Chukizo Kuu Linashindwa Kuleta Amani
“Wakati mtakapoona Yerusalemu umezungukwa na majeshi yaliyopiga kambi . . . hapo wale walio katika Yudea waanze kukimbia kwenye milima.”—LUKA 21:20, 21, NW.
1, 2. (a) Ni kwa sababu gani mwanadamu hataleta amani kamwe kupitia matengenezo kama Umoja wa Mataifa? (b) Mungu ataletaje amani duniani?
HATA wanadamu wajaribu namna gani kuleta amani na usalama kupitia vyama kama Umoja wa Mataifa, hawatafaulu kamwe. Kwa sababu gani? Kwa sababu wanadamu leo hawana amani na Mungu, na usalama wenye kudumu unaweza kuletwa ikiwa tu mwanadamu ana amani pamoja na Muumba wake. (Zaburi 46:1-9; 127:1; Isaya 11:9; 57:21) Tatizo hilo linaweza kumalizwaje? Jambo la kufurahisha ni kwamba Yehova mwenyewe amekwisha kuanza kushughulikia jambo hilo. Mwishowe amani na usalama utaletwa kwenye dunia hii kupitia Ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Mwanaye, Yesu, ambaye wakati wa kuzaliwa kwake malaika waliimba hivi: “Utukufu kwa Mungu juu mbinguni, na amani duniani kwa watu aliopendezwa nao.”—Luka 2:14, HNWW; Zaburi 72:7.
2 Katika karne ya kwanza, Yesu alitangaza Ufalme wa Mungu na kuwatolea watu wenye kuamanika nafasi ya kuwa wana wa Mungu na watawala wenzake katika Ufalme huo. (Mathayo 4:23; 5:9; Luka 12:32) Matukio yaliyofuata yalifanana sana na matukio ya karne hii yetu wenyewe. Tukiyachunguza tutafundishwa mengi juu ya mwendo utakaofuatwa wakati ujao na tengenezo la wanadamu la kuletea “amani na usalama,” yaani, Umoja wa Mataifa.
Wayahudi Wafanya Uchaguzi
3. Ni nani aliyekuwa akijaribu kudumisha amani na usalama siku za Yesu, na kwa sababu gani jambo hilo halingeweza kufaulu kabisa?
3 Siku za Yesu, Milki ya Roma ndiyo iliyotawala sehemu kubwa ya dunia na ilikuwa na mawazo yake yenyewe juu ya amani na usalama. Kwa kutumia majeshi yake, ilikuwa imetekeleza ile Pax Romana (Amani ya Kiroma) katika sehemu kubwa ya ulimwengu uliojulikana wakati huo. Lakini Pax Romana hiyo haikuweza kamwe kuwa amani ya kudumu, kwa sababu Roma ya kipagani na majeshi yake haikuweza kamwe kuleta upatanisho kati ya mwanadamu na Mungu. Kwa hiyo, Ufalme uliotangazwa na Yesu uliizidi ubora kwa mbali.
4. Wayahudi walio wengi walitendaje kuhusu mahubiri ya Yesu? Hata hivyo, ni jambo gani lililotokea hatua kwa hatua katika karne ya kwanza?
4 Hata hivyo, wengi wa wananchi wenzi wa Yesu waliukataa Ufalme wa Mungu. (Yohana 1:11; 7:47, 48; 9:22) Watawala wao wakimwona Yesu kuwa ni tisho kwa usalama wa kitaifa, walimpeleka akauawe, wakisisitiza hivi: “Sisi hatuna mfalme ila Kaisari.” (Yohana 11:48; 19:14, 15) Lakini, Wayahudi fulani, na baadaye watu wengi wa Mataifa, walimtambua Yesu kwa furaha kuwa ndiye Mfalme aliyechaguliwa na Mungu. (Wakolosai 1:13-20) Walihubiri habari zake katika nchi nyingi, na Yerusalemu pakawa ndipo mahali pakuu pa ushirika wa Wakristo wa mataifa yote.—Matendo 15:2; 1 Petro 5:9, NW.
5, 6. (a) Uhusiano kati ya Wayahudi na Roma uliharibika ukawaje? (b) Yesu alitoa onyo gani, nalo liliokoaje maisha za Wakristo mwaka 70 W.K.?
5 Ijapokuwa Wayahudi walikuwa wamechagua Kaisari badala ya Kristo, baada ya muda mfupi uhusiano kati ya Yerusalemu na Roma uliharibika. Washupavu wa Kiyahudi waliendesha mashambulizi ya kuvizia-vizia kinyume cha milki ile mpaka mwishowe, mwaka 66 W.K., kukatokea kishindo cha vita ya waziwazi. Askari Waroma walijaribu kurudisha Pax Romana, na baada ya muda mfupi Yerusalemu ukazingirwa. Hilo lilikuwa jambo lenye maana kubwa kwa Wakristo. Miaka mingi kabla ya hapo, Yesu alikuwa ameonya hivi: “Wakati mtakapoona Yerusalemu umezungukwa na majeshi yaliyopiga kambi, hapo jueni kwamba umekaribia kuwekwa ukiwa. Hapo wale walio katika Yudea waanze kukimbia kwenye milima, na wale walio katikati yao waondoke ndani.” (Luka 21:20, 21, NW) Sasa Yerusalemu ulikuwa umezungukwa, na Wakristo walingoja wapate nafasi ya kukimbia.
6 Nafasi hiyo ilitokea upesi. Waroma walikuwa wakiufukua ukuta wa hekalu ili wauangushe, na Wayahudi wengi walikuwa tayari kusalimu amri wakati jemadari Mroma, Sestio Gallo, alipoondoa askari zake wakaenda zao, bila kutazamiwa. Wale washupavu waliitumia nafasi hiyo kutengeneza upya kinga zao, lakini Wakristo wakauacha mji huo uliohukumiwa maangamizi. Mwaka 70 W.K., majeshi ya Kiroma yalirudi yakazunguka kuta za Yerusalemu, na safari hii mji uliangamia. Msiba huo wa kihistoria unatuhusuje? Hivi: Onyo la Yesu lililookoa maisha za wafuasi wake lina maana kwetu leo pia.
Zaidi ya Utimizo Mmoja
7-9. (a) Tunajuaje kwamba unabii wa Yesu juu ya kuzungukwa kwa Yerusalemu na majeshi ungekuwa na zaidi ya utimizo mmoja? (b) Kukisoma kitabu cha Danieli ‘kwa ufahamu’ kunaliungaje mkono jambo hilo?
7 Onyo hilo lilikuwa sehemu ya unabii mrefu uliotamkwa na Yesu akijibu ulizo la maana. Wafuasi wake walikuwa wameuliza: “[Uharibifu wa hekalu la Yerusalemu utakuwa] wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (NW) Kwa kujibu, Yesu alitabiri ishara yenye sehemu nyingi, kutia na kuzingirwa kwa Yerusalemu. (Mathayo 24; Marko 13; Luka 21) Katika miaka iliyofuata kifo cha Yesu, nyingi za sehemu zilizo katika unabii huo zilitimizwa, zikafikia upeo katika uharibifu wa Yerusalemu na mfumo wa mambo wa Kiyahudi mwaka 70 W.K.—Mathayo 24:7, 14; Matendo 11:28; Wakolosai 1:23.
8 Lakini, wanafunzi walikuwa pia wameuliza habari za “kuwapo” kwa Yesu, ambako Biblia inashirikisha na mwisho wa mfumo wa mambo ya ulimwengu mzima. (Danieli 2:44; Mathayo 24:3, 21) Kwa kuwa kuwapo kwa kiroho kwa Yesu na mwisho wa mfumo wa mambo ya ulimwenguni pote hakukutukia katika karne ya kwanza, utimizo mkubwa zaidi wa wakati ujao kuhusu unabii wa Yesu ungeweza kutazamiwa, na matukio hayo ya karne ya kwanza ni kiolezo cha utimizo mkubwa zaidi. Hiyo ingetia ndani utimizo mkubwa zaidi wa onyo la Yesu juu ya uharibifu wa Yerusalemu.
9 Jambo hilo linakuwa wazi zaidi tukichunguza namna onyo hilo lilivyoandikwa katika zile sura nyingine mbili za Biblia ambamo linapatikana. Katika Mathayo, askari wenye kuzingira wanasimuliwa kuwa ndio “chukizo kuu lenye kufanyiza uharibifu, kama lilivyosemwa kupitia kwa Danieli nabii, likisimama katika mahali patakatifu.” (Mathayo 24:15, NW) Katika masimulizi ya Marko, “chukizo” hilo linasimama “pasipolipasa.” (Marko 13:14) Masimulizi ya Mathayo yanasema kwamba “chukizo kuu” hilo lilitajwa pia katika kitabu cha Danieli. Kwa kweli, maneno “chukizo” yanapatikana mara tatu katika kitabu hicho: mahali pamoja linapatikana katika Danieli 9:27 ambapo hilo ni sehemu ya unabii uliotimizwa wakati Yerusalemu ulipoharibiwa mwaka 70 W.K., halafu katika Danieli 11:31 na Danieli 12:11. Kulingana na maandiko hayo mawili ya mwisho, “chukizo kuu” lingesimamishwa katika “wakati ulio-wekwa,” au “wakati wa mwisho.” (Danieli 11:29; 12:9, NW) Tumekuwa tukiishi katika “wakati wa mwisho” tangu mwaka 1914; na kwa hiyo, onyo la Yesu linahusika leo, pia.—Mathayo 24:15, NW.
Uchaguzi wa Jumuiya ya Wakristo
10, 11. Matukio katika karne yetu yamefananaje na yale yaliyokuwa katika karne ya kwanza?
10 Katika karne yetu, matukio yamefuata kiolezo kinachofanana na kile cha karne ya kwanza. Leo, kama ilivyokuwa wakati huo, kuna milki yenye kutawala ulimwengu. Ile ya kisasa ni serikali kuu ya ulimwengu ya Waingereza na Waamerika, ambayo inajaribu sana kufanya wanadamu wafuate maoni yake yenyewe juu ya amani na usalama. Katika karne ya kwanza, Israeli wa kimwili walimkataa Yesu asiwe Mfalme aliye mpakwa mafuta wa Mungu. Mwaka 1914, “kuwapo” kwa Yesu akiwa ndiye mfalme aliyetawazwa na Yehova kulianza. (Zaburi 2:6; Ufunuo 11:15-18) Lakini mataifa, kutia na yale ya Jumuiya ya Wakristo, yalikataa kumtambua. (Zaburi 2:2, 3, 10, 11) Kwa kweli, yalijiingiza katika vita kali sana ya ulimwengu ili yawe na enzi kuu juu ya mataifa yote. Pia viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo ndio wameongoza kumkataa Yesu, kama viongozi wa Kiyahudi. Tangu mwaka 1914 wameendelea kuhusika katika siasa bila kuacha, wakapinga kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme.—Marko 13:9.
11 Hata hivyo, kama ilivyokuwa katika siku za Yesu, watu wengi mmoja mmoja leo wamemtambua kwa furaha Mfalme aliyewekwa na Yehova na kueneza habari njema za Ufalme wake sehemu zote za ulimwengu. (Mathayo 24:14) Matokeo yamekuwa kwamba Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni mbili na nusu wanaonyesha ushikamanifu sasa kwa Ufalme wa Mungu. (Ufunuo 7:9, 10) Wakiwa hawamo katika siasa za ulimwengu huu, wao wanao imani kamili katika mipango ya Yehova ya kuletea amani na usalama.—Yohana 17:15, 16; Waefeso 1:10.
Lile “Chukizo Kuu” la Leo
12. “Chukizo kuu” la kisasa ni nini?
12 Basi, je! ni nini “chukizo kuu lenye kufanyiza uharibifu” wakati wa kisasa? Katika karne ya kwanza lilikuwa ni askari Waroma waliotumwa wakalazimishe watu kuanza kuifuata tena Pax Romana katika Yerusalemu. Lakini, katika nyakati za kisasa mataifa yaliyopigana katika Vita ya Ulimwengu ya Kwanza yalikatishwa tamaa na kutofaa kwa vita ya kufa au kupona ili kulazimisha watu wafuate amani. Basi walijaribia jambo jipya: tengenezo la kimataifa la kuhifadhi amani ya ulimwengu. Lilianza kuwa hai mwaka 1919 likiwa Ushirika wa Mataifa na lingali lipo likiwa ndilo Umoja wa Mataifa. Hilo ndilo lile “chukizo kuu lenye kufanyiza uharibifu” wakati wa kisasa.
13, 14. (a) Ni maneno gani ya kusifusifu yamesemwa na Jumuiya ya Wakristo juu ya lile “chukizo kuu”? (b) Ni kwa sababu gani tendo hilo lilikuwa ibada ya sanamu, nalo lililiweka lile “chukizo kuu” mahali gani?
13 Jambo la kupendeza ni kwamba, neno la Kiebrania lililotafsiriwa ‘chukizo’ katika Danieli ni shiq·qutsʹ. Katika Biblia, neno hilo linatumiwa hasa kuhusu sanamu na ibada ya sanamu. (1 Wafalme 11:5, 7) Kwa kufikiria hilo, soma maneno fulani yaliyosemwa na viongozi wa kidini juu ya ule Ushirika:
“Shirika hili la kuunganisha wanadamu ulimwenguni ni wonyesho wa nini . . . kama si Ufalme wa Mungu?” “Msingi wa Umoja wa Mataifa ni Gospeli.” (Muungano wa Baraza la Makanisa ya Kristo Katika Amerika) “Kila moja ya shabaha za [Ushirika wa Mataifa] na utendaji wao inaweza kusemwa kuwa inatimiza mapenzi ya Mungu kama yanavyojulishwa katika fundisho la Yesu Kristo.” (Maaskofu wa Kanisa la Uingereza) “Basi mkutano huu unapendelea kwamba watu wote walio Wakristo wauunge mkono na kuutolea sala Ushirika wa Mataifa kuwa ndio chombo kimoja tu kinachopatikana ili kuleta [amani duniani].” (Baraza Kuu la Wabaptisti, Wakongrigeshenali na Wapresbiteri katika Uingereza). “[Ushirika wa Mataifa] ndilo tengenezo moja tu ambalo limeagizwa litekeleze matakwa yenye kurudiwa-rudiwa na Makao ya Papa Mtakatifu.” (Kardinali Bourne, aliye Askofu Mkuu wa Westminster).
14 Mataifa yalipoukataa Ufalme wa Mungu kisha pia yakachukua hatua ya kuanzisha tengenezo lao wenyewe la kuleta amani, huo ulikuwa uasi. Wakati viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo walipohusianisha tengenezo hilo na Ufalme wa Mungu na Gospeli, wakautangaza kuwa “chombo kimoja tu kinachopatikana” ili kuleta amani, hiyo ilikuwa ibada ya sanamu. Walikuwa wakiuweka mahali panapoupasa Ufalme wa Mungu, “katika mahali patakatifu.” Kwa uhakika, ulikuwa ‘ukisimama pasipoupasa.’ (Mathayo 24:15, NW; Marko 13:14) Na viongozi wa kidini wanaendelea kuunga mkono mwandamizi wa Ushirika, yaani Umoja wa Mataifa, badala ya kuelekeza wanadamu kwenye Ufalme wa Mungu uliosimamishwa.
Hatari kwa Jumuiya ya Wakristo
15, 16. Uhusiano unaendelea kuwaje kati ya Jumuiya ya Wakristo na mataifa yanayounga mkono lile “chukizo kuu”?
15 Ingawa dini za Jumuiya ya Wakristo zilichagua Ushirika wa Mataifa na mwandamizi wake badala ya Ufalme wa Mungu, uhusiano wao na mataifa yaliyo washirika wa matengenezo hayo umeharibika. Jambo hilo linafanana na lile lililotukia kati ya Wayahudi na Roma. Tangu mwaka 1945, Umoja wa Mataifa umetia ndani nchi zaidi na zaidi ambazo ama si za Kikristo ama zinaupinga Ukristo, na hiyo ni dalili mbaya kwa Jumuiya ya Wakristo.
16 Tena, katika nchi nyingi kuna mzozano kati ya dini za Jumuiya ya Wakristo na Serikali. Katika Polandi Kanisa Katoliki linaonwa kuwa mpinzani wa utawala wa huko. Katika Ailandi ya Kaskazini na Lebanoni, dini za Jumuiya ya Wakristo zimeongezea matatizo ya ukosefu wa amani na usalama. Zaidi ya hilo, dini za Jumuiya ya Wakristo zimetokeza watu wanaofanana na wale Washupavu wa Kiyahudi, wenye kutia wengine moyo wa kufanya jeuri. Kama ilivyo, Baraza la Ulimwengu la Makanisa ya Kiprotestanti limeyapa michango matengenezo yenye kuvamia nchi, huku makasisi Wakatoliki wakiwa ni wapiganaji wa kuvizia-vizia wa porini na kutumikia pia katika serikali za mapinduzi.
17. (a) Yerusalemu wa kisasa ni nini? (b) Ni jambo gani litakaloupata mwishowe?
17 Ni baada tu ya muda kupita itakapofunuka ni kwa kiasi gani uhusiano utazidi kuharibika kati ya dini za Jumuiya ya Wakristo na mataifa, lakini matukio katika karne ya kwanza yamekwisha kuonyesha mapema mwisho wa mambo yote hayo. Kama Yesu alivyotangulia kuona, mwishowe majeshi ya Roma katika karne ya kwanza yaliuharibu Yerusalemu kwa dhiki nyingi. Kulingana na kiolezo hicho na unabii, mataifa pamoja na Umoja wa Mataifa yatashambulia na kuharibu “Yerusalemu,” yaani, dini zote za Jumuiya ya Wakristo.—Luka 21:20, 23, NW.
Kimbia Kwenye Milima
18. Watu wenye mioyo mipole wanapaswa kufanya nini wakifahamu kwamba lile “chukizo kuu” limekwisha kusimama?
18 Katika karne ya kwanza, baada ya lile “chukizo kuu” kuonekana, Wakristo walipata nafasi ya kukimbia. Yesu aliwashauri wafanye hivyo mara tu baada ya hapo kwa sababu hawakujua nafasi hiyo ingeendelea kuwapo kwa muda gani. (Marko 13:15, 16) Kwa njia iyo hiyo, wakati watu wenye mioyo mipole leo wanapofahamu kwamba hilo “chukizo kuu” lipo, wanapaswa kukimbia mara moja watoke katika milki ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo. Kila nukta wanayoendelea kukaa humo maisha yao ya kiroho yanakuwa hatarini, tena ni nani ajuaye nafasi yao ya kukimbia itaendelea kuwa wazi mpaka wakati gani?
19, 20. (a) Wakristo wa karne ya kwanza walifanya nini walipoona Yerusalemu umezungukwa na majeshi ya Kiroma? (b) Ni nini leo kinachofananishwa na “milima,” na ni jambo gani linalopasa kuharakisha watu wenye mioyo inayofaa leo wakimbie huko?
19 Gospeli ya Luka ilionya Wakristo wa siku zake wakimbie wakati walipoona “Yerusalemu umezungukwa na majeshi yaliyopiga kambi.” Kama ilivyokwisha kuonwa, majeshi hayo yalikuja mwaka 66 W.K., na nafasi ya kukimbia ikatokea mwaka uo huo wakati Sestio Gallo alipoondoa askari zake. Baada ya Wakristo kukimbia, vita iliendelea kati ya Wayahudi na Waroma—ingawa si karibu na Yerusalemu. Vespasian alitumwa Palestina na mfalme Nero, akaendesha kwa mafanikio shughuli za kijeshi huko katika miaka 67 na 68. Halafu Nero akafa, naye Vespasian akaanza kushughulikia kurithi Mfalme. Lakini alipokwisha kufanywa mfalme mwaka 69 W.K., alimtuma Tito, mwanaye, akamalizie vita huko Yudea. Mwaka 70 W.K., Yerusalemu uliharibiwa.
20 Ingawa hivyo, Wakristo hawakungoja ili wayaone yote hayo wakiwa ndani ya Yerusalemu. Mara tu walipoyaona majeshi yenye kuzingira walijua mji ulikuwa katika hatari kubwa sana. Vivyo hivyo leo, chombo kitakachotumiwa kuleta uharibifu wa Jumuiya ya Wakristo tayari kipo. Kwa hiyo, mara tu tukiisha kuifahamu hatari ambayo Jumuiya ya Wakristo imo, tunapaswa ‘kukimbia kwenye milima,’ mahali pa Yehova pa kimbilio palipo na tengenezo lake la kitheokrasi. Unabii ule mwingine mbalimbali hautoi msingi wa kuamini kwamba kutakuwako muda fulani wa utulivu katikati ya lile shambulio la kwanza juu ya Jumuiya ya Wakristo na kule kuharibiwa kwake kwa mwisho. Kwa kweli, hakutakuwa na uhitaji wa kukomesha mashambulizi hayo kwa muda. Watu wenye mioyo mipole wanakimbia wakitoka ndani ya Jumuiya ya Wakristo sasa.
Yerusalemu na Jumuiya ya Wakristo
21. Ni kwa sababu gani “chukizo kuu” lilionekana mwishoni mwa wakati wa mwisho wa Yerusalemu na hali katika karne hii lilionekana kuelekea mwanzoni mwa wakati wa mwisho wa mfumo huu?
21 Je! inatupasa tushangae kwamba katika karne ya kwanza lile “chukizo kuu” lilionekana muda mfupi tu kabla ya Yerusalemu kuharibiwa, hali leo lilionekana pale pale mwanzoni mwa wakati wa mwisho wa ulimwengu huu? Hapana. Katika kila kimoja cha visa hivi, lile “chukizo kuu” lilionekana katika wakati ambao Yehova alitaka watu wake wakimbie. Katika karne ya kwanza, Wakristo walipaswa kubaki kwa muda ndani ya Yerusalemu ili wahubiri humo. (Matendo 1:8) Ulipofika mwaka 66 W.K., wakati uharibifu ulipokaribia, hapo tu ndipo “chukizo kuu” lilipoonekana ili kuwaonya wakimbie. Lakini kuwa “ndani” ya “Yerusalemu” wa kisasa ni kuwa sehemu ya milki ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo.a Haiwezekani kutumikia Yehova kwa njia inayokubalika katika mazingira hayo yenye upotovu wa tabia na uasi-imani mwingi. Kwa hiyo, mapema katika wakati wa mwisho wa ulimwengu huu lile “chukizo kuu” lilionekana, likaonya Wakristo wakimbie. Kimbio la kuiacha Jumuiya ya Wakristo linaendelea, na kila mtu anapata onyo la kukimbia mara tu akiisha kufahamu kwamba lile “chukizo kuu” limekwisha kusimama.
22. Ni maulizo gani yanayobaki kujibiwa?
22 Ingawa hivyo, ni jambo gani linaloongoza kwenye tendo hilo lisilokuwa limetazamiwa hata kidogo, kutumia sehemu za kijeshi za Umoja wa Mataifa ziharibu Jumuiya ya Wakristo? Tendo hilo litatokea wakati gani? Na hilo linaweza kusaidiaje kuleta amani na usalama kwenye dunia yetu? Tutazungumza maulizo hayo katika makala inayokuja.
[Maelezo ya Chini]
a Tofauti inayokaribia kulingana na hiyo ipo kati ya mji wa Babuloni, ambamo Wayahudi walitoka wakakimbia mwaka 537 K.W.K., na Babuloni Mkuu wa kisasa, ambamo Wakristo wanatoka na kukimbia leo.—Isaya 52:11; Yeremia 51:45; Ufunuo 18:4.
Wewe Unakumbuka?
◻ Kwa sababu gani bila shaka unabii wa Yesu kuhusu lile “chukizo kuu” una utimizo wa kisasa?
◻ Leo lile “chukizo kuu” ni nini, nalo limekwisha kusimama tangu wakati gani?
◻ Ni nini “Yerusalemu” wa kisasa unaotajwa katika unabii wa Yesu?
◻Andiko la Luka 21:20, 21 linatusaidiaje kuona uharaka wa kukimbia?
◻Ni nini “milima” inayokimbiliwa na watu wenye mioyo mipole?
[Blabu katika ukurasa wa 11]
Wakati viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo walipohusianisha Umoja wa Mataifa na Ufalme wa Mungu na gospeli, hiyo ilikuwa ibada ya sanamu