Kizazi cha Matusi
KATIKA kiwanda kilichoko Cleveland, Ohio, U.S.A., ambako Inez alikuwa ameajiriwa kazi, yeye alikuwa ndiye malkia (bingwa) asiyeshindika kwa maneno machafu. Siku moja Alice akagongana na Inez bila kutaka. Mabishano yalitokea naye Alice akamtolea Inez maneno machafu. Wenye kutazama walishangazwa sana na harara hiyo.
Inez akalipa kisasi kwa kutoa mbubujiko wa matusi mengi. Kukawa na kivumbi cha kutupiana maneno machafu yenye kuudhi yaliyotokeza makelele mengi mpaka wafanya kazi wenzao wakaja mbio kushangilia yule waliyempendelea. Kwanza ilionekana kwamba hakuna angeweza kumshinda mwenzake, huku wakizidi kutupiana maneno machafu kwa wingi sana.
Mwishowe Inez akaanza kupata ushindi kwa sababu ya ujuzi wake mkubwa zaidi wa kuchanganya-changanya matusi. Alionekana kuwa asiyeweza kuishiwa na maneno ya matusi, akamshinda Alice kwa kumnyamazisha, naye Alice akaenda polepole zake uso wake ukiwa umebadilika kwa kuudhika. Kelele za kushangilia ushindi wa Inez zilisikiwa huku wafanya kazi akirudia mashine zao. Inez aliiona hiyo kuwa kawaida tu, akaanza tena kazi yake kwa utulivu.
Visa vya namna hiyo vinaonekana mara nyingi leo. Usemi ambao hapo zamani ulikuwa ukisemwa kuwa ni wa watu walio ovyo-ovyo umekuwa kawaida ya watu siku hizi. Sasa ni jambo “linalokubalika” wanawake na hata watoto kutoa maneno machafu. Watoto wanatumia sana usemi ambao hapo zamani walikuwa wakikanywa sana walipoutumia. Na ingawa zamani maneno machafu yalikuwa hayaandikwi wazi katika maandishi, bali yalikuwa yakisimamiwa na alama za mfano wa nyota (**) au na vistari-chali (—,—), sasa yanaandikwa wazi ili msomaji ayasome.
Badiliko la maoni kuelekea matusi linaonekana katika sinema pia. Sasa sinema nyingi zimejawa na mazungumzo ya kukosa adabu na matusi. Watengeneza-sinema wanaingiza ndani maneno ya namna hiyo mara nyingi ili sinema ziingiwe na watu wazima kusudi wapate pesa. Kwa mfano, hapo kwanza ile sinema inayoitwa Annie ilitangazwa kuwa inakubalika ionwe na watazamaji wa umri wote, lakini mwenye kuitokeza akaogopa kwamba tangazo hilo halingevuta watu wote. Kwa hiyo akaingiza katika sinema hiyo maneno machafu.
Ukuzi wa Matusi
Muda wote wa historia maneno machafu yamekuwa yakitumiwa sana. Maneno machafu ni usemi wo wote mchafu. Usemi wa namna hiyo unaonyesha kwamba mtu hana woga wa kuheshimu mambo matakatifu, wala haheshimu Mungu wala mambo yote yanayohusiana na sifa zake na njia zake. Mara nyingi usemi huo unakuwa wa kuomba kiungu fulani ‘kilaani’ mtu fulani. Au huenda kwa kutumia usemi mchafu mtu akachafua na kutukana watu au vitu ambavyo Mungu anaviona kuwa vitakatifu. Hata hivyo Biblia inasema hivi: “Mimi, yule BWANA Mungu wako, nitaadhibu mtu ye yote anayetumia vibaya jina langu.”—Kutoka 20:7, Today’s English Version.
Lakini, katika miaka ya majuzi badiliko kubwa limetukia katika hali ya kutoa maneno machafu. Imekuwa ya kuonyesha wazi mambo ya ngono—matusi—kukazia akili mambo ya siri yanayohusiana na viungo vya uzazi na matumizi yavyo. Ukosefu wa heshima, hata madharau, unaonyeshwa sana kuhusu utakatifu wa ndoa na uzazi. “Kelele za kushangilia michezo ya uanariadha zimebadilika katika karibu hali zote,” linaeleza gazeti U.S. News & World Report, “zikawa matusi yasiyozuilika na yenye kutamkwa wazi kutukana wapinzani wa upande ule mwingine kwa kutaja viungo vya uzazi.”
Matusi hayo yanakuwa na misemo inayohusiana na mambo ya uasherati. Leo hewa imejawa na uchafuzi huo wa usemi. Kulingana na gazeti Time, Tommy Lasorda aliye meneja wa mchezo wa besiboli “aliropoka matusi 144 katika hotuba fupi aliyotolea kikoa chake cha uanamichezo ili kuwasisimua wafanye vizuri zaidi.” Vilevile viongozi wengi wa ulimwengu wa kisiasa wanatumia matusi. Kwa kweli, wakati zile tepe za makao ya urais wa Amerika (“White House”) zilipoachwa zisikike wazi, Richard Nixon alitumia usemi usiofaa ukazoelewa na jamaa nyingi katika nyumba zao. Naye aliyekuwa Rais wa United States (Amerika), Jimmy Carter, alitumia neno linalohusiana na mambo ya ngono ingawa anajulikana kuwa mtu mwenye imani za kidini. Gazeti The New York Times lilikataa kulipiga chapa neno alilolitumia. Lilisema kifupi tu kwamba ulikuwa “usemi wa Kiamerika wa kukosa adabu.”
Huenda watu fulani wakawa wanakumbuka siku ambazo watu wenye kuudhika walikuwa wakitumia maneno kama “pumbavu,” “mshenzi,” “jinga wewe” na “zuzu.” Lakini badala ya maneno hayo, siku hizi matusi yenye kunenwa na kuandikwa yamekuwa jambo la kawaida, nayo yanatuzunguka pande zote. Sasa maneno ya kukosa adabu yenye kueleza tendo la kufanya ngono (kulalana) yanatajwa na watu wengi karibu kila wakati wanaposema jambo fulani. Wanayatumia kuhusiana na karibu mambo yote yanayoweza kuwaziwa. Na si kwamba yanasemwa tu wakati watu wanapokuwa na hasira au uchungu, bali sasa watu wanatumia maneno machafu ya kutukana ili wajisikie tu kwamba wametukana mtu.
Kuanzia kadi za kupelekea watu salamu mpaka kwenye michoro, ni wazi kwamba usemi mchafu sana unatumiwa. T-shati (nguo), matangazo yanayobandikwa ukutani, vibandiko vingi sana na vifungo vya nguo vyenye maneno ya matusi vinaweza kuonekana karibu kila mahali. Usemi wa namna hiyo umekuwa jambo lenye kupendeza watu wengi. Gazeti U. S. News & World Report linasema “watu wengi sana wamekubali matumizi ya maneno machafu mbele ya watu hivi kwamba ingekuwa vigumu kubadili kielelezo hicho hata kama halitakuwa jambo lisilowezekana kufanya hivyo.” Basi si ajabu kwamba kizazi chetu kimeitwa “Kizazi cha matusi’’!
Sababu Ni Nini?
Ukuzi wa matusi unahusiana kabisa na kuharibika kwa jamii zenye kuongoza mapokeo ya watu na kuharibika kwa viwango vya tabia. “Ni ishara ya nyakati,” anasema mnenaji mmoja wa kidini. Kuvunjika kwa mwungano wa jamaa, kukosa kuheshimu wenye mamlaka na ile tabia mpya ya kusema mambo yote yanafaa, hayo yote ndiyo mambo ambayo yamefanya kutokee matusi ya waziwazi yasiyozuiwa, ya kutaja-taja mambo yanayohusu viungo vya uzazi. Usemi wa namna hiyo unaonyesha kwamba ni kawaida ya watu leo kufuata mara nyingi mtindo wa maisha ya ufisadi.
Thomas Cottle, mhadhiri (mhutubiaji) wa mambo yanayohusiana na matatizo ya akilini wa huko Havard, alisema hivi: “Watu wanaona maisha zao kuwa zisizopendeza, zisizoridhisha, nao wana hasira. . . . Uchokozi ndio unaochochea hasira hiyo.” Inadaiwa kwamba kutumia maneno machafu ni njia moja ya kufungulia hasira na mvurugiko uliojaa moyoni. “Ninapoendesha gari katika barabara ya kwenda mbio halafu mtu anikatize upande wa mbele nami nimtolee maneno machafu,” anasema Chaytor Mason, mchunguzi wa matendo yanayofanywa na watu kwa sababu ya hali yao ya akilini, “hiyo inanionyesha kwamba mimi ni bora kuliko yeye, kisha heshima yangu inanirudia.”
Kuna maana fulani ya mambo tunayoona yakitukia wakati watu wanapotukana wengine. Biblia inaonyesha huo ni ushuhuda wa kwamba mwisho wa mfumo mbovu uko karibu. “Lakini ufahamu neno hili,” Biblia inaonya, “ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe . . . wenye kutukana . . . wasingiziaji, wasiojizuia.”—2 Timotheo 3:1-5.
[Sanduku katika ukurasa wa 4]
Michezo ya Video Ambayo Si Watu wa Umri Wote Wanaoruhusiwa Kutazama
Toleo la Agosti 30, 1982 la Advertising Age lilisema kwamba michezo ya video ambayo si watu wa umri wote wanaoruhusiwa kutazama inatengenezwa sasa, kisha likaeleza hivi: “Onyesho la michezo ile mipya, ‘Kikusanyiko cha Waseja,’ ‘Wapige na Uwale’ na ‘Kisasi cha Custer’ linaionyesha kuwa yenye maajabu na mambo mazito kweli kweli. Kwa mfano, katika onyesho la mchezo huu wa mwisho, Jenerali Custer anaonyeshwa akiwa uchi akikimbia apite jangwa linalomzuia ili amfikie na kumchafua msichana wa Kihindi. . . .
“Bw. Kopels, mkuu wa shirika lenye kuchapa gazeti hilo, alisema ingawa onyesho hilo linakazia viungo vya uzazi, likitengenezwa onyesha lisiloonyesha waziwazi viungo vya mwili katika televisheni watu wataacha kupendezwa sana.
“Sinema zenye picha zisizoruhusiwa kutazamwa na watu wa umri wo wote zitakuja hatimaye kuanza kuuzwa na wauzaji wa rejareja wanaouza zile tu zisizo na mambo mazito sana, akatabiri Bw. Kopels.
“Akisema juu ya wafanya biashara wa kaseti za video ambao hapo kwanza walikataa kabisa kuweka katika akiba yao kaseti zenye picha zisizoruhusiwa kutazamwa na watu wa umri wo wote, Bw. Kopels alisema walilazimika kupunguza ugumu wa nia zao ‘kwa sababu wanunuzi walianza kwenda kwenye maduka ya ng’ambo ile nyingine ya barabara ambayo yalikuwa na sinema zile za mambo mazito-mazito. Mimi nafikiri itakuwa hivyo kuhusu picha za kuonyeshea ile michezo, pia.’’’