Maoni ya Biblia
Sababu Inayofanya Lugha Chafu Isiwafae Wakristo
MTAYARISHAJI fulani wa vipindi vya redio vya shirika la utangazaji la BBC katika Wales alikemewa kwa kukataa kuondoa “maneno yenye kuudhi” yaliyosemwa alipomhoji mtu fulani mgoni-jinsia-moja ambaye, kulingana na msemaji fulani wa BBC aliyenukuliwa katika gazeti la habari la The Guardian, alitumia “lugha chafu sana alipokuwa akifafanua matendo ambayo yanaweza kufanya mtu aambukizwe UKIMWI.” Kwa kuongezea, asilimia 22 za programu zilizochunguzwa katika uchunguzi wa majuma mawili uliofanywa katika vituo vinne vya televisheni vya Uingereza zilikuwa na “lugha mbaya, kuapa [kulaani] na/au kufuru.”
Habari hizo zaonyesha tofauti kubwa katika mitazamo ya watu. Kwa watu wengi mazungumzo yenye kujaa uchafu hushtua na kuudhi. Wengine huachilia lugha kama hizo wakiziona kuwa zenye kuvutia na zenye ufidhuli, na kwamba hazipasi kuchukuliwa kwa uzito. Lakini, je, lugha chafu ipatikane katika mazungumzo ya Wakristo, ambao huthamini uhusiano wao na Mungu na vilevile na wanadamu wenzao?
Kwa Nini Lugha Chafu Imeenea Sana?
Lugha chafu ni “zoea lolote la matusi.” Kufuru, kulaani, na kuapa zaingia katika ufafanuzi huo. Lugha chafu huonyesha ghadhabu, na hata shutuma za matukano. Mary Marshall, mtungaji wa kitabu Origins & Meanings of Oaths & Swear Words, asema kwamba “viapo na maneno ya kulaani hutumiwa zaidi katika mazungumzo kuliko katika maandishi.” Lakini, riwaya nyingi hujaa lugha chafu.
Kwa nini lugha chafu imeenea sana? Watu fulani ambao hawana msamiati wa kutosha hutumia sana maneno ya kulaani. Wengine hutumia lugha chafu ili waweke mkazo. Kupatana na ufafanuzi wake, lugha chafu mara nyingi huhusisha hisia za kukasirika, kufadhaika na hasira. Kwa kweli, wanapokabiliwa na majaribu, watu wengi huachilia mifoko ya matusi eti “kutoa . . . hisia walizokandamiza.” Mtafiti Marshall asema kwamba kadi yake ya kupanga maneno ya kulaani ya Kiingereza kwa alfabeti imejaa zaidi chini ya maneno yanayoanza kwa konsonanti zenye mkazo.
Ingawa kulaani kwaweza kuonekana kama kunaondosha hisia zao, wengi hugundua kwamba lugha chafu hutokeza tu lugha chafu. Kwa nini? Lugha chafu huchochea hisia-moyo. Kwa mfano, katikati ya mvurugo wa msongamano mkubwa sana wa magari katika jiji moja kuu katika Afrika Magharibi, dereva mmoja aliyeghadhibika alitoka nje ya gari lake na kumwendea dereva ambaye gari lake lilikuwa limeziba njia. Hasira zilipowaka, matusi yakaenea, kila mmoja akijaribu kumshinda mwenzake. Wenye magari wengine waliokwama walitoa vichwa vyao nje wakiwashangilia watu hao waendelee kutukanana hata zaidi.
Matusi ambayo hushusha hadhi ya mtu yanaweza kutokeza lugha mbaya. Matusi yaweza kuwa maneno yamlinganishayo mtu na mnyama au hata mdudu fulani, maneno ya kushusha hadhi kuhusu wazazi wa mtu na uzaliwa wake wenye kutiliwa shaka, maneno yalengayo kasoro fulani za kimwili, na, yale yawezayo kuudhi hata zaidi, matusi, kufuru, na maneno machafu ya kingono.
Maoni ya Mungu juu ya Lugha Chafu
Kwa hakika, ni kosa zito kutumia vibaya jina la kimungu. Kutoka 20:7 lataarifu: “Usilitaje bure jina la BWANA, Mungu wako.” Lakini, je, kuvunja agizo hilo kulihatarisha uhusiano wa mwabudu huyo na Mungu? Ndiyo; Sheria iliendelea kusema: “BWANA hatamhesabia kuwa hana hatia mtu alitajaye jina lake bure.”
Ili kutoa kielezi cha jinsi ilivyokuwa muhimu kutii amri hiyo, Biblia imerekodi pigano fulani baina ya Mwisraeli na mtu mwingine. Na huyo mtu “akalikufuru hilo Jina, na kuapiza.” Mungu alihukumuje katika kisa hicho? Yeye aliamuru: “Yeye atakayelikufuru jina la BWANA hakika atauawa.” (Mambo ya Walawi 24:10-16) Ingawa kielelezo hicho cha kimaandiko hakiandai mambo mengi juu ya hali hiyo ya kufuru, hata hivyo chafunua maoni ya Mungu juu ya usemi na tabia isiyo na staha.
Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yalitabiri kuhusu siku zetu kwamba “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa . . . wakufuru [Kigiriki, blaʹsphe·moi], . . . na geukia mbali kutoka kwa hawa.” (2 Timotheo 3:1, 2, 5) Neno la Kigiriki bla·sphe·miʹa lamaanisha zaidi ya usemi usio na staha dhidi ya mambo matakatifu. Kwa kweli, maana yake yatia ndani usemi wowote wenye kuumiza na kukashifu ambao humdhuru mtu mwingine.
Watu ambao usemi wao ni wenye matukano hudhihirisha “utu wa zamani” ambao Wakristo wanahimizwa ‘wauvue’ kana kwamba ni koti lenye uvundo ambalo hawawezi kulitumia tena.a Mtume Paulo ashauri: “Yawekeni mbali nanyi hayo, hasira ya kisasi, hasira, ubaya, usemi wenye kuudhi, na maongezi yenye aibu kutoka katika kinywa chenu.” “Acheni uchungu wote wenye nia ya kudhuru na hasira na hasira ya kisasi na kupiga kelele na usemi wenye kuudhi viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote.” (Wakolosai 3:8, 9; Waefeso 4:31) Isitoshe, tafadhali ona kwamba wale ambao hutukana wengine, ambao Paulo anawaita kuwa “watukanaji,” wamo miongoni mwa “watu wasio waadilifu [ambao] hawatarithi ufalme wa Mungu.”—1 Wakorintho 6:9, 10.
Kataa Kutumia Lugha Chafu!
Upendo wa kweli kwa Mungu utamsukuma Mkristo afanye kile ambacho kinampendeza Yeye. (1 Yohana 5:3) Kama vile tu Mungu awahangaikiavyo wanadamu wote, ndivyo na Mkristo ataonyesha hisia kama hizo kwa wengine, hivyo basi akitii amri mbili zilizo kubwa zaidi, yaani, kumpenda Mungu na jirani. (Mathayo 22:37-39) Basi, “acheni kila mmoja wetu ampendeze jirani yake katika lililo jema kwa ajili ya kujengwa kwake.” (Waroma 15:2) Basi jiulize, ‘Je, maneno niyatumiayo ni yenye kuudhi au ni yenye kujenga?’
Ni kweli kwamba si rahisi kwa mtu ambaye amekolea tabia ya kutumia lugha chafu kurekebisha lugha yake iwe safi. Lakini, inawezekana—kwa msaada. Roho ya Mungu yaweza kumsaidia mtu abadili usemi wake. Hata hivyo, ni lazima mtu huyo awe tayari kwanza kujenga msamiati uliojaa maneno mazuri—na kuutumia kwa ukawaida.—Waroma 12:2.
“Ulimi usemao maovu utakomeshwa,” akaonya Mfalme Solomoni mwenye hekima. Basi usiruhusu lugha chafu ichafue usemi wako. Badala ya hivyo, jaribu kuwa mtu ajuaye jambo safi la kusema na ambaye hulisema kwa neema!—Mithali 10:31, 32, Today’s English Version; Wakolosai 4:6.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Waefeso 5:3, 4, ambako muktadha waonyesha kwamba “maongezi ya kipumbavu” na “mwenendo wa aibu” una maana ya kingono. Basi, usemi na mizaha michafu ya kingono haiwafai Wakristo.