Upendo “Kifungo Kikamilifu cha Mwungano”
“Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha mwungano.”—WAKOLOSAI 3:14, NW.
1. Kwa sababu gani amri iliyo kwenye Wakolosai 3:14 ina mwito wa ushindani leo?
AMRI ambayo Neno lililoandikwa la Mungu linawapa Mashahidi wa Yehova leo kwenye Wakolosai 3:14 ina mwito wa ushindani kweli kweli katikati ya ulimwengu wenye kujawa na chuki na ukosefu wa mwungano. Inaelekea kuwa isiyowezekana kufuatwa, kwa maana inawaamuru kwamba: “Zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha mwungano.’’ (NW) Hata hivyo, amri hiyo yenye kuongozwa na Mungu inaendelea kutimizwa, na hivyo yeye anapata utukufu.
2. Ni nini kinachoelekea kuwa ndicho kifungo cha uunganishi kati ya madhehebu za Jumuiya ya Wakristo, na jambo hilo linaifanya Jumuiya ya Wakristo iwe sehemu ya nini?
2 Ni jambo lisiloweza kukanwa kwamba upendo ulio kifungo kikamilifu cha mwungano haumo katika Jumuiya ya Wakristo, kwa maana jumuiya hiyo imegawanyika katika mamia ya madhehebu za kidini zenye kutofautiana, ikiwa na imani na mazoea ya kidini yasiyopatana. Ni jambo linalostahili kuangaliwa kwamba, mambo yanayoelekea kuwa kifungo cha kuunganishia mifumo ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo ni chuki yao na upinzani wao kulielekea kundi la Kikristo la watu wa Yehova walio wakf na waliobatizwa, mashahidi wake wa leo. (Isaya 43:10, 12) Kwa kuonyesha chuki na upinzani huo, matengenezo ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo yanajifunganisha kabisa na ulimwengu ulio chini ya usultani wa Shetani Ibilisi, “mungu wa ulimwengu huu.” (2 Wakorintho 4:4, Authorized Version) Iko sawa na vile Mwanzilishi wa Ukristo alivyosema ingekuwa. Alipokuwa akiwapa mitume wake waaminifu hotuba yake ya mwisho, baada ya mhaini Yuda Iskariote kwenda zake, Yesu alisema hivi: “Mambo haya ninawaamuru ninyi, kwamba ninyi mpendane mtu na mwenzake. Ulimwengu ukiwachukia ninyi, mjue kwamba umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngalikuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungalikipenda kilicho chake wenyewe. Sasa kwa kuwa ninyi si sehemu ya ulimwengu, bali mimi nimewachagua kutoka katika ulimwengu, kwa sababu hii ulimwengu unawachukia ninyi.”—Yohana 15:17-19, NW.
3. Ni ulizo gani linalotokea juu ya lengo ambalo ulimwengu unaelekezea chuki yao?
3 Kwa sababu ya maneno ya Yesu, ulizo linatokea kwa wepesi, Ni kikundi gani cha kidini leo ambacho ulimwengu, ukiwa pamoja na Jumuiya ya Wakristo, unakichukia na kukihasimu (kukionea upinzani mkali)? Hasa tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, historia ya kibinadamu inasaidia mwulizaji ye yote mwenye moyo mnyofu akijue kikundi hicho bila kukosea.
4. Amri ya Paulo kwenye Wakolosai 3:14 inahusu nani, na ni nani aliye Baba wa kiroho wa watu wote wa namna hiyo?
4 Kutokana na maneno ya utangulizi ya barua ambayo mtume Paulo aliwaandikia Wakolosai, Mashahidi wa Yehova wa leo wanajua kwamba amri yake inawahusu wao moja kwa moja: “Jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha mwungano.” Tunasoma hivi: “Paulo, mtume wa Kristo Yesu kupitia mapenzi ya Mungu, na Timotheo ndugu yetu kwa walio watakatifu na ndugu waaminifu walio katika mwungano pamoja na Kristo huko Kolosai: Na mwe na fadhili zisizostahilika na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu.” (Wakolosai 1:1, 2, NW) Sasa, basi, ni nani aliyekuwa Baba wa kimbingu wa Wakristo hao wote wa karne ya kwanza katika mji wa Kolosai, Asia Ndogo? Ni Baba ya Kiongozi wao wa kiroho, Yesu Kristo, na Baba yake ndiye yule Mungu aliye “juu, juu ya nchi yote” na ndiye ‘aitwaye jina lake Yehova.’—Zaburi 83:18.
5. Bila shaka wenye kuandikiwa barua ya Paulo ni waabudu wa nani, na jambo hilo lilionyeshwaje na Yesu na mtume Yohana?
5 Kumbe hakuna shaka kwamba wale ambao Paulo anaandikia barua yake ni waabudu wa Yehova Mungu, sawa na vile Yesu Kristo mwenyewe alivyo mwabudu wake! Yesu alipokuwa juu ya mlima wa kishawishi alikataa toleo la Ibilisi la kumpa ulimwengu mzima kama tu akikubali kuinama chini amwabudu huyo. Yesu alifanya haraka ya kumfukuza Mshawishi huyo aende zake na akatumia maneno ya amri hii iliyotolewa na Mungu: “Msujudie [Yehova] Mungu wako, umwabudu yeye peke yake.” (Mathayo 4:8-11; Luka 4:8; Kumbukumbu la Torati 6:4, 5, 13) Ni lazima wanafunzi wa Yesu wamwabudu Mungu yule yule ambaye yeye mwenyewe amemwabudu sikuzote, yaani, Yehova. (Yohana 20:17) Kupatana na hilo, wakati mtume Yohana aliposujudu aabudu mbele za malaika aliyempokeza Ufunuo, malaika huyo alikataa, akisema: “Msujudie Mungu. Kwa maana ushuhuda wa Yesu ndio roho ya unabii.”—Ufunuo 19:10; 1:1.
6. Ni baada ya Jumuiya ya Wakristo kufuata mwendo gani amri iliyo kwenye Ufunuo 18:4, 5 ilipasa kutiiwa wa haraka zaidi, na ni akina nani wameifuata amri hiyo, na matokeo yamekuwa nini?
6 Baada ya Babeli Mkuu, ile milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, kujifanyia yenyewe kumbukumbu la kumvunjia Mungu heshima, amri ya kimungu iliyoonyeshwa katika Ufunuo 18:4, 5 ilipata uhitaji wa kutiiwa haraka zaidi ya wakati toleo la gazeti Watch Tower la Desemba 1880 au la kabla ya hapo. Amri hiyo inasema: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake. Kwa maana dhambi zake zimefika hata mbinguni, na Mungu amekumbuka maovu yake.”a Kwa kutii amri hiyo, wale waliotaka kuwa “watu” wa Yehova Mungu walitoka ndani ya Babeli Mkuu wakaandamana kama kundi moja lenye kupendelea umoja wa Kikristo, kuukuza upendo ule, ambao ni “kifungo kikamilifu cha mwungano.” Waliyathamini kwa uzito maneno ya mtume yaliyo kwenye 1 Wakorintho 14:33: “Mungu si Mungu wa machafuko, bali wa amani.” Basi, tunapoyatazama makundi ya Mashahidi wa Yehova leo yanayozidi arobaini na tatu (43) elfu, tunalazimika kuyatamka kwa sauti maneno haya ya Zaburi 133:
“Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, ndugu wakae pamoja, kwa umoja. Ni kama mafuta mazuri kichwani, yashukayo ndevuni, ndevu za Haruni, yashukayo mpaka upindo wa mavazi yake. Kama umande wa Hermoni ushukao milimani pa Sayuni. Maana ndiko [Yehova] alikoamuru baraka, naam, uzima hata milele.”—Zaburi 133:1-3.
7. Ni wajibu wa nani leo kudumisha umoja huo, na Mungu aliwahifadhi mashahidi wake wakaipita Vita ya Ulimwengu ya Kwanza kwa kusudi gani?
7 Kama ilivyokuwa kuhusu kundi la huko Kolosai wakati wa karne ya kwanza ya ule unaoitwa Wakati wa Kikristo wetu, ni wajibu wa mashahidi wa kisasa wa Yehova kudumisha umoja huo wa kutamanika wa tengenezo katikati ya ulimwengu uliofarakana. Ndivyo hasa ilivyo tangu mwisho wa “majira ya Mataifa” katika mwaka ule wa 1914 wenye uharibifu mwingi uliotokana na vita! (Luka 21:24) Vita ya ulimwengu ya kwanza ilikaribia kufutilia mbali Mashahidi wa Yehova walio tengenezo la Kikristo la kweli kweli. Lakini kwa ajili ya kazi ya kuzihubiri ‘habari njema hizi za ufalme dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote’ Mungu Mwenye Nguvu Zote hakuwaacha adui walioungana katika Jumuiya ya Wakristo na katika jumuiya ya wapagani wawafutilie mbali mashahidi wake wote waliotiwa mafuta kiasi cha kuwamaliza kabisa duniani. (Mathayo 24:14, NW; Marko 13:10) Katika mwaka ule wa kwanza ulioifuata vita, yaani mwaka wa 1919 W.K., Yehova Mungu aliwaweka huru wakatoka katika vizuizi na kuwatuma wakaifanye kazi ya kuhubiri kati ya mataifa yote.
8. Kwa kuwa Shetani ameshindwa kuuvunja umoja huo wa Kikristo kwa kutumia njia za kinje, yeye amechukua hatua gani ili kujaribu kufanya hivyo?
8 Shetani Ibilisi alikuwa ameshindwa kuwaangamiza Mashahidi wa Yehova kwa njia na mashirika ya nje, na kwa hiyo tangu wakati huo amejitahidi kuvunja-vunja umbo lao lenye umoja kwa hila, kwa kuwachokora-chokora tokea ndani, tokea ndani ya tengenezo lenyewe. Kwa habari hiyo ilitabiriwa katika Ufunuo 12:17 hivi: “Joka akamkasirikia yule mwanamke, akaenda zake afanye vita juu ya wazao wake waliosalia, wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu.”
Utu Ambao Mtu Binafsi Anapaswa Kuhangaikia Awe Nao
9. Mashahidi wa Yehova wanahitaji kujilinda wasipatwe na maambukizo gani, na Zaburi 91 inasema nini juu ya jambo hilo?
9 Chuki ambayo ulimwengu huu mbovu umeambukizwa inaenea, sawa na vile Yesu Kristo mwenyewe alivyotabiri katika unabii wake juu ya “umalizio wa mfumo wa mambo,” akisema: “Na manabii wengi wa uongo watatokea na kupotosha wengi; na kwa sababu ya kuongezeka kwa kutokutii sheria upendo wa wengi zaidi utapoa. Lakini yeye atakayekuwa amevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mathayo 24:3, 11-13, NW) Roho ya chuki ni yenye kueneza sana maambukizi yake, na kwa hiyo hata washiriki wa tengenezo linaloonekana la Yehova Mungu wanahitaji kujilinda wasiambukizwe roho hiyo. Mtunga zaburi aliyeongozwa na Mungu anaonyesha tunavyoweza kufanya hivyo, akisema: “[Mtu ye yote] aketiye mahali pa siri pake Aliye juu atakaa katika uvuli wake Mwenyezi. Nitasema, [Yehova] ndiye kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu nitakayemtumaini. Hutaogopa hofu ya usiku, wala mshale urukao mchana, wala tauni ipitayo gizani, wala uele uharibuo adhuhuri, ijapo watu elfu waanguka ubavuni pako. Naam, kumi elfu mkono wako wa kuume! Hata hivyo hautakukaribia wewe. Ila kwa macho yako utatazama, na kuyaona malipo ya wasio haki.”—Zaburi 91:1, 2, 5-8.
10. Tutaepukaje kuwa na utu unaotufanya tuonekane kama walimwengu, na Mungu ana maoni gani juu yetu, tofauti na vile anavyouona ulimwengu huu ulio mfu?
10 Tunahakikishiwa kupewa ulinzi wa kimungu, lakini ni lazima tukae bila kuruka masharti yanayoambatana na ulinzi huo. Tukiuepuka urafiki mwingi wenye kuleta kifo cha kiroho kuhusiana na ulimwengu huu mgonjwa, hatutakuwa tukijivika utu utakaotufanya tufanane na watu wa ulimwengu. Hatutakuwa tukijivika hali ya kuonyesha chuki iliyo na ulimwengu huu. Kinyume kamili cha chuki ni upendo, kumpenda Yehova na Kristo wake na kupenda ndugu na dada zetu Wakristo. Utu unaoonyesha sifa hiyo ni utu ule ambao mtume Paulo mwenye kuongozwa na Mungu anatuambia tuuvae tukiwa wanafunzi wa Yesu Kristo. Tukifanya hivyo tutakuwa tukijipendekeza wenyewe kwa wengine kuwa tu wahudumu (maminista) wa Mungu kwa kuwa na “upendo usio unafiki.” (2 Wakorintho 6:4-10) Upendo huo asili yake ni Mungu, nasi tukiwa nao inamaanisha kwamba tumekwisha kuingia katika uhusiano pamoja naye kwa kuupa ulimwengu visogo vyetu kwa habari ya kujipatanisha nao kwa moyo na nafsi. Maoni ya Mungu ni kwamba ulimwengu ni mfu, na wale walio sehemu yao ni wafu pia; kwa hakika hawana uhai machoni pake. Kwa maoni ya Mungu sisi wanafunzi wa Yesu Kristo, tuliojiweka wakf na kubatizwa, tuko hai; ndiyo, tuko hai tukiwa sehemu ya tengenezo Lake, ambamo upendo umekaa kwa imara. Basi andiko la 1 Yohana 3:14 halitii chumvi linapotuambia hivi: “Sisi tunajua ya kuwa tumepita toka mautini kuingia uzimani, kwa maana twawapenda ndugu. Yeye asiyependa, akaa katika mauti.”
11. Upendo unatuingiza katika udugu gani?
11 Hivyo tunaona kwamba upendo unatupa ruhusa ya kuingia katika udugu ambamo Yesu Kristo, yule Mwana wa Mungu, ndiye kaka yetu (ndugu mkubwa). Sifa hiyo ya Kikristo ni vazi, au nguo, na kwa kuwa na sifa hiyo tunapaswa kuonyesha waziwazi kabisa sisi ni watu wa namna gani, bila unafiki. Hiyo ndiyo sifa kubwa kuliko zote ambayo Neno la Mungu linasema lazima tuisitawishe na kuizoea.
12. Ni hatua gani ambazo lazima zichukuliwe ili kuufikia upendo huo, na je! ni lazima mambo yanayohusika katika hatua hizo yaje kuachiliwa mbali baadaye?
12 Ni jambo la wazi kwamba kuna hatua fulani ambazo mwanafunzi mtiifu anahitaji kuzichukua ili aifikie ile namna ya kweli ya upendo. Andiko la 2 Petro 1:5-8 (NW) linawaambia hivi wale wamejiwekea shabaha ya kuifikia zawadi tukufu ya kiungu katika mbingu: “Naam, kwa sababu ii hii, kwa kuitikia kwenu kutoa jitihada yenu yote ya moyo, tieni wema wa adili kwenye imani yenu, kwenye wema wenu wa adili maarifa, kwenye maarifa yenu kujiweza, kwenye kujiweza kwenu uvumilivu, kwenye uvumilivu wenu utawa, kwenye utawa wenu shauku ya kidugu, kwenye shauku yenu ya kidugu upendo. Kwa kuwa ikiwa mambo hayo yanakaa ndani yenu na kufurika, yatawazuieni msiwe ama wasiotenda ama wasiozaa matunda kwa habari ya maarifa sahihi ya Bwana yetu Yesu Kristo.” Mambo hayo mengi ambayo yameongezewa hayapasi kamwe kuachiliwa mbali baada ya mtu kuifikia ile sifa kubwa kupita zote ya upendo. Hapana, bali imani, wema wa adili, maarifa, kujiweza, uvumilivu, utawa na shauku ya kidugu ni lazima yabaki yakiwa sehemu zinazohitajiwa kabisa ili kuukamilisha vizuri utu wetu. Ni lazima mambo hayo yawepo kwa utele pamoja na upendo. Ikiwa hivyo, wenye kudumisha vitabia hivyo vya kiutu wataipokea kwa Mungu ile zawadi katika wakati wake.
13. Paulo anaongezaje maelezo marefu zaidi juu ya hatua hizo za msingi kwenye Wakolosai 3:12-14?
13 Kuongezea mambo tunayohitaji kuzifanyia nafsi zetu ili tupate thawabu inayofaa, ingefaa tutaje hapa sifa ambazo mtume Paulo anasema ni lazima tuzivae kuonyesha namna utu wetu ulivyo. Kabla ya kutaja ni jambo gani lililo kifungo kikamilifu cha mwungano, Paulo anasema: “Kulingana na hivyo, mkiwa wachaguliwa wa Mungu, watakatifu na wapendwa, jivikeni shauku nyororo za huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu. Endeleeni kuchukuliana na kusameheana kwa hiari ikiwa mtu ye yote ana sababu ya kulalamikia mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, fanyeni hivyo ninyi pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha mwungano.”—Wakolosai 3:12-14, NW.
Tofauti na Wale Wasio na Mwungano
14. Washiriki wa kundi la Kikristo walikuwa watu wa namna gani kabla hawajachukua hatua ya kuyafuata maagizo ya mitume?
14 Maagizo hayo ya mitume yanaonyesha aina ya watu ambayo washiriki wa kundi la Kikristo wanapaswa kuwa. Zamani walikuwa sehemu ya ulimwengu huu usiomcha Mungu na usiopendeka, pamoja na sifa zao zote za kiibilisi. Basi wao walikuwa watu wa namna gani huko nyuma? Kwenye 1 Wakorintho 6:9-11 mtume Paulo anaonyesha hilo akisema: “Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi . . . Na baadhi yenu mlikuwa watu wa namna hii; lakini mlioshwa, lakini mlitakaswa, lakini mlihesabiwa haki katika jina la Bwana Yesu Kristo, na katika [roho ya] Mungu wetu.”
15. Kwa sababu gani walimwengu hawana ‘kifungo cha mwungano’ chenye kuendelea kuwapo?
15 Ni vigumu kwa walimwengu wa hali zilizoelezwa hapo juu kuwa na jambo lisilo na choyo, jambo safi kabisa la kuwa kiunganishi chao kikamilifu kisichoweza kuvunjika. Kusema kweli, wao hawana “mwungano mkamilifu wa umoja.” Kwa hiyo, jamii ya kibinadamu iliyoko nje katika ulimwengu ule wa kale haishikani pamoja. Huenda kwa kitambo kidogo mambo yanayowapendeza wao kwa ujumla yakawashikanisha pamoja. Lakini baada ya muda kupita, mambo hayo yenye kuhangaikiwa na wote kwa ujumla yanapoondolewa, mlimwengu anaacha kupendezwa na mlimwengu mwenzake. Vifungo vya uunganishi vinamalizika. Kwa hiyo, huenda mwishowe wakalazimika kuvumiliana kwa sababu tu wao ni binadamu kwa binadamu na haiwezekani kuepukana mitaani maana hali zinawalazimisha kuishi pamoja.
16. Wakati walimwengu wanapokuwa hawana mambo yenye kuwaunganisha kwa kitambo kidogo, wanarudia nini, na kwa sababu gani?
16 Utukuzo wa taifa! Uzalendo! Mgawanyiko wa madhehebu za kidini! Ukabila! Wakati mambo hayo yenye kuchochea sana mawazo ya moyoni yanapochachishwa kweli kweli, wenye kuhusika wanaona yakiwazidia mno kisha wanaanza kutimiza wajibu unaowapasa tu. Hata hivyo, wanadamu ni wale wale tu nyakati zote. Wanaendelea kuhangaikia kwanza mambo yao wenyewe. Kwa hiyo, wanapopata nafasi ya kutokuwa katika kazi zinazowapasa kutimiza, wanapokuwa huru kujitia katika anasa kulingana na mambo yanayowapendeza au yasiyowapendeza kibinafsi, wanajionyesha kuwa hawajabadilika, bali ni watu wale wale wenye kujitafutia mambo yao wenyewe. Ingawa huenda watu wanaojipatanisha na ulimwengu huu wakashangiliwa mno kiasi cha kupakwa mafuta, na kutangazwa kuwa wanastahili heshima na utukufu ulioinuka sana kama mbingu kwa sababu ya utumishi wao wa kilimwengu wenye kutokeza, au kwa sababu ya kutumikia sana jambo fulani la ulimwengu bila kuyumba-yumba, kulingana na viwango vya Biblia hawawezi kuhesabiwa kuwa wanastahili kupata nafasi katika Ufalme wa kimbingu wa Yehova Mungu wakatawale pamoja na Kristo.
17. Ufalme wa Mungu unawataka wale wanaoutafuta huo kwanza wawe na nini, na ni nini kinachowasaidia katika jambo hilo?
17 Ufalme wa Mungu hauna urafiki na ulimwengu huu wala wafuasi wanaoutumikia. Kwa kuwa ulimwengu wenye kuongozwa na Shetani umeshindwa kwa njia kubwa kuunganisha wafuasi wao, Ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Kristo unawataka Wakristo waliojiweka wakf na kubatizwa, wanaoutafuta huo kwanza, wawe na utumishi uliounganishwa kwa umoja. Ufalme huo ni zao la upendo wa Mungu. Roho kubwa inayoongoza serikali hiyo ya kimbingu ni upendo, na zaidi sana kumpenda Mungu na kumchukia adui yake aliye mkubwa wa wote, Shetani, na kuuchukua ulimwengu ambao yeye ndiye “mungu” wao. Shetani ajapofanya jitihada zote za kuleta mchafuko, upendo huo unaotokana na Yehova Mungu, yule Baba wa kimbingu, unaendelea kufanya kazi ukiwa ndio “kifungo kikamilifu cha mwungano” kwa ajili ya wale wanaoshikana na tengenezo lake la kidunia linaloonekana, ndiyo, kwa ajili ya jamaa yote ya Mungu, huko mbinguni na hapa duniani pia.
[Maelezo ya Chini]
a Katika ukurasa wa 6 toleo hilo lilikuwa na makala yenye kusema ‘Babeli Mkuu.’
Je! Unakumbuka?
□ Wakristo wa kweli wameunganaje, tofauti na Jumuiya ya Wakristo?
□ Shetani anajaribu kuvunja umoja wetu wa Kikristo kwa njia gani?
□ Tunaweza ‘kujivikaje upendo’ ulimwengu ujapokuwa wenye chuki?
□ Upendo unaweza kutufunganishaje pamoja zaidi ya vifungo vilivyo katika ulimwengu?
[Picha katika ukurasa wa 8]
Wakristo ni sehemu ya udugu wenye upendo ambamo Yesu Kristo ni kaka yao