Kutazama Ufunuo kwa Njia ya Uchunguzi
KAMA ungekuwa ukipanga orodha ya vitu vinavyoweza kukufurahisha, je! wewe ungepanga kitabu cha Biblia cha Ufunuo katika orodha yako?
Inaelekea kuwa kwamba watu walio wengi wasingefanya hivyo. Hata hivyo kila mtu aliye na ufahamu wa kadiri wa kitabu cha Ufunuo anaweza kukubaliana na maneno ya mtume Yohana katika mwanzo wa kitabu hicho: “Heri asomaye na wao wayasikiao maneno ya unabii huu, na kuyashika yaliyoandikwa humo.”—Ufunuo 1:3.
‘Lakini,’ huenda ukasema, ‘ni vigumu sana kufahamu ninayosoma katika Ufunuo.’ Sababu moja ni kwamba sehemu kubwa ya kitabu hicho iko katika usemi wa mfano. Ili kuelewa maana, tunahitaji maarifa ya kuijua Biblia kwa ujumla na pia ya kujua matendo ya kushughulika kwa Mungu na watu wake muda wa miaka iliyopita.
Huenda ukawa umepata kipingamizi kingine katika kuelewa Ufunuo. Kwa kuwa kitabu hicho kina njozi au picha nyingi za maelezo tofauti-tofauti, watu wengi wana maelekeo ya kutokufahamu yanayomaanishwa kwa ujumla. Kwa usemi wa mfano, wao wanaelekeza fikira kwenye miti mmoja mmoja na kushindwa kupiga hatua ya kurudi nyuma waangalie namna msitu wote kwa ujumla ulivyo. Kwa kufikiria jambo hilo, tuchungue kitabu cha Ufunuo kwa njia inayoonyesha namna sehemu au njozi zacho mbalimbali zinavyohusiana. Kwa kutoa kifano kidogo, angalia kwamba mfuatano mmoja wa mambo, kama zile muhuri saba, unaelekeza ndani ya mfululizo mwingine, zile tarumbeta (baragumu) saba. Picha iliyo katika ukurasa wa 21 itakusaidia. Tunapoendelea kutazama, tutaongeza maelezo machache tu ya kufasiri, kwa kuwa mengi zaidi yanapatikana katika vitabu vilivyotajwa hapa chinia
Kufunua Kunaanza
Kitabu cha Ufunuo kimeandikwa kwa namna ya barua, nacho kiliandikwa karibu na mwaka wa 96 W.K., na mtume Yohana kwa “makundi saba” katika Asia Ndogo, hayo yakiwa yanawakilisha kundi lote la Wakristo waliopakwa mafuta kwa roho. (1:4, NW) Utangulizi (1:1-3) unatambulisha kwamba Mungu ndiye chanzo cha Ufunuo na Yesu ndiye kipitio cha kuutoa. Unahakikisha kwamba wale wanaosikia na kushika maneno ya unabii watapata furaha (heri).
Baada ya kumtaja Yehova na Yesu, mtume anaeleza yeye mwenyewe ni nani kisha anaonyesha kwamba yanayofuata yanahusu hasa “siku ya Bwana” (tangu mwaka wa 1914). Yeye anaona njozi ya sura yenye utukufu ya Yesu mfufuliwa, ambaye kupitia kwake kitabu hicho kilipokezwa Yohana. Barua zitaandikwa kwa makundi saba. (1:4–3:22) Kwa kuijua hali ya kiroho ya Wakristo wanaohusika, Yesu anatoa sifa, mashauri na onyo. Jambo hilo linapasa kutupa sisi uhakikisho wa kwamba Mungu amekuwa akiwapa mazoezi wale watakaokuwa mbinguni wakiwa wafalme wa kutawala dunia.
Akiisha kuona Yule aliye kipitio cha kutolea ufunuo, ndipo sasa Yohana anapata njozi ya Mtoaji wa ufunuo wenyewe. (4:1-11) Mungu ni mtukufu na mwenye uwezo wa kuogopesha sana, naye anastahili tumheshimu sana na kumwabudu. Kando-kando ya kiti cha enzi cha Mungu wako viumbe hai wanaokazia sifa zake. Wazee 24 (Wakristo wanaotawala mbinguni) wanamwabudu Muumba na hata kukubali kwamba viumbe wote wanapaswa kufanya ivyo hivyo. Yehova ana kitabu cha kukunjwa kilichotiwa muhuri, lakini nani aweza kukifungua?—5:1-4.
Yohana anamwona Mwana-Kondoo, Yesu, akichukua kitabu cha kukunjwa hicho. Sura ya 5 inaeleza kwamba Kristo anastahili utukuzo huo. Kwa hiyo inatupasa sisi tumhesabie yeye utukuzo na kutaka kuujua ujumbe wa kitabu cha kukunjwa unaohusu kusudi la Mungu linalotendeka katika mbingu na dunia katika siku zetu. Badala ya kukisoma tu kitabu cha kukunjwa hicho bila kuona matukio yo yote, Yohana anaona vituko. Kristo anaanza kufungua muhuri saba za kitabu hicho.
Muhuri ya kwanza inamfunua Yesu kuwa mtawala wa kifalme akienda zake kwenye ushindi wa mwisho. Muhuri za pili mpaka nne zinatumia wapanda farasi wengine kuonyesha vita kubwa isivyo kawaida, njaa kubwa na kifo kisicho cha kawaida (kama vile ambavyo tumeona tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza) ambacho kilipeleka halaiki kubwa ya watu kwenye Hadesi, kaburi. Muhuri ya tano inapovunjwa, uhakikisho unatolewa kwamba Mungu atawalipizia kisasi Wakristo wenye kuteswa na kuuawa kwa ajili ya imani. Anachoona Yohana wakati muhuri ya sita inapofunguliwa kinaonyesha kwamba kutakuwako mabadiliko ya kimbingu na kidunia na kwamba wanadamu watatafuta maficho wasipatwe na hasira kali ya Mungu inayokuja.–6:1-17.
Wakati wa kipindi cha katikati kabla ya muhuri ya saba kufunguliwa, Yohana anaona kazi ambayo lazima ifanywe kabla Mungu hajaruhusu tufani ya dhiki kuja. (7:1-17) Kukamilishwa kwa kazi ya kuwatia muhuri wale 144,000 ni lazima kutukie. (Baadaye [14:1-3], kunaonyeshwa kuwa kumekamilishwa.) Kuzuia kwa malaika dhiki hiyo yenye uharibifu kunaruhusu “mkutano mkubwa” upate kibali ya Mungu na kumwabudu yeye pamoja na wale 144,000. Sasa muhuri ya saba inavunjwa kisha kunakuwa na kipindi kifupi cha sala na matayarisho kwa ajili ya mambo yatakayokuja.—8:1-6.
Tarumbeta Saba
Malaika saba watapiga tarumbeta (baragumu) saba. (Watumishi wa kidunia wa Mungu walianza kutoa ujumbe mbalimbali wa hukumu kwenye makusanyiko yao katika miaka ya 1922-1928). Kwa hiyo, katika kufungua mfululizo wa muhuri saba, ile ya mwisho inapanuka kwa kutoa njozi ya mambo mengine saba, yaani, tarumbeta. Ujumbe wa namna tano ulio kama tarumbeta ambao unahusu visehemu vya tengenezo la Shetani unatangazwa. Ule wa tano unahusu wahubiri walio kama nzige; pia unasemwa kuwa ndio wa kwanza kati ya ule ole wa namna tatu. Wakati tarumbeta ya sita inapolilishwa, inasemwa kwamba wale waliofungwa huko Eufrate watafunguliwa, huko ambako Babuloni wa kale ulikuwa. (Katika nyakati za kisasa. Wakristo fulani walifunguliwa kutoka utumwa wa Kibabuloni baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza.) Njozi hiyo inaonyesha pia jeshi la askari-wapanda-farasi 200,000-000.—8:7–9:21.
Kunakuwa na kukatizwa kwa tarumbeta (baragumu) ya sita; Yohana anaona malaika akiwa na kitabu cha kukunjwa kidogo ambacho kinaweza kuliwa. (10:1-11) Mtume anapata kujua kwamba katika siku za kulilishwa kwa tarumbeta ya saba fumbo la Mungu litakuwa limemalizika. Kisha anapata kitabu cha kukunjwa hicho akile na kuambiwa habari ya kazi nyingine itakayofanywa ya kutoa unabii. Ni lazima yeye apime pia hekalu (la kiroho). Yohana anaambiwa juu ya mashahidi waliotoa unabii kwa muda (1914-1918), kisha wakauawa na mnyama-mwitu na mwishowe wakafufuliwa. Angalia kwamba mnyama-mwitu fulani anatajwa lakini bado haijaelezwa maana yake ni nini. Kusimama kwa wale mashahidi wawe hai kunatangulia tetemeko la ardhi katika Yerusalemu wenye kuasi imani, na hapo mwisho unakuja wa ile tarumbeta ya sita na ole wa pili.—11:1-14.
Tarumbeta ya saba inapolilishwa tangazo linatolewa juu ya Ufalme uliosimamishwa (ule “ole wa tatu” kwa adui za Mungu). Jambo hilo linatokeza mateso yenye hasira kali kutoka kwa mataifa. (11:15-19) Sura inayofuata inaeleza kwa ukamili zaidi kile kilichotukia. Yohana anaona mwanamke mwenye utukufu (tengenezo la Mungu la kimbingu) akizaa mtoto wa kiume (ule Ufalme) kwa usalama kujapokuwako upinzani wa Ibilisi. Baada ya vita mbinguni, Shetani anatupwa kwenye dunia, ambapo anatesea mabaki Wakristo kwa sababu ya uaminifu wao. (12-1 17) Jambo hilo linatoa onyo juu ya yule adui mkuu zaidi, Shetani. Lakini adui wengine wanaonekana. Mmoja ni mnyama (tengenezo la kisiasa la Ibilisi lililo la kinyama) kutoka baharini. Anafanya vita na Wakristo, ambao kwa sababu hiyo wanahitaji uvumilivu na imani. (13:1-10) Mnyama mwingine, mwenye pembe mbili, anayetia watu moyo waabudu sanamu ya yule mnyama wa baharini, kwa kufaa anafananisha mwungano wa kisiasa wa tawala zenye nguvu za Uingereza na Amerika ambazo zimekuwa na mamlaka nyingi ulimwenguni katika nyakati za karibuni. –13:11-18.
Je! adui wote hao watazuia kutiwa muhuri kwa wale 144,000? Hapana! Yohana anawaona wale 144,000 wakiimba kwa furaha juu ya Mlima Sayuni. (Yote hayo bado yanatukia wakati wa ile tarumbeta ya saba.) Halafu malaika watatu hasa wanajulisha kwamba huko mbele kutakuwa na matata kwa adui wale. Malaika mmoja anatangaza kwamba Mungu atafikiliza hukumu. Kwa hiyo, anaamuru hivi: “Mcheni Mungu, na kumtukuza.” Wa pili anatangaza kwamba Babeli (Babuloni) Mkuu ameanguka. Wa tatu anaahidi kutakuwa na kuteswa-teswa kwa waabudu wa yule mnyama au wa sanamu yake. Malaika wengine wanatabiri tendo la kuvuna kisha wanatangaza maangamizi kwenye Har–Magedoni.—14:1-20.
Mabakuli (Vitasa) Saba na Babeli Mkuu
Baada ya hukumu hizo na matangazo ya mwanzo-mwanzo, Yohana anaona malaika saba wakiwa na mapigo saba. (Hilo pia linatukia baada ya kulilishwa kwa tarumbeta ya saba; kwa hiyo, tena, mfululizo mmoja unaelekeza ndani ya ule unaofuata.) Kujapokuwa na mateso, wengi wanatokea wakiwa wameshinda na kuimba sifa. Malaika wale saba watamimina mabakuli saba ya hasira, ambayo yanaonyesha maoni ya Mungu juu ya hali mbalimbali za ulimwengu na matokeo ya maoni yake ya hukumu. Kama vile ilivyokuwa kuhusu tarumbeta ya sita, bakuli la sita linahusu Mto Eufrate (Babuloni). Inatajwa pia juu ya kukusanywa kwa watu kwenye “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” (Har–Magedoni), lakini bado maelezo marefu hayajatolewa. Bakuli la saba linapomiminwa sauti inasema, “Imekwisha kuwa”! Kisha Babeli Mkuu anatikiswa mpaka anavunjika-vunjika na kubomoka.—15:–16:21.
Ndipo Ufunuo unapoeleza uharibifu wa Babeli (Babuloni) wa kisasa, na hiyo inakumbusha kwamba Babuloni wa kale ulikuwa chemchemi ya dini ya uongo. Babeli katika Ufunuo unafananishwa na kahaba anayeendesha mnyama wa rangi nyekundu sana ambaye ana vichwa saba vinavyowakilisha wafalme—mfalme wa nane anatokana na wale saba waliotangulia. (Kwa kufaa sana anafananisha Ushirika wa Mataifa, ambao nafasi yao baadaye ilichukuliwa na Umoja wa Mataifa—na mashirika yote hayo mawili yamefanyizwa na mataifa mengi.) Malaika anasema kwamba baadaye pembe za kijeshi za mnyama zitapigana na Mwana-Kondoo. Lakini kwanza pembe 10 hizo zitamgeuka yule kahaba na kumharibu. (17:1-18) Watu mmoja mmoja wanahimizwa watoke katika Babeli Mkuu wa kidini kabla ya tukio hilo. Baada ya yeye kuharibiwa, wafalme na wafanya biashara wanajisikia wakimkosa, lakini mbingu zinashangilia uharibifu wake kamili na wa mwisho. (18:1-24) Mungu anapaswa kusifiwa kwa sababu ya kufikiliza hukumu hiyo. Jambo hilo linaleta furaha kubwa hasa kwa bibi-arusi wa Mwana-Kondoo ambaye ni “watakatifu.” Bibi-arusi huyo anafurahi kwa sababu amekuwa ndiye mshindi juu ya kahaba huyo.—19:1-10.
Sasa habari ya vita ya Mungu na wale wanaopigana na Mwana-Kondoo inatajwa tena na kuelezwa kwa urefu. Matengenezo yenye upinzani na watu mmoja mmoja wanakuja kwenye mwisho wao. (19:11-21) Namna gani juu ya roho wabaya? Hatua inayofuata ni kwamba Shetani anatupwa ndani ya shimo lisilo na mwisho kwa miaka elfu moja. Kwa kipindi hicho Kristo na wale 144,000 watakuwa wafalme na makuhani katika maana ya pekee. Ikiruka upesi na kufikia mwisho wa miaka elfu moja ili kuonyesha mwisho kamili wa Shetani, ile njozi inaonyesha kufunguliwa kwake na uasi wa wanadamu fulani. (20:1-10) Ikirudi nyuma kueleza matukio ya wakati wa Mileani, njozi inaonyesha wafu wakiwa wamefufuliwa na wakihukumiwa kuwa wanastahili uzima wa milele au uharibifu.—20:11-15.
Kwa kuwa mbingu za kale na dunia ya kale zimekimbia, Yohana anaona mbingu mpya na dunia mpya, na vilevile baraka zinazoletwa nazo kwa wanadamu. Pia anaona mji, si Babeli, bali bibi-arusi wa Kristo. Ni mji mtakatifu na mkamilifu, wenye mto wa uzima unaotiririka kutoka huo. Maandalizi mengi yanafanywa kwa ajili ya uzima wenye afya. Mfululizo wa njozi za Ufunuo unakaribia kumalizika kwa wonyesho huo mtukufu na wenye kutazamisha wa tengenezo linalosimamia mfumo mpya wa mambo.—21:1–22:7.
Yohana anasisimuka kabisa moyoni na anataka kuabudu wakili aliyempokeza njozi hiyo; lakini anakaripiwa. Unabii huo haupasi kutiwa muhuri. Wenye kuusikia wanapaswa kukaribisha wengine watwae “maji ya uzima bure.” Hakuna mtu anayepaswa kuongeza wala kuondoa kitu kwenye kitabu cha kukunjwa. Kwa mara nyingine Yesu anakumbusha wasomaji kwamba yeye anakuja upesi. Yohana anaitika na kumalizia kwa kuwatakia heri watakatifu.—22:8-21.
Ukitazama orodha ile iliyoambatanishwa na habari hii, je! sasa wewe unaweza kusema kwamba una ufahamu mzuri zaidi juu ya mambo yaliyo katika Ufunuo na namna visehemu vyao vinavyounganishwa pamoja? Ingawa hivyo, mengi zaidi yanahitajiwa. Inatupasa kujifunza na kufahamu kwa ukamili maana ya mfano ya njozi zilizo katika kitabu hicho kilichoongozwa na Mungu, kisha tutumie ujumbe wacho kuhusu maisha yetu wenyewe. Hapo ndipo tutakapoelekea kupata mibaraka, kutia ndani furaha (heri) ile ambayo Yohana aliitaja katika mistari ya mwanzo-mwanzo.
[Maelezo ya Chini]
a Mashahidi wa Yehova wanapata msaada mkubwa katika vitabu viwili vya kusaidia kujifunza Biblia ambavyo vinazungumza Ufunuo mstari kwa mstari, yaani, “Babylon the Great Has Fallen!” God’s Kingdom Rules’. (1963) na “Then Is Finished the Mystery of God” (1969). Vyote viwili vinapatikana kwa wachapishaji wa gazeti hili.
[Picha katika ukurasa wa 21]
Kufunguliwa kwa muhuri saba kunaelekeza kwenye kulilishwa kwa tarumbeta saba
Wakati tarumbeta tatu za mwisho zinapoendelea kulilishwa, ole wa namna mbalimbali unatangazwa. Ole wa tatu unaelekeza kwenye mfululizo wa mabakuli saba
Malaika saba wanamimina mabakuli ya hasira ya Mungu, mapigo saba juu ya dunia