Neno la Mungu Li Hai
Yesu Kristo—Ni Kitoto Kichanga au Ni Mfalme Anayetawala?
WAKATI wa majira ya Krismasi watu wengi wanamfikiria Yesu kuwa kitoto kichanga tu kilicho katika hori ya ng’ombe. Tamasha zinaonyeshwa za “watu wenye hekima” wakipelekea kile kitoto kilichozaliwa zawadi. Watu wanasema kwamba Yesu alizaliwa katika majira hayo ya mwaka. Je! hivyo ndivyo Biblia inavyosema?
Fungua Biblia yako uone inavyosema hasa. Soma kwa uangalifu Luka 2:1-20 na Mathayo 2:1-16. Sasa, je! Biblia haisemi kwamba wachungaji walikuwa katika makonde (porini) wakilisha makundi ya mifugo yao wakati Yesu alipozaliwa? Kwa kuwa mwezi wa Desemba katika Palestina ulikuwa ndiyo majira yenye mvua na baridi, haielekei kuwa kwamba wachungaji wangekuwa porini pamoja na makundi ya mifugo yao katika wakati huo wa mwaka.
Angalia, pia, kwamba huo ulikuwa ndio wakati wa kuandikishwa ambao watu walitakwa wasafiri kwenye mji wa kwao wakaandikishwe. Kwa uhakika haielekei kuwa kwamba watawala Waroma wangetaka watu ambao tayari walikuwa na maelekeo ya kufanya maasi juu yao wafunge safari hiyo wakaandikishwe wakati wa baridi nyingi sana kama huo. Pia, ushuhuda mwingine unathibitisha kwamba Yesu hakuzaliwa wakati wa Krismasi. (Ona ukurasa wa 10.)
Je! pia umeona kwamba wakati wale wanaoitwa kuwa wenye hekima walipomletea Yesu zawadi, yeye hakuwa bado kitoto kichanga ndani ya hori ya ng’ombe? Biblia inasema “wakaingia nyumbani, wakamwona mtoto pamoja na Mariamu mamaye.” (Mathayo 2:11) Kwa kweli “watu wenye hekima” walioongozwa na nyota, si kwa maagizo ya malaika, walikuwa akina nani? Walikuwa mamajusi, au wanajimu. Na ingawa unajimu unafuatwa na watu wengi, Mungu anaukataza.—Isaya 47:12-15.
Kama vile andishi la Biblia linavyoonyesha, wanajimu hao hawakuelekezwa na nyota waende kwanza mahali Yesu alipokuwa katika Bethlehemu, bali walielekezwa waende kwanza kwa Mfalme Herode mwuaji katika Yerusalemu. Sasa, ikiwa Mungu ndiye aliyekuwa ametumia nyota kuwaongoza wanajimu hao, je! angaliwaelekeza kwanza Yerusalemu ili waonane na mfalme hatari huyo? Ni wazi asingalifanya hivyo!
Wakati nyota ile ilipowaongoza wanajimu wakafika mwishowe mahali Yesu alipokuwa, Mungu alichukua hatua akaonya wanaume hao katika ndoto wasimrudie Herode. Kwa njia hiyo Mungu aliokoa uhai wa Yesu. Tunajuaje? Kwa sababu wakati Herode alipojua kwamba wanajimu wamekimbia bila kumrudia yeye, alijaribu kumwua Yesu. Lakini kufikia wakati huo Mungu akawa amemtafutia Yesu njia ya kuokoka. Kwa hiyo nyota ile kusema kweli ilikuwa mpango wa hila wa Shetani Ibilisi wa kutaka Yesu auawe!
Leo pia ni mpango wenye hila wa Ibilisi kujaribu kuwafanya watu wamfikirie Yesu kuwa kitoto kidogo tu kisichojiweza. Lakini sivyo alivyo! Kabla Yesu hajazaliwa, malaika Gabrieli alimwambia mama yake hivi kumhusu: ‘Atamiliki hata milele, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho.’ (Luka 1:33) Sasa Yesu Kristo anatawala akiwa mfalme hodari mbinguni, na ikiwa sisi tunataka kupokea uzima chini ya utawala wa Ufalme wake, tunahitajiwa kabisa tuukubali uhakika huo.—Isaya 9:6, 7.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Ni jambo gani lisilo sahihi katika tamasha hii?
[Picha katika ukurasa wa 9]
Wale “watu wenye hekima” walifuata nyota—nyota hiyo ilitoka wapi?
Wewe unamwona Yesu kuwa namna gani?