwa kusawazika. Pengine kuondoa mambo mengine yasiyo ya lazima ili kuendelea kuishi kwa njia nzuri kunaweza kusaidia.
23 Hakuna mtu anayepaswa kulaumu yale ambayo wengine wanafanya kuhusiana na jambo hilo. Jambo la maana ni kuchanganua kama sisi binafsi tunaonyesha kuthamini sana sehemu yetu katika kufanya kazi kubwa kuliko hizo alizofanya Yesu.
24. Mjane maskini alituwekea mfano gani mzuri?
24 Pengine tunafanya yote tuwezayo, ingawa yanakuwa machache kuliko yale ambayo afya na hali za mwingine zinamruhusu kufanya. Walakini wingi peke yake sio njia ya kukadiria. Ebu kumbuka pongezi ya Yesu juu ya mjane maskini aliyechanga sarafu mbili za thamani ndogo sana. Sarafu hizo (leptas) thamani yake ilikuwa 1 kwa 64 ya mshahara (malipo) wa siku moja. Ni nini thamani ya hiyo mahali unapoishi? Hata hivyo Yesu alipongeza mwendo wake, maana ‘alitia vyote alivyokuwa navyo, ndiyo riziki yake yote pia.’ (Marko 12:41-44) Vilevile tunaweza kuwa na hakika tutapata kibali iyo hiyo tukitoa yote—tukifanya kazi kwa bidii na kujikaza—katika kazi ya kutoa ushuhuda.
25. Mariamu alimfanyia Yesu nini muda mfupi kabla ya kufa kwake?
25 Vilevile tunaweza kukumbuka wakati Mariamu, dada ya Lazaro, alipompaka Yesu mafuta yenye manukato ya bei kubwa. Wanafunzi wengine walilalamika, maana mafuta hayo yalikuwa yenye thamani ya dinari 300. Pakiwa na sabato na sikukuu, huo ndio uliokuwa mshahara wa mfanya kazi kwa mwaka mzima. Je! wewe, mshiriki mmoja wa jamaa, mshahara wako wa mwaka mzima ni nini? (Yohana 12:3-8; Mt. 20:2) Yesu alisema hivi kuhusiana na jitihada ya Mariamu:
“Amenitendea kazi njema. . . . Ametenda aliyoweza; ametangulia kuupaka mwili wangu marhamu kwa ajili ya maziko. Amin, nawaambia, Kila ihubiriwapo Injili katika ulimwengu wote, na hili alilotenda huyu litatajwa kwa kumbukumbu lake.”—Marko 14:6-9.
26, 27. Mariamu alikuwa mfano mzuri kwa njia gani!
26 Angalia maneno hayo, “Ametenda aliyoweza.” Hakuna ushuhuda kwamba Mariamu alikuwa amepewa uwezo wa kufanya miujiza; yeye hakuwa mtume, wala mzee wakati kundi la Kikristo lilipoanzishwa; na huenda hakuweza kusafiri sana akiwa na “habari njema.” Walakini ‘alitenda aliyoweza.’ Maana yake hiyo ni nini? Katika lugha fulani usemi “Fanya uwezayo” unamaanisha ‘Usijitaabishe; usijisumbue.’ Hata hivyo Yesu hakumaanisha hivyo. Mariamu alikuwa amejitoa kabisa. Tafsiri fulani za Biblia zimetafsiri maneno hayo kuwa, “Amefanya yote ambayo angeweza kufanya kwa uwezo wake.”—W. Barclay.
27 Kujitoa kabisa kwa Mariamu kulikuwa jambo lenye kuendelea, wala si tendo la wakati mmoja. Mapema Mariamu alikuwa ameonyesha moyo wake ulipokuwa kwa kuketi miguuni pa Yesu apate kusikiliza mafundisho yake. (Luka 10:38-42) Sasa akaendelea kuunga mkono mhubiri huyo mwenye kutokeza, Yesu. Na, kwa kupendeza, Yesu akahusianisha tendo la Mariamu na kazi ya kuhubiri ya ulimwenguni pote, akasema kwamba po pote “habari njema” zingeenezwa angekumbukwa. Mariamu alikuwa anapendezwa na kuhubiri huko. Yesu pia, hata kufikia kufa kwake.
28. Ukristo ni dini ya namna gani, nalo hilo likiwa na maana gani kwetu?
28 Je! sisi tuko kama wanawake hao wawili waliotoa vyote? Je! tunapendezwa sana na kazi ya kuhubiri ambayo Yesu alianzisha alipokua duniani na ambayo sasa inaendelezwa na Wakristo duniani pote? Inapasa kuwa hivyo. Ndivyo ilivyo kwa Mungu. Ukristo ulipoanza katika siku ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K., ulikuwa ni dini yenye kutoa ushuhuda, naye Mungu aliutegemeza kupitia kwa roho yake. Yeye angali anafanya hivyo, maana yeye hajabadilika. Yeye ni “Mungu aliye hai,” akiwa yu hai mwenyewe na mwenye kutoa uhai kwa waabudu wake wa kweli. Kwa hiyo Ukristo leo unapasa kuwa dini yenye kutoa ushuhuda, na ndivyo ulivyo hata sasa. Nao Wakristo wana kila sababu ya kuwa wafanya kazi wenye shauku katika utumishi wa Mungu, “ambaye ni Mwokozi wa watu wa namna zote, hasa wa waaminifu.”—1 Tim. 4:10, NW.
[Maelezo ya Chini]
a Kazi zenye nguvu za Yesu zilichochea wengi wapendezwe naye. Hata hivyo ni Jambo linalofaa kuangaliwa kwamba hakupata kujulikana kama “Mfanya-miujiza” au kama hivyo. Kwa kutokeza zaidi, yeye alipata kujulikana kuwa “Mwalimu.”—Mt. 8:19: 19:16; 26:18; Marko 4:38; Yohana 3:2.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Walifanya yote waliyoweza