Uhuru wa Kweli Chini ya Utawala wa Ufalme
“Viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.”—WARUMI 8:21.
1. Ni nani peke yake anayeweza kuwapa wanadamu mauhuru ambayo wanayahitaji sana, na kwa sababu gani?
WANADAMU wana uhitaji mkubwa sana wa kuwekwa huru watoke katika zile hali nyingi zenye kuwataabisha sana ambazo zimekuwako kwa muda mrefu sana. Lakini, kama historia inavyoonyesha, si jambo lililo katika uwezo wa kibinadamu kuleta mauhuru ya namna hiyo. “Ni mingi mipango iliyo katika moyo wa mwanadamu, lakini shauri la Yehova ndilo litakalosimama.” (Mithali 19:21, NW) Hilo “shauri” la Yehova linaahidi kwamba “atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Hayo ni matazamio yenye kutia moyo kama nini! Lo! jinsi yanavyofaana na masimulizi ya uhuru wa kweli ambao Biblia inasema utaletwa na Yehova: “Viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu”!—Warumi 8:21.
2. Ni chombo gani anachokitumia Yehova kuleta mauhuru hayo?
2 Chombo kitakacholeta mauhuru hayo yaliyo mazuri ajabu ni ile serikali iliyoanzishwa na Yehova itawale dunia nzima, ule Ufalme wa kimbingu wa Mungu. Kupitia huo mapenzi ya Mungu yatatendeka “hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 6:10) Ufalme uo huo ndio karibuni “utavunja falme hizi zote [zilizopo leo] vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.
3. Kwa sababu gani haitupasi kudanganywa na mipango ya kibinadamu ya kutatua matatizo ya ulimwengu huu?
3 Hapana, Mungu hatabadili au kugeuza ulimwengu huu wenye ufisadi. Ulimwengu huu umepita kipimo cha kuweza kupata nafuu. Kwa hiyo mtu ye yote akikuambia kwamba kama tu wanadamu wangefanya jambo hili au lile, hapo ulimwengu ungetatua matatizo yake, usiamini. Badala ya hivyo, Neno la Mungu linaonyesha kikweli kwamba majaribio ya miaka kama 6,000 yaliyoleta huzuni kuu, ya kuona kama mwanadamu anaweza kujitawala bila kutegemea Mungu, yamekwisha kuingia sana katika “siku za mwisho.”—2 Timotheo 3:1-5, 13.
Serikali Moja
4. Ile serikali moja ya Ufalme italetea wanadamu faida gani?
4 Utawala wa Ufalme wa kimbingu wa Mungu utamaanisha kwamba itakuwako serikali moja tu ya kusimamia dunia yote. Msimamizi mkuu atakuwa ni Yesu Kristo, na pamoja naye kitakuwako kikundi kidogo kwa kulinganishwa cha watumishi wengine wa Mungu walio waaminifu, watumikie wakiwa watawala wenzake. Ebu fikiria faida zitakazoletwa duniani na serikali moja, yenye kutawalwa na sheria na kanuni za Mungu! Mipaka yote ambayo sasa inagawanya mataifa katika visehemu-visehemu vyenye ukatili itaanguka. Watu wataungana wawe jamaa moja kubwa ya kibinadamu, yenye uhuru wa kutembea-tembea kote kote duniani bila kipingamizi. Hakutakuwa tena na vyeti vya paspoti za kuingia nchi nyingine au viza, wala hakutakuwa na walinzi wa mipaka.—2:9, 10; Ufunuo 14:4; 20:6.
5. Uhitaji wa kuwa na serikali moja tu kwa dunia yote umekubaliwaje?
5 Kwa muda mrefu watu wengine wameutambua uhitaji wa kuwa na serikali moja. Katika kichapisho cha Philippines, Bulletin Today, Gwynne Dyer aliye mwandikaji wa habari anaeleza hivi: “A. J, P. Taylor, mmoja wa wanahistoria mashuhuri wa kizazi chetu, aliniambia majuzi kwamba anaamini tumaini la pekee la kuepuka vita ya ulimwengu yenye maangamizi makuu ambayo yangemaliza ustaarabu ni kuwa na mtu wa kuunda ufalme mmoja wa ulimwengu mzima. . . . Kwa njia fulani lazima tuiache hali yetu ya sasa ya kuishi katika mataifa mbali mbali [zaidi ya 150] yenye enzi za utawala—yote yakiwa yamelundika silaha kweli kweli, na yote yakiwa na uwezekano wa kuangamizwa—kisha tuwe na mamlaka moja tu ya ulimwengu mzima . . . Na lazima tufanye hivyo haraka. Ile hali dhaifu sana na yenye kugawanyika-gawanyika daima ya Umoja wa Mataifa ni kipimo cha kuonyesha tunapaswa kufanya jitihada nyingi sana. . . . Ule msemo uliokuwako katika miaka ya 1950 ungali unafaa: kusipoweza kuwa na ulimwengu mmoja, basi kusiwe na wo wote.”
6. Ule Ufalme utakuwa ni usimamizi wa namna gani?
6 Kutakuwako ulimwengu mmoja, chini ya serikali moja ya Mungu. Itakuwa baraka iliyoje kuwa na usimamizi utakaoshughulikia kila mtu kwa fadhili, haki na bila upendeleo! Ikisema juu ya Mfalme, Yesu Kristo, Biblia inasema hivi kwa unabii: “Kwa uadilifu lazima yeye ahukumu wale wa hali ya chini, na kwa unyofu lazima yeye atoe karipio kwa ajili ya wale wapole wa dunia.” (Isaya 11:3, 4, NW) Ndiyo, Kristo atafanya yaliyo haki. Alithibitisha hilo alipokuwa duniani, kwa maana alitetea hali ya wenye kugandamizwa, wala hakushughulikia matajiri na wenye vyeo, ingawa hata wao hakuwabagua. Basi, akiwako msimamizi hodari kama huyo, ambaye amethibitisha anafaa na mwenye kufanya kazi chini ya mwelekezo wa Yehova, “ukweli wenyewe utachipuka kutoka kwenye dunia yenyewe, na uadilifu wenyewe utatazama chini ukiwa kwenye mbingu zenyewe.”—Zaburi 85:11, 12, NW.
Amani ya Kweli na Ufanisi
7. Wale watakaohifadhiwa hai waingie katika Taratibu Mpya watakuwa wamekwisha kufanya nini?
7 Itakuwa baraka iliyoje kwa kutokuishi tena chini ya utawala uliogawanyika wa kibinadamu wenye kuhudumia majeshi makubwa yenye silaha na kufanya vita daima! Mali za asili za dunia hazitaharibiwa tena. Bali, mali hizo zitatumiwa kwa makusudi ya amani, yenye kujenga. Kwa kweli, wale ambao Mungu atawahifadhi hai kuupita mwisha unaokuja wa mfumo wa mambo ya sasa watakuwa wamekwisha kutimiza unabii wa Mika 4:3: “Nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” Ni nani kati ya makundi yote ya watu wa dunia ambao tayari wanatimiza unabii huo? Matukio ya historia ya kisasa yanaonyesha ni Mashahidi wa Yehova. Wao ni ushuhuda ulio hai wa kwamba amani ya duniani pote chini ya utawala wa Mungu itakuwako kikweli kwa sababu amani ya duniani pote tayari iko kati yao sasa!
8, 9. Chini ya utawala wa Ufalme amani na ufanisi ni mambo yatakayopatikana kwa kiasi gani?
8 Katika taratibu mpya ya Mungu amani itapanuliwa ifikie kila sehemu ya dunia. Isaya 32:17, 18 inataja “unyamavu na usalama mpaka wakati usiojulikana,” kisha inaongezea: “Watu wangu lazima wakae katika mahali pa kukaa penye amani na katika makao ya uhakika kamili na katika mahali-mahali pa kupumzikia pasiposumbuliwa.” (NW) Ebu wazia kuwa na amani nyingi sana hivi kwamba hutalazimika hata kutia kufuli kwenye milango yako, na kwamba utaweza kutembea ko kote, wakati wo wote wa mchana au usiku, bila kuogopa waoteaji au wenye kuingilia wanawake kwa nguvu! Basi Biblia ina sababu nzuri inaposema hivi: “Watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:11.
9 Ufanisi utaambatana na amani hiyo, badala ya mamilioni ya watu kuuawa na utapiamlo (kukosa chakula kinachofaa) kama inavyotukia kila mwaka. Kwa kuwa Yesu alikuwa na uwezo wa kulisha maelfu ya watu kwa kuzidisha kimwujiza mikate michache na samaki wachache tu, chini ya usimamizi wake wa Ufalme ataweza kuwaongoza wanadamu watimize Zaburi 72:16: “Kutapata kuwako wingi wa nafaka juu ya dunia; juu ya kilele cha milima kutakuwa na mfuriko.” (NW) Na kwa kuwa Ufalme wa Mungu utaondoa kabisa vizuizi vyote vya kisiasa, na pia pupa ya kibiashara na mashindano yenye kuleta hasara, mazao tele ya dunia yatamiminika kwa wingi kwa faida ya wanadamu wote, si wachache tu. Basi itatokomea daima dawamu ile hali ya kuona watoto wenye vikono na viguu vyembamba, na vitumbo vilivyofura kwa sababu ya njaa.
Kazi Yenye Matunda Iliyo ya Kufurahika
10. Kazi katika Taratibu Mpya itatofautianaje na ile ya leo?
10 Leo, watu wengi wana huzuni kwa sababu ya namna ya kazi wanayolazimika kufanya wajipatie riziki. Mamilioni mengi ya wengine hawana kazi yo yote, hawakuajiriwa. Lakini katika Taratibu Mpya ya Mungu watu watapata raha nyingi sana katika kazi. Nao hawatakuwa katika hatari ya kuona jitihada zao zikiwa za bure tu kwa sababu ya kuharibiwa na hali mbaya za uchumi, au na maafa fulani au vita. “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine . . . Wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda siku nyingi. Hawatajitaabisha kwa kazi bure.”—Isaya 65:21-23.
11. Raia za Ufalme wa Mungu watatimiza nini kuelekea dunia hii na uhai ulio juu yayo?
11 Kukiwa na hali kama hizo za kazi yenye kuinua moyo, na watu wakiwa na upendo halisi kuelekea jirani, ili kuleta hali bora ya dunia hii na maisha yaliyo juu yake raia za Ufalme watatimiza mambo yaliyo mazuri ajabu mara elfu kuliko jambo lo lote ambalo limepata kuonekana na ulimwengu huu. Hiyo ndiyo sababu Yesu angeweza kuonyesha kwamba Paradiso ingekuja. (Luka 23:43, ZSB) Ni kama vile Isaya anavyotabiri: “Jangwa litaimba na kupiga kelele kwa shangwe; lita-kuwa na uzuri wa kuonekana kama Milima ya Lebanoni na lenye rutuba kama mashamba ya Karmeli na Sharoni. . . . Vijito vya maji vitatiririka kupita jangwani; ule mchanga wenye kuchoma utakuwa ziwa la maji, na nchi kavu itajawa na mabubujiko. . . . Watakuwa wenye furaha milele, milele watakuwa huru bila huzuni na kihoro.”—Isaya 35:2, 6, 7, 10, Today’s English Version.
Hakuna Tena Magonjwa na Kifo
12. Yesu alionyeshaje mpango mkubwa wa kuponya watu ambao atatekeleza akiwa katika mamlaka ya Ufalme?
12 Walakini, lingekuwa jambo lenye kuudhi sana kuwa na vitu vyote hivyo kisha uvipoteze kwa sababu ya kuwa mgonjwa, kuzeeka na kufa. Lakini, mambo ambayo madaktari na wanasayansi hawawezi kufanya sasa, Mungu atayafanya chini ya utawala wake wa Ufalme. Mungu ndiye aliyeumba mwili wa mtu, akili yake na maoni ya moyoni. Yeye anajua ni kitu gani kitamfanya apone, awe mkamilifu. Yesu aliuonyesha uwezo wa kuponya aliopewa na Mungu naye atautumia katika Taratibu Mpya: “Wakamwendea makutano mengi wakimletea viwete, vipofu, mabubu, vilema na wengine wengi, wakawaweka miguuni pake; akawaponya; hata ule mkutano wakastaajabu, walipowaona mabubu wanasema, vilema wanakuwa wazima, viwete wanakwenda, na vipofu wanaona.” (Mathayo 15:30, 31) Tena, wanadamu wakiisha kuinuliwa wafikie ukamilifu wa kibinadamu chini ya utawala wa Ufalme, mauti itamezwa milele.’ (Isaya 25:8) Upendo wa Yehova utanyoka uwafikie hata wale waliokufa zamani za kale kwa maana wao watapata nafasi ya kuishi katika Taratibu Mpya ya Mungu kwa kufufuliwa wawe hai. Ndipo ufufuo huo wenye kufurahisha utakaporudiwa-rudiwa mara zisizohesabika. Hiyo itakumbusha watu juu ya wakati ambao Yesu alifufua kisichana, kisha wenye kushuhudia jambo hilo “wakashangaa mshangao mkuu.”—Marko 5:41, 42; Yohana 5:28, 29.
13. Watu wataweza kuchagua kufanya mambo gani katika Taratibu Mpya?
13 Ebu fikiria ni mambo mengi namna gani ungeweza kufanya katika Taratibu Mpya yenye amani na ufanisi ukiwa na akili na mwili mkamilifu—tena bila kufa! Ebu yafikirie mambo yale mengi ambayo umekuwa ukitaka kuyafanya lakini ukakosa wakati na pesa! Ebu fikiria kuipeleleza milima yenye kuvuta macho na kuifurahia, kupitia misitu yenye kuburudisha, mashamba yenye maua mazuri na pia bustani mbalimbali, wanyama wenye kusisimua maono, vijito vyenye kumeremeta kwa maji safi na maziwa-maji yasiyo na uchafu, vyakula vitamu-vitamu vya nchi nyingi. Yafikirie majaliwa ambayo wanaume na wanawake watakuza katika ufundi, uchoraji wa ramani za nyumba, kusitawisha na kutunza wanja ili zipendeze macho, kupamba-pamba nyumba, uchoraji-picha na muziki. Bila shaka, wanadamu watachochewa wafikie vilele vipya vya usemi na upendezi. Fikiria pia kufahamiana vizuri zaidi na Yule mwenye kuyawezesha yote hayo, Yehova Mungu. Maarifa yenye kuongezeka kuhusu ulimwengu wote alioufanya ukiwa wa kustaajabisha sana, wenye magalaksi ya nyota, nyota moja moja na sayari mbalimbali, yatasisimua pia. Ndiyo, ni kweli kwamba “viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.”—Warumi 8:21.
Kuikubali Ile Kweli
14. Kwa sababu gani tunaweza kuwa na tumaini hakika kabisa katika ahadi zote za Yehova?
14 Je! unaweza kweli kuziamini ahadi zote hizo za Mungu? Ndiyo, unaweza. Unaweza kujisikia kama Yoshua mcha-Mungu aliposema hivi: “Halikuwapungukia ninyi hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena [Yehova], Mungu wenu, katika habari zenu; yote yametimia kwenu, hapana neno lo lote mlilopungukiwa.” (Yoshua 23:14) Ndiyo, unaweza kuangika (kutegemeza) uhai wako juu ya ahadi za Mungu kwa sababu anayosema ni kweli na pasipo shaka yatatimia.—Isaya 46:9-11.
15. Watumishi wa Mungu wanakataa maoni gani ya ulimwengu huu?
15 Biblia inaonyesha wazi kwamba kweli iko, na inaeleza kweli hiyo ni nini, iko wapi na ni nani walio nayo. Ulizo kwa kila mmoja wetu ndilo hili: Je! wewe unaitaka ile kweli, kuitaka kabisa kabisa? ‘Kwani watu walio wengi hawaitaki kweli?’ huenda wengine wakauliza? Hapana, kwa maana Yesu alisema njia ya kwenda kwenye uzima wa milele ni nyembamba na, kwa kulinganishwa, ni wachache walio katika njia hiyo. (Mathayo 7:13, 14) Wanadamu walio wengi zaidi wana maoni yanayoelezwa na Biblia kwenye Ayubu 21:14-16: “[Wanamwambia] Mungu, Tuondokee; kwani hatutaki kuzijua njia zako. Huyo Mwenyezi ni nani, hata tumtumikie? Nasi tutafaidiwa nini tukimwomba?” Lakini Ayubu anasema, “Mashauri ya waovu na yawe mbali nami.” Njia yao ya kufikiri haitegemei kweli bali inategemea uongo wa Shetani kwamba wanadamu watafanikiwa zaidi wasipomtegemea Mungu.
16. Kwa sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kwamba mtu ye yote anayetaka ile kweli kwa moyo mweupe ataipata?
16 Mtu ye yote ambaye kwa unyofu wa moyo anaitaka ile kweli, na anayemwomba Mungu amsaidie kuipata, hakika ataongozwa ilipo. Tena si kitu anaishi wapi au hali zake ni nini. Kwa sababu gani? Kwa sababu ingawa Yehova anatumia watumishi wake waaminifu duniani kuzihubiri habari njema za Ufalme kabla ya mwisho kuja, kazi ya kuwatafuta wapendao kweli si kazi ya kibinadamu tu. Mfalme wa kimbingu Yesu Kristo na halaiki za majeshi yake ya kimbingu yenye nguvu nyingi wanauunga mkono ujumbe unaosambaa ulimwenguni kote ukizidi daima kupata nguvu.—Mathayo 25:31, 32; Ufunuo 14:6, 7.
17. Ikiwa mtu anataka ile kweli kabisa, ni lazima afanye nini?
17 Mfumo mzima wa mambo unakaribia kwisha. Ikiwa wewe unaitaka ile kweli kabisa na unataka kabisa kuendelea kuishi unahitaji kumwonyesha Mungu hivyo na hata wanadamu. Twaa maarifa ya kulijua Neno la Mungu. Kusanyika pamoja na watu wake. ‘Basi, endelea kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake yeye.’—Mathayo 6:33, NW; Yohana 17:3; Waebrania 10:24, 25.
18. Ni faida gani zinazovunwa hata sasa na wale wanaoishi kwa kuifuata ile kweli?
18 Unapofanya hivyo, utaanza kupata faida nyingi hata sasa. Wale wanaojifunza ile kweli na kubaki ndani yake wanapata uhuru mkubwa wa akilini na moyoni, kwa kuwa wanajua sababu ya nyakati hizi kuwa mbaya sana, na wanajua mambo ya wakati ujao. Wanawekwa huru pia na njia ya maisha ya ubatili ya watu katika ulimwengu huu, ambao wanafuatia sana faida za kimwili tu, lakini waje kuzipoteza zote wakati mfumo huu umalizikapo, (1 Yohana 2:15-17) Kisha wanapata kitulizo kingi kwa kuwekwa huru watoke kwenye makosa ya kidini.
19. Wewe utafanya nini ikiwa unaipenda ile kweli?
19 Je! wewe unaipenda ile kweli kabisa? Ikiwa ndivyo, utampenda Mungu mwenye kweli. Utazipenda kweli za ajabu anazofunua sasa juu ya utawala wake wa Ufalme. Utalipenda tengenezo lake lionekanalo duniani, la watu anaowakusanya pamoja sasa ili wapate wokovu. (Isaya 2:2-4) Nawe hutaruhusu kitu kiwacho chote katika mbingu au duniani kikukomeshe kumtumikia kwa uaminifu yule Mungu mwenye kweli anayeweza kukuweka huru kwa kweli yake.—Yohana 8:31, 32.—Kutoka w4/15/83.
Je! wewe unaweza kujibu maulizo haya?
□ Yehova atawaleteaje wanadamu uhuru wa kweli?
□ Serikali moja ya ulimwengu wote italetea watu faida gani?
□ Kuna ushuhuda gani ulio hai wa kuonyesha kwamba hakika kutakuwa na amani ya kweli chini ya utawala wa Ufalme?
□ Kutakuwa na tofauti gani kati ya kazi katika mfumo huu na ile itakayokuwa katika Taratibu Mpya?
□ Kwa sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kwamba wenye kuitafuta kweli kwa moyo mweupe wataongozwa ilipo?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Wale watakaookoka mwisho wa mfumo huu watakuwa wamekwisha ‘kufua panga zao zikawa majembe’
[Picha katika ukurasa wa 17]
Katika Taratibu Mpya ya Mungu, watu wataona raha kubwa katika hali za kufanyia kazi zenye kuinua moyo