Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 4/15 kur. 5-8
  • Kimbia Kukiwa Kungali Kuna Wakati!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kimbia Kukiwa Kungali Kuna Wakati!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Mahali Patakatifu” na “Chukizo Kuu”
  • ‘Kimbieni Kwenda Kwenye Milima’
  • Hakuna Kukawia
  • Huu Ndio Wakati wa Kukimbia!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Chukizo Kuu Linashindwa Kuleta Amani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • “Mwacheni Msomaji Atumie Ufahamu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Kukimbilia Usalama Kabla ya “Dhiki Kubwa”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 4/15 kur. 5-8

Kimbia Kukiwa Kungali Kuna Wakati!

WAKATI Yesu alipoutabiri mwisho wa huo mfumo wa kidini wa Wayahudi katika karne ya kwanza, alikuwa pia akifikiria jambo fulani lililo kubwa zaidi. Alijua mwisho huo ungekuwa kielelezo cha jambo ambalo lingetazamiwa kutukia kwa kadiri kubwa zaidi wakati wa “siku za mwisho” za huu mfumo wa mambo.​—2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 24:3.

Tunawezaje kuwa na uhakika kwamba kuna matumizi zaidi ya tukio hilo? Mfano mmoja ni kwamba Yesu alitaja katika unabii wake juu ya kuja kwake wakati ujao “pamoja na nguvu na utukufu mwingi.” Tokeo moja la jambo hilo lingekuwa kwamba ‘mataifa yote ya ulimwengu wataomboleza’ kwa sababu ya maafa yenye kuwafikilia. (Mathayo 24:30) Mambo hayo hayakutukia wakati Yerusalemu na Yudea ilipopinduliwa katika karne ya kwanza. Fasiri ya Luka ya unabii uo huo inamtaja Yesu kama akisema: “Yerusalemu utakanyagwa na Mataifa, hata majira ya Mataifa yatakapotimia.”​—Luka 21:24.

“Yerusalemu” unaotajwa hapa ni nini? Ni wakati gani hayo “majira ya Mataifa” yanapokoma?

“Mahali Patakatifu” na “Chukizo Kuu”

Ufalme wa Mungu ulio kifananishi ulitawala katika Yerusalemu kuanzia mwaka wa 1070 mpaka mwaka wa 607 KWK. Uliwakilisha enzi kuu ya Mungu duniani. Lakini nasaba hiyo ya ukoo wa Daudi ilipinduliwa na Wababeli. Hakuna ufalme ambao umepata kutawala tena katika Yerusalemu wa kidunia, mpaka siku hii ya leo. Walakini, Yerusalemu umeacha kukanyagwa katika njia hii: Sasa enzi kuu ya Mungu imekuja kuendeshwa kupitia ‘Yerusalemu wa kimbingu’​—ule ufalme ulioahidiwa wa Masihi, Kristo Yesu. Orodha ya tarehe za Biblia, utimizo wa unabii na ushuhuda unaotolewa na wanahistoria ni mambo yanayojumlika pamoja kuonyesha kwamba mwaka ule wa 1914 ndio uliokuwa mwisho wa “majira ya Mataifa’’ na mwanzo wa kipindi cha “dhiki ya mataifa.”​—Waebrania 12:22; Luka 21:24-26; Ufunuo 11:15.

‘Yerusalemu wa kimbingu,’ unaowakilishwa na Wakristo waaminifu watiwa-mafuta walio duniani, sasa upo katika “mahali patakatifu.” Lakini je! mataifa ya dunia yamelikubali jambo hilo? Wapi! Katika mwaka wa 1919 yaliupendekeza Ushirika wa Mataifa, ambao viongozi wakubwa wa kidini waliutangaza kuwa ndio “wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu duniani.” Vivyo hivyo, viongozi wa kidini wameueleza Umoja wa Mataifa uliotokezwa baada ya Ushirika huo katika mwaka wa 1945 kuwa ndilo ‘tumaini la pekee kwa amani yenye kudumu.’ Kwa hiyo viongozi wa kidini wangependa kifano hicho cha kibinadamu kisichofaa sana kisimame katika “mahali patakatifu” ambapo ni ufalme wa Mungu tu kupitia Kristo wake ulio na ruhusa ya kupasimama ukiendesha shughuli zake. Woo, ni “chukizo kuu” kama nini machoni pa Mungu na wote wapendao uadilifu!

Walakini, tunapozidi kushuka kuuelekea wakati wa Mungu wa kuharibu mfumo mbovu wa sasa wa ulimwengu, hilo “chukizo kuu,” yaani Umoja wa Mataifa, linatisha dini ya ulimwengu yenyewe. Namna gani? Kwa sababu mataifa yenye nguvu yaliyo wanachama wa Umoja wa Mataifa, sana-sana yale ya Kikomunisti, yameingilia makao ya dini. Hasa makundi hayo yasiyoamini kuna Mungu yametisha kukatiza utendaji wa dini za Jumuiya ya Wakristo, kama kwa mfano katika China, katika Urusi na katika nchi nyingine za Ulaya ya Mashariki. Hivyo wanachama wa Umoja wa Mataifa wanasimama kama tisho kwa “mahali patakatifu” ambapo Jumuiya ya Wakristo inadai pake. Hapo panafananisha kila kitu ambacho dini zake zinakichukua kuwa kitakatifu​—maeneo yake ya utendaji, matengenezo yake, majengo yake ya makanisa na mali nyinginezo, na haki inayodai nayo ya kutawala maisha za watu wake kutakuwa na mwisho gani wa kabiliano hili?

Mharibu wa kisasa, yaani Umoja wa Mataifa ulio ‘mnyama-mwitu mwenye vichwa saba na pembe kumi,’ anatabiriwa kwamba ataifanya dini ya uongo iwe ‘ukiwa na uchi’ na ‘kuiteketeza kabisa kwa moto. (Ufunuo 17:3, 16) Kwa kufanya hivyo hawatakuwa wakitenda kinyume cha upendo wa Mungu, kwa maana hata Rumi ya kale ilipoleta uharibifu haikutenda kinyume cha upendo huo. Lile “chukizo kuu la ki-siku-hizi lina mataifa mengi sasa yanayomchukia Mungu. Yanachukia pia utawala wa ufalme wake na watu wenye jina la Mungu, Yehova. Na kwa uhakika mleta-ukiwa huyu ni sehemu ya mfumo huu wa mambo unaoongozwa na Shetani Ibilisi.​—Luka 4:5-8; 2 Wakorintho 4:4; Mathayo 6:9, 10.

‘Kimbieni Kwenda Kwenye Milima’

Wakati Umoja wa Mataifa ulipotokea mwaka wa 1945, ukiwa mrithi wa Ushirika wa Mataifa, hata wakati huo ulikuwa na mataifa yenye kumpinga Mungu katikati yake. Kwa njia hiyo kiishara kile kilionyeshwa upya, tena kwa mkazo zaidi, kwamba watu wenye mioyo ya uadilifu alitii onyo la Yesu la kuanza “kukimbia kwenda kwenye milima.”​—Mathayo 24:16, NW; Ufunuo 7:9, 10; 18:4.

Leo milima hiyo ya mfano ni nini? Ni pale mahali pa kimbilio palipowekwa na Mungu, yaani, mpango wa Yehova wa kulindia watu wake duniani waipite “dhiki” kuu inayosimuliwa kwenye Ufunuo 7:1, 14, NW. Milima hiyo inahusianishwa na tengenezo la kitheokrasi la Yehova, ambalo linawakilishwa duniani leo na kundi la Kikristo la kweli. (1 Timotheo 3:15;) Katika “siku za mwisho” kundi hili linaelekeza watu ndani ya ibada ya kweli kwenye ‘mlima wa nyumba ya Yehova.’ (Isaya 2:2, 3) Vivyo hivyo, Mithali 18:10 inasema hivi: “Jina la [Yehova] ni ngome imara; mwenye haki huikimbilia, akawa salama.”

Kulikimbilia tengenezo la Mungu na ibada safi iliyotukuzwa ya tengenezo hilo kunamaanisha kukimbia na kuiacha mifumo ya dini ya uongo ya ulimwengu huu, kukata uhusiano wo wote na mifumo hiyo. Kunamaanisha kujitambulisha kuwa mtumishi wa kweli wa Yehova na mwanafunzi wa Yesu Kristo.

Hakuna Kukawia

Hakuna mtu anayepaswa kukawia kukimbia, akifikiri kwamba siku zetu zitakuwa kabisa kama ilivyokuwa wakati majeshi ya Kirumi yalipoondoka mwaka wa 66 WK, halafu kuwe na wakati wa kukimbia. Haitatazamiwa kwamba kutakuwa na tukio kama hilo la kihistoria, kwa kuwa hakuna uhitaji wa mtu kukimbilia eneo fulani la nchi. Badala yake, kutokea kwa Ushirika wa Mataifa baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na kutokea tena kwa ‘mnyama-mwitu’ huyo katika mwaka wa 1945 akiwa Umoja wa Mataifa ni onyo la kutosha.

Watu wanahitajiwa wakimbie haraka sana sasa. Kwa sababu gani? Kwa sababu ushuhuda unaonyesha kwamba karibuni lile “chukizo kuu” litapafanya ukiwa “mahali patakatifu” pia, pale panapodaiwa kuwa makao ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Tukio hilo litakuwa ndilo mwanzo wa “dhiki kuu.”

Kwa kuwa wale watakaoiokoka “dhiki kuu” wanapasa watafutwe kabla haijaanza, Yehova hahitaji kuruhusu kuwe na “mazingiwa” yenye kuchukua muda mrefu sana. Ni kweli kama Yesu alivyotabiri, kwamba huo utakuwa ndio wakati wa taabu nzito mno isiyopata kuonekana katika historia yote ya kibinadamu. Lakini kwa kulinganishwa utakuwa wakati mfupi, kwa maana utakuwa ‘umefupizwa’ kama mazingiwa ya zamani ya Yerusalemu, kwa kuwa ‘wachaguliwa’ wa Mungu watakuwa wamekwisha kukimbia.

“Ulimwengu unapita na ndivyo na tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele,” inasema 1Yohana 2:17, NW. Kwa hiyo, wale wanaofanya “mapenzi ya Mungu” kwa kumwabudu inavyofaa ndio “mwili” utakaoiokoka “dhiki kuu” inayokuja. Kama unavyoonyesha Ufunuo 7:9-17, kati ya watu hao kutakuwako “mkutano mkubwa” kutoka mataifa yote.

Namna gani wale wasiotii onyo na wasioitumia vizuri nafasi ya kukimbilia “milima” ya Yehova sasa? Unabii kwenye 2 Wathesalonike sura ya 1, mistari 7 mpaka 9, unajibu waziwazi, ukisema habari za “kufunuliwa kwake Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika wa uweza wake; katika mwali wa moto; huku akiwalipiza kisasi wao wasiomjua Mungu, na wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu; watakaoadhibiwa kwa maangamizi ya milele.”

Ndiyo, watu wanahitajiwa kwa haraka sana waikubali kazi ambayo Mungu anafanyisha katika dunia leo kwa utimizo wa maneno ya Yesu yaliyo kwenye Mathayo 24:14, NW: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” Wale wanaotii na kukimbia wataishi milele wawe wakionekana wakiwa ushuhuda wa kwamba ni ya kweli ahadi ya Biblia inayosema hivi: “[Yehova] hatawatupa watu wake.” (Zaburi 94:14) Naye Yesu alisema: “Mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka.”​—Mathayo 24:13.

Wakati wa Mungu wa kufikiliza hukumu juu ya Jumuiya ya Wakristo na “mahali patakatifu” pake uko karibu. Karibuni mleta-ukiwa ataipiga dharuba jumuiya hiyo, akomeshe nafasi ya kukimbilia ulinzi wa Yehova. Je! wewe umekwisha kuikimbilia ile “milima” ya mfano? Ikiwa bado, basi usikawie. Ni jambo la kufa au kupona.​—Sefania 1:14-18; 2:3.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo walidai kwamba Ushirika wa Mataifa na Umoja wa Mataifa ungeweza kutimiza mambo ambayo ni ufalme wa Mungu tu ulio mfano wa mlima unaweza kufanya. Basi wao waliviweka vifano hivyo vya kibinadamu katika “mahali patakatifu”

[Picha katika ukurasa wa 7]

“Pembe” za kijeshi za “mnyama” aliye Umoja wa Mataifa sasa zinatisha “mahali patakatifu” pengine, yaani, vitu vyote ambavyo Jumuiya ya Wakristo inavithamini sana kuwa eneo lake la mamlaka na utendaji

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki