“Tazama! Yehova Alikuja Pamoja na Maelfu Kumi Watakatifu Wake”
“Tazama! Yehova alikuja pamoja na maelfu kumi watakatifu wake ili atekeleze hukumu juu ya wote, na kuwatia hatiani wote wasiomwogopa Mungu kuhusu matendo yao ya kutokumwogopa Mungu waliyofanya kwa jinsi isiyo ya kumwogopa Mungu, na kuhusu mambo yote ya kuchukiza sana ambayo watenda dhambi wasiomwogopa Mungu walisema kinyume chake.”—Yuda 14, 15, NW.
1. Akiwa ndiye Hakimu Mkuu Zaidi, Yehova amepaswa aonweje?
YEHOVA, yule Hakimu Mkuu Zaidi anastahili kuheshimiwa. (Isaya 33:22) Hata hivyo wengi wanamtendea dharau kubwa. Waliokuwa miongoni mwa watenda mabaya hao wenye majivuno ni “makafiri” ambao juu yao mwanafunzi Yuda aliandika katika barua yake iliyoongozwa na Mungu. Walakini, hakuna anayeweza kumdharau Mungu asipate adhabu, kwa maana hakuna shaka juu ya ‘kuja kwa Yehova ili atekeleze hukumu juu ya wasiomwogopa Mungu.’—Yuda 14, 15, NW; Ayubu 9:1-4.
2. (a) Mpaka hapa mazungumzo yetu ya barua ya Yuda yameleta mambo gani kwenye fikira zetu? (b) Shauri zaidi la Yuda linapasa litufanyie nini?
2 Mazungumzo yetu yaliyotangulia juu ya barua ya Yuda yalikazia uhitaji wa kupinga walimu wa uongo na wale wanaotaka kuuchafua mwili, lakini kutii maonyo ya Kimaandiko na kuheshimu mamlaka iliyowekwa kimungu. (Yuda 1-10) Sasa shauri zaidi la Yuda na likuze heshima yetu tunayopaswa kumtolea yule Hakimu Mkuu Zaidi hivi kwamba tutasimama imara miongoni mwa mashahidi wake tukiwa na tumaini la uzima wa milele.
‘Ni Vibaya Mno Kwao!’
3. Kaini alikuwa na hatia ya nini?
3 Kuhusu wale “makafiri” waliomkaidi Yehova, Yuda aliandika hivi:
“Ni vibaya mno kwao kwa sababu wameenda katika njia ya Kaini, na kuukimbilia mwendo wenye makosa wa Balaamu wa kupata thawabu, na wamepotea katika mazungumzo ya uasi ya Kora!” (Yuda 11, NW)
Katika kusema “ni vibaya mno kwao,” Yuda alionyesha kwamba ole ungewaangukia “makafiri” hao waliokuwa wamejiingiza kwa siri katika kundi la watu wa Yehova. (Linganisha Luka 11:42-47, 52.) Watu hao walikuwa “wameenda katika njia ya Kaini.” Ijapokuwa kibali ya Mungu ilikuja juu ya Abeli na dhabihu yake ya nyama na damu ya mnyama, toleo lisilo na damu la Kaini, lililofanywa kwa roho isiyofaa, lilikataliwa. Kaini alikosa imani na hakuuheshimu utukufu au adhama ambayo Mungu aliweka juu ya Abeli. Katika husuda na chuki, Kaini hata alidharau onyo la kimungu akamwua ndugu yake.—Mwanzo 4:2-8; Waebrania 11:4; 1 Yohana 3:12.
4. (a) Ni nini iliyokuwa “njia ya Kaini”? (b) Sababu gani imekupasa uepuke “njia ya Kaini”?
4 Kwanza, Kaini alionyesha kukosa kumheshimu Yehova, na mwendo wake wa kukosa heshima uliitwa “njia ya Kaini.” Kama vile tendo lake la ukaidi na nia yake yenye uovu ilivyokuwa mbaya, ndivyo ilivyo leo na mtu ye yote anayejidai kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova lakini anayetaka kugeuza fadhili zisizostahilika za Mungu kuwa kisababu cha mwenendo mpotovu. Mtu ye yote kama huyo anafuata “njia” ya Kaini. Kama Kaini, aliyechukia na kumwua ndugu yake, watu kama hao mmoja mmoja ni ‘wauaji’ kwa sababu wanachukia Wakristo waaminifu ambao Yehova ameheshimu kwa kuwapa utumishi Wake. (1 Yohana 3:15) Mungu alimlaani Kaini, na wakati wa ile Gharika wazao wake walifutiliwa mbali. Hali moja na hiyo, itakuwa “vibaya mno” kwa wale wanaofuata “njia ya Kaini,” kwa maana haimpendezi Yehova na inaongoza kwenye uharibifu.
5. (a) Ni mwendo gani ambao Balaamu alifuatia? (b) Katika siku za Yuda ni nani ‘waliokimbia kuingia katika mwendo wenye makosa wa Balaamu’? (c) Ni nini litakalowapata wo wote wanaotaka sasa kupotoa watu wa Yehova kwa mafundisho uongo na kwa kushiriki tamaa za unyama?
5 Wale wachafuaji wa mwili wasiomwogopa Mungu vilevile walikuwa ‘wamekimbia katika mwendo wenye makosa wa Balaamu ili kupata thawabu.’ Akiyakubali matoleo ya thawabu ya Mfalme Balaki Mmoabi aliyotolewa mara nyingi, Balaamu alijaribu kuwalaani Waisraeli mara tatu, lakini nyakati zote Yehova aligeuza ile laana ikawa baraka. Kwa hiyo, Balaamu mwenye pupa alipendekeza kwa Balaki kwamba ikiwa Waisraeli wangeweza kushawishwa waingie katika dini ya uongo na kuzishiriki tamaa za unyama, Mungu angelaani hata watu Wake mwenyewe. Shauri hilo bovu lilifuatwa, na kwa sababu ya mwenendo mpotovu wa Waisraeli, watu 24,000 kati yao waliuawa na pigo lililopelekwa na Mungu na kwa kuuawa moja kwa moja. (Hesabu 22:1-25:9; Ufunuo 2:14) Baadaye, Balaamu mwenyewe alikufa katika mikono ya wale aliokuwa akijaribu kulaani. (Hesabu 31:8) Hali moja na hiyo, msiba utawaangukia wo wote wanaodai kuwa Mashahidi wa Yehova lakini ambao ni wenye pupa na wanataka kupotoa watu wa Yehova kwa mafundisho ya uongo na kwa kushiriki tamaa za unyama. Zimekuwako pindi za kufanya hivyo katika nyakati za kisasa, nao mashahidi waaminifu waliojiweka wakf kwa Yehova wamepaswa wajihadhari!
6, 7. (a) Kora Mlawi alikuwa na hatia ya nini? (b) Ni nini lililompata Kora na wale waliojiunga naye? (c) Imetupasa tuoneje “mazungumzo ya uasi”?
6 Mfano mwingine wa kuonya uliotajwa na Yuda ulikuwa ni ule wa Kora Mlawi, aliyetumia “mazungumzo ya uasi.” Akiongozwa na tamaa ya makuu, alimshtaki Musa kwa uongo kwamba alikuwa amefanya mpango wa kichoyo ili Haruni ndugu yake mwenyewe, awe kuhani mkuu, na akamshtaki Haruni kwamba alikuwa amejinyakulia mwenyewe na jamaa yake ile heshima ya ukuhani. Kora hakuuheshimu ule utukufu au adhama ambayo Mungu alimpa Haruni na wanawe, lakini akaasi kuweka kwa Mungu.
7 Ijapokuwa Kora na wazao fulani wa Reubeni waliovutwa wawe upande wake walikuwa wameokolewa katika Misri, hawakuingia kamwe katika ile Nchi ya Ahadi. Badala yake, dunia ilifunguka na baadhi yao wakazikwa wakiwa hai, hali wengine walichomwa mpaka wakafa kwa moto uliotoka kwa Yehova. Halafu, Waisraeli 14,700 walionung’unikia hukumu hiyo iliyotoka kwa Mungu walikufa kwa pigo lililotoka kwa Yehova. (Hesabu, sura ya 16) Kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu juu ya “makafiri” hao waasi kulikuwa hakika sana hivi kwamba Yuda akasema ‘wamepotea.’ Ilikuwa kama imefikilizwa! Lo! jinsi yote hayo yamepasa yatuchochee tuepuke “mazungumzo ya uasi”!
8. Ile mifano ya kuonya ya Kaini, Balaamu na Kora ina maana gani leo?
8 Ndiyo, ole utawaangukia hakika wo wote wanaofuatia mwendo wa kuasi Yehova na mipango yake ya kitengenezo. Yuda alionyesha kwamba ingekuwa “vibaya mno” kwa wale ambao wangekosa upendo na imani (kama Kaini), ambao (kama Balaamu) wangetamani kulipwa kwa ajili ya mafundisho ambayo yangeendeleza mwenendo mpotovu, na ambao (kama Kora) wangekosa kuiheshimu mamlaka iliyotolewa na Mungu. Na bila shaka maneno ya Yuda yalitoa onyo lenye nguvu juu ya wo wote wanaodai kuwa Mashahidi wa Yehova lakini wenye maoni ya kulaumu au ya kutokuheshimu mpango wa Mungu wa kitheokrasi wa siku hizi.
Maonyo katika Ulinganifu
9. Ilikuwa maana gani ya kufananisha walimu wa uongo wasiomwogopa Mungu na “miamba iliyofichwa chini ya maji”?
9 Akiendelea kutoa onyo, Yuda alisema kwa kulinganisha:
“Hao ndiyo miamba iliyofichwa chini ya maji katika karamu zenu za upendo wanapokula karamu pamoja nanyi, wachungaji wanaojilisha wenyewe bila hofu; mawingu yasiyo na maji yanayopelekwa huku na kule kwa pepo; miti katika vuli ya mwisho, lakini isiyo na matunda, ikiwa imekufa mara mbili, ikiwa imekwisha kung’olewa mizizi; mawimbi ya bahari yasiyotulia yanayotoa povu la visa vyao yenyewe vya aibu; nyota zisizo na njia iliyowekwa, ambazo kwa ajili ya hizo weusi tititi unaendelea kuwekwa akiba milele.” (Yuda 12, 13, NW)
Miongoni mwa mambo mengine, wale walimu wa uongo walikuwa kama “miamba iliyofichwa chini ya maji.” Watu hao walisingizia kuwa wanawapenda waamini na kwa hiyo walikuwa kama miamba iliyochongoka chini ya maji ambayo ingeweza kupasua na kuua waogeleaji au kuharibu merikebu. Isipokuwa Mashahidi wa Yehova wanaendelea ‘kuishindania imani,’ walimu hao wenye kudanganya wangeweza kuongoza watu mmoja mmoja wasio imara kwenye ‘maangamizi ya imani yao.’—1 Timotheo 1:19.
10. (a) Inaelekea zile ‘karamu za upendo’ za kwanza za Kikristo zilikuwa nini, na “makafiri” wale walizihudhuria wakiwa na nia gani? (b) Ni nini linalopasa kuepukwa kwenye vikusanyiko vya kirafiki miongoni mwa Mashahidi wa Yehova?
10 “Makafiri” hao walikwenda mara nyingi kwenye ‘karamu za upendo’ hizo za Wakristo. Labda vipindi hivyo vilikuwa ni karamu kubwa ambazo kwa hizo Wakristo wenye ufanisi wa mali walikaribisha waamini wenzao waliokuwa maskini. Lakini wale waliotaka kuchafua mwili walihudhuria karamu hizo wakiwa na nia mbaya. (Linganisha 2 Petro 2:13.) Hali kadhalika, leo kuna wengine wanaojaribu kugeuza vituko vya kirafiki miongoni mwa Mashahidi wa Yehova viwe vipindi vya ulafi, ulevi na vya nyimbo na dansi za kilimwengu. Mashahidi Wakristo walio waaminifu wasiruhusu hilo kamwe litukie katika vikusanyiko vyao vya kirafiki.
11. (a) Wale walimu wa uongo wasiomwogopa Mungu walikuwa wachungaji wa namna gani? (b) Ni maoni gani ambayo Wakristo washikamanifu wamepaswa wawe nayo kuelekea walimu hao wa uongo leo?
11 Walimu hao wa uongo wasiomwogopa Mungu vilevile walikuwa kama wachungaji waliokata manyoya na kuzitoa kondoo dhabihu ili wajivike na kujilisha wenyewe. Walijaribu kuongoza wale wasio imara katika mwendo wa upotovu na hawakuwalisha chakula cha kiroho kinachofaa. (Linganisha Ezekieli 34:7-10.) Ni lazima kama nini kwamba Wakristo washikamanifu wayakatae maoni ya ye yote wa walimu hao wa uongo wa leo!
12. Walimu hao wa uongo wa siku za Yuda walifananaje na mawingu yasiyo na maji, yenye kuchukuliwa na upepo?
12 Walimu hao wa uongo wa siku za Yuda vilevile walikuwa kama mawingu yenye udanganyifu yenye kuonyesha dalili ya mvua nyingi inayohitajiwa, kumbe yalikuwa mawingu yasiyo na maji kweli kweli na yaliyoondolewa na pepo. Watu hao walichukuliwa uku na huku na pepo za makosa, na kwa sababu ya kuwa kama “mawingu yasiyo na maji” wao walikuwa tupu kiroho na wasiofaa kitu. Mashahidi wa Yehova na wajihadhari na walimu hao wote wa uongo wenye kimbelembele.
13. Sababu gani walimu hao wa uongo walikuwa kama miti isiyo na matunda iliyokuwa “imekufa mara mbili” na ‘iliyong’olewa’?
13 Wakikosa kuwa na matunda ya roho takatifu ya Mungu, watu hao waovu vilevile walikuwa kama miti isiyo na matunda wakati wa vuli, mwishoni mwa majira ya kuzaa matunda. Walikuwa kama miti iliyokuwa “imekufa mara mbili,” au ilikuwa “imekufa kabisa.” (Today’s English Version) Watu hao ‘walijiingiza kwa siri’ katika lile kundi kwa kusingizia kuwa wako hai kiroho wakiisha kubatizwa rasmi katika maji. Lakini kwa kuwa hawakuzaa matunda kwa utukufu wa Mungu, walipaswa wachukuliwe hatua kama vile miti isiyozaa matunda katika Palestina ya zamani ilivyochukuliwa hatua. Iling’olewa na kuharibiwa ili kuepuka kutozwa kodi juu ya miti yenye kuzaa matunda. ‘Kung’olewa’ kulionyesha waziwazi kwamba walimu hao makafiri na wasiotubu walikabili uharibifu.
14. Walimu hao wa uongo walifananaje na “mawimbi ya bahari yasiyotulia”?
14 Kwa sababu walimu hao wa uongo walikuwa hawana roho takatifu ya Mungu, vilevile walikuwa kama “mawimbi ya bahari yasiyotulia.” Walikuwa wasiotulia kama mawimbi yenye kusukasuka ya bahari yanayotifua matope na majani ya baharini. Kwa kulinganisha, kwa wazi watu hao wasiotulia wenye tabia ya unyama, walikuwa wenye kelele katika kufanya madai yao ya imani, lakini matendo na mafundisho yao yasiyo ya kumwogopa Mungu yaliwatambulisha kuwa watenda mabaya wachafu wenye sababu ya kuaibishwa.—Isaya 57:20, 21.
15. Walimu hao wa uongo walifanana na nyota za aina gani, nao waliwekewa akiba gani?
15 Kwa kuwa walimu hao wa uongo hawakudumisha mwendo ulio imara katika uadilifu, walikuwa kama “nyota zenye kutangatanga.” (Authorized Version) Bila shaka, kusafiri kwa kuongozwa na nyota kusingewezekana iwapo nyota hizo zingetangatanga pasipo utabiri. Kwa kulingana, kama vile nyota zisizo na “njia iliyowekwa,” makafiri hao hawangeweza kutegemewa watoe uongozi mzuri wa kiroho. Mianga hiyo ya uongo ‘Mungu aliiwekea akiba milele’ ule “weusi tititi,” na hiyo ilimaanisha uharibifu wao wa milele. Kweli kweli, mashahidi Wakristo waaminifu wa Yehova wanawakataa kabisa walimu wa uongo na mafundisho yao kwa sababu nyingi.
Yehova Achukua Hatua ya Kutekeleza Hukumu
16. Enoki alikuwa nani, na alitabiri nini?
16 Ili athibitishe kwamba Yehova anachukulia wasiomwogopa Mungu hatua, Yuda alisema:
“Ndiyo, yule wa saba katika mstari wa kutoka Adamu, Enoki, alitabiri pia habari yao, aliposema hivi: ‘Tazama! Yehova alikuja pamoja na maelfu kumi watakatifu wake, ili atekeleze hukumu juu ya wote, na kuwatia hatiani wote wasiomwogopa Mungu kuhusu matendo yao ya kutokumwogopa Mungu waliyofanya kwa jinsi isiyo ya kumwogopa Mungu, na kuhusu mambo yote ya kuchukiza sana ambayo watenda dhambi wasiomwogopa Mungu walisema kinyume chake.’ “(Yuda 14, 15, NW)
Kuhesabu Adamu, yule mtu wa kwanza, Enoki alikuwa “wa saba katika mstari.” Waliokuwa katikati ni Sethi, Enoshi, Kenani, Mahalaleli na Yaredi. (Mwanzo 5:3-18) ‘Enoki alitembea pamoja na Mungu,’ akifuatia mwendo uliopatana na kweli ya Yehova iliyofunuliwa. (Mwanzo 5:24, NW; Waebrania 11:5) Upotovu wa kiroho ulimzunguka Enoki, lakini yeye kwa ujasiri alitumikia akiwa nabii wa Mungu.
17. Inaelekea Yuda alipataje habari za unabii wa Enoki?
17 Namna Yuda alivyojifunza juu ya unabii wa Enoki haikufunuliwa. Haionekani mapema katika Maandiko yaliyoongozwa na Mungu. Labda Yesu alitumia maneno ya unabii wa Enoki katika mahubiri nayo yakapelekwa kwa mdomo kama mapokeo. Lakini hakuna ushahidi unaoonyesha kwamba Yuda alitumia maneno yanayofanana na hayo yanayopatikana katika Kitabu cha Enoki ambacho si sehemu ya Maandiko yaliyoongozwa na Mungu. Kwa kuwa Yuda aliandika akiongozwa na Mungu, kutiwa kwa unabii wa Enoki katika barua yake kunathibitisha ukweli wa maneno hayo.
18. (a) Sababu gani ingeweza kusemwa kwamba Enoki alitabiri vilevile juu ya walimu wa uongo wa siku za Yuda? (b) Kulingana na unabii wa Enoki, yule Hakimu Mkuu Zaidi angeshughulikaje na wale wenye kumtendea kwa dharau?
18 Kwa wazi, Enoki “alitabiri pia habari yao [wale walimu wa uongo wa siku za Yuda] “kwa kuwa yale aliyotabiri kuhusu watenda mabaya wa kwanza vilevile yaliwahusu wao. Yehova, yule Hakimu Mkuu Zaidi, ambaye kuelekea yeye wasiomwogopa Mungu au watu wasio na heshima kwa Mungu walionyesha dharau, angetekeleza hukumu yake kali juu yao. Kwa kufanya hivyo, Yehova angekuja pamoja na “maelfu kumi watakatifu,” yaani, malaika waadilifu katika idadi zilizo kubwa mno. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 33:2; Danieli 7:9, 10.) Aliye mkuu wa “maelfu kumi” hao ndiye yule Masihi, ambaye kupitia yeye Yehova anakuja na kufanya hukumu.—Luka 1:35; Yohana 5:27; Matendo 17:30, 31.
19. (a) Kama wale watu waovu wa siku za Enoki, wale “makafiri” walisemaje ‘mambo ya kuchukiza sana’ juu ya Yehova? (b) Ni nini kilichokuwa kinakuja hakika juu ya wachafuaji wa mwili wasiomwogopa Mungu? (c) Hivyo imewapasa Mashahidi wa Yehova wajiendesheje?
19 Yehova aliruhusu hao wasiomwogopa Mungu au watu wasiomheshimu Mungu nafasi tele ili waonyeshe hatia yao, kwa njia ya “mwenendo mpotovu” wao. Kwa vitendo vyao viovu na maneno maovu hali yao ya kutokumwogopa Mungu ilifanywa ionekane wazi na juu ya msingi huo walithibitishwa kuwa wenye hatia, ‘walitiwa hatiani’ na Mungu. Kama vile waovu wa siku za Enoki walivyosema ‘mambo ya kuchukiza sana’ juu ya Mungu, ndivyo “makafiri” hao walivyodharau ubwana na kuwatukana wale ambao juu yao Yehova alikuwa ameweka kadiri fulani ya utukufu. (Yuda 8-10) Hivyo walikuwa wakisema ‘mambo ya kuchukiza sana’ juu ya Yehova nao walihukumiwa. Kulingana na unabii wa Enoki, Mungu alitekeleza hukumu juu ya wasiomwogopa Mungu wakati wa gharika ya siku za Noa. Kwa sababu hiyo, kutekelezwa kwa hukumu ya kimungu juu ya wachafuaji wa mwili wasiomwogopa Mungu kulikuwa kwa hakika, na Mashahidi wa Yehova wanaweza kutazamia utekelezi wa hukumu unaofanana na huo katika wakati huu. Kwa hakika, basi, imetupasa tulinde matendo yetu na usemi wetu ili yampendeze Mungu na kuepuka uharibifu.
Epuka Kunung’unika na Msemo wa Kutakabari
20. Watumishi wa Yehova wamepaswa waoneje manung’uniko na malalamiko ya wale “makafiri”?
20 Akitaja tabia nyingine zisizo za kumwogopa Mungu, Yuda aliandika:
“Watu hao ni wanung’unikaji, walalamikaji juu ya fungu lao katika maisha, wakianza kulingana na tamaa zao wenyewe, na vinywa vyao vinasema mambo ya kutakabari, huku wakiwasifu watu mashuhuri kwa sababu ya faida yao wenyewe.” (Yuda 16, NW)
Mashahidi Wakristo wa Yehova wanapewa onyo la upole ‘waendelee kutenda mambo yote pasipo manung’uniko.’ (Wafilipi 2:14, 15) Lakini “makafiri” hao walikuwa “wanung’unikaji” kama vile Waisraeli wale waliomnung’unikia Musa na Haruni na kwa hiyo ikawalazimu wafe katika jangwa kwa sababu ya kumnung’unikia hasa Mungu. (Hesabu 14:1-38; 1 Wakorintho 10:10) Vilevile watu hao wenye tabia ya unyama walikuwa “walalamikaji juu ya fungu lao katika maisha” hata kama vile maskini wa ulimwengu wanavyoweza kulalamika kwa sababu hawana mali, na kadhalika. Bila shaka, kama Wakristo wa kweli wa wakati wa Yuda, Mashahidi wa Yehova leo wanaitegemea hekima ya kimbingu na msaada wa roho ya Mungu ili wavumilie hali zenye shida. Sisi tusiwe kamwe kama wanung’unikaji wale wasiomwogopa Mungu wa siku za Yuda!
21. (a) Ni katika njia gani wale “makafiri” ‘walianza kulingana na tamaa zao wenyewe’? (b) Watu hao wapotovu ‘waliwasifuje watu mashuhuri kwa ajili ya faida yao wenyewe,’ na kwa sababu gani hilo lilikuwa jambo baya?
21 Wapotovu hao ‘walianza kulingana na tamaa zao wenyewe,’ wakiongozwa na tamaa za anasa za uasherati lakini si kulingana na amri zile za Mungu wala za Mwanaye. (Linganisha Yakobo4:1-3.) Na huku ‘vinywa vyao vikisema mambo ya kutakabari,’ au vilikuwa “vimejaa mazungumzo ya kujisifu” (Jerusalem Bible), walichagua watu fulani ambao waliwaonyesha sifa isiyo ya unyofu wa moyo. (Linganisha Zaburi 140:11; Tito 1:10, 11; 2 Petro 2:18, 19.) Watu hao wasio na adili ‘walisifu watu mashuhuri kwa sababu ya faida yao wenyewe.’ Walisitawisha upendeleo na kuunga mkono matajiri, wenye vyeo, au wengine, kwa kutumaini kupata mali au faida ya cheo. Lakini huo ulikuwa uchoyo mbaya sana na ulipofusha watenda mabaya hao hata wakakosa kuiona shabaha ya juu sana ya kimungu ya kusitawisha kibali ya Yehova. Kwa sababu hiyo, walishindwa kumheshimu yule Hakimu Mkuu Zaidi na hivyo wakaja chini ya hukumu yake ya uharibifu.
22. Kama tulivyozungumza mpaka hapa, ni nini ambalo Yuda ametoa kwa faida yetu, na maneno yake ya kumalizia yanatia ndani nini?
22 Yuda aliwasihi waamini wenzake waziwazi ‘waishindanie imani.’ Alielekeza kwenye maonyo ya Kimaandiko juu ya ufisadi, uasi na kunung’unika, naye hakuacha shaka juu ya kutekelezwa kwa hukumu ya kimungu. Ni wakati unaofaa sana kama nini kwamba Mashahidi wa Yehova wayafikirie sana mambo hayo! Kama tutakavyoona, maneno ya kumalizia ya Yuda, yanayotia ndani kusihi kwa kutoka moyoni, vilevile yana maana kubwa kwa waabudu wa Yehova.
Je! unaweza kujibu maulizo haya?
□ Ni nini iliyokuwa “njia ya Kaini,” na kwa sababu gani ni lazima watu wa Yehova waiepuke?
□ Ni nani ‘waliokimbia kuingia katika mwendo wa Balaamu,’ na kwa sababu gani wewe ungeuepuka?
□ Ni mfano gani wa kuonya tulio nao kwa habari ya Kora Mlawi?
□ Wale “makafiri” ambao Yuda anazungumza juu yao walilinganaje na miti isiyozaa matunda ‘iliyokuwa imekufa mara mbili’ nayo ‘iling’olewa’?
□ Enoki alitabiri nini, na maneno yake yamepasa yatuongoze tufanye nini?
□ Juu ya msingi wa shauri la Yuda ni maoni gani tunayopaswa kuwa nayo kuelekea kunung’unika na ‘kusifu watu mashuhuri kwa ajili ya faida yetu wenyewe’?
[Picha katika ukurasa wa 11]
Walimu makafiri wasiotubu walikabili uharibifu, hata kama vile miti isiyozaa matunda ilivyong’olewa