“Dawa Inayofanya Maajabu” kwa Ukuzi wa Kitoto Kichanga Ni Upendo
Huko Philadelphia Katika Hospitali ya Watoto ya Mtakatifu Christopher, vitoto vichanga vilivyo vidogo sana kwa umbo vinalazwa hospitali kwa “kushindwa kukua.” Kwa kawaida vitoto hivyo vinakuwa vidogo kwa umbo na vyepesi kwa uzito kuliko mtoto wa kadiri na vinakuwa na hali ya kuhara na kumalizikiwa na maji mwilini. Vinalia-lia saa zote ili vishikwe. Kivulana mmoja mchanga wa miezi sita alikuwa na kisehemu kidogo chenye upara nyuma ya kichwa chake alipofika hospitalini, kuonyesha kwamba ni mara chache sana wazazi wake walipomwinua mahali walipokuwa wakimlaza.
Kwa muda fulani, ilikuwa ikikisiwa kwamba vitoto vya namna hiyo havikui vizuri kwa sababu viungo vya mwili vinavyotokeza umajimaji wenye chembe za ukuzi havikuwa vikifanya kazi. Lakini madaktari na wafunga wa hospitali hiyo ya Mtakatifu Christopher wanaamini kwamba “katika visa vingi kuna ukosefu wa kitu cha kuchochea ukuzi, ukosefu wa mazingira yenye upendo ili mtoto aweze kukua kwa sababu ya kujisikia katika maoni ya ndani kwamba kuna mtu anayemjali.” Daktari mmoja kwenye Hospitali ya Watoto ya Boston anaripoti hivi; ‘‘Wakati wanapoacha kuwa watoto wenye huzuni na wagonjwa-wagonjwa kisha wanakuwa watoto wenye furaha kwa sababu ya kutunzwa, hapo ndipo wanapoanza kukua,”
Kama wazazi wangefuata maoni ya kwamba watoto ni “urithi kutoka kwa Yehova,” kama Biblia inavyosema, kusingekuwa na “ukosefu wa mazingira yenye upendo.” (Zaburi 127:3, NW) Kwa uhakika, inachukua wakati na jitihada kutunza urithi wo wote na kuufanya ukue. Haijajulikana bado namna hormoni yenye kuchochea ukuzi wa kitoto kichanga inavyofanya kazi. Lakini kuna “dawa inayofanya maajabu” unayoweza kutumia kwa usalama usaidie mtoto wako akue awe mtu mwenye afya, asiye na kasoro za mwili, nayo ni UPENDO.