Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 2/1 kur. 5-7
  • Kuivunja Minyororo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuivunja Minyororo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuogopa Kisichojulikana
  • Imani ya Mambo ya Ajabu
  • Je, Kuna Upatano Kati ya Ushirikina na Mafundisho ya Biblia?
    Amkeni!—2008
  • Dini ya Kweli Inafukuzia Mbali Woga Jinsi Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Je, Ushirikina Unaongoza Maisha Yako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Ushirikina—Mbona Umedumu Sana?
    Amkeni!—1999
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 2/1 kur. 5-7

Kuivunja Minyororo

KATIKA karibu kila sehemu ya dunia, ushirikina unazitawala maisha za watu wengi. Ijapokuwa Wazungu wengi wanaamini kwamba kiatu cha farasi au wayo wa sungura utawakinga, Waafrika wengi wanavaa hirizi katika shingo yao ili kuwakinga na roho mbaya. Kwa sababu iyo hiyo, wao vilevile wanafunga kamba ya kuwakinga katika kiwiko cha mkono wa mtoto mchanga aliyezaliwa. Makabila fulani yanaamini kwamba kufunga kipande kidogo cha mfupa wa sokwe-mtu kwenye kamba hiyo kutamfanya mtoto mchanga awe mkubwa na mwenye nguvu.

Watu wanaokaa kwenye mito wanaamini kwamba kuna mazimwi ya majini, yanayoitwa Mami Wata katika Jamhuri ya Afrika ya Kati. Hayo yanafikiriwa kuwa yana nywele ndefu za rangi ya shaba, na inaaminiwa kwamba mazimwi hayo yanashawishi watu waje karibu na maji yawakamate na kuwazamisha. Wengine wanafuata sana imani hiyo. Wanamimina matambiko ya vinywaji katika mto ili kutia moyo Mami Wata kukamata adui yao wakati mwingine atakapokuja kwenye ukingo wa mto.

Wa maana sana katika ushirikina wa Kiafrika ni mtu mwenye uwezo wa kutoa hirizi na mganga. Mtu mwenye uwezo wa kutoa hirizi anatupa nzeke (magamba au makombe madogo ya baharini) ili aone yatakayotokea wakati ujao. Mganga anatoa dawa ya upendo ili ahuishe upendo wa mwenzi unaofifia. Ikiwa umeme wa mvua unatokea karibu-karibu, inafikiriwa kwamba inaelekea mtu fulani ambaye umegombana naye amemwajiri mchawi ili amsaidie kujilipiza kisasi. Wengine wanaamini kwamba mchawi huyo anaweza kugeuza wanaume wawe wanawake, na wanawake wawe wanaume, hata kugeuza wanadamu wawe wanyama!

Kwa mshirikina, matukio yanakuwa na maana mbaya sana. Iwapo nyoka au kinyonga anaruka njia yako, nenda nyumbani upesi kabla jambo lo lote baya halijatokea. Ikitukia kwamba ndege anaruka kuingia katika nyumba yako, mtu fulani atafia humo. Ikiwa mbwa wanapiga makelele mengi mno usiku, mtu fulani anakaribia kufa, au amekufa sasa hivi.

Huenda mambo hayo ya ushirikina yakaonekana kuwa ya kipumbavu kwa watu wenye elimu katika Afrika na katika sehemu nyingine za ulimwengu. Lakini namna gani watu wenye elimu ambao kwa uangalifu wanaepuka kutembea chini ya ngazi, wanafuta safari isiyo ya lazima Ijumaa ya tarehe kumi na tatu, wanamwalika mgeni bila taarifa ya mapema ili aepuke kukalia kiti cha kumi na tatu kwenye chakula kikuu au wanaotazama falaki (au nyota) yao katika gazeti la asubuhi? Je! Hao vilevile hawako katika minyororo ya ushirikina?

Lakini ushirikina ni nini? Na ni nini kinachouwezesha upate kutawala watu?

Kuogopa Kisichojulikana

Ushirikina unafasiliwa kuwa “kuamini au zoea linalotokana na ujinga, kuogopa kisichojulikana, kutumainia uchawi au bahati.” Unawashika watu kwa muda wote wanapoendelea kuwa wajinga au kuuamini. Mtu mshirikina anapopata maarifa ya kweli na anaona upumbavu wa imani zake, ule uwezo wa ushirikina uliompata unamwondoka. Na kile chanzo bora zaidi cha maarifa kinachozuia ushirikina ndicho Biblia.

Wawa alijua hilo. Alipokwisha kujifunza hali ya wafu ilivyo kweli kweli, aliacha kuogopa. Aliacha kufanya mambo yaliyodaiwa na ushirikina naye hakuumia. Sasa yeye anajua kwamba hofu zake za ushirikina zilikuwa za bure.

Waafrika wengi wameona vivyo hivyo. Wanapoisoma Biblia na kujua kwamba Mungu alimwumba kila mnyama “kwa jinsi yake,” wanafahamu kwamba Mami Wata​—nusu-samaki, nusu-binadamu​—hangeweza kuwako. (Mwanzo 1:20-27) Zaidi ya hayo, hakuna mvuvi wa samaki ambaye amepata kumkamata kiumbe wa namna hiyo wakati wo wote katika nyavu zake za kuvulia samaki na kumweka katika maonyesho. Hali moja na hiyo, wanafahamu kwamba mchawi hawezi kugeuza mtu awe chui au mamba kwa kuwa hizo ni “jinsi” (aina) zilizo tofauti kabisa.

Vilevile, Biblia inataja wanyama kuwa “wasio na akili.” (2 Petro 2:12) Basi ndege au mbwa anawezaje kujua kwamba mtu fulani atakufa? Au nyoka au kinyonga (au paka mweusi, katika Ulaya) anawezaje kumletea msiba mtu fulani ambaye anajikuta akivuka njia yake? Kwa kweli mwenye uwezo wa kutoa hirizi anawezaje kutabiri mambo ya wakati ujao na hali Biblia inasema kwamba ni Mungu peke yake anayejua kweli kweli mambo ya wakati ujao? (Isaya 44:6-8) Akili inatuambia kwamba hawawezi kufanya hivyo, kama vile nyota na sayari zilizo umbali wa mabilioni ya kilomita, haziwezi kufanyiza yo yote katika maisha za waamini wa falaki hapa katika dunia-sayari.

‘Lakini,’ huenda mtu fulani akapinga akisema, ‘nyoka alivuka njia yangu, na baada ya siku mbili kaka yangu akawa mgonjwa!’ Bila shaka hilo lingeweza kutukia. Lakini namna gani wale wote ambao watoto wao wanakuwa wagonjwa bila kuwaona nyoka wala vinyonga? Au namna gani wale wanaoona viumbe hao lakini wasipatwe na matatizo mara baada ya hapo? Ikisimulia yanayowapata wanadamu, Biblia inasema: “Wakati na tukio huwapata wote.” (Mhubiri 9:11, Revised Standard Version) Ndiyo, mambo yanaweza kutendeka kwa tukio tu. Kwa sababu mtu anakuwa mahali fulani wakati usiofaa, huenda akaumizwa na dhoruba. Si lazima magonjwa na misiba isababishwe na mpango fulani mbaya wa adui. Wengi sasa wanaona hilo kuwa hivyo, na sasa maisha zao hazitawalwi tena na woga wa ushirikina.

Imani ya Mambo ya Ajabu

Hata hivyo, kuna sehemu nyingine ya ushirikina isiyoweza kupuzwa. Mara nyingine inaonekana kuna uwezo wa kigeni unaohusika​—wengine wanauita uwezo wa kufanyiza maajabu​—ambao ni zaidi ya tukio linalotokea wakati ule ule na misiba halisi. Katika nchi za Wazungu watu wanajua kwamba mambo mageni yanaweza kutukia wakati wa mikutano inayohusiana na kupata habari za viumbe wa roho. Kijana mmoja wa kiume alisimulia tukio lililohusiana na ubao wa kuagulia. Alisema kwamba yeye na rafiki zake walikuwa wameketi kuzunguka ubao huo ili waone mambo ambayo yangetukia wakati yeye alipoangushwa vibaya katika kiti chake na kupigwa kwenye ukuta kwenye pembe ya mbali ya chumba.

Katika Afrika mambo mageni yanaripotiwa vilevile. Watu wanasisitiza kwamba wameona mwanamke aliye nusu-samaki na mwenye rangi ya shaba akiwatolea ishara waingie mtoni. Au ripoti zinasikiwa juu ya wanyama wanaosema wakidai kwamba hapo zamani walikuwa wanadamu. Au magonjwa yanaelekea kutokea kwa sababu ya ulogi wa mchawi. Tunaweza kuelezaje hilo?

Mambo mageni yanatendeka kweli kweli, nayo Biblia inatuambia sababu yake. Tena, maarifa ndiyo njia ya kuivunja minyororo ya ushirikina. Kulingana na Biblia kuna majeshi yenye uovu ya viumbe vya kiroho wanaotaka kutudanganya. Walakini, hao si roho za wafu. Na mtu anaweza kupinga uwezo wao.

Jambo la kwanza, wenye nguvu hizo za kiroho ni nani au ni nini? Katika Biblia wanaitwa mashetani, na mkuu wao ndiye Shetani. Haitupasi kudhihaki wazo hilo la kuwako kwao. Yesu mwenyewe alijua habari zao. Walitoka wapi? Biblia inaonyesha kwamba walikuwa watumishi wa kimalaika wa Mungu walioasi wakawa wapinzani.​—Mathayo 12:26-28; 2 Petro 2:4.

Vilevile Biblia inasema kwamba Shetani ‘anaudanganya ulimwengu wote.’ (Ufunuo 12:9) Kwa sababu hiyo, si jambo la kushangaza kwamba yeye anataka kuwaweka watu katika minyororo ya ushirikina. Je! anaweza kufanyiza matendo mageni ili awadanganye? Ndiyo, anaweza. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba kuna mwasi fulani “ambaye kuja kwake ni kwa mfano wa kutenda kwake Shetani, kwa uwezo wote, na ishara na ajabu za uongo; na katika madanganyo yote ya udhalimu kwa hao wanaopotea.”​—2 Wathesalonike 2:9, 10.

Hivyo, ikiwa mambo mageni yanaonekana kuwa yanatendeka, lazima yawe ni kupitia uvutano wa Shetani na mashetani wake. Bila shaka, Shetani ni mwenye uwezo mkubwa kuliko mwanadamu ye yote. Lakini hatuko bila msaada, kwa sababu Mungu ni mwenye uwezo hata zaidi ya Shetani na Yeye ametutolea msaada ikiwa tunautaka.

Yakobo mwandikaji wa Biblia anasema:“Basi mtiini Mungu. Mpingeni Shetani, naye atawakimbia.” (Yakobo 4:7) Wawa na Waafrika wengine wengi wameukubali mwito huo. Wakiisha kuikubali kweli inayotoka katika Neno la Mungu, Biblia, wakafuata amri juu ya jinsi inavyowapasa kujiendesha wenyewe, wanaona kwamba ushirikina wa Kishetani hauna uwezo katika maisha zao. Wana uhuru pasipo ule woga wa zamani.

Kwa hiyo wamezifungua zile hirizi katika shingo zao na zile kamba za kukinga watoto wao wakazichoma katika moto. Hawashiriki sherehe za ushirikina ili wazitulize roho za wafu; wala hawaogopi ulogi wa wachawi. Vilevile wamejiepusha na maovu kama vile uasherati na jeuri.

Je! watu hao mmoja mmoja wamepata taabu kwa sababu ya ujasiri huo? Hasha! Yesu aliwaahidi wanafunzi wake hivi: “Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” (Yohana 8:31, 32) Dhambi haiwi tena bwana ya watu hao. Wamekingwa na Mungu juu ya utendaji wo wote wa mashetani, na maarifa yao mapya yanafunua ubatili wa ushirikina wao wa zamani. Kweli imevunja minyororo yao!

Uhuru kama huo unapatikana kwa wote wanaoutaka. Ikiwa ungependa kufurahia uhuru huo wa kutokuogopa ambao Wawa anao sasa, Mashahidi wa Yehova wangefurahi kukusaidia kama walivyomsaidia.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki