Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • re sura 16 kur. 89-99
  • Wana-Farasi Wanne Katika Mwendo!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wana-Farasi Wanne Katika Mwendo!
  • Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Farasi Mweupe na Mpandaji Wake Mashuhuri
  • Kutoka Kwenda Akishinda
  • Ona, Farasi wa Rangi-Moto!
  • Farasi Mweusi Aruka Kuja Mbele
  • Farasi Rangi Nyeupe-Nyeupe na Mpandaji Wake
  • Kazi Tukufu Inayofuata Uendeshaji wa Wapanda-Farasi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Mpanda Farasi wa Ufalme Aendelea
    “Ufalme Wako Uje”
  • Wapanda Farasi Wanne​—Jinsi Wanavyokuhusu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2017
  • Wapanda Farasi wa Kitabu cha Ufunuo—Jinsi Unavyopatwa na Matokeo ya Upandaji Wao
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
Pata Habari Zaidi
Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
re sura 16 kur. 89-99

Sura ya 16

Wana-Farasi Wanne Katika Mwendo!

Njozi ya 3—Ufunuo 6:1-17

Habari: Upandaji wa wana-farasi wanne, mashahidi wafia imani walio chinichini ya madhabahu, na siku kubwa ya hasira-jeuri

Wakati wa utimizo: Kuanzia 1914 kufikia uharibifu wa huu mfumo wa mambo

1. Yehova anaonyeshaje Yohana vilivyomo ndani ya hati-kunjo yenye kuvutia ambayo Yesu anafungua?

KATIKA siku hii yenye hatari, je! sisi hatupendezwi sana na “vitu ambavyo lazima vitukie karibuni”? Hakika tunapendezwa, kwa kuwa sisi wenyewe tunahusika! Basi acheni sisi tuandamane na Yohana wakati Yesu anapofungua hati-kunjo yenye kuvutia. Kwa kustaajabisha, Yohana halazimiki kusoma. Kwa nini sivyo? Kwa sababu vitu vilivyomo vinatolewa kwake “kwa ishara” kwa mfululizo wa mandhari zenye nguvu-msukumo, na zinazojaa matendo.—Ufunuo 1:1, 10, NW.

2. (a) Yohana anaona na kusikia nini, na kuonekana kwa kerubi kunadokeza nini? (b) Amri ya huyo kerubi wa kwanza inatolewa kwa nani, na sababu gani wewe unajibu hivyo?

2 Msikilize Yohana wakati Yesu anapofungua kifungo cha kwanza cha hati-kunjo: “Na mimi nikaona wakati Mwana-Kondoo alipofungua mmoja wa vile vifungo saba, na mimi nikasikia mmoja wa wale viumbe hai wanne akisema kwa sauti kama ya ngurumo: ‘Njoo!’” (Ufunuo 6:1, NW) Hii ni sauti ya kerubi wa kwanza. Kuonekana kwake kama simba kungemdokezea Yohana kwamba tengenezo la Yehova litatenda kwa ujasiri katika kutekeleza hukumu Zake za uadilifu. Nayo amri hiyo inatolewa kwa nani? Hangeweza kuwa Yohana, kwa kuwa Yohana alikuwa amekwisha kualikwa ashiriki mandhari hizi za kiunabii. (Ufunuo 4:1) Hiyo “sauti ya ngurumo” inawaita wajitokeze washiriki wengine katika wa kwanza wa ule mfululizo wa vituko vinne vyenye kuamsha.

Farasi Mweupe na Mpandaji Wake Mashuhuri

3. (a) Sasa Yohana anaeleza nini? (b) Kupatana na mifananisho ya Biblia, ni lazima huyo farasi mweupe atoe picha ya nini?

3 Yohana, na pamoja naye ile jamii ya Yohana na waandamani wayo leo, wanapendelewa kuona drama yenye mwendo wa kasi sana! Yohana anasema hivi: “Na mimi nikaona, na, tazama! farasi mweupe; na mmoja aliyeketi juu yake alikuwa na upinde; na taji lilipewa kwa yeye, na yeye akatoka kwenda akishinda na kukamilisha ushindi wake.” (Ufunuo 6:2, NW) Ndiyo, katika kujibu sauti yenye mngurumo “Njoo!” farasi mweupe atokea. Katika Biblia, mara nyingi farasi hufananisha vita. (Zaburi 20:7; Mithali 21:31; Isaya 31:1) Farasi huyu, yaelekea ni farasi dume mwenye sura nzuri, anameta kwa weupe unaoonyesha utakatifu usio na ila. (Linga Ufunuo 1:14; 4:4; 7:9; 20:11.) Hiyo inafaa kama nini, kwa kuwa inaonyesha vita iliyo safi na ya uadilifu machoni pa Yehova!—Ona pia Ufunuo 19:11, 14.

4. Ni nani aliye Mpandaji-farasi mweupe? Eleza.

4 Ni nani aliye Mpandaji-farasi huyu? Yeye ana upinde, silaha ya vita ya kushambulia, lakini anapewa pia taji. Wale waadilifu pekee wanaoonekana wakivaa taji katika pindi ya ile siku ya Bwana ni Yesu na ile jamii inayowakilishwa na wale wazee 24. (Danieli 7:13, 14, 27; Luka 1:31-33; Ufunuo 4:4, 10; 14:14)a Haielekei kwamba mshiriki wa kile kikundi cha wazee 24 angeonyeshwa kuwa akipokea taji kwa ustahili wake mwenyewe. Kwa sababu hiyo, huyu mpanda-farasi aliye pekee lazima awe Yesu Kristo na si mwingine. Yohana anamwona katika mbingu wakati ule wa kihistoria wenye maana kubwa katika 1914 wakati Yehova anapotangaza “Mimi, hata mimi, nimeweka mfalme wangu,” na kumwambia kwamba hili ni kwa kusudi la “kwamba mimi nipate kukupa mataifa yawe urithi wako.” (Zaburi 2:6-8, NW)b Hivyo, katika kufungua kile kifungo cha kwanza Yesu anafunua jinsi yeye mwenyewe, akiwa Mfalme ambaye amevikwa taji sasa hivi, anatoka kwenda kupiga vita katika wakati wa Mungu uliowekwa.

5. Mwandikaji wa zaburi anaelezaje habari ya Mpandaji katika njia inayofanana na Ufunuo 6:2?

5 Mandhari hii inapatana vizuri na Zaburi 45:4-7, NW, inayoelekezwa kwa Mfalme aliyeketishwa na Yehova juu ya kiti cha ufalme: “Na katika umaridadi wako songa mbele ukapate fanikio; panda kwa sababu ya ukweli na unyenyekevu na uadilifu, na mkono wa kulia wako utakufunza wewe katika vitu vyenye kuvuvia hofu. Mishale yako ni mikali—chini yako vikundi vya watu vinafuliza kuanguka—katika moyo wa maadui wa mfalme. Mungu ndiye kiti cha ufalme chako kwa wakati usio dhahiri, hata milele; fimbo ya umaliki wako ni fimbo ya unyoofu. Wewe umependa uadilifu na wewe wachukia uovu. Hiyo ndiyo sababu Mungu, Mungu wako, amepaka wewe mafuta ya mchachawo zaidi ya washirika wako.” Akiwa anazoelea elezo hili la kiunabii, Yohana anathamini kwamba linatumika kuhusu utendaji wa Yesu akiwa Mfalme.—Linga Waebrania 1:1, 2, 8, 9.

Kutoka Kwenda Akishinda

6. (a) Ni kwa nini lazima Mpandaji atoke aende akishinda? (b) Ni kupitia miaka ipi upandaji wa ushindi unaendelea?

6 Ingawa hivyo, ni kwa nini lazima huyo Mfalme mvikwa-taji sasa hivi apande hali akienda kwenye vita? Ni kwa sababu umaliki wake unasimamishwa kukiwa na upinzani mkali kutoka kwa yule hasimu mkuu wa Yehova, Shetani Ibilisi, na wale walio juu ya dunia ambao—wakijua au pasipo kujua—wanatumikia makusudi ya Shetani. Uzawa wa Ufalme wenyewe wataka kuwe vita kuu katika mbingu. Akipiga vita kwa jina Mikaeli (linalomaanisha “Ni Nani Aliye Kama Mungu?”), Yesu anamshinda Shetani na roho waovu wake na kuwavurumisha chini kwenye dunia. (Ufunuo 12:7-12) Upandaji wenye ushindi wa Yesu unaendelea kupitia miongo ya kufungua ya siku ya Bwana wakati binadamu wenye mfano wa kondoo wanakusanywa. Ijapokuwa ulimwengu kwa ujumla ungali unalala “katika uwezo wa yule mwovu,” kwa upendo Yesu anaendelea kuchunga ndugu zake wapakwa-mafuta na waandamani wenzao, akisaidia kila mmoja apate ushindi wa imani.—1 Yohana 5:19, NW.

7. Ni ushindi gani ambao Yesu amepata katika miongo ya kwanza-kwanza ya siku ya Bwana, na azimio letu lapasa liwe nini?

7 Yesu amepata ushindi gani mwingine wakati wa miaka 90 na zaidi ya siku ya Bwana? Kuzunguka tufe lote, watu wa Yehova wakiwa mmoja mmoja na wakiwa kundi, wamepatwa na magumu mengi, mikazo, na minyanyaso, inayofanana na ile aliyoieleza mtume Paulo katika kutoa ithibati ya huduma yake. (2 Wakorintho 11:23-28) Mashahidi wa Yehova wamehitaji “nguvu zinazopita zilizo za kawaida,” ili wavumilie, hasa katika sehemu za vita na jeuri. (2 Wakorintho 4:7, NW) Lakini hata katika hali zenye kujaribu zaidi Mashahidi waaminifu wameweza kusema kama alivyosema Paulo: “Bwana alisimama karibu na mimi na akatia nguvu ndani ya mimi, kwamba kupitia mimi kuhubiri kupate kutimizwa kikamili.” (2 Timotheo 4:17, NW) Ndiyo, Yesu alishinda kwa niaba yao. Naye ataendelea kwenda akishinda kwa niaba yetu, maadamu sisi tunaazimia kukamilisha ushindi wetu wa imani.—1 Yohana 5:4.

8, 9. (a) Ni ushindi gani ambao kundi la Mashahidi wa Yehova la pote katika tufe limeshiriki? (b) Ni wapi ambako ukuzi wa Mashahidi wa Yehova umekuwa wenye kutokeza kweli kweli?

8 Kundi la Mashahidi wa Yehova la pote katika tufe limeshiriki ushindi mwingi chini ya mwongozo wa Mfalme walo mwenye kushinda. Kwa kutokeza sana, yeye aliwapa himaya hawa Wanafunzi wa Biblia wasipatwe na utowesho katika 1918, wakati wao wenyewe ‘waliposhindwa’ kwa muda na tengenezo la Shetani la kisiasa. Hata hivyo, katika 1919, alivunja mapingo ya gereza awaache huru, kisha akawahuisha ili wapige mbiu ya habari njema “mpaka kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.”—Ufunuo 13:7; Matendo 1:8, NW.

9 Kabla na wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, yale Mataifa Mhimili ya kidikteta yalijaribu kufutilia mbali Mashahidi wa Yehova katika mabara mengi ambako viongozi wa kidini, hasa mapadri wa Roma Katoliki, walitoa uungaji-mkono wa waziwazi au usio wa waziwazi kwa madikteta waonezi. Lakini Mashahidi 71,509 waliokuwa wakihubiri wakati vita ilipoanza katika 1939 wakawa 141,606 kufikia mwisho wayo katika 1945, hata ingawa zaidi ya 10,000 walikuwa wametumia miaka mirefu katika magereza na kambi za mateso, na 2,000 hivi walikuwa wameuawa. Hesabu ya Mashahidi watendaji duniani pote imepanuka kuwa zaidi ya milioni sita leo. Ukuzi umekuwa wenye kutokeza katika mabara ya Kikatoliki na katika nchi ambako minyanyaso ilikuwa mikali zaidi sana—kama Ujeremani, Italia, na Japani, ambamo Mashahidi wanaripoti jumla ya wahudumu wa shamba watendaji zaidi ya 600,000.—Isaya 54:17; Yeremia 1:17-19.

10. Ni kwa ushindi gani yule Mfalme mwenye kushinda amebariki watu wake “katika kutetea na kuthibitisha kisheria habari njema”?

10 Mfalme wetu mwenye kushinda amebariki pia watu wake wenye bidii kwa kuwaongoza kwenye ushindi mwingi “katika kutetea na kuthibitisha kisheria habari njema” katika mahakama ya sheria na mbele ya watawala. (Wafilipi 1:7; Mathayo 10:18; 24:9, NW) Hiyo imekuwa katika mataifa yote—katika Australia, Ajentina, Kanada, Ugiriki, India, Swazilandi, Swizalandi, Uturuki na mabara mengineyo. Miongoni mwa ushindi mbalimbali 50 wa kisheria waliopata Mashahidi wa Yehova katika Mahakama Kuu Zaidi Sana ya United States umekuwa ule unaohakikishia haki ya kujulisha wazi habari njema “peupe na nyumba kwa nyumba” na kutofanya sherehe za kuabudu sanamu za kizalendo. (Matendo 5:42; 20:20, NW; 1 Wakorintho 10:14) Hivyo, njia imeachwa wazi kwa ajili ya kupanua kazi ya kutoa ushahidi katika tufe lote.

11. (a) Yule Mpandaji ‘anakamilishaje ushindi wake’? (b) Kufunguliwa kwa kifungo cha pili, cha tatu, na cha nne kwapasa kuwe na tokeo gani juu yetu?

11 Yesu ‘anakamilishaje ushindi wake’?c Yeye anafanya hivyo, kama tutakavyoona, kwa kukomesha dini bandia na kisha kuvurumisha kila kisehemu kinachobaki cha tengenezo linaloonekana la Shetani ndani ya “ziwa la moto” la ufananisho wa uharibifu, katika kutetea enzi kuu ya Yehova. Kwa uhakika, sasa sisi tunatazamia siku hiyo kwenye Har–Magedoni wakati “Mfalme wa wafalme” wetu atajipatia ushindi juu ya tengenezo la Shetani la kisiasa lenye uonevu! (Ufunuo 16:16; 17:14; 19:2, 14-21; Ezekieli 25:17) Kwa wakati uliopo, Mshindi huyo asiyeshindika akiwa juu ya farasi mweupe anaendelea kupanda akisonga mbele kadiri Yehova anavyoongeza watu wenye mioyo minyofu kwenye taifa Lake lenye uadilifu duniani. (Isaya 26:2; 60:22) Je! wewe unashiriki pamoja na jamii ya Yohana iliyopakwa mafuta katika upanuzi huo wa Ufalme wenye shangwe? Ikiwa ndivyo, anachoona Yohana wakati vile vifungo vitatu vinavyofuata vinapofunguliwa bila shaka kitakuchochea wewe kwenye ushiriki mkubwa hata zaidi katika kazi ya Yehova kwa ajili ya siku hii.

Ona, Farasi wa Rangi-Moto!

12. Yesu alisema ni nini kingetia alama kuwapo kwake kusikoonekana akiwa Mfalme?

12 Kuelekea mwisho wa huduma ya Yesu duniani, wanafunzi wake walimuuliza faraghani hivi: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Katika kujibu, yeye alitabiri maafa ambayo yangekuwa “mwanzo wa maumivu makali ya ghafula ya taabu.” Akasema Yesu: “Taifa litainuka dhidi ya taifa, na ufalme dhidi ya ufalme; na kutakuwa na matetemeko ya dunia makubwa, na katika mahali pamoja baada ya pengine magonjwa ya kipuku na upungufu wa chakula; na kutakuwa na maono ya kutia hofu na kutoka mbinguni ishara kubwa.” (Mathayo 24:3, 7, 8; Luka 21:10, 11, NW) Vitu ambavyo Yohana anaona wakati vifungo vinavyobaki vya hati-kunjo vinapofunguliwa huandaa ulingano wa kustaajabisha wa unabii huo. Angalia sasa Yesu aliyetukuzwa afunguapo kifungo cha pili!

13. Ni tofauti gani inayokaribia kuwa wazi kwa Yohana?

13 “Na wakati yeye alipofungua kifungo cha pili, mimi nikasikia kiumbe hai wa pili akisema: ‘Njoo!’” (Ufunuo 6:3, NW) Ni yule kerubi wa pili, aliye na mwonekano wa fahali, anayetoa amri. Hapa nguvu ndiyo sifa inayofananishwa, lakini ni nguvu iliyotumiwa kwa uadilifu. Ingawa hivyo, kwa kutofautisha, sasa Yohana ataona wonyesho wenye kukirihisha sana wa nguvu, wenye kuleta kifo.

14. Ni farasi na mpandaji gani anayefuata kuonwa na Yohana, nayo njozi hii inatoa picha ya nini?

14 Basi, mwito huu “Njoo!” unajibiwaje? Katika njia hii: “Na mwingine akatokea, farasi wa rangi-moto; na yule mmoja aliyeketi juu yake alipewa ruhusa ya kuondolea mbali amani kutoka dunia ili wao wapaswe kuchinja mmoja na mwenzake; na upanga mkubwa akapewa yeye.” (Ufunuo 6:4, NW) Ni njozi ya kutia hofu kweli kweli! Na hakuna shaka juu ya inachotolea picha: vita! Si vita ya uadilifu, yenye ushindi wa Mfalme wa Yehova mwenye kushinda bali ni vita yenye ukatili ya kimataifa, yenye kufanyizwa na binadamu, yenye umwagaji-damu na maumivu ya bure. Inafaa kama nini kwamba mpandaji huyu anampanda farasi wa rangi-nyekundu kama moto!

15. Ni kwa nini haitupasi sisi tutake sehemu yoyote ya upandaji wa yule mwana-farasi wa pili?

15 Kwa hakika, Yohana hangetaka sehemu yoyote ya mwana-farasi na upandaji wake wenye haraka isiyo na akili, kwa kuwa unabii ulitolewa kuhusu watu wa Mungu hivi: “Wala hawatajifunza vita tena kamwe.” (Isaya 2:4) Ingawa wangali “katika ulimwengu,” Yohana na, kwa upanuzi, ile jamii ya Yohana na umati mkubwa leo wao “si sehemu” ya huu mfumo wenye madoa ya damu. Silaha zetu ni za kiroho na “zinajaa nguvu kwa njia ya Mungu” kwa ajili ya kupiga mbiu ya ukweli kwa bidii, bila vita ya kimwili.—Yohana 17:11, 14; 2 Wakorintho 10:3, 4, NW.

16. Ni lini na jinsi gani mpandaji-farasi mwekundu alipewa “upanga mkubwa”?

16 Kulikuwa kumekuwa na vita vingi kabla ya 1914, ule mwaka Mpandaji-farasi mweupe alipopokea taji lake. Lakini sasa mpandaji-farasi mwekundu anapewa “upanga mkubwa.” Hiyo inadokeza nini? Kwa mlipuko wa Vita ya Ulimwengu 1, vita vya binadamu vimekuwa vyenye umwagaji-damu mwingi zaidi, vyenye uharibifu mwingi zaidi ya vilivyopata kuwa kabla ya hapo. Wakati wa mwosho-damu wa 1914-18, matanki, gesi zenye sumu, eropleni, sabmarini, mizinga mikubwa, na silaha za otomatiki zilitumiwa ama kwa mara ya kwanza ama kwa kadiri isiyotangulia kufanywa. Katika mataifa yapata 28, idadi ya watu wa nchi kwa ujumla, si wale tu ambao kazi yao ya maisha ni askari-jeshi, walisukumizwa kwenye jitihada za vita. Majeruhi walikuwa kadiri ya kuogopesha. Askari-jeshi zaidi ya milioni tisa walichinjwa, na majeruhi ya raia walikuwa wengi mno. Hata ilipokwisha vita, hakukuwa na kurudia amani halisi duniani. Zaidi ya miaka 50 baada ya vita, Konrad Adenauer waziri wa serikali Mjeremani alitoa elezo hili: “Usalama na utulivu vimetoweka katika maisha ya watu tangu 1914.” Kweli kweli yule mpandaji-farasi wa rangi-moto alipewa ruhusa aondolee mbali amani duniani!

17. Utumizi wa huo “upanga mkubwa” umeendeleaje, kufuata Vita ya Ulimwengu 1?

17 Halafu, kiu yake ya kutaka kuona damu ikimwagwa ikiwa imechochewa, yule mpandaji-farasi mwekundu alijitumbukiza ndani ya Vita ya Ulimwengu 2. Zana za uchinjaji zilizidi kuwa za kishetani zaidi, nayo majeruhi yakapanda juu kuwa mara nne ya yale ya Vita ya Ulimwengu 1. Katika 1945 bomu mbili za atomu zililipuka juu ya Japani, kila mojapo ilifutilia mbali—kwa dharuba moja—makumi ya maelfu ya majeruhi. Katika pindi ya vita ya pili ya ulimwengu, yule mpandaji-farasi mwekundu alivuna mavuno makubwa ya maisha zapata milioni 55, na hata wakati huo yeye hakutosheka. Imeripotiwa kwa njia yenye kuaminika kwamba nafsi zaidi ya milioni 20 zimeanguka chini ya ule “upanga mkubwa” tangu Vita ya Ulimwengu 2.

18, 19. (a) Badala ya huo kuwa ushindi wenye shangwe wa tekinolojia ya kivita, lile chinjo tangu Vita ya Ulimwengu 2 ni uhakika wa ushuhuda gani? (b) Ni hatari gani inayokabili aina ya binadamu, lakini yule Mpandaji-farasi mweupe atafanya nini kuisawazisha?

18 Je! sisi tungeweza kuita huu kuwa ushindi wenye shangwe wa tekinolojia ya kivita? Badala ya hivyo, huo ni ushuhuda wa kwamba yule farasi mwekundu asiye na rehema yuko katika mwendo. Na mwendo huo utaishia wapi? Baadhi ya wanasayansi wanasema kwamba kuna uwezekano wa vita ya nyukilia kutokea kiaksidenti—achia mbali mteketezo mkubwa wa kinyukilia uliopangwa! Lakini kwa furaha yule Mpandaji-farasi mweupe mwenye kushinda ana fikira tofauti juu ya jambo hili.

19 Maadamu msingi wa jamii ya watu ni kiburi cha kitaifa na chuki, lazima aina ya binadamu iendelee kukalia kipipa cha hatari ya nyukilia. Hata kama mataifa yangekwangulia mbali silaha zayo za nyukilia kwa kutamauka, yangebaki na huo ujuzi. Kwa muda mfupi sana, wangeunda tena vidude vyao vya nyukilia vya uuaji-makusudi; kwa sababu hiyo, vita yoyote ikitumia silaha za kadiri ingevuvumuka upesi kama uyoga na kuwa maangamizi makubwa. Kile kiburi na chuki inayofunika mataifa leo lazima viongoze kwenye ujiuaji wa binadamu, isipokuwa—aha, ndiyo, isipokuwa yule Mpandaji-farasi mweupe ageuzie mbali mwendo wa kichaa wa yule mpandwaji wa rangi-moto. Acheni sisi tuwe na uhakika kwamba Kristo Mfalme atapanda, ili akamilishe ushindi wake juu ya ulimwengu wenye kudhibitiwa na Shetani na pia ili asimamishe jamii mpya ya kidunia ambayo msingi wayo ni upendo—upendo kwa Mungu na kwa jirani—kani kwa ajili ya amani, iliyo ya juu zaidi ya ile yenye kutikisika ya mazuio ya vita ya nyakati zetu zenye kichaa.—Zaburi 37:9-11; Marko 12:29-31; Ufunuo 21:1-5.

Farasi Mweusi Aruka Kuja Mbele

20. Sisi tuna uhakikisho gani kwamba Mpandaji-farasi mweupe ataiweza hali yoyote yenye balaa?

20 Yesu anafungua sasa kifungo cha tatu! Yohana, unaona nini? “Na wakati yeye alipofungua kifungo cha tatu, mimi nikasikia kiumbe hai wa tatu akisema: ‘Njoo!’” (Ufunuo 6:5a, NW) Kwa furaha kerubi huyu wa tatu “ana uso kama wa binadamu,” kuonyesha sifa ya upendo. Upendo wenye kuongozwa na kanuni utakuwa mwingi sana katika ulimwengu mpya wa Mungu, hata kama vile sifa hiyo nzuri sana inavyoenea katika tengenezo lote la Yehova leo. (Ufunuo 4:7; 1 Yohana 4:16) Sisi tunaweza kuwa na hakika kwamba Mpandaji-farasi mweupe, ambaye “lazima atawale akiwa mfalme mpaka Mungu awe ameweka maadui wote chini ya nyayo zake,” kwa upendo ataondoa ile hali yenye maafa ambayo inafuata kuletwa kwenye uchunguzi wa Yohana.—1 Wakorintho 15:25, NW.

21. (a) Ni nini kinachotolewa picha na yule farasi mweusi na mpandaji wake? (b) Ni nini kinachothibitisha kwamba huyo farasi mweusi angali katika mwendo wake wenye ukali?

21 Basi, Yohana anaona nini, wakati ule mwito wa tatu “Njoo!” unapojibiwa? “Na mimi nikaona, na, tazama! farasi mweusi ti; na mmoja aliyeketi juu yake alikuwa na jozi ya mizani katika mkono wake.” (Ufunuo 6:5b, NW) Njaa tupu! Huo ndio ujumbe wa kutisha wa mandhari hii ya kiunabii. Unaelekeza mbele kwenye hali za mapema katika siku ya Bwana wakati lazima chakula kipimwe kwa mizani. Tangu 1914 njaa imekuwa tatizo la ulimwenguni pote lenye kuendelea. Vita vya ki-siku-hizi huleta njaa ikifuatana navyo, kwa kuwa rasilimali ambazo kwa kawaida hutumiwa kulisha watu wenye njaa mara nyingi hugeuzwa na kutumiwa kutoa ugavi wa silaha za vita. Wafanya kazi wa mashamba wanaingizwa jeshini kwa nguvu, nazo sera zinazokataza kulima nyanja zenye makovu ya vita na dunia iliyounguzwa hupunguza uzalishaji wa chakula. Hiyo ilikuwa kweli kama nini wakati wa vita ya kwanza ya ulimwengu, mamilioni yalipotaabishwa na njaa na wakafa! Zaidi ya hilo, yule mpandaji-farasi mweusi wa njaa hakuacha ilipoisha vita. Wakati wa muda wa tangu 1930, milioni tano walipotea katika njaa moja tu katika Ukraine. Ile vita ya pili ya ulimwengu ilileta pamoja nayo upungufu zaidi wa chakula na njaa. Kadiri yule farasi mweusi alivyoendelea na mwendo wake, Baraza la Chakula Ulimwenguni liliripoti katikati ya 1987 kwamba binadamu milioni 512 walikuwa wakifa njaa na kwamba watoto 40,000 wanakufa kila siku kwa visababishi vinavyohusiana na njaa.

22. (a) Sauti inasema nini, ikionyesha uhitaji gani? (b) Ni jambo gani linalodokezwa na bei ya kwarti moja ya ngano na kwarti tatu za shayiri?

22 Je! Yohana ana zaidi ya kutuambia sisi: “Na mimi nilisikia sauti kana kwamba ni katikati ya viumbe hai wanne ikisema: ‘Kwarti moja ya ngano kwa dinari moja, na kwarti tatu za shayiri kwa dinari moja; na usidhuru mafuta ya zeituni na divai.’” (Ufunuo 6:6, NW) Makerubi wote wanne wana umoja katika kuonyesha uhitaji wa kulinda ugavi wa chakula kwa uangalifu—kama vile watu walikuwa hawana budi ‘kula chakula kwa uzani na katika ujalifu wenye wasiwasi’ kabla ya uharibifu wa Yerusalemu katika 607 K.W.K. (Ezekieli 4:16, NW) Katika wakati wa Yohana, kwarti ya ngano ilihesabiwa kuwa ndiyo posho ya kila siku ya askari-jeshi. Posho kama hiyo ingegharimu kiasi gani? Dinari moja—mshahara wa siku nzima! (Mathayo 20:2)d Namna gani kama mtu alikuwa na jamaa? Basi, badala ya hiyo yeye angeweza kununua kwarti tatu za shayiri isiyosafishwa. Hata hiyo ingeweza kulisha jamaa ndogo tu. Na shayiri haikuonwa kuwa chakula bora kama vile ngano.

23. Ni nini kinachodokezwa na taarifa, “Usidhuru mafuta ya zeituni na divai”?

23 Ni nini kinachodokezwa na taarifa, “Usidhuru mafuta ya zeituni na divai”? Wengine wameiona kuwa ikimaanisha kwamba ingawa wengi wangepungukiwa na chakula na hata wafe njaa, vitu vya anasa vya matajiri havingedhuriwa. Lakini katika Mashariki ya Kati, mafuta na divai si vitu vya anasa kwa kweli. Katika nyakati za Biblia, mkate, mafuta, na divai vilionwa kuwa chakula kikuu. (Linga Mwanzo 14:18; Zaburi 104:14, 15.) Sikuzote maji hayakuwa safi, kwa hiyo divai ilitumiwa sana kwa kunywa na nyakati nyingine kwa makusudi ya kitiba. (1 Timotheo 5:23) Kwa habari ya mafuta, katika siku ya Eliya mjane wa Sarepta, ajapokuwa maskini, bado alikuwa amebakiza mafuta kiasi fulani ya kupikia unga wake uliobaki. (1 Wafalme 17:12) Kwa hiyo, amri “usidhuru mafuta ya zeituni na divai” inaonekana kuwa shauri la kutotumia bidhaa hizo za msingi kwa uharaka mno lakini kuzitumia kwa kulimbika. La sivyo, ‘zitadhuriwa,’ yaani, zitakwisha kabla ya njaa kwisha.

24. Ni kwa nini farasi mweusi hataendelea na mwendo wake kwa muda zaidi ulio mrefu?

24 Jinsi tunavyoweza kuwa na furaha kwamba yule Mpandaji-farasi mweupe karibuni atazuia kwa hatamu mwendo wa farasi huyo mweusi! Kwa maana imeandikwa kuhusu uandalizi Wake wa upendo kwa ajili ya ulimwengu mpya hivi: “Katika siku zake mwadilifu atachipuka, na wingi wa amani mpaka mwezi uwe haupo tena. . . . Kutakuja kuwa na utele wa nafaka juu ya dunia; juu ya kilele cha milima kutakuwa na mfuriko.”—Zaburi 72:7, 16, NW; ona pia Isaya 25:6-8.

Farasi Rangi Nyeupe-Nyeupe na Mpandaji Wake

25. Wakati Yesu anapofungua kifungo cha tatu, Yohana anasikia sauti ya nani, na hiyo inaonyesha nini?

25 Hadithi haijaisha kabisa kusimuliwa. Yesu anafungua kifungo cha nne, naye Yohana anatusimulia tokeo: “Na wakati yeye alipofungua kifungo cha nne, mimi nikasikia sauti ya kiumbe hai wa nne ikisema: ‘Njoo!’” (Ufunuo 6:7, NW) Hii ni sauti ya kerubi anayeshabihi tai arukaye. Hekima yenye kuona mbali ndiyo inayoonyeshwa hapa, na kweli kweli Yohana, jamii ya Yohana, na wengine wote wa watumishi wa Mungu duniani wamehitaji kuona na kutenda kwa muono-ndani kwa sababu ya kinachoonyeshwa na picha hapa. Kwa kufanya hivyo, sisi tunaweza kupata kadiri fulani ya himaya tusipatwe na mapigo yanayosumbua wenye hekima ya kilimwengu wa kizazi cha leo chenye kiburi na utovu wa maadili.—1 Wakorintho 1:20, 21.

26. (a) Mwana-farasi wa nne ni nani, na ni kwa nini rangi ya farasi wake inafaa? (b) Ni nani anayemfuata mwana-farasi wa nne, na ni nini kinachopata majeruhi wake?

26 Basi, ni hofu gani mpya zinazoachiliwa, wakati mwana-farasi wa nne anapoitikia mwito? Yohana anatusimulia hivi: “Na mimi nikaona, na, tazama! farasi rangi nyeupe-nyeupe; na mmoja aliyeketi juu yake alikuwa na jina Kifo. Na Hadesi alikuwa akifuata yeye karibu-karibu.” (Ufunuo 6:8a, NW) Mpandaji-farasi wa mwisho ana jina: Kifo. Ni yeye pekee kati ya hao wana-farasi wanne wa Apokalipsi ambaye amefunua jina lake hivyo moja kwa moja. Kwa kufaa, Kifo hupanda farasi ambaye ni rangi nyeupe-nyeupe, kwa kuwa neno -eupe-eupe (Kigiriki, khlo·rosʹ) hutumiwa katika fasihi za Kigiriki kueleza nyuso ambazo zimefanywa kuwa nyeupe, kana kwamba kwa kifo. Pia kwa kufaa, Kifo kinafuatwa karibu-karibu na Hadesi (kaburi kwa ujumla) kwa njia fulani isiyoelezwa, kwa kuwa Hadesi hupokea ndani yake idadi iliyo kubwa zaidi ya wale wanaokuwa majeruhi wa mikumbo ya huyo mwana-farasi wa nne. Kwa furaha, kwa hao kutakuwako ufufuo, wakati ‘kifo na Hadesi vinapotoa wafu walio ndani yavyo.’ (Ufunuo 20:13, NW) Lakini Kifo kinadaije hao majeruhi?

27. (a) Mpandaji Kifo anadaije majeruhi wake? (b) Ni nini kinachomaanishwa na “sehemu ya nne ya dunia” ambayo juu yayo Kifo ana mamlaka?

27 Njozi inataja baadhi ya njia hizo: “Na wao walipewa mamlaka juu ya sehemu ya nne ya dunia, kuua kwa upanga mrefu na kwa upungufu wa chakula na kwa tauni yenye kufisha na kwa hayawani-mwitu wa dunia.” (Ufunuo 6:8b, NW) La, hasha, si sehemu ya nne halisi ya idadi ya watu wa dunia lakini fungu kubwa la dunia, iwe inasongamana watu au inakaliwa na wachache, ingeathiriwa na upandaji huu. Mwana-farasi huyu anavuna majeruhi ya ule upanga mkubwa wa mwana-farasi wa pili na njaa na upungufu wa chakula wa yule wa tatu. Vilevile, anavuna vuno lake mwenyewe kutokana na tauni yenye kufisha na pia vuno kutokana na matetemeko ya dunia, kama inavyoelezwa kwenye Luka 21:10, 11, NW.

28. (a) Kumekuwaje na utimizo wa unabii kuhusu “tauni yenye kufisha”? (b) Watu wa Yehova wamepewaje himaya juu ya magonjwa mengi leo?

28 Lenye umaana wa kisasa hapa ni “tauni yenye kufisha.” Kufuata mikumbo ya Vita ya Ulimwengu 1, homa-mafua ya Hispania ilivuna maisha za binadamu milioni 20 katika miezi michache tu ya 1918-19. Eneo pekee duniani lililoepuka pigo hili ni kisiwa kidogo cha St. Helena. Katika mahali ambako idadi ya watu waliuawa sana na ugonjwa huu marundo ya kuni za maziko yaliwashwa ili kuchoma maiti chunguchungu. Na leo kuna tukio lenye kuogofya la ugonjwa wa moyo na kansa, na chenye kuyasababisha sana ni uchafuzi wa tumbako. Katika kile kilichoelezwa kuwa “mwongo wenye sura mbaya” wa miaka ya 1980, njia ya maisha ambayo ni ya uasi wa sheria kulingana na viwango vya Biblia iliongeza lile pigo la UKIMWI kwa ile “tauni yenye kufisha.” Katika mwaka wa 2,000, iliripotiwa kwamba daktari mkuu wa Marekani alisema kwamba “huenda [UKIMWI] ndio ugonjwa mbaya zaidi wenye kuambukiza uliopata kutokea ulimwenguni.” Alisema kwamba watu milioni 52 ulimwenguni pote walikuwa na virusi vya UKIMWI, na milioni 20 kati yao tayari walikuwa wamekufa. Jinsi watu wa Yehova walivyo wenye shukrani kwamba lile shauri la hekima la Neno lake linawaepusha na uasherati na tumizi baya la damu, ambalo kupitia kwalo magonjwa mengi sana yanapitishwa leo!—Matendo 15:28, 29, NW; linga 1 Wakorintho 6:9-11.

29, 30. (a) Kungekuwa na tumizi gani leo la yale ‘matendo manne yenye kudhuru’ ya Ezekieli 14:21? (b) Sisi tuelewe nini kwa usemi “hayawani-mwitu” wa Ufunuo 6:8? (c) Ni nini linaloonekana kuwa jambo kuu la mandhari hiyo ya kiunabii?

29 Njozi ya Yohana hutaja hayawani-mwitu kuwa kisababishi cha nne cha kifo cha mapema. Kweli kweli, hivyo vitu vinne vilivyoonyeshwa kwa kufunguliwa kwa kifungo cha nne—vita, njaa, ugonjwa, na hayawani-mwitu—vilionwa katika nyakati za kale kuwa visababishi vikuu vya kifo cha mapema. Hivyo vingetangulia kuweka kivuli cha visababishi vyote vya kifo cha mapema leo. Ni kama vile Yehova alivyoonya Israeli: “Ndivyo, vilevile, itakuwa wakati kutakuwa matendo yangu manne yenye kudhuru ya hukumu—upanga na njaa na hayawani-mwitu wenye kudhuru na ugonjwa wa kipuku—ambayo mimi hakika nitapeleka juu ya Yerusalemu ili kukatilia mbali kutoka hilo mwanadamu wa dunia na mnyama wa nyumbani.”—Ezekieli 14:21, NW.

30 Si mara nyingi ambapo vifo vinavyoletwa na hayawani-mwitu vimekuwa vichwa vikuu magazetini katika nyakati za ki-siku-hizi, ingawa katika nchi za kitropiki wanyama-mwitu wamezidi kudai majeruhi. Katika wakati ujao, huenda wakadai hata zaidi ikiwa mabara yanaachwa ukiwa kwa sababu ya vita au watu wanadhoofishwa mno na njaa wasiweze kufukuzia mbali wanyama wenye njaa. Kwa kuongezea, kuna binadamu wengi sana leo ambao, kama wanyama wasiofikiri, wanaonyesha mielekeo ya kihayawani tofauti kabisa na ile inayoelezwa kwenye Isaya 11:6-9. Watu hawa ndio sana sana walio na daraka la mweneo wa pote katika tufe wa uhalifu unaohusiana na ngono, uuaji-makusudi, uvamizi-haramu, na milipuko ya mabomu katika ulimwengu wa ki-siku-hizi. (Linga Ezekieli 21:31; Warumi 1:28-31; 2 Petro 2:12.) Yule mwana-farasi wa nne huvuna majeruhi wao vilevile. Kweli kweli, jambo kuu la mandhari hii ya kiunabii linaonekana kuwa kwamba yule mpandaji-farasi rangi nyeupe-nyeupe huvuna kwa njia nyingi kifo cha mapema cha aina ya binadamu.

31. Ijapokuwa mikumbo inayosababishwa na wale wapandaji-farasi mwekundu, mweusi, na mweupe-mweupe, ni kwa sababu gani sisi tunaweza kutiwa moyo?

31 Ile habari iliyofunuliwa kwa kufunguliwa vile vifungo vinne vya kwanza hutumainisha sisi kwa sababu inatufundisha kutotamaushwa na vita, njaa, magonjwa, na visababishi vingine vya kifo cha mapema ambavyo vinaenea sana leo; wala haitupasi kupoteza tumaini kwa sababu viongozi wa kibinadamu wameshindwa kutatua matatizo ya sasa. Ikiwa hali za ulimwengu zinaifanya iwe wazi kwamba wale wapandaji-farasi mwekundu, mweusi, na rangi nyeupe-nyeupe wako kotekote, usisahau kwamba Mpandaji-farasi mweupe alikuwa wa awali kuanza upandaji wake. Yesu amekuwa Mfalme, na tayari yeye ameshinda kwa kadiri ya kumtupa Shetani nje ya mbingu. Ushindi wake mwingine mbalimbali unatia ndani kukusanywa kwa mabaki ya wana wa Israeli wa kiroho na umati mkubwa wa kimataifa, unaofikia hesabu ya mamilioni, ili wakaokolewe kupitia ile dhiki kubwa. (Ufunuo 7:4, 9, 14) Upandaji wake lazima uendelee mpaka akamilishapo ushindi wake.

32. Ni nini kinachotofautisha kufunguliwa kwa kila kimoja cha vifungo vinne vya kwanza?

32 Kufunguliwa kwa kila kimoja cha hivyo vifungo vya kwanza kumefuatwa na ule mwito: “Njoo!” Kila wakati, farasi na mpandaji wake walitoka wakiwa katika mwendo. Kuanzia na kifungo cha tano, sisi hatusikii tena mwito kama huo. Lakini wana-farasi hao wangali wanapanda, nao wataendelea katika mwendo muda wote wa huu umalizio wa mfumo wa mambo. (Linga Mathayo 28:20.) Ni matukio gani mengine yenye maana kubwa ambayo Yesu anafunua anapofungua vifungo vitatu vinavyobaki? Baadhi ya matukio ni yasiyoonekana na macho ya kibinadamu. Mengine, ingawa ni yenye kuonekana, bado ni ya wakati ujao. Hata hivyo, utimizo wayo ni hakika. Acheni sisi tuone ni matukio gani hayo.

[Maelezo ya Chini]

a Hata hivyo, angalia kwamba “mwanamke” wa Ufunuo 12:1 ana “taji la nyota kumi na mbili” la kitamathali.

b Kupata ithibati yenye maelezo mengi ya kwamba Yesu aliingia katika Ufalme wake katika 1914, ona ukurasa wa 215-218 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

c Ingawa tafsiri nyingi hufasiri fungu hili la maneno “kushinda” (Swahili Union Version, Revised Standard, The New English Bible, King James Version) “akiwa amenuia kupata ushindi” (Phillips, New International Version), tumizi hapa la namna ya kitenzi katika Kigiriki asilia bila kuonyesha kukamilika au muda wa tendo hutoa maana ya ukamilisho au mwisho kabisa. Kwa sababu hiyo, Word Pictures in the New Testament cha Roberts hutoa elezo hili: “Kitenzi-wakati hapa cha kutoonyesha kukamilika au muda wa tendo huelekeza kwenye ushindi wa mwisho kabisa.”

d Ona New World Translation Reference Bible, kielezi cha chini.

[Picha katika ukurasa wa 92]

Yule Mfalme Apanda kwa Ushindi

Katika Miaka ya 1930 na 1940, maadui wenye kujikaza walijaribu kufanya ionekane kwamba huduma ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa haramu, yenye uhalifu, au hata yenye kufitini serikali. (Zaburi 94:20) Katika mwaka 1936 pekee, kulikuwako kutiwa mbaroni kulikorekodiwa 1,149 katika United States. Mashahidi walipiga vita ya kesi za kisheria mwendo wote kufikia ile Mahakama Kuu Zaidi Sana, na ufuatao ni baadhi ya ushindi wao mbalimbali wenye kutokeza.

Katika Mei 3, 1943, Mahakama Kuu Zaidi Sana katika kesi ya Murdock v. Pennsylvania iliamua kwamba Mashahidi hawakuhitaji leseni ili waangushe vitabu kwa pesa. Siku iyo hiyo, ule uamuzi katika kesi ya Martin v. City of Struthers ulishikilia kwamba si kinyume cha sheria kupiga kengele ya mlango wakati wa kushiriki kugawa karatasi na vitu vingine vya kuvumisha habari.

Katika Juni 14, 1943, Mahakama Kuu Zaidi Sana iliamua katika kesi ya Taylor v. Mississippi kwamba Mashahidi hawakutia moyo utovu wa ushikamanifu kwa serikali kwa kuhubiri kwao. Siku iyo hiyo, katika kesi ya West Virginia State Board of Education v. Barnette, Mahakama hiyo ilishikilia kwamba baraza la shule halikuwa na haki ya kufukuza kutoka shuleni watoto wa Mashahidi wa Yehova waliokataa kusalimu bendera. Kesho yake yenyewe, Mahakama Kuu ya Australia iliyojaa iliondoa marufuku ambayo nchi hiyo iliwekea Mashahidi wa Yehova, hiyo ikitangazwa kuwa “isiyo ya haki, bila sababu nzuri na yenye uonevu.”

[Picha katika ukurasa wa 94]

“Alipewa Ruhusa Kuondolea Mbali Amani Kutoka Dunia”

Tekinolojia inaongoza wapi? The Globe and Mail, Toronto, Kanada, Januari 22, 1987, iliripoti yafuatayo kutokana na hotuba ya Ivan L. Head, msimamizi wa International Development Research Centre:

“Inakadiriwa kwa njia yenye kutegemeka kwamba mmoja wa kila wanasayansi na wanatekinolojia wanne katika ulimwengu wanaofanya utafiti na usitawishi anafanya kazi ya kuunda silaha. . . . Kwa makadirio ya 1986, gharama ni zaidi ya dola milioni 1.5 kwa dakika. . . . Je! sisi sote ni wenye usalama zaidi kama tokeo la mkazo wa aina hii ya tekinolojia? Silaha za nyukilia yalizo nazo yale mataifa yenye nguvu zaidi zina kani ya baruti ya zana zote za vita zilizotumiwa na wapiganaji wote katika Vita ya Ulimwengu 2 yote—mara 6,000. Vita ya Ulimwengu 2 elfu sita. Tangu 1945, kumekuwa na [muda] ulio punde ya majuma saba wakati ulimwengu umekuwa bila utendaji wa kivita. Kumekuwako zaidi ya vita 150 vya asilia ya kimataifa au vya raia wenyewe kwa wenyewe, ambavyo vimekadiriwa kuwa vilidai maisha milioni 19.3, vingi vyavyo vikiwa ni tokeo la tekinolojia mpya zenye usahihi zaidi ambazo zimezuka katika wakati huu wa Umoja wa Mataifa.”

Kufikia 2005, utendaji wa kijeshi ulikuwa umesababisha vifo zaidi ya milioni 20.

[Picha katika ukurasa wa 98 99]

Muundo wa Kitabu cha Ufunuo

Tukiwa tumeendelea kufikia hapa katika mazungumzo yetu ya kitabu cha Ufunuo, tunaanza kuona kwa wazi zaidi muundo wa kitabu. Baada ya utangulizi wacho wenye kusisimua (Ufunuo 1:1-9), Ufunuo kinaweza kuonwa kuwa kimegawanywa katika njozi 16 kama ifuatavyo:

NJOZI YA 1 (1:10–3:22): Yohana kwa kuvuviwa anamwona Yesu Kristo aliyetukuzwa, ambaye anapeleka jumbe zenye uchangamshi za shauri kwa yale makundi saba.

NJOZI YA 2 (4:1–5:14): Mwono wenye uzuri mwingi mno wa kiti cha ufalme cha kimbingu cha Yehova Mungu. Huyu Mmoja anamkabidhi Mwana-Kondoo hati-kunjo.

NJOZI YA 3 (6:1-17): Akivunja na kufungua vile vifungo sita vya kwanza vya hati-kunjo, Mwana-Kondoo anafunua kwa mwendeleo njozi yenye matukio mengi ambayo hayana budi kuwa katika siku ya Bwana. Wale wana-farasi wanne wa Apokalipsi wanatoka wakiwa wamepanda, watumwa wa Mungu waliofia imani wanapokea majoho meupe, na siku ya hasira-jeuri inaelezwa.

NJOZI YA 4 (7:1-17): Malaika wanazuia zile pepo za uharibifu mpaka Waisraeli wa kiroho 144,000 watiwe kifungo. Umati mkubwa kutoka mataifa yote wanawahesabia Mungu na Kristo wokovu nao wanakusanywa kwa ajili ya wokovu kupitia dhiki kubwa.

NJOZI YA 5 (8:1–9:21): Wakati wa kufunguliwa kwa kifungo cha saba, kunakuwa na mipigo saba ya tarumbeta, sita ya kwanza ya hiyo inafanyiza njozi ya tano. Mipigo hii sita ya tarumbeta yatoa habari ya maonyesho ya hukumu ya Yehova juu ya aina ya binadamu. Zile tarumbeta za tano na sita pia zinajulisha ole wa kwanza na wa pili.

NJOZI YA 6 (10:1–11:19): Malaika kabambe anampa Yohana hati-kunjo ndogo, hekalu linapimwa, nasi tunajifunza habari ya yanayopata mashahidi wawili. Inafikia upeo kwa kupulizwa kwa tarumbeta ya saba, ambayo inatoa habari ya ole wa tatu kwa ajili ya maadui wa Mungu—Ufalme wa Yehova na wa Kristo unaokuja.

NJOZI YA 7 (12:1-17): Hii hueleza habari za uzawa wa Ufalme, matokeo yakiwa ni Mikaeli kuvurumisha chini duniani yule nyoka, Shetani.

NJOZI YA 8 (13:1-18): Hayawani-mwitu anayejaa nguvu anakuja kutoka bahari, na hayawani-mwitu mwenye pembe mbili kama mwana-kondoo ahimiza aina ya binadamu iabudu huyo.

NJOZI YA 9 (14:1-20): Mtazamo-tangulizi mzuri ajabu wa wale 144,000 juu ya Mlima Sayuni. Jumbe za kimalaika zasikiwa kuzunguka dunia yote, mzabibu wa dunia unavunwa, nalo shinikizo la divai la kasirani ya Mungu lakanyagwa.

NJOZI YA 10 (15:1–16:21): Mtazamo mwingine mfupi wa kitala cha kifalme cha kimbingu, ukifuatwa na kumiminwa kwa mabakuli saba ya kasirani ya Mungu ndani ya dunia. Sehemu hii, vilevile, inaisha kwa elezo la kiunabii la mwisho wa mfumo wa Shetani.

NJOZI YA 11 (17:1-18): Kahaba mkubwa, Babuloni Mkubwa, apanda hayawani-mwitu wa rangi nyekundu-angavu, ambaye anaingia kifupi ndani ya abiso lakini anatokea tena na kumwangamiza.

NJOZI YA 12 (18:1–19:10): Anguko na uharibifu wa mwisho wa Babuloni Mkubwa watangazwa. Baada ya kuuawa kwake, baadhi waomboleza, wengine wanasifu Yehova; ndoa ya Mwana-Kondoo yatangazwa.

NJOZI YA 13 (19:11-21): Yesu anaongoza majeshi ya mbingu kutekeleza hukumu za Mungu zenye kujaa hasira-jeuri juu ya mfumo wa Shetani, majeshi yao, na waunga-mkono wao; ndege-wala-nyama wafanya karamu ya kula mizoga yao.

NJOZI YA 14 (20:1-10): Kutiwa ndani ya abiso kwa Shetani Ibilisi, Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo na wafalme wenzake, mtihani wa mwisho kabisa wa aina ya binadamu, na kuharibiwa kwa Shetani na roho waovu wake.

NJOZI YA 15 (20:11–21:8): Ufufuo wa watu wote na Siku ya Hukumu iliyo kubwa; mbingu mpya na dunia mpya zatokea, zikiwa na baraka za milele kwa aina ya binadamu yenye uadilifu.

NJOZI YA 16 (21:9–22:5): Ufunuo unafikia upeo kwa njozi tukufu ya Yerusalemu Jipya, mke wa Mwana-Kondoo. Uandalizi wa Mungu wa kuponya na uhai kwa aina ya binadamu watiririka kutoka jiji hilo.

Ufunuo wamalizika kwa maneno machangamfu ya salamu na shauri kutoka kwa Yehova, Yesu, malaika, na Yohana mwenyewe. Mwaliko kwa kila mmoja ni “Njoo!”—Ufunuo 22:6-21.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki