Kazi Tukufu Inayofuata Uendeshaji wa Wapanda-Farasi
1. Inaonekanaje wazi kwamba Majira ya Mataifa ya kukanyaga-kanyaga kile kilichowakilishwa na mji wa Yerusalemu yalimalizika mwaka wa 1914?
MFALME wa wafalme na Bwana wa mabwana,’ Yesu Kristo, yupo sasa. (Ufunuo 19:11, 16) Tuna “ishara” ya kutuonyesha hivyo. Yeye amekuwa katika Ufalme wake aliopewa na Mungu tangu mwisho wa “majira ya Mataifa” mwaka wa 1914, miaka 69 iliyopita. (Luka 21:24) wakati huo ndipo kulimalizika kukanyagwa-kanyagwa kwa Ufalme wa Yehova Mungu uliokuwa umewakilishwa wakati mmoja na ufalme wa Israeli katika Yerusalemu ukiwa katika ukoo wa kifalme wa Mfalme Daudi. Huko katika Mashariki ya Kati mji wa Yerusalemu hauna mfalme wa ukoo wa Daudi bali huo ni mji mkuu wa Jamhuri ya Israeli, yenye waziri mkuu Myahudi. Lakini namna gani juu ya “Yerusalemu wa mbinguni”? (Waebrania 12:22) Mji huo uko kule juu katika milki yenye nguvu zipitazo za kibinadamu na za Mataifa. Mtawala wa milki hiyo ni “Mwana wa Daudi,” Yesu Kristo. Anatawala akiwa ‘Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana’ tangu yalipomalizika Majira ya Mataifa mwaka wa 1914. Mataifa yasiyo ya Kiyahudi yanaweza kuupinga Ufalme na wenye kuutangaza hapa duniani, lakini hayawezi kuugusa Ufalme wenyewe. Hayawezi kuutawala, kama ulivyotawalwa wakati mmoja na zile serikali tano kubwa-kubwa za ulimwengu katika historia, yaani Babuloni, Mwungano wa Umedi na Uajemi, Ugiriki, Roma na serikali ya ulimwengu ya Mwungano wa Waingereza na Waamerika wa United States.—Ufunuo 21:1, 2.
2. Kwa kujibu ulizo la ile ambayo ingekuwa ishara ya kuwapo kwake na ya umalizio wa mfumo wa mambo, Yesu alisema maneno gani yanayolingana na yale yaliyo katika njozi ya Ufunuo 6:1-8?
2 Njozi aliyopewa mtume Yohana, inayoonyeshwa kwenye Ufunuo 6:1-8, inaonyesha kwa njia ya unabii jambo ambalo lingeufuata mwanzo wa uendeshaji wa ‘Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana’ akiwa juu ya farasi mweupe wa mfano akielekea kwenye pigano la kukata maneno kabisa kwenye uwanja wa Har–Magedoni. Yanayoonyeshwa na njozi hiyo yanalingana na maneno ambayo Yesu Kristo mwenyewe aliwaambia wanafunzi wake akijibu ulizo lao hili: “Mambo hayo yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo [Kigiriki, parousía] kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3, NW) Kwa habari ya “utungu” ambao ungeionyesha “ishara” ya kuwapo kwake, [au parousía] na ya “umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alisema: “Kwa maana taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; kutakuwa na matetemeko ya nchi mahali mahali; kutakuwako na njaa; hayo ndiyo mwanzo wa utungu [wenye kuonyesha kuzaliwa kwa mfumo mpya wa mambo].” (Marko 13:8) “Kisha aliwaambia, Taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; kutakuwa na matetemeko makubwa ya nchi; na njaa na tauni mahali mahali; na mambo ya kutisha na ishara kuu kutoka mbinguni.”—Luka 21:10, 11; Mathayo 24:7, 8.
YULE FARASI MWEKUNDU SANA
3. Mwanzo wa kuwapo kwa Kristo ungeonyeshwaje, na kwa hiyo njozi ya kufunguliwa kwa muhuri ya pili inaonyesha nini?
3 Kwa hiyo mwanzo wa “kuwapo” kwa Kristo, au parousía, tangu kumalizika kwa Majira ya Mataifa mwaka wa 1914 haungekuwa na amani wala mbinguni wala duniani. Njozi aliyopewa Yohana kwenye Ufunuo sura ya 6 inahakikisha jambo hilo. Basi, je! kufunguliwa kwa muhuri ya pili kungetufunulia nini? Tunatazama pamoja na mtume Yohana tuone ni kitu gani: “Na alipoifungua muhuri ya pili, nikamsikia yule mwenye uhai wa pili akisema, Njoo! Akatoka farasi mwingine, mwekundu sana, na yeye aliyempanda alipewa kuiondoa amani katika nchi, ili watu wauane, naye akapewa upanga mkubwa.”—Ufunuo 6:3, 4.
4. Tukio hilo la mfano lilionyesha nini, na kwa sababu gani?
4 Tukio hilo la mfano lilifananisha nini? Si jambo jingine ila kutokea kwa vita, tena duniani pote, kwa sababu mwendeshaji wa huyo farasi mwekundu sana alipaswa “kuiondoa amani katika nchi.”
5. Je! hiyo inamaanisha kwamba mwendeshaji wa yule farasi mweupe ndiye aliyetokeza kwa ghafula vita ya ulimwengu, na Ufunuo 12 unaonyesha ni nini kingefuata mwanzo wa utawala wake?
5 Kwa kuwa huyo farasi mwekundu sana na mwendeshaji wake mwenye kunuka vita alimfuata mwendeshaji aliyempanda farasi mweupe, je! hiyo ina maana ya kwamba mpanda-farasi wa kwanza alianzisha Vita ya Ulimwengu ya Kwanza baada ya yeye kutawazwa kisherehe mwaka wa 1914 na hivyo akaanza kutumia “uta” wake? Hata kidogo! Ufunuo sura ya 12 unaonyesha kile ambacho kingeufuata uzaliwa wa Ufalme wa yule mpanda-farasi wa kwanza katika mwaka wa 1914. Kungetokea vita isiyoonekana, ya kutumia nguvu zipitazo zile za kibinadamu. “Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka; yule joka akapigana nao na malaika zake, nao hawakushinda, wala pahali pao hapakuonekana tena mbinguni. Yule joka akatupwa, yule mukubwa, nyoka ya zamani anayeitwa Diabolo, na Shetani, anayedanganya dunia yote; akatupwa hata dunia, na malaika zake wakatupwa pamoja naye. Nikasikia sauti kubwa katika mbingu ikisema: Sasa kumekuwa wokovu, na nguvu, na ufalme wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake; kwa maana ametupwa chini mushitaki wa ndugu zetu, yeye anayewashitaki mbele ya Mungu wetu, muchana na usiku. . . . Kwa sababu hii, furahini mbingu, nanyi munaokaa ndani. Ole wao wanaokaa kwa dunia na bahari! Kwani yule Diabolo ameshuka kwenu mwenye gazabu nyingi kwa sababu anajua ana wakati mufupi tu.”—Mistari 7-12, ZSB.
6. Kwa hiyo, zile sehemu mbalimbali zinazohusu mpanda-farasi wa pili zinafananisha nini?
6 Masimulizi hayo yanaweka lawama juu ya Ibilisi na mashetani wake kwa sababu ya vita ya ulimwengu ya kwanza iliyochukua maisha za kibinadamu zaidi ya milioni 8 kuanzia Julai 28, 1914. Mwendeshaji wa farasi wa pili wa mfano alifananisha makundi ya kijeshi ya ulimwengu, ambayo Shetani ndiye “mungu” wao; na yule farasi mwenye rangi nyekundu sana alilingana na hasira kali-kali na hali ya vita hiyo na ya ile nyingine iliyoitokeza, yaani, Vita ya Ulimwengu ya Pili. Ule “upanga mkubwa” wa askari-mpanda-farasi ulipewa kwa mwendeshaji huyo wa kijeshi, autumie kukata-kata majeruhi wake. Ukubwa wa silaha hiyo ya vita ungeonyesha pia ukubwa wa namna ya vita ambayo sasa ilianzishwa duniani pote, vita ya kutumia silaha zote, vita ya ulimwenguni pote. Kabla ya hapo hakukuwa na nyingine kama hiyo! Vitabu vya historia vinapatikana katika maktaba mbalimbali ikiwa tunataka kuelezwa kirefu habari za Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na ya Pili! Kwa uhakika vita ya ulimwenguni pote ililipuka mwishoni mwa Majira ya Mataifa mwaka wa 1914.—Luka 21:24
7. Ili kulingana na Ufunuo 6:1-8, ni nini kilichoanza kutokea mwaka wa 1914 kuonyesha ulinganifu pamoja na maneno ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi wake juu ya ishara ya kuwapo kwake?
7 Mwenye kumpa mtume Yohana ishara za Ufunuo sura ya 6 ndiye yule yule aliyewapa mitume wake, kutia na Yohana, habari za kujibu ulizo lao hili, huko nyuma mwaka wa 33 W.K.: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Kwa kuwa mfuatano wa matukio aliyotaja huko nyuma muda mfupi tu kabla ya kifo chake unapatana na mfuatano wa matukio anayoonyesha kwenye Ufunuo sura ya 6, hiyo inaonyesha kwamba maono yaliyopangwa katika sura ya sita yanaonyesha kwamba mwisho wa Majira ya Mataifa katika mwaka wa 1914 na kutokea kwa ghafula kwa vita ya ulimwenguni pote ulionyesha mwanzo wa “kuwapo” kwake katika Ufalme wake wa kimbingu na mwanzo wa “umalizio wa mfumo wa mambo.” Kama alivyotabiri Yesu kwenye Mathayo 24:7, 8 na Luka 21:11, kweli taifa liliinuka juu ya taifa na ufalme juu ya ufalme, kuonyesha kwamba alikuwa ameanza “kuwapo” kwake kusikoonekana au kuelekeza fikira zake kwenye mambo ya dunia kwa kuwa sasa ilikuwa imekuwa eneo la Ufalme wake uliosimamishwa karibuni. Lakini namna gani juu ya “njaa” na “tauni mahali mahali”? Mambo hayo pia yalitangulia kuonwa kutokana na uendeshaji wa wale wapanda-farasi wanne wanaoelezwa kwenye Ufunuo 6:1-8.
YULE FARASI MWEUSI
8. Ni nini zilizokuwa sehemu za njozi iliyofuata kufunguliwa kwa muhuri ya tatu?
8 Baada ya uendeshaji wa aliyempanda farasi mwenye rangi nyekundu sana, njozi inatuonyesha nini? “Na alipoifungua muhuri ya tatu, nikamsikia yule wa tatu mwenye uhai akisema, Njoo! Nikaona, na tazama, farasi mweusi, na yeye aliyempanda ana mizani mkononi mwake. Nikasikia kama sauti katikati ya hao wenye uhai wanne, ikisema, Kibaba cha ngano kwa nusu rupia, na vibaba vitatu vya shayiri kwa nusu rupia, wala usiyadhuru mafuta wala divai.”—Ufunuo 6:5, 6.
9. Sehemu za njozi hiyo zinaonyesha nini waziwazi, na kwa sababu gani rangi ya yule farasi ilifaa kuwa nyeusi?
9 Ni wazi kwamba maneno hayo yanaonyesha kungekuwa na upungufu wa vyakula, uchache wa viliwavyo. Na je! sivyo ilivyotukia wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza “mahali mahali”? Kwa kuwaondoa wakulima katika mashamba na bustani zao ili wakaandikwe katika majeshi ya vita yenye mamilioni ya watu, je! si kweli kwamba njaa ingetawala maeneo mengi sana, kuwe na chakula haba au hata kusiwe na cho chote cha kumaliza njaa hiyo? Ndivyo! Si ajabu basi kwamba mamilioni ya wanadamu waliuawa na njaa. Bei za vyakula zilipanda mno mpaka watu wasiohesabika wakaumizwa sana na njaa kwa kushindwa kuvinunua. Nayo thamani ya pesa ilishuka ajabu gani! Ebu fikiri, mshahara wa mchana kutwa, “nusu rupia” (“dinari moja,” NW), ukimalizika kwa kununua kibaba kimoja tu cha ngano! Jamani! mshahara wa mchana kutwa umalizike kwa kununua vibaba vitatu tu vya kile chakula cha hali ya chini cha shayiri, chakula cha kila siku cha maskini wa pesa. Ni ajabu gani! Wale waliotajirika kupitia shughuli za kuendesha vita na kutengeneza silaha za kivita waliweza kununua mafuta na divai yo yote iliyopatikana sokoni. Kwa hiyo, kwa watu hao “mafuta [ya mzeituni, NW] wala divai” hayakuharibishwa. Mishahara mikubwa-mikubwa ingeweza kushindana nguvu na bei kubwa-kubwa! Yote hayo yanaonyesha kulikuwa na huzuni kubwa kuhusiana na vita ya duniani pote iliyowaondoa wanaume wengi kwenye shughuli zenye mazao, kama ukulima, waingie katika matendo ya uharibifu. Basi hakuna sababu ya kushangaa kwamba farasi aliyembeba mwendeshaji yule mwenye kitu cha kupimia watu chakula kidogo-kidogo kwa bei za juu sana alikuwa wa rangi nyeusi! Masikitisho! farasi mtia-huzuni tu, mleta-njaa yenye kuua!
YULE FARASI WA KIJIVUJIVU
10. Shahidi wa tatu alitokezwaje katika njozi ya Yohana ili kuhakikisha mwanzo wa kuwapo kwa mwendeshaji wa yule farasi mweupe?
10 Wapandaji wa farasi mwenye rangi nyekundu sana na farasi mweusi walikuwa mashahidi wawili wa kuhakikisha kwamba Mfalme Yesu Kristo alikuwa amevikwa taji na kuanza uendeshaji wake wenye ushindi kuupita “umalizio wa mfumo wa mambo” mpaka kwenye mwisho wao katika Har–Magedoni. Lakini, kuna shahidi wa tatu wa jambo hilo. Amesimamishwa kwenye jukwaa la kutolea ushahidi ili tumsikilize. Miaka zaidi ya 60 kabla ya Yohana kupewa njozi hii, mwendeshaji aliyevikwa taji aliyempanda yule farasi mweupe alikuwa amesema, “Kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno lithibitike.” (Mathayo 18:16) Basi, namna gani juu ya huyo shahidi wa tatu? Yeye si mwendeshaji anayefananisha kitu chenye kutukia ndani ya dunia, matetemeko ya ardhi; anafananisha kitu kilichoupiga uso wa dunia kwa nguvu nyingi mpaka watu milioni 20 wakafa katika mwaka wa 1918 kufika wa 1919 mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Haya basi, ewe shahidi Namba 3 ingia: “Na alipoifungua muhuri ya nne, nikasikia sauti ya yule mwenye uhai wa nne akisema, Njoo! Nikaona, na tazama, farasi wa rangi ya kijivujivu, na yeye aliyempanda jina lake ni Mauti, na Kuzimu [Hadesi, NW] akafuatana naye. Nao wakapewa mamlaka juu ya robo ya nchi, waue kwa upanga na kwa njaa na kwa tauni na kwa hayawani wa nchi.”—Ufunuo 6:7, 8.
11. Kwa sababu gani rangi ya huyu farasi wa nne ilifaa kuwa ya kijivujivu, na aliyempanda anafananisha kifo (mauti) cha namna gani mapema ili awaweke tayari watu wa kuingia Hadesi?
11 Farasi akiwa na rangi ya kijivujivu angeonekana kuwa mnyama mgonjwa- mgonjwa, na Mauti lingekuwa jina linalomfaa anayemwendesha. Hapa mauti inayomaanishwa ingekuwa ni mauti iliyoharakishwa, si mauti inayopata wanadamu katika uzee. Ni mauti inayomtia mtu katika Hadesi, lile kaburi, mapema mno. Namna gani hivyo? Kwa sababu ni mauti ambayo mtu anatupiwa bila kuikaribisha na ule “upanga mkubwa” wa vita vibaya sana, na upungufu wa chakula unaoleta njaa kubwa sana au na “tauni” (ugonjwa wa kipuku, NW), ugonjwa wenye kuambukia watu wengi katika eneo kubwa linalokaliwa, kisha unakomesha haraka-haraka uhai wa watu wengi. Na je! si kweli kwamba “ile fluu,” ile homa kali sana ya Kispania, iliyoupiga ulimwengu mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilifikia kiwango hicho? Ndivyo hakika! Nayo Hadesi ilifungua kinywa chayo chenye njaa ikameza watu wanaokadiriwa kuwa milioni 20. Homa hiyo haikuletwa na Mungu, lakini Mungu aliruhusu itukie. Bila kuruka mipaka ingeweza kusemwa kuhusu Mauti na Kuzimu (Hadesi) kwamba ‘walipewa mamlaka [ruhusa] juu ya robo ya nchi.’ Mungu hakuingilia jambo hilo alikatize bali aliyaacha mambo hayo yenye kuua yalete uharibifu mkubwa katika dunia hii iliyokuwa ikiwaka vita, ingawa vitu hivyo vilichukua uhai wa wengine kati ya waaminifu wake. Habari za kifo chenye kuletwa na “hayawani” (wanyama-mwitu) wenye kunyemelea wanadamu hoi hazielezwi.
12. Uendeshaji wenye uharibifu wa wapanda-farasi hao watatu wa mwisho-mwisho unahakikisha nini kwa sababu ya kutukia wakati ulipotukia?
12 Uendeshaji wenye maangamizi makubwa wa hao mashahidi watatu, yaani, mwendeshaji wa yule farasi mwekundu sana, mwendeshaji wa yule farasi mweusi na mwendeshaji wa yule farasi wa kijivujivu akiwa amefuatwa karibu-karibu sana na Hadesi, hauwezi kusahaulishwa wala kufutwa katika historia ya zamani hizi. Kwa kuwa yalitukia kwa namna yalivyotukia mwishoni mwa Majira ya Mataifa mwaka wa 1914, bila shaka yanamaanisha kitu fulani cha maana ulimwenguni pote. Kitu gani? Ule Ufalme, ambao wanafunzi walifunzwa kumwomba Mungu katika Sala ya Bwana, ulisimamishwa katika mbingu, kwa kuwa sasa muda wa Majira ya Mataifa wa kukanyaga-kanyaga Ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Masihi wake ulikuwa umekwisha. (Luka 21:10, 11, 24) Kwa hiyo sasa Ufalme ndio huu. Mfalme wao amekwisha kupakwa mafuta awe Mtawala aliyetawazwa na Mungu na akavikwa taji. “Kuwapo” kwake katika Ufalme kumeanza. “Umalizio wa mfumo wa mambo” umeanza. Yehova amepeleka fimbo ya kifalme ya nguvu zake kutoka Sayuni wa kimbingu, akisema: “Nenda uwe ukishinda katikati ya adui zako.” (Zaburi 110:1, 2, NW) Kwa hiyo wakati ulikuwa umefika wa Mtawala huyo kuanza uendeshaji wake akiwa juu ya farasi wake mweupe wa kifalme, akienda mbio akapate ushindi wa mwisho ulio kamili juu ya maadui wake duniani na mbinguni pia.
Pendeleo Lenye Kuheshimika
13. Wanafunzi wa mwendeshaji wa yule farasi mweupe wanapaswa kuchukua hatua gani kwa sababu ya habari hizi, na ni pendeleo gani la utumishi lililotabiriwa wanalopaswa kuliona kuwa ni heshima kwao kuwa nalo?
13 Wakiwa mbele ya hao wapanda-farasi wanne wanaoonyeshwa kwenye Ufunuo 6:1-8, wanafunzi wa yule mwendeshaji wa farasi mweupe wanapaswa kufanya nini hapa duniani wakati wa huu “umalizio wa mfumo wa mambo”? Inawapasa watumikie kwa mwungano wakiwa wanenaji wake kwa kutimiza sehemu ya maana sana ya ile “ishara” ya kuwapo kwake katika Ufalme, yaani, “Na habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14, NW) Ni lazima ushahidi huo wa duniani pote utolewe na ‘wahubiri’ wake na kumalizwa kabla ya “mwisho” kamili ya huu “mfumo wa mambo” uliohukumiwa maangamizi. Kwa kuwa sasa miaka 69 imepita tangu yule mwendeshaji aliyevikwa taji aanze kuendesha farasi mweupe ili akajipatie ushindi kamili juu ya wapinzani wa Ufalme wake, na kwa kuwa hali za ulimwengu za sasa zimezidi kuwa mbaya kama zilivyo, bila shaka huo “mwisho” kamili uko karibu sana. “Wakati mufupi” ambao Shetani Ibilisi ameruhusiwa kuwa nao hapa duniani ni kama umekwisha. (Ufunuo 12:12) Basi, ni nani watakaolikubali lile pendeleo lenye kuheshimika la kuitoa ile sehemu ya mwisho ya ushahidi wa duniani pote kuhusu Ufalme wa Mungu uliosimamishwa ukiwa mikononi mwa Kristo? Mashahidi wa Yehova walioungana duniani pote wanajibu wakisema, “Sisi tutalikubali!” Yehova na awasaidie kufanya hivyo, ili malawama yaondolewe juu yake akiwa ndiye Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote!
14. Kwa sababu gani ni lazima mwendeshaji aliye juu ya yule farasi mweupe aendelee tu kumwendesha?
14 Uendeshaji wa yule mwendeshaji aliyevikwa taji aliye juu ya farasi mweupe haujafikia hatua ile yenye shangwe ya ‘kumaliza ushindi wake,’ naye hatashindwa kamwe kufikia mradi huo. Kwa hiyo ni lazima azidi kuendesha. Vita vya ulimwengu viwili tayari vimetokea na kupita, lakini matayarisho ya vita vyenye ukubwa wa kutisha yangali yakiitikisa amani ya wanadamu.
15. (a) Je! kuendeshwa kwa yule farasi mweusi na yule wa kijivujivu kumemalizika? (b) Kwa sababu gani mambo ambayo yamekuwa yakitimia tangu mwaka wa 1914 yanasisimua na ni matukufu?
15 Mamilioni ya watu wasiopata chakula cha kuwatosha wanalazimika kukaza mishipi yao ili kujiondolea maumivu makali ya njaa, wakingojea bure tu upungufu wa vyakula uweze kushindwa nguvu na bei zilizopanda zishuke ziwe za kiasi ili maskini waweze kujipatia mahitaji ya lazima. Sayansi ya dawa imevurugwa akili na namna mpya za magonjwa. Magonjwa yenye kuumiza sana yanajifungilia kwenye watu wengi zaidi na zaidi bila kuwaacha, kuonyesha kwamba mwendeshaji anayeitwa Mauti hajamsimamisha farasi wake wa kijivujivu, hivi kwamba ni lazima Hadesi ya ukaaji wa kaburini iifuate Mauti karibu-karibu sana. Lakini yote hayo ambayo yametukia tangu mwisho wa Majira ya Mataifa katika mwaka wa 1914 yamekuwa na maana ya kusisimua, ndiyo, yenye utukufu! Katika tarehe hii ambayo muda umepita sana, tunachokikaribia ni mwisho wa “umalizio wa mfumo wa mambo” ambao umetokea tangu Gharika ya siku za Noa, mwaka wa 2370 K.W.K., au miaka 4,352 iliyopita. Kwa kweli hizo ni habari njema.
Kazi Tukufu Inafuata
16. Je! hiyo inamaanisha au haimaanishi mwisho wa dunia yetu inayokaliwa na watu?
16 Mwisho wa huu “umalizio wa mfumo wa mambo” haumaanishi mwisho wa makao haya ya kidunia ya wanadamu. Hata kidogo! Unamaanisha kuanza kwa mfumo mpya wa mambo, ndiyo, wa kufaidi dunia ii hii ya kale ambayo wanadamu wenye dhambi wanatisha kuiharibu iwe utupu. Muumba mwenye kiti cha enzi anasema hivi: “Tazama, nayafanya yote kuwa mapya.”—Ufunuo 21:5.
17. Ni pendeleo gani la kazi ambalo sasa ni heshima kwetu kulitimiza mpaka ndani ya mfumo mpya wa mambo?
17 Hakika ni kazi tukufu sana iliyoko mbele ya wale watakaouokoka mwisho wa huu “umalizio wa mfumo wa mambo” wauingie ule mfumo mpya ambamo yule farasi mwekundu sana, yule farasi mweusi na yule farasi wa kijivujivu mwenye kufuatwa na Hadesi hawatapiga shoti (mbio) tena katika sehemu zote za dunia itakayokaliwa na watu—hasa sana kwa sababu ufufuo wa wanadamu wote waliokombolewa utakuwa hapo hapo karibu! Lakini hata sasa, kabla ya uendeshaji wa wale wapanda-farasi wanne kumalizika, ina utukufu kazi ya Mashahidi wa Yehova ya kuzitangaza habari njema zipitazo zote kwa ubora. Ni habari za serikali ya kifalme ya Yehova iliyo mikononi mwa Kristo itakayoleta upendezi katika mfumo mpya wa mambo, kuwe na Paradiso itakayoizunguka dunia nzima na kuijaza wanadamu waliokombolewa wenye kuendeleza amani, waliobarikiwa kwa kupewa uzima wa milele katika ukamilifu wa kibinadamu kuonyesha wana mfano na sura ya Mungu. (Mwanzo 1:26-28) Letu sasa ndilo pendeleo lenye kuheshimika ambalo Mungu ametupa tuishiriki kazi hiyo tukufu!—Kutoka w5/15/83.
Ni sehemu gani zinazohusiana za “ishara” yenye mambo mengi zinazoelezwa kwenye
Ni pendeleo gani ambalo Mashahidi wa Yehova wanafurahia sasa, na wana tazamio la kuwa na kazi gani huko mbele?