Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 5/15 kur. 18-23
  • Kujivika Wenyewe Upendo na Kuendelea Kuuvaa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kujivika Wenyewe Upendo na Kuendelea Kuuvaa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kushinda Mambo Yanayoweza Kuleta Mgawanyiko
  • Wenye Mwungano kwa Ajili ya Kazi ya Pekee
  • Endeleeni Kuunganishwa na Upendo
  • Upendo “Kifungo Kikamilifu cha Mwungano”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Upendo Ukiwa “Kifungo cha Mwungano” Wathibitika Kuwa “Mkamilifu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Upendo wa Kikristo Wenye Msingi wa Upendo wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Mjengwe na Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 5/15 kur. 18-23

Kujivika Wenyewe Upendo na Kuendelea Kuuvaa

1. Ni kitu gani tunachopaswa kujivika, na ni wakati gani kitu hicho kitakapopatwa na jaribu lililo kubwa zaidi ya yote?

KWA KUWA upendo ni “kifungo kikamilifu cha mwungano,” huo ndio sifa iliyo ya maana kupita zote ambayo tunapaswa kujivika bila unafiki. Ni lazima tuuvae daima kwa unyofu wote wa moyo. Upendo si joho (vazi la nje) la kufunika utu halisi wa mtu ili ubaya wake usionekane. Maneno haya yaliyoongozwa na Mungu yamehifadhiwa ili kutushauri sisi leo: “Acheni upendo wenu uwe bila unafiki. . . . Katika upendo wa kidugu iweni na shauku nyororo kwa mtu na mwenzake.” (Warumi 12:9, 10, NW) Jaribu lililo kubwa zaidi la ukweli wa upendo wetu, la hiki “kifungo cha mwungano,” lingali liko mbele yetu​—katika wakati ujao ulio karibu.

2. Je! upendo unaweza kupatikana bila kuchukua kwanza hatua yo yote ya msingi?

2 Basi, sasa ndio wakati unaofaa tusitawishe upendo huo. Ni lazima hatua zote zinazoongoza mtu aifikie sifa hiyo zichukuliwe sasa. Hiyo ndiyo sababu mtume Paulo anafikia kipeo cha pendekezo lake la mambo mbalimbali ambayo wanafunzi walio wakf na waliobatizwa wa Yesu Kristo walihitaji kuyafanya, kwa kusema hivi: “Zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha mwungano.” (Wakolosai 3:14, NW) Kwa hiyo “mambo haya” zaidi ambayo ni lazima tujivike, zaidi ya kujivika upendo, ni mambo gani?

Kushinda Mambo Yanayoweza Kuleta Mgawanyiko

3. Kulingana na Wakolosai 3:9-13, ni hatua gani zinazohitaji kuchukuliwa ili kujipatia upendo?

3 Huko nyuma siku za mitume Paulo na Yohana yalikuwako mambo ambayo yangaliweza kuwa sababu za kutokeza mgawanyiko. Lakini sababu hizo zilizokuwa halali wakati fulani zilipasa kuachiliwa mbali sasa, kisha ubora na uzito wazo ubatilishwe, Wakristo wote walikuwa kundi moja kwa ujumla, shirika moja lililo chini ya Kichwa mmoja wa kiroho, Yesu Kristo. Misingi yote ya kimwili yenye kuleta migawanyiko ilipasa kufagiliwa mbali. Yale mambo ya hakika ya kiroho yenye uunganishi yalipasa kutangulizwa mbele. Kupatana na hilo, mtume Paulo aliendelea kusema hivi: “[Vueni] kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake: mkivaa utu mpya, unaofanywa upya upate ufahamu sawasawa na mfano wake yeye aliyeuumba. Hapo hapana Myunani wala Myahudi, kutahiriwa wala kutokutahiriwa, mgeni wala mshenzi, mtumwa wala mwungwana, bali Kristo ni yote, na katika yote. Basi, kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake.”​—Wakolosai 3:9-13.

4. Kwa sababu gani kulikuwa na uhitaji wa kuchukuliana (kupatana) katika kundi la karne ya kwanza, na ni juu ya msingi gani mambo fulani yangaliweza kuachiliwa mbali?

4 Katika kundi kulikuwa na magumu ya kuchukuliana (kupatana) kwa sababu kulikuwako tofauti zote hizo za taifa ambalo mtu alitokana nalo na malezi yake ya kidini, msimamo wake katika jamii ya watu, mambo ya kikabila na rangi ya ngozi. Kulikuwa na uhitaji wa ufahamu na kuachilia makosa ya mtu na mwenzake Sababu ni kwamba, ingawa mambo hayo labda yalichukuliwa kuwa makubwa na wanadamu wa kimwili, hayakuwa hivyo kwa Mungu na kwa Mwanaye Yesu Kristo, ambaye alifia wanadamu wote katika wakati ambao tofauti zote hizo zilikuwa zimekwisha kusitawi na zikawa zingaliko. Bila shaka, huenda watu wenye kuwaza mambo kwa ufahamu mpana wakawa waliachilia tofauti hizo bila kukosana na wenzao kwa sababu ya ukarimu wa nafsi zao wenyewe, kwa sababu ya kufuata kanuni za ujumla. Walifanya hivyo kwa kufuata desturi nzuri tu, kwa sababu ya ubinadamu tu. Lakini huenda ikawa upendo safi usio na choyo ulikosekana.

5. Ni lazima Mashahidi wa Yehova wachukue hatua inayopita hali gani zilizo kawaida ya kibinadamu wakati wanapoachilia mbali mambo ambayo yangaliweza kuleta mgawanyiko, na kwa njia hiyo wataonyesha wana mwungano pamoja na nani?

5 Kwa sababu hiyo, sisi wafuasi tulio wakf na tuliobatizwa wa Yule aliyetoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kwa ajili ya namna zote za watu ni lazima tuchukue hatua inayoizidi desturi tu, inayozidi hali ya kuweza kukubaliana na watu tu, inayozidi kuwa watu wenye upendezi tu, inayozidi kuwa na adabu njema tu, inayozidi kuwa na maoni ya huruma ya kibinadamu; ni lazima tuchochewe na upendo wenye unyofu wa kweli, usio wa kujifikiria, ulio tunda la roho ya Yehova Mungu. Tunda hilo linatafuta faida na pato la wengine. Linafurahia kushiriki kuongeza masilahi ya kiroho na furaha ya wengine. Linaonyesha kwamba tuna mwungano pamoja na Mungu, ambaye ndiye mwenye kujawa pomoni na upendo. Ndani ya upendo huo mna uwezo wenye uvutano. Kupatana na hilo 1 Yohana 4:19 inataja hivi: “Sisi twapenda kwa maana yeye alitupenda sisi kwanza.”

6. Washiriki wa lile “kundi moja” wanavutiana kupitia kitu gani, nalo tunda la roho ya Mungu halitegemei nini?

6 Hivyo, wakati wale watu mbalimbali wanaolifanyiza lile “kundi moja” chini ya “mchungaji mmoja” wanapoonyeshana upendo, unawavuta wakaribiane kwa kushikana sana kisha unayasukuma kando yale mavutano yenye kuleta mgawanyiko ya malezi ya namna mbalimbali ya washiriki wa hilo “kundi moja.” Wanavutiana kwa sababu wamekwisha kujivika “utu mpya.” Wote wana “roho moja” inayotokana na Chemchemi moja ya kimungu, yule Mungu na Mpaji-Uzima wa wote. Tunda lenye kuchangamsha moyo la roho yake ni upendo, si wenye kutegemea ngono au nyege mbaya za kichoyo, bali wenye kutegemea kuzithamini kwa moyo zile sifa za kiungu za “utu mpya.” Upendo huo pekee unakuwa “kifungo kikamilifu cha mwungano,” nao unahifadhi upatano na ushirikiano wa utendaji.

Wenye Mwungano kwa Ajili ya Kazi ya Pekee

7. Tangu mwaka wa 1914 kuna uhitaji wa kufanya nini upande wa Mashahidi wa Yehova, na watafanya hivyo kwa faida ya kazi gani?

7 Katika wakati huu ambao siku zimesonga sana katika “umalizio wa mfumo wa mambo” tangu mwaka wa 1914, kuna uhitaji wa kujikakamua (kujibidiisha sana) kwa umoja upande wa Mashahidi wa Yehova, ambao si sehemu ya mfumo huu wa mambo. Wajibu umewakalia wa kutoa ushuhuda wa ulimwenguni pote juu ya tukio lililo la maana kuliko matukio yote katika historia yote ya kibinadamu. (Mathayo 24:14, NW; Marko 13:10) Ni lazima hali hiyo iwe yenye kutokeza kama ile ambayo mtume Paulo anaitaja kuwa ilikuwa mashuhuri katika siku zake. Akivuta fikira kwenye jambo hilo katika Wakolosai 1:23 (NW), alisema hivi: “Tumaini la habari njema zile mlizozisikia, na zilizohubiriwa katika kuumba kote kuliko chini ya mbingu. Juu ya habari njema hizo mimi Paulo nikawa mhudumu.” Na sasa, enyi nyote wahudumu wa zile habari njema leo, je! sisi pia tusifanye kazi ya namna iyo hiyo katika kuumba kote kwa kuzihubiri habari njema zilizowekwa akibani kwa ajili ya wakati wetu wenyewe ulio wa hatari?

8. Sisi leo tunaona njozi gani iliyosimuliwa na Yohana katika Ufunuo 14:6-12 ikiendelea kutimizwa?

8 Sisi leo tunauona utimizo wa njozi aliyopewa mtume Yohana, ambayo aliieleza katika Ufunuo 14:6-12 kwa maneno haya: “Kisha nikaona malaika mwingine, akiruka katikati ya mbingu, mwenye Injili ya milele, awahubiri hao wakaao juu ya nchi, na kila taifa na kabila na lugha na jamaa, akasema kwa sauti kuu, Mcheni Mungu, na kumtukuza, kwa maana saa ya hukumu yake imekuja. Msujudieni yeye aliyezifanya mbingu na nchi na bahari na chemchemi za maji. Kisha mwingine, malaika wa pili, akafuata, akisema, Umeanguka, umeanguka Babeli, mji ule ulio mkubwa, maana ndio uliowanywesha mataifa yote mvinyo ya ghadhabu ya uasherati wake. Na mwingine, malaika wa tatu, akawafuata, akisema kwa sauti kuu, Mtu awaye yote akimsujudu huyo mnyama na sanamu yake, na kuipokea chapa katika kipaji cha uso wake, au katika mkono wake, yeye naye atakunywa katika mvinyo ya ghadhabu ya Mungu iliyotengenezwa, pasipo kuchanganywa na maji, katika kikombe cha hasira yake; naye atateswa kwa moto na kiberiti mbele ya malaika watakatifu, na mbele za Mwana-Kondoo. Na moshi wa maumivu yao hupanda juu hata milele na milele, wala hawana raha mchana wala usiku, hao wamsujuduo huyo mnyama na sanamu yake, na kila aipokeaye chapa ya jina lake. Hapa ndipo penye subira ya watakatifu, hao wazishikao amri za Mungu, na imani ya Yesu.”

9. Ni wakati gani Mashahidi wa Yehova walipoona kutimizwa kwa njozi ya mtume Yohana, na kwa sababu gani sasa walikuwa huru kueleza watu habari njema kila mahali?

9 Je! mabaki watiwa mafuta waliofananishwa na mtume Yohana wameona ulinganifu wa kisasa wa huyo malaika mwenye kuruka katikati ya mbingu akiwa na “Injili ya milele” iliyopasa kutangaziwa wakaaji wote wa dunia, ndiyo, kila taifa, kabila, lugha na watu wa rangi iwayo yote? Ndivyo, wameuona kuanzia kiangazi cha mwaka ule ulioifuata vita, wa 1919, na kuendelea. Wakati huo ndipo unabii wa Yesu wenye amri ulio katika Mathayo 24:14 ulipoanza kutimizwa. Je! mabaki waliookoka walikuwa wakati huo na “Injili ya milele” ya kutangaza katika kuumba kote kuliko chini ya mbingu? Ha-sa-a! Zilikuwako habari njema za kusimulia juu ya kusimamishwa kwa Ufalme wa Mungu mikononi mwa Kristo katika mbingu, habari za kwamba tukio hilo lilifanyika mwishoni mwa Majira ya Mataifa mwaka wa 1914. Na lo! zilikuwa habari njema za kuwasisimua namna gani mabaki wa Waisraeli wa kiroho kwa kujulishwa na matukio yaliyoifuata vita kwamba mwonezi wao hasa, yaani, Babeli Mkuu, alikuwa ameanguka, akapotewa na uwezo wake wa kuwashikilia Mashahidi wa Yehova! Sasa wao walikuwa huru kukitangaza kipande kikubwa hicho cha habari njema kwa jamii zote za watu waliokuwa katika utumwa wa kidini, kuwaambia watoke katika Babeli Mkuu na kuwasaidia wafanye hivyo.​—Ufunuo 18:4.

10. Wale ambao wametoka katika Babeli Mkuu wamejishirikisha na nini, na wameingia ndani ya kifungo gani cha mwungano?

10 Tayari “mkutano mkubwa” wa wenye kupenda uhuru umekwisha kuitikia ile “Injili ya milele” na kuuitikia mwito wa wakati wake wa kutoka katika milki ile ya Kibabeli ya ulimwenguni pote ya dini ya uongo. Wamemiminika upande wa mabaki waliowekwa huru wa Waisraeli wa kiroho. Hivyo wamejishirikisha na tengenezo la Yehova linaloonekana kisha wao wenyewe wakawa Mashahidi wa Yehova. Wameingia ndani ya kile “kifungo kikamilifu cha mwungano,” ule upendo ulio tunda la roho ya Yehova Mungu.​—Wakolosai 3:14, NW; Wagalatia 5:22.

11. Upendo ambao Jumuiya ya Wakristo imejizoeza umekuwa wa kupenda nani, na ni wakati gani Mashahidi wa Yehova watakapoyatumia kwa shangwe yale maneno ya Ufunuo 19:1, 2?

11 Sehemu iliyo kuu ya Babeli Mkuu ni ile inayoitwa Jumuiya ya Wakristo. Ijapokuwa ina jina la Ukristo, hiyo haiuzoei Ukristo wa kweli, na mamia ya mamilioni ya washiriki wayo hawashikanishwi pamoja na kile “kifungo kikamilifu cha mwungano.” Jambo hilo linashuhudiwa na mfarakano wayo ikiwa na mamia mengi ya madhehebu za kidini. Upendo ambao Jumuiya ya Wakristo imejivika ni upendo wa kuwapenda wapenzi-makahaba (hawara) wa Babeli Mkuu, wale wanasiasa na wanajamii wa ulimwengu huu, ambao imefanya nao uasherati wa kidini. Kutakuwako furaha kubwa sana wakati wa uharibifu kamili wa Babeli Mkuu, si anguko lake tu. Hayo yatafanyika wakati wa Mungu wa kufanya hesabu naye. Hiyo itatia ndani Jumuiya ya Wakristo. Ndipo mashahidi wake watakapofanya shangwe kwa kutumia maneno ya Ufunuo 19:1, 2: “Haleluya; Wokovu na utukufu na nguvu zina Bwana Mungu wetu; kwa kuwa hukumu zake ni za kweli na za haki; maana amemhukumu yule kahaba mkuu aliyeiharibu nchi kwa uasherati wake, na kuipatiliza damu ya watumwa wake mkononi mwake.” Kuharibiwa kwayo kama kwa moto hakutakuwa na mwisho, kutakuwa ‘kwa milele.’​—Ufunuo 19:3.

12. Hali inawahitaji Mashahidi wa Yehova wajizoeze sifa gani mpaka wakati Babeli Mkuu atakapoharibiwa, na ni lazima wachukue msimamo wa namna gani wa kukabiliana na adui za ile nuru?

12 Kwa sasa, wakati Babeli Mkuu inapoendelea kuwako kwa ruhusa ya Yehova, hali ya kidunia ya wale “wazishikao amri za Mungu, na imani ya Yesu” inawabidisha kujizoeza “subira” (au uvumilivu). (Ufunuo 14:12) Wao wana sababu ya kuwapasisha wayatumie kuhusu nafsi zao wenyewe maneno ya Yesu yaliyo katika unabii wake juu ya “umalizio wa mfumo wa mambo,” kwenye Mathayo 24:13 (NW), yaani: “Yeye ambaye amevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” Maneno hayo yalisemwa muda mchache tu baada ya maneno ya Yesu yaliyoyatangulia: “Kwa sababu ya kuongezeka kwa kutokutii sheria upendo wa wengi zaidi utapoa.” (Mathayo 24:12, NW) Upendo kwa upande wa Mashahidi wa Yehova utawawezesha kuvumilia mpaka mwisho wa mfumo huu wa zamani wa mambo. Kwa kadiri wanavyozidi kujizoeza upendo kati yao wenyewe na kuelekea wale wanaojaribu kuingia katika uhusiano pamoja na Yehova Mungu, ndivyo kile “kifungo kikamilifu cha mwungano” kinavyozidi kuwa chenye nguvu. Haya basi, enyi Mashahidi wa Yehova, songeni mbele na ushuhudiaji wa ulimwenguni pote wa ule Ufalme katika nchi hizo 205 ambamo tayari mnafanya kazi, mkitazamia kuupanua katika nchi nyingine zaidi! Huu ndio wakati wa kumkabili adui kwa mwungano. Ni lazima tujikusanye pamoja kisha tupigane kwa umoja na yale majeshi ya giza la ulimwengu huu.

13. Ni shirika gani linalotumiwa na Mungu linalostahili kuendelea kuungwa mkono nasi kwa ushikamanifu?

13 Kwa muda wa karibu karne moja sasa Sosaiti ya Pennsylvania, United States (Amerika), imekuwa shirika lenye uunganishi ambalo Yehova ametumia kwa ajili ya mashahidi wake. Limekuwa chombo chenye nguvu nyingi ambacho jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” imetumia kuwapa Mashahidi wa Yehova ‘chakula chao cha kiroho kwa wakati wake.’ (Mathayo 24:45-47) Baraka ya Yehova inaonekana wazi ikiwa juu yacho pamoja na matengenezo yacho ya matawi 95 yaliyo katika sehemu zote za dunia. Hicho kinaendelea kustahili kuungwa mkono kwa ushikamanifu na kuonyeshwa ushirikiano nasi maadamu Yehova Mungu anafurahia kukitumia. Lo! sisi tuna deni kubwa namna gani kwa chombo hicho-o!

Endeleeni Kuunganishwa na Upendo

14. Ni vazi la namna gani inatupasa tuendelee kulivaa, na kwa hiyo ni kwa sifa gani lazima watu wa Yehova waonyeshe kwamba wao ni mashahidi wake?

14 Shetani Ibilisi na ulimwengu wake wenye uadui ataendelea kujaribu kuvunja mwungano tulio nao sisi kwa sisi, lakini upendo ambao ndio tunda kubwa zaidi la roho ya Mungu utaendelea kuthibitika kwamba ni mkamilifu katika kuwa ‘kifungo cha mwungano.’ Tunapouvaa “utu mpya,” tunajivika upendo, kama vile mtume Paulo alivyotuambia tufanye, na ni lazima tuendelee kuuvaa ukiwa sehemu ya utu wetu unaoonyesha tuko katika mfano wa Mungu. Alipokuwa akiwapa wanafunzi wake maagizo ya mwisho, Mwana wa Mungu alisema: “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:34, 35) Maneno hayo yalifaa sana kusemwa na Mwana wa Mungu, kwa maana Baba yake wa kimbingu, Yehova, ni mfananishwa wa upendo, na ni lazima sisi tujulishe wanadamu wote kwamba tu mashahidi Wake kikweli kwa kusitawisha tunda la roho Yake, ambalo ni upendo!

15. Katika kuonyesha wanampenda Mungu, ni lazima Mashahidi wa Yehova wapende nani mwingine?

15 Ili tumpende Yehova kwa upendo usio na kigeu-geu, ni lazima tuwapende mashahidi wenzetu. Katika kuthibitisha ukweli wa jambo hilo, andiko la 1 Yohana 4:20, 21 linatukumbusha hivi: “Mtu akisema, Nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona. Na amri hii tumepewa na yeye, ya kwamba yeye ampendaye Mungu, ampende na ndugu yake.”

16. Kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova hawawezi kuacha kupendana, na kwa sababu gani upendo hautang’olewa duniani hata siku moja?

16 Bila kujali kama wao ni sehemu ya wale waliozaliwa kwa roho wakawa warithi wenye ushirika pamoja na Mfalme Yesu Kristo au ni sehemu ya “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” walio na tumaini la kuishi katika Paradiso ya kidunia, Mashahidi wa Yehova wa leo wanapendana kwa unyofu wa moyo kuonyesha wanaifuata kanuni hiyo. Tungewezaje kukosa kuwapenda wale wanaopenda Yehova Mungu na Mwanaye mpendwa Yesu Kristo? Hakika tunawapenda na kwa kufanya hivyo tunafungamanishwa pamoja na kile “kifungo kikamilifu cha mwungano.” Hata Shetani Ibilisi na ulimwengu wake mbovu wajaribu kufanya jambo liwalo lote ili kuliharibu tunda hilo la roho ya Yehova, upendo hautang’olewa duniani hata siku moja. Wale watakaoendelea kujivika upendo mpaka wakati wa kuharibiwa kwa mfumo huu wa mambo ya kiibilisi watalindwa na Mungu wao mshikamanifu waipite “dhiki kubwa” ambayo haijapata kuonekana katika dunia hii. (Mathayo 24:21; Wagalatia 5:22) Kwa njia hiyo ni wale tu wapendao Mungu na jamaa yake, tengenezo lake, watakaookoka waingie katika dunia itakayokuwa imesafishwa igeuzwe iwe Paradiso yenye utukufu. Paradiso hiyo haitafutiliwa mbali hata siku moja bali itakaliwa daima dawamu, iwe na upendezi mwingi wa kuwa na wanadamu walio wafananishwa wa upendo. Upendo utapata ushindi wa milele hata umletee utukufu yule aliye Chemchemi ya kimungu ya upendo, yaani, Yehova Mungu.​—Kutoka The Watchtower, December 15,1982.

Je! Umefahamu?

□ Kwa sababu gani Wakristo wa karne ya kwanza wangeweza kupatana wajapotoka katika hali za malezi yenye kutofautiana?

□ Upendo unakuwa na matokeo gani juu ya vile vikundi viwili vinavyofanyiza “kundi moja” la Wakristo leo?

□ Andiko la Ufunuo 14:6-12 linatimizwaje leo?

□ Ni shirika gani ambalo Mungu ametumia kusaidia watu wake?

□ Kulingana na Wakolosai 3:14, ni lazima upige moyo konde ufanye nini?

[Picha katika ukurasa wa 20]

Chini ya uongozi wa malaika . . .

[Picha katika ukurasa wa 21]

. . . Mashahidi wa Yehova leo wana “Injili ya milele” ya kutangazia watu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki