“Mwishindanie Imani”
“Wapenzi, . . . naliona imenilazimu kuwaandikia, ili niwaonye kwamba mwishindanie imani waliyokabidhiwa watakatifu mara moja tu.”—Yuda 3.
1. Ni baadhi ya mambo gani ambayo Shetani anatumia katika jitihada yake ya bure kuharibu Ukristo wa kweli?
NI LAZIMA watumishi wa Yehova washindanie imani ya kweli kwa uthabiti mwingi sana. Mpinzani wao, Ibilisi, anajaribu kutumia mateso ya moja kwa moja na “matendo ya ufundi” wenye ujanja ili aharibu uhusiano wao wenye thamani kubwa pamoja na Yehova Mungu kupitia Yesu Kristo. (Waefeso 6:11, Kingdom Interlinear Translation; 1 Petro 5:8) Katika jaribio lake la bure la kuumaliza kabisa Ukristo wa kweli, Shetani amejaribu kuubomoa nyakati nyingine. Haya ni mengine kati ya mambo ya kuchafua yanayoweza kutimiza kusudi lake: (1) Mafundisho ya uongo; (2) mwenendo mpotovu; (3) ukosefu wa imani; (4) kudharau mamlaka iliyowekwa na Mungu; (5) kunung’unika na kulalamika; na (6) kupendezwa sana na nyutu za watu kwa faida ya kichoyo.
2. Ni habari gani mbalimbali zinazotolewa hapa juu ya barua ya Yuda?
2 Yehova anatolea watumishi wake vitu vyote wanavyohitaji kiroho ili kuwalinda kisha waweze kumenyana na yule Mdanganyaji mkubwa kupita wote. (Isaya 59:1) Msaada mmoja wa namna hiyo ni ile barua ya Yuda iliyoongozwa na Mungu. Inaelekea kwamba mwanafunzi Yuda aliiandika akiwa Palestina kabla ya mwaka wa 66 W K, kwa maana yeye hataji kuinuka kwa Sesho Galo juu ya Yerusalemu mwaka huo wala hataji anguko la mji huo mikononi mwa Warumi wakiwa chini ya Tito mwaka wa 70 WK.a
3. Ni katika njia zipi barua ya Yuda iliyoongozwa na Mungu inaweza kuwa yenye faida kubwa leo?
3 Ingawa barua ya Yuda iliandikwa karne nyingi zilizopita, ina thamani kubwa kwetu sisi leo. Waangalizi wa Kikristo waliowekwa kwa roho wanaweza na wanapaswa kuitumia kama msingi wa kutolea watu mashauri. Zaidi ya hilo, tukijifunza barua hiyo kwa njia ya sala na kwa unyenyekevu, inaweza kutusaidia sisi binafsi. Hasa ndivyo ilivyo tukihisi hatari yenye kuongezeka kutokana na mafundisho ya uongo au kishawishi cha tamaa ya uasherati, tukifahamu kwamba imani yetu inapungua, au tukiona katika moyo wetu maelekeo yenye kuongezeka ya kudharau mamlaka iliyowekwa na Mungu, kulalamika kwa njia ya manung’uniko au kusifu-sifu mno watu fulani ili tuweze kujipatia faida za kichoyo. Tunapoizungumza mstari kwa mstari hii barua iliyoongozwa na Mungu, bila shaka tutaona upesi namna ya kutumia mashauri yake yenye kudumu kwa njia ya kibinafsi na katika kundi.
Ombi la Kutaka Rehema, Amani na Upendo Zaidi
4. Yuda alijitambulishaje, na kwa umaana gani?
4 Yuda alianza barua yake kwa maneno haya:
“Yuda, mtumwa wa Yesu Kristo, ndugu yake Yakobo, kwa hao walioitwa, waliopendwa katika Mungu Baba, na kuhifadhiwa kwa ajili ya Yesu Kristo.” (Yuda 1)
Akiwa “mtumwa wa Yesu Kristo,” Yuda hakuwa katika hali ya kutumikishwa ovyo tu, ya kiunyonge. Bali ‘utumwa’ huo ulitegemea uhakika wa kwamba wafuasi wa Yesu wamenunuliwa kwa damu yenye thamani kubwa ili wampe yeye utumishi wenye fadhili, kwa tazamio la uzima wa milele. Wao wamefanywa mateka na upendo wa Yesu na wakajitolea wenyewe kwake kwa moyo wa kupenda. (Mathayo 11:29, 30; linganisha Waefeso 5:21-33.) Yuda alisema alikuwa “mtumwa” wa Kristo, lakini “ndugu yake Yakobo,” na inaelekea kuwa ni Yakobo aliyekuwa mmoja wa “nguzo” za kiroho za kundi la Yerusalemu na “ndugu yake Bwana.” (Wagalatia 2:9; 1:19; linaganisha Matendo 12:17; 15:13-21.) Kwa hiyo kwa wazi Yuda alikuwa ndugu-mzazi-mmoja-na-Yesu, lakini kwa unyenyekevu yeye hakujitafutia umashuhuri (ukubwa) kwa sababu ya uhusiano wake wa kijamaa pamoja na Mwana wa Mungu.—Marko 6:3.
5. (a) Ni nani waliokuwa wale “walioitwa”? (b) Hao “walioitwa” ‘walihifadhiwaje kwa ajili ya Kristo’? (c) Zaidi ya hao “walioitwa,” barua ya Yuda ni yenye kutia moyo kwa akina nani?
5 Barua ya Yuda ilikusudiwa ienezwe kote kote kusaidia jumla ya watu. Ilitumwa kwa “walioitwa,” yaani, kwa wale walioitwa na Mungu kwenye ufalme mtukufu wa kimbingu wa Mwanawe. (Yohana 6:44; linganisha Matendo 16:14.) Yehova aliwapenda hawa “walioitwa,” na ilikuwa raha njema yake kuwapa ufalme kama wao binafsi walidumisha hali ya kiroho yenye kukubalika. (Luka 12:32; Warumi 8:38, 39; linganisha Isaya 52:11.) ‘Walihifadhiwa kwa ajili ya Yesu Kristo’ kwa maana ya kwamba Yehova Mungu aliwalinda kwa sababu walikuwa katika mwungano pamoja na Mwanawe, wakiwa washiriki wa mwili wake. Wakiwa waaminifu, wangeshirikiana na Yesu katika ufalme wake. (Waefeso 4:15, 16; 2 Timotheo 1:12; 1 Petro 1:3-5) Lakini onyo zuri la upole la barua hii halihusu hao “walioitwa” peke yao. Linaweza pia kuutia sana moyo “mkutano mkubwa” wa washikamanifu wengine ambao leo wanashiriki pamoja na “ndugu” za kiroho za Kristo katika kuwa watumwa kwa ajili ya ufalme.—Mathayo 24:14; 25:34-40; Ufunuo 7:4, 9, 15.
6. Ni katika njia zipi rehema ya Mungu ilikuwa imeonyeshwa kuelekea waabudu wenzi wa Yuda?
6 Halafu, Yuda alieleza maoni haya kutoka moyoni ndani:
“Mwongezewe rehema na amani na upendano.” (Yuda 2)
Wale walioandikiwa barua ya Yuda walipewa rehema, amani na upendo wa kimungu walipokuwa waamini walio wakf, kisha wakapokea msamaha wa Yehova juu ya dhambi zao kupitia Yesu Kristo. Rehema ya Mungu ilionyeshwa katika msaada wa ukombozi alioufanya kupitia Yesu. (Tito 3:4-7) Udhihirisho (wonyesho) mwingine wa rehema ya Mungu ulikuwa kutokuwa chini ya utumwa wa sheria ya Musa, utumwa wa mapokeo yasiyo ya Kimaandiko, utumwa wa mwenendo usiomheshimu Mungu na kadhalika. (Warumi 7:4; Wagalatia 5:13; 1 Petro 1:18, 19; linganisha Ufunuo 18:1-5.) Yehova alionyesha rehema zaidi alipowahifadhi kwa ajili ya Yesu Kristo, wapate kutumikia wakiwa watumwa wake, kama vile wakati wa kuitangaza “habari njema.” (Marko 13:10, NW) Katika sala yake Yuda alitaka waabudu wenzake wawe na rehema ya kimungu kwa kadiri iliyoongezeka.
7. Wakristo wanaipata amani kwa sababu gani na kwa namna gani?
7 Vilevile Yuda alisali waamini wenzake wapate amani iliyoongezeka. Kwa sababu ya kujiweka wakf kabisa kwa Mungu, Mashahidi wa Yehova leo wana uhusiano wa karibu sana na yeye. Hivyo wana amani pamoja na Yehova na vilevile wanayo “amani ya Mungu, ipitayo akili zote,” utulivu wa moyo na akili ambao wasioamini hawafahamu. (Wafilipi 4:6, 7; Wakolosai 1:19, 20) Isitoshe, wanasitawisha na kuonyesha amani, tunda la roho ya Mungu, nao wanaweza kufuatia amani pamoja na wanadamu wenzao. (Wagalatia 5:22, 23; Waebrania 12:14) Halafu, pia, Wakristo waaminifu hawaogopi wala wakati ujao wala kifo chenyewe, bali wana amani, wakijua kwamba Yehova yu pamoja nao na anazifanya kazi zake zote zishirikiane kwa faida ya wale wanaompenda.—Mathayo 10:28; Warumi 8:28.
8. Upendo wa Yehova umeonyeshwaje kwetu?
8 Upendo mkuu wa Yehova ulionyeshwa kwa kumtoa Mwanaye “ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Tulipokuwa tungali wenye dhambi tusiwe na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova, aliuonyesha upendo huo kwetu. (Warumi 5:8) Lakini, kwa kuamini mpango huo wa ukombozi, tunahitaji kujiweka wenyewe katika upendo wa Mungu. Vilevile Yuda alisali ili upendo uongezeke kuelekea wale alioandikia barua yake.
9. Ni kwa sababu gani waamini wenzi wa Yuda walihitaji rehema, amani na upendo kwa kadiri iliyoongezeka?
9 Yuda alisali ili rehema ya Mungu, amani na upendo viongezeke kuelekea waamini wenzake wapendwa kwa sababu hali yao ya kiroho ilikuwa ikihatirishwa. Kwa sababu hiyo, walihitaji rehema ya Mungu, amani na upendo kwa wingi unaozidi wakati wo wote uliotangulia.
“Mwishindanie Imani”
10. Yuda alikuwa amekusudia kuandika juu ya nini?
10 Kisha Yuda alikazia uzito wa mambo, akisema:
“Wapenzi, nilipokuwa nikifanya bidii sana kuwaandikia habari ya wokovu ambao ni wetu sisi sote, naliona imenilazimu kuwaandikia, ili niwaonye kwamba mwishindanie imani waliyokabidhiwa watakatifu mara moja tu.” (Yuda 3)
Kutumia kwa Yuda usemi wenye kuonyesha mapenzi “Wapenzi” kulihakikishia waabudu wenzake shauku yake ijapokuwa ujumbe wake wenye nguvu. (Yohana 13:35; linganisha Warumi 1:7; 3 Yohana 1, 2.) Alikuwa amekusudia kuandika juu ya ‘wokovu wa wote’ wale “walioitwa” kwenye ufalme wa kimbingu. (Wagalatia 3:26-29) Ulihusiana na lile tumaini lenye thamani la wokovu ambao Wakristo walikuwa nalo ‘katika imani waliyoishiriki’ wakati wa Yuda.—Tito 1:4.
11. Ni nini iliyokuwa “imani waliyokabidhiwa watakatifu”?
11 Ile “imani waliyokabidhiwa watakatifu” ilikuwa ni jumla ya imani juu ya Yehova Mungu na ufalme wake waliyokabidhiwa Wakristo na Yesu na wanafunzi wake walioongozwa kwa roho. Kwa wazi, ilikabidhiwa “mara moja tu” katika maana ya kwamba wafuasi waliopakwa mafuta wa Yesu, wale “watakatifu,” waliipokea karne kumi na tisa zilizopita kuwa ndizo habari njema peke yake za kweli. Inaendelea kuwa ndiyo “imani” ambayo Mashahidi wa Yehova leo wanafahamu ni lazima washikamane nayo sana, kwa kuwa hakuna habari njema au ujumbe mwingine wa wokovu unaostahili kuaminiwa. (Wagalatia 1:6-8) Na sehemu iliyo kubwa ya habari njema hizo ni ya kwamba Yesu Kristo aliufia ulimwengu mzima wa wanadamu. Kwa hiyo ni ya maana sana sana kwa ule “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wa wakati wetu.—Yohana 10:16; 1 Yohana 2:1, 2; Ufunuo 7:9.
12. Sababu gani Yuda aliandika ili awatie moyo waamini wenzake ‘waishindanie imani’?
12 Katika wakati wa Yuda walimu wa uongo wenye kujidai kuwa Wakristo walikuwa wakijitahidi kuingiza kwa hila habari njema ya bandia katika watu wa Mungu. Mafundisho hayo yalitisha kuharibu imani na wokovu wao. (Mathayo 24:13; 2 Wakorintho 11:3, 4) Kwa sababu hiyo, ili kuzuia jambo hilo lisisitawi, na kama alivyoongozwa na roho takatifu na upendo, Yuda ‘aliona ilimlazimu’ aandike barua na kuwatia moyo waamini wenzake ili ‘waishindanie imani.’
13. Ili kuepuka kudanganywa na kupoteza wokovu, ni lazima Mashahidi wa Yehova leo wafanye nini?
13 Ikiwa sisi mashahidi Wakristo wa Yehova wa leo, tunataka kuendelea kuwa washikamanifu kwa Mungu na kuepuka kudanganywa na kupoteza wokovu, sisi, vilevile, ni lazima ‘tushindane’ dhidi ya habari njema yo yote ya uongo, tupinge kwa bidii, tushindane mweleka na jitihada za kuongeza au kuondoa cho chote katika mafundisho ya Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho yake, lililosafishwa. (Kumbukumbu la Torati 4:2; Mithali 30:5, 6; Ufunuo 22:18, 19) Ni lazima tuyapime mafundisho yo yote mapya au ya kigeni kwa msaada wa Neno zima la Mungu na kushikamana sana na ile imani inayoongoza kwenye wokovu.—Waebrania 1:1, 2; 2:3, 4.
14, 15. (a) Ni katika njia gani Yuda alieleza ile sababu ya kubadili kusudi lake la barua? (b) Ni kwa sababu gani walimu wa uongo hawangefanikiwa kupindua au kulichafua kundi zima la Kikristo?
14 Akieleza badiliko lake la kusudi la kuandika, Yuda alisema:
“Kwa maana kuna watu waliojiingiza kwa siri, watu walioandikiwa tangu zamani hukumu hii, makafiri, wabadilio neema ya Mungu wetu kuwa ufisadi, nao humkana yeye aliye peke yake Mola, na Bwana wetu Yesu Kristo.” (Yuda 4)
Watu hao waliokuwa ‘wamejiingiza kwa siri’ miongoni mwa Wakristo wa kweli walifundisha uongo. (Linganisha Wagalatia 2:4; 1 Yohana 2:19) Yesu alikuwa ametabiri mwendo wa adui wenye kusudi la kupotoa watu wa Yehova, kwa maana alionyesha kwamba yule Ibilisi angepanda “magugu,” au Wakristo wa uongo, miongoni mwa “ngano,” au wafuasi wa kweli wa Kristo. (Mathayo 13:24-30, 36-43) Vilevile kulikuwa kumekuwako maonyo ya mitume juu ya ukafiri (ukengeufu), Petro hasa alitaja “waalimu wa uongo.”—2 Petro 2:1; Matendo 20:29, 30; 2 Wathesalonike 2:3.
15 Walakini, watu hao waovu hawangefanikiwa kupindua au kulichafua kundi zima. “Tangu zamani,” hata kabla ya unabii wa uaminifu wa Henoko, watu hao waliwekwa ili wapate hukumu kali ya Mungu. (Mwanzo 3:15; 5:21-24; Yuda 14, 15) Kwa wazi “hukumu hii” inaelezwa na yanayofuata katika barua ya Yuda.
16. “Makafiri” walikuwaje na hatia ya ‘kuibadili neema ya Mungu wetu kuwa ufisadi,’ na kufikiri kwao kulikuwa na kasoro gani?
16 Walimu hao wa uongo walikuwa “makafiri,” au wale “wasio na heshima kwa Mungu.” (The New Testament in Modern English, iliyotafsiriwa na J. B. Phillips) Waliwatazama watu wa Yehova waliotakaswa kwa madhumuni yasiyo safi na macho machafu. Watu hao wasio na heshima walikata kauli kwa makosa kwamba kwa vile Mungu alivyowasamehe wale ambao zamani walikuwa waasherati, waabudu sanamu, wazinzi, na kadhalika, angekuwa mwenye rehema sana hata amsamehe mtu ambaye kwa kukusudia angerudia mambo hayo yenye dhambi. Walidhani kwa makosa kwamba wangeweza kuzivunja sheria za Mungu za adili wasiwe na hatia, kisha watubu na kuendelea kuwa mionogni mwa watu wa Yehova mpaka wakati mwingine tena ambapo wangetamani kuingia katika dhambi na ‘kutongoza nafsi zisizo imara’ ziingie katika ufisadi. (2 Petro 2:14, NW) Hivyo “makafiri” hao walikuwa na hatia ya ‘kuibadili neema ya Mungu wetu kuwa ufisadi.’ Kwa kweli wao hawakuthamini wala kukiri kwamba Mungu alikuwa mwenye rehema kwa kuosha dhambi za waamini katika damu ya Kristo hivyo wapate baada ya hapo kufuatia mwendo wa uadilifu.—Warumi 6:11-23; 1 Wakorintho 6:9-11.
17. Ni katika njia gani huenda wengine ‘wakamkana yeye aliye peke yake Mola, na Bwana,’ na kinachowangojea ni nini?
17 Iwapo wo wote kati yetu sisi Mashahidi wa Yehova walio wakf, wangefuata watu hao makafiri na kuwa watumwa wa dhambi kwa ajili ya anasa ya mwili ya kichoyo, tungekuwa ‘tukimkana’ yeye aliyetununua kwa damu yake ya thamani. Tungekuwa tukimkana Yesu Kristo asiwe Mwenyeji na Bwana wetu. (1 Wakorintho 7:22, 23) Kwa kuwa uharibifu unawangoja wale wanaofanya hivyo, ni jambo la maana sana kama nini kwetu kuwapinga watu hao waovu!
Shauri Lenye Nguvu kwa Wakati Wetu
18, 19. (a) Ni mwendo gani wenye dhambi ambao wengine wenye kujidai kuwa Wakristo wameufuata? (b) Wengine wamevutwaje? (c) Ni shauri gani lililoongozwa na Mungu ambalo limepasa kuwasaidia Wakristo waaminifu wajiandae vizuri zaidi ili ‘waishindanie ile imani’?
18 Leo wachache ambao wameshirikana na kundi la Mashahidi wa Yehova wametaka kuendeleza mafundisho ya uongo na mwenendo mpotovu. Jamaa hao washupavu hawajali viwango vya uadilifu vya Mungu nao ni hatari sana kwa Wakristo washikamanifu.
19 Inasikitisha kusema kwamba wafuasi wa Yesu Kristo wenye bidii, wenye kufuata uadilifu, wanaweza kuvutwa na mafundisho ya uongo na mwenendo mpotovu. Lakini shauri lenye nguvu la Yuda nguvu walio waaminifu ili wasizikubali jitihada hizo za Kishetani ziharibu uhusiano wao na Yehova Mungu. Na sasa tunapoendelea kuichunguza barua ya Yuda iliyoongozwa na Mungu, na tujiandae vizuri zaidi ili ‘tuishindanie ile imani.’
[Maelezo ya Chini]
a Ona Aid to Bible Understanding, kur. 978, 979; “All Scripture Is Inspired of God and Beneficial,” kur. 259, 260.
Unaweza kujibu maulizo haya?
□ Barua ya Yuda inashughulika na mambo gani yanayoweza kuhatirisha Wakristo wa kweli?
□ Barua ya Yuda ni yenye thamani kubwa kwetu namna gani?
□ Ni kwa sababu gani wale ambao Yuda aliandikia wangehitaji rehema, amani na upendo kwa kadiri iliyoongezeka?
□ Ni ipi iliyo “imani waliyokabidhiwa watakatifu”?
□ Ni kwa sababu gani Yuda aliwasihi waamini wenzake ‘waishindanie ile imani’?
[Picha katika ukurasa wa 21]
Je! wewe, kama Wakristo waaminifu katika vipindi vyote, ‘unaishindania kwa uhakika ile imani’?