Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • si kur. 261-263
  • Kitabu cha Biblia Namba 65—Yuda

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kitabu cha Biblia Namba 65—Yuda
  • “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YALIYOMO KATIKA YUDA
  • KWA NINI NI CHENYE MAFAA
  • “Wapendwa, . . . Jidumisheni Katika Upendo wa Mungu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • ‘Fanyeni Pigano Kali kwa Ajili ya Imani’!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • “Mwishindanie Imani”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Tunapaswa Kufanya Pigano Kali Ili Kubaki Katika Kweli
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2019
Pata Habari Zaidi
“Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
si kur. 261-263

Kitabu cha Biblia Namba 65—Yuda

Mwandikaji: Yuda

Mahali Kilipoandikiwa: Palestina (?)

Uandikaji Ulikamilishwa: c. (karibu) 65 W.K.

1. Ni kwa sababu ya hali zipi ndani ya kundi Yuda aliona ikihitajiwa kabisa kuandika barua yake thabiti kwa ajili ya ndugu zake?

NDUGU Wakristo wa Yuda walikuwa hatarini! Katika wakati uliokuwa umepita tangu kifo na ufufuo wa Kristo Yesu, watu wenye tabia ngeni walikuwa wamejongelea kwa siri wakaingia ndani ya kundi la Kikristo. Adui hao walikuwa wamepenya kwa kusudi la kuibomoa imani, kama vile mtume Paulo, karibu miaka 14 iliyotangulia, alivyokuwa ameonya. (2 The. 2:3) Akina ndugu wapaswa kuwekwaje macho na kufanywa wajihadhari na hatari? Barua ya Yuda, ambayo ni thabiti na yenye nguvu katika taarifa yayo ya kutoboa wazi, ilitoa jibu. Yuda mwenyewe alieleza msimamo wake waziwazi katika mistari 3 na 4: ‘Niliona imenilazimu kuwaandikia kwa maana kuna watu waliojiingiza kwa siri, makafiri, wabadilio neema ya Mungu wetu kuwa ufisadi.’ Misingi yenyewe ya fundisho timamu na maadili ilikuwa ikitishwa. Yuda alihisi akihitajika kupigania masilahi (faida) ya ndugu zake, ili kwamba wao, nao, waweze kufanya pigano kali kwa ajili ya imani.

2. (a) Yuda alikuwa nani? (b) Ni uhusiano gani pamoja na Yesu ambao Yuda aliuthamini zaidi ya mwingine wote?

2 Lakini Yuda alikuwa nani? Maneno ya kufungua yatuambia kwamba barua hiyo iliandikwa na “Yuda, mtumwa wa Yesu Kristo, ndugu yake Yakobo, kwa hao walioitwa.” Je! Yuda, au Yudasi, alikuwa mtume, kwa kuwa 2 wa mitume 12 wa awali wa Yesu waliitwa Yuda? (Luka 6:16) Yuda hajisemi kuwa mtume, bali awataja mitume kwa nafsi ya tatu “wa-” (“wao,” NW), ikiwa dhahiri kwamba yeye mwenyewe hajitii ndani. (Yuda 17, 18) Zaidi ya hilo, yeye ajiita “ndugu yake Yakobo,” kwa wazi akimaanisha yule mwandikaji wa barua ya Yakobo, aliyekuwa ndugu-nusu wa Yesu. (Mst. 1) Akiwa mmoja wa “nguzo” za kundi katika Yerusalemu, Yakobo huyu alijulikana sana, na kwa sababu hiyo Yuda ajitambulisha naye. Hiyo yafanya Yuda pia kuwa ndugu-nusu wa Yesu, naye ameorodheshwa kuwa hivyo. (Gal. 1:19; 2:9; Mt. 13:55; Mk. 6:3) Hata hivyo, Yuda hakujifaidi kibinafsi kwa kutumia uhusiano wake wa kimwili pamoja na Yesu, bali kwa unyenyekevu alitia mkazo juu ya uhusiano wake wa kiroho akiwa “mtumwa wa Yesu Kristo.”—1 Kor. 7:22; 2 Kor. 5:16; Mt. 20:27.

3. Ni nini kithibitishacho uasilia wa barua ya Yuda?

3 Uasilia wa kitabu hiki cha Biblia waungwa mkono na mtajo wacho katika Muratorian Fragment, cha karne ya pili W.K. Kwa kuongezea, Clement wa Aleksandria (karne ya pili W.K.) alikikubali. Origen alikirejezea kuwa kazi yenye “mistari michache, lakini iliyojawa na maneno yenye afya ya neema ya kimbingu.”a Tertullian pia alikiona kuwa asilia. Hakuna shaka kwamba chafaa kuwa pamoja na Maandiko yale mengine yaliyopuliziwa na Mungu.

4. Yuda ni barua ya aina gani, labda iliandikiwa wapi, na ni nini lionyeshwalo juu ya wakati wa kuandikwa?

4 Yuda awaandikia “hao walioitwa,” bila kutaja kundi au mtu fulani hasa, hivyo basi waraka wake ni barua ya ujumla iliyoenezwa mahali pengi kwa Wakristo wote. Mahali ambapo yaelekea sana ndipo iliandikiwa ni Palestina, ingawa jambo hilo halitajwi. Ni vigumu pia kukaza tarehe hiyo kwa uhakika. Hata hivyo, ni lazima iwe ilikuwa ni muda mwingi baada ya ukuzi wa kundi la Kikristo, kwa maana Yuda avuta uangalifu kwenye “maneno yaliyonenwa zamani na mitume wa Bwana wetu Yesu Kristo” na yaonekana anukuu 2 Petro 3:3. (Yuda 17, 18) Zaidi ya hilo, kuna ufanani mwingi kati ya Yuda na sura ya pili ya Petro wa Pili. Hiyo yaonyesha kwamba aliandika karibu wakati mmoja na Petro, kwa kina kirefu akihangaikia hatari kwa kundi wakati huo. Kwa sababu hiyo, 65 W.K. yadokezwa kuwa ndiyo tarehe inayokaribia. Tarehe hii yaungwa mkono pia katika jambo la kwamba Yuda hataji kuingia kwa Sesho Gallo ili kukomesha uasi wa Wayahudi katika 66 W.K., wala hataji anguko la Yerusalemu katika 70 W.K. Yuda katika waraka wake arejezea hukumu zilizo wazi za kimungu zilizofikilizwa juu ya watenda dhambi, na ni jambo la akili kufikiri kwamba kama Yerusalemu lingalikuwa tayari limeanguka, yeye angaliimarisha hoja yake kwa kutaja mfikilizo huu wa hukumu, hasa kwa kuwa Yesu alitabiri tukio hilo.—Yuda 5-7; Luka 19:41-44.

YALIYOMO KATIKA YUDA

5. (a) Kwa nini Yuda aona ikihitajiwa kabisa kuwaandikia walioitwa ili ‘waishindanie imani’? (b) Ni vielelezo gani vya kuonya ambavyo Yuda ataja?

5 Maonyo juu ya uasherati na kupuuza ubwana (mist 1-16). Baada ya kuwapa salamu za upendo “hao walioitwa,” Yuda asema alikusudia kuandika “habari ya wokovu ambao ni wetu sisi sote,” lakini sasa ameona ikihitajika kabisa kuwaandikia ‘waishindanie imani waliyokabidhiwa.’ Jinsi gani hivyo? Kwa sababu watu wasiohofu Mungu wamepenya ndani, wakigeuza fadhili zisizostahilika za Mungu ziwe udhuru wa kuwa na mwenendo mlegevu. Watu hawa, asema Yuda, ‘humkana Bwana wetu Yesu Kristo.’ (Mist. 1, 3, 4) Yeye awakumbusha kwamba ingawa Yehova aliokoa watu kutoka Misri, baadaye Yeye “aliwaangamiza baadaye wale wasioamini.” Kwa kuongezea, Yehova amewaweka akibani “kwa hukumu ya siku ile kuu” malaika wale walioacha makao yawafaayo. Vilevile, adhabu ya milele juu ya Sodoma na Gomora na majiji yaliyo jirani ya hayo ni kielelezo cha kuonya juu ya msiba wa wale ‘waliofuata uasherati na kufuata mambo ya mwili yasiyo ya asili.’—Mist. 5-7.

6. Wanadamu wasiohofu Mungu wajitia katika nini, na Yuda atoaje kielezi cha ubaya na tokeo la mwenendo wao?

6 Sasa, kwa namna iyo hiyo, watu wasiohofu Mungu “huutia mwili uchafu, hukataa kutawaliwa, na kuyatukana matukufu.” Kwani, hata Mikaeli yule malaika mkuu hakusema kwa kumtusi Ibilisi alipokuwa akitoa ubishi juu ya mwili wa Musa, alisema haya tu: “Bwana [Yehova, NW] na akukemee.” Hata hivyo watu hawa hutumia usemi wa matusi na kuendelea kujipotosha kama wanyama wasiofikiri. Wameenda katika njia ya Kaini, Balaamu, na Kora mwasi. Wao ni kama miamba iliyofichwa chini ya maji, kama mawingu yasiyo ya maji, kama miti isiyo na matunda iliyokufa mara mbili na kung’olewa, kama mawimbi yenye fujo ambayo huumua (hutokeza) aibu yayo, na kama nyota zisizo na mwendo wa njia moja. Kwa hawa “weusi wa giza ndio akiba yao waliowekewa milele.” (Mist. 8, 9, 13) Henoko alitoa unabii kwamba Yehova atafikiliza hukumu juu ya watu hawa wasiohofu Mungu. Hawa ni wanung’unikaji na walalamikaji, nao wasifu nyutu za watu kwa ubinafsi.

7. (a) Mitume walionyaje kwa habari ya wadhihaki? (b) Kwa sababu ya tumaini la uhai wa milele, “waliopendwa” wapaswa kufanya nini kwa ajili yao wenyewe na wengine?

7 Shauri juu ya kubaki katika upendo wa Mungu (mist. 17-25). Yuda awakumbusha akina ndugu jinsi mitume wa Bwana Yesu Kristo walivyokuwa wakionya kwamba “katika wakati wa mwisho kutakuwako wadhihaki, wakiendelea kulingana na tamaa zao wenyewe kwa ajili ya mambo yasiyo ya kuhofu Mungu.” Wafanya-matata hawa ni “wanadamu wa kinyama, wasio na hali ya kiroho.” Kwa hiyo, “wapendwa” wapaswa kujijenga katika imani na kujiweka katika upendo wa Mungu, huku wakiingojea rehema ya Kristo “kwa tazamio la uhai wa milele.” Halafu, acheni wao nao wawatolee rehema na msaada wale wenye kuyumbayumba. Yuda afunga akipitisha katika Bwana Yesu Kristo sifa ya utukufu kwa “Mungu Mwokozi wetu,” yule Mmoja awezaye kuwalinda wasikwazike.—Mist. 18-21, 25, NW.

KWA NINI NI CHENYE MAFAA

8. Yuda alifanya utumizi gani wa Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu na wa “kitabu cha asili” katika kuwaonya kwa upole ndugu zake?

8 Yuda mwenyewe aliyaona Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu kuwa yenye mafaa kwa kuonya, kuhimiza, kutia moyo, kuagiza, na kuwaonya kwa upole “waliopendwa.” Katika kufichua ile dhambi mbaya sana ya wajidukizi (wajiingizaji) wasiohofu Mungu, yeye alitumia vielezi dhahiri kutokana na Maandiko ya Kiebrania, kama vile vya Waisraeli wenye kurudi nyuma, malaika waliotenda dhambi, na wakaaji wa Sodoma na Gomora, akionyesha kwamba wote wazoeao maovu kama hayo watapata adhabu kama hiyo. Alilinganisha wanadamu wafisadi na wanyama wasiofikiri, na kusema kwamba walikuwa wakienda katika kijia cha Kaini, wakifanya haraka kuingia katika kosa la Balaamu, na kuangamia kama Kora kwa maongezi yao ya uasi. Pia alieleza waziwazi “kitabu cha asilia.” Barua yenyewe ya Yuda yenye kusema mambo waziwazi ilikuja kuwa sehemu ya “kila andiko,” ya kujifunzwa pamoja na Maandiko mengine yote, ikionya kwa upole juu ya mwenendo unaofaa “wakati wa mwisho.”—Yuda 17, 18, 5-7, 11-13; Hes. 14:35-37; Mwa. 6:4; 18:20, 21; 19:4, 5, 24, 25; 4:4, 5, 8; Hes. 22:2-7, 21; 31:8; 16:1-7, 31-35.

9. Kwa nini onyo la Yuda bado lahitajiwa wakati huu, na ni katika maeneo gani lazima Wakristo waendelee kujijenga?

9 Upinzani na majaribu kutoka nje yalikuwa yameshindwa kuzuia ukuzi wa Ukristo, lakini sasa akina ndugu walikuwa wanahatarishwa na upotovu kutoka ndani. Miamba iliyofichwa chini ilitishia kubomoa kundi lote. Akitambua kwamba hatari hiyo ingeweza kuwa yenye kuleta uharibifu mkubwa, Yuda alitoa hoja yenye nguvu juu ya ‘kushindania imani.’ Barua yake ni ya wakati unaofaa leo kama ilivyokuwa kule nyuma. Onyo lilo hilo lingali lahitajiwa. Bado lazima imani ilindwe na kupiganiwa, ukosefu wa adili kung’olewa, wenye kutia shaka kusaidiwa kwa rehema na “kuwanyakua katika moto,” iwapo hilo lawezekana. Kwa faida ya ukamilifu wa kiadili, kufaa kiroho, na ibada ya kweli, lazima Wakristo leo waendelee kujijenga katika imani iliyo takatifu zaidi. Lazima watetee kanuni zinazofaa na kukaribia Mungu katika sala. Pia walihitaji kuwa na staha ifaayo kwa “ubwana,” wakistahi mamlaka katika kundi la Kikristo iliyopewa na Mungu.—Yuda 3, 23, 8.

10. (a) Ni lazima kundi liwatendeeje wanadamu wa kinyama, na hilo litatokeza nini? (b) Ni thawabu gani yawangoja warithi wa Ufalme, nao wajiunga na Yuda katika nini?

10 “Wanadamu wa kinyama, wasio na hali ya kiroho,” hawataingia kamwe katika Ufalme wa Mungu nao watawahatarisha tu wale walio katika njia ya uhai wa milele. (Yuda 19; Gal. 5:19-21) Ni lazima kundi lionywe juu yao, na ni lazima liwaondolee mbali! Hivyo, “rehema na amani na upendo” vitaongezwa kuelekea wapendwa, nao watajiendeleza katika upendo wa Mungu, ‘huku wakingojea rehema ya Bwana wao Yesu Kristo kwa tazamio la uhai wa milele.’ Mungu Mwokozi atawaweka warithi wa Ufalme “bila waa machoni pa utukufu wake kwa shangwe kubwa.” Kwa uhakika hawa wajiunga na Yuda katika kumhesabia Yeye “utukufu, adhama, uweza na mamlaka” kupitia Yesu Kristo.—Yuda 2, 21, 24, 25, NW.

[Maelezo ya Chini]

a The Canon of the New Testament, 1987, cha B. M. Metzger, ukurasa 138.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki