Tunaweza ‘Kushangilia Siku Zetu Zote
“Utushibishe asubuhi kwa fadhili zako, nasi tutashangilia na kufurahi siku zetu zote.”—Zaburi 90:14.
1. Yehova anaonyeshaje kwamba anataka watu wake na furaha?
YEHOVA MUNGU anataka watu wake wawe wenye furaha. Anajua kwamba raha yenye kutoka moyoni inahitajiwa kabisa ndipo mtu aweze kuridhika na kuwa na maisha yenye afya. (Mithali 17:22) Kwa hiyo, Yehova akiwa ni Mungu wa fadhili za upendo, anatoa uongozi utakaozidisha maoni ya kujiona wenye furaha ikiwa uongozi huo utatumiwa maishani.
2. Kwa sababu gani Wakristo wa kweli wanaweza kuwa na uhakika wanaposali kuomba furaha?
2 Mashahidi wa Yehova, walio Wakristo wa kweli, wanaweza kusali wapewe furaha wanapoelekeana na mikazo ya maisha katika mfumo wa mambo usiomcha Mungu. Furaha ni tunda la roho takatifu ya Mungu, naye anawapa roho hiyo watu wake waaminifu waliojiweka wakf ambao wanaiomba. (Luka 11:13; Wagalatia 5:22, 23) Wao wanaweza pia kutoa maoni kama haya ya moyoni yaliyotamkwa katika sala na Musa nabii wa Mungu: “Utushibishe asubuhi kwa fadhili zako, nasi tutashangilia na kufurahi siku zetu zote.” (Zaburi 90:14) Wale wanaomtumaini Yehova wanaweza kuwa na uhakika kwamba atayajibu maombi hayo yenye kutolewa kwa bidii.—1 Yohana 5:13-15.
3. III tuweze ‘kushangilia siku zetu zote,’ ni lazima tufanye mambo gani mawili ya msingi?
3 Lakini, zaidi ya kusali kuna mambo mawili ya msingi ambayo ni lazima tukumbuke ndipo tuweze ‘kushangilia siku zetu zote.’ Yalikaziwa wakati watu wa Mungu wa nyakati za kale walipoambiwa kwamba laana zingewaangukia ‘wasipoisikiliza sauti ya Yehova kwa kushika amri zake,’ na ‘wasipotumikia Yehova kwa kushangilia na furaha ya moyo.’ (Kumbukumbu la Torati 28:45-47, NW) Kwa hiyo, ili tuweze kuwa na furaha maisha yetu yote, ni lazima sisi (1) tumtii Yehova na (2) kumtumikia kwa furaha.
4. (a) Yehova anatoa nini ili watu wake waweze kumtumikia wakiwa na moyo wenye kujaa furaha? (b) Ni semi gani zenye hekima tunazoweza kufikiria, na matokeo yatakuwa nini?
4 Yehova anawatolea watu wake kichocheo wanachohitaji pamoja na msaada ili wamtumikie kwa moyo wenye kujaa furaha. Zaidi ya hilo, yeye anatoa kwa neema miongozo yenye kutegemeka inayoendeleza furaha. Kwa mfano, angalia namna semi zenye hekima zilizo katika visehemu fulani vya kitabu cha Biblia cha Mithali zinavyoweza kutokeza furaha nyingi sana. Mashauri hayo yanaweza kutufanya ‘tushangilie siku zetu zote’ tukiyatumia maishani.
Furaha Ndani ya Jamaa
5. (a) Yehova anatazamia nini kwa wazazi? (b) Kwa habari ya utii, watoto wanaweza kuwa na matokeo gani ndani ya jamaa?
5 Ili kupata na kudumisha furaha ya jamaa, watu wanahitajiwa kabisa wamtii Mungu, wawe wepesi wa kuitikia mashauri yaliyo katika Neno lake. Kwa mfano, Yehova anatazamia wazazi wafanye yote wawezayo wazoeze watoto wao. Baba ndiye anayepaswa kuongoza katika jambo hilo, lakini mama anapaswa ashiriki kwa bidii. (Mithali 22:6; 31:1) Namna gani watoto? Mtoto “amdhihakiye babaye na kudharau kumtii mamaye” hatafanikiwa kamwe. Atawaletea wazazi wake kihoro, wala si furaha. (Mithali 30:17; 17:21) Kwa upande mwingine, wana na binti wenye hekima wanaokubali kwa utii nidhamu wanayopewa na wazazi wacha Mungu na kuishi kupatana na kanuni za Maandiko wanaletea jamaa zao furaha na heshima.—Mithali 10:1; 15:20; 23:15,15, 16.
6, 7. (a) Ni shauri gani linalotolewa kwenye Mithali 23:22-25, na matokeo yanakuwa nini likifuatwa? (b) Lile shauri linalosema “inunue kweli, wala usiiuze’ lina maana gani?
6 Wazazi wacha Mungu wanaolea watoto wao kwa njia inayovuta watoto wafuatie mwendo wa uadilifu wana sababu ya kuwa na furaha halisi. Kuhusu jambo hilo tunaambiwa hivi katika Maandiko: “Msikilize baba yako aliyekuzaa, wala usimdharau mama yako akiwa mzee. Inunue kweli, wala usiiuze; naam, hekima, na mafundisho [nidhamu], na ufahamu. Baba yake mwenye haki atashangilia; naye amzaaye mtoto mwenye hekima atamfurahia. Na wafurahi baba yako na mama yako na afurahi aliyekuzaa.”—Mithali 23:22-25.
7 Mtoto mwenye hekima atatii mafundisho ya kiroho ya baba yake Mkristo wala hatapuza maneno ya mama yake mcha Mungu, hata kama mama huyo amekwisha kuwa mzee. Ingawaje, mtu mzima mwenye kujua la kufanya anaweza bado kujifunza jambo fulani kutokana na wazazi wake wazee. Ni wazi kwamba lile shauri linalosema “inunue kweli, wala usiiuze” linamaanisha kushikilia sana kanuni za kweli ili ziwe mwongozo maishani. Mtoto mwenye maelekeo ya uadilifu hataachilia kweli mbali ili ajipatie raha mbalimbali, apate mali wala heshima. Hakika jamaa ambayo washiriki wote wanaambatana sana na Yehova itakuwa na furaha yenye kudumu.—Kumbukumbu la Torati 10:20, 21.
Kudumisha Furaha Wajapokuwako Watenda Makosa
8, 9. Kama inavyoonyeshwa kwenye Mithali 2:10-14, kutumia hekima ya kimungu kunaweza kutulindaje tusipatwe na madhara ya watenda makosa?
8 Kutii mashauri ya Yehova kunatusaidia tudumishe furaha tukiwa chini ya hali mbalimbali. Kwa mfano, kwa kutumia hekima ya kimungu, tunaweza kupata ulinzi wa kutokupatwa na madhara ya watenda makosa. Maandiko yanasema hivi: “Maana hekima itaingia moyoni mwako, na maarifa yatakupendeza nafsi yako; busara itakulinda; ufahamu utakuhifadhi. Ili kukuokoa na njia ya uovu, na watu wanenao yaliyopotoka; watu waziachao njia za unyofu, ili kuziendea njia za giza; wafurahio kutenda mabaya; wapendezwao na upotoe wa waovu.”—Mithali 2:10-14.
9 Kibali ya Yehova inakalia wale wanaothamini sana hekima ya kweli na kuacha mioyo yao iongozwe na hekima hiyo. Kwa hekima wao wanaepuka ushirika wa mtu ye yote ‘anenaye yaliyopotoka,’ yaani, mambo yaliyo kinyume cha kweli na haki. Uwezo wa kufikiri inavyofaa na busara ya kweli ni ulinzi wa kujiepusha na wale wanaokataa hekima ya kimungu, wanaofurahia vitendo viovu na kujaribu kuchafua wengine.—Linganisha Mithali 4:16.
10. Kosa la mtu mbaya linamtegaje yeye?
10 Huenda mtenda kosa ‘akafurahia kutenda mabaya,’ lakini je! Ni nani mwenye furaha ya kweli? Mithali nyingine inajibu hivi: “Kuna mtego katika kosa la mtu mbaya; bali mwenye haki huimba na kufurahi.” (Mithali 29:6) Ndiyo, kosa la mtu mbaya linamtia yeye katika mtego. Huenda dhambi moja ikamwongoza kwenye nyingine, naye anaweza kupatwa na ole mwingi bila kutazamia. Kwa mfano, huenda akatunga hila ya kumhadaa (au kuumiza) mtu mwingine, lakini lo, anajikuta katika kitanzi alichompangia mwenzake. Katika Israeli wa kale, ingewezekana shahidi wa uongo kujaribu kufanya mtu asiye na hatia aelekee kuuawa kwa kutoa ushuhuda wa uongo juu ya mtu huyo. Lakini mtunga hila mwenyewe ndiye aliyekuwa akiuawa ikiwa mpango wake wa hila uligunduliwa.—Kumbukumbu la Torati 19:16-21.
11. Kwa sababu gani mtu aliye na maelekeo ya uadilifu anaweza ‘kushangilia kwa furaha’?
11 Basi hali ya mtu mwadilifu ni afadhali zaidi. Yeye wala hatungi hila juu ya jirani yake wala hazoei dhambi. Kwa sababu hiyo, anaepuka kutegwa na kosa na hapatwi na matata yanayofuatana na kutenda kosa wala hapati adhabu ya kugunduliwa kuwa ni mtenda kosa mwenye hila. Basi mtu mwenye maelekeo ya uadilifu “huimba na kufurahi.” Kwanza, yeye hapati pigo la dhamiri yenye hatia. Zaidi ya hilo, anafurahia upendeleo wa Mungu, “kwa maana mtu wa kupotoka-potoka ni kitu cha kuchukiza sana Yehova, lakini usiri Wake u pamoja na walio wanyofu.”—Mithali 3:32, NW.
Je! Tufurahi Wakati Adui Anapopatwa na Mabaya?
12. Inampasa Mkristo awe na maoni gani adui akipatwa na mabaya? Kwa sababu gani?
12 Lakini, inampasa Mkristo awe na maoni gani adui akipatwa na mabaya? “Usifurahi, adui yako aangukapo,” inasema mithali nyingine, “wala moyo wako usishangilie ajikwaapo.” Kwa sababu gani? “[Yehova] asije akaliona hilo, likamkasirisha; akageuzia mbali naye hasira yake.” (Mithali 24:17, 18) Hapo inakatazwa kabisa ile inayoweza kuitwa furaha ya kutakia watu madhara, kufurahi wakati adui anapopatwa na msiba wa namna fulani. Kwa kuwa lingekuwa kosa kutakia adui mabaya kwa sababu tu mtu anataka kujiridhisha binafsi, mwenye kufurahi angebidishwa kumtolea Yehova hesabu kwa dhambi yake. Basi, Mungu anaweza kuusoma moyo na kwa hiyo anajua kama tunashangilia kwa siri mabaya yaliyopata mtu mwingine. Basi, ijapofichika kwa wanadamu wenzetu hiyo roho mbaya, iko wazi kwa Yehova, anayesema hivi: “Kisasi ni changu mimi, na kulipa.” (Kumbukumbu la Torati 32:35; Waebrania 10:30) Kwa hiyo, huenda Mungu akamwadhibu kwa njia fulani huyo mwenye kusimanga (kufurahia msiba wa mwenzake).—Linganisha Mithali 17:5.
13. Ni nini maana ya Mithali 11:10?
13 Kwa upande mwingine, tunaambiwa: “Wenye haki wasitawipo, mji hufurahi [huterema]; waovu waangamiapo, watu hupiga kelele [ya furaha].” (Mithali 11:10) Maneno hayo yafahamike kuwa na maana gani? Kwa ujumla watu wenye haki (waadilifu) wanapendwa na kufurahisha jirani zao. Lakini hakuna mtu anayependa sana “waovu.” Mtu mkatili anajiletea mwenyewe hali ya kuepukwa na wengine. (Mithali 11:17) Tena, wakati waovu wanapokufa kwa ujumla watu hawawaombolezi na kwa uhakika kusingekuwa na huzuni Yehova akiwaangamia watenda makosa hao. Bali, kungekuwa na furaha kwa sababu wameondolewa kati ya watu. Je! sisi tunajiendesha kwa njia inayozidisha furaha au ‘mteremo’ wa wengine?
Moyo Wenye Kujaa Furaha Ni Baraka
14. Kama ilivyokwisha. kuzungumzwa kufikia hapo kumtii Yehova kunatuwezeshaje ‘tushangilie siku zetu zote’?
14 Kumtii Yehova kunatuwezesha ‘tushangilie siku zetu zote.’ Kama ilivyo kwisha kutajwa, wakati mashauri ya kimungu yanapotumiwa maishani uhusiano wa wazazi na mtoto unakuwa wa furaha. Kukubali mwongozo wa Mungu kunatulinda na mavutano mabaya ya watenda makosa na kutufanya tufurahi. Kuongezea hilo, kushikilia sana mafundisho ya Yehova kunatuepusha na hali ya kukuza nia mbaya kuhusu maafa yo yote ya waovu, na hivyo tunaweza kudumisha furaha. Ndivyo, kwa kumtii Yehova Mungu tutakuwa na moyo wenye kujaa furaha. Hali hiyo yenyewe ni baraka.
15. Badala ya kuruhusu “hangaiko” lifanye moyo wetu ‘uiname’ kwa huzuni, inatupasa tufanye nini, na kwa sababu gani?
15 Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema: “Moyo wa furaha huchangamsha uso; bali kwa huzuni ya moyo roho hupondeka.” (Mithali 15:13) Ni kweli kwamba maoni ya furaha na huzuni yanaonekana katika uso wa mtu. Bila shaka, kuna mahangaiko mengi maishani na yanaweza kutuhuzunisha sana. “Hangaiko katika moyo wa mtu ndilo litakalofanya uiname,” inasema mithali nyingine, “lakini neno lililo jema ndilo linalofanya ushangilie.” (Mithali 12:25, NW) Basi, badala kuruhusu “hangaiko” lifanye mioyo yetu ‘iiname’ kwa huzuni, ni jambo la hekima sana kumkaribia Yehova kwa kuitafakari ile bohari (ghala) ya mambo mema, Neno aliloliongoza kwa roho yake! Kwa uhakika kufanya hivyo kunaweza kurudisha furaha ndani ya moyo wenye huzuni lakini wenye uadilifu.
16. (a) Ripoti nzuri ‘inanenepeshaje mifupa’? (b) Ingawa ‘moyo wenye kujawa na furaha ni dawa nzuri,’ inatupasa tuwe na maoni ya namna gani juu ya kucheka-cheka daima?
16 Sulemani alisema hivi pia: “Mng’ao wa macho huufurahisha moyo; habari njema huinenepesha mifupa.” (Mithali 15:30) Habari njema “huinenepesha mifupa,” yaani, zinaijaza mafuta katika matundu yake. Hivyo mwili mzima unatiwa nguvu na moyo unajulikana kuwa umejaa furaha wakati macho yanapong’aa kwa uangavu mwingi. Ijapokuwa huzuni au ‘roho iliyopigwa’ inakuwa na matokeo mabaya mwilini, ‘moyo wenye kujaa furaha ni dawa nzuri.’ (Mithali 17:22, NW; linganisha The Amplified Bible.) Hata hivyo, ni wazi kwamba moyo haupasi kuwa wenye kutokeza-tokeza daima kicheko cha kiujinga, kwa maana Sulemani alisema “juu ya kicheko, Ni wazimu; na juu ya furaha, Yafaa nini?” (Mhubiri 2:2) Walakini, kwa uhakika mtu anafaidiwa na moyo unaoshangilia katika kutenda mapenzi ya Mungu.
17, 18. (a) Kwa sababu gani rafiki mwaminifu anaweza kufananishwa na ‘mafuta na ubani unaofanya moyo ushangilie’? (b) Ni kwa njia gani Yesu Kristo amekuwa Rafiki wa kimbingu aliye msema-wazi? (c) Ni ulizo gani la kibinafsi linalotokezwa?
17 Ikitaja jambo jingine linalotokeza furaha, mithali nyingine inasema: “Mafuta na ubani ndivyo vinavyofanya moyo ushangilie, pia utamu wa mwenzi wa mtu kwa sababu ya shauri la nafsi.” (Mithali 27:9, NW) Sawa na vile mafuta yanavyoburudisha na kutuliza maumivu na ubani kuleta raha kwa sababu ya manukato yake, rafiki mshikamanifu anayetoa mashauri akiwa na shabaha ya kusaidia mtu anaufanya moyo wa mpokea-mashauri ushangilie. Kuna utamu katika urafiki wa namna hiyo, kwa maana wale wanaoambiana mambo wazi bila kuogopana wanaweza kusaidiana wafanye maendeleo, wafanye masahihisho ya makosa yao na kujitia nguvu katika pande fulani za maisha yao ambazo ni dhaifu. Kwa kweli, kuwa na rafiki mwema anayefikiria mambo kwa unyofu na kukuambia mambo kimachomacho kunaweza kuleta furaha.
18 Yesu Kristo aliyetukuzwa ni Rafiki wa kimbingu aliye msema-wazi ambaye alielekeza ujumbe mbalimbali kwa yale makundi saba yaliyotajwa katika Ufunuo, sura ya pili na ya tatu. Pongezi (sifa) zilitolewa zilipofaa, lakini maonyo ya upole yalitolewa pia. Kwa mfano, kundi lililokuwako Efeso lilikuwa limepoa katika juhudi nyingi ya upendo wa Kikristo liliokuwa limemwonyesha Yehova hapo kwanza. Lakini Yesu alitaka kuuwasha tena upendo huo. (Ufunuo 2:1-7) Mkristo ye yote Mwefeso aliyelifikiria kisala shauri hilo la Rafiki huyo wa kimbingu kisha akajisahihisha pande alizokuwa akikosea angeweza kuendelea kumtumikia Yehova akiwa na moyo wenye kujaa furaha. Je! wewe binafsi unaona mahali unapohitaji kuchukulia hatua za marekebisho ili uthibitishe unapenda Mungu kwa kufanya maendeleo katika utumishi unaomtolea Yehova?
Kushangilia Katika “Ile Kazi Takatifu”
19. Kwa sababu gani inampasa kila mtu aliyejiweka wakf kwa Yehova agawie wengine “habari njema kwa ukawaida?
19 Ulizo jingine ni hili: Je! wewe unajitia katika ile kazi takatifu ya habari njema za Mungu’ kwa moyo wote, kwa ukawaida na kwa furaha? (Warumi 15:16, NW) Hakuna utendaji mwingineo duniani unaoipita kazi hiyo kwa ubora. Hivyo ni sababu kuu inayofanya kundi la kikristo liweze kuendelea kuwako! (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Kwa hiyo kila mtu aliyejiweka wakf kwa Yehova anapaswe awe akigawia wengine “habari njema kwa ukawaida. Na mara nyingi watangazaji wa ufalme wenye bidii wanapata maono na baraka kubwa sana katika utumishi wa Yehova mpaka mioyo yao inawavuta ‘kushangilia kwa furaha.’—Zaburi 90:14; Malaki 3:10.
20. Mara kwa mara, ni kwa njia gani wahubiri wa kundi wenye juhudi na madaraka mazito ya Kimandiko wameongeza furaha yao katika utumishi wa Yehova?
20 Wahubiri wa kundi wenye juhudi na madaraka mazito ya Kimaandiko wanaongeza furaha yao mara kwa mara kwa kufanyia maendeleo ubora wa utumishi wanaomtolea Yehova. Zaidi ya hilo, jamaa fulani za Kikristo zimepata uradhi wa kweli kwa kutumikia mahali ambako kuna uhitaji mkubwa wa watangazaji wa ufalme. Wengine wamefurahia kazi ya kutoa ushuhuda wakati wote wakati wa miezi fulani ya mwaka, na bado wengine wakaweza kushiriki kwa ukawaida katika huduma ya wakati wote. Yehova anapendezwa sana na jitihada hizo zenye bidii na zenye kufanywa kwa moyo wote.—Marko 12:29, 30.
21. Wenye kuhitimu masomo katika Shule ya Biblia ya Gileadi wana sababu gani ya kushangilia?
21 Wanaume na wanawake wengi Wakristo wamehitimu masomo ya Shule ya Biblia ya Gileadi, nao wanashangilia katika kutumia nishati zao wakimtumikia Yehova katika sehemu mbalimbali za dunia. Wanapendezwa kuwa wahudumu wa wakati wote wanaoweza kusaidia watu wengi wajue habari za Yehova Mungu na makusudi yake yaliyo mazuri ajabu. Kwa mfano, baada ya kutumia zaidi ya miongo miwili (miaka zaidi ya 20) akiwa misionari katika Afrika Magharibi yenye joto jingi, misionari mmoja aliandika hivi: “Je! Mimi najisikia kwamba wakati umefika wa kuiacha kazi ili walio vijana kuliko mimi ndio waiendeshe? Hapana, ninapoona baraka na ukuzi wa tengenezo la Yehova ninajisikia kama Kalebu, baada ya yeye kuhifadhiwa hai muda wa miaka zaidi ya 45, akiwa mkaaji wa jangwani mpaka alipokuja kuiingia Nchi ya Ahadi. Yeye alisema: ‘Hata sasa mimi nina nguvu zangu hivi leo kama nilivyokuwa siku hiyo Musa aliyonituma; kama nguvu zangu zilivyokuwa wakati huo, na nguvu zangu ndivyo zilivyo sasa.’ (Yoshua 14:11) Ijapokuwa kumekuwa na hali zisizofaa na hata magumu, miaka hiyo iliyopita imekuwa ni mazoezi bora kabisa na matayarisho kwa ajili ya wakati ujao.”
22. Utumishi wa Betheli ni nini, na mwanamke mmoja mwenye pendeleo alitoa maoni gani?
22 Pendeleo jingine la furaha, lililo wazi kutumikia huko betheli. Linahusu kazi inayoambatana moja kwa moja na uchapishaji wa vitabu vya habari za Biblia na kusonga mbele kwa faida za ufalme. Wenye kupendelewa hivyo wanatumikia ama wakiwa sehemu ya wafanya kazi wa Betheli wa Sosaiti huko New York State, ama wakiwa pamoja na jamaa zilizo kwenye maafisi ya matawi mbalimbali ulimwenguni pote. Mwanamke mmoja, aliyeanza utumishi wake wa wakati wote katika nchi ya Swisi mwezi Januari wa 1924 na sasa anatumikia akiwa mshiriki wa jamaa ya Betheli katika Jamhuri ya Mwungano wa Ujeremani, aliandika hivi: “Mimi nataka kumpigia Yehova asante kwa wema wote ambao amenionyesha, akaniacha nitumie maisha yenye furaha na baraka nyingi yenye kujawa na mapendeleo mazuri ajabu katika utumishi wake.” Ndiyo, mwanamke huyo anashangilia katika utumishi wa Yehova.
23. Unaweza kuthibitishaje Kimaandiko kwamba wale wanaoweka utumishi wa Mungu kwanza maishani wana sababu ya kushangilia?
23 Ni kweli kwamba wale ambao wameweka utumishi wa Mungu kwanza katika maisha wamekuwa na sababu ya kushangilia. Maisha zao hazikukosa kabisa kuwa na matatizo yaliyo kawaida ya wanadamu, hiyo ni kweli. Lakini Yehova amewaunga mkono wakati wa majaribu yao. (1Wakorintho 10:13; 2 Wakorintho 4:8, 9) Wamefanikiwa kwa sababu ‘furaha ya Yehova ndiyo ngome yao.’ (Nehemia 8:10, NW) Ebu fikiri: Musa ‘aliona ni afadhali kupata mateso pamoja na watu wa Mungu’ naye akabarikiwa kwa kupewa mapendeleo makubwa. (Waebrania 11:23-29) Ruthu Mmoabi aliwaacha watu wake na miungu yake, akachagua kutumikia Yehova, naye alithawabishwa kwa kuwa nyanya (bibi) wa kale wa Yesu Kristo. (Ruthu 1:14-17; 4:13-17; Mathayo 1:1, 5) Simeoni mzee mcha-Mungu na pia Ana mzee mwaminifu walikuwa na furaha ya kukiona kitoto kichanga Yesu hekaluni kwa sababu walihangaikia ibada ya kweli wakawa wakienda hekaluni kwa ukawaida.—Luka 2:25-38.
24. Ni juu ya msingi gani tunaweza ‘kushangilia siku zetu zote’?
24 Basi sisi tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutapata mapendeleo makubwa na baraka nyingi tukiweka ibada ya Yehova na utumishi wake kwanza katika maisha. (Mathayo 6:33) Na hata tukikutana na magumu tunapofanya hivyo, tunajua kwamba Yehova “anafanya kazi zake zote zishirikiane pamoja kwa faida ya wale wanaopenda Mungu.” (Warumi 8:28, NW) Basi, na tuazimie kumtii Baba yetu wa kimbingu na kumtumikia tukiwa na moyo wenye kujaa furaha. Kwa uhakika, ikiwa tuna upendo kamili kwa Yehova, tuna sababu nzuri za ‘kushangilia na kufurahi siku zetu zote.’—Zaburi 90:14.—Kutoka The Watchtower, November 1982.
Je! Wewe Unaweza Kukumbuka?
□ Ili tuweze ‘kushangilia siku zetu zote,’ ni lazima tukumbuke mambo gani mawili ya msingi?
□ Ni lazima wazazi na watoto wafanye nini ndipo kuweze kuwa na furaha ndani ya jamaa?
□ Wakristo wanaweza kudumishaje furaha hata watenda makosa wajapofanya matendo yao mabaya?
□ Ni kwa njia gani moyo wenye kujaa furaha ni baraka?
□ Ni nini mengine ya mapendeleo ya furaha katika utumishi wa Yehova, na kwa hiyo imetupasa tuazimie kufanya nini?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Ili jamaa iwe na furaha ya kudumu, ni lazima wazazi na Watoto wafuate mashauri yaliyo katika Neno la Mungu
[Picha katika ukurasa wa 17]
Furaha inaweza kuja badala ya huzuni tukitenda mapenzi ya Yehova kwa uaminifu
[Picha katika ukurasa wa 17]
Watumishi waaminifu wa Yehova wa nyakati zilizopita na wa sasa wamekuwa na sababu ya ‘kushangilia siku zao zote’