Matusi—Kweli Yanaumiza?
KATIKA majiji fulani ya United States (Amerika), inakadiriwa kwamba kila neno la tano linalotamkwa ni neno chafu la kutukana mtu. Katika Italia, kulingana na makadirio ya Mwungano wa Kitaifa wa Kupinga Makufuru, makufuru (matukano) zaidi ya bilioni moja yanatamkwa kila siku kuelekea Mungu au kanisa. Kwa kweli, katika mahali pengi watu wanatumia maneno machafu kama njia kubwa ya kupitisha wakati, wanapokuwa wamestarehe bila kujua la kufanya.
Tendo hilo linapasa kushangiliwa, anasema Reinhold Aman, mhariri wa gazeti Maledicta linalohusu mambo ya usemi mchafu. Maoni yake ni kwamba kuchokoza watu kwa maneno kuna faida kwa sababu kufanya hivyo ni afadhali kuliko kumshambulia kwa kumpiga. “Afadhali mimi niitwe [*@*@] badala ya kutiwa risasi au kisu kifuani,” anasema Aman.
Vilevile akitetea maneno mabaya, Chaytor Mason anasema: “Kutumia maneno machafu, kutukana au vyo vyote utakavyoliita jambo hilo, ni njia ambayo imejaribiwa muda mrefu ikaonekana kuwa ni njia nzuri ya kufungulia hasira zilizojaa moyoni kwa sababu ya kuvurugika mawazo.”
Watu wengi zaidi na zaidi wanaendelea kuachilia usemi mchafu kwa kukosa kuujali sana, wakiwa na maoni ya kwamba ni haki kutumia matusi ikiwa hali ya kutoleana matusi imetokea. Kwa kweli, gazeti la wasichana matineja linaloitwa Seventeen linatoa maoni haya: “Mara kwa mara, inapendeza kukusanyika pamoja na wasichana au wavulana—au tuseme mchanganyiko wa wasichana na wavulana—ili kuwe na kipindi cha kuona ni nani anayeweza kushinda wengine wote katika matumizi ya maneno ya kukosa adabu. Ninalowazia ni lile ‘shindano la skatoloji’ (shindano la maneno ya kitakataka) lililofanywa katika orofa ya tatu ya bweni la wanawake ninalosimamia katika chuo kikuu. Maneno mabaya yaliyorushwa-rushwa usiku huo yangaliwezi kumtia aibu hata polisi aliye na ujuzi wa kupambana na ufisadi.”
Je! wewe unakubali kwamba ni haki kutumia usemi mchafu? Je! matusi kweli yanaumiza?
‘Ni ya Kujifurahisha Tu?’
“Shindano la skatoloji” ni nini? Kulingana na kamusi inayoitwa Webster’s New Collegiate Dictionary, neno “scatology” (skatoloji) linaelezwa kuwa hivi: “Uchunguzi wa kusomea mavi; kwa hiyo, uchunguzi wa kusema matusi.” Wewe unafikiri nini juu ya kujaribu kuwashinda wengine kwa kutumia usemi mbovu?
Katika vipindi vya kutupiana maneno ya kutukanana ambavyo vijana wengi leo wanashiriki mara nyingi, kusudi linakuwa ni kutukana mama ya yule mwingine kwa njia ya kushindana ili ionekane ni nani anayeweza kutukana mwenzake kwa njia mbaya zaidi. Wenye kupingana, ambao mara nyingi wanakuwa wawili, wanazungukwa na kikundi cha marafiki wanaocheka wanaposikia mama ya rafiki yao akishushiwa heshima na mpinzani hodari zaidi. Kuna zoea linalofanana na hilo la kumwita mtu majina mabaya sana ya madharau. Ni zoea la kueleza namna sura ya yule mwingine ilivyo, kuifananisha na mnyama fulani wa kuchukiza kama nguruwe, panya au kimnyama chenye harufu mbaya.
Mazoea hayo, pamoja na kusimulia mizaha yenye matusi ili kufurahisha watu, yamekuwa mambo ya kawaida sana. Kwa kuyashiriki, washiriki wanampa mtu wazo la kwamba hali za kukosa adabu si mbaya sana kwa kuwa wao wanaweza kuzifanyia mzaha. Halafu wanasema ya kwamba, ‘Ni watu wengi sana wanaochekeshwa na hali hizo.’ Bila shaka mazoea kama hayo yameshiriki kufanya matusi yawe sehemu ya usemi wa kila siku, hata ikawa kwamba wenye kuitwa “wataalamu” na “wastaarabu” wanayatumia. Lakini, je! inaweza kuwa kwamba kutumia matusi kunaumiza zaidi ya vile watu wengi wanavyodhani?
Matokeo ya Matusi
Matusi yanaletea mdomo matokeo yale yale ambayo picha za umalaya zinaletea jicho. Kutaja maneno ya umalaya kunafanya mtu awazie kuufanya. Kwa hiyo inaweza kuwaje ikiwa maneno yenye kutaja viungo vya uzazi waziwazi yanatumiwa kwa ukawaida? Je! mwenye kuyatumia hataelekea zaidi kufanya mambo anayoyasema? Hakika inastahili kuangaliwa kwamba ongezeko kubwa sana la kutumia matusi limelingana na ongezeko la uasherati, uzinzi na kulalana kwa wanaume na wanaume wenzao.
Kwa sababu hiyo, huenda ukawa unaona hekima ya shauri la Biblia, wakati linaposema hivi: “Lakini uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wala kutamani, kama iwastahilivyo watakatifu; wala aibu wala maneno ya upuzi wala ubishi [utani wa kimatusi, NW]; hayo hayapendezi.”—Waefeso 5:3, 4.
Ukweli ni kwamba, mwenye kutumia usemi wa kimatusi anajichafua mwenyewe. Naye anaeneza hali hiyo ya kuoza iwapate wengine kila wakati anaporudia matusi. Basi, ni kwa sababu nzuri Biblia inashauri hivi: “Lakini sasa yawekeni mbali nanyi haya yote, hasira, na ghadhabu, na uovu, na matukano, na matusi vinywani mwenu.” “Neno lo lote lililo ovu [lililooza] lisitoke vinywani mwenu.” (Wakolosai 3:8; Waefeso 4:29) Vilevile, inahimiza hivi: “Wekeeni mbali uchafu wote.” (Yakobo 1:21) Kutenda kinyume cha shauri hilo kunafanya Mungu achukizwe na mtu.
Pia, fikiria jambo hili: Watu wawili wakitupiana matukano, je! baada ya ubishi wao wanakuwa wameleta maendeleo katika uhusiano wao? Na hata kama hawatapigana kwa sababu ya matukano, je! unaweza kusema watu hao wawili wametatua matatizo yao kikweli? Ni vigumu kusema hivyo! Kwa upande mwingine, si kweli kwamba matukano yenye kusemwa kwa kelele kubwa yanaongezea uwezekano wa kupigana badala ya kupunguza uwezekano huo?
Basi, je! upendo na ufahamiano mzuri unaendelezwaje? Ni kwa kukataa ‘kulipa mtu ovu kwa ovu.’ Neno la Mungu linaamuru likisema, “Msijilipize kisasi.” Bali, “ipisheni ghadhabu” kwa kuacha kisasi katika mikono ya Mungu. Maneno na matendo yako yenye fadhili kuelekea mtu mwenye matusi ‘yatampalia makaa ya moto kichwani pake,’ na labda yamfanye apunguze ukali wa nia yake kukuelekea. Kwa hekima, nyakati zote fuata shauri hili la Kimaandiko lenye mwelekeo mzuri: “Barikini, wala msilaani.”—Warumi 12:17-20, 14.
Epuka Kunaswa Mtegoni
Ni wazi kwamba lazima tujihadhari daima tusivutwe tuambatane na maelekeo ya ulimwengu huu mchafu (najisi). Hakuna ye yote kati yetu asiyeweza kunaswa na minyemeleo yao. Ni kama vile mwandikaji wa kitabu kimoja kinachohusu maneno machafu, Burges Johnson, anavyosema: “Ikiwa usemi mchafu kwa ujumla ni ugonjwa wa kuwa na msamiati mbaya wa maneno, unapitishwaje na ni nani anayeambukiwa nao? Jibu ni jepesi: si kwamba tu huo ni wenye kuenea bali pia ni wenye kuambukia, kwa maana viini vyenye magonjwa vya usemi huo vimekaa ndani sana katika sisi sote.” Biblia inahakikisha kwamba sisi wanadamu wasio wakamilifu tuna maelekeo ya kuvutwa kwenye makosa na ufisadi. Kwa hiyo ni lazima tujitahidi tusitumie usemi wa matusi.—Mwanzo 8:21; Zaburi 51:5.
Kuepuka usemi wa matusi kunaanza na kujifunza namna ya kuzuia mawazo ya moyoni na matendo yanayoutokeza. Hayo ni mawazo na matendo gani? Biblia inajibu hivi “Uchungu wote na ghadhabu na hasira na kelele na matukano yaondoke kwenu.” (Waefeso 4:31) Kwa hiyo kabla hujafikia hatua ya kukasirika sana juu ya mtu fulani hivi kwamba unataka kumtolea maneno machafu, ngoja kidogo na ujilazimishe kukaza fikira zako juu ya mema unayojua juu ya mtu huyo. Usiruhusu hasira ikufanye utumie usemi wa matusi. Jaribu kutii amri hii ya Biblia: “Msiache cho chote kitokee bila ya kuzuiwa katika kinywa chenu.”—1 Samweli 2:3, NW.
Mahali pamoja ambapo unaweza kupata mawazo yanayofaa kwa wingi ni Neno la Mungu, Biblia. Kwa kujaza akili yako kwa mawazo yanayofaa, utakuwa ukikuza tamaa zinazofaa za moyoni. Kufanya hivyo kutakuwa na matokeo gani juu ya usemi wako? Yesu alisema: “Kinywa cha mtu huyanena yaujazayo moyo wake.”—Mathayo 12:34.
Usisite kusali upate usaidizi wa Mungu na kuomba roho yake. Mtunga zaburi alisali hivi: “Ee [Yehova], uweke mlinzi kinywani pangu, mngojezi mlangoni pa midomo yangu.” (Zaburi 141:3) Kwa kukesha kwetu wenyewe tuzuie ulimi wetu, pamoja na kupata msaada wa Mungu, tutaweza kuuepuka mtego wa kutumia usemi mchafu.
[Picha katika ukurasa wa 6]
Je! Wewe utalipa kisasi ukitukanwa na mtu mwingine?