Huu Ndio Wakati wa Kukimbia!
1. (a) Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, ni jambo gani lililotukia duniani katika sehemu takatifu ya “mahali patakatifu”? (b) Basi ni ulizo gani linalotokea?
KAMA tulivyoona, “mahali patakatifu” pa kweli pako katika milki ya “Yerusalemu wa mbinguni,” ufalme wa kimasihi wa Mungu. Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, “watakatifu” wanaotumikia pamoja na wenzao, lile “kundi kubwa,” katika sehemu takatifu ya hapo “mahali patakatifu” duniani walikanyagwa-kanyagwa hasa katika nchi za mamlaka ya ulimwengu ya mwungano wa Waingereza na Waamerika. (Danieli 7:27; 8:10-12; Ufunuo 7:9, 15, NW) Basi je! tunakata kauli kwamba Uingereza na Amerika ndizo “kile kitu chenye kuchukiza chenye kuharibu”? Hapana, kwa maana “makosa” ya hiyo mamlaka ya ulimwengu ya mwungano wa sehemu mbili yanatia ndani jambo jingine. Jambo gani?
2, 3. (a) Ufalme wa Mungu wa kiuongo umetokezwaje? (b) Jambo hilo limeelezwaje katika Ufunuo? (c) Basi “kile kitu chenye kuchukiza” cha Danieli 11:31 na Mathayo 24:15 ni nini?
2 Mamlaka ya ulimwengu ya mwungano wa Waingereza na Waamerika imetumikia kusudi la Shetani kwa njia nyingine. Imetokeza ufalme wa Mungu wa bandia (wa kiuongo). Katika kitabu cha Ufunuo cha Biblia, sawa na katika unabii wa Danieli, ‘wanyama’ na “pembe” zao wanatumiwa kufananisha mamlaka za kisiasa za ulimwengu. Ufunuo sura ya 13 unasimulia mamlaka ya ulimwengu ya saba ya historia ya Biblia, yaani, Uingereza na Amerika, kuwa mnyama-mwitu mwenye pembe mbili ambaye anaipa uhai “sanamu” ya tawala za kibinadamu zilizo mfano wa mnyama-mwitu. Hii “sanamu” ya mnyama ina sehemu nyingi ndani yake. Ni ‘mnyama mwekundu sana mwenye vichwa saba na pembe kumi.’ (Ufunuo 17:3) Kwa mara ya kwanza alitokea akiwa Ushirika wa Mataifa mwaka wa 1920, halafu tena akafufuka mwaka wa 1945 akiwa Umoja wa Mataifa. Wakati huo watetezi wake wakuu walikuwa Uingereza na Amerika, pamoja na Urusi. (Ufunuo 13:11,15; 17:8) Jambo hilo pia lilitimiza Danieli 11:31, panaposema: “[Na mahali pake] watalisimamisha chukizo la uharibifu.”a
3 Basi huo ndio kile kitu cha kisasa “chenye kuchukiza” alichokitaja Yesu kwenye Mathayo 24:15, NW. Lakini ‘kimesimamishwaje katika mahali patakatifu’? Mambo ya uhakika yanaonyesha nini?
4. (a) Kwa sababu gani Ushirika wa Mataifa unaweza kuelezwa kuwa ni “kitu chenye kuchukiza”? (b) Ni madai gani ‘ya kuchukiza’ ambayo viongozi wa kidini wamesema juu ya Umoja wa Mataifa?
4 Wakati Uingereza na Amerika zilipoongoza katika kupendekeza Ushirika wa Mataifa uanzwe mwaka wa 1918, makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yaliunga jambo hilo mkono kwa moyo wote. Mwungano wa Baraza ya Makanisa ya Kristo katika Amerika uliushangilia kuwa “wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu duniani.” Si makufuru hayo-o-o! Ai, ati mwungano wa mataifa ya kisiasa ya ulimwengu wa Shetani yangeweza kuwa ufalme wa Mungu duniani! Lo! ni chukizo lililoje, karaha gani, machoni pa Yehova na pa wale wanaosimama kikweli katika “mahali patakatifu” wakiwa mabalozi duniani wa “Yerusalemu wa mbinguni’ ambao sasa unatawala! Nao viongozi wa kidini wa ulimwengu wamesema nini juu ya mrithi wa Ushirika huo, yaani, Umoja wa Mataifa? Wameueleza kwa njia mbali mbali kuwa ‘ndio tumaini moja la pekee la wokovu’ kwa wanadamu, “tumaini la mwisho la upatani na amani” na “mahakama kuu zaidi ya zote ya amani na haki.” Kama walivyofanya na Ushirika wa Mataifa, wanauweka Umoja wa Mataifa katika “mahali patakatifu” kwa kudai kwamba utaleta mambo ambayo ni ufalme wa Mungu pekee uwezao kutimiza.
5. Kwa sababu gani tunaweza kusema kwamba Umoja wa Mataifa haupaswi kuwa katika “mahali patakatifu”
5 Viongozi wa kidini wamechagua kuuweka Umoja wa Mataifa katika “mahali patakatifu” ambapo ni haki ya “Yerusalemu wa mbinguni,” ufalme wa Mungu na ya “watakatifu” wanaowakilisha ufalme huo duniani. Lakini hakuna kitu chochote ‘kitakatifu’ kuhusiana na Umoja wa Mataifa. Ni kweli kwamba una kikanisa cha maombi na kengele ya Kibuddha, kisha ukuta wake ulio katika uwanja mkubwa wa watu wote jijini umeandikwa maneno haya ya Isaya 2:4: “Nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” Lakini vitu hivyo haviufanyi uwe ‘mtakatifu.’ Mataifa yaliyo washiriki wake yanazozana daima, na hesabu kubwa ya mataifa hayo sasa inapinga dini, inapinga Mungu. Walakini, katika maana nyingine pia tunaona “kile kitu chenye kuchukiza . . . kikisimama katika mahali patakatifu.”
Ulinganifu wa Kustaajabisha
6. (a) Ni vikundi gani viwili vyenye kupingana vilivyoishi katika Yerusalemu wa karne ya kwanza? (b) Wanadini wa Kiyahudi waliwalandaje (walikuwaje kama) babu zao?
6 Mpaka mwaka wa kuharibiwa kwa Yerusalemu wa kale, mji huo ulitegemewa na Wayahudi kuwa mji mtakatifu, mahali patakatifu. Karibu na mwaka wa 56 WK hata mtume Paulo alikwea kwenye hekalu lililokuwa katika Yerusalemu halafu akajisafisha kisherehe huko pamoja na Wakristo wengine wanne waliokuwa chini ya nadhiri. (Matendo 21:23-26) Huko akatendwa jeuri na watu wenye ghasia waliokuwa Wayahudi wa namna ile yenye kutesa Wakristo wa kweli, wakidai kwamba hao ‘walikuwa wamejaza Yerusalemu mafundisho yao.’ (Matendo 5:28) Wayahudi hao walishikilia mapokeo yao na ibada yao ya kuasi imani, basi wakawa kama babu zao wa siku za Yeremia, walioweka tumaini lao katika ‘maneno ya uongo, wakisema, Hekalu la Yehova, Hekalu la Yehova, Hekalu la Yehova ndiyo haya’! (Yeremia 7:4, NW) Lakini tumaini hilo liliwekwa pasipofaa.
7. (a) Jumuiya ya Wakristo inalinganaje na Yerusalemu wenye kuasi imani? (b) “Mahali patakatifu” ambapo Jumuiya ya Wakristo inadai kuwa ni mali yake ni nini?
7 Leo kuna hali inayofanana na hiyo, kwa maana mji wa Yerusalemu wenye kuasi imani wa nyakati za kale na hekalu lake una ulinganifu wa kustaajabisha katika Jumuiya ya Wakristo ya kisasa. Angalia kwamba dini ya Jumuiya ya Wakristo inadai pia kwamba ina “mahali patakatifu,” yaani, haki za kidini inazodai kuwa nazo na makao ya utendaji wake. Kwa muda wa karne zilizopita jumuiya hiyo imefanyiza milki inayoithamini sana na humo ndimo inamoongozea umati mkubwa sana wa watu. Inadai kwamba hiyo ndiyo haki yake ya kiroho. Milki yake ni pamoja na makathedro ya bei kubwa pia, madhabahu (altare) za johari, madirisha yenye vioo vya bei weee, vikiwa vimepakwa rangirangi. Ina mali za mashamba na mapesa mengi sana katika banki. Hayo yote ni sehemu ya “mahali patakatifu” inapodai kwamba ni mali yake. Mahali hapo pana utakaso kulingana na maoni yake, na ebu mtu athubutu kupakanyaga akione chamtema-kuni! Angalau hivyo ndivyo jumuiya hiyo inavyofikiri.
8. (a) Dini ya Jumuiya ya Wakristo ina uhusiano gani na “Babeli Mkuu”? (b) Jumuiya ya Wakristo inaulandaje Yerusalemu wenye kuasi imani?
8 Walakini, ni nini kilichoupata Yerusalemu wa kale na “mahali patakatifu” pake—katika utimizo wa unabii—mwaka wa 607 KWK na pia mwaka wa 70 WK? Naye Bwana Yesu anatuonyesha nini katika Ufunuo aliompokeza mtume Yohana? Humo, katika sura ya kumi na saba, tunasoma habari za hukumu ya Mungu itakayofikilizwa juu ya ‘Babeli Mkuu, mama wa makahaba na machukizo ya nchi.’ (Ufunuo 17:5) Huyu “Babeli Mkuu” si mwingine ila ile milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yakiwa ndiyo sehemu kubwa ya milki hiyo. Jumuiya ya Wakristo, inayojisema kuwa katika uhusiano wa agano pamoja na Mungu, ndiyo “Yerusalemu” wa kisasa wenye kuasi imani.
9. “Mama wa makahaba” ametendaje kwa habari ya yule “mnyama” katika utimizo wa kisasa?
9 Muda wa karne zilizopita, “mama wa makahaba,” yaani, dini ya uongo, amefanikiwa sana katika kuongoza mambo ya mataifa na falme zilizo kama mnyama. Kama vile Ufunuo 17:9 unavyoonyesha, yeye ameketi juu ya milima ya kiserikali, na mstari wa 15 unamweleza kuwa ameketi juu ya “maji’” maana yake “jamaa na makutano na mataifa na lugha.” Wakati yule “mnyama mwekundu sana” mwenye sehemu nyingi ndani yake alipotokea mwaka wa 1920 akiwa Ushirika wa Mataifa, na wakati alipotokea tena mwaka wa 1945 akiwa Umoja wa Mataifa, “Babeli Mkuu” alitumia werevu aweze kuambatana na hii baraza ya kimataifa, ili apate faida za pesa na mambo mengine. Yeye hakumbuki kwamba hiki “kitu chenye kuchukiza” cha kisiasa kimesimama kisipopaswa kusimama, kikaweka mguu isivyo halali katika “mahali patakatifu” ambapo sasa ni haki ya milki ya “Yerusalemu wa mbinguni,” ufalme wa Mungu kupitia Masihi.
Zile “Pembe” Zinachukua Hatua
10. Ni mfikilizo gani wa hukumu unaoingoja dini ya uongo?
10 Lakini lo! Katika wakati ambao mataifa hayo yatasema: “Kuna amani na salama,” “pembe” za huyo “mnyama” wa kutisha zitafanya fujo zenye jeuri kwa ghafula! Chuki ambayo zimekuwa nayo kwa muda mrefu juu ya yule “kahaba” haitazuiliwa tena! Zitamwondosha malaya huyo mahali ambapo amekuwa akiketi kiurembo sana juu ya “mnyama.” Hizo pembe za kijeshi zenye kutaka mabadiliko, na yule “mnyama,” zitamchana-chana huyo “kahaba” ‘zimfanye uchi, zimle nyama yake na kumteketeza kabisa kwa moto.’ (Ufunuo 17:16) Dini ya uongo itafanya ukiwa kabisa, kutia ndani Jumuiya ya Wakristo, ambayo imedai kuwa na hali patakatifu” mbele za Mungu duniani. Kwa hiyo, uharibifu wa Jumuiya ya Wakristo utakuwa kamili kama ule wa hekalu la Yerusalemu wa kidunia, ambao juu yake Yesu alisema: “Halitasalia hapa jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomolewa.—1 Wathesalonike 5:3; Marko 13:2.
11. (a) Kwa habari ya “mahali patakatifu” pa kweli ni jambo gani lililotukia mwaka wa 1914? (b) Ni hatua gani zilizoanza wakati huo za kuingilia “mahali patakatifu” ambapo Jumuiya ya Wakristo inadai ni mali yake?
11 Je! dini ya uongo iliyo mfano wa kahaba, kutia ndani Jumuiya ya Wakristo ina wasiwasi juu ya jambo litakaloipata? Inapasa kuwa nao, kama inaweza kufahamu ni kwa sababu gani matukio ya leo ya ulimwengu yanafuata kielelezo kimoja. Tena ingekuwa takatifu kabisa kabisa kama ingezitii kweli za kiunabii zilizo katika Biblia. Ndiyo, muda mfupi tu “Yerusalemu wa mbinguni” ulipokwisha kuzaliwa mwaka wa 1914 ukiwa na haki ya kuwa katika “mahali patakatifu,” hapo ndipo Jumuiya ya Wakristo ilipoanza kupatwa na mikazo mikali sana juu ya pale ambapo hiyo yenyewe inadhani ni “mahali patakatifu”—milki yake ya utendaji. Mwaka wa 1917 mapinduzi yenye kufuata maoni ya Marx (juu ya usawa wa watu wote na maongozi ya kiujamaa) yalitokea Urusi. Tangu wakati huo mamlaka za kiujamaa zisizoamini kuna Mungu zimenyakua sehemu kubwa, za dunia. Zimezidisha sana jeuri yao tangu Vita ya Ulimwengu ya Pili. Zinapaza sauti kutangaza kwamba dini ndiyo “kasumba ya watu.” Nayo Jumuiya ya Wakristo inaomboleza kwamba Wakomunisti hao wameingilia “mahali patakatifu” inapodai ni pake, na kuomboleza pia kwa kupoteza “makutano” ya watu waliotoka kwake.
Tisho kwa “Mahali Patakatifu” pa Jumuiya ya Wakristo!
12, 13. Ripoti za magazeti zimekaziaje tisho linaloelekea “mahali patakatifu” pa Jumuiya ya Wakristo?
12 Yaliyotukia katika nchi zenye kutawalwa na Wakomunisti yanaonyeshwa na ripoti inayofuata iliyotangazwa katika gazeti Star la Hong Kong mwishoni mwa mwaka wa 1981: “Serikali ya Kikomunisti ya Vietnam imeandikisha majina ya watawa wa Kibuddha jeshini, ikafunga gerezani mamia ya viongozi wa dini za Kikristo na kufunga vyuo vya kidini na makanisa. Hayo yalisemwa na wajumbe wa nchi za Magharibi na viongozi wa dini wa nchi za kigeni. Wanasema shabaha ya kufanya hivyo ni kufanya dini zote zisimamiwe kikamili na serikali. Wakimbizi (watoro) wanadai kwamba Kanisa Katoliki la Rumi katika Vietnam ya kusini ndilo hasa limekazwa sana, na wenye mamlaka wametaja misukosuko iliyo katika Poland ya Wakatoliki kuwa uthibitisho wa kwamba Kanisa hilo ‘lina maelekeo ya kupinga mabadiliko ya kiserikali yanayofanywa.’”
13 Jarida Journal and Constitution la Atlanta la Januari 2, 1982, lilikuwa na kichwa cha maneno yenye kusema: “Nyingi za Hadithi Zinazoeleza Matukio Makubwa-Makubwa ya [1981] Zahusiana Dini.” Liliendelea kuonyesha orodha jaribio la kumwua Papa John Paulo wa Pili, kuuawa kwa Rais Sadat wa Misri wanajeshi Waislamu, mauaji na kunyongwa kwa watu wengi sana katika Iran, kufyatuliana risasi kwa njia hatari kati ya Waarabu wavamiaji na Israeli, na kutupwa kwa makombora, kuua watu vifo vinavyotokana na kugomea chaki katika Irelandi. Ndiyo, hasa-a, dini inayohusiana na mengi ya matata yaliyo ulimwenguni. Lakini habari zote hizo zitakuwa kijambo kidogo sana kisichostahili kukumbukwa wakati zile ‘pembe kumi yule mnyama’ zitakapochukua hatua, hivi karibuni, ziiteketeze kikamili dini uongo, kutia na Jumuiya ya Wakristo mahali pake inapopadhania kuwa ni “mahali patakatifu.”
14. Wale walio katika “mahali patakatifu” pa kweli watatishwaje hata wao?
14 Walakini, namna gani wale wanaoabudu katika “mahali patakatifu” halisi—wale walio hapa duniani wakifanya “utumishi mtakatifu” kwa kuunga mkono “Yerusalemu wa mbinguni”? Hao, pia, watashambuliwa na “pembe” za kijeshi, ambazo hata sasa ni sehemu ya uanachama wa Umoja wa Mataifa. Kulingana na Ufunuo 17:14, mwungano huo wa kisiasa utaonyesha kwamba hauna haki ya kusimama katika “mahali patakatifu,” kwa maana huo ‘utapigana na yule Mwana-Kondoo.’
15. (a) Ni nani atakayeshiriki sehemu kubwa katika kushambulia “watakatifu”? (b) Huyo ‘atakujaje kwenye mwisho wake’?
15 Danieli 11:40-45 inaonyesha kwamba yule “mfalme wa kaskazini” ambaye ni wa Kikomunisti atahusika kwa njia kubwa katika shambulio hili juu ya “watakatifu,” lakini “yeye atapaswa kuja njia yote hiyo mpaka mwisho wake, na kutakuwa hakuna msaidiaji kwake.” (NW)b Hivyo, “pembe” zote za kitaifa na yule “mnyama mwekundu sana” mwenyewe zitauawa na Kristo Yesu na majeshi yake ya kimalaika. “Na Mwana-Kondoo atawashinda, kwa maana Yeye ni Bwana wa Mabwana, na Mfalme wa Wafalme.” Hapo penye Har–Magedoni, mfalme mwenye kutawala wa “Yerusalemu wa mbinguni” ataupata ushindi wenye kukata maneno ayaweze mataifa yote ambayo ‘yampa yule mnyama nguvu zao na mamlaka yao.’—Ufunuo 17:12-14; 16:16.
“Kukimbia Kwenye Milima”
16. Ni namna gani na mahali gani watu wa Mungu wanaweza kupata ulinzi?
16 Basi, watu wa Mungu wanapataje ulinzi? Wanaupata kwa “kukimbia kwenye milima.” (Mathayo 24:16, NW) Leo, “milima” hiyo ni pale mahali pa kimbilio lililotayarishwa kwa njia ya kimungu, yaani, mpango wa Yehova wa kuwalinda waliobaki duniani wa wale “watakatifu,” na pia “kundi kubwa” la “kondoo wengine,” ili waipite ile “dhiki kubwa.” Jambo hilo linapatana na unabii wa Yesu kwamba “mwili fulani utaokolewa. (Mathayo 24:22, NW) Kwa kuwa milima ni vitu vyenye kudumu na mara nyingi katika Maandiko inahusianishwa na shughuli za kiserikali, basi ngome iliyo kimbilio lililotayarishwa na Mungu inapatikana katika tengenezo la kitheokrasi lake. Hilo linawakilishwa duniani na “lile kundi la yule Mungu anayeishi, nguzo na tegemezo la ile kweli,” ambalo sasa linahusianishwa na jamii ya duniani pote ya Mashahidi wa Yehova.—1 Timotheo 3:15, NW.
17. Ni hatua gani ya uhakika wanayotakwa wachukue wale wanaopenda kukimbilia kwenye usalama?
17 Ni lazima wote wanaokimbilia tengenezo la Yehova wakome kuunga mkono sehemu yo yote ya mfumo wa Shetani duniani. Ni lazima wasiwe“sehemu ya ulimwengu,”na ni lazima wajitenge nao Lazima waepuke dini ya ulimwengu huo, siasa zake, pilikapilika zake za kutenda jeuri, ufuatiaji wake wa mali, uasherati wake. (Yohana 18:36, NW) Ni lazima wajiweke wakf kwa Yehova Mungu, waishi kulingana na kanuni zake za uadilifu na kujulisha wengine makusudi yake matukufu ya ufalme. Hawapaswi kamwe kusinzia wala kurudia maisha ya raha ulimwengu. Lazima waendelee ‘kujitahidi sana’ wapate ukubali wa Mungu na ruhusa ya kuingia katika taratibu mpya yake.—Luka 13:24; 9:23; 2 Timotheo 2:15.
18. Kwa sababu gani ni jambo la haraka watu mmoja mmoja walio na mioyo inayofaa “waanze kukimbia kwenye milima” sasa?
18 Mwaka jana, 1982, “mahali patakatifu” ambapo Jumuiya ya Wakristo inadai ni mali yake palitishwa kweli kweli. Kwa kweli, kao la dini ya ulimwengu juu ya Mataifa limekuwa katika hatari ya kugeukwa kwa ghafula. Kwa sababu ya ‘kufahamu’ hivyo, Mashahidi wa Yehova wanapaza sauti kwa haraka hivi: ‘Kimbieni mtoke katika dini ya uongo, ndiyo, mtoke katika mfumo wote wa ulimwengu wa Shetani—pigeni mbio kwenye tengenezo la Mungu mkapate kimbilio!’ Kama Yerusalemu wa karne ya kwanza, sasa Jumuiya kufanywa ukiwa . . . maangamizi kamili.” Na ndivyo pia milki nzima ya ulimwengu ya dini ya uongo, Babeli yule Mkuu!—Danieli 9:26b, 27b, NW; Ufunuo 18:2, 4.
19. (a) Zaburi 72 inasema nini juu ya “milima”? (b) Ni kwa njia gani tunaweza kustahili kuja kufurahia “wingi wa amani”?
19 Jambo la kufurahisha ni kwamba “milima” ya kimbilio itakuwa pia “milima” ya baraka, kwa maana Zaburi 72:1-8 (NW) inatuambia: “Acha milima iwapelekee watu amani, pia vilima, kupitia uadilifu . . . [katika siku za Masihi, Mfalme,] mwadilifu atachipuka, na wingi wa amani mpaka mwezi utakapokuwa haupo.” Je! wewe unataka kuhesabiwa kati ya wale watakaofurahia “wingi wa amani”? Basi ‘uwe imara, bila kuondoleka, sikuzote uwe na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’ Maadamu kungali kuna wakati, ni jambo la haraka zaidi sana ujitahidi kweli kweli kusaidia watu wenye mioyo inayofaa “waanze kukimbia kwenye milima.” Basi, “dumu katika mambo hayo; maana kwa kufanya hivyo utajiokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia.”—1 Wakorintho 15:58, NW; 1 Timotheo 4:16.—Kutoka The Watchtower, September 15, 1982.
[Maelezo ya Chini]
a Ili upate mazungumzo yenye maelezo marefu angalia kurasa 336-349 za kitabu “Then Is Finished the Mystery of God,” kilichochapwa na kutangazwa na Sosaiti.
b Angalia kurasa 297-307 za kitabu “Your Will Be Done on Earth,” kilichochapwa na kutangazwa na Sosaiti.
Je! Unaweza Kujibu Maulizo Haya:
□ “Mahali patakatifu” pa kweli ni nini?
◻ “Kile kitu chenye kuchukiza chenye kuharibu” ni nini?
◻ “Kile kitu chenye kuchukiza” kinasimama kwa njia gani “katika mahali patakatifu”?
◻ “Mahali patakatifu” ambapo Jumuiya ya Wakristo inapadhania kuwa mali yake ni nini?
◻ “Mahali patakatifu” ambapo Jumuiya ya Wakristo inapadhania kuwa mali yake panatishwaje sasa?
◻ Leo Wakristo wanatii kwa njia gani amri ya “kukimbia kwenye milima”?
[Blabu katika ukurasa wa 16]
Mwezi Oktoba wa mwaka wa 1965: Papa Paulo wa Sita, katika kuueleza Umoja wa Mataifa kuwa ndio “lile tengenezo kubwa kupita matengenezo yote ya kimataifa,” alisema hivi pia: “Mataifa ya watu wa dunia yanaugeukia Umoja wa Mataifa kuwa ndilo tumaini la mwisho la upatani na amani.”
[Blabu katika ukurasa wa 17]
Mwezi Oktoba wa mwaka wa 1979: Papa John Paulo wa pili alihutubia Kusanyiko Kuu la Umoja wa Mataifa. Ingawa hakutaja hata kidogo Yesu Kristo wala ule Ufalme, papa alisema hivi: “Mimi natumaini Umoja wa Mataifa utadumu nyakati zote kuwa mahakama iliyo kubwa kupita zote ya amani na haki, kao la kweli la uhuru.”
[Picha katika ukurasa wa 19]
“Pembe” za kijeshi zinatisha pale ambapo Jumuiya Wakristo inadai ni “mahali patakatifu” pake