“Wapendwa, . . . Jidumisheni Katika Upendo wa Mungu”
“Wapendwa, kwa kujijenga wenyewe juu ya imani yenu iliyo takatifu zaidi sana, na kusali kwa roho takatifu, jidumisheni katika upendo wa Mungu.”—Yuda 20, 21, NW.
1, 2. Zaidi ya maonyo, ni agizo gani linalopatikana katika barua ya Yuda?
FADHILI zisizostahilika za Yehova ziko wazi katika kushughulika kwake pamoja na wale wanaompenda. Kupitia Neno lake lililoongozwa kwa roho yake yeye anaonyesha anayowataka wafanye. Tunaweza kuwa wenye shukrani kama nini kwa vile sehemu ya Neno la Mungu, ile barua ya Yuda, inatoa maonyo yanayoweza kutusaidia ili tudumishe uhusiano unaofaa pamoja na Yehova Mungu!
2 Hata hivyo, zaidi ya kutoa maonyo yanayohitajiwa, Yuda anatuonyesha mambo ambayo ni lazima tufanye ili tujengwe kiroho na ‘kujidumisha katika upendo wa Mungu.’ Kwa sababu hiyo, tutafaidika sana kwa kuichunguza ile sehemu ya kumalizia ya barua ya Yuda.
Wadhihaki Watabiriwa
3, 4. Yuda alielekeza kwenye “semi” gani za mitume wa Yesu?
3 Akitoa kikumbusho cha maana, Yuda aliandika:
“Kwa habari yenu ninyi, wapendwa, zikumbukeni zile semi zilizotangulia kusemwa na wale mitume wa Bwana yetu Yesu Kristo, jinsi walivyozoea kuwaambia ninyi; ‘Katika wakati wa mwisho watakuwapo wadhihaki, wakianza kulingana na tamaa zao wenyewe kwa ajili ya mambo yasiyo ya kumwogopa Mungu.’ Hao ndio wale wanaofanyiza matengano, watu wenye tabia ya unyama, wasio na hali ya kiroho.” (Yuda 17-19, NW)
Yuda alisema mengi sana ili awafunue hao “makafiri” ambao kwa siri walijiingiza katika kundi. Kisha, akisihi waamini wenzake ambao alikuwa ameonyesha shauku kubwa, Yuda aliwaambia wayakumbuke maneno yaliyotangulia kusemwa na mitume wa Yesu. Kukumbuka maneno hayo kungaliwaongoza Wakristo wote wa kweli ‘waishindanie imani.’
4 Yule mtume Paulo alionya waangalizi wenzake kwamba kutoka miongoni mwao ‘wangeinuka watu, wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao.’ (Matendo 20:29, 30) Alimwambia Timotheo kwamba ‘katika nyakati za mwisho wengine wangejitenga na imani.’ (1 Timotheo 4:1, 2) Naye mtume Petro alionya waziwazi kwamba ‘katika siku za mwisho wangekuwapo wadhihaki, wakisema: “Iko wapi ahadi ile ya kuja?”’—22 Petro 3:1-4.
5. Inaelekea Wakristo waaminifu walitendewa namna gani na wale “makafiri” waliokuwa wamejiingiza kwa siri katika kundi, lakini ingaliwapasa watu wenye kumwogopa Mungu waitikieje hilo?
5 Kwa hiyo, wapokeaji wa barua ya Yuda walikuwa na sababu nzuri ya kutazamia “wadhihaki” kutokea wakati wa kipindi kilichoanza mara kabla ya mwisho wa ule mfumo wa mambo wa Kiyahudi. Inaelekea kwamba wale “makafiri” waliokuwa wamejiingiza kwa siri katika kundi walikuwa wakidhihaki waamini waaminifu walioshikamana na viwango vya uadilifu vya Yehova na ambao hawangejiunga na hao “ndugu za uongo” katika mwenendo mpotovu. Lakini ilikuwa lazima watu hao wenye kumwogopa Mungu ‘waishindanie imani,’ hata ingawa wangalielekea kudhihakiwa na walimu wa uongo ‘walioanza kulingana na’ nao wakaongozwa na ‘tamaa zao wenyewe za mambo yasiyo ya kumwogopa Mungu’ za ufisadi.—Linganisha 2 Wakorintho 11:26; Wagalatia 2:4, 5.
6. Ijapokuwa Mungu alihakikisha kuwako kwa umoja wa wale wanaompenda, wadhihaki wale wasiomwogopa Mungu walijaribu kufanya nini?
6 Ijapokuwa Mungu, kwa roho yake, alihakikisha kwamba kungekuwako umoja wa wale wanaompenda, wadhihaki hao wasiomwogopa Mungu walijaribu ‘kufanyiza matengano,’ au “mafarakano,” wakijitahidi kuendeleza kazi ya kutenganisha miongoni mwa watu wa Yehova. (Yuda 19, New World Translation, chapa ya mwaka 1950, footnote; Zaburi 133:1-3; 1 Wakorintho 1:10) Ijapokuwa wadhihaki hao walisema kinyume cha wanaume waaminifu wenye madaraka katika kundi, makafiri hao walisifu watu mmoja mmoja ambao wangeweza kuwafaidi. (Yuda 8, 16) Kama vile Mafarisayo, waliwadharau wanyenyekevu, washiriki wenye kumwogopa Mungu wa kundi. Badala ya kukusanya pamoja na Bwana, walijaribu kutawanya. Hata leo hii wengine wanajaribu kuwavuta mbali wasio imara waingie katika vikundi vya faragha, vinavyodhaniwa kuwa “funzo la Biblia.” Hiyo haingeweza kamwe kuendeleza upendo kwa Mungu, Kristo na lile kundi la Kikristo.—Luka 11:23.
7. Kwa sababu gani wale “makafiri” walifaa kutajwa “wenye tabia ya unyama”?
7 Watu hao ambao kwa kufaa wanatajwa “wenye tabia ya unyama,” au “wa nafsi,’ kwa maana walikuwa viumbe wenye akili wakifuata mishtuo, tamaa na maelekeo ya kimwili. (Linganisha Kingdom Interlinear Translation, mstari wa 19.) Ijapokuwa walijiona wenyewe kuwa wenye kutiwa nuru kiroho, Yuda aliwataja kuwa “wasio na hali ya kiroho,” au, kwa halisi, wasio na “ile roho.” Kwa hakika, hao “watu wenye tabia ya unyama” walikosa roho ya Yehova, hawangeweza kufahamu mambo ya kiroho nao hawakuwapita wanyama wasio na akili. Iwapo sisi tuna roho ya Yehova na tunayafahamu “mafumbo ya Mungu” imetupasa tuwe wenye shukrani sana sana kwa Baba yetu wa kimbingu.—1 Wakorintho 2:6-16.
Namna ya Kudumu katika Upendo wa Mungu
8. Usemi huu ‘imani iliyo takatifu zaidi sana’ inaelekea ulihusu nini?
8 Kisha Yuda akageukia kusihi kwa bidii, akisema:
“Lakini ninyi, wapendwa, kwa kujijenga wenyewe juu ya imani yenu iliyo takatifu zaidi sana, na kusali kwa roho takatifu, jidumisheni katika upendo wa Mungu, huku mkingojea rehema ya Bwana yetu Yesu Kristo kwa tumaini la uzima wa milele.” (Yuda 20, 21, NW)
Kwa upendo Yuda alionyesha namna waamini wenzake aliothamini sana wangeweza kudumu katika upendo wa Yehova. Kwa hakika kufuata shauri lake kungetia ndani kusitawishwa kwa imani, tunda la roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22, 23) Lakini kulingana na mtajo wa Yuda uliotangulia wa kupigania ‘imani iliyokabidhiwa kwa watakatifu’ (mst. 3), usemi huu ‘imani iliyo takatifu zaidi sana’ unaelekea ulihusu ile jumla yote ya mafundisho ya Kikristo, kutia ndani zile habari njema za wokovu. Msingi wa imani hiyo ya kweli ni Kristo, nayo iliitwa “iliyo takatifu zaidi sana” kwa sababu ilimtegemea Mungu wa utakatifu na msingi ulikuwa ni Neno lake takatifu peke yake.—Matendo 20:32; 1 Wakorintho 3:10-15.
9. Ni lazima tufanye nini ili ‘tujijenge wenyewe juu ya imani yetu iliyo takatifu zaidi sana’?
9 Ili Wakristo ‘wajijenge wenyewe juu ya imani yao iliyo takatifu zaidi sana,’ au ili waitie nguvu ni lazima wajifunze kwa bidii Neno la Mungu kibinafsi na pamoja na kundi. Kuzungumza kikawaida Maandiko na mashahidi Wakristo wa Yehova wenzao, vilevile kuzitangaza habari njema kwa wengine, kutaongeza ule mkazo ambao Biblia inafanyiza katika mioyo yetu. Lakini hakuna moja la hayo linaloweza kutimizwa pasipo sala ya bidii. Mtu mmoja mmoja ‘anasali pamoja na roho takatifu’ wakati anaposali chini ya uongozi wayo na kwa kupatana na yale mambo yaliyo katika Neno la Yehova. Zaidi ya hayo, Maandiko yaliyoandikwa chini ya uongozi wa roho ya Mungu, yanatuonyesha namna ya kusali na mambo ya kuomba katika sala. Kwa mfano, tunaweza kusali tukiwa na uhakika ili tujazwe roho takatifu ya Mungu. ‘Tukisali pamoja na roho takatifu,’ sala zetu zitafunua hali ya moyo inayofaa, ile inayopendwa na Mungu. Kwa njia hiyo tutalindwa juu ya mavutano yasiyofaa, kutia ndani na yale maoni ya “makafiri” wo wote ambao huenda wakajiingiza katika kundi.—Luka 11:13; Warumi 8:9, 26, 27.
10. Ili ‘wajidumishe katika upendo wa Mungu,’ waamini wenzi wa Yuda walitakwa kufanya nini?
10 Ili ‘kujidumisha katika upendo wa Mungu,’ waamini wenzi wa Yuda walipaswa wazishike amri za Yehova na zile za Mwana Wake. (Yohana 15:10; 1 Yohana 5:3) Kudumu katika ule upendo wa Mungu kunahitaji usemi na mwenendo unaokubaliwa na Yehova. Kwa kuwa wasiokamilika na wenye dhambi, ili wadumu katika upendo wa Mungu, wale waaminifu wangeendelea kutaka rehema ya Yehova itolewe kwao kupitia Yesu Kristo na kuwezeshwa kupitia ile dhabihu ya ukombozi ya Bwana yao. (Warumi 5:8; 9:14-18; 1 Yohana 4:9, 10) Mwishowe kuendelea huko kwa rehema ya kimungu kuelekea wafuasi waaminifu wa Yesu kunatokeza uzima wa milele.—Yohana 3:16.
Uhitaji wa Kuonyesha Wengine Rehema
11. Yuda alisema nini juu ya rehema, na katika kuionyesha ilikuwa lazima kutofautisha kati ya nani?
11 Kwa habari ya uhitaji wa kuonyesha rehema, Yuda alisema:
“Vilevile, endeleeni kuonyesha rehema wengine wenye mashaka; waokoeni kwa kuwanyakua kutoka motoni. Walakini endeleeni kuonyesha wengine rehema, mkifanya hivyo kwa woga, huku mkilichukia hata vazi la ndani lililochafuliwa na mwili.” (Yuda 22, 23, NW)
Ikiwa waamini wenzi wa Yuda walitazamiwa kuendelea kupokea rehema ya kimungu, iliwapasa wawarehemu wengine ambao uzima wao wa milele ulikuwa hatarini. (Yakobo 2:13) Lakini ili waaminifu ‘waendelee kuonyesha rehema wengine wenye mashaka,’ ilikuwa lazima kwao watofautishe kati ya wale waliostahili rehema na wale ‘waotaji ndoto.’
12. (a) Kwa sababu ya kuvutwa na wale “makafiri,” inaelekea wengine walikuwa wamekuwa na mashaka gani? (b) Ingewezekanaje ‘kunyakua wengine kutoka motoni’?
12 Kwa mafundisho yao ya uongo, manung’uniko yao, malalamiko yao, na kadhalika, “makafiri” hao walikuwa wakiwafanya watu wasio imara kiroho wajawe na mashaka. Wakitikiswa na maneno ya kutakabari ya walimu wa uongo, inaelekea watu hao wenye mashaka walikuwa wakiwaza kama kweli Wakristo waliojiweka wakf walikuwa watu wa Yehova. Na labda waliacha kushiriki pamoja nao katika ibada na katika kuzihubiri habari njema. Watu hao wasio imara walikuwa katika hatari ya ‘moto,’ au uharibifu wa milele. (Linganisha Mathayo 18:8, 9; 25:31-33, 41-46.) Lakini kwa kuwasaidia upesi kwa kitia moyo cha kiroho na sala, Wakristo walio imara, hasa waangalizi wa kundi, wangeweza kuwaokoa, ‘wakiwanyakua kutoka motoni.’—Wagalatia 6:1; Yakobo 5:13-20.
13. (a) Ni katika njia gani wengine ‘walichafua vazi lao la ndani’? (b) Ingewezekanaje wavaaji wa ‘mavazi yaliyochafuliwa’ ‘waokolewe’?
13 Huenda wengine walifuata wale wenye kuchafua mwili wakaanguka pamoja na wao katika hali isiyo ya adili, au katika uasherati wa kiroho. (Yakobo 4:4) Kwa kufuata mazoea ya kinyama, ilikuwa kana kwamba ‘wamelichafua vazi la ndani.’ Walikuwa wameuchafua utu wao wa ndani wa kuwa Wakristo wa kweli, kama vazi linalovaliwa likiwa karibu na ngozi. (Linganisha Ufunuo 3:4, 5.) Mashahidi waaminifu wa Yehova walilinda wasipate kulitia madoa vazi lao la utu wa Kikristo katika njia hiyo kwa sababu hilo halikumpendeza Yehova Mungu na lingeelekea kuongoza kwenye uharibifu. Hata hivyo, watu wanaomwogopa Mungu, hasa wale wazee waliowekwa, kwa huruma walijaribu kusaidia wavaaji wasio imara wa ‘mavazi yaliyochafuliwa’ wairudie njia ya wokovu. Ikiwa toba ya kweli ingeonyeshwa na wenye kupotoka, ingewezekana ‘kuwaokoa’ wasipatwe na kifo cha kutopata kibali ya kimungu ambacho kwa hicho mwendo mchafu ungeongoza.—Mithali 28:13.
Mpe Mungu Utukufu, Adhama, Uweza na Mamlaka
14, 15. (a) Ni Nani aliyekuwa na uwezo wa kulinda waabudu wenzi wa Yuda waliopakwa mafuta wasijikwae, na mtu angeweza kujikwaa katika nini? (b) Mashahidi waaminifu wa Yehova waliopakwa mafuta wangewezaje ‘kuwekwa bila mawaa’ mbele za Mungu? (c) “Mkutano mkubwa” unatazamia nini?
14 Kwa kumalizia, Yuda alikabidhi wasomaji wake kwa Mungu, akisema:
“Sasa kwa yeye anayeweza kuwalinda ninyi msipate kujikwaa na kuwaweka ninyi kuwa wasio na mawaa machoni pa utukufu wake kwa furaha kuu, kwa yule Mungu pekee Mwokozi wetu kupitia Yesu Kristo Bwana yetu, kuwe utukufu, adhama, uweza na mamlaka kwa umilele wote uliopita na sasa na katika umilele wote. Amina.” (Yuda 24, 25, NW)
Akiisha kutoa onyo lililoongozwa na Mungu na shauri zuri, ilimpasa Yuda awatie waamini wenzake waliohatirishwa kiroho katika kabidhi (ulinzi) ya Mungu. Yehova peke yake angeweza kuwafanikisha katika kuwapinga “makafiri” waliokuwa miongoni mwao. Hivyo kwa kufaa Yuda alimalizia barua yake kwa kumpa Mweza Yote sifa.
15 Waabudu waliopakwa mafuta wenzi wa Yuda wangeweza kuwa na uhakika na Yehova akiwa ‘yeye anayeweza kuwalinda wasipate kujikwaa.’ Mungu angeweza kuwakinga wasianguke katika kosa na kutokushawishwa washiriki mwenenedo usio wa adili uliotiwa moyo na wenye kuchafua mwili wasiomwogopa Mungu. Kwa kweli, Yehova angeweza kuwalinda wenye kumwogopa Mungu ‘wasijikwae’ katika dhambi mbaya na uharibifu ule unaowangojea Wakristo wa uongo wasiotubu na wenye tabia ya unyama. Isitoshe, Yehova alikuwa na uwezo wa ‘kuweka mashahidi wake waaminifu wasiwe na mawaa machoni pa utukufu wake,’ au, “mbele ya uso wake wenye utukufu.” (NW, chapa ya mwaka 1950) Wangeweza kusimama bila madoa ya kiroho kwa sababu ya fadhili zisizostahilika za Mungu. (Waefeso 2:1-7; Wakolosai 1:21-23) Mashahidi waaminifu wapakwa-mafuta wa Yehova wanamtaka Yesu Kristo awafufue na kuwaonyesha katika ukamilifu wa kiroho mbele ya “uso wenye utukufu” wa Mungu. (Yohana 5:25; 11:24, 25) Bila shaka hilo litatokeza “furaha kuu” kwao. Hali moja na hiyo, ule “mkutano mkubwa” unatazamia mbele kwenye kuchungwa kupita katika “ile dhiki kubwa” na kuyafurahia mapendeleo zaidi ya “utumishi mtakatifu” kwa kadiri watakavyoendelea mpaka kufikia ukamilifu wa kibinadamu hapa duniani.—Ufunuo 7:9, 10, 14-17, NW.
16. (a) Sababu gani Yehova anaweza kuitwa “Mungu pekee Mwokozi wetu kupitia Yesu Kristo Bwana yetu”? (b) Yuda alimpa Mungu nini, na sababu gani kwa kufaa hivyo?
16 Kama Yuda alivyosema, Yehova ndiye “Mungu pekee Mwokozi wetu kupitia Yesu Kristo Bwana yetu.” Mara nyingi katika Maandiko Yehova anatambulishwa kuwa Mwokozi. (Zaburi 106:21; Isaya 43:3; Yeremia 14:8; Luka 1:46, 47) Yeye Ndiye anayetoa wokovu kupitia Bwana Yesu Kristo. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16; Warumi 5:8; 1 Yohana 4:9, 14) Kwa kufaa, Yuda alimpa Yehova “utukufu” (Kigiriki, doxa), ikionyesha fahari. (Linganisha Zaburi 29:1, 2.) Vilevile alimpa Mungu “adhama” (Kigiriki, megalōsynē), ikimaanisha “ukuu” wa aina ya kifalme. (Int) Huo ni ukubali unaofaa wa mamlaka kuu ya kifalme ya Yehova akiwa “mfalme wa umilele.” (1 Timotheo 1:17, NW) Kratos,au “uweza,” vilevile, ulitolewa kwa Yehova, kwa wazi ikimaanisha milki yake, au utawala, kwamba ni mbinguni au juu ya dunia hii. (Linganisha Danieli 4:25; Ufunuo 11:16-18.) Zaidi Yuda alimpa Mungu “mamlaka” (Kigiriki, exousia), kwa maana Yehova anayo mamlaka na uwezo wa kutenda kama Yeye anavyotaka.—Danieli 4:34, 35.
17. Sababu gani Yuda kumpa Mungu mambo hayo kungefaa (a) “kwa umilele wote uliopita”? (b) “sasa”? (c) “katika umilele wote”?
17 Kwa kufaa Yuda alimpa Yehova utukufu, adhama, uweza na mamlaka “kwa umilele wote uliopita,” au “kabla ya wakati wote,” kwa kadiri wanadamu wanavyoweza kujua, kwa sababu Yehova ni Mungu “tangu wakati usiojulikana mpaka wakati usiojulikana.” (Yuda 25, NW, chapa ya mwaka 1950, footnote; Zaburi 90:2, NW) Waabudu wa Yehova wangempa Yeye kwa kufaa mambo hayo “sasa,” yaani, wakati Yuda alipoandika na vilevile leo. Isitoshe, Yehova anastahili kupewa mambo hayo “katika umilele wote,” kwa maana yeye hatakufa kamwe naye sikuzote atakuwa na wasifaji waaminifu. (Habakuki 1:12, NW; Zaburi 148) Kwenye mwisho wa Yuda ulio kama sala, aliongeza “Amina,” au “Iwe hivyo.” Na mashahidi Wakristo wote waaminifu wa Yehova wanakubaliana kwa moyo na wonyesho wake wa sifa.
Utie Ujumbe wa Yuda Moyoni!
18. Kutokana na barua ya Yuda, tumejifunza nini juu ya (a) walimu wa uongo? (b) “mwenendo mpotovu’‘? (c) kukosa imani? (d) kuheshimu mamlaka? (e) kunung’unika na kulalamika? (f) kuwasifu wengine kwa faida ya kichoyo?
18 Barua ya Yuda ina maana sana kwa Mashahidi wa Yehova leo. Ni lazima tushikamane na Neno la Mungu na kuepuka kabisa walimu wa uongo. (Ayubu 13:16; 27:8, 9; Yeremia 17:13; Yuda 4, 19) Ni lazima waaminifu wapinge kishawishi cho chote cha kuingia katika “mwenendo mpotovu.” (Yuda 3, 4, NW; Mwanzo 39:7-12) Wala tusikubali hali ya kukosa imani, kwa maana hiyo ingeweza kutukosesha uzima wa milele. (Waebrania 3:12; Yuda 5) Vilevile ujumbe wa Yuda umepasa utuongoze tuheshimu mamlaka iliyowekwa kimungu na kupinga kishawishi cho chote cha kusema kinyume cha wale wanaotimiza kwa uaminifu daraka la kundi. (Waebrania 13:17; Yuda 8, 9) Badala ya kunung’unika na kulalamika, imetupasa tuongozwe na barua ya Yuda tumwonyeshe Yehova na waamini wenzetu upendo. (Mathayo 22:37-40; Yohana 13:34, 35; Warumi 13:8-10; Yuda 16) Vilevile maneno ya Yuda yanatusaidia tuepuke kuwasifu wengine kwa sababu ya kutaka faida ya choyo, hiyo ikiwa ni kati ya njia za upotoe ambazo zingetufanya tuwe wenye kuchukiza sana kwa Yehova.—Mithali 3:32; Yuda 16.
19. Sababu gani imetupasa tuuweke moyoni ujumbe wa Yuda ulioongozwa na Mungu?
19 Kwa hiyo, tukiwa mashahidi Wakristo waliojiweka wakf kwa Yehova na Mwanaye mpendwa, sote na tuweke katika moyo ule ujumbe mzito na wa upendo wa mwanafunzi Yuda. (Linganisha Isaya 43:10-12; Matendo 1:8.) Maneno yake yatatufanya tuwe walio imara hata zaidi tunapotembea katika “njia ya uzima.” (Zaburi 16:11) Na ‘tuendelee kulinda kulingana na neno la Yehova,’ kutia ndani na ile barua ya Yuda. (Zaburi 119:9-16, NW) Katika njia hiyo, tutafanikiwa katika ‘kuishindania imani’ na tukiwa na msaada wa kimungu, ‘tutajidumisha katika upendo wa Mungu.’—Kutoka The Watchtower, September 1, 1982.
Je! unakumbuka mambo haya?
□ Ni nani aliyeonya kwamba ‘katika wakati wa mwisho wangekuwapo wadhihaki,’ na kwa sababu gani Yuda alivuta fikira kwenye hilo?
□ Ni nini iliyokuwa ‘imani takatifu zaidi sana,’ na tunawezaje kujijenga wenyewe juu yake?
□ Waamini wenzi wa Yuda wangewezaje ‘kujidumisha katika upendo wa Mungu’?
□ Ni kwa sababu gani wengine waliojidai kuwa Wakristo walihitaji rehema, na ‘kuwanyakua kutoka motoni’ kulimaanisha nini?
□ Sababu gani ilimfaa Yuda ampe Yehova Mungu utukufu, adhama, uweza na mamlaka?
□ Imetupasa tuweke ujumbe wa Yuda moyoni kwa sababu unatusaidia kushughulika kwa kufanikiwa na matatizo gani?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Mashahidi waaminifu wa Yehova wa karne ya kwanza ‘waliishindania imani,’ hata ingawa inaelekea walidhihakiwa na walimu wa uongo
[Picha katika ukurasa wa 17]
‘Sali pamoja na roho takatifu’