Mwenye Shughuli Katika Kazi Zisizo Hai au Katika Utumishi wa Yehova?
“POLE, lakini nina shughuli.” Hilo ni mojawapo vipingamizi ambavyo Mashahidi wa Yehova hukabili wanapohubiri peupe habari njema za Ufalme. (Mathayo 24:14) Na ijapokuwa dai la “nina shughuli” nyakati nyingine huwa udhuru tu, ukweli ni kwamba watu wengi ni wenye shughuli. Kwa kweli wamemezwa na “shughuli za dunia”—mibano ya kupata riziki, kulipa gharama, kwenda na kurudi kutoka kazini, kulea watoto, kutunza nyumba, gari, na mali nyinginezo.—Mathayo 13:22.
Hata hivyo, ingawa watu huenda kwa kweli wakawa wenye shughuli, wachache hushiriki katika kazi ambazo kwa kweli ni zenye kuzaa matunda au zenye matokeo. Ni kama vile yule mwanamume mwenye hekima Sulemani alivyoandika wakati mmoja: “Mtu hupata nini kwa kazi yake yote, na kwa juhudi ya moyo wake alivyojitahidi chini ya jua? Kwa kuwa siku zake zote ni masikitiko, na kazi yake ni huzuni; naam, hata usiku moyoni mwake hamna raha. Hayo nayo ni ubatili.”—Mhubiri 2:22, 23.
Biblia pia huita utendaji huo wa ubatili “kazi zisizo na uhai.” (Waebrania 9:14, NW) Je! kazi za jinsi hiyo hutawala maisha yako? Hilo lapasa kuwa jambo la kukuhangaisha sana ukiwa Mkristo, kwa maana Mungu ‘atalipa kila mtu sawasawa na haki yake.’ (Zaburi 62:12) Na kwa kuwa “muda ubakio si mwingi,” twapaswa hasa tuhangaike kwamba hatupotezi wakati na kazi zisizo na uhai. (1 Wakorintho 7:29) Lakini ni nini hasa kazi hizo zisizo na uhai? Twapaswa kuzionaje? Na twaweza kuhakikishaje kwamba sisi ni wenye shughuli katika kazi zenye thamani ya kweli?
Kutambulisha Kazi Zisizo na Uhai
Kwenye Waebrania 6:1, 2, Paulo aliandika hivi: “Kwa sababu hiyo, tukiacha kuyanena mafundisho ya kwanza ya Kristo tukaze mwendo ili tuufikie utimilifu; tusiweke msingi tena wa kuzitubia kazi zisizo na uhai, na kuwa na imani kwa Mungu, na wa mafundisho ya mabatizo, na kuwekea mikono, na kufufuliwa wafu, na hukumu ya milele.” Ona kwamba “mafundisho ya kwanza” yalitia ndani “kuzitubia kazi zisizo na uhai.” Wakiwa Wakristo wasomaji wa Paulo walikuwa tayari wamezitubia kazi hizo zisizo na uhai. Kwa jinsi gani?
Kabla ya kumkubali Kristo, wengine katika karne ya kwanza walikuwa wameshiriki katika “matendo ya mwili” yasiyo na uhai, yaani, “uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi,” na matendo mengine mabaya. (Wagalatia 5:19-21) Ikiwa kazi hizo hazikuzuiwa zingeongoza kwenye kifo chao cha kiroho. Lakini kwa rehema, Wakristo hao walikuwa wamegeuka kutoka kwa mwendo wao wa uharibifu, wakatubu, na ‘kuoshwa.’ Hivyo walionea shangwe msimamo safi pamoja na Yehova.—1 Wakorintho 6:9-11.
Lakini, si Wakristo wote walihitaji kutubu kutoka kwa kazi zilizokuwa mbovu au zenye kukosa adili. Barua ya Paulo ilielekezwa hasa kwa Wayahudi waamini, wengi wao ambao bila shaka walikuwa wameshikamana sana na Sheria ya Musa kabla ya kumkubali Kristo. Basi, wao walikuwa wametubia kazi zipi zisizo na uhai? Kwa hakika hakukuwa kosa lolote kufuata kwao kawaida za dini na matakwa ya Sheria juu ya chakula. Je! Sheria haikuwa, “takatifu, na ya haki, na njema”? (Warumi 7:12) Naam, lakini kwenye Warumi 10:2, 3, Paulo alisema hivi kuhusu Wayahudi: “Kwa maana nawashuhudia kwamba wana juhudi kwa ajili ya Mungu, lakini si katika maarifa. Kwa maana, wakiwa hawaijui haki ya Mungu, na wakitaka kuithibitisha haki yao wenyewe, hawakujitia chini ya haki ya Mungu.”
Naam, Wayahudi waliamini kwa kosa kwamba kwa kufuata Sheria kwa makini, wao wangeweza kustahili wokovu wao. Lakini, Paulo alieleza kwamba “mwanadamu hahesabiwi haki kwa matendo ya sheria, bali kwa imani ya Kristo Yesu.” (Wagalatia 2:16) Baada ya fidia ya Kristo kuandaliwa, kazi za Sheria—zijapokuwa za uchaji Mungu au za heshima jinsi gani—zilikuwa kazi zisizo na uhai na zisizo na thamani yoyote katika kupata wokovu. Hivyo Wayahudi wenye mioyo ifaayo walitafuta kibali cha Mungu kwa kuzitubia kazi hizo zisizo na uhai na kubatizwa ili kuonyesha toba yao.—Matendo 2:38.
Tunajifunza nini kutoka kwa jambo hilo? Kwamba kazi zisizo na uhai huenda zikatia ndani zaidi ya matendo maovu au yasiyo ya kiadili; zinatia ndani kazi yoyote isiyo na uhai kiroho, ya ubatili, au isiyo yenye kuzaa matunda. Lakini je, Wakristo wote hawazitubii kazi hizo zisizo na uhai kabla ya ubatizo wao? Ni kweli, lakini baadhi ya Wakristo katika karne ya kwanza walirudia tena mwenendo wenye kukosa adili. (1 Wakorintho 5:1) Na miongoni mwa Wakristo Wayahudi, kulikuwa na mwelekeo wa kurudia kuzoea kazi zisizo na uhai za Sheria ya Musa. Paulo alihitaji kuwakumbusha watu kama hao wasirudie kazi zisizo na uhai.—Wagalatia 4:21; 5:1.
Kujilinda Dhidi ya Kazi Zisizo na Uhai
Kwa hiyo ni lazima watu wa Yehova leo wawe waangalifu wasinaswe na mtego wa kazi zisizo na uhai. Kwa kweli tunashambuliwa kutoka pande zote na mibano ya kuridhiana kiadili, kutofuatia haki, na kushiriki katika matendo ya mwenendo mbaya wa kingono. Kwa kusikitisha, maelfu ya Wakristo kila mwaka hushindwa na mibano hiyo, na wakikosa kutubu, wao huondoshwa katika kundi la Kikristo. Basi, zaidi ya wakati mwingine wowote, ni lazima Mkristo atii shauri la Paulo kwenye Waefeso 4:22-24: “Mvue kwa habari ya mwenendo wa kwanza utu wa zamani, unaoharibika kwa kuzifuata tamaa zenye kudanganya; na mfanywe wapya katika roho ya nia zenu; mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.”
Bila shaka, Waefeso ambao Paulo aliandika kwao walikuwa tayari wamevaa utu mpya kwa kadiri kubwa. Lakini Paulo aliwasaidia wafahamu kwamba kufanya hivyo kulikuwa jambo la kuendelea! Bila jitihada ya kuendelea, Wakristo wangerudishwa kwenye kazi zisizo na uhai na tamaa zenye kudanganya zinazoendelea kuwako zikiwa uvutano wenye kufisidi. Hali ndiyo iyo hiyo leo. Ni lazima tujitahidi daima kuvaa utu mpya, tusiuruhusu uchafuliwe na vitabia vyovyote vilivyopatikana katika njia yetu ya maisha ya zamani. Ni lazima tuepuke—tuchukie—namna yoyote ya kazi za mwili zilizo mbovu. “Enyi mmpendao BWANA [Yehova, NW], uchukieni uovu,” ahimiza mtunga zaburi.—Zaburi 97:10.
Kwa kustahili pongezi, walio wengi wa watu wa Yehova leo wametii shauri hilo na wameendelea kuwa safi kiadili. Lakini, baadhi yao wamekengeushwa na kazi ambazo si mbaya zenyewe lakini ambazo hatimaye ni za ubatili na zisizozaa matunda. Kwa mfano, wengine wamejihusisha kabisa katika mipango ya kuchuma pesa au katika kupata vitu vya kimwili. Lakini Biblia huonya hivi: “Hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu.” (1 Timotheo 6:9) Kwa wengine, elimu ya kilimwengu imethibitika kuwa mtego. Ni kweli, kadiri fulani ya elimu ya kilimwengu huenda ikahitajiwa ili kupata kazi ya kuajiriwa. Lakini katika ufuatiaji wenye kutumia wakati mwingi wa elimu ya juu ya kilimwengu, wengine wamejidhuru wenyewe kiroho.
Naam, kazi nyingi huenda zenyewe zisiwe mbaya kiadili. Lakini hata hivyo zinakosa uhai ikiwa kwa kweli haziongezei uhai wetu sasa au kutupa sisi kibali cha Yehova Mungu. Kazi za jinsi hiyo hutumia wakati na nishati lakini hazitokezi manufaa za kiroho, hazitoi burudisho la kudumu.—Linganisha Mhubiri 2:11.
Bila shaka unajitahidi sana kuwa mwenye shughuli katika utendaji wa kiroho unaostahili. Lakini, inasaidia kujichunguza mwenyewe kwa ukawaida. Mara kwa mara, huenda ukajiuliza mwenyewe maswali kama vile: ‘Je! kushiriki kwangu katika utumishi wa shambani na kuhudhuria mikutano kunakatizwa kwa sababu nimechukua kazi ya kimwili isiyohitajiwa?’ ‘Je! nina wakati wa tafrija lakini wakati mchache wa funzo la kibinafsi na la familia?’ ‘Je! mimi hutumia wakati na nishati nyingi kutunza mali za kimwili lakini hushindwa kutunza wenye uhitaji walio kundini, kama vile wagonjwa na wazee-wazee?’ Majibu ya maswali hayo huenda yakafunua uhitaji kwa upande wako wa kutanguliza zaidi kazi za kiroho.
Endelea Kuwa Mwenye Shughuli Katika Utumishi wa Yehova
Kama vile 1 Wakorintho 15:58, NW, isemavyo, kuna “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” Ya kwanza kabisa ni kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Kwenye 2 Timotheo 4:5, Paulo alisihi hivi: “Fanya kazi ya kuhubiri Habari Njema iwe kazi yako ya maisha, katika utumishi wa kikamili.” (Jerusalem Bible) Wazee na watumishi wa huduma pia wana mengi ya kufanya katika kutunza mahitaji ya kundi. (1 Timotheo 3:1, 5, 13; 1 Petro 5:2) Vichwa vya familia—wengi wao ambao ni wazazi wasio na mwenzi wa ndoa—huwa pia na madaraka mazito katika kutunza familia zao na kusaidia watoto wao wakue katika uhusiano wao pamoja na Mungu. Kazi hiyo yaweza kuchosha, hata kulemeza, nyakati nyingine. Lakini tofauti na kuwa zenye kukosa uhai, kazi za jinsi hiyo huleta uradhi wa kweli!
Tatizo ni: Mtu aweza kupataje wakati wa kutimiza kazi hizo zote za lazima zenye kustahili? Kujitia nidhamu na kupanga mambo kibinafsi ni muhimu. Kwenye 1 Wakorintho 9:26, 27, Paulo aliandika hivi: “Mimi napiga mbio vivyo hivyo, si kama asitaye; napigana ngumi vivyo hivyo, si kama apigaye hewa; bali nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa.” Njia moja ya kutumia kanuni ya andiko hilo ingekuwa kuchunguza mara kwa mara utaratibu na mtindo-maisha wako binafsi. Huenda kwa kweli ukagundua kwamba waweza kuondo-lea mbali mambo yanayotumia wakati na nishati yako isivyohitajiwa.
Kwa mfano, je, nishati na wakati wako mwingi unatumiwa kwa kutazama televisheni, kwa tafrija, kwa kusoma vichapo vya kilimwengu, au kwa utendaji wa kujipendeza? Kulingana na makala moja katika The New York Times, mtu mzima wa wastani katika United States hujifurahisha kwa kutazama televisheni kwa muda wa “saa zipitazo kidogo 30 kila juma.” Kwa hakika wakati huo waweza kutumiwa kwa njia bora zaidi. Mke wa mwangalizi msafirio mmoja aripoti hivi: “Niliacha kabisa karibu kila kitu kipotezacho wakati, kama vile kutazama televisheni.” Tokeo likawa nini? Aliweza kusoma mabuku yote mawili ya ile ensaiklopidia ya Biblia Insight on the Scriptures!
Huenda wewe pia ukahitaji kufikiria ni kwa kadiri gani unaweza kurahisisha mtindo-maisha wako. Sulemani alisema hivi: “Usingizi wake kibarua ni mtamu, kwamba amekula kidogo, au kwamba amekula kingi; lakini kushiba kwake tajiri hakumwachi kulala usingizi.” (Mhubiri 5:12) Je! wakati na nishati yako nyingi hutolewa ili kutunza mali za kimwili zisizohitajiwa? Kwa kweli, kadiri tulivyo na mali zaidi, ndivyo tulivyo na vitu vingi zaidi vya kutunza, kulipia bima, kurekebisha, na kulinda. Je! ingekufaidi zaidi kuondolea mbali mali fulani?
Kuwa na ratiba inayofanya kazi ndiyo njia nyingine ya kutumia wakati wako vizuri zaidi. Ratiba ya jinsi hiyo yapasa itie ndani uhitaji wa mtu wa pumziko au tafrija. Lakini masilahi ya kiroho yapasa yatangulizwe. Wakati wapasa uwekwe kando kwa ajili ya kuhudhuria mikutano yote ya kundi kwa ukawaida. Huenda pia ukaamua kimbele ni siku au jioni zipi ziwezazo kutolewa kwa kazi ya kueneza evanjeli. Ukipanga kwa uangalifu, huenda hata ukaweza kuongeza ushiriki wako katika utumishi, labda kwa kutumikia ukiwa painia msaidizi mara kwa mara. Lakini, hakikisha kuratibu wakati kwa ajili ya funzo la kibinafsi na la familia, kutia ndani utayarishaji wa kikamili kwa ajili ya mikutano. Kwa kujitayarisha, hutajifaidi tu kutokana na mikutano bali utaweza ‘kuhimiza katika upendo na kazi nzuri’ kwa njia ya maelezo yako.—Waebrania 10:24.
Kupata wakati wa kujifunza huenda ukahitaji kudhabihu mambo fulani. Kwa mfano, familia za Betheli ulimwenguni pote huamka mapema kila asubuhi ili kuwa na mazungumzo ya andiko la siku. Je! wewe ungeweza kukomboa wakati mchache kila asubuhi kwa ajili ya funzo la kibinafsi? Mtunga zaburi alisema hivi: “Kutangulia mapambazuko naliomba msaada, naliyangojea maneno yako kwa tumaini.” (Zaburi 119:147) Bila shaka, kuamka mapema kungehitaji kuratibu wakati unaofaa wa kulala usingizi ili kwamba uweze kuanza siku ifuatayo ukiwa na afya na ukiwa umepumzika.
Manufaa za Kuwa Mwenye Shughuli Katika Utumishi wa Yehova
Kuwa na “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana” huhitaji kupanga mambo, kujitia nidhamu, na kujidhabihu. Lakini tokeo litakuwa kwamba utaonea shangwe manufaa zisizohesabika. Kwa hiyo endelea kuwa mwenye shughuli, si katika kazi zisizo na uhai au za ubatili zinazoleta tu utupu na uchungu, bali katika utumishi wa Yehova. Kwani ni kwa kazi za jinsi hiyo kwamba unadhihirisha imani yako, unapata kibali cha Mungu, na, hatimaye, kupata ile zawadi ya uhai wa milele!
[Picha katika ukurasa wa 28]
Kufanya ratiba inayofanya kazi kunasaidia Mkristo atumie wakati wake kwa hekima zaidi